Monday, December 10, 2012

Tujivunie nini miaka 51 ya uhuru?

JANA tulipoadhimisha miaka 51 ya uhuru wa Tanganyika, Watanzania wa kada mbalimbali wanakitazama kipindi hicho kwa namna tofauti, kama wanavyoeleza katika mahojiano haya yaliyofanywa na  Elias Msuya. Endelea…

Frank Moyo
NDANI ya miaka 51 ya uhuru, kuna mambo mengi ya maendeleo yamefanyika. Kwa mfano, kuna ajira nyingi, rasmi na zisizokuwa rasmi, zimejitokeza. Wakati huu vijana wengi tumejiajiri kwenye usafiri wa bajaj, hii inasaidia kujikimu kimaisha.
 

Siyo kwamba tunapata fedha nyingi, lakini tunaweza kujikimu tu kimaisha.
Hata hivyo naweza kusema kuwa bado nchi yetu haijaendelea kama zilivyo nchi za wenzetu. Wenzetu wana treni zinazopita chini ya ardhi, wana barabara za angani (flyovers). Sisi bado reli na barabara ni zile zile tu.
 

Nashauri Serikali iwaangalie na wananchi walio katika ajira zisizo rasmi kwa kuwa ndiyo wengi kuliko watumishi wa umma na wafanyakazi walio katika sekta rasmi.
Serikali pia iimarishe miundombinu kama reli na barabara ili kuongeza maendeleo.


Japhet Kanyika
SAWA tumepata uhuru, lakini ni wa maneno tu. Hakuna uwajibikaji wa kweli wa kuleta maendeleo.
 

Kwa mfano elimu yetu tangu tumepata uhuru bado haijazaa matunda katika jamii. Watanzania wengi hawana elimu ya kuwawezesha kueleza kero zao, ukilinganisha na raia wa Kenya ambao wanajua haki zao kwetu bado.
 

Utakuta mtu hajui hata haki zake au anashindwa kueleza shida yake, mwisho anabaki na umasikini wake.
 

Kwa upande mwingine, ukiangalia maeneo ya vijijini, vijana wengi wamejiajiri kwenye biashara ya bodaboda, lakini hawana mafunzo ya kutosha ya biashara hiyo.
Isitoshe Serikali inaweka ukiritimba kwa vijana, mfano kijana akihitaji leseni ambayo gharama yake ni Sh40, 000 tu, atazungushwa hadi anajikuta ametoa Sh200, 000.

Kwa upande wa kilimo, mimi ni mkulima natoka wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro. Wakulima wengi hawana elimu ya kilimo, matokeo yake wanalima mashamba makubwa bila utaalamu, hivyo kuishia kupata mazao kiduchu. Wanatumia nguvu na fedha nyingi lakini hakuna cha zaidi wanachopata.
Nashauri Serikali iwekeze kwenye elimu ili wananchi wajikwamue kiuchumi.


David William
MIAKA 51 ya uhuru, bado hatuna la kujivunia kwa sababu vijana wengi hatuna ajira. Ukiacha vijana waliosoma hadi vyuo vikuu, lakini wengi wetu hatuna cha kufanya, tumebaki na umasikini mtupu.
 

Mimi ni mwanamichezo na nimechezea timu za Kombaini ya Makuburi na Simba ‘B’, lakini nimeshindwa kuendelea kwa sababu ya mazingira magumu. Sina uwezo wa kujikimu kimaisha wala kujikita kikamilifu kwenye michezo.
 

Hilo ndio tatizo linalotukumba sisi vijana. Naamini kabisa kwa kipaji changu hiki cha michezo ningefika mbali, lakini kwa umasikini huu nimeshindwa.

Serikali haina mkakati wowote wa kutukwamua vijana, ndiyo maana sioni faida za kusheherekea uhuru.
Kwa sasa najishughulisha na biashara ya taxi ili kujikimu kimaisha hata kama ndoto yangu ya kuwa mwanamichezo imepotea.

Naishauri Serikali iwekeze kwenye michezo kwa kutambua vipaji vya vijana na kuviendeleza. Waanzishe shule za soka na michezo mingine.
Huko ndiko tutakapotokea, siyo lazima vijana wote tukae ofisini, hata huku mitaani tunaweza kujikwamua. Kwa nchi za wenzetu wanamichezo wanalipwa vizuri kuliko hata maofisa wa Serikali.


Saleh Mpiga
NI kweli katika miaka hii 51 ya uhuru kuna mafanikio mengi yaliyopatikana. Uchumi umekua, kilimo kimeimarika, barabara zimejengwa na miundombinu mingine, ukilinganisha na miaka ya nyuma.
 

Lakini bado kuna tatizo la ajira kwa vijana. Wengi hatuna ajira tunaishi maisha ya kubahatisha. Kibaya zaidi hata vijana waliosoma vyuo vikuu hawana ajira.
 

Chanzo cha tatizo hili ni utandawazi ambapo raia wa mataifa mengine wanakuja na kuchukua ajira zetu. Ukifuatilia utaona elimu zao ziko juu, sisi tunaishi kwa ujanja tu.
Tatizo jingine liko kwa viongozi wetu ambao wamekalia kujilimbikizia mali kuliko kujali maslahi ya umma. Wananchi wengi wanataabika kwa umasikini lakini wao wanafaidi kwa maisha ya anasa.


Ally Juma
KWA kweli mimi bado sijaona matunda ya uhuru, ikiwa hadi leo, wakulima vijijini wanakosa hata matreka ya kulimia.

Serikali imeshindwa kupeleka matrekta ili kuwasaidia wakulima, matokeo yake wanalima kwa kubahatisha tu na bei za vyakula zinakuwa juu kwa sababu kilimo hakijaboreshwa.
 

Mimi nimetokea Mzumbe, Morogoro ambako nilikuwa mkulima. Kule matrekta yanamilikiwa na watu wachache. Mbunge wetu alikuwa na matrekta yake ambayo hayakuwa yakitumia na wananchi wote.
 

Tunashindwa kuelewa kwa nini Serikali isipeleke matrekta hayo kwa Serikali za vijiji ili wananchi wachangie tu gharama za mafuta. Lakini kwa hali ya sasa mkulima atapata wapi fedha za kukodi trekta ili alime?
 

Hiyo ndiyo sababu ya vijana wengi kukimbilia mijini kutafuta vibarua. Ni tatizo la kitaifa.
Mimi sasa nimejiajiri kama dereva wa taxi. Tumeunda umoja na tuna mfuko wetu tunaokusanya fedha kwa ajili ya kukopeshana. Ila bado tunatafuta mfadhili wa kutuongeza mtaji, ili tupate mikopo ya maendeleo. Huo ndiyo ukombozi kwa vijana wasio na mitaji.
Naishauri Serikali iwekeze kwa vijana ili kuleta maendeleo ya kweli.


Zainab Kapoma
MAFANIKIO yaliyopatikana kwa miaka 51 ya uhuru kwa kweli yananichanganya. Hakuna kitu kinachoniuma kama vijana wetu wanaosoma hadi vyuo vikuu kukosa ajira, eti kwa sababu tu hawana uzoefu. Atapataje uzoefu wakati ndiyo katokea shule?

Wazee wanang’ang’ania madarakani huku vijana wakisotea ajira kwa muda mrefu. Watu wamekuwa madarakani tangu tupate uhuru lakini wamo tu. Sana sana wanawaachia watoto wao, huku vijana wengi wenye sifa wakisota tu.

Ndiyo maana nasema sioni mafanikio ya uhuru. Labda hilo treni waliloleta hapo juzi, kwa sababu tumekuwa wa kwanza kwa Afrika Mashariki na kati kuwa na treni la abira jijini Dar es Salaam.
 

Lakini nashauri kuwepo kwa utaratibu kwa vijana wenye elimu kupewa ajira haraka, siyo kwa watoto wa vigogo peke yao.



Friday, December 7, 2012

Jaji Mark Bomani awashukia polisi

KUJIRUDIA kwa matukio ya polisi kutumia silaha za moto dhidi ya raia, kumepokewa kwa hisia tofauti, huku Mwanasheria Mkuu wa Kwanza wa Serikali, Jaji Mark Bomani akilitaka jeshi hilo kuacha kutumia nguvu wanapokuwa katika operesheni zao.
Wakizungumza jana kwa nyakati tofauti kuhusu tukio la hivi karibuni la kupigwa risasi mwandishi wa habari wa gazeti la Tanzania Daima, watu wa kada mbalimbali walisema, kitendo cha polisi kutumia nguvu sio busara.
Jaji Bomani kitendo cha polisi kutumia nguvu badala ya busara katika operesheni zao kinaweza kuleta uhasama kati ya wananchi na jeshi hilo.
“Kwa ujumla matumizi ya nguvu kwa polisi si mazuri  na nadhani tunatakiwa kubadilika katika hilo.” alisema Jaji Bomani.
Bomani alieleza kuwa  kwa ujumla polisi wanatumia vibaya silaha zao ingawa bado hajapata uhakika wa jinsi  tukio la kujeruhiwa kwa Matutu lilivyokuwa .
Alisema tukio la Mwangosi lilikuwa baya zaidi lakini picha anayoiona na kuihusisha na tukio la juzi, ni kuwa kuna matumizi mabaya ya mashambulizi ya polisi kwa raia.
Hata hivyo wakati Jaji Bomani akieleza hayo Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Jaji mstaafu Amiri Ramadhan Manento  alisema kila tukio linalofanywa na polisi linatakiwa kufanyiwa uchunguzi kabla ya kuanza kulizungumzia.
Jaji Manento alisema akiwa ni mwanasheria hawezi kutoa hitimisho ya tukio la kujeruhiwa kwa Matutu kabla ya uchunguzi wa kisheria kufanyika.
“Tunahitaji kujua mambo mengi, ya michakato ya makosa ya jinai, (criminal procedure) kwa mfano polisi walipoingia walifanya nini, walipotoka, ni maneno gani walimuuliza mtu wa kwanza waliyekutana naye.
Tunahitaji kujua iwapo walitumia kizuizi cha usalama(safe cage) katika silaha zao au la” alisema Jaji Manento
Alisema kulingana na taarifa zilizopo katika magazeti bado unahitajika uchunguzi wa kujua  ni namna gani polisi waliingia ndani ya nyumba hiyo.
Aidha Jaji huyo mstaafu alisema hawezi kuwahukumu polisi moja kwa moja kwani hakuna ushahidi kuwa walikuwa wakimwinda mwandishi, bali inawezekana waligundua kuwa ni mwandishi baada ya kumjeruhi.

Thursday, December 6, 2012

HII NI WODI YA WAZAZI YA HOSPITALI YA TEMEKE

Kwa hali hii ni kweli Serikali yetu inawajibika kwa Wananchi/ wapiga kura wake????

Wednesday, December 5, 2012

Semina: KATIBA NA HAKI ZA WATOTO YATIMA NCHINI



SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA JUKWAA LA WAZI LA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII MTOA MADA NI Daniel Samson/ UDSM

MADA: KATIBA NA HAKI ZA WATOTO YATIMA NCHINI 

Lini: Jumatano Tarehe 5/12/2012

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI:  Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni  


WOTE MNAKARIBISHWA

Wakili: Korti ilikosea kumvua Lema ubunge

WAKILI wa Serikali Mkuu Timon amedai kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ilikosea kutengua ubunge wa aliyekuwa Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema, kwa madai ya kutumia lugha za matusi kwa kuwa Bunge limeruhusu wanasiasa kutukanana kwenye kampeni.

Wakili Vitalis alitoa madai hayo jana, wakati wa usikilizwaji wa rufaa ya Lema, aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),katika Mahakama ya Rufani jijini  Dar es Salaam.
Wakati wakili huyo wa serikali akitoa madai hayo, Wakili wa wajibu rufaa, ambao walishinda katika kesi ya msingi, Alute Mughway, naye alidai kuwa Mahakama Kuu, Arusha ilikosea katika uamuzi wake, pamoja na mambo mengine, kwa kukataa baadhi ya madai yao.
Lema alivuliwa ubunge April 5, 2012, katika hukumu iliyotolewa na Jaji Gabriel Rwakibalia, kufuatia kesi iliuyofunguliwa makada watatu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mussa Mkanga, Happy Kivuyo na Agnes Mollel, wakipinga ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Lema kupitia kwa Wakili wake Method Kimomogoro alikata rufaa Mahakama ya Rufani, lakini Novemba 8, 2012 mahakama ilitupilia mbali rufaa hiyo baada ya kuini kuwepo kwa dosari za kisheria, kutokana na pingamizi lililowekwa na upande  wa wajibu rufaa.
Hata hivyo mahakama hiyo ilimpa nafasi nyingine ya  kukata rufaa tena baada ya kumpa siku 14 kufanya marekebisho ya dosari hizo za kisheria na kuiwasilisha mahakamani ndani ya muda huo, amri ambayo aliitekeleaza.
Wakati Lema akikata rufaa kupinga hukumu ya Mahakama Kuu kumvua ubunge, wajibu rufaa nao walikata rufaa (Cross Appeal) kupinga uamuzi wa mahakama hiyo, huku wakibainisha hoja nne.
Katika hoja ya kwanza hadi ya tatu walidai kuwa Jaji alikosea katika hukumu yake kwa kuchanganya vituo vilivyotolewa ushahidi na mashahidi wanne na hatimaye akakataa ushahidi wapo, pamoja na tarehe za ratiba ya kampeni ya CCM nay a Chadema.
Hoja ya nne walidai kuwa Jaji alikosea kwa kuamua kuwa hata kama Lema kwenye kampeni zake alidai kuwa Dk. Buriani ni mkazi wa Zanzibar hatafaa, wakidai kuwa ukazi si sifa ya kuchaguliwa kuwa mbunge.
Hatimaye rufaa hizo zilisikilizwa jana na jopo la   Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, lililoundwa na Jaji Salum Massati, Jaji Bernard Luanda, chini ya uongozi wa  Jaji Nathalia Kimaro.
Wakati wa usikilizwaji wa rufaa hiyo, mawakili wawili ambao ni ndugu, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lisu na kaka yake Mghway, walipambana vikali kwa hoja za kisheria.
Lisu, Kada wa Chadema ambaye pia ni Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alikuwa akimtetea Lema mrufani (Lema), akisaidiana na Wakili  Method Kimomogolo, huku Mughway akiwatetea wajibu rufani ambao ni makada wa CCM.

Udasa: Maslahi ya taifa kwanza

JUMUIYA ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udasa), kimewataka wananchi kuweka siasa kando pale unapofika wakati wa kujadili masuala yanayohusu mustakabali wa taifa.Pia, Udasa imesema iwapo raslimali za taifa zitasimamiwa na kutumika vizuri kwa mapato yanayopatikana, wananchi wake wataondokana na ugumu wa maisha.

Hayo yalisemwa Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa Udasa, Dk Francis Michael alipokuwa akizungumzia Kongamano la kujadili Mstakabali wa Taifa kwa miaka 50 ijayo ya uhuru, litakalofanyika chuoni hapo Desemba 9, mwaka huu.

Dk Michael alisema kongamano hilo halilengi kukuza mitazamo ya kisiasa, bali litakuwa na nia ya kulijenga taifa kwa vizazi vijavyo.

Alisema mada kuu ‘Uhuru Wetu na Mustakabali wa Taifa kwa Miaka 50 ijayo’, Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandala kufungwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.

Tuesday, December 4, 2012

TGNP: Madawati ya Kutetea Jinsia Yasimamiwe

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), umetoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa madawati yaliyowekwa katika vituo mbalimbali vya polisi nchini, ambayo yanatetea haki za jinsia yanasimamiwa kikamilifu ili kupunguza unyonyaji na unyanyasaji nchini.

Wito huo ulitolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Usu Mallya, jijini Dar es Salaam katika mjadala wa kupinga ukatili wa kijinsia, kauli mbiu ya mtandao huo ni ‘Tokomeza Ukatili wa Kijinsia, Jitokeze kutoa maoni ya Katiba Mpya’.

“Madawati haya yawe ni ya kusaidia na kukomesha ukatili wa kijinsia, hivyo ni jukumu la serikali kuhakikisha kwamba kesi zote ambazo zinafunguliwa zinasimamiwa kikamilifu,” allisema Mallya.

  Usu alisema Mikoa ya Singida na Mara inaongoza kwa kiasi kikubwa kwa ukatili wa kijinsia hususani katika suala la ukeketaji na sababu nyingine ambayo inachangia ni ukosefu wa mgawanyo sawa wa matumizi ya rasilimali za taifa.

Alisema ukatili wa kijinsia una sura tofauti na kwamba hali hiyo inaongezeka kila uchao kutokana na kutokuwepo kwa sera makini za kiuchumi zinazowalinda wanawake katika kumiliki mali.

Monday, December 3, 2012

Kumekucha Mabilioni Ya Uswisi

  • WEREMA ASEMA USALAMA WA TAIFA,INTERPOL KUSHIRIKI UCHUNGUZI NDANI, NJE YA NCHI
Na: Claud Mshana
SERIKALI imeamua kuunda kikosikazi kitakachohusisha Idara ya Usalama wa Taifa,  Polisi wa Kimataifa (Interpol) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa ajili ya kuanza uchunguzi kuhusu  Watanzania wanaotuhumiwa kuficha kiasi cha Sh314 bilioni nchini Uswisi.
 
Hatua hiyo ya uchunguzi inatokana na Bunge kutoa maazimio ya kuitaka Serikali kufuatilia sakata hilo katika kikao chake kilichopita mjini Dodoma na kutoa majibu katika kikao cha Bunge cha Aprili mwakani.

Akizungumza na Mwananchi Jumapili jana, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema, “Tuhuma hizo siyo jambo dogo na Serikali haiwezi kuzipuuza, sasa tunachukua hatua madhubuti.”
Jaji Werema alisema kuwa Serikali imeshapiga hatua katika kufanya uchunguzi huo.

“Tumepiga hatua katika suala hili, ila ukianza kusema sana utakuwa unaharibu. Tumeamua kuwa na kikosi maalumu cha upelelezi kitakachoshirikisha Idara ya Usalama wa Taifa, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Wizara ya Fedha na wachunguzi binafsi wakiwamo Polisi wa Kimataifa (Interpol) pamoja na Benki ya Dunia (WB).
 
“Serikali inaweza kuwashirikisha watu wengine kama Benki ya Dunia (WB) na Polisi wa Kimataifa (Interpol) kwa ajili ya kusaidia uchunguzi huo.”
 
Aliongeza kuwa katika timu hiyo, wameamua kumshirikisha Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kutaka ukweli wa sakata hilo.
“Tumeamua kulifuatilia jambo hili, kama tutafanikiwa litakuwa jambo jema. Kama hatutafanikiwa tutakuwa tumejaribu,” alisema.

Hata hivyo, Werema alisema kuwa, bado hawajamwita Zitto ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema kwa ajili ya ushauriano zaidi.
“Unajua kuwa mwanasheria mkuu siyo kujua kila kitu, Zitto pia anaweza akawa na mbinu, ambazo zitasaidia katika jambo hili,” alisema Werema.
 
Uchunguzi
Hivi karibuni akiwa jijini Mwanza, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika alisema kuwa Serikali ya Uswisi imeitaka Tanzania kuwasilisha kwake majina ya watu wanaotuhumiwa kuficha mabilioni ya fedha nchini humo, kama sharti la kusaidia uchunguzi dhidi ya tuhuma hizo.
 
Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa na gazeti moja la Kiingereza nchini, maofisa wa Uswisi walitaka ushahidi zaidi wa majina kama sharti la kutoa ushirikiano katika uchunguzi huo.
 
Kwa mujibu wa habari hizo, maofisa hao waliwataka wenzao wa Tanzania kupeleka majina ya wahusika, pia kutoa ushahidi usio shaka unaoonyesha nani alimpa nani rushwa, kuonyesha mazingira ya rushwa yaliyosababisha kupatikana kwa fedha hizo.

Maofisa hao pia walitaka Serikali ya Tanzania kuonyesha jinsi fedha hizo zilivyohamishwa hadi kwenye benki zao.
 
Kauli ya Zitto
Akizungumzia masharti hayo, Zitto alisema uchunguzi utakaofanywa utafuata mfumo wa uchunguzi binafsi na kubainisha kuwa, kufuata mfumo wa kiserikali kunaweza kuwa na vikwazo vingi.
“Sisi hatufuati mfumo wa kiserikali, mfumo wa kiserikali ndiyo una masharti hayo. Sisi tunafuata mfumo wa uchunguzi binafsi,” alisema Zitto.
Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa

Thursday, November 29, 2012

Jaji chande aikwepa kesi ya Lema

JAJI Mkuu wa Tanzania, Mohamed Othman Chande amejitoa kusikiliza rufaa ya kesi ya aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, badala yake nafasi yake imechukuliwa na Jaji Bernard Luanda.
Kujitoa kwa jaji mkuu kumekuja ikiwa zimebaki siku tano kusikilizwa upya kwa rufaa hiyo Desemba 4, mwaka huu, baada ya awali Mahakama ya Rufani, kuona rufaa hiyo ilikuwa na dosari.
Mahakama hiyo ilikubali hoja ya wajiburufaa kuwa rufaa hiyo ilikuwa na dosari kutokana na tofauti ya vifungu vya sheria vilivyotumika katika hukumu iliyomvua ubunge Lema na vilivyotumika katika hati ya kukaza hukumu, iliyowasilishwa mahakamani sambamba na rufaa hiyo.
Hata hivyo, kilichomwokoa Lema ni kifungu cha 111 cha Kanuni za Mahakama, ambapo mahakama hiyo ilisema kuwa chini ya kanuni hiyo, dosari hizo zinaweza kurekebishwa.
Jaji Chande ndiye aliyekuwa kiongozi wa jopo la majaji watatu katika kesi hiyo akiwamo Salum Massati na Natalia Kimaro.
Jaji Mkuu aliingia kwenye kesi hiyo akichukua nafasi ya Jaji Mbarouk Salim Mbarouk aliyekuwa amepangwa awali, ambaye sababu za kuondolewa hazikuwekwa wazi.
Wakili wa  Lema, Method Kimomogoro alithibitisha kuwa amepata taarifa kuwa jaji mkuu hatasikiliza rufaa hiyo na badala yake Jaji Luanda ndiye atachukua nafasi yake.
“Ni kweli jaji mkuu hatakuwapo kusikiliza rufaa ya Lema nimewasiliana na Msajili Dar es Salaam ameniambia hatokuwepo kwenye hilo jopo,” alisema Kimomogoro na kuongeza:
Hata hivyo, Wakili Kimomogoro alisema “Huu ni utaratibu wa kawaida wa mahakama kwa kuwa huenda jaji mkuu akawa amesafiri au ana shughuli nyingine.”
Wakili wa wajiburufaa, Alute Mughwai alisema hajapata taarifa kama Jaji Mkuu ameondolewa kwenye jopo hilo kwa kuwa huo si utaratibu wa mahakama kutoa taarifa hizo.
“Mahakama huwa haitoi taarifa, zinawekwa (taarifa) kwenye ubao wa mahakama siku ambayo rufaa inasikilizwa,” alisema.
Aliendelea, “Jaji yeyote atakayepangwa sisi hatuna tatizo kwa kuwa wote ni majaji, wewe uko huko Dar na mimi niko huku bara (Arusha), hivyo unaweza ukazipata taarifa zaidi huko kwa kuwa ndiyo uko jikoni Dar.”

Tuesday, November 27, 2012

MAADHIMISHO YA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA




BIG BANG          BIG BANG             BIG BANG

UNAKARIBISHWA KATIKA JUKWAA LA WAZI LA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII MTOA MADA NI  TGNP/GDSS  

MADA: SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA   

Lini: Jumatano Tarehe 28/11/2012

Muda: Saa 03:00 Asubuhi7:00 Mchana
 
MAHALI:  Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni  


WOTE MNAKARIBISHWA


Hotuba Ya Mwenyekiti Wa WILDAF Kwenye Uzinduzi Wa Kupinga Ukatili Wa Kijinsia...!

Ukumbi wa Diamond Jubilee, TAREHE 26/11/2012

Ndugu Mgeni Rasmi, Naibu Waziri wa Sheria na  Katiba,Mheshimiwa, Angelah Kairuki,

Mheshimiwa  Balozi wa Ireland, Fionnula Gilsenan

Waheshimiwa wawakilishi wa Balozi mbalimbali,

Mheshimiwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Said Mwema,

Wawakilishi wa Mashirika wahisani,

Ndugu Viongozi Vyama na Serikali,

Waandishi wa habari,

Wageni waalikwa,

Mabibi na mabwana,

Itifaki imezingatiwa.

Kwa niaba ya wanachama wa WiLDAF Tanzania na kwa niaba ya Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) na  Kikosi kazi cha kuandaa maandalizi ya siku 16 za Kupiga Vita ukatili wa kijinsia, ningependa kuchukua fursa hii kuwakaribisha rasmi kwenye uzinduzi huu wa Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia.

Tunatoa shukrani za pekee kwako mgeni rasmi kwa kuitikia wito wetu wa kuja kujumuika nasi katika uzinduzi huu na hasa ukizingatia kwamba una majukumu mengi, na nyeti yanayohusu taifa letu.

Kweli unatuthibitishia kwamba wewe ni mwanaharakati mwenzetu.

Ndugu mgeni Rasmi,

Aidha ningependa kuchukua nafasi hii kipekee kabisa kulishukuru kwa namna ya pekee Shirika la Msaada la Ireland (Irish Aid), Shirika la Msaada la Marekani  USAID, UN –Women  na CONCERN kwa kutupa uwezo wa kiuchumi ili kuweza kuadhimisha siku hii.

Tunapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru washiriki wote kwa kujumuika nasi katika uzinduzi wa Siku hizi 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia kwa mwaka huu 2012.

Ndugu mgeni rasmi,

Naomba uniruhusu nikufahamishe kwa ufupi tu kuhusu  chimbuko la kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia. Kampeni hii ilianzishwa rasmi mnamo mwaka 1991 na Taasisi ya Kimataifa  ya Wanawake  katika  Uongozi, huko nchini Marekani kwa nia ya kuamsha ari ya kuzuia na kupambana na ukatili dhidi ya wanawake kwa kuzingatia haja  ya kuleta usawa wa kijinsia.

Ndugu mgeni rasmi,
Kampeni hii ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia  inaanza rasmi tarehe 25 Novemba ambayo ilichaguliwa na Umoja wa Mataifa mwaka 1999 kuwa ni SIKU YA KIMATAIFA YA KUPINGA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE . Hivyo basi, Umoja wa Mataifa unashauri serikali, mashirika ya Kimataifa na asasi zisizo za kiserikali kufanya shughuli zinazolenga kufahamisha jamii juu ya ukatili dhidi ya wanawake.Wanawake duniani kote wamekuwa wakikumbwa na ukatili ikiwemo kubakwa, vipigo, ukatili majumbani, ukeketaji na aina mbalimbali za ukatili. Tarehe hii ni ya kihistoria kwani ni kumbukumbu ya mauaji ya kinyama waliofanyiwa kina dada wa Mirabelle nchini Dominika mwaka 1960.  Wanawake hawa  waliuawa kikatili kwa kuwa walikuwa  wanapinga utawala wa kidikteta wa Rais wa nchi ya Dominika (1930-1961) Rafael Truijilo na kutetea haki  katika jamii yao.  Wakina dada hawa walifanyiwa vitendo vingi vya kudhalilishwa utu wao na mwishowe Raisi Rafael Truijilo aliamua wauawe.  Aidha Kampeni hii inahitimishwa tarehe 10 Desemba  ambayo  ni siku ya Kimataifa ya  TAMKO LA HAKI ZA BINADAMU ikiwa ni ishara ya kuhusisha ukatili dhidi ya  wanawake na  haki za binadamu na  kutia msisitizo kwamba ukatili kama huu ni uvunjwaji wa haki za binadamu.

Ndugu mgeni rasmi,
Kati ya tarehe 25 Novemba na Desemba 10 kuna matukio mbali mbali ya kimataifa kama ifuatavyo:-

-  Tarehe 29 Novemba ni Siku ya Kimataifa ya Watetezi wa Haki za Wanawake.

-  Desemba 1 ni siku ya UKIMWI duniani.

-  Desemba 6 ni siku ya kukumbuka mauaji ya kikatili ya wanawake wahandisi mjini Montreal, Canada.

Ndugu mgeni rasmi,
Kwa kipindi cha tangu mwaka 1991 inakadiriwa kiasi cha nchi 156 duniani na mashirika zaidi ya 2,000 yanashiriki katika kampeni hii ya siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia kwa kufanya yafuatayo:-

-    Kuhamasisha jamii juu ya ukatili wa kijinsia na masuala yanayohusu haki za binadamu katika ngazi ya kitaifa, kikanda na kimataifa.

-   Kuimarisha mshikamano wa kupambana na vitendo vyote vya ukatili  dhidi ya wanawake.

-   Kuanzisha ushirikiano wa dhati kati ya wanaharakati wa ndani na nje ya nchi ili kutokomeza ukatili wa kijinsia.

-  Kuandaa jukwaa lenye kuleta fursa ya kubadilishana  mawazo, uzoefu na kuweka mikakati thabiti kwa pamoja ya kupambana na ukatili wa kijinsia.

-  Kuonesha mshikamano wa wanawake duniani kote na kuwa na sauti ya pamoja  katika kupinga ukatili dhidi ya wanawake.

-    Kuunganisha nguvu za wanawake pamoja ili iwe nyenzo thabiti kuishawishi serikali kutekeleza ahadi walizoweka ili kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake.

Ndugu mgeni rasmi,
Nchini Tanzania katika  Siku hizi 16, mashirika, taasisi na idara mbali mbali chini ya  mwamvuli wa Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI), Kikosi Kazi cha kuratibu maadhimisho ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia yakiratibiwa na  WiLDAF yanaungana na wapenda haki wote duniani kuwakumbuka  wanawake na wasichana wote walioathirika na vitendo vya ukatili kama vile kupigwa, kubaguliwa kijinsia, kukeketwa, kuuawa, wajane kunyang’anywa mali, kunyimwa haki ya kumiliki ardhi na kadhalika.  Ni dhahiri kwamba, ukatili wa kijinsia ni dhana  pana inayogusa jinsi zote lakini kwa kiasi kikubwa wahanga  wakubwa wa ukatili huu ni wanawake.
Ndugu mgeni rasmi, kampeni ya mwaka huu imekuwa na muitikio mkubwa na msisimko wa aina yake kwani wadau wengi wamejitokeza katika kampeni hii. Mathalani, Jeshi la Polisi limekuwa na ushiriki mkubwa na wa kipekee. Kwa kutilia mkazo na kutekeleza nguzo ya Polisi Jamii, Jeshi la Polisi linaungana nasi kwa kufanya shughuli mbali mbali za kuhamasisha amani na usalama katika makazi yetu na maeneo ya barabarani. Kwa kutumia fursa ya rasilimali watu ambayo jeshi la Polisi linayo, watatoa elimu ya athari na madhara ya ukatili, watahamasisha jamii kukemea vitendo vyote viovu vinavyosababisha ukatili kwani ukatili wa kijinsia ni kosa la jinai na pia unachochea uvunjwaji wa amani katika nyumba zetu na Taifa kwa ujumla. Napenda kutumia fursa hii kulipongeza Jeshi la Polisi kwa kuchukua hatua hizi. Pia nampongeza Mkuu wa Jeshi la Polisi Inspecta Generali Said Mwema kwa juhudi kubwa anazofanya. Inatupa faraja kubwa sisi wanaharakati kuona Jeshi la Polisi limevalia njuga kampeni hii. Hii inatoa ishara nzuri kwamba kwa kushirikiana nasi basi tutaweza kuutokomeza ukatili dhidi ya wanawake.
Ndugu Mgeni Rasmi, pamoja na Jeshi la Polisi, Mashirika mengine yanayoshirikiana nasi na yana shughuli mbalimbali katika kipindi hiki cha kampeni ya Siku 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake ni kama ifuatavyo,
  • World Vision watakuwa na kampeni kuhusu afya ya mtoto sasa itakayofanyika Hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro, Kempiski
  • Chama cha Wanawake Wanasheria (TAWLA) watakuwa na mjadala kuhusu ukatili wa kijinsia tarehe 29 katika ukumbi wa Diamond Jubillee
  • Equality for Growth (EFG) watakuwa na uzinduzi wa kupiga vita ukatili wa kijinsia kwa kutembelea masoko mbalimbali ya wilaya ya Ilala, tarehe 5/12/2012
  • Engender Health/Champion Project watakuwa na uzinduzi wa kupiga vita ukatili wa kijinsia tarehe 6/12/2012 kwa kutembelea vijiji 20 vya mkoa wa Iringa
  • Children Dignity Forum (CDF) watatoa msaada wa kisheria mkoa wa Pwani. Pia wataendesha shughuli mbalimbali kupiga vita ukeketaji tarehe 8/12/2012 katika wilaya ya Tarime mkoa wa Mara.
  • Pamoja na mashirika mengine Action Aid, Concern, CSOs coalition na YWCA watakuwa na shughuli mbalimbali za kupinga vita ukatili wa kijinsia.
  • Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu wataadhimisha siku ya Tamko Rasmi la Haki za Binadamu na kuhitimisha maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa Kijinsia.
Ndugu Mgeni Rasmi, uwepo wetu leo hapa katika kuadhimisha uzinduzi wa kampeni ya Siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia unaambatana na shughuli mbalimbali zikiwemo za kutoa msaada wa kisheria kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, maonesho ya programu mbalimbali za asasi zinazolenga kutokomeza ukatili wa kijinsia, mada mbalimbali zinazohusiana na ukatili wa kijinsia. Aidha uzinduzi huu una shughuli mbili za kipekee. Kwanza uzinduzi wa Fomu ya Polisi namba 3 (PF 3), Fomu hii mpya ya Polisi imefanyiwa maboresho na kuongezewa vipengele muhimu pamoja na mambo mengine vinavyohusu ukatili wa kingono. Ni imani yetu kubwa kuwa Fomu hii mpya ya Polisi ni nyenzo muhimu na itasaidia katika ushahidi na hivyo kurahisisha upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia.
Ndugu Mgeni rasmi

 Shughuli nyingine ya kipekee ni uzinduzi wa msafara wa kupinga ukatili wa kijinsia (CARAVAN). Msafara huu umebeba Mabalozi kutoka makundi mbalimbali ya wanaume, wanawake, vijana na walemavu. Mabalozi hawa watatoa ujumbe na kuhamasisha jamii za kitanzania kukemea vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia. Aidha, wataunganisha nguvu za pamoja kwa kuhamasisha jamii zetu kuwa kila mtu mwanaume awe au mwanamke ana wajibu wa kukemea na kuchukua hatua dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Msafara huu utatembea katika kanda tatu (3) ambazo ni kanda ya Kaskazini, Mkoa wa Kilimanjaro, Kanda ya Kati, Mkoa wa Singida, na Kanda ya Ziwa, Mkoa wa Mara-Tarime, ambapo takwimu zinaonesha kuna kiwango kikubwa cha ukatili dhidi ya wanawake hususan ukeketaji. Ni matarajio yetu makubwa kuwa msafara huu utakuwa ni chachu kubwa katika jamii zetu kuanza kuzungumza na kutoa taarifa ya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake. Aidha utaamsha ari kwa jamii zetu kuweza kukemea vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia

Ndugu mgeni rasmi 
Kampeni hii ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia itafanyika kikanda. Kanda hizo ni Kanda ya Ziwa (Mwanza, Mara, na Shinyanga) chini ya usimamizi wa Shirika la KIVULINI na ABC Foundation, Kanda ya Kaskazini (Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga) chini ya usimamizi wa NAFGEM,  Kanda ya Kati (Dodoma, na Singida) chini ya usimamizi wa  AFNET, Kanda ya Kusini (Mtwara, Songea, Mbeya, Iringa na Lindi) itaadhimisha  shughuli hii chini ya kituo cha wasaidizi wa kisheria Iringa na Kanda ya  Kaskazini (Tabora na Kigoma) chini ya Jeshi la Polisi wakishirikiana na WiLDAF. Aidha kampeni hii mikoani inazinduliwa rasmi leo  26/11/2012.

Ndugu Mgeni Rasmi,
Tunafahamu kuwa serikali ya Tanzania imefanya juhudi mbalimbali za kuzuia na kutokomeza vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia.  Juhudi hizi ni pamoja na kutengeneza mpango mkakati  wa kitaifa wa  kuzuia na kupambana na ukatili wa kijinsia wa mwaka 2001,  kutunga sheria na sera  mbalimbali zinazolenga kuleta usawa kwa mfano:-

-          Dira ya Maendeleo  ya mwaka 2025.

-          Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000 inayolenga kuwaendeleza wanawake kijamii, kiutamaduni, kiuchumi na kisiasa.

-        Sheria ya Kanuni Za Adhabu Sura Na. 16 hususan vipengele vya makosa ya kujamiiana

-          Sheria ya Ardhi Na. 4 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5, zote za mwaka 1999 kama zilivyorekebishwa mwaka 2002 zinazolenga kutoa haki sawa ya umiliki wa ardhi kati ya wanaume na wanawake.

-         Mkakati wa Kitaifa wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia unaolenga kuwa na jamii isiyokuwa na aina yoyote ya ukatili ifikapo 2015.

Ndugu Mgeni Rasmi,
Pamoja na jitihada zote hizi nzuri zinazofanywa na serikali, vitendo vya  ukatili wa kijinsia bado vinakithiri katika jamii zetu. Hivyo basi, tuna sababu za makusudi kabisa kuishirikisha jamii katika kuzuia ukatili wa Kijinsia kwani kwa kiasi kikubwa jamii imekuwa ikichochea au ikikubali uwepo wa ukatili wa kijinsia.

Mathalani katika utafiti uliofanywa na WiLDAF mwaka 2012 katika magazeti, unaoonesha kwamba taarifa 6,001 za ukatili wa kijinsia zimeripotiwa kwenye magazeti ikilinganishwa na taarifa 3,542 za mwaka 2011.

Ndugu Mgeni Rasmi, vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake sio tu kwamba  vinawadhoofisha kiafya, bali pia vinaathiri  uwezo wao wa kushiriki na kuchangia katika kuleta maendeleo kiuchumi ndani ya familia zao na nchi kwa ujumla.
Aidha, jitihada za serikali katika kupunguza umaskini chini ya mkakati wa kuzuia na kutokomeza umaskini (MKUKUTA) na malengo ya Maendeleo ya Millenia (MDG) hasa lengo kuu la tatu hayataweza kufikiwa iwapo hakutakuwa na mikakati ya makusudi ya kuhakikisha kuwa ukatili dhidi ya wanawake unatokomezwa.

Ndugu mgeni rasmi mwaka huu kauli mbiu yetu ni “FUNGUKA! KEMEA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE. SOTE TUWAJIBIKE” Kauli mbiu hii ina maana kwamba sote tunatakiwa kuamka katika masuala ya kuzuia Ukatili. Ni vema kutafakari kwa kina  jinsi ambavyo ukatili wa kijinsia, hususan ukatili dhidi ya wanawake unavyoathiri maendeleo ya familia na nchi kwa ujumla. Sote tunafahamu jinsi jamii inavyofumbia macho vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia vinapotokea, jamii kwa kiasi kikubwa haitoi ushirikiano kwa vyombo husika kuhakikisha tatizo hili linapotea.. Hatuwezi kuwa na Taifa imara bila kutokomeza ukatili wa kijinsia.  Hivyo basi, kauli mbiu inaweka msisitizo kuwa ni wajibu wa kila mmoja wetu kuzinduka na kukemea ukatili dhidi ya wanawake ili kudumisha taifa imara.
Ndugu Mgeni Rasmi,  katika utekelezaji wa kuzuia na kupambana na Ukatili  wa Kijinsia nchini Tanzania, WiLDAF pamoja na mashirika/taasisi  zingine zinazotetea haki za binadamu zinakabiliana na changamoto zifuatazo:-
  1. Mgongano wa sheria mbalimbali na sheria kandamizi ambazo bado zinatumika, Aidha ukosefu wa sheria mahususi dhidi ya ukatili majumbani.
  2. Ushiriki mdogo wa jamii katika kujihusisha katika utetezi na kukabiliana na matatizo ya ukatili wa kijinsia, hususan ukatili dhidi ya wanawake.
  3. Ukosefu wa fedha za kutosha za kutoa mafunzo na kujenga uelewa wa umma katika masuala ya ukatili wa kijinsia.
  4. Mtazamo hasi ndani ya jamii unaopelekea kuhalalisha vitendo vya ukatili  wa kijinsia uliojijenga kwenye mfumo dume.
  5. Ushiriki duni/hafifu wa Wizara mbali mbali na hivyo kutokutoa kipaumbele suala la ukatili wa kijinsia katika wizara zao.
  6. Ukosefu wa takwimu za kutosha kuhusu masuala yanayohusiana na ukatili wa kijinsia
  7. Ukosefu wa huduma bora za afya katika vituo vya afya kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia mathalani sehemu za kuwahifadhi waathirika hao.
  8. Uelewa mdogo na kutotilia maanani suala zima la ukatili wa kijinsia kwa watoa huduma katika jamii.
  9. Uchelewashaji wa kesi za ukatili wa kijinsia hivyo kupelekea waathirika kukata tama na kutokuwa na ushirikiano katika kutoa ushahidi na upatikanaji wa haki.

Ndugu mgeni rasmi
Pamoja na changamoto hizo bado tunayo nafasi ya kurekebisha  hali  iliyopo. Hivyo basi sisi wadau wa kupinga ukatili wa kijinsia  tunaiomba wizara yako kuangalia mambo yafuatayo:-.

-          Kuchukua  hatua za makusudi za kutunga  sera zinazolenga kuleta usawa,  kubadilisha/kurekebisha Sheria ya Ndoa na kutunga sheria mpya ya mirathi pamoja na Sheria  dhidi ya  ukatili nyumbani.

-          Tunaomba Wizara yako iunde kitengo maalumu katika mahakama cha kusimamia kesi za ukatili wa kijinsia, ili kuwezesha upatikanaji wa haki kwa haraka, kwani haki inayocheleweshwa ni sawa na haki iliyonyimwa.

-          Wizara izidi kuweka msukumo ili serikali itenge fedha na rasilimali za kutosha kwa ajili ya kuelimisha wanajamii juu ya haki na wajibu wao kwa mujibu wa sheria na sera zilizopo. Pia kutoa fedha kwa mashirika yanayotetea haki za binadamu hususan haki za wanawake.

-          Serikali kuanzisha sehemu maalumu kwa ajili ya hudma za waathirika wa ukatili wa kijinsia (one stop centre)

-          Serikali ijenge hifadhi zitakazohudumia waathirika wa ukatili wa kijinsia

Mwisho kabisa tunakutakia kila la kheri katika shughuli zako na Mungu akubariki.


                              Mh. Naomi A.M. Kaihula

                                           MWENYEKITI