Monday, May 31, 2010

'Wanawake acheni kutangaza sigara'

CHAMA cha Afya ya Jamii (TPHA), kimewataka wanawake kuacha kutumika kutangaza aina yoyote ya sigara ili kuzuia athari zitokanazo na matumizi ya tumbaku kiafya.

Msemaji wa chama hicho, Elizabeth Nchimbi alisema hayo jana Dar es Salaam wakati akizungumzia Siku ya Kupinga Uvutaji Sigara, inayoadhimishwa kitaifa Mwanza leo.

Ujumbe wa maadhimisho ya siku hiyo mwaka huu ni ‘Mkinge mwanamke na matumizi ya tumbaku’.

Alisema matangazo ya bidhaa hiyo yana lengo moja la kuwapasha habari wateja wake kuhusu ubora wake ili wanunue zaidi huku wakisahau athari zitokanazo na mvutaji.

Elizabeth alikumbushia kuwa moshi utokanao na jani la tumbaku una sumu kali ijulikanayo kama nikotini na wakati mtumiaji wa sigara akivuta, moshi huo huchanganyika na hewa na kuzaa sumu aina ya kabonimonoksaidi.

“Ili kuhakikisha kuwa ujumbe wa kuzuia utumiaji wa tumbaku unawafikia walengwa, kuzuia matumizi ya tumbaku kwa wanawake ni muhimu katika mkakati wa kupambana na matumizi ya tumbaku,” alisema Elizabeth.

Alisema wanawake wamekuwa wakitumika kama chombo cha matangazo ya sigara nchini, lakini maadhimisho ya siku ya kupinga matumizi ya tumbaku yanalenga kulinda hadhi pamoja na afya zao kwa ujumla kwani madhara yake humkuta mvutaji moja kwa moja na wengine walio karibu yake.

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani alizozitaja Elizabeth, asilimia saba ya wanawake wanapenda sana kuvuta sigara huku wanaume wakiwa ni asilimia 12 na kwamba kati ya wavutaji bilioni mbili, milioni 200 ni wanawake.

“Ikiwezekana serikali ipige vita wanawake kutangaza bidhaa hiyo, ama kuzuia kabisa matumizi yake, bidhaa hiyo ipandishwe bei ili ifikie mahali wananchi washindwe kumudu gharama,” alisema Elizabeth.

Alisema Tanzania imetoa umuhimu mdogo sana kupinga madhara ya tumbaku na hata neno ‘onyo’ katika baadhi ya matangazo limeandikwa kwa maandishi yasiyoonekana kwa urahisi juu ya paketi za sigara.

Thursday, May 27, 2010

'Rais Mkapa alimruhusu Yona'

MBUNGE wa Makunduchi Zanzibar, Abdisalaam Issa Khatib (70), amedai katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwamba Ikulu ilitoa ridhaa ya kuendelea na mchakato wa kumpata mzabuni wa ukaguzi wa dhahabu.

Khatib, ambaye alikuwa Naibu Waziri wa Fedha 1995-2008, alidai hayo jana alipokuwa akijibu swali la wakili wa upande wa utetezi, Herbert Nyange, katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi inayowakabili mawaziri wa zamani; wa Fedha, Basil Mramba, wa Nishati na Madini, Daniel Yona na aliyekuwa Katibu Mkuu Hazina, Gray Mgonja.

Nyange alimhoji shahidi huyo wa saba wa upande wa Jamhuri ambaye alidai alikaimu nafasi ya Waziri wa Fedha Mei 2003, baada ya kumwonesha barua iliyoko mahakamani kama kielelezo, ambayo inadaiwa Yona alimwandikia Rais akimwelezea mchakato wa kumpata mzabuni huyo na Rais kujibu kwa kuandika kwa kalamu “nakubali endeleeni haraka”.

Baada ya kumwambia asome maneno hayo, alimuuliza kama Rais akipokea ushauri wa Waziri Yona na kuufanyia kazi, uamuzi huo utakuwa ni wa nani kati ya Rais na Waziri, Khatib alijibu kuwa utakuwa wa Rais.

Wakati huo Rais alikuwa Benjamin Mkapa. Hata hivyo, kulingana na kauli hiyo, Mahakama ilihoji ili kujiridhisha kama kauli hiyo ilikuwa ikimaanisha nini na kuna uthibitisho gani kwamba uamuzi unakuwa wa Rais, Khatib alijibu kama Rais amekubali na amesaini, moja kwa moja ni uamuzi wake Rais.

Khatib pia alijibu kwamba hakuwahi kuona barua iliyoandikwa na Yona kwenda kwa Rais na jibu alilotoa Rais, hata hivyo alikiri hakuna shida yoyote kama Waziri ataamua kufanya mawasiliano na Rais bila kupitia kwa waziri mwingine.

Khatib awali alidai akiwa katika nafasi aliyokuwa akikaimu, Mei 17, 2003, alimwandikia barua Waziri Yona, akitoa ushauri kama wizara yake ilivyoombwa na Wizara ya Nishati na Madini kuhusu mchakato wa kupata mzabuni wa kufanya ukaguzi wa madini.

Katika kumjibu, Yona aliandika akitaka mchakato wa kuipata kampuni itakayofanya kazi hiyo usimame mpaka watakapokwenda wataalamu katika sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, kujifunza na kupata uzoefu kuhusu ufanyaji kazi na gharama zake, ili watakaporudi waweze kupata kampuni inayostahili.

Ushauri huo ulioandaliwa na Khatib baada ya kupata ushauri kutoka jopo la wataalamu waliokuwa katika wizara hiyo ulipomfikia, Yona alijibu Mei 20, 2003 akimfahamisha, kwamba kuna barua aliyoipata kutoka Ikulu ikitoa maelekezo kuhusu suala hilo.

Hata hivyo, kulingana na kielelezo kilichotolewa mahakamani hapo kikidaiwa kuwa ni barua iliyokuwa ikitoka kwa Yona kwenda Ikulu, Yona alijibiwa aendelee kabla hajaomba ushauri wa Wizara ya Fedha.

Nyange alimwuliza Khatib: “Ushauri wako kwa Yona ulikuwa na manufaa yoyote wakati Rais ambaye ni bosi wenu alikuwa ameshaamua?” Khatib alijibu kuwa hakujua hilo na kama angejua kama Rais alishaamua, angewarejea wataalamu na kuwaeleza ili kujua wajibu ulikuwa nini, akadai “nisingeweza kubadili uamuzi wa Rais.”

Shahidi wa nane katika kesi hiyo, Immanuel Mahendeka kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), alidai kuwa kampuni ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation, haikulipa kodi katika kipindi chote tangu iliposajiliwa na TRA Oktoba 3, 2003 na kama ingelipa, Serikali ingepata Sh bilioni 11.7 kuanzia 2004 hadi 2007.

Kesi hiyo iliyoko mbele ya jopo la mahakimu wakiongozwa na Hakimu John Utamwa; Mramba, Yona na Mgonja wanadaiwa kuruhusu kutolewa kibali cha Serikali kilichoisaidia kampuni hiyo kutolipa kodi tofauti na mapendekezo ya TRA, uamuzi ulioisababishia Serikali hasara ya Sh 11,752,350,148 kati ya mwaka 2002 na Mei 2005.

Kampuni hiyo inadaiwa kuidhinishwa kusimamia ukaguzi wa dhahabu nchini kwa ‘kubebwa’ bila kuzingatia ushauri na kuisababishia Serikali hasara ya mabilioni ya fedha. Kesi hiyo inaendelea leo.

UZINDUZI WA ILANI YA UCHAGUZI YA WAPIGA KURA 2010-2015

Wednesday, May 26, 2010

UZINDUZI WA ILANI YA UCHAGUZI YA WAPIGA KURA 2010-2015

Mtandao wa Jinsia Tanzania
na


FemAct


Wanayo furaha kukualika Katika Uzinduzi wa Ilani ya Uchaguzi ya Wapiga Kura 2010-2015 na Jopo la Majadiliano tarehe 2 Juni 2010, saa 3:00 asubuhi hadi Saa 10.00 Jioni katika viwanja vya TGNP Mabibo Dar es Salaam.


Mada Kuu

"Rasilimali za Uchaguzi ziwanufaishe wanawake na makundi yaliyoko pembezoni"


Wasiliana nasi: 022 2443204/450, 255 754 784050 au info@tgnp.org

Monday, May 24, 2010

Liyumba apatikana na hatia,ahukumiwa kwenda jela miaka miwili

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, leo imesoma Hukumu dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Amatus Liyumba,Katika hukumu hiyo Liyumba amepatikana na hatia na kuhukumiwa kwenda jela miaka miwili dhidi ya kesi ya utumiaji mmbaya wa madaraka .
===================

Awali Liyumba alifikishwa mahakamani hapo akiwa pamoja na aliyekuwa meneja miradi wa BoT Deogratius Kweka, ambapo kwa pamoja walikabiliwa na mashtaka mawili likiwamo la kutumia vibaya madaraka aliyokuwa nayo, jambo lililopelekea serikali kupata hasala ya sh bilioni 221, kupitia ujenzi wa majengo pacha ya BoT.
Hata hivyo kabla ya kuanza kusikilizwa kwa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka, upande wa mashtaka ulimuachia aliyekuwa mshtakiwa mwenza wa Liyumba {Kweka}, na kumshitaki Liyumba kwa kesi hiyo.Upande huo wa mashtaka uliita mahakamani hapo mashahidi 8, wakiwamo waliokuwa wajumbe wa bodi ya wakurugenzi wa BoT, pamoja na kutoa vielelezo mbali mbali vinavyohusiana na kesi hiyo.
Baada ya ushahidi huo kumalika kusikilizwa, Mahakama ilifikia uamuzi wa kumfutia Liyumba shtaka la kuisababishia serikali hasala ya bilioni 221 baada ya Upande huo wa serikali kupitia ushahidi na vielelezo vyake kushindwa kuithibitishia mahakama hiyo kama Liyumba alihusika na kosa hilo.Kufuatia uamuzi huo, mahakama ilimtaka Liyumba kujitetea juu ya uhusika wake katika shtaka la kutumia vibaya madaraka aliyokuwa nayo.
Katika utetezi wake Liyumba alijitetea mwenyewe kama shahidi wa kwanza kutoka upande wa utetezi, na baadae alimwiita shahidi wa pili ambaye ni Bosco Ndimbo Kimela, aliyekuwa katibu wa BoT.Baada ya kumaliza usikilizwaji wa ushahidi huo, mahakam hiyo ilizitaka pande zote mbili kuwasilisha hoja zao za kisheria, ambapo alipanga kusoma hukumu dhidi ya Liyumba ifikapo May 24, 2010.

HUKUMU YA KESI YA LIYUMBA KUTOLEWA LEO


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, leo inatarajiwa kusoma Hukumu dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Amatus Liyumba.

Hukumu hiyo dhidi ya kesi ya utumiaji mbaya wa madaraka inayomkabili Liyumba, inatarajiwa kusomwa na jopo la Mahakimu wa mahakama hiyo linaloongozwa na Hakimu Edson Mkasomongwa.

Liyumba ambaye anasota rumande kwa zaidi ya mwaka mmoja na miezi mitatu, kesho anatarajia kujua hatima ya kesi yake hiyo.

Awali Liyumba alifikishwa mahakamani hapo akiwa pamoja na aliyekuwa meneja miradi wa BoT Deogratius Kweka, ambapo kwa pamoja walikabiliwa na mashtaka mawili likiwamo la kutumia vibaya madaraka aliyokuwa nayo, jambo lililopelekea serikali kupata hasala ya sh bilioni 221, kupitia ujenzi wa majengo pacha ya BoT.

Hata hivyo kabla ya kuanza kusikilizwa kwa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka, upande wa mashtaka ulimuachia aliyekuwa mshtakiwa mwenza wa Liyumba {Kweka}, na kumshitaki Liyumba kwa kesi hiyo.

Upande huo wa mashtaka uliita mahakamani hapo mashahidi 8, wakiwamo waliokuwa wajumbe wa bodi ya wakurugenzi wa BoT, pamoja na kutoa vielelezo mbali mbali vinavyohusiana na kesi hiyo.

Baada ya ushahidi huo kumalika kusikilizwa, Mahakama ilifikia uamuzi wa kumfutia Liyumba shtaka la kuisababishia serikali hasala ya bilioni 221 baada ya Upande huo wa serikali kupitia ushahidi na vielelezo vyake kushindwa kuithibitishia mahakama hiyo kama Liyumba alihusika na kosa hilo.

Kufuatia uamuzi huo, mahakama ilimtaka Liyumba kujitetea juu ya uhusika wake katika shtaka la kutumia vibaya madaraka aliyokuwa nayo.

Katika utetezi wake Liyumba alijitetea mwenyewe kama shahidi wa kwanza kutoka upande wa utetezi, na baadae alimwiita shahidi wa pili ambaye ni Bosco Ndimbo Kimela, aliyekuwa katibu wa BoT.

Baada ya kumaliza usikilizwaji wa ushahidi huo, mahakam hiyo ilizitaka pande zote mbili kuwasilisha hoja zao za kisheria, ambapo alipanga kusoma hukumu dhidi ya Liyumba ifikapo May 24, 2010 ambayo ni leo.

Friday, May 21, 2010

Wanafunzi walioolewa waanza kusakwa

MKUU wa Mkoa wa Mara, Kanali Enos Mfuru, ameagiza kufanyika msako mkali dhidi ya wanafunzi walioolewa badala ya kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu.

Hadi sasa wanafunzi 3,173 sawa na asilimia 13.4 waliochaguliwa kuendelea na elimu ya sekondari mkoani Mara hawajulikani walipo, kwa mujibu wa Kanali Mfuru.

“Wanafunzi 3, 173 walitakiwa kuwa shuleni lakini hawapo. Wilaya inayoongoza ni Rorya kwa kuwa na wanafunzi 700 ambao hawajaripoti,” Kanali Mfuru alisema juzi.

Mkuu wa Mkoa aliwataka wakuu wa wilaya, kusaka wanafunzi hao na kuhakikisha wanakuwa shuleni kabla ya mwezi huu kumalizika.

“Itumike nguvu ya ziada kwa mzazi na hata mwanafunzi na wote ambao wameolewa warudishwe shuleni,” aliagiza Mfuru alipozungumza na viongozi waandamizi kutoka wilaya zote za mkoa huo juzi.

Aliongeza: “Mwisho wa mwezi huu wote wawe shuleni na hili halina mjadala”. Alitaja wilaya zingine na idadi ya wanafunzi ambao hawajaripoti kwenye mabano kuwa ni Musoma Vijijini (633), Tarime (567), Serengeti (431), Bunda (369) na Musoma Mjini (357).

Kanali Mfuru alisema wazazi waliopeleka watoto kwenye shule zisizo za Serikali, walitakiwa kutoa taarifa badala ya kukaa kimya kana kwamba wapo.

Hivi karibuni, Rais Jakaya Kikwete, aliagiza wakuu wa wilaya kusaka nyumba kwa nyumba, wanafunzi ambao wamechaguliwa kidato cha kwanza mwaka huu, lakini wajaripoti.

Thursday, May 20, 2010

Mimba zakatisha masomo ya watoto wa kike 400

Zaidi ya watoto wa kike 400 wa shule za msingi na sekondari mkoani Ruvuma wamekatisha masomo yao kutokana na kupata mimba kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Kati ya hao waliopata mimba kwa kipindi cha kuanzia Februari 2009 hadi 2010 wa shule za sekondari walikuwa 301 na 98 wa Shule za Msingi.

Tatizo la mimba ni kubwa zaidi katika Wilaya ya Mbinga ambayo hadi mwishoni mwa Februari mwaka huu, jumla ya wanafunzi 149 walikuwa wamesitisha masomo baada ya kubainika kuwa wamepata ujauzito.

Taarifa za uhakika zilizohakikiwa na kufanyiwa uchunguzi na Gazeti la Nipashe kupitia vyanzo vyake mbalimbali ikiwemo taarifa za elimu za Wilaya na Mkoa, zinaonyesha kwamba Wilaya zenye hali tete ni Mbinga na Songea Vijijini.

Katika taarifa ya elimu ya Mkoa wa Ruvuma ambayo wiki chache zilizopita iliwasilishwa kwenye kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa huo (RCC), inaeleza kwa kuna mapungufu ya namna kesi zinazohusiana na watuhumiwa waliowapa mimba vijana hao, zikishughulikiwa kwa kasi ndogo na maofisa watendaji wa kata, huku zilizopo mahakamani zikiwa bado hazijapatiwa ufumbuzi.

Tatizo la mimba katika kila wilaya na idadi ya wanafunzi waliopata mimba kwenye mabano ni Songea Vijijini (106), Tunduru (77), Namtumbo (41) na Manispaa ya Songea (26).

Tatizo hilo linaonekana kuwa kubwa kutokana na wahusika wa elimu mkoani hapa kutowajibika kuielimisha jamii ipasavyo kuachana na mila potofu dhidi ya mtoto wa kike.

Aidha, taarifa hiyo inafafanua kuwa hadi sasa ni mashauri 10 yamefikishwa mahakamani, 16 yapo Polisi, wakati 58 yanashughulikiwa katika ngazi za Kata na Vijiji.

Akitoa ufafanuzi kuhusu tatizo hilo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma (RAS) Salehe Pamba, alisema Serikali imechukua hatua kukabiliana na hali hiyo ikiwa ni pamoja na kuzielekeza Mahakama kushughulikia haraka kesi hizo sanjari na kuwahimiza maofisa Watendaji wa Kata na Vijiji kuzisukuma katika vyombo vya dola ili watuhumiwa wachukuliwe hatua za kisheria.

“Kuna hatua ambazo uongozi wa Serikali ya Mkoa wa Ruvuma umechukua kukabiliana na hali hiyo kwanza ni kuhakikisha mahakama inazishughukia kesi zote haraka ili kupunguza kasi ya watoto hao kupata mimba…Watendaji wa Kata na Vijiji tumewaelekeza kuzisukuma kesi hizo haraka kwenye vyombo vya dola ili zipatiwe ufumbuzi wa kudumu lakini pia kuielimisha jamii kuhusiana na mila potofu dhidi ya mtoto wa kike.

CHANZO: NIPASHE

Wednesday, May 19, 2010

VACANCY ANNOUNCEMENT

Tanzania Gender Networking Programme (TGNP)


Vacancy Announcement


Tanzania Gender Networking Programme (TGNP) is a non governmental organisation which advocates for a transformed Tanzanian society where there is gender equality, equity and social justice. The overall objective is building a feminist social movement that is capable of engaging, challenging and claiming changes in policies, institutional structures and processes at all levels for social gender transformation and women’s empowerment. TGNP’s main strategies are policy analysis and research, training and capacity building, information, lobbying and advocacy, coalition building and networking.

TGNP seeks to recruit suitable and qualified candidates for the vacant positions listed below. For all posts, we are looking for persons with: a) commitment to gender, women empowerment, social justice and human rights issues, b) commitment to team work and participatory approaches c) motivation with strong interpersonal relations.

The advertised posts carry an attractive salary with fringe benefits.

TGNP is an equal opportunity employer and encourages applications from qualified women and men Tanzanian citizens.

1.0 Gender training institute (GTI) Director (Re Advertised)

Responsibilities: Providing overall Leadership and direction for the Gender Training Institute (GTI) (i.e. vision, team building, coaching & mentoring, facilitation) using high level conceptual and participatory capacities and methodological approaches in programme designing, planning, implementation and monitoring processes and in human resource management, resource mobilisation, financial accountability and administration functions for the achievement of the GTI objectives. Responsible for the coordination and delivery of quality gender training products and services, monitoring and impact evaluating. Oversee expanded development and updating GTI curriculum, training manuals and materials, tools and methodologies for enhancing feminist/gender, participatory animation, and analytical capacities of development actors at different levels within and outside the country. Responsible for strengthening and developing linkages with clients and acting as the chief spokesperson of GTI.



Key Qualifications and experience:-
• Minimum of a Masters Degree in social sciences or equivalent plus course work in training and management of training institutions
• Training and facilitation experience for minimum 3 - 5 years.
• Experiences in leading/working in training institutions and training processes
• Course work on gender or women’s studies
• Relevant experience of 3 - 5 years of working on gender and development issues.
• Inter-personal relationships and marketing management
• MS word, power point, excel and e-mail and internet

Key Competencies
• Programming skills, participatory project management of training institutions and administration;
• Financial literacy relating to budgeting, expenditure monitoring and fund raising skills
• Gender/feminist analysis and training, animation, participatory facilitation and public-speaking;
• Capacity in curriculum development, training & manual materials development
• Good writing, public speaking and presentational skills
• Coaching/mentoring ability
• Communication, spoken and written in Kiswahili and English.
• Computer literacy in word, power point, excel and e-mail and internet

Key Job skill requirements

Competencies
• High level research and policy analysis & report-writing
• Social Gender analysis of society at all levels, linked to macro and micro policy and structures
• Participatory methodology in training and workshop facilitation and public-speaking
• Participatory project management and administration
• Coaching/mentoring
• Financial literacy to budgeting and expenditure monitoring level
• Computer proficiency in word, PowerPoint, excel and e-mail and internet

2.0 Programme Officer - Capacity Building ( 1 Vacancy).

Responsibilities: Overall responsible for the designing, planning, implementation and monitoring of training programme activities, outputs and impacts. Responsible for the coordination and delivery of quality gender training products and services, monitoring and impact evaluating. Develops and updates training manuals and materials, tools and methodologies for enhancing feminist, animation gender capacities of development actors at different levels within and outside the country. Responsible for identifying, developing, strengthening, expanding of the base of resource persons / trainers and facilitators. Responsible for the strengthening and developing linkages with clients, peer Gender Training Institutions and other strategic actors/institutions for the promotion of GTI activities.

Key Qualifications and experience:-
 Minimum of a Masters Degree in social sciences or equivalent plus course work in training and management of training institutions
 Training and facilitation experiences for minimum 2-3 years.
 Experiences in working in training institutions, training processes and curriculum development.
 Course work on gender or women’s studies
 Relevant experience of 3-5 years of working with gender and development issues.
 inter-personal relationships and marketing management
 MS word, power point, excel and e-mail and internet

Key Competencies
 Capacity in training institutions management.
 Capacity in curriculum development, training& manual materials development
 Gender analysis and training.
• Good writing, public speaking and presentational skills
• coaching/mentoring ability
• Communication, spoken and written in Kiswahili and English.
computer literacy in word, power point, excel and e-mail and internet

3.0 Programme Officer Training/ Curriculum Development (1 Vacancy)

Programme responsibility
1.Advises and contributes to the overall planning, implementation and monitoring of GTI programme activities, outputs and impacts

2.Responsible for ddeveloping/strengthening curriculum materials/tools and methodologies for enhancing gender capacities of development actors at different levels within and outside the country

3.Link with all other programmes within TGNP with the objective of developing training manuals/materials tools and packages in relation to the needs of particular programmes.

4.Responsible in the formulation of project plans and budgets, and work closely with GTI Director (and other programme staff) in integrating the GTI activities in the overall programme planning and budgeting.

5.Facilitate Pre testing of curriculum, training materials /tools to ensure the development of quality materials.

6.In collaboration with M & E Officer responsible in facilitating, coordinating, organising, implementing, monitoring and evaluating activities in relation to the GTI within the programme.

7. Facilitates the development of systems and tools for enhancing the implementation, monitoring and documentation processes of the assigned activities.

8.Monitors respective work performance for efficiency, effectiveness, quality and cost-benefit as per the standards set by the organisation.

5. Job Specifications


5.1 Qualifications Requirements


Minimum of a Masters Degree in social sciences or equivalent plus course work in gender or women’s studies

Key Job skill requirements

Competencies
• policy and gender analysis
• curriculum development
• materials development and writing
• public speaking and presentational skills
• coaching/mentoring
• Communication, spoken and written in Kiswahili and English.
• computer literacy in word, power point, excel and e-mail and internet
• inter-personal relationships and marketing management

Experience
• 3 years working with gender and development issues from an NGO perspective AND/OR
• Curriculum and/or materials development for minimum 2 years AND/OR
• Training and facilitation for minimum 2 years

4.0 Programme Officer Marketing and Fundraising(1Vacancy)

Programme officer marketing and fundraising will be responsible for;
1. Identify, package and market GTI training services
2. Study new areas of market for GTI services
3. Link with likeminded organizations in and outside Tanzania to market GTI
4. Develop proposals for fundraising
5. Maintain links with existing and potential funding partners
6. Design and update marketing strategies
Qualifications required
Minimum of Masters Degree in social sciences with specification in social marketing and fundraising


Key job skills requirement;

• Proposal development for fundraising
• Designing marketing materials
• Report writing
• Public speaking and presentation skills
• Communication, spoken and written in Kiswahili and English
• Inter-personal relationship and marketing management
• Computer literacy in different software

Work experience;

• 3 year experience in marketing and fundraising from a social development perspective
• Involvement in report writing and designing of marketing materials
• Experience in working with NGOs involved in trainings


Applications should be addressed to:

The Executive Director,
Tanzania Gender Networking Programme (TGNP),
P.O. Box 8921,
Dar es Salaam, Tanzania.
E Mail: info@tgnp.org
Website: www.tgnp.org


Note: Only short listed applicants will be contacted.

For more information about TGNP visit our website www.tgnp.org

Tuesday, May 18, 2010

'Kikwete hajabariki takrima'

MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, amesema, takrima haijaruhusiwa na pia Rais Jakaya Kikwete hajaibariki.Tendwa amesema, vyombo vya habari vinaupotosha umma katika jambo hilo.

Tendwa amesema,anashangazwa na alichokiita usanii wa kisiasa kugeuza utani wa Rais Jakaya Kikwete alioutoa wiki iliyopita kwa viongozi wa dini na kuufanya ukweli na watu hao kutangaza kuwa amebariki takrima.

Msajili amesema Rais hana mamlaka ya kubadilisha takrima kwa matamshi, kama ilivyogeuzwa na baadhi ya wanasiasa kwamba alibariki takrima katika mkutano wa viongozi hao wa dini uliofanyika Dar es Salaam wiki iliyopita.

“Rais alizungumza kwa wanasemina wale, alipenda kuwa na urafiki, akatoa utani…mimi sikuona utata wala hakubariki takrima…huu ni usanii wa kisiasa,” alisema Tendwa jana Dar es Salaam katika mkutano na waandishi na habari.

Tendwa, amesema,utani hauna budi kuchukuliwa kama utani na mambo ya sheria yakachukuliwa kwa upande wake.

Msajili alitoa ufafanuzi huo baada ya kuulizwa swali likimtaka aeleze kilichojiri katika mkutano huo, kiasi cha kuibua mjadala katika baadhi ya vyombo vya habari vikinukuu wanasiasa wakimshutumu Rais.

Kwa mujibu wa Tendwa ambaye alikuwa miongoni mwa washiriki wa mkutano huo, Rais Kikwete aliwatania maaskofu kupitia kwa Askofu wa mkoa wa Kilimanjaro kwa kutumia mfano wa ‘kitochi’ kwa kusema sheria ya takrima ni ngumu, lakini akahitimisha kwa kuwasisitiza kwamba lazima ifuatwe.

Akiwashangaa waliochukulia utani huo kama hoja muhimu, Tendwa alisema Marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi yamefuta ibara katika Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2007 zilizokuwa zikibariki takrima na Rais hana mamlaka ya kuzirejesha ibara na vifungu hivyo ili kuhalalisha takrima kama inavyodaiwa.

Katika Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi, ibara za 14 na 17 zinafuta mafungu ya 87, 97, 98 na 109 ya Sheria ya Uchaguzi yanayoruhusu utoaji takrima.

“Rais hana mamlaka ya kubadilisha takrima kwa matamshi … nanyi mkachukulia umuhimu; ni vizuri kujifunza mambo ya sheria. Inabidi kuchukua utani kama utani na sheria kama sheria,” alisema.

Akisisitiza kwamba kipindi hiki ni kigumu kisiasa, Tendwa alisema yapo mambo mengi ambayo yanasikika. “Niko tayari kwa hili, Rais hakubariki takrima na wala hana mamlaka wala uwezo,” alisisitiza.

Msajili pia kwa upande wake alisisitiza kwamba sheria ya gharama za uchaguzi ni nzuri na ni ngumu kuitekeleza, kutokana na utamaduni wa rushwa uliokwishajengeka miongoni mwa jamii.

Alisema elimu ya uraia ndiyo itakayokabili ugumu huo wa kutekeleza sheria husika. Kwa mujibu wake, Serikali imejipanga ifikapo mwishoni mwa Juni mwaka huu, elimu iwe imesambazwa nchi nzima.

Alisema kwa sasa wameshakamilisha utoaji elimu kwa viongozi wa madhehebu ya dini, Jeshi la Polisi na jana ilikuwa zamu ya makamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru). Pia vyombo vya habari vitapewa semina.

Alisema kipaumbele cha ofisi yake ni kuhusu sheria hiyo hali ambayo aliamua kufanya Jumanne na Alhamisi kila wiki, kuwa siku za kukutana na waandishi wa habari kupokea madukuduku mbalimbali kutoka kwao.

Sheria ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2009 ilisainiwa mwaka huu na Rais.

Vitendo vinavyokatazwa ndani ya sheria visifanyike pamoja na matumizi ya fedha ni kufanya malipo kwa wapiga kura ili wamchague mgombea.

Mambo mengine yanayokatazwa ni kuahidi kazi au cheo au wadhifa kwa mpiga kura; kutoa zawadi, ahadi, mkopo au makubaliano yoyote kwa mpiga kura ili ashawishike kumchagua mgombea.

Sheria inakataza kutoa malipo kwa ajili ya takrima ya chakula, vinywaji au starehe yoyote ya kuwashawishi wapiga kura, kuwasafirisha na kuweka mkataba wowote wa pango kwa niaba ya wapiga kura.

Katika hatua nyingine, Tendwa aliwaambia waandishi wa habari kwamba masahihisho ya kanuni za uchaguzi yamekamilishwa na leo kuna kikao kitakachohusisha mawaziri wa Katiba na Sheria ambacho ndicho kitakuwa na mamlaka ya kupitisha kanuni hizo.

Monday, May 17, 2010

Karume, Seif kuzindua kampeni kura za maoni

RAIS wa Zanzibar, Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Seif Sharif Hamad, wanatarajiwa kuzindua kampeni ya kueneza uelewa kuhusu umuhimu wa kupiga kura za maoni, maofisa wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) wamesema.

“Tumepanga kufanya kampeni kubwa Zanzibar nzima kuelimisha wananchi kuhusu kura za maoni kabla ya kushiriki kwao katika kuchagua au kutokuchagua mpango wa kuwa na Serikali ya Mseto (GNU).

“Tumepanga kumualika Rais Karume na Maalim Seif kwa kuwa ndio waanzilishi wa mpango huu,” alisema Mwenyekiti wa ZEC, Khatib Mwinyichande katika mkutano wake na waandishi wa habari.

Alisema tume hiyo bado haijamchagua mtu yeyote wa kuifanya kampeni hiyo na iwapo kwa sasa kuna mtu anafanya kampeni hiyo, atakuwa anakwenda kinyume na kanuni kwa kuwa ZEC ndio yenye mamlaka ya kusimamia utekelezaji wa kura hizo za maoni.

Kumekuwa na fununu kwamba baadhi ya watu wameanza kampeni mitaani wakihamasisha wananchi kupiga kura dhidi ya GNU katika siku ya kupiga kura za maoni ambayo imepangwa kufanyika Julai 31, mwaka huu.

Hata hivyo maofisa wa tume hiyo wamesema iwapo fununu hizo ni za kweli, wanaofanya hivyo anafanya makosa. “Tunataka watu wapewe taarifa sahihi ili wachague wenyewe kwa uhuru wao kuhusu upigaji kura za maoni.”

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa ZEC, Sh bilioni 3.7 zitatumika kwa ajili ya upigaji huo wa kura za maoni ambao utafanyika kabla ya uchaguzi mkuu Oktoba 31, mwaka huu.

Iwapo Wazanzibari wengi wataipigia kura GNU, Rais ajaye wa Zanzibar atatakiwa kuunda serikali ya mseto na chama kitakachokuwa imekaribia kura za rais.

Friday, May 14, 2010

Watoro shule kusakwa

WAKUU wa wilaya nchini wanatakiwa kuendesha msako wa nyumba kwa nyumba kubaini waliofaulu kuingia kidato cha kwanza mwaka huu, lakini wako nyumbani.

Katika msako huo ulioagizwa jana na Rais Jakaya Kikwete, mzazi atakayeshindwa kujieleza ni kwa nini mwanawe haendi shule, atawajibishwa. Hakueleza hatua atakazochukuliwa mzazi huyo.

Kikwete alitoa agizo hilo mwanzoni mwa wiki hii akiwa Masasi, na kutaka msako huo ufanyike kwa mtindo unaofanana na wa kukusanya kodi uliotumika zamani, kwa nia ya kuhakikisha wanafunzi hao wanakwenda shuleni.

Kwa mujibu wa taarifa aliyosomewa Mtwara, asilimia 35.6 ya watoto 12,843 waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka jana na kuchaguliwa kuingia sekondari, hawajaripoti shuleni.

Katika ripoti hiyo ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Anatoli Tarimo, ilielezwa kuwa asilimia 64 sawa na watoto 8, 278 walioripoti na kuanza masomo ya sekondari wakati watoto 4,565 hawajaripoti shuleni na hawajulikani waliko.

Katika idadi hiyo, Wilaya ya Mtwara ndiyo inayoongoza kwa kuwa na asilimia 54 ya wasioripoti, ikifuatiwa na Nanyumbu (48%), Masasi (35%), Tandahimba (32%), Mikindani (22%) na Newala asilimia 21.

Moja ya sababu za utoro, Rais Kikwete aliambiwa ni baadhi ya wanafunzi kupata mimba, kuozwa au kuzuiwa na wazazi. “Hizi takwimu ni za juu sana.

Haiwezekani tukaendelea kudhulumu watoto wetu maisha bora, kwa kuwazuia kwenda shule wakati zipo, nafasi zipo na kila kitu kipo.

“Tafuteni majina ya watoto hawa wote, wazazi wao waitwe, wajieleze na kama hawana majibu wawajibishwe.

Afuatwe mtoto mmoja baada ya mwingine bila kumwacha mtu. Na njia rahisi ufanywe msako wa nyumba kwa nyumba, kama ilivyokuwa zamani wakati wa kukusanya kodi,” alisema Rais Kikwete

Alisisitiza kuwa wakati wa mahojiano wazazi wa watoto hao wasihojiwe sababu za kuzuia watoto, bali mahojiano yahakikishe watoto wanapelekwa shuleni mara moja na kazi hiyo ifanyike katika kila wilaya nchini na kusimamiwa na wakuu wa wilaya.

Tuesday, May 11, 2010

Wanasheria: Serikali ya Tanzania ni sikivu

WAKATI Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) likiituhumu Serikali kutosikiliza madai yao kuhusu nyongeza ya kima cha chini cha mshahara, Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) kimeipongeza kwa kuwa sikivu kutekeleza haki za binadamu na utawala bora.

Pamoja na pongezi hizo, pia Tawla imeitaka Serikali kuthamini hoja na mapendekezo ya asasi na vyama vya kiraia, katika mchango wa mabadiliko ya sera na sheria za nchi, kwa kuviwezesha kifedha na maoni yao kuzingatiwa ipasavyo.

Mwenyekiti wa Tawla, Maria Kashonda, alisema hayo jana kwa nyakati tofauti katika sherehe za maadhimisho ya miaka 20 ya chama hicho, katika viwanja vya Mnazi Mmoja ambako mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Rais, Dk Ali Mohamed Shein.

Katika sherehe hizo, pia Shein alizindua Mpango Kazi wa chama hicho wa miaka mitano (2010 – 2015) ambao pamoja na mambo mengine, unalenga kuendeleza huduma ya msaada wa kisheria kwa wahitaji, ikiwa ni pamoja na wajane na watoto.

Kashonda aliliambia gazeti hili mara baada ya sherehe hizo, kuwa ushirikiano baina ya
Tawla, vyama vingine na Serikali, umekuwa mkubwa kiasi cha kuwezesha kuona uhakika kuwa nchi inatekeleza haki na kuzingatia utawala bora.

“Katika kipindi hicho chote, tunajivunia mambo mengi ambayo yamewezekana kufanyika kwa kuwa Serikali ilikuwa nasi, miongoni mwayo ni marekebisho ya sheria mbalimbali ikiwamo ya Makosa ya Kujamiiana (SOSPA) ya mwaka 1998 na marekebisho ya mwaka 2002,” alisema Kashonda.

Alizitaja sheria nyingine ambazo walishirikishwa katika maboresho kuwa ni pamoja na Sheria ya Ardhi, Sheria ya Vijiji iliyowezesha kuundwa kwa Mabaraza ya Ardhi ya Kata na Vijiji, Sheria ya Mtoto na mchakato wa marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971.

Mwenyekiti huyo alibainisha pia kuwa Tawla inajivunia ushirikiano mzuri, si na serikali pekee, bali na vyama na asasi zingine kama Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (Tamwa), Mtandao wa Kijinsia Tanzania (TGNP), Chama cha Wanasheria Tanganyika
(Tanganyika Law Society) na asasi zingine.

Kashonda alisema ni kutokana na ushirikiano huo wamefanikiwa kufikia watu zaidi ya 10,000 katika mikoa kadhaa nchini na kuwapa msaada wa kisheria, hasa wanawake na watoto, na pia kuunda madawati 28 ya jinsia, ambayo yapo katika vituo vya Polisi kuwawezesha watu wa ndoa na matatizo ya uhusiano, kusikilizwa kwa faragha wafikapo Polisi.

Akitoa hotuba katika sherehe hizo, Dk Shein alisema Serikali wakati wote imekuwa ikitambua mchango wa vyama vya kisheria na asasi za kiraia, kwa maendeleo ya nchi na utekelezaji wa haki na utawala bora, hivyo maombi yao kuhusu kutengewa fungu kutoka serikalini, atayafanyia kazi.

“Serikali tunategemeana nanyi katika kutafuta haki kwa wananchi wetu, bila haki hakuna amani, hivyo ninyi ndio mnaiwezesha Serikali kutekeleza haki, juhudi za kulinda amani zinafanikiwa kwa sababu yenu,” alisema Shein.

Alisema Tawla ina haki ya kujivunia uwezo mkubwa iliowajengea wanawake kujua haki zao na matunda yanaonesha kuwa wanawake wanaweza, kwa kuwa miongoni mwao kama Dk Asha-Rose Migiro (Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mwanaidi Maajar na majaji kadhaa, ni matunda ya chama hicho.

Shein aliitaka Tawla kutoridhika kwa mafanikio hayo bali miaka hiyo 20 iwe chanzo cha kujitathimini upya na kurekebisha upungufu wao ili kuwezesha ufanisi zaidi kwao na kuleta manufaa kwa wananchi wanaohitaji msaada wao.

Katika sherehe hizo pia watu mbalimbali walitunukiwa vyeti vya kutambua mchango wao katika kuanzishwa Tawla hadi ilipofika ambapo Jallya Katende, alitoa ushuhuda wa jinsi chama hicho kilivyomwezesha kupata haki zake baada ya kutalikiana na mumewe mwaka 2005.

Monday, May 10, 2010

TAWLA yatimiza miaka 20

MAKAMU wa Rais, Dk. Ali Mohamed Shein leo atakuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za maadhimisho ya miaka 20 ya Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (TAWLA) zitakazofanyika Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisi ya Makamu wa Rais, katika sherehe hizo, Dk. Shein atapokea maandamano ya wanasheria hao yatakayoanzia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu saa tatu asubuhi na kumalizikia viwanja vya Mnazi Mmoja.

Aidha, Makamu wa Rais atazindua Mpango Mkakati wa TAWLA wa miaka mitano unaoanzia mwaka 2010-2015, unaolenga katika kuendeleza utoaji wa msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto.

Mpango Mkakati huo pia unalenga kutoa elimu kuhusu haki za wanawake kumiliki mali, utawala bora kwa ujumla wake, masuala ya haki na ajira kwa watoto na kuendelea kufanya tafiti na kuelimisha jamii juu ya sheria zinazomkandamiza mwanamke ili zifanyiwe marekebisho.

Katika kuadhimisha miaka 20 ya TAWLA, wanasheria hao wamepanga kutoa huduma za msaada wa kisheria kwa wiki nzima katika ofisi zao zilizopo Dar es Salaam na kwenye vituo vingine mikoani vya Tanga, Arusha, Dodoma na Pwani.

Friday, May 7, 2010

Mkapa anguruma

NCHI za Afrika zimeambiwa kutegemea misaada kwa ajili ya maendeleo yao ni fedheha.

Hayo yalisemwa jana na Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa aliyekuwa akizungumza na wanahabari kuhusu Afrika kuendelea kubaki nyuma kimaendeleo.

Alionya tabia ya viongozi wa Afrika kufikiria wapi pa kupata misaada, badala ya nini cha kufanya wao wenyewe na wananchi wao kujiletea maendeleo, huku akisisitiza kuwa Wazungu wanaotusaidia huwaza namna ya kututawala.

Alikuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari kuhusu tatizo linalosababisha Bara la Afrika kuendelea kuwa nyuma kimaendeleo wakati lina maliasili za kutosha kujipatia maendeleo.

Kabla ya kujibu maswali hayo, Mkapa, Waziri Mkuu wa Ethiopia, Meles Zenawi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi (UN-Habitat), Profesa Anna Tibaijuka na Balozi wa zamani wa Uingereza nchini Ethiopia, Myles Wickstead, walikuwa wakizindua kwa mara ya pili Kamisheni ya Afrika.

Kamisheni hiyo iliandika ripoti iliyotumika kuangalia namna ya kukabiliana na changamoto za Afrika wakati wa Mkutano wa Nchi Tajiri Duniani (G8) mwaka 2005 na kuzinduliwa kwake kuna lengo la kuangalia kama mapendekezo ya ripoti hiyo yalitekelezwa.

“Nadhani tatizo ni kwa Waafrika kufikiria kuwa kuna watu wako mahali ambao wana jukumu la kuja kutuendeleza,” alisema na kurudia kauli hiyo mara mbili kuonesha kuwa hakukosea, bali anasisitiza.

“Hii biashara ya kutegemea wafadhili kuliko ilivyo kawaida inashtua na inadhalilisha, tunaangalia huku na huko kuangalia nani anatupa nini? “Mkitaka tuendelee, naweza kusema simameni wenyewe kwa miguu yenu, jipangeni na mjipe matumaini ya kufanikiwa, hiyo ndiyo iliyokuwa dhana ya kujitegemea,” alisema Mkapa kwa kujiamini.

Alimsifu Zenawi aliyekuwa katika mkutano huo, kuwa yeye anatumia fikra zake kwa nchi yake.

Kabla ya Mkapa kujibu, Zenawi alitaja baadhi ya mambo yanayosababisha Afrika kutoendelea kuwa ni pamoja na kuwa na miundombinu mibovu.

Baada ya kumalizika kwa mkutano huo wa habari kuhusu kuzinduliwa kwa kamisheni hiyo, Mkapa aliendelea kuelezea namna Afrika inavyoweza kuendelea katika hali ya sasa ya utandawazi.

“Hawa Wazungu tulipambana nao wakati wa Ukoloni mpaka ukafikia wakati wakaamua kutupa,” alisema na kuongeza kuwa bora kushirikiana na Wachina kuliko Wazungu ambao wanataka kututawala.

“Wachina ni rahisi kushirikiana nao, hawana takataka za Ukoloni, wanajua tuko huru na wao wako huru,” alisema Mkapa.

Kauli hiyo ya Mkapa, iliungwa mkono na Profesa Tibaijuka ambaye alisema tatizo lingine la nchi za kiafrika ni utamaduni.

Alifafanua kwamba nchi zilizofanikiwa Bara Asia zilipata mafanikio baada ya kubadilisha utamaduni wao na kujijengea wa kujiamini zaidi.

Wednesday, May 5, 2010

Kesi za Jeetu Kisutu zasimamishwa

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imetoa amri ya kusimamisha kesi ya wizi wa Sh bilioni 3.9 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), inayomkabili mfanyabiashara maarufu, Jayantkumar Chandubhai Patel, maarufu kwa jina la Jeetu Patel na wenzake watatu, hadi kesi yao ya kikatiba Mahakama Kuu itakapotolewa maamuzi.

Uamuzi huo ulitolewa jana na jopo la mahakimu linaloongozwa na Hakimu Ignas Kitusi, ambaye alikubaliana na maombi yaliyowasilishwa na mawakili Martin Matunda na Mabere Marando wa upande wa utetezi katika kesi hiyo.

Jeetu alifungua kesi Mahakama Kuu akidai kuvunjiwa haki ya kikatiba na Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni ya IPP, Reginard Mengi.

Mawakili wake wanadai kuwa Aprili 23, mwaka jana Mengi alitumia vyombo vya habari
kumuhukumu Jeetu kwa kumuita ‘Fisadi Papa’ wakati Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu inayosikiliza kesi dhidi ya mteja wao haijatoa hukumu.

Katika kesi hiyo mawakili hao wanaomba tafsiri ya kisheria kwani wanaamini haki ya mteja wao imevunjwa.

Jeetu pia anamshitaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kwa madai kuwa kwa nafasi zao walishindwa kutimiza wajibu wao kikamilifu baada ya Mengi kumuhukumu kupitia vyombo vya habari.

Katika kesi nyingine zinazofanana na hizo zinamkabili katika mahakama hiyo kwa mahakimu tofauti, mahakama hiyo ilitoa uamuzi kwamba kesi hizo zisimame ili kesi ya kikatiba iliyoko Mahakama Kuu iendelee.

Wakati huo mshtakiwa huyo ameukatia rufaa uamuzi wa Mahakama Kuu ulioamuru majalada ya kesi dhidi yake kurudi Mahakama ya Kisutu kutoka mahakama Kuu yalipokuwepo ili kuruhusu kesi dhidi yake na wenzake ziendelee.

Jeetu pamoja na wenzake Devendra Vinodbhai Patel, Amit Nady na Ketan Chohan wanakabiliwa na kesi nne za wizi wa fedha katika Akaunti ya EPA katika Mahakama ya Kisutu ambazo zilifunguliwa Novemba mwaka juzi.

Tuesday, May 4, 2010

Spika Sitta: Wala rushwa ni Wakoloni wapya

WALA rushwa wakubwa wanapaswa kuchukiwa kama Wakoloni wapya wanaopindisha kila jema linalojaribiwa ndani ya nchi na kufanya sera za siasa zionekane sawa na debe tupu.

Hayo yalisemwa jana na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania, Samuel Sitta, wakati akifungua kongamano la kitaifa la wadau wa kuzuia nakupambana na rusghwa nchini.

Sitta ambaye alimtaka Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) asinyooshewe vidole pekee kwa kuwa mapambano dhidi ya rushwa ni ya kila mtu, alisema dawa ya rushwa haiko mahakamani.

“Viongozi wenzetu wanaosema eti dawa ya rushwa ni Mahakama, hawana tofauti na watu wanaopuuzia kinga na kuhubiri tiba katika mazingira ambapo maradhi yanaongezeka kusambaa,” alisema Sitta.

Alisema ili rushwa iweze kutokomezwa, hapana budi kila mtu aunganishe nguvu zake katika hilo, la sivyo mapambano hayo yatakuwa ni sawa na bure.

Alisema jamii imekuwa ikifikiri kuwa mapambano ya rushwa ni ya Takukuru peke yake, suala alilosema ni dhana potofu na ambalo baadaye linaweza likaleta madhara makubwa.

“Hatupaswi kuiachia Takukuru peke yake katika mapambano haya,tena siku hizi watu hawasemi Takukuru bali kila mmoja Hoseah, Hoseah … kwa hilo tutakuwa hatusongi mbele, ni vema sote tukashirikiana kuitokomeza,” alisema Sitta katika mahojiano na waandishi wa habari baada ya ufunguzi.

Akitoa sababu ya kuifananisha rushwa na ukoloni, Sitta alisema sababu ni kwamba inaliwezesha kundi dogo la walafi wa mali na madaraka, kupindisha kila jema ndani ya nchi, hali inayochangia maisha ya wananchi kudidimia huku umasikini ukiongezeka.

Akizungumzia dawa ya rushwa kutokuwa mahakamani, Sitta alisema tatizo ni athari zake kuanzia mifumo mingine ya nyuma hadi kesi kufika mahakamani.

“Wapo wangapi ambao wametuhumiwa na makosa mbalimbali lakini hatujawaona kufikishwa mahakamani? Hivyo tiba si mahali hapo bali sote tukishikamana kwa pamoja na kuikataa rushwa,” aliongeza Sitta.

Dk Hoseah alisisitiza kuwa mapambano dhidi ya rushwa nchini yanahitaji nguvu zaidi na za pamoja ili kupata matunda mazuri.

Alisema siku zote jamii imekuwa ikipiga kelele za rushwa kila mahali, lakini tatizo hilo litaendelea kuathiri uchumi wa nchi kama mshikamano wa pamoja hautokuwapo.

Kongamano hilo la siku moja, lilikuwa na lengo la kutathmini mchango, changamoto za kila mmoja dhidi ya rushwa kwa mwaka jana sambamba na kuweka mikakati ya kuzikabili changamoto hizo mwaka huu.

Rais Kikwete:TUCTA waongo

“TUCTA ni waongo! Tucta ni wanafiki! Tucta wana hiana!... wafanyakazi watakaogoma tarehe 5, watakuwa wamekiuka sheria na watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria na kanuni za Serikali. Na wale wafanyakazi wataokwenda kazini lakini wasifanye kazi, pia watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

“Kiongozi bora ni yule anayewaeleza wananchi wake ukweli hata kama ukweli huo utakuwa unauma.”

Hiyo ni kauli nzito ya Rais Jakaya Kikwete, alipozungumza na Taifa kupitia wazee wa mkoa wa Dar es Salaam jana, kuhusu mgomo ulioitishwa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) kuanzia kesho, kwa madai kuwa Serikali imepuuza mapendekezo ya kuongezwa kwa kima cha chini ya mshahara kufikia Sh 315,000 kwa mwezi.

Rais alisema Serikali haiwezi kulipa kima cha chini cha Sh. 315,000 kutokana na mapato inayopata.

“Nimewasikia Tucta, wanasema huu ni mwaka wa uchaguzi, hawatanipigia kura kama sitalipa kima cha chini wanachokitaka, nipo tayari kuzikosa kura za wafanyakazi kuliko kuwadhulumu Watanzania walio wengi, wakakosa dawa, maji, barabara, elimu, pembejeo za kilimo na huduma nyingine,” alisisitiza Rais akionesha dhdhiri kukerwa na msimamo wa Shirikisho hilo.

Alisema pamoja na mazungumzo yanayoendelea sasa kwa lengo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi ikiwamo mishahara, viongozi wa Tucta kwa makusudi, wameamua kuitisha mgomo wa wafanyakazi huku wakitoa madai ya uongo, kwamba Serikali haisikii na viongozi wa Serikali hawawajali wafanyakazi.

Alieleza kushangazwa na kauli za viongozi wa Tucta wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), kauli ambazo kimsingi alisema zinajenga taswira kwamba hakuna mazungumzo yoyote yanayoendelea baina ya Serikali, waajiri na wafanyakazi, kupitia vyama vyao ya kushughulikia maslahi yao na kujenga hisia mbaya kwa wafanyakazi kwamba Serikali haiwathamini.

“Si kweli, Serikalii inawajali na kuwathamini sana wafanyakazi. Zipo hatua ambazo imechukua na inaendelea kuchukua katika kuboresha maslahi ya wafanyakazi.

“Tuliingia madarakani kima cha chini ya mshahara kikiwa Sh 65,000 lakini sasa ni Sh 104,000. Kwa makusudi viongozi wa Tucta wanawadanganya wafanyakazi kwamba Kikwete ameongeza Sh 4,000 tu tangu amekuwa Rais wa nchi, jambo ambalo ni uongo mkubwa,” alisema Rais Kikwete.

Alitoa mfano wa mazungumzo yaliyofanyika mwezi uliopita, ambapo pande hizo tatu; Serikali, waajiri na wafanyakazi, walikutana mara tatu Aprili 6, Aprili 26 na Aprili 27 kujadiliana kuhusu kima cha chini ya mshahara na wakashindwa kuafikiana kutokana na viongozi wa Tucta kuleta mapendekezo ya viwango vitatu vya kima cha chini cha mshahara baada ya Serikali kukataa kima cha chini cha awali cha Sh 315,000.

Alisema mazungumzo hayo yakapangwa kuendelea Mei 8 mwaka huu. “Wakati mazungumzo yamepangwa kufanyika tena Mei 8, ili wao waje na mapendekezo yao mengine ya kima cha chini cha mshahara, na sisi Serikali tulete mapendekezo yetu ili tujadiliane, viongozi hawa wa Tucta wanashindwa kusema ukweli na wanakana hata kile walichokisema na kupendekeza wao wenyewe ndani ya vikao halali,” alisema.

Rais alisistiza kuwa Serikali kwa upande wake, imekuwa ikiheshimu mapendekezo ya nyongeza ya kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi kupitia bodi nane za kisekta, na ndiyo maana kutokana na mazungumzo hayo, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya, alitangaza kima kipya kwa sekta binafsi Aprili 30, mwaka huu, ambacho kilianza kutumika Mei Mosi.

Alisema pia Serikali kupitia majadiliano hayo, imekubali kuongeza kima cha chini cha mshahara kwa watumishi wa umma, ongezeko ambalo litatangazwa katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha wa 2010/11, tofauti na kauli zinazotolewa na viongozi wa Tucta kwa wafanyakazi.

Aliongeza kuwa Serikali ina wafanyakazi 350,000 na endapo italipa kima cha chini cha mshahara cha Sh 315,000 italazimika kutumia Sh bilioni 6,852.93, fedha ambazo ni nyingi kuliko mapato ya Serikali, kwani katika bajeti ijayo, Serikali imepanga kukusanya Sh bilioni 5,757.3, na ili iweze kulipa kiasi hicho, italazimika kukopa jambo ambalo ni kichekesho.

“Kama tutalipa mishahara hii kama wafanyakazi wanavyotaka maana yake ni kwamba tutawaridhisha wafanyakazi hawa 350,000, lakini tutawadhulumu Watanzania milioni 39,650,000.

Hatutakuwa na pesa ya kuwanunulia dawa, kuwajengea barabara, kununua madaftari, kununua pembejeo za kilimo wala kuwapa maji safi na salama jambo ambalo siwezi kukubali litokee,” alisema.

Rais Kikwete katika hotuba hiyo iliyorushwa moja kwa moja na baadhi ya vituo vya redio na televisheni, alizungumzia pia mkutano mkubwa wa uchumi kwa Bara la Afrika, utakaofanyika kwa siku tatu Dar es Salaam kuanzia kesho, kwamba utasaidia kukuza na kutangaza jina la Tanzania.

Alisema viongozi na wakuu wa nchi 11 wamethibitisha kushiriki mkutano huo utakaoshirikisha zaidi ya watu 959 kutoka nchi 85 Duniani.

Alisema Tanzania kwa upande wake itanufaika kutangaza fursa ilizonazo katika vivutio vya utalii na uwekezaji.