Thursday, June 23, 2011

‘Wanawake hujamiiana bila ridhaa yao’

WANAWAKE wengi nchini wanadaiwa kujamiiana kwa mara ya kwanza bila ya maridhiano baina yao na wanaume.

Mwezeshaji kutoka Maendeleo ya Jamii ya Shirika lisilo la Kiserikali la Plan International, Geryson Frednand alisema hayo katika washa ya siku mbili ya haki za wasichana na wanawake iliyoandaliwa na shirika la Care International.

Frednand alisema, katika utafiti waliowahi kuufanya, unaonesha kuwa wanawake wengi hasa katika maeneo ya vijijini wamekwa wakishurutishwa kufanya mapenzi au kuozeshwa kabla ya muda wao kufika.

Alisema, katika maeneo ya vijijini ndipo vitendo vya ukatili wa wanawake hufanyika kwa wingi.

Pamoja na mambo mengine, mwezeshaji huyo alisema utafiti unaonesha asilimia kati ya 15 na 71 ya wanawake wananyanyaswa na waume zao huku wakiogopa kutoa taarifa katika ngazi husika kwa kuogopa kuachika.

Alisema, kwa sasa hatuna budi elimu ya uzazi na juu ya haki za msingi itolewe kwa wingi kwa jamii vijijini ili kupunguza ukatili wa wanawake kutoka kwa waume zao.

“Nashangaa kuona wanawake wengi hawatoi taarifa katika ngazi husika pindi wanapofanyiwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia na waume zao, hali ambayo inawafanya kuathirika kisaikolojia na kujikuta wakikosa sehemu ya kukimbiza malalamiko yao kwa wakati,” alisema.

No comments: