Tuesday, September 11, 2012

Tanpress: Mwema, Nchimbi wang’oke

Shirika Huru la Habari (Tanpress) limemtaka Rais Jakaya Kikwete amfukuze kazi Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Said Mwema na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi.

Limesema viongozi hao wanatakiwa kuwajibishwa kutokana na mauaji ya mwaandishi wa habari wa kituo cha televisheni cha Channel Ten, Daudi Mwangosi yaliyotokea mkoani Iringa.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi wa Tanpress, Mobini Sarya, imeeleza kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda anatakiwa kuwajibika kutokana na amri yake aliyoitoa wakati wa vurugu kati ya polisi na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleoi (Chadema).

Shirika hilo limeitaka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo itoe ufafanuzi kwa kushindwa kutoa tamko na msaada kufuatia kifo cha mwandishi huyo licha ya kwamba polisi wanatuhumiwa kuhusika na mauaji hayo.

 “Kuna mauaji ya watu watano yaliyotokea Tarime ambayo yalifanywa na polisi walitoa ubani kwa familia zao.”

Shirika hilo limeziomba nchi wafadhili zinazotoa misaada kuhusu ukuaji wa demokrasia na utawala bora ziangalie kama ina umuhimu kwa sasa kutokana na nchi wanayoifadhili kutoheshimu utawala bora.

Monday, September 10, 2012

Nchi ya kitu kidogo, nchi ya watu wadogo


NI dhahiri kwamba nchi inaweza kuwa ndogo lakini watu wake wakawa wakubwa, wakati ambapo nchi inaweza kuwa kubwa na watu wake wakawa wadogo. Hapa nazungumzia nchi yenye ukubwa wa ardhi na ukubwa wa idadi ya watu. Wakati mwingine sifa hizi zinaweza pia kuambatana na nchi kuwa na rasilimali kubwa na nyingi za kutosha.

Ziko nchi kubwa kwa maana ya ukubwa wa ardhi na watu na pia rasilimali maridhawa, lakini ambazo watu wake wamebakia kuwa wadogo, na mataifa yaliyoundwa na watu hao yakawa ni madogo pia. Hizi ni jamii na nchi za watu wapuuzi. Nchi ambazo kwa ukubwa wa maili za mraba na ukubwa wa idadi ya watu ni ndogo lakini zikawa na watu wakubwa na mataifa yake yakawa makubwa ni nchi za watu walio makini.
Napenda kuvitaja vielelezo kadhaa vinavyodhirisha kiwango cha juu cha upuuzi ndani ya jamii au nchi ambayo inakuwa kubwa kwa eneo la maili za mraba, wingi wa watu na rasilimali kubwa.

 Mojawapo ya vielelezo vikubwa vya upuuzi unaoweza kufanywa na jamii au nchi ni pale nchi au jamii inaposhindwa kutumia rasilimali zake kwa manufaa ya watu wake na badala yake ikaziruhusu zikaendelea kuwanufaisha wageni wakati watu wake wanaendelea kudhalilika.

Aina hii ya nchi kimsingi ni nchi iliyokosa uongozi na ikawa inaendeshwa na watawala ambao ama hawana uwezo ama hawana utashi wa kuwaongoza watu wao kuelekea katika maendeleo ya kweli. Mara nyingi hawa ni watawala wanaotawaliwa na uroho wa utajiri binafsi na ambao muda wao mwingi watakuwa katika shughuli za kujikusanyia mali wasiweze kufikia masuala magumu ya maendeleo ya watu wao.

Aghalabu pia watawala wa aina hii watakuwa ni wapagazi wa mabwana wao kutoka nje, hawa wakiwa ni watu binafsi, serikali, makamupuni ya biashara na asasi za kiulinzi na kijasusi. Watawala wa aina hii wanawatumikia wageni na hawana haya kuonyesha hali hiyo. Ndio wale ambao kila wakishutumiwa kwa hili au lile wanakuwa wepesi kusema, “Mbona huko nje wanatushangilia?” Kana kwamba “huko nje’ ndiko kulikowachagua.

Mwisho wa siku watawala kama hawa hupoteza haiba (kama waliwahi kuwa nayo), huonekana zaidi wakijipendekeza kwa wageni, na huanza pole pole kuwaogopa watu wao kwa sababu hawana majibu kw maswali wanayoulizwa na watu wao ambao hawawezi kuelewa ufukukara wao unasababishwa na nin katika mazingira ya utajiri mkubwa. Na wala hawawezi kuelewa ubadhirifu unaofanywa na watawala ambao maelezo yao ya siku zote ni hali ngumu ya uchumi duniani.

Hawa ndio watawala wa nchi kama Zaire/Kongo niliowajadili majuzi, na ndio watawala wa nchi kama Nigeria. Zote hizi mbili ni nchi kubwa zenye watu wadogo zinaotawaliwa na watawala walafi. Haziwezi hata kidogo kuwa mataifa makubwa hata zingekuwa na utajiri mkubwa kiasi gani.

Nje ya bara la Afrika, ni nchi kama Urusi ambayo baada ya kusambaratika kwa himaya ya Sovieti (ambayo nayo ilikwisha kupoteza pumzi mapema) imekuwa ikijikokota chini kabisa ya utajiri ilio nao na uwezo wa watu wake. Leo Warusi ni watu wadogo, na taifa lao ni dogo likilinganishwa na ‘potensho’ yake. (Vijana wa Kenya waliimba: “Nchi ya kitu kidogo, nchi ya watu wadogo”).

Upande mwingine tunaona mataifa makubwa yaliyojengeka ndani ya nchi ndogo, kama Botswana na Mauritius, nchi zenye rasilimali kidogo lakini zenye uongozi makini ambazo zimeweza kuwafanya watu wake wawe wakubwa na watambulike hivyo duniani.

Katika historia ya dunia ya karne kadhaa zilizopita tunajifunza kwamba ‘kijinchi’ kama Uingereza, ambacho hakikuwa na lo lote wakati huo, kikiwa kimefungwa katika kisiwa ambacho kwa nusu ya mwaka kimeganda na barafu, kiliweza kutawala nusu ya dunia ya wakati ule na kuwaweka mamilioni ya wanadamu chini ya himaya yake kutoka mashariki hadi magharibi, kaskazini hadi kusini.

Ni jambo gani liliifanya Uingereza iweze kuitawala dunia, kutawala Bara Hindi pamoja na watu wengi wale, tena wenye mapokeo na utamaduni wa fahari? Ni nguvu ya kujiamini, kuamini katika uwezo mkubwa wa jamii na uongozi wake na kuamini katika uwezo usiotishika wala kutikisika mbele ya adui au mpinzani ye yote.

Imani hii katika uwezo wa Uingereza ilipandikizwa akilini na mioyoni mwa watoto wa Uingereza tangu wakiwa ‘nkeremeke’ (neno la Kihaya linalomaanisha kichanga) na imani ambayo walikuwa nayo ikawa ni silaha kubwa kila walikokwenda kupora nchi za watu wengine ili kuiletea fahari himaya ya Uingereza.
Hawakuendekeza watawala wala rushwa na wasaliti wa watu wao, na angalau mara moja mfalme wao alipodhihirika kutaka kuwakandamiza walizua uasi na wakamkamata na kumkata kichwa. Katika msukumo wa kutafuta fahari ya Uingereza hawakuvumilia upuuzi.

Mzee mmoja wa Uingereza aliyewahi kufanya kazi kama mtawala wa kikoloni nchini Tanganyika aliniambia kuwa siku ya kwanza shuleni walikusanywa kwenye gwaride la shule nzima na mkuu wa shule akawaambia:
‘Nyie watoto mna bahati kwani mmezaliwa mkiwa Waingereza. Hiyo ina maana mmeshinda bahati nasibu ya kwanza katika maisha yenu.”

Nani anaweza kuwaambia watoto wa Tanzania kitu kama hicho leo hii? Katika mazingira mengi watoto wanaweza hata kumzomea kwa sababu hawaoni ni nini hasa kiwafanye waone fahari ya kuwa Watanzania, watu wenye mashaka katika kila idara ya maisha yao, wanaoongozwa na watawala ambao wanaelekea bado wanatafuta kuelewa ni nini hasa maana ya uongozi?

Jamii au nchi inakuwa ya kipuuzi iwapo ina kila aina ya rasilimali lakini rasilimali hizo haziisaidii jamii wala nchi kuendelea wala kuwa jamii au nchi ya furaha. Furaha ndani ya jamii si lazima itokane na maendeleo makubwa ya kiuchumi na ujenzi wa vitu kama barabara na majumba. Hivi ni muhimu, lakini si kila kitu. Zipo jamii duniani ambazo kwa vigezo hivi zinaitwa jamii masikini, lakini viwango vyake vya furaha viko juu sana.
Hizi ni jamii ambazo zimeridhika na hali ya maisha kwa sababu zimeweza kujenga utangamano kati ya rasilimali zilizopo na mafanikio ya kimaisha ya watu wake. Mathalan, jamii inaingiza kipato cha shilingi kumi, kila mwanajamii analijua hilo, halafu jamii inanufaika kwa kiwango cha shilingi kumi, na kila mwanajamii analijua na kulielewa hilo, na wanajamii wote, isipokuwa mwendawazimu, wanaridhika.

Jamii inajihatarisha yenyewe iwapo itafanya kinyume cha hilo, iwapo, mathalan, itaingiza kipato cha shilingi kumi kisha ikaruhusu shilingi moja tu itumike kwa manufaa ya jamii halafu jamii isijue shilingi tisa zilizobaki zimetumika vipi. Hata kama hakuna wizi au ubadhirifu katika matumizi bado misingi ya vita itakuwa imekwisha kujengwa kutokana na nakisi ya taarifa, uwazi, uelewa na maridhiano.

Maridhiano ni tunda la maelewano na maelewano ni tunda la kueleweshana katika uwazi. Uwazi unapopungua na sehemu ya jamii ikahisi kwamba inadhulumiwa au haitendewi haki unakuwa ndio mwanzo wa chokochoko na mfarakano.

Uwezo wa kuchagua umo ndani yetu. Tunaweza kuchagua kuwa nchi kubwa kwa maana ya eneo la maili za mraba na idadi kubwa ya watu (na rasilimali nyingi na kubwa) lakini papo hapo tukawa taifa la wapuuzi, tukajulikana hivyo duniani, au tukachagua kuwa taifa dogo kwa vigezo vya ukubwa wa ardhi, idadi ya watu na rasilimali lakini tukatumia rasilimali hizo ndogo, udogo wa idadi ya watu wetu na udogo wa eneo la mraba la nchi yetu kuwa (na kutambulika kama) taifa kubwa.

Ni kuchagua baina ya kuwa kama Uingereza ama kuwa kama Zaire/Kongo.

Friday, September 7, 2012

Mauaji Ya Raia Yataathiri Mchakato Wa Katiba Mpya

TAMKO LA JUKWAA LA KATIBA TANZANIA DHIDI YA MAUAJI YA MWANDISHI DAUDI MWANGOSI

‘‘Mauaji Ya Waandishi Na Wananchi YatavurugaMchakato Wa KupataKatiba
Mpya Tanzania!’’

JUKWAA LA KATIBA TANZANIA tumepokea taarifa za kuuawa kinyama

kwaMwandishi Daudi Mwangosi wa Channel 10na Mwenyekiti wa Chama cha
waandishi wa Habari mkoani Iringa (IPC) kwa mshtukona masikitiko
makubwa. Kama ilivyokwishaelezwa na wengi, kifo cha mwandishi huyu ni
cha kwanza cha aina yake katika tasnia ya habari nchini na kinatishia
si tu uhuru wa kutoa maoni na uhuru wa habari kwa ujumla wake, bali
pia kifo hiki na vingine vya siku za karibuni vinauweka mchakato wa
Katiba Mpya njia panda. Vitendo vya mauaji ya raia vinazidi kushamiri
siku hadi siku. 


Wapo wananchi wanaouawa na watu wanaoitwa wenye hasira
kali kwa tuhumaza uhalifu. Wapo raiawanaouliwa na majambazi na
wahalifu wenginekwa sababu ya ulinzi duni katika maeneowanayoishi.
Aidha, wapo pia wananchi wanaopoteza maisha yao kila siku kwa tuhuma
za kwamba ni wachawi.Ukiacha hao, idadi kubwa ya watanzania wanaishi
na ulemavu wa ngozi wamepotezamaisha kwa kukatwa viungo au kuuliwa
kabisa kwa imani za kishirikina. Hali sasa imefikia kuwa mbaya hadi
kuna watanzania wanajisikia salama zaidi wakiwa mwituni kuliko
majumbani. Yote haya yanasikitisha sanakwa ujumla wake! Haki ya kuishi
inayowekwa na kulindwa na ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania imeanzakuingia dosari katika Tanzania.Ukiacha mauaji
yanayofanywa na watu wasiojulikana au miongoni mwa raia, yamekuwepo
pia mauaji yanayozidi kuongezeka ya raia yanayofanywa na wawekezaji au
matajiri nchini. Zipo kesi kadhaa za mauaji ya namna hii.

Hayo nayo yamekuwa yakitokea kwa sababu ya ulinzi mdogo ambao wananchi

wanao kutoka kwa vyombo vya ulinzi na usalama nchini. Jeshi la Polisi,
ambalo ndio lenye dhamana ya kulinda watu na mali zaohaliwezi kukwepa
lawama katika aina zote hizo za mauaji. Itakumbukwa pia kuwa ajali za
magari, mabasi na meli zinagharimu sanamaisha ya watanzania katika
siku za karibuni. Kwa kiasi fulani, hata kukithiri kwa ajali hizi nako
kunahusishwa na mwenendo mbovu wa usimamizi wa vyombo vya usafiri
unaofanywa na idara mbalimbali za serikali ikiwemo kikosi cha usalama
barabarani. 


 Roho zawatanzania zinazidi kupotea kutokana na udhaifu mkubwa unaosababishwa na rushwa na mambo mengine ya ukosefu wa maadili
katika vyombo vya usimamizi wa haki. Mauaji ya raia yanayofanywa moja
kwa moja naaskari wa Jeshi la Polisi nayo yanazidi kuongezeka
sanakiasi cha kutishia amani na utulivu wa nchi yetu. Aidha, mauaji
yanayohusishwa na siasa nayo yanazidi kuongezeka na kuzidisha chuki ya
kisiasa ambayo ni mbaya sana kwa ustawi wa nchi yetu. Kwa mfano katika
miezi ya Karibuni, kumekuwepo matumizi ya nguvu kuzidi kiasi kwa raia
wanaokuwa wakipanga na kufanyamaandamano au mikusanyiko yenye lengo la
kujadili au kupinga jambo fulani. Matokeo yake, kumetokea majeruhi na
mauaji ambayo yamesababishwa na vurugu ambazo zinatokana na Jeshi la
Polisi kudhibiti vitendo halali vya wananchi. Kwasababu hiyo, JUKWAA
LA KATIBA TANZANIA tunatoa witoufuatao kwa Jeshi la Polisi na idara
nyingine za serikali zenye dhamana ya kulinda usalama wa raia, malina
mipaka ya Nchi yetu:

1. Jeshila Polisi liache kutumia nguvu kuzidi kiasi katika matukio

yote ya kulinda mikutano na matukio ya hadhara. Tujuavyo sisi, Jeshi
la Polisi linalotumia risasi za moto, mabomu ya kivita, maji ya
kuwasha na gesi ya kutoa machozi dhidi ya raia ambao hawajabeba hata
fimbo za kuchungia mifugo. Ni Jeshi lisilojiamini na linaloonesha woga
wa ajabu. Kwa hadhira kama za Nyololo, Morogoro, Mbeya, Dar es Salaam
na nyinginezo miezi yaKaribuni, Jeshi la Polisi lingeweza kuwatuliza
wananchi kwa kutumia filimbi tu. Matumizi ya nguvu na kumwagia maji ya
kuwasha hata wazee wastaafu wanaodai haki zao inaweza kuwa ndio laana
inayopelekea Polisi kusikia furaha kuua kila mara. Ipo kanuni ya
kimataifa inayowataka Polisi kutumia nguvu kidogo sana inayolingana tu
na nguvu ya umma wanaokabiliana nao katika kutuliza ghasia.

2.Wakati huu wa mchakato wa kutengeneza Katiba mpya ya Tanzania na

hata baada ya hapo, Jeshi la Polisi lijiepushe kuingilia shughuli za
Kisiasa kwa kuziunga mkono au kuzivuruga. Mikusanyiko mingi ambayo
imepelekea mauaji wakati polisi ikijaribu kuivunja ni matukio
yaliyolenga kupata majibu ya kisiasa na siyo ya kipolisi. Wajibu wa
Jeshi la Polisi

katika wakati kama huo ni kulinda na kuwezesha wananchi husika kueleza

madaiyao kwa uhuru na bila kuvurugwa na kundi jingine lolote la watu
wasiopendezwa na madai ya kundi husika. Tabia inayozidi kushamiri ya
Jeshi la Polisi kutaka kujibu au kuzima hoja za Kisiasa au kiuchumi
kwa mtutu wa bunduki, mabomu, maji ya kuwasha na virungu ni tabia ya
Jeshi kutaka kuingilia kazi isiyo yake na ndio maana inawashinda.
Aidha, kama Polisi wangekuwa niwataalam wa Siasa, wangegundua kuwa
wanachokifanya ni kuahirisha matatizo na si kuyatatua!

3. Jeshi la Polisi na vyombo venye dhamana ya ulinzi vijitambue upya

kuwa vina wajibu wa kulinda raia, mipaka na mali zao si vinginevyo.
Mauaji yanayoendelea nchini ni uporaji wa haki ya kuishi na haki
nyingine nyingi chini ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzaniana
ile ya Zanzibar.Aidha, Jeshi la Polisi na serikali kwa ujumla wana
wajibu wa kuhakikisha na kudumisha ustawi wa wananchi kwa mujibu wa
ibara ya 8 (1) (b) nahawana mamlaka ya kuua raia. Ikumbukwe kuwa
mamlaka yote kikatiba katika Tanzaniayako kwa wananchi na serikali
pamoja na Jeshi lake la Polisi watapata madaraka na mamlaka hayo
kutoka kwa Wananchi. Nani amewapa Polisi mamlaka ya kuua watanzania?
Nani amewapa Jeshi la magereza mamlaka ya kuwapiga na kumwaga damu za
Waandishi? Nani amewapa askari wanyamapori mamlaka ya kupiga risasi
hovyo nakuua ng’ombe mbele ya wenye maliyao?

4.Athari za matukio ya mauaji na fujo zinazosababishwa na Jeshi la

Polisi kutawanya waandamanaji au mikusanyiko mingine ni kubwa sana
katika kuathiri vibaya hamasa ya wananchi kwenye Mchakato wa Katiba.
Mpaka sasa, tayari watu wengi wameingia wasiwasi na wameamua
kutoshiriki mikutano ya kutoa maoni ya Katiba inayoendeshwa na Tume ya
Mabadiliko ya Katiba nchini. Endapo Jeshi la Polisi halitaacha kuua na
kutishiaraia kwa kila wanachokifanya, mchakato wa Katiba utavurugika
kabla Katiba mpya haijapatikana. Kwa mwenendo wa sasa, Jeshi la Polisi
litakuja kupiga mabomu na kuua hata wananchi watakapokuwa katika
Mabaraza ya Katiba wakijadili na kupinga baadhi ya vipengele
vitakavyoingizwa katika rasimu ya Katiba. Pia, itafika wakati wananchi
watataka kuandamana kwa amani kuunga mkono au kupinga mambo Fulani
katikaKatiba. Kwa hali ilivyo, Jeshi la Polisi litaona hiyo ni fursa
ya kutumia mabomu na risasi kuzuia wasiseme wanayotaka kusema. Hii ni
hatari kubwa sana!

5. Mikusanyiko, maandamano na shughuli za mikutano ya Siasa ni matendo

halali na haki ya kila mtanzania kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya
Muungano, 1977 ibara ya 8, 20 na 21. Suala la kutoa taarifa kwaJeshi
la Polisi kwa mujibu wa sheria ya Jeshi la Polisi ni suala la
kuwajulisha tu kwa lengo la kuwaweka tayari endapo kutahitajika msaada
wa Jeshi la Polisi wakati wa shughuli kamahiyo. Tabia iliyoota mizizi
ya Polisi kujiona kama wamepewa taarifaili watoe au kukataa kibali ni
uelewa finyu wa Katiba na sheria za Nchi. Ipo haja ya kuongeza uelewa
wa wasimamizi wetu wa sheria ili wawe na uelewa mpana wa sheria na
ibaraza Katiba wanazozisimamia badala ya kujiona kama wana wajibu wa
Msajili wa vyama vya Siasa wa kuratibu shughuli za vyama. Mikutano,
mikusanyiko, mihadhara, maandamano na mijadala ni haki ya Kikatiba ya
Kila mtanzania binafsi na kwa makundi. Kwa kuwa haki ya kuishi
iliyoporwa kwa MwandishiDaudi Mwangosi ndio haki kubwa kuliko zote,
JUKWAA LA KATIBA TANZANIA tunataka jambo hili lisiishiekuunda Tume za
uchunguzi pasipo kufanyia kazi mapendekezo yake. Aidha, kwa kuwa
uchunguzi unaofanywa hauhusiani na kilichomuua ndugu Mwangosi wala
kundi gani limemuua, tunapendekeza busara itumike kwa viongozi wa
Jeshi la Polisi, kuanzia Kamanda wa Polisi Mkoawa Iringa kuachia ngazi
ili kupisha uchunguzi huru wa Tume itakayoundwa na Mheshimiwa Rais
ikihusisha na kuongozwa na mhimili wa Mahakama. Taarifa ya uchunguzi
ipelekwe Bungeni na Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kujadiliwa na ushauri
wa kibunge. 

Kamati iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi
tunaitamka rasmi kuwa batili kwa kutumia kanuni ya sheria za kiasili
inayosema kuwa mtu au kundi hawezi kuwahakimu wa kesi inayomhusu
mwenyewe. Bila kufanya hivyo, tunapata wasiwasi kama Tume ya namna
hiyoinaweza kufanya kazi yake kwa uhuru. Kuachia ngazi kwa Kamanda wa
Polisi mkoani Iringa kutakuwa ishara kuwa Jeshi la Polisi linahitaji
kuwa makini zaidi katika kufanya kazi yake ya kulinda amani, mali na
maisha ya watanzania. Kwa sasa, zipo hisia kuwa Jeshi la Polisi lipo
juu ya sheria na Katiba, jamboambalo tunapenda kulikanusha vikali!

Mwisho, tunapenda kutoa rai kwa serikalikutangaza rasmi kuwa itachukua

jukumu la kutunza, kusomesha, kulisha na kuhudumia familia aliyoiacha
Daudi Mwangosi kuanzia sasa kwa muda wa miaka 20 watakapoweza
kujitegemea wenyewe. Itakuwa ni fedheha kuiona familia aliyoianzisha
Marehemu Mwangosi ikisambaratika kwa sababu kichwa cha nyumba hiyo
kimesambaratishwa na bomu la Polisi ambalo kodi yake
Mwangosiilichangia kulinunua. Kufikia hapa, tunapenda kutangaza rasmi
kuwa msiba huu nimsiba wa KIKATIBA na tunaomba ufahamike hivyo kwa
umma wote wa watanzania na kote duniani.

Mungu ailazeroho ya Marehemu Mwanahabari Daudi Mwangosi mahali pema

peponi Amina!

Imetolewana kusainiwa kwa niaba ya JUKWAA LA KATIBA TANZANIA,

Deus MKibamba
Mwenyekiti
Alhamis, 06 Septemba 2012

Mahakama Kuu Yaamuru Tanesco iwalipe Dowans

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetupilia mbali maombi ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kutaka isitishe utekelezaji wa malipo ya Sh96 bilioni kwa Kampuni ya Kufua Umeme ya Dowans kutokana na kuvunja mkataba wa kibiashara kinyume na sheria.

Kufuatia uamuzi huo, Tanesco sasa inatakiwa kuilipa Dowans kiasi hicho cha fedha ambacho kwa ujumla kinaliongezea shirika hilo mzigo wa madeni.

Tanesco kupitia mawakili wake Rex Attorneys iliwasilisha mahakamani hapo maombi mawili; kibali cha kukata rufaa kupinga hukumu ya Mahakama hiyo iliyotolewa Septemba 28, 2011 na kuomba kusimamishwa kwa utekelezwaji wa hukumu hiyo.

Katika hukumu ya awali iliyotolewa na Jaji Emilian Mushi, mahakama hiyo ilikubali maombi ya Tuzo kwa Dowans iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICC), Novemba 15, 2010.
ICC iliamuru Tanesco kuilipa Dowans fidia ya Dola za Marekani billion 65,812,630.03, kutokana na kuvunja mkataba wa kibiashara kinyume cha sheria. Mahakama Kuu Tanzania ilikubaliana na tuzo hiyo na kuipa kampuni hiyo nguvu ya kisheria.

Hata hivyo, Tanesco haikuridhika na hukumu hiyo, badala yake ikawasilisha mahakamani hapo taarifa ya kusudio la kukata rufaa kuipinga.

Jana, kwa mara nyingine mahakama hiyo iliendelea kubariki Dowans kupewa tuzo hiyo na kutupilia mbali maombi ya Tanesco, ikiwamo pingamizi la utekelezaji wake.
Katika uamuzi wake aliousoma jana asubuhi, Jaji Dk Fauz Twaib alikubaliana na hoja za Wakili wa Dowans, Kennedy Fungamtama kwamba mahakama hiyo haina mamlaka kisheria kusimamisha utekelezaji wa malipo hayo baada ya hukumu ya ICC.

Awali, wakili Fungamtama katika hoja zake, alidai kuwa maombi hayo yamefunguliwa chini ya Kanuni ya 11 (2) na ya 47 ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania ya mwaka 2009.
Alidai kuwa kanuni hiyo ya 47 inatumika kwa maombi ambayo Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu nchini zina mamlaka ya kisheria lakini, katika maombi hayo ya Tanesco kusimamisha utekelezaji wa malipo hayo, mahakama kuu haina mamlaka hayo.

Kwa mujibu wa Fungamtama, kanuni ya 11(2) (b) ya kanuni za Mahakama ya Rufani za 2009, zinaihusu Mahakama ya Rufani tu na kwa maana hiyo, ni Mahakama ya Rufaa pekee ndiyo inaweza kusimamisha utekelezwaji wa malipo.
Hata hivyo, wakili wa Tanesco aliyejitambulisha kwa jina la Mwandambo akijibu hoja za Wakili Fungamtama alidai kuwa, kanuni hizo zinaipa nguvu mahakama hiyo kusimamisha utekelezaji wa malipo iliyotolewa katika mahakama hiyo ambazo zinakatikwa rufaa katika Mahakama ya Rufaa.

Lakini, Jaji Dk Twaib alikubaliana na hoja za wakili Fungamtama kwamba kifungu cha kanuni ambacho Tanesco ilikitumia katika maombi hayo, hakiipi mamlaka Mahakama Kuu kusimamisha utekelezaji wa hukumu zake.
Jaji Dk Twaib alisema kuwa, namna na masharti ya kusimamisha utekelezaji wa hukumu yalivyoainishwa katika kifungu (d) cha kanuni hizo za Mahakama ya Rufani.

Alisema kama Wakili Fungamtama alivyoeleza kwa usahihi, kanuni hizo zinaihusu Mahakama ya Rufaa tu kama ilivyoainishwa vizuri katika Kanuni ya 3 ya Kanuni za Mahakama ya Rufaa za mwaka 2009.

“Mheshimiwa Jaji Mkuu anatambua msimamo wa kisheria uliowekwa katika maamuzi mbalimbali kwa misingi kwamba, mchakato wa rufaa unapokuwa umeanza kwa kuwasilisha taarifa ya kusudio la kukata rufaa, mahakama hii inakoma kuwa na mamlaka ya kusimamisha utekelezaji wa hukumu,”, alisema Jaji.
Jaji Dk Twaib alisema mahakama hiyo inaweza kuwa na mamlaka hayo kabla kuwasilisha taarifa ya kusudio la kukata rufaa.

“Mara tu taarifa ya kusudio la kukata rufaa inapokuwa imewasilishwa (kama ilivyo katika kesi hii), Mahakama Kuu inakoma kuwa mamlaka,” alisisitiza Jaji Dk Twaib na kuongeza:

“Kwa misingi iliyoelezwa mahakama hii haina mamlaka ya kisheria kushughulikia maombi ya kusimamisha utekelezaji yaliyowasilishwa na muombaji (Tanesco)”, alihitimisha uamuzi wake Jaji Dk. Twaib.

Sakata lenyewe Mwaka juzi jopo la majaji watatu wa ICC lilitoa uamuzi wa kuitaka Tanesco kuilipa Dowans Tuzo ya Sh96 bilioni, kutokana na madai ya kuvunja mkataba wa kibiashara kinyume cha sharia. Hata hivyo, uamuzi huo umekuwa ukipingwa na baadhi ya watu wakisema Dowans ilirithi mkataba haramu wa Richmond hivyo, mkataba huo haukuwa halali.

Tanesco nayo kwa upande wake, katika maombi yake ilidai kuwa kama mchakato wa utekelezaji wa hukumu hiyo utaendelea, itaathiri uwezo wake wa kuzalisha na kusambaza umeme nchini na hivyo kusababisha tatizo kubwa la ukosefu wa umeme nchini na hivyo kuathiri uchumi wa nchi kwa jumla.

Pia lilidai kuwa iwapo maombi yao hayatakubaliwa itapata hasara kubwa na hivyo kuathiri kwa kiwango kikubwa utendaji wake na hata kuleta wasiwasi wa kusimama kwa shughuli zake za kila siku. Mawakili hao walisihi mahakama hiyo kuzingatia maombi hayo kwa madai kuwa hasara itakayotokana na tatizo la ukosefu wa umeme itakuwa ni kubwa na isiyoweza kufidiwa kwa namna yoyote ile.

Walidai kuwa ingawa taarifa ya kusudio la kukata rufaa siyo kigezo cha kuzuia utekelezaji huo, lakini kwa hoja za kesi yake ni nzito kiasi cha kutosha kuifanya mahakama kutumia uwezo wake wa kisheria kuzingatia maombi yao. “Mahakama ina uwezo wa kuamuru kusimama kwa utekelezaji huo kwa namna itakavyoona inafaa.”, walisisitiza mawakili hao wa Tanesco katika maombi hayo.

Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/habari

Wednesday, September 5, 2012

Tamko Rasmi La MISA Tanzania Kuhusiana Na Kifo Cha Mwandishi Daudi Mwangosi

TAARIFA KWA UMMA / VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KUUAWA KWA MWANDISHI WA HABARI WA CHANNEL TEN NA MWENYEKITI WA KLABU YA WAANDISHI WA HABARI MKOA WA IRINGA (IPC) DAUDI MWANGOSI

Tasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Nchi za Kusini mwa Afrika (MISA Tan) imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha mwandishi na kiongozi mahiri wa waandishi hapa nchini.

Aidha tunaungana na waandishi na wafanyakazi katika tasnia ya habari nchini, Jumuiya ya Klabu za Waandishi nchini (UTPC) pamoja na familia ya marehemu Mwangosi katika kipindi hiki kigumu ambacho tasnia yetu ya habari imelazimika kuingia matatani kutokana na matumizi ya mabavu ya Jeshi la Polisi.

Tunalaani kwa nguvu zote matumizi ya mabavu ya polisi ambayo yamesababisha kifo cha mwandishi wa habari akiwa kazini na pia akiwa chini ya ulinzi wa Polisi. Tunatambua uhasama kati ya Polisi wa mkoa wa Iringa dhidi ya waandishi wa habari uliodumu kwa muda mrefu.

Uhasama huu kiini chake ni kutokana na matumizi ya nguvu kupita kiasi yanayotekelezwa mkoani Iringa na hivyo kila mara waandishi wanaporipoti habari wanaingia katika mlolongo wa uhasama na vituko vya mara kwa mara. Hatimaye polisi kwa makusudi wameamua kuua mwandishi. Hili ni doa ambalo litaichukua Tanzania kujisafisha machoni pa jumuiya ya kimataifa.

Huu ni mwendelezo wa matumizi ya nguvu kupita kiasi yanayofanywa na polisi kwa raia wa nchi hii. Ni lini polisi watasimamia ulinzi wa raia na mali zao badala ya kugeuka kuwa jeshi la mauaji kila wananchi wanapokusanyika kwa minajili ya kutimiza ndoto zao?

Kifo cha Mwangosi kimegubikwa na sintofahamu hasa ukijua kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa Bwana Michael Kamuhanda alikuwa anamtambua kama kiongozi wa waandishi wa habari mkoa na alikuwepo kwenye tukio wakati Mwangosi akiwa mikononi mwa polisi, na kuuliwa mbele yake.

Lakini ikumbukwe kuwa siku zote hata katika vita waandishi wanafanya kazi bega kwa bega na askari ili kuwajuza wananchi nini kinachotokea kwenye uwanja wa mapambano. Kwa jeshi la polisi hapa nchini limedhihirisha kuwa baada visa na mikasa kuwatokea raia wa kawaida sasa wamewageukia waandishi wa habari na kukatisha maisha yao kikatili.

Sasa Polisi wamevunja daraja lililokuwa linawanganisha wananchi na serikali yao. Hii itazidisha chuki ya wananchi dhidi ya serikali yao kuliko kipindi kinginecho chote.

Ikumbukwe pia kuwa wakati mauaji haya yanatokea kuna mkutano mkuu wa UTPC unaoanza wiki hii huku wawakilishi wa vyama vya waandishi wa mbalimbali wa kimataifa wakitegemea kushiriki katika mkutano huo wa mwaka. Na hii itatoa taswira halisi ya jinsi Jeshi la Polisi linavyofanya kazi hapa nchini.

Jumuiya ya kimataifa itaweza kujionea hali halisi jinsi waandishi wa habari hapa nchini wanavyofanya kazi katika mazingira hatarishi na kwamba sasa Tanzania inawezekana isiwe mahali salama pa kuishi kama walivyokuwa wakisikia kwenye vyombo vya habari vya kwao. Mfano halisi ni mhanga Daudi Mwangosi ambaye ataingia katika vitabu vya kumbukumbu duniani kwa mwaka 2012.

Tunaiomba serikali ichukue maamuzi makini ya kukaa pamoja na vyama vya siasa ili kutafuta njia muafaka ya kutuliza mikusanyiko ya wananchi kwa njia za amani na sio kutumia mabavu katika kuwatawanya.

Ni imani yetu kuwa historia imeonyesha kuwa nguvu kupita kiasi kwa wananchi inaongeza chuki dhidi ya serikali yao ya wakati huo na kamwe hainyamazishi dukuduku zilizoko mioyoni mwa wananchi. Kokote kule duniani matumizi ya polisi yalipovuka mipaka yakaamsha hasira za wananchi na kuzifanya nchi hizo zisikalike.

Matumizi ya mabavu, nguvu kupita kiasi kuzima vuguvugu za wananchi kwa kile wanachokiamini pamoja na mauaji na hasa kwa wanahabari na raia wasio na silaha hayajawahi kufanikiwa kokote kule duniani.

Tunaamini kuwa serikali yetu ni sikivu na itachukua hatua stahiki. Pamoja na kwamba uchunguzi huru sio utamaduni wa serikali yetu lakini katika hili la mwandishi akiwa na kalamu na kamera yake afie mikononi mwa polisi tunahitaji uchunguzi huru na wa kina.

Taasisi yetu imetoa ubani wa shilingi laki tano (500,000/-) kwa familia ya marehemu Mwangosi. Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi. Amen!

Tumaini Mwailenge
Mkurugenzi,
MISA Tanzania

Tuesday, September 4, 2012

SEMINA: Katiba na Mtazamo wa Vijana Juu ya Huduma za Jamii, Ushiriki Katika Jamii na Upiganiaji Haki Zao: Matokeo ya utafiti wa TAMASHA



SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

 UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII 

Richard Mabala na timu ya TAMASHA  WATAWASILISHA

MADA  Katiba na Mtazamo wa Vijana Juu ya Huduma za Jamii, Ushiriki Katika Jamii na Upiganiaji Haki Zao: Matokeo ya utafiti wa TAMASHA

Lini: Jumatano Tarehe 5/9//2012

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI:  Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni  


WOTE MNAKARIBISHWA

Wanahabari Dodoma walaani mauaji ya Mwangosi

CHAMA cha waandishi wa habari Mkoa wa Dodoma (CPC) wamelaani vurugu zilizotokea juzi mkoani Iringa na kusababisha kifo cha mwandishi wa habari wa kituo cha utangazaji cha Chanel Ten Daud Mwangosi. Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa chama hicho Habel Chidawali alipokuwa akitoa tamko hilo mbele ya waandishi wa habari mkoani hapa.

Chidawali amesema kuwa kamwe chama hicho hakikubaliani na nguvu kubwa iliyotumiwa na jeshi la polisi kwa ajili ya kumwaga damu ya mwandishi huyo ambaye hakuwa na hatia na kamwe Jeshi la Polisi haliwezi kujitetea kwa kudai kifo cha mwandishi huyo ni bahati mbaya.

Amesema kuwa jeshi la polisi limekuwa liki onesha wazi wazi kuwa linatumia nguvu, ubabe na matumizi mabovu ya silaha za moto ambayo hayajaweza kusaidia siku zote na badala yake kinachoachwa ni maumivu na vilio kwa wananchi. Katibu huyo amesema kama Jeshi la Polisi linatuliza ghasia hakuna siku hata moja haijatokea wakamuua kiongozi yoyote wa siasa ambao ni vinara wa mikutano mbalimbali.

Kwa upande wao wananchi mbalimbali mkoani hapa wamekemea nguvu kubwa inayotumika na Polisi katika vurugu mbalimbali zinazotokea. Wamesema tabia ya Jeshi la Polisi kutumia nguvu na silaha za moto
ambazo zinasababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia.

Catheline Muhinte, amesema kuwa tukio lililofanywa na Jeshi la Polisi la kumuua mwandishi wa habari linaonyesha dhairi kuwa kwa sasa jeshi hilo linafanya kazi kwa kukiuka maadili ya malengo yao.
Amesema katika mwonekano wa picha ambazo zinaonekana katika vyombo mbalimbali vya habari inaonyesha dhairi kuwa polisi walihusika moja kwa moja na kifo cha mwandishi huyo.