Thursday, November 29, 2012

Jaji chande aikwepa kesi ya Lema

JAJI Mkuu wa Tanzania, Mohamed Othman Chande amejitoa kusikiliza rufaa ya kesi ya aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, badala yake nafasi yake imechukuliwa na Jaji Bernard Luanda.
Kujitoa kwa jaji mkuu kumekuja ikiwa zimebaki siku tano kusikilizwa upya kwa rufaa hiyo Desemba 4, mwaka huu, baada ya awali Mahakama ya Rufani, kuona rufaa hiyo ilikuwa na dosari.
Mahakama hiyo ilikubali hoja ya wajiburufaa kuwa rufaa hiyo ilikuwa na dosari kutokana na tofauti ya vifungu vya sheria vilivyotumika katika hukumu iliyomvua ubunge Lema na vilivyotumika katika hati ya kukaza hukumu, iliyowasilishwa mahakamani sambamba na rufaa hiyo.
Hata hivyo, kilichomwokoa Lema ni kifungu cha 111 cha Kanuni za Mahakama, ambapo mahakama hiyo ilisema kuwa chini ya kanuni hiyo, dosari hizo zinaweza kurekebishwa.
Jaji Chande ndiye aliyekuwa kiongozi wa jopo la majaji watatu katika kesi hiyo akiwamo Salum Massati na Natalia Kimaro.
Jaji Mkuu aliingia kwenye kesi hiyo akichukua nafasi ya Jaji Mbarouk Salim Mbarouk aliyekuwa amepangwa awali, ambaye sababu za kuondolewa hazikuwekwa wazi.
Wakili wa  Lema, Method Kimomogoro alithibitisha kuwa amepata taarifa kuwa jaji mkuu hatasikiliza rufaa hiyo na badala yake Jaji Luanda ndiye atachukua nafasi yake.
“Ni kweli jaji mkuu hatakuwapo kusikiliza rufaa ya Lema nimewasiliana na Msajili Dar es Salaam ameniambia hatokuwepo kwenye hilo jopo,” alisema Kimomogoro na kuongeza:
Hata hivyo, Wakili Kimomogoro alisema “Huu ni utaratibu wa kawaida wa mahakama kwa kuwa huenda jaji mkuu akawa amesafiri au ana shughuli nyingine.”
Wakili wa wajiburufaa, Alute Mughwai alisema hajapata taarifa kama Jaji Mkuu ameondolewa kwenye jopo hilo kwa kuwa huo si utaratibu wa mahakama kutoa taarifa hizo.
“Mahakama huwa haitoi taarifa, zinawekwa (taarifa) kwenye ubao wa mahakama siku ambayo rufaa inasikilizwa,” alisema.
Aliendelea, “Jaji yeyote atakayepangwa sisi hatuna tatizo kwa kuwa wote ni majaji, wewe uko huko Dar na mimi niko huku bara (Arusha), hivyo unaweza ukazipata taarifa zaidi huko kwa kuwa ndiyo uko jikoni Dar.”

Tuesday, November 27, 2012

MAADHIMISHO YA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA




BIG BANG          BIG BANG             BIG BANG

UNAKARIBISHWA KATIKA JUKWAA LA WAZI LA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII MTOA MADA NI  TGNP/GDSS  

MADA: SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA   

Lini: Jumatano Tarehe 28/11/2012

Muda: Saa 03:00 Asubuhi7:00 Mchana
 
MAHALI:  Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni  


WOTE MNAKARIBISHWA


Hotuba Ya Mwenyekiti Wa WILDAF Kwenye Uzinduzi Wa Kupinga Ukatili Wa Kijinsia...!

Ukumbi wa Diamond Jubilee, TAREHE 26/11/2012

Ndugu Mgeni Rasmi, Naibu Waziri wa Sheria na  Katiba,Mheshimiwa, Angelah Kairuki,

Mheshimiwa  Balozi wa Ireland, Fionnula Gilsenan

Waheshimiwa wawakilishi wa Balozi mbalimbali,

Mheshimiwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Said Mwema,

Wawakilishi wa Mashirika wahisani,

Ndugu Viongozi Vyama na Serikali,

Waandishi wa habari,

Wageni waalikwa,

Mabibi na mabwana,

Itifaki imezingatiwa.

Kwa niaba ya wanachama wa WiLDAF Tanzania na kwa niaba ya Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) na  Kikosi kazi cha kuandaa maandalizi ya siku 16 za Kupiga Vita ukatili wa kijinsia, ningependa kuchukua fursa hii kuwakaribisha rasmi kwenye uzinduzi huu wa Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia.

Tunatoa shukrani za pekee kwako mgeni rasmi kwa kuitikia wito wetu wa kuja kujumuika nasi katika uzinduzi huu na hasa ukizingatia kwamba una majukumu mengi, na nyeti yanayohusu taifa letu.

Kweli unatuthibitishia kwamba wewe ni mwanaharakati mwenzetu.

Ndugu mgeni Rasmi,

Aidha ningependa kuchukua nafasi hii kipekee kabisa kulishukuru kwa namna ya pekee Shirika la Msaada la Ireland (Irish Aid), Shirika la Msaada la Marekani  USAID, UN –Women  na CONCERN kwa kutupa uwezo wa kiuchumi ili kuweza kuadhimisha siku hii.

Tunapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru washiriki wote kwa kujumuika nasi katika uzinduzi wa Siku hizi 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia kwa mwaka huu 2012.

Ndugu mgeni rasmi,

Naomba uniruhusu nikufahamishe kwa ufupi tu kuhusu  chimbuko la kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia. Kampeni hii ilianzishwa rasmi mnamo mwaka 1991 na Taasisi ya Kimataifa  ya Wanawake  katika  Uongozi, huko nchini Marekani kwa nia ya kuamsha ari ya kuzuia na kupambana na ukatili dhidi ya wanawake kwa kuzingatia haja  ya kuleta usawa wa kijinsia.

Ndugu mgeni rasmi,
Kampeni hii ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia  inaanza rasmi tarehe 25 Novemba ambayo ilichaguliwa na Umoja wa Mataifa mwaka 1999 kuwa ni SIKU YA KIMATAIFA YA KUPINGA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE . Hivyo basi, Umoja wa Mataifa unashauri serikali, mashirika ya Kimataifa na asasi zisizo za kiserikali kufanya shughuli zinazolenga kufahamisha jamii juu ya ukatili dhidi ya wanawake.Wanawake duniani kote wamekuwa wakikumbwa na ukatili ikiwemo kubakwa, vipigo, ukatili majumbani, ukeketaji na aina mbalimbali za ukatili. Tarehe hii ni ya kihistoria kwani ni kumbukumbu ya mauaji ya kinyama waliofanyiwa kina dada wa Mirabelle nchini Dominika mwaka 1960.  Wanawake hawa  waliuawa kikatili kwa kuwa walikuwa  wanapinga utawala wa kidikteta wa Rais wa nchi ya Dominika (1930-1961) Rafael Truijilo na kutetea haki  katika jamii yao.  Wakina dada hawa walifanyiwa vitendo vingi vya kudhalilishwa utu wao na mwishowe Raisi Rafael Truijilo aliamua wauawe.  Aidha Kampeni hii inahitimishwa tarehe 10 Desemba  ambayo  ni siku ya Kimataifa ya  TAMKO LA HAKI ZA BINADAMU ikiwa ni ishara ya kuhusisha ukatili dhidi ya  wanawake na  haki za binadamu na  kutia msisitizo kwamba ukatili kama huu ni uvunjwaji wa haki za binadamu.

Ndugu mgeni rasmi,
Kati ya tarehe 25 Novemba na Desemba 10 kuna matukio mbali mbali ya kimataifa kama ifuatavyo:-

-  Tarehe 29 Novemba ni Siku ya Kimataifa ya Watetezi wa Haki za Wanawake.

-  Desemba 1 ni siku ya UKIMWI duniani.

-  Desemba 6 ni siku ya kukumbuka mauaji ya kikatili ya wanawake wahandisi mjini Montreal, Canada.

Ndugu mgeni rasmi,
Kwa kipindi cha tangu mwaka 1991 inakadiriwa kiasi cha nchi 156 duniani na mashirika zaidi ya 2,000 yanashiriki katika kampeni hii ya siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia kwa kufanya yafuatayo:-

-    Kuhamasisha jamii juu ya ukatili wa kijinsia na masuala yanayohusu haki za binadamu katika ngazi ya kitaifa, kikanda na kimataifa.

-   Kuimarisha mshikamano wa kupambana na vitendo vyote vya ukatili  dhidi ya wanawake.

-   Kuanzisha ushirikiano wa dhati kati ya wanaharakati wa ndani na nje ya nchi ili kutokomeza ukatili wa kijinsia.

-  Kuandaa jukwaa lenye kuleta fursa ya kubadilishana  mawazo, uzoefu na kuweka mikakati thabiti kwa pamoja ya kupambana na ukatili wa kijinsia.

-  Kuonesha mshikamano wa wanawake duniani kote na kuwa na sauti ya pamoja  katika kupinga ukatili dhidi ya wanawake.

-    Kuunganisha nguvu za wanawake pamoja ili iwe nyenzo thabiti kuishawishi serikali kutekeleza ahadi walizoweka ili kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake.

Ndugu mgeni rasmi,
Nchini Tanzania katika  Siku hizi 16, mashirika, taasisi na idara mbali mbali chini ya  mwamvuli wa Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI), Kikosi Kazi cha kuratibu maadhimisho ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia yakiratibiwa na  WiLDAF yanaungana na wapenda haki wote duniani kuwakumbuka  wanawake na wasichana wote walioathirika na vitendo vya ukatili kama vile kupigwa, kubaguliwa kijinsia, kukeketwa, kuuawa, wajane kunyang’anywa mali, kunyimwa haki ya kumiliki ardhi na kadhalika.  Ni dhahiri kwamba, ukatili wa kijinsia ni dhana  pana inayogusa jinsi zote lakini kwa kiasi kikubwa wahanga  wakubwa wa ukatili huu ni wanawake.
Ndugu mgeni rasmi, kampeni ya mwaka huu imekuwa na muitikio mkubwa na msisimko wa aina yake kwani wadau wengi wamejitokeza katika kampeni hii. Mathalani, Jeshi la Polisi limekuwa na ushiriki mkubwa na wa kipekee. Kwa kutilia mkazo na kutekeleza nguzo ya Polisi Jamii, Jeshi la Polisi linaungana nasi kwa kufanya shughuli mbali mbali za kuhamasisha amani na usalama katika makazi yetu na maeneo ya barabarani. Kwa kutumia fursa ya rasilimali watu ambayo jeshi la Polisi linayo, watatoa elimu ya athari na madhara ya ukatili, watahamasisha jamii kukemea vitendo vyote viovu vinavyosababisha ukatili kwani ukatili wa kijinsia ni kosa la jinai na pia unachochea uvunjwaji wa amani katika nyumba zetu na Taifa kwa ujumla. Napenda kutumia fursa hii kulipongeza Jeshi la Polisi kwa kuchukua hatua hizi. Pia nampongeza Mkuu wa Jeshi la Polisi Inspecta Generali Said Mwema kwa juhudi kubwa anazofanya. Inatupa faraja kubwa sisi wanaharakati kuona Jeshi la Polisi limevalia njuga kampeni hii. Hii inatoa ishara nzuri kwamba kwa kushirikiana nasi basi tutaweza kuutokomeza ukatili dhidi ya wanawake.
Ndugu Mgeni Rasmi, pamoja na Jeshi la Polisi, Mashirika mengine yanayoshirikiana nasi na yana shughuli mbalimbali katika kipindi hiki cha kampeni ya Siku 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake ni kama ifuatavyo,
  • World Vision watakuwa na kampeni kuhusu afya ya mtoto sasa itakayofanyika Hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro, Kempiski
  • Chama cha Wanawake Wanasheria (TAWLA) watakuwa na mjadala kuhusu ukatili wa kijinsia tarehe 29 katika ukumbi wa Diamond Jubillee
  • Equality for Growth (EFG) watakuwa na uzinduzi wa kupiga vita ukatili wa kijinsia kwa kutembelea masoko mbalimbali ya wilaya ya Ilala, tarehe 5/12/2012
  • Engender Health/Champion Project watakuwa na uzinduzi wa kupiga vita ukatili wa kijinsia tarehe 6/12/2012 kwa kutembelea vijiji 20 vya mkoa wa Iringa
  • Children Dignity Forum (CDF) watatoa msaada wa kisheria mkoa wa Pwani. Pia wataendesha shughuli mbalimbali kupiga vita ukeketaji tarehe 8/12/2012 katika wilaya ya Tarime mkoa wa Mara.
  • Pamoja na mashirika mengine Action Aid, Concern, CSOs coalition na YWCA watakuwa na shughuli mbalimbali za kupinga vita ukatili wa kijinsia.
  • Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu wataadhimisha siku ya Tamko Rasmi la Haki za Binadamu na kuhitimisha maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa Kijinsia.
Ndugu Mgeni Rasmi, uwepo wetu leo hapa katika kuadhimisha uzinduzi wa kampeni ya Siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia unaambatana na shughuli mbalimbali zikiwemo za kutoa msaada wa kisheria kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, maonesho ya programu mbalimbali za asasi zinazolenga kutokomeza ukatili wa kijinsia, mada mbalimbali zinazohusiana na ukatili wa kijinsia. Aidha uzinduzi huu una shughuli mbili za kipekee. Kwanza uzinduzi wa Fomu ya Polisi namba 3 (PF 3), Fomu hii mpya ya Polisi imefanyiwa maboresho na kuongezewa vipengele muhimu pamoja na mambo mengine vinavyohusu ukatili wa kingono. Ni imani yetu kubwa kuwa Fomu hii mpya ya Polisi ni nyenzo muhimu na itasaidia katika ushahidi na hivyo kurahisisha upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia.
Ndugu Mgeni rasmi

 Shughuli nyingine ya kipekee ni uzinduzi wa msafara wa kupinga ukatili wa kijinsia (CARAVAN). Msafara huu umebeba Mabalozi kutoka makundi mbalimbali ya wanaume, wanawake, vijana na walemavu. Mabalozi hawa watatoa ujumbe na kuhamasisha jamii za kitanzania kukemea vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia. Aidha, wataunganisha nguvu za pamoja kwa kuhamasisha jamii zetu kuwa kila mtu mwanaume awe au mwanamke ana wajibu wa kukemea na kuchukua hatua dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Msafara huu utatembea katika kanda tatu (3) ambazo ni kanda ya Kaskazini, Mkoa wa Kilimanjaro, Kanda ya Kati, Mkoa wa Singida, na Kanda ya Ziwa, Mkoa wa Mara-Tarime, ambapo takwimu zinaonesha kuna kiwango kikubwa cha ukatili dhidi ya wanawake hususan ukeketaji. Ni matarajio yetu makubwa kuwa msafara huu utakuwa ni chachu kubwa katika jamii zetu kuanza kuzungumza na kutoa taarifa ya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake. Aidha utaamsha ari kwa jamii zetu kuweza kukemea vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia

Ndugu mgeni rasmi 
Kampeni hii ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia itafanyika kikanda. Kanda hizo ni Kanda ya Ziwa (Mwanza, Mara, na Shinyanga) chini ya usimamizi wa Shirika la KIVULINI na ABC Foundation, Kanda ya Kaskazini (Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga) chini ya usimamizi wa NAFGEM,  Kanda ya Kati (Dodoma, na Singida) chini ya usimamizi wa  AFNET, Kanda ya Kusini (Mtwara, Songea, Mbeya, Iringa na Lindi) itaadhimisha  shughuli hii chini ya kituo cha wasaidizi wa kisheria Iringa na Kanda ya  Kaskazini (Tabora na Kigoma) chini ya Jeshi la Polisi wakishirikiana na WiLDAF. Aidha kampeni hii mikoani inazinduliwa rasmi leo  26/11/2012.

Ndugu Mgeni Rasmi,
Tunafahamu kuwa serikali ya Tanzania imefanya juhudi mbalimbali za kuzuia na kutokomeza vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia.  Juhudi hizi ni pamoja na kutengeneza mpango mkakati  wa kitaifa wa  kuzuia na kupambana na ukatili wa kijinsia wa mwaka 2001,  kutunga sheria na sera  mbalimbali zinazolenga kuleta usawa kwa mfano:-

-          Dira ya Maendeleo  ya mwaka 2025.

-          Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000 inayolenga kuwaendeleza wanawake kijamii, kiutamaduni, kiuchumi na kisiasa.

-        Sheria ya Kanuni Za Adhabu Sura Na. 16 hususan vipengele vya makosa ya kujamiiana

-          Sheria ya Ardhi Na. 4 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5, zote za mwaka 1999 kama zilivyorekebishwa mwaka 2002 zinazolenga kutoa haki sawa ya umiliki wa ardhi kati ya wanaume na wanawake.

-         Mkakati wa Kitaifa wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia unaolenga kuwa na jamii isiyokuwa na aina yoyote ya ukatili ifikapo 2015.

Ndugu Mgeni Rasmi,
Pamoja na jitihada zote hizi nzuri zinazofanywa na serikali, vitendo vya  ukatili wa kijinsia bado vinakithiri katika jamii zetu. Hivyo basi, tuna sababu za makusudi kabisa kuishirikisha jamii katika kuzuia ukatili wa Kijinsia kwani kwa kiasi kikubwa jamii imekuwa ikichochea au ikikubali uwepo wa ukatili wa kijinsia.

Mathalani katika utafiti uliofanywa na WiLDAF mwaka 2012 katika magazeti, unaoonesha kwamba taarifa 6,001 za ukatili wa kijinsia zimeripotiwa kwenye magazeti ikilinganishwa na taarifa 3,542 za mwaka 2011.

Ndugu Mgeni Rasmi, vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake sio tu kwamba  vinawadhoofisha kiafya, bali pia vinaathiri  uwezo wao wa kushiriki na kuchangia katika kuleta maendeleo kiuchumi ndani ya familia zao na nchi kwa ujumla.
Aidha, jitihada za serikali katika kupunguza umaskini chini ya mkakati wa kuzuia na kutokomeza umaskini (MKUKUTA) na malengo ya Maendeleo ya Millenia (MDG) hasa lengo kuu la tatu hayataweza kufikiwa iwapo hakutakuwa na mikakati ya makusudi ya kuhakikisha kuwa ukatili dhidi ya wanawake unatokomezwa.

Ndugu mgeni rasmi mwaka huu kauli mbiu yetu ni “FUNGUKA! KEMEA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE. SOTE TUWAJIBIKE” Kauli mbiu hii ina maana kwamba sote tunatakiwa kuamka katika masuala ya kuzuia Ukatili. Ni vema kutafakari kwa kina  jinsi ambavyo ukatili wa kijinsia, hususan ukatili dhidi ya wanawake unavyoathiri maendeleo ya familia na nchi kwa ujumla. Sote tunafahamu jinsi jamii inavyofumbia macho vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia vinapotokea, jamii kwa kiasi kikubwa haitoi ushirikiano kwa vyombo husika kuhakikisha tatizo hili linapotea.. Hatuwezi kuwa na Taifa imara bila kutokomeza ukatili wa kijinsia.  Hivyo basi, kauli mbiu inaweka msisitizo kuwa ni wajibu wa kila mmoja wetu kuzinduka na kukemea ukatili dhidi ya wanawake ili kudumisha taifa imara.
Ndugu Mgeni Rasmi,  katika utekelezaji wa kuzuia na kupambana na Ukatili  wa Kijinsia nchini Tanzania, WiLDAF pamoja na mashirika/taasisi  zingine zinazotetea haki za binadamu zinakabiliana na changamoto zifuatazo:-
  1. Mgongano wa sheria mbalimbali na sheria kandamizi ambazo bado zinatumika, Aidha ukosefu wa sheria mahususi dhidi ya ukatili majumbani.
  2. Ushiriki mdogo wa jamii katika kujihusisha katika utetezi na kukabiliana na matatizo ya ukatili wa kijinsia, hususan ukatili dhidi ya wanawake.
  3. Ukosefu wa fedha za kutosha za kutoa mafunzo na kujenga uelewa wa umma katika masuala ya ukatili wa kijinsia.
  4. Mtazamo hasi ndani ya jamii unaopelekea kuhalalisha vitendo vya ukatili  wa kijinsia uliojijenga kwenye mfumo dume.
  5. Ushiriki duni/hafifu wa Wizara mbali mbali na hivyo kutokutoa kipaumbele suala la ukatili wa kijinsia katika wizara zao.
  6. Ukosefu wa takwimu za kutosha kuhusu masuala yanayohusiana na ukatili wa kijinsia
  7. Ukosefu wa huduma bora za afya katika vituo vya afya kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia mathalani sehemu za kuwahifadhi waathirika hao.
  8. Uelewa mdogo na kutotilia maanani suala zima la ukatili wa kijinsia kwa watoa huduma katika jamii.
  9. Uchelewashaji wa kesi za ukatili wa kijinsia hivyo kupelekea waathirika kukata tama na kutokuwa na ushirikiano katika kutoa ushahidi na upatikanaji wa haki.

Ndugu mgeni rasmi
Pamoja na changamoto hizo bado tunayo nafasi ya kurekebisha  hali  iliyopo. Hivyo basi sisi wadau wa kupinga ukatili wa kijinsia  tunaiomba wizara yako kuangalia mambo yafuatayo:-.

-          Kuchukua  hatua za makusudi za kutunga  sera zinazolenga kuleta usawa,  kubadilisha/kurekebisha Sheria ya Ndoa na kutunga sheria mpya ya mirathi pamoja na Sheria  dhidi ya  ukatili nyumbani.

-          Tunaomba Wizara yako iunde kitengo maalumu katika mahakama cha kusimamia kesi za ukatili wa kijinsia, ili kuwezesha upatikanaji wa haki kwa haraka, kwani haki inayocheleweshwa ni sawa na haki iliyonyimwa.

-          Wizara izidi kuweka msukumo ili serikali itenge fedha na rasilimali za kutosha kwa ajili ya kuelimisha wanajamii juu ya haki na wajibu wao kwa mujibu wa sheria na sera zilizopo. Pia kutoa fedha kwa mashirika yanayotetea haki za binadamu hususan haki za wanawake.

-          Serikali kuanzisha sehemu maalumu kwa ajili ya hudma za waathirika wa ukatili wa kijinsia (one stop centre)

-          Serikali ijenge hifadhi zitakazohudumia waathirika wa ukatili wa kijinsia

Mwisho kabisa tunakutakia kila la kheri katika shughuli zako na Mungu akubariki.


                              Mh. Naomi A.M. Kaihula

                                           MWENYEKITI

Monday, November 26, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI: Shilingi Bilioni 86 zaibwa Wizara ya Nishati/TANESCO, Gridi ya Taifa hatarini

Gazeti la The East African la Novemba 24 – 30, 2012 limetoa taarifa kwamba jumla ya dola za kimarekani milioni 54 zimegundulika kuibwa na watumishi waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la TANESCO kupitia manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mtambo wa Umeme wa IPTL. Gazeti hili limenukuu taarifa ya ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Tanzania (Controller and Auditor General). Taarifa hiyo inasema kuna kikundi (racket) ambacho kazi yake kubwa ni kujifaidisha binafsi na mpango wa umeme wa dharura kupitia manunuzi ya Mafuta mazito ya IPTL.
Itakumbukwa kwamba toka mwaka 2011 kumekuwa na shinikizo lililotolewa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwamba zabuni za ununuzi wa mafuta ya kuendesha mpango wa umeme wa dharura na mchakato mzima wa manunuzi ya mafuta haya ufanyiwe uchunguzi wa kina (forensic audit).

Katika mkutano wa 3 wa Bunge la Kumi (April 2011) niliuliza swali Bungeni kuhusu kashfa hii ya ununuzi wa mafuta ya kuendesha mtambo wa IPTL na baadaye tarehe 16 Aprili 2011 nilimwomba Spika airuhusu Kamati ya Nishati na Madini kufanya uchunguzi kuhusu kashfa hii. Kamati ya Nishati na Madini chini ya aliyekuwa Mwenyekiti ndugu January Makamba ililitaka Bunge kuazimia kufanyika kwa uchunguzi kuhusu suala hili kwenye Taarifa yake ya mwaka 2011 iliyowasilishwa Bungeni mwezi Aprili mwaka 2012. Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ndugu John Mnyika katika Hotuba yake ya Bajeti ya Wizara hiyo mwaka 2011 alipendekeza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu kashfa hii pia. Juhudi zote hizo hazikuzaa matunda.

Kipindi hicho kiwango kilichokuwa kinahojiwa kuibwa ni shilingi bilioni 15 tu. Taarifa ya The East African kama walivyonukuu kutoka kwenye taarifa ya CAG inaonyesha fedha zilizoibwa ni shilingi bilioni 86.
Zabuni za kununua mafuta ya kuendesha umeme wa dharura zimekuwa zikitolewa bila kufuata utaratibu wa zabuni kwa mujibu wa Sheria ya manunuzi. Hivi sasa kila mwezi Tanzania inatumia dola milioni 70 kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme.

Fedha hizi zinatoka Hazina na sehemu ndogo kutoka TANESCO. Wakati fedha hizi bilioni 112 zinachomwa kila mwezi kununua mafuta mazito na dizeli ya kuendesha mitambo ya umeme, Taarifa za kitaalamu zinaonyesha kwamba Bwawa la Mtera hivi lina kina cha maji chini ya kiwango kinachotakiwa na uzalishaji wa umeme ni asilimia 20 tu ya uwezo (installed capacity). Iwapo TANESCO wataendelea kutumia zaidi maji yaliyopo Mtera, Mitambo itashindwa kazi na Gridi nzima itasimama maana Mtera ndio nguzo kuu ya Gridi ya Taifa. Hali hii ni hatari sana kwa uchumi na ulinzi na usalama wa Taifa. Kimsingi Gridi ya Taifa ipo hatarini kutokana na kiwango cha Maji kilichopo Mtera hivi sasa na kuendelea kupungua kwa kina hicho cha maji.

Wananchi wanapaswa kuelezwa kinaga ubaga nini kinaendelea katika sekta ndogo ya umeme hapa nchini;

1.      Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kuhusu zabuni za manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura iwekwe wazi na ‘racket’ inayosemekana kuiba jumla ya shilingi bilioni 86 ionyeshwe na hatua za kisheria zichukuliwe mara moja na bila kuchelewa.

2.      Waziri wa Nishati na Maadini auleze umma hali yalisi ya sekta ya umeme nchini, uzalishaji wa umeme upoje, hali ya maji katika bwawa mkakati la Mtera na nini hatma ya mitambo ya IPTL, kesi zake na utekelezaji wa mapendekezo ya Bunge kuwa kesi za kampuni hii zimalizwe nje ya mahakama. Pia Taifa lielezwe Mpango wa Dharura wa umeme unakwisha lini maana muda uliotolewa na Bunge mwezi Agosti mwaka 2011 tayari umekamilika. Waziri aeleze hatua agni amechukua baada ya kukabidhiwa taarifa na CAG kuhusu maafisa waandamizi wa Wizara waliohusika na wizi wa shilingi bilioni 86 za kununua mafuta ya IPTL.

3.      Waziri wa Fedha na Uchumi aueleze umma ni kiwango gani cha fedha Hazina imetoa kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura kati ya Mwezi Novemba mwaka 2011 na Oktoba mwaka 2012 na kama taratibu zote za zabuni zilifuatwa na pale ambapo hazikufuatwa ni hatua gani PPRA wamechukua dhidi ya waliokiuka sheria ya manunuzi na kuleta hasara ya mabilioni ya fedha kwa Serikali.

Kabwe Zuberi Zitto, Mb
Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha
Dar es Salaam. Novemba 25, 2012

Friday, November 23, 2012

TGNP Yawaasa Wananchi Kushiriki Mchakato wa Katiba Mpya

Mkurugenzi wa TGNP Usu Mallya akizungumza

Baadhi ya Washiriki wa Tamasha


Kikundi cha sanaa na maigizo kikitoa Igizo

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Usu Mallya akijumuika na Wananchi wa Mkambarani kucheza Ngoma
MKURUGENZI Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Usu Mallya amewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika uundwaji wa Katiba mpya ili itakapo kamilika sera na sheria za nchi ziendane na wananchi wake, jambo ambalo litasaidia kutatua migogoro anuai.

Mkurugenzi huyo aliyasema hayo jana eneo la Mkambarani mje kidogo ya Mji wa Morogoro ambapo linafanyika tamasha la Jinsia katika ngazi ya wilaya lililoandaliwa na TGNP, kuchochea juhudi za wananchi hasa waliopo pembezoni kushiriki katika mchakato wa maendeleo yao.

Akizungumza katika mkutano huo unaowashirikisha wanavijiji kutoka baadhi ya vijiji vya Mkoa wa Morogoro na baadhi ya mikoa ambao ni wanaharakati wa ngazi za jamii, alisema ushiriki wa wananchi ipasavyo katika mchakato huo itasaidia mabadiliko ya mfumo wa uandaaji wa sera na sheria ili zisiendelee kulalamikiwa na wananchi.

“Mfumo uliopo sasa yawezekana kabisa ukawa na upungufu, ndio maana hata kwa sasa baadhi ya maeneo yanapata huduma za kijamii huku maeneo mengine yakilegalega kihuduma,” alisema.

Alitolea mfano eneo la Mkambarani wananchi wanalalamikia migogoro ya ardhi hali hiyo inachangiwa na mfumo katika mgawanyiko wa rasilimali ikiwemo ardhi, ambapo baadhi ya makundi yamekuwa yakisahaulika huku wajanja wakineemeka na mifumo hiyo.

Alisema wananchi wanapaswa kushirikishwa kwa karibu katika uandaaji wa sera na sheria na pia kushirikishwa kwenye mipango ya maendeleo ili kuondoa mkanganyiko ambao hujitokeza hapo baadaye. “Wananchi lazima tushirikishwe katika mipango ya maendeleo…tukumbuke kwamba hakuna sera na sheria inayonihusu mimi bila mimi kushirikishwa,” alisema Mallya.

Aidha aliwataka wanawake na wapenda mabadiliko kushiriki katika vuguvugu la kupambana na mfumo dume na kandamizi ambao kwa kiasi kikubwa unawaathiri akina mama. “Tukubali kuwa huu ni mchakato wa mabadiliko, tukatae uonevu na kupambana na mifumo yote kandamizi kwa kutumia umoja wetu pamoja na ushirikiano…umefika wakati wa kushirikiana katika masuala ya maendeleo, tusiishie kwenye harusi na misiba tu,” aliongeza.

Tamasha la jinsia ngazi ya wilaya linalofanyika nje kidogo ya mji wa morogoro linatarajiwa kumalizika leo jioni ambapo washiriki kwa pamoja watatoka na maazimio ambayo yatafanyiwa kazi kulingana na mahitaji.


Thursday, November 22, 2012

Tamasha La Jinsia Mkambarani Lafana

Mgeni rasmi na Mkuu wa Chuo cha Jinsia Dkt Diana Mwiru wakifuatilia

Wananchi wa Morogoro walioshiriki Tamasha wakiendelea kusikiliza watoa mada

TAMASHA la Jinsia Ngazi ya Wilaya linalofanyika Kijiji cha Mkambarani-Morogoro limeanza rasmi kwa kufunguliwa kwa mjadala wa wazi uliotoa nafasi kwa washiriki kushirikishana maswala anuai ya kijamii.

Mada Kuu ya Tamasha hilo inasema; "Haki ya Uchumi, Rasilimali Ziwanufaishe Wanawake Walioko Pembezoni". Tamasha hilo linaendelea kwa siku tatu mfululizo nje kidogo ya Mji wa Morogoro, eneo la Moseka-Mkambarani, ambapo wananchi mbalimbali pamoja na wanaharakati ngazi ya jamii wanahudhuria kuchangia mada mbalimbali zinazotolewa eneo hilo.


Masuala yaliyoibuka kwenye Tamasha la jana ni pamoja na migogoro ya ardhi kati ya wananchi na wanakijiji wa eneo la Mkambarani dhidi ya wawekezaji wanaoingia kutaka kuwekeza hasa kwenye mashamba.


Baadhi ya wananchi wameomba viongozi wa juu kuingilia mgogoro wa ardhi uliopo kati ya wananchi na taasisi ya Islamic Foundation, ambapo inadaiwa wananchi kuyaachia mashamba yao waliyokuwa wakilima awali ili yachukuliwe na taasisi hiyo.

Wananchi hao wakizungumza kwa nyakati tofauti wameomba zifuatwe taratibu kama kuna wawekezaji wanataka kuingia kwenye ardhi ya wanakijiji ili mazungumzo yafanywe na Serikali ya kijiji na si vinginevyo.


Tamasha hilo linaendelea tena leo na linatarajiwa kufikia kikomo Ijumaa ya wiki hii.

Wednesday, November 21, 2012

Mabadiliko Ya Sheria Ya Habari Yasiachiwe MCT Pekee

Na: Daniel Mbega, Iringa
KWA takriban miaka 20 sasa, wadau wa habari wamekuwa wakipiga kelele kuhusu kuwepo kwa Uhuru wa Habari, hasa Uhuru wa Vyombo vya Habari na Wanahabari kwa ujumla wake.

Jitihada za kelele hizo ndizo hasa kimsingi zilizozaa Baraza la Habari Tanzania (MCT), ambalo lilisajiliwa rasmi mwaka 1997 likiwa na majukumu mbalimbali, ikiwemo kuwasimamia wanahabari nchini.

Hata hivyo, pamoja na majukumu mengi iliyonayo, MCT kwa kushirikiana na wadau wengine kama Misa-Tan, Tamwa, Nola, LHRC, TLS, TGNP, Leat, TEF, TUJ, na wadau wa nje kama Article 19 ya Uingereza na Commonwealth Human Rights Initiatives (CHRI) ya India, imekuwa ikipigania kutambuliwa rasmi Kikatiba kwa Uhuru wa Haki ya Kupata Habari pamoja na Uhuru wa Vyombo vya Habari.
Hali hii inatokana na ukweli kwamba, Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, haitaji wala kuvitambua moja kwa moja vyombo vya habari na wanahabari, pamoja na kutambua uhuru wa kutoa maoni na kujieleza.

Vuguvugu hilo ndilo lililotoa shinikizo kwa Serikali kuandaa Muswada wa Uhuru wa Kupata Habari wa mwaka 2006 ambao uliainisha haki ya kupata habari, huduma za vyombo vya habari, faragha, ulinzi kwa watoto na kashfa, ingawa serikali hiyo hiyo iliweka vifungu kadhaa vinavyominya usajili wa vyombo vya habari, jambo ambalo limeendelea kuzua mgongano mkubwa na wadau wa habari. 

Tuesday, November 20, 2012

Jaji Warioba: Wananchi zaidi ya 900,000 watoa maoni Katiba Mpya

Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, amesema hakuna chombo chochote kilichowahi kuwafikia watu wengi nchini zaidi ya tume yake, ambayo hadi awamu ya tatu ya kazi yake ya kukusanya maoni inamalizika, imekwishafikiwa na wananchi zaidi ya 900,000 kutoa maoni kuhusu Katiba Mpya katika mikoa 24 ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kwa lengo la kutoa tathmini baada ya tume yake kumaliza awamu ya tatu na kuendelea na awamu ya nne, ambayo ni ya mwisho ya kazi yake ya kukusanya maoni ya wananchi kuhusu Katiba Mpya.

Alisema katika awamu zote hizo, tume imefanya jitihada kubwa kuhakikisha inakutana na kila kundi katika jamii, wakiwamo makundi tisa ya watu wenye ulemavu, ambao alisema wote wamepata maoni yao.
“Hakuna chombo kilichowahi kupata watu wengi kama tume hii. (Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania, Deus Kibamba) Aniambie ni chombo gani katika nchi hii kilichowahi kuwafikia watu wengi? Anataka tume ifanye kazi kulingana na mawazo yake na siyo kwa kufuata sheria,” alisema Jaji Warioba.
Alisema awamu ya tatu ya kazi ya tume yake ilifanyika kuanzia Oktoba 8 hadi Novemba 6, mwaka huu katika mikoa ya Rukwa, Njombe, Iringa, Singida, Tabora, Mtwara, Kilimanjaro, Kaskazini Unguja na Kaskazini Pemba.

Jaji Warioba alisema awamu ya kwanza ilifanyika kati ya Julai 2-30, mwaka huu na kwamba, ilihusisha mikoa ya Dodoma, Kagera, Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Pwani, Shinyanga na Tanga.
Alisema katika awamu ya pili, iliyofanyika kuanzia Agosti 27 hadi Septemba 28, mwaka huu, tume ilitembelea mikoa ya Kigoma, Lindi, Mwanza, Morogoro, Mbeya, Katavi na Ruvuma.
Jaji Warioba alisema katika awamu ya tatu iliyomalizika Novemba 6, tume ilifanya mikutano 522 katika mikoa yote tisa ingawa ilipanga kufanya mikutano 496.

Alisema hali hiyo ilitokana na mahitaji mapya katika maeneo mbalimbali ya mikoa hiyo na kuifanya tume kuitisha mikutano ya ziada ili kuwapa fursa wananchi wengi zaidi.
Jaji Warioba alisema katika awamu ya pili, tume ilifanya mikutano 449 wakati awamu ya kwanza ilifanya mikutano 388.

Alisema katika awamu ya tatu, wananchi 392,385 walihudhuria mikutano na kwamba, wananchi 21,512 walitoa maoni yao kwa kuzungumza katika mikutano hiyo na wananchi 84,939 walitoa maoni ya kwa maandishi.

Aidha, alisema katika awamu hiyo, wananchi 1,639 walitoa maoni yao kwa kuzungumza na pia kwa maandishi katika mikutano hiyo.

Kutokana na hali hiyo, alisema tume inaridhika na kazi inavyoendelea na namna wananchi wanavyojitokeza kutoa maoni kwa njia mbalimbali zilizotolewa na tume.

Alisema tume yake haitaingilia misimamo ya vyama vya siasa vinavyominya uhuru wa wafuasi wao kutoa maoni na kusema kazi ya tume ni kuchukua maoni na kwamba, yeyote anayetoa maoni popote aliko watayachukua.  
CHANZO: NIPASHE

Monday, November 19, 2012

Tume Ya Mabadiliko Ya Katiba Itakuwa Ilala...!


CCM Kurejesha Imani Ya Chama, Kuwaengua Walioingia Kwa Rushwa Madarakani

SEKRETARIETI mpya ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyoingia madarakani hivi karibuni chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete, imesema itahakikisha vitendo vya rushwa hasa kwenye chaguzi za chama hicho vinakoma mara moja, tofauti na ilivyokuwa imezoeleka.

Kauli hiyo ya viongozi wa juu wa CCM, Mwenyekiti Taifa (Rais Kikwete), Makamu Mwenyekiti Tanzania Bara (Phillip Mangula) na Katibu Mkuu (Abdulrahman Kinana) imetolewa jana na viongozi hao wakati wakizungumza na wana-CCM Mkoa wa Dar es Salaam katika mkutano wa kumpongeza Rais Kikwete kuchaguliwa kushika nafasi hiyo tena.

Akizungumza na umati wa wanachama hao, Rais Kikwete aliwataka viongozi wapya kufanya kazi ya ziada ya kuhakikisha wanarejesha imani ya Watanzania kwa CCM, ambayo haiko kama ilivyokuwa zamani.
“Lazima kujiuliza nini kimekifanya chama hiki kufikia hapo kilipo na kuangalia nini cha kufanya ili kuondokana na hali hiyo. Pale mnapohisi hali ya kuungwa mkono inapungua lazima tujiulize, kulikoni..! Nini cha kufanya ili kuimarisha chama,” alisema na kuongeza kuwa kazi nyingine ni kuhakikisha wanakijenga chama na kuimarisha zaidi ili kiendelee kuwaongoza Watanzania.
“Chama chetu hakifanyi mikutano…wenzetu wanafanya kwanini sisi hatufanyi, sasa tutatengeneza utaratibu maalumu kuhakikisha viongozi wa chama kwa nafasi zao wanafanya kazi yao ipasavyo ndani na nje ya chama,” alisema Rais Kikwete.
Alisema ipo haja ya kujipanga na kuangalia namna ya kupambana na propaganda hasi za baadhi ya vyombo vya habari na wapinzani ili kukabiliana na hali hiyo. Aliwataka wanaCCM kuacha makundi na chuki ambayo yamekuwa yakikigawa chama hicho. 
Awali akizungumza Kinana alisema vitendo vya rushwa ndani ya CCM watahakikisha vinakoma mara moja ili kurejesha imani ya Watanzania iliyopungua kutokana na tuhuma za wachache dhidi ya vitendo viovu.
Alisema chini ya uongozi wake atahakikisha mashaka yaliotawala kwa wananchi dhidi ya CCM yanaondoka kwa kuwaengua wale wanaoendeleza vitendo vya rushwa, majumbu na vitendo vinavyo leta sifa mbaya ya chama hicho.
“Hatuwezi kuiongoza nchi yetu wakati watu wanamashaka na sisi, lazima tuondoe mashaka akisimama mwana-CCM wote waseme naam huyu anaweza kusema…sio akisimama mwana-CCM kusema watu wanahoji haaah, na huyu naye anakemea rushwa? 
Aliwataka wana-CCM kushirikiana katika kukisafisha chama na si kuwaachia viongozi jukumu hilo, ambalo wao kama viongozi wamekubali kuongoza mapambano hayo.
Alisema CCM ina wanachama milioni 5 ambao asilimia 99.9 wengi wakiwa ni masikini na waadilifu huku asilimia 0.1 wakiwa ni wala rushwa wakubwa, wapenda mizengwe, wapendeleaji hivyo kujikuta idadi hiyo ikikichafua chama chote jambo ambalo alisema chini ya uongozi wao hawawezi kuacha hali hiyo iendelee.
Alisema atahakikisha anasimamia ilani ya chama vizuri huku kanuni mbalimbali zikifuatwa ili kuleta haki ndani ya chama hicho, alisema kuna kazi kubwa ya kukijenga chama hicho,
Alisema pamoja na viongozi wenzake watahakikisha baadhi ya wana-CCM waliokuwa na tabia za mizengwe pamoja na kupanga safu za viongoli ili kubebana kimaslahi inatoweka, hivyo kumtaka kila mwanachama afanye kazi ya kumuingizia kipato na si kutegemea kunufaika na nafasi ya uongozi.
Naye Makamu Mwenyekiti Bara, Mangula alisema wapo baadhi ya viongozi wameingia ndani ya chama kwa rushwa na tayari malalamiko juu ya mizengwe ya uchaguzi wa chama hicho uliofanyika yamewafikia, hivyo kwa sasa wataanza kupitia kwa kina kila malalamiko na atayebainika kuingia kwa rushwa ataenguliwa bila kumuogopa. 
“Tunajipa miezi sita ndani ya miezi sita walioingia kihalali wataendelea lakini walioingia hovyo hovyo ‘out’…walioingia kwa pesa nje, hata wale waliokuwa wanatumwa vibahasha nao tukiwajua wale nje, hatukubali chama chetu kituhumiwe kwa rushwa, wala hatuta ngoja ushahidi sijui wa TAKUKURU, Polisi hakuna tutakisafisha Chama Cha Mapinduzi,” alisema.
“…Lakini na nyingi mliokubali kununuliwa kama sambusa mlifanya makosa, tusikubali tena…kwanini mtu ukubali kuthaminishwa kama sambusa?,”