Friday, November 28, 2008

Tukemee Ukatili wa aina hii !


Mimba Mashuleni, nini chanzo? Jamii iwajibike kupambana na hali hii!

Thursday, November 27, 2008

UKATILI HUU DHIDI YA ALBINO UTAISHA LINI?

Pichani Mwajuma Hassan ambaye anaulemavu wa ngozi (ALBINO) akibubujikwa na machozi baada ya kuona mchoro wa msichana albino aliyekatwa mikono hivi karibuni. Mchoro huu ni mojawapo wa michoro mingi ambayo ipo katika banda la maonyessho ya maadhimisho ya siku 16 za uanaharakati zinazoazimishwa katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Tanzania(TGNP. Maonyesho hayo yanaendela mpaka tarehe 10 Desemba 2008, karibu ujionee michoro inyoeleza hali halisi ya ukatili wa kijinsia. Usisubiri kusimuliwa!


(Picha Kwa hisani ya The Guardian, 27/11/2008.)

KILA KITUO CHA POLISI KUWA NA DAWATI LA KUHUDUMIA WAHANGA WA UKATILI WA KIJINSIA

Jeshi la Polisi nchini limejiandaa kikamirifu kuanzisha dawati (chumba) maalum la kushughulikia makosa ya ukatili wa kijinsia nchini. Kwa majaribio, kuanzia mwezi ujao (Desemba, 2008) kila kituo cha polisi kanda maalum ya Dar es Salaam kutakuwa na dawati hilo, na baadae mwakani kwa vituo vyote nchini. Hayo yalisemwa na Katibu wa Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania, Kamishna wa Polisi Elice Mapunda, ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Maafisa wa Polisi Kurasini Dar es Salaam, wakati akitoa tamko la Jeshi la Polisi kuhusu ukatili wa kijinsia kwenye tamasha la kuadhimisha siku 16 za Uanaharakati wa kupambana na ukatili wa kijinsia. Tamasha hilo liliandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na kufanyika katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Mabibo, Dar es Salaam.

Aliwataka wananchi na hasa wanawake wasiwe na wasiwasi na wawe na imani na polisi. “Najua wanawake wamekata tamaa na jinsi askari walivyokuwa wanawa-treat (wanawahudumia) wakifanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia. Awali tulikuwa hatujui nini maana ya ukatili wa kijinsia, lakini kwa jitihada za Mtandao wa Wanawake Polisi na Mashirika ya Wanaharakati mbali mbali, Polisi karibu wote wamepata mafunzo ya kupambana na ukatili wa kijinsia, kwa sasa tunaongea lugha moja. Tutumieni, tushirikiane tuweza kupunguza na hatimaye kutokomeza kabisa vitendo hivi”, alisema Kamishna Mapunda.

Aliwakumbusha wanaharakati kuwa ni haki ya kila mmoja kuhudumiwa na polisi pale anapofanyiwa ukatili wa kijinsia, na kuwataka kuakikisha kuwa watumia fursa hiyo ipasavyo. Pia alikariri tamko la mgeni rasmi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Utawala Bora, Mheshmiwa Sophia Simba kuwa mapambano ya kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia ni jukumu la jamii nzima. “Ukatili wa kijinsia ni suala la jamii nzima, si la mtu mmoja mmoja. Hivyo ili tuweze kutokemeza vitendo hivyo lazima jamii nzima tushirikiane. Polisi hawatoshi, jeshi lina takiribani polisi elfu thelathini na idadi ya watanzania ni takribani milioni arobaini kwa sasa; ambayo ni uwiano wa askari mmoja kwa watu mia nne hamsini!. Jamii nzima lazima ipambane” alisisitiza kikamanda.

Kamishna Mapunda alimalizia kwa kutoa changamoto kuwa kuwepo na dawati la kuhudumia wahanga wa ukatili wa kijinsia katika kila kituo cha polisi sio dawa, bali jamii bado inatakiwa kuelimishwa na kuamasishwa ili iweze kuona kuwa suala la ukatili wa kijinsia halifai na halina nafasi katika jamii yetu.

Tamko hilo lilipokelewa kwa furaha na mamia ya wanaharakati walioudhuria maadhimisho hayo kutoka mikoa yote ya Tanzania.

Wednesday, November 26, 2008

Pinga Ubakaji kwa Wanawake na Watoto


Wanawake na watoto wataendelea kubakwa mpaka lini? Usikae kimya, hakikisha sheria inachukua mkondo wake!

Tuesday, November 25, 2008

KONGAMANO KONGAMANO KONGAMANO

KATIKA KUADHIMISHA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA NCHINI TANZANIA NA MIAKA SITINI TANGU KUTOLEWA KWA TAMKO LA DUNIA LA HAKI ZA BINADAMU, MTANDAO WA JINSIA TANZANIA (TGNP), KWA KUSHIRIKIANA NA MASHIRIKA YANAYOTETEA MASUALA YA KIJINSIA, HAKI ZA BINADAMU NA UKOMBOZI WA MWANAMKE KIMAPINDUZI YAANI FEMACT, WAMEANDAA KONGAMANO KUBWA LITAKALOJADILI HATUA AMBAZO TANZANIA IMEFIKIA KATIKA KAMPENI YA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA NA JUU YA NINI KIFANYIKE KUBORESHA HALI ILIVYO SASA

KAULI MBIU YA MWAKA HUU NI: SISI KAMA JAMII TUNA UWEZO NA NIA YA KUZUIA UKATILI WA KIJINSIA

JOPO LA WAZUNGUMZAJI:
- TAMWA
- WLAC
- WOFATA
- KIWOHEDE / HOUSE OF PEACE
- WD
- TGNP

LINI: Jumatano Tarehe 26 Novemba 2008

Muda: Saa 8:00 Mchana – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo
Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni



WOTE MNAKARIBISHWA!!

Monday, November 24, 2008

AJIRA KWA VIJANA MUHIMU BARANI AFRIKA- JK

Jakaya Mrisho Kikwete amesema Mahitaji ya ajira kwa vijana ni makubwa zaidi katika nchi za Afrika , hivyo suala la kutengeneza ajira kwa vijana hao ni changamoto kubwa ya maendeleo inayolikabili Bara hilo na dunia kwa ujumla hivi sasa.

Rais kikwete ameyasema hayo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Afrika uliofanyika kwa siku moja tarehe 20 Novemba, 2008 Addis Ababa nchini Ethiopia ambao Mwenyekiti wake alikuwa Bwana Anders Fogh Rasmussen ambaye ni waziri Mkuu wa Denmark.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha Rose-Migiro.

Akifungua rasmi Mkutano huo uliofanyika katika Hoteli ya Sheraton Addis, Bwana Rasmussen amesema ajira ndiyo injini muhimu kwa maendeleo ya Bara la afrika na kwamba ongezeko la idadi ya vijana linawakilisha fursa pekee kwa Bara hilo ambayo inatakiwa kutumiwa kikamilifu katika harakati za kuleta maendeleo.

Amesema hatua madhubuti zinatakiwa kuchukuliwa ili kutoa msukumo katika kutekeleza Maendeleo ya Milenia (MDGs).Aidha amesema ukuaji wa uchumi hauna budi kuwanufaisha raia wote na ndiyo maana jitihada za Tume zimelenga, pamoja na mambo mengine, katika masuala ya ajira.
Kwa upande wake, Rais Kikwete amesema kwa zaidi ya asilimia 89 ya vijana duniani wanaishi katika nchi zinazoendelea na kwamba idadi ya vijana wanaoishi katika nchi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara ni asilimia 13 ya vijana wote duniani.

Amesema ajira kwa vijana zinahitaji ongezeko kubwa la uzalishaji na utengenezaji wa fursa zaidi za ajira kwa kuongeza kiwango cha uwekezaji wenye tija zaidi.

Ameainisha mambo muhimu katika kukabiliana na tatizo la ajira kuwa ni pamoja na utekelezaji wa dhana ya ushindani, ukuaji wa uchumi, ujasiriamali, maendeleo katika biashara pamoja na maendeleo ya elimu, mafunzo na ujuzi.

Mambo mengine ni uwezeshaji na kuwepo kwa fursa za kupata mikopo na kutumia vema fursa za sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano. Amesema ujasiriamali unatoa fursa kubwa zaidi za ajira kwa vijana na wanawake na hivyo kupunguza kiwango cha umaskini.

Hata hivyo amesema changamoto zilizopo ni namna ya kuwawezesha vijana kuwa wajasiriamali kati ya mamilioni ya vijana waliopo ambao kwa sasa hawana ajira, namna ya kuwasaidia wale ambao tayari wameanzisha biashara zao na namna ya kuwafanya wajasiriamali wadogo kukua hadi kufikia ngazi ya kati ya ujasiriamali.

Amevitaja vikwazo viwili vikubwa vya ujasiriamali kuwa ni kukosekana kwa ujuzi wa ujasiriamali na uhaba wa fursa za kupata mitaji.

Wednesday, November 19, 2008

EPA: Kama vile mchezo wa kuigiza

Baadhi ya watuhumiwa walalamika wanasiasa kuwatosa

WAKATI baadhi ya watuhumiwa wakiwa wamekwisha kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa fedha katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) ndani yaBenki Kuu (BoT), mbinu chafu zilizotumika na vigogo katika kuchota mabilioni ya fedha katika akaunti hiyo sasa zimebainika.

Mbinu hizo ni pamoja na kughushi nyaraka mbalimbali na kutumia kivuli cha siasa katika kupitisha nyaraka husika bila kufanyika kwa uhakiki wa kina wa uhalali wa nyaraka hizo, kazi iliyofanyika kwa kasi iliyowashangaza hata wakaguzi wazalendo na wale wa kimataifa waliopitia hesabu za BoT.

Mfano wa dhahiri uliotolewa tokea mwanzo ni ule wa kampuni ya Kagoda Agricultural Limited, ambayo ilithibishwa tokea mwanzo jinsi vigogo walivyoghushi nyaraka za kampuni 12 za kigeni kuweza kujichotea kiasi cha Sh bilioni 40.

Katika mchakato huo, Kagoda ilighushi nyaraka mbalimbali kuweza kujichotea kiasi cha Dola za Marekani 30,732,658.82 (takriban Sh bilioni 40), ikiwa ni pamoja na nyaraka hizo kupitishwa na maofisa wa BoT bila kufanyiwa uhakiki.

Waliowasha moto wa wizi huo walikuwa ni wakaguzi wa kimataifa wa kampuni ya Deloitte & Touche, ambao walitimuliwa na serikali baada ya kutokea kutokuelewana katika ukaguzi wa akaunti hiyo ambayo sasa inazidi kuisakama Serikali.

Deloitte & Touche, ambayo ilipewa kazi ya kukagua akaunti za BoT, ilikumbana na utata mkubwa katika akaunti ya EPA namba 99915091 01, na hivyo kuwa kiashirio cha kwanza cha utata mkubwa katika akaunti hiyo.

Maelezo yaliyoibua utata huo yanaonyesha kwamba aliyekuwa Gavana wa BoT, Marehemu Dk. Daudi Ballali, alianza kujulishwa mapema kuhusiana na wizi huo akipewa mfano wa dhahiri jinsi Kagoda Agriculture Limited ilivyoghushi nyaraka.

Mfano uliotolewa kudhihirisha uhalifu huo ni jinsi ambavyo mikataba ya ununuzi wa madeni kwa kampuni 12 ilivyosainiwa katika kipindi kifupi cha kati ya Septemba 10, 2005 na Novemba 5, 2005, kipindi ambacho kilielezwa kuwa ni vigumu kwa wahusika kutembelea mbalimbali duniani kutiliana saini.

Aidha, imefahamika kwamba nyaraka zote zilisainiwa na wakili mmoja tu B.M. Sanze, na kati ya hizo mikataba minne ilisainiwa Oktoba 18, 2005 na mitano ilisainiwa siku moja baadaye Oktoba 19, 2005, jambo ambalo lilitia shaka jinsi wawakilishi wa kampuni hizo za kigeni walivyoweza kusafiri kwa wakati mmoja wakitofautiana kwa saa chache, jambo ambalo lilishindwa kuthibitishwa kwa kutumia kumbukumbu za Uhamiaji.

Katika nyaraka hizo, mikataba miwili iliyosainiwa Oktoba 18, 2005 kuhusiana na kampuni mbili za Ujerumani, Lindeteves J Export BV na Hoechst ikionyesha kwamba kulikuwa na deni la Euro 1,164,402.76 badala ya fedha za Ujerumani (Deutsche Marks.)

Wachunguzi na wakaguzi wameshitushwa na kasi ya ajabu ya jinsi marekebisho ya makosa hayo yalivyofanyika kwa kipindi kifupi baada ya BoT kuifahamisha Kagoda Agriculture Limited; huku barua ya kutaka marekebisho yafanyike ikiwa na maelekezo ya kuidhinisha malipo ya Sh 8,196,673,600.53 kwenda kwenye akaunti ya Kagoda. Kampuni hiyo iliwasilisha mkataba uliorekebishwa siku mbili tu baada ya kujulishwa.

"Haiwezekani hata kidogo kwa kampuni ya kigeni inayodai kuandika fedha zisizo sahihi huku BoT ikiendelea kuidhinisha malipo bila kuhakiki mikataba yote 12 ambayo imeonekana kufanana kwa kila kitu ikiwa ni pamoja na maneno," inaeleza sehemu ya waraka wa wakaguzi.

Pamoja na kubainika kuwa mikataba na nyaraka zote hazikuwa na nembo ya kampuni huusika, nyaraka zote zilisainiwa katika ukurasa mmoja pekee wa mwisho tofauti na nyaraka za kisheria zinavyopasa kuwa.

Uchunguzi wa kina umebaini kufanana kwa mihuri ya kampuni zote zilizopitishwa ikiwa inalandana kabisa na muhuri wa kampuni za Kitanzania, tofauti ikiwa ni majina na anuani ya kampuni husika.

Mfano uliotolewa ni wa kampuni za Kitaliano za Fiat Veicoli Industriali na Adriano Gardella S.P.A pamoja na kampuni ya Kimarekani ya Valmet ambazo zote zimeonekana kuwa na mihuri na lugha zilizofanana katika nyaraka zote.

Utata mwingine uliodhihirika kughushi ni katika mkataba wa kampuni ya Valmet ya Marekani uliohusu Dola za Marekani 2,398,439.96 kusainiwa na Patrick Kevin, aliyetajwa kuwa Mhasibu wa kampuni hiyo, jambo ambalo limeelezwa kwamba ingekuwa vigumu kwa mhasibu kuachiwa kufanya kazi hiyo.

Utata mwingine uliobainika ni katika mkataba wa kampuni ya Daimler Benz AG ambao ulionyesha kusainiwa na Mkurugenzi aliyetajwa kwa jina la Christopher Williams, huku sahihi yake ikisomeka 'W Christopher'.

Uchunguzi wa ziada ulithibitisha kwamba baadhi ya kampuni zilikwishakufa wakati mikataba hiyo ikisainiwa na kampuni za Kitanzania, jambo ambalo linaendelea kuthibitisha wizi mkubwa wa kutumia maandishi uliofanywa katika akaunti ya EPA.

Mifano hai ni kampuni za Hoechst AG iliyobadilika na kuwa Aventis mwaka 1999, Daimler Benz AG iliyobadilika na kuwa Daimler Chrysler AG mwaka 1998 na Fiat Veicoli Industriali iliyobadilishwa na kuwa Industrial Vehicle Corporation (IVECO) tokea Januar1 1, 1975.

Kampuni nyingine zilizobadilika ni Mirrlees Blackstone kuwa MAN B&W Diesel Limited mwaka 2002/03 na Valmet iliyobadilishwa na kuwa Metso Paper kuanzia Mei 10, 2000. Utata huo uliwafanya wachunguzi na wakaguzi kujiuliza ilikuwaje kampuni zote hizo kuingia mikataba mwaka 2005 kwa kutumia majina ya zamani.

Pamoja na kuingiwa kwa mikataba hiyo na kampuni zilizokwisha badilishwa majina na umiliki wake, kampuni za sasa zenye uhusiano na kampuni zilizoingia mkataba zimekanusha kufahamu watu waliotajwa kuziwakilisha katika mikataba hiyo.

Kagoda ambayo ilisajiliwa Septemba 29, 2005, na kujichotea Sh bilioni 40 katika kipindi cha mwezi mmoja tu, jambo ambalo limewashangaza wengi kuona kampuni ngeni isiyofahamika inawezaje kuaminiwa kiasi kikubwa cha fedha bila kuhakikiwa.

"Inashangaza jinsi BoT ilivyoweza kuamini kampuni mpya kuwasilisha nyaraka za mabilioni ya fedha kwa kuingia makubaliano na kampuni za kigeni katika nchi za Ujerumani, Italia, Yugoslavia, Uingereza, Marekani na Japan kwa muda mfupi kiasi hicho bila kutilia shaka," wamehoji wakaguzi waliokagua hesabu za BoT.

Tayari kampuni ya Kagoda Agricultural Limited imekuwa gumzo katika sakata zima la EPA. Inafahamika kwamba kati ya shilingi bilioni 90 zilizoibwa katika akaunti ya EPA, sehemu kubwa ilichukuliwa na kampuni ya Kagoda Agricultural Limited ambayo hadi sasa wahusika wake hawajaguswa pamoja na kujitokeza kwa vigogo wawili kurejesha fedha zilizoibwa na kampuni hiyo.

Vyanzo vya uhakika vinaeleza kwamba sehemu kubwa ya Shilingi bilioni 90 zilizothibitika kuchukuliwa kihalifu zilichukuliwa na makundi mawili tu, kundi la kwanza likiwa chini ya Jeetu Patel na lingine likiwa chini ya usimamizi wa vigogo wawili waliotumia kampuni ya Kagoda.

Imefahamika kwamba kwa sasa kuna hekaheka kubwa za kutaka kuzuia kushitakiwa kwa wahusika wa Kagoda, lakini vyanzo vya ndani ya Serikali vimeeleza kwamba kwa sasa Serikali haitabiriki na lolote linaweza kutokea wakati wowote kabla ya mwisho wa mwaka.

Kumekuwa na utata kuhusiana na ilipo na umiliki wa Kagoda Agricultural Limited. Hakuna anayeweza kubainisha hasa zilipo ofisi na wahusika wa kampuni hiyo tata.

Kumbukumbu za BRELA zinaonyesha kwamba ofisi zake zipo Kipawa Industrial Area Plot namba 87, Temeke, Dar es Salaam lakini eneo hilo lina makampuni tofauti jirani lakini namba iliyotajwa haionekani na badala yake eneo lenye ofisi na kampuni viwanja vyenye namba 77, 86 na 88 katika eneo hilo la viwanda.

Katika ukaguzi wake wa awali wa mkaguzi wa nje Samuel Sithole kutoka kampuni ya Kimataifa ya Deloitte & Touche yenye makao yake Afrika Kusini alionya kuhusu matendo ya kihalifu ndani ya Kagoda kabla ya kuandikiwa barua na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji kwamba fedha hizo zilienda katika mambo "nyeti" ya kiusalama.

Hata hivyo siku nne baada ya kuandika barua hiyo, Meghji alifuta barua hiyo akielezea kupotoshwa na aliyekua Gavana, Dk. Daudi Ballali, uamuzi ambao ulimgharimu kwa kiasi kikubwa mwanamama huyo makini ambaye alijikuta akiachwa nje ya Baraza la Mawaziri.

Wakati Rais Jakaya Kikwete akisema serikali yake haitomuingilia Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), watuhumiwa wengi walikamatwa na kufikishwa mahakamani walikuwa wamejiaminisha kuwa wamekwishapona na sasa waliobaki "hawalali" kuhofia kushitukizwa na kupandishwa kizimbani.

Tayari watu 20 wamekwisha kufikishwa mahakamani baada ya wafanyabiashara watatu kufikishwa mahakamani Jumatatu wiki hii wakitanguliwa na watuhumiwa wengine wakiwamo watumishi wa BoT waliohusika katika mchakato wa wizi huo.

Waliopandishwa kizimbani ni Ajay Somani na Jai Somani wanaodaiwa kula njama ya wizi wakiwa na watu wengine ambao hawajafahamika kuiibia BoT na kwamba Septemba 2, 2005 waliiba Sh. bilioni 5.9 mali ya benki hiyo.

Mtuhumiwa mwingine aliyefikishwa mahamani ni mfanyabiashara Mwesiga Lukaza, aliyepandishwa kizimbani akiunganishwa na mshtakiwa mwingine Johnson Lukaza, ambaye alishapandishwa kizimbani mapema wiki hii.

Watuhumiwa wengine ambao tayari wamefikishwa mahakamani ni Farijala Hussein, Rajab Maranda, Japhet Lema, Bahati Mahenge, Davis Kamungu, Godfrey Mosha, Manase Mwakale na Eddah Mwakale, Devendra Vinodbhai Patel, Amit Nandy, Ketan Chohan, Jayantkumar Chandubahi Patel na Johnson Lukaza.

Wengine ni wafanyakazi wa BoT ambao ni Mkuu wa Idara ya Madeni ya Biashara, Iman David Mwakyosa, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Madeni, Ester Mary Komu na makaimu Katibu wa benki wawili ambao ni Bosco Ndimbo Kimela na Sofia Joseph Lakila.

Raia Mwema
November 19, 2008

Monday, November 17, 2008

Policy and Budget Analysis training

TGNP through ALC is conducting a training on policy and budget analysis for its partners and stakeholders (IGNs Networks/Movement Building Groups and GDSS). The training will be conducted for four days between 17th - 18th and 20th- 21st November 2008 at TGNP Mabibo Dar Es Salaam from 8.30 am.

The objectives of this session are:

-To share key gender/transformative feminist issues in policy and budgeting

-Enhance participants on policy and budget analysis from Transformative Feminist outlook

-To share tools of analysis with participants to be used in their own areas

-To share experiences/information and Networking

We are banking on your collective collaborations in organizing for this training.

Monday, November 10, 2008

Mrejesho wa Semina ya GDSS ya Tarehe 05/11/2008.

Mrejesho wa Semina ya GDSS ya Tarehe 05/11/2008.

Mada katika semina ya Jumatano ya tarehe 05/11/2006 ilikuwa ni, Mrejesho wa Wanaharakati kutoka katika vikundi mbalimbali ambao walikwenda kufuatilia kero zilizopo katika maeneo yao. Vikundi ambavyo vilifanikiwa kutoa mrejesho ni pamoja na; Kigamboni clusters, Kigogo, Makuburi, Mwananyamala, Kinondoni, na Kawe.

Baadhi ya Kero ambazo zilitajwa na wanaharakati wengi ni pamoja na;

- Haki ya kushiriki katika ngazi mbalimbali za maamuzi hasa ngazi ya Kata na Serikali ya mtaa. Katika Maeneo mengi bado wananchi hawapati fursa ya kushiriki katika vikao vya serikali za mitaa, hivyo kushindwa kufuatilia ama kutoa maamuzi ya mambo mbalimbali ya maendeleo katika maeneo hayo.

- Haki ya kupata maji safi na salama. Bado katika maeneo mengi jijini Dar es Salaam maji safi na salama limekuwa ni tatizo sugu, wakazi wengi bado hawapati maji safi na salama ya kunywa na ya matumizi ya kawaida, hivyo wanawake wamekuwa wakitumia muda mwingi kutafuta maji maeneo ya mbali hivyo kuwazidishia mzigo wa kazi wanawake.

- Haki ya kuendelea na masomo kwa watoto wa kike wanaopata mimba wakiwa shuleni. Bado watoto wanaopata mimba wakiwa mashuleni hawaruhusuwi kuendelea na masomo, kitu ambacho kinawanyima haki watoto wa kike kuendela na masomo. Pia wahalifu wanaowapa mimba watoto wa kike hawachukuliwi hatua kali za kisheria kitu ambacho kinaongeza wigo wa tatizo hili.

- Rushwa katika vituo vya polisi na ukatili wa kijinsia. Katika baadhi ya vituo vya polisi hapa nchini vimekuwa vikituhumiwa kwa vitendo vya rushwa; ambapo askari wanawadai rushwa watuhumiwa wa kesi mbalimbali na kusababisha kupindishwa kwa haki za wadai. Pia askari wa wanaume wamekuwa wakilalamikiwa kwa kuwatendea watuhumiwa wanawake vitendo vya unyanyasaji wakijinisa kwa kuwadai rushwa ya ngono.

- Ajira kwa watoto wa kike hasa wale wanaoachishwa shule ili waende kutumika katika kazi za ndani, katika mabaa, ama katika madanguro.

Changamoto.
Harakati hizi za kutatua kero za wananchi zinakabiliwa na changamoto zifuatazo;

- Changamoto kubwa iliyopo ni kuweza kuunganisha nguvu ya pamoja ya wanaharakati katika ufuatiliaji kero mbalimbali, kwa mfano wanaharakati wameshindwa kuunganisha nguvu za pamoja katika kudai maswala mbalimbali ya kijamii, jambo ambalo limesababisha nguvu nyingi kupotea inapotokea vikundi viwili ama zaidi kupigania swala moja na kuacha sekta zingine bila utetezi.

- Kukosekana kwa mbinu shirikishi katika ufuatiliaji wa mambo mbalimbali katika ngazi ya mtaa, jambo amblo limesababisha wanaharakati kufanya kazi pekee yao badala ya kuwatumia wanajamii hivyo kuweza kuongeza ushiriki mkubwa zaidi katika kufuatilia mambo. Pia hii itasaidia jamii kudai mambo ambayo wanahisi wanayahitaji zaidi kuliko wanaharakati kupambana pekee yao.

- Changamoto nyingine kwa wanaharakati ni katika kutambua kiini cha tatizo ambacho kinasababisha kuwepo kwa kero nyingi katika jamii. Kwa mfano badala ya wanaharakati kupambana na huduma mbovu za afya hasa katika swala la afya ya uzazi kwa kuwatupia mpira waauguzi wa afya pekee na kuacha mfumo mzima ambao unasababisha huduma ziwe mbaya, kwa mfano kuna hospitali zina waaguzi wawili wa afya na wanahudumia zaidi ya wazazi 50 kwa siku, kwa hali hiyo lazima huduma itakuwa si nzuri. Hivyo changamoto kwa wanaharakti ni kuongeza wigo wa mapambano na kuungalia kiini halisi cha tatizo.

Mwanaharakati unafanya nini cha ziada kuhakikisha kwamba serikali inatatua kero hizi? Kwa maoni yako, Serikali imefanya vya kutosha katika kutatua kero hizi?

Monday, November 3, 2008

Tunataka haki, si kafara za kisiasa

WIKI na miezi imepita, na sasa umepita ule muda ambao Rais Jakaya Kikwete aliwapa mafisadi waliokwiba fedha za umma za EPA, kuzirejesha.

Wakati akilihutubia Bunge, mjini Dodoma, Agosti 21, 2008, Rais Kikwete aliiongezea muda kamati yake maalumu inayochunguza wizi huo na kuipa hadi Oktoba 31 kuikamilisha kazi hiyo; hatua iliyolenga kuwapa mafisadi hao fursa nyingine ya kurejesha fedha hizo na mpaka hivi juzi wakati akilihutubia taifa katika utaratibu wake wa wa kila mwezi aliueleza umma wa watanzania kuwa muda aliowapa wanaotuhumiwa kuiba fedha hizo wazirudishe baadadhi yao hawajafanya hivyo na kusema ambao hawajarejesha watafikishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa.

Tulipata kusema huko nyuma, na hatuoni haya kurudia kusema tena na tena; kwamba haki haipo katika kurejeshwa kwa fedha hizo; bali ipo katika kuwachukulia hatua za kisheria wezi hao.

Tulisema huko nyuma na tunasisitiza kusema tena kwamba Serikali itakuwa haisimamii haki kama itaacha kuwafikisha mafisadi hao mahakamani; eti kwavile tu wamerejesha pesa walizoiba.

Na kama ndivyo itakavyotokea hiyo Novemba mosi; yaani mafisadi waliorejesha fedha hizo kutoshitakiwa, basi, ingekuwa vyema pia kwa Serikali kuwatangazia msamaha wezi wote wa pesa za umma walioko vifungoni kama nao watarejesha fedha walizokwiba.

Maana; hatuwezi kukubali kuiachia nchi yetu kuwa na sheria mbili – moja kwa wanyonge na nyingine kwa vigogo na mafisadi. Kwa usalama na amani yetu sote na ya wanetu, ni lazima tuendelee kujenga nchi ambayo raia wote ni sawa mbele ya sheria.

Aidha, wananchi walitarajia kwamba mafisadi walioghushi na kuiba fedha za EPA watakaofikishwa mahakamani, ni vigogo hasa wa wizi huo wa pesa za umma, na si watu waliotafutwa kutolewa kafara za kisiasa; ilhali vigogo wenyewe wa ufisadi wa EPA wamefichwa nyuma ya pazia.

Labda tumkumbushe tena Rais wetu, Jakaya Kikwete kwamba wizi huo wa kihistoria wa pesa za EPA, umemweka yeye binafsi katika majaribu makubwa.

Wizi huo wa EPA ni mtihani mkubwa ambao Rais anapaswa kuuvuka kwa kutenda haki, na hiyo ni kama hataki wananchi waendelee kupoteza imani na namna anavyoiendesha vita dhidi ya ufisadi nchini.

Yeye mwenyewe Rais ni shuhuda, wakati wa ziara zake mikoani, jinsi wananchi wanavyoilalamikia kero hiyo ya kushamiri kwa ufisadi nchini. Wasiwasi wetu ni kwamba kama atashindwa kuchukua hatua za kuridhisha dhidi ya wahusika, atapoteza imani ya wananchi wake, na wakati mwingine itadhaniwa kuwa kuna kundi la mafisadi nchini ambalo “halishikiki”.

Na ili hilo lisitokee, ni vyema basi, kwa Rais Kikwete kujipa ujasiri wa hali ya juu na kuwafikisha mafisadi wote wa EPA mahakamani; bila kujali walirejesha fedha walizoiba au la, na bila kujali ni wafadhili au si wafadhili wa chama chake CCM.