Tuesday, May 31, 2011

Mwanafunzi mgonjwa wa moyo auawa kwa kubakwa

GENGE la watu wasiofahamika, wanatuhumiwa kumbaka na kumsababishia kifo mwanafunzi wa kike wa kidato cha nne mwenye umri wa miaka 21, aliyekuwa akisumbuliwa pia na ugonjwa wa moyo.

Mwanafunzi huyo alikuwa akisoma katika sekondari ya Msakila mjini Sumbawanga na moyo wake baada ya kupimwa kitabibu ulibainika kuwa mkubwa kuliko kawaida.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Dk. Saduni Kabuma, alisema jana kuwa mwanafunzi huyo alifariki dunia usiku wa kuamkia jana, muda mfupi baada ya kufikishwa katika hospitali ya mkoa mjini hapa kwa matibabu.

Alikizungumza jana kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi, Dk. Kabuma alisema alibainika amejeruhiwa vibaya sehemu za siri na pamoja na majeraha hayo pia kiafya alikuwa dhaifu.

"Alipokewa akiwa mzima ila alikuwa amejeruhiwa sehemu za siri na hali yake ilibadilika ghafla na kufariki dunia muda mfupi hali iliyotufanya tufikie uamuzi wa kuchunguza mwili wake zaidi ndipo tukabaini kuwa alikuwa na moyo mkubwa kupita kiasi … kubakwa kwake kuliharakisha kifo chake," alisema Dk. Kabuma

Alisema rekodi ya afya yake hospitalini hapo imeonesha kuwa alikuwa akisumbuliwa mara kwa mara na ugonjwa wa moyo na pumu.

Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Isuto Mantage, alisema mwanafunzi huyo alifikwa na mauti Jumamosi saa mbili usiku katika kitongoji cha Hali ya Hewa, eneo la Chanji mjini hapa.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda Mantage, alisema, usiku huo wa tukio marehemu aliaga nyumbani kuwa alikuwa anakwenda kununua vocha, ili aongeze salio kwenye simu yake ya mkononi.

"Sasa wakati akiwa anarejea nyumbani tena akiwa peke yake, alivamiwa na genge la watu wasiofahamika ambao walimbaka kwa zamu wakamjeruhi sehemu za siri kwa kitu chenye ncha kali na kumsababishia maumivu makali.

Wasamaria wema walipomkuta walimkimbiza hospitali ya mkoa, lakini alifariki dunia wakati anapatiwa matibabu," alisema Kamanda.

Kwa mujibu wa Kamanda wabakaji hao walikimbilia kusikojulikana na Polisi inaendelea kuwatafuta ili iwakamate na sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Dk. Slaa, Lema wanusurika kusota rumande

UPEPO wa kuswekwa rumande jana nusura uwakumbe Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa na Aquelini Chuwa mkoani Arusha baada ya polisi kutaka kuwakamata walipokwenda kujisalimisha mahakamani.

Wiki iliyopita Mei 27, Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Arusha Charles Magesa alitoa
amri ya kukamatwa kwa Lema, Dk. Slaa, Freeman Mbowe, Philemon Ndesamburo na Josephin Slaa kwa kushindwa kuhudhuria mahakamani bila ya taarifa yoyote na kuamuru polisi kuwakamata popote walipo.

Sakata hilo lilianza saa 8.15 mchana wakati watuhumiwa hao waliporudi mahakamani saa
saba baada ya kufika saa 3 asubuhi na kuambiwa kurudi muda huo.

Baada ya kukaa kwa muda wa saa 1.15 mawakili wa washitakiwa hao Method Kimomogolo na Albart Msando walimwona Hakimu Mfawidhi kumjulisha kuwa watuhumiwa Lema na Slaa walikuwa nje na walikwenda kujisalimisha, hatua iliyopingwa na Hakimu Magesa.

Kwa mujibu wa Msando, Hakimu Magesa alisema yeye alishatoa amri ya watuhumiwa wote
kukamatwa kwa kudharau mahakama wao na wadhamini wao hivyo kilichotakiwa ni kukamatwa na kupelekwa Kituo Kikuu cha Polisi na baadayekuletwa mahakamani.

Wakili Msando alisema, sababu hiyo iliungwa mkono na Wakili wa Serikali Mwandamizi EdwinKakoraki na kupiga simu polisi kuwaita ili wawakamate Lema, Slaa na Chuwa ili waende
kwanza rumande na baadaye kuletwa mahakamani kujibu shitaka la kuidharau mahakama.

Muda mfupi tu magari mawili ya polisi yaliwasili yenye namba za usajili PT 1177 na PT 1414
yakiwa na askari wasiopungua 12 huku wakiwa na silaha tayari kuwapeleka watuhumiwa hao rumande.

Ubishi ulizuka kwa Dk. Slaa na Lema kugoma kwenda polisi na kudai kuwa wao wamekwenda
wenyewe mahakamani kujisalimisha baada ya kutolewa hati ya wao kukamatwa “hivyo
mwenye mamlaka ya sisi kukamatwa kwenda rumande ni hakimu mwenyewe na sio nyie polisi hapa hatuondoki,” alisema Dk. Slaa.

Wakati malumbano hayo yakiendelea mawakili wa washitakiwa walikuwa katika chumba cha
hakimu Magesa wakimsihi asikilize sababu za watuhumiwa kujisalimisha; alikubali kusikiliza
hoja zao.

Alisikiliza hoja za upande wa utetezi kuhusu kutokufika mahakamani kwa wateja wao na kutolewa sababu mbalimbali, lakini upande wa serikali uliomba muda kupitia uhalali wa vyeti kwa watuhumiwa ambao walidai kwamba walikuwa wagonjwa.

Hakimu huyo aliahirisha kesi hiyo hadi leo saa 7 mchana ili asikilize sababu za wakili wa serikali na kutoa uamuzi wa jumla ya juu ya kufuta dhamana na kutofuta dhamana kwa washitakiwa kwa kukiuka kuhudhuria mahakamani bila ya sababu za msingi.

Monday, May 30, 2011

Askofu amtaka Kikwete kutowavumilia wazembe

MWENYEKITI wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa la Mennonite Tanzania (KMT), Askofu Steven Mang’ana amemtaka Rais Jakaya Kikwete kutokuwa tayari kuwavumilia viongozi wazembe serikalini ambao hawatekelezi na kutimiza wajibu wao kwa wananchi.

Askofu Mang’ana aliyasema hayo jijini hapa wakati wa sherehe za kusimikwa kwa Askofu Mteule Albert Randa kuwa Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Mwanza, ambazo Rais Kikwete alikuwa mgeni rasmi.

Alisema ifike wakati kila mtendaji serikalini aone kuwa ana jukumu kubwa la kutanguliza uzalendo na mapenzi ya nchi yake kwa kutumia nafasi aliyonayo, ashughulike na changamoto lukuki zinazowakabili wananchi, zikiwemo zile za huduma muhimu za kijamii.

Alisema wapo viongozi walioteuliwa na Rais katika nafasi nyeti serikalini, lakini utendaji wake umekuwa sio wa kuridhisha na kumtaka Rais Kikwete achukue hatua mara moja za kuwawajibisha.

“Mheshimiwa Rais anamteua mtu kushika nafasi nyeti serikalini na badala ya yeye kuwajibika na kumsaidia, anabaki kucheza tu, Rais nakuomba uwaondoe viongozi wa aina hii…wapo wengi na wenye uwezo wa kufanya kazi, viongozi wa aina hii hawakusaidii,” alisema.

Aliwataka viongozi wa madhehebu ya dini kutokuwa mahiri katika kukosoa serikali, bali waipe ushirikiano wa kutosha.

“Viongozi wa dini msiwe wepesi katika kuilaumu na kuikosoa serikali, tambueni kuwa Mungu anawapeni nafasi hiyo ili kusaidia taifa letu na Rais wetu ni msikivu ana hekima, busara na upendo hivyo mpeni ushirikiano,” alisema Askofu Mang’ana na kuongeza: “Katika nchi yetu, tunawataka viongozi wawajibikaji walio na uchungu na nchi, wanaomsaidia Rais wetu katika kutekeleza majukumu ya msingi ya kulihudumia taifa, sio Rais wetu aende kushughulikia tatizo dogo la ukosefu wa maji Ubungo, ilihali wasaidizi wake wapo.

“Tunawataka watendaji wa mitaa, serikali za vijiji, wabunge na mawaziri wawajibike kwa wananchi.”

Aidha, aliwataka baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nchini kuacha tabia ya kushiriki kwenye maandamano kwa lengo la kujipatia umaarufu wa kisiasa na kusema kuwa kufanya hivyo ni kuingiza nchi katika machafuko na kusababisha kupotea kwa amani nchini kama hali ilivyo katika nchi za Libya na Misri.

“Viongozi wetu lazima wawe tayari katika kuilinda amani iliyopo nchini, kushiriki katika maandamano kama njia ya kuishinikiza serikali ili kudai haki sio sawa, hivi hakuna njia nyingine ya kudai haki, sharti watu washiriki kwenye maandamano tu?” Alihoji askofu huyo.

Kwa upande wake, Rais Kikwete aliwataka viongozi wa dini nchini kuwapatia fursa za nafasi za kusoma kwenye shule zao vijana watakaokuwa wanajiunga na shule za sekondari za kidato cha tano na sita kwa kuwa mahitaji ya shule hizo kwa sasa yatakuwa makubwa kwa miaka ijayo kutokana na wingi wa wanafunzi wanaofaulu kutoka katika sekondari za kata nchini.

“Niwaombe viongozi wa madhehebu ya dini na shule zenu muwapatie fursa vijana wetu wanaochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na sita kwa miaka ijayo ili waweze kusoma maana mahitaji ya nafasi hizo ni makubwa na serikali peke yake haiwezi, maana nikiri kuwa tulijenga sekondari za kata bila ya kuwa na maandalizi ya nafasi za shule kwa ajili ya kidato cha tano na sita,” alisema Rais Kikwete.

Kuhusu udhibiti wa dawa ya kulevya nchini, aliyaomba madhehebu ya dini nchini kwa kushirikiana na wananchi kuongeza udhibiti wa vitendo vya dawa za kulevya, kwani alisema hali sio nzuri kwa sasa.

Alisema mwaka jana, watu 12,119 walifikishwa mahakamani kutokana na kupatikana na dawa za kulevya, ambapo kiasi cha kilo 190 na gramu 780 za heroini zilikamatwa, kilo 65 za kokeini na kilo 27,9520 za bangi na mirungi kilo 10,310 ilikamatwa.

“Hali sio nzuri kwa Mkoa wa Mwanza juu ya kuwa na wingi wa dawa ya kulevya, naomba kwa pamoja viongozi wa dini na serikali tushirikiane katika kuidhibiti hali hiyo,” alisema Rais Kikwete.

Friday, May 27, 2011

Yanayoendelea Nyamongo




Ndugu zangu,

PICHA ya jeneza lililotelekezwa barabarani imeongea zaidi ya maneno milioni moja. Kwa Watanzania, imetutia simanzi, imetutoa machozi. Ndani ya jeneza hilo pichani kuna mwili wa marehemu Emmanuel Magige iliyotelekezwa kijijini Nyakunguru, Tarime. Emmanuel Magige hakuwa jambazi. Ni Mtanzania mwenzetu mwanakijiji wa kawaida. Aliyetelekezwa si Magige tu, kuna maiti nyingine tatu.

Mauaji ya Nyamonngo yanatukumbusha Arusha, yanatukumbusha Mbarali. Yanatutia hofu mpya pia. Hatujui kesho yatafanyika wapi.Kupunguza aibu hii ni kwa wote waliohusika na mauaji haya kuchukuliwa hatua za kisheria.

Jeneza la Emmanuel Magige lililotelekezwa barabarani ni kielelezo cha mahali tulipofikia. Kuna chuki inajengeka. Na katika tofauti zetu hizi za kiitikadi tusifike mahali tukashindwa kuongea kama Watanzania. Tusifike mahali tukachochea machafuko makubwa ya kijamii. Wanasiasa wana jukumu la kutanguliza busara katika kila maamuzi wayafanyao.

Na tuyalaani vikali mauaji ya Nyamongo. Tusipoyalaani nasi tutalaaniwa. Na Mungu huyu anatupenda Watanzania, kuna tunachoonyeshwa. Na tuzisome kwa makini alama hizi za nyakati. Na Miungu yetu, mizimu ya mababu zetu, inatupenda pia. Walikolala mababu zetu, nao wanaturajia tulaani kitendo hiki, maana, hata katika mila na desturi zetu, Waafrika hatutelekezi maiti zetu. Tunazizika.

Ndio, kwa jadi yetu, Waafrika tunahesabu wafu wetu, tunawatambua kwa majina, tunawaombea kwa imani zetu. Ndio, tunawazika wafu wetu. Kwa heshima zote.
Kwa desturi, Watanzania hatupendi kuwa katika hali ya kudharauliwa na kutothaminiwa kwa utu wetu tukiwa hai. Na kamwe, tusikubali Watanzania wenzetu wasithaminiwe wakiwa katika hali ya umauti. Na hilo ni Neno la Leo.

Maggid
Iringa,
Alhamisi, Mei 26, 2011

Thursday, May 26, 2011

UVCCM Arusha si shwari

HALI si shwari ndani ya Umoja wa Vijana Mkoa wa Arusha (UVCCM) kwa kuwa jana kundi lingine la umoja huo liliibuka na kumtaka Mwenyekiti wa umoja huo Mkoa wa Arusha, James Ole Millya aache kufikiria kwa kutumia tumbo na badala yake atumie kichwa.

Wiki iliyopita, kundi lingine linaloonekana linamuunga mkono Millya, lilifanya maandamano hadi katika ofisi za Mkoa za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kumtaka Katibu wa CCM Mkoa, Mary Chatanda kuachia ngazi kwa kumtuhumu kuwa alisababisha Jimbo la Arusha kwenda upinzani na vurugu za umeya wa Jiji la Arusha.

Akisoma tamko la UVCCM Mkoa wa Arusha mbele ya wajumbe zaidi ya 40 wa umoja huo kutoka wilaya za Arusha, Ally Said maarufu kwa jina la Babu, alidai Millya ameshindwa kuitumikia jumuiya, hivyo afukuzwe ama ajiuzulu mwenyewe kwa kukosa sifa.

Said katika tamko hilo ambalo gazeti hili ina nakala, alidai Millya ameshindwa kuwajibika ndani ya UVCCM mkoa na badala yake anagawa vijana kwa kutumiwa na mafisadi, hatua aliyodai ni hatari hapo baadaye.

Saidi ambaye ni Mjumbe wa Baraza la UVCCM Wilaya ya Arusha Mjini, alidai Ally Bananga anayedaiwa kuwa kibaraka wa Millya anayetumiwa na Mwenyekiti huyo kutoa matamko, si kiongozi wa jumuiya hiyo kuanzia ngazi ya tawi hadi Taifa hivyo kumtaka akae kimya kwani anatumia mdomo kuganga njaa yake.

Tamko hilo pia lilimuonya Mbunge wa Viti Maalumu kupitia UVCCM Mkoa wa Arusha, Catherine Maige aache mara moja kutumia fedha za mafisadi kuwagawa vijana wa Arusha kabla ya haijatumika haki ya kikanuni ya kumsimamisha ubunge.

Said alisema, maamuzi ya kujivua gamba kwa watu walioamriwa na NEC ni lazima yatekelezwe ili kukisafisha chama kwa wananchi.

Akizungumzia tamko hilo, Millya alisema hao ni vijana kutoka katika kata mbili za mjini Arusha na ni vijana wanaoshinda katika vijiwe vya kahawa na sio wajumbe kutoka katika wilaya za Mkoa wa Arusha.

Huku akikanusha kutumiwa na mafisadi, Millya alisisitiza kuwa msimamo wake ni kutaka Chatanda kuachia ngazi kwani anakula mishahara miwili kinyume cha taratibu za kikazi na hawezi kuwajibika katika Mkoa wa Arusha kama katibu wa chama.

Kwa upande wake, Magige alipoulizwa kwa simu juu ya madai ya kutumia fedha za mafisadi kuigawa UVCCM Mkoa wa Arusha, alisema sio kweli, bali anasaidia vijana kujikomboa na kugawa misaada sehemu mbalimbali za mkoa huo.

Lissu atoka mahabusu, maiti wote wazikwa

WAKATI Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) na wenzake saba wakipata dhamana na kutoka rumande jana wilayani Tarime mkoani Mara, polisi ameuawa wakati akifuatilia wavamizi wa hifadhi ya taifa, wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa.

Lissu na wenzake saba juzi walilala rumande baada ya kukosa dhamana katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime, wakikabiliwa na mashitaka ya uchochezi na uvunjifu wa amani wilayani humo.

Pia Mbunge huyo na wenzake hao wanadaiwa kuchochea ndugu za watu wanne katika kesi ya uchochezi inayowakabili Tarime,waliouawa na polisi wakati wakivamia mgodi wa dhahabu wa North Mara Barrick Mei 16, wasusie miili ya marehemu.

Mbele ya Hakimu Mkazi wa Wilaya hiyo, Yusto Ruboroga, Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Hussein Kiria, alidai juzi kuwa kwa nyakati tofauti, Mei 23, washitakiwa walishawishi ndugu za marehemu kutochukua miili katika mochari ya hospitali ya wilaya kwa ajili ya mazishi.

Marehemu hao ni Chacha Ngoka wa Kewanja, Nyamongo, Emmanuel Magige wa Nyakunguru, Mwikwabe Marwa na Chawali Bhoke wote wa Mugumu Serengeti.

Washitakiwa wengine katika kesi hiyo iliyofikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Mei 24, Mwita Waitara (36), Mwita Maswi (48), Abdalah Suleman ‘Sauti’ (31), Stanslaus Nyembea (33) na Underson Chacha (35) ambao ni wakazi wa Tarime. Wengine ni Andrew Andalunyandu (63) na Irahim Juma (27) ambao ni wakazi wa Singida.

Washitakiwa hao jana walikamilisha masharti ya dhamana yakiwamo ya kuwa na wadhamini wanaofahamika, wenye mali isiyohamishika na barua za watendaji wa kata zenye picha za wadhamini. Kesi hiyo itatajwa Juni 27 mwaka huu.

Mbunge Viti Maalumu, Esther Matiko (Chadema) hakufikishwa mahakamani kama ilivyoripotiwa jana, badala yake alishikiliwa na kuhojiwa na polisi kwa muda kabla ya kujidhamini na kuruhusiwa.

Wengine walioshikiliwa na kuhojiwa Polisi ni waandishi wa habari wanne ambao ni Anthony Mayunga (Mwananchi), Mabere Makubi (Channel ten TV), Berdina Nyakeke (The Citizen) na Anna Mroso (Nipashe).

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu Tarime/Rorya, Constantine Massawe alisema jana kwamba maiti wote wanne walichukuliwa na ndugu zao mochari na kuzikwa bila ya mikusanyiko ya aina yoyote baada ya kupigwa marufuku.

Alisema tangu juzi na jana, hali mjini Tarime ilikuwa shwari na hakuna fujo za aina yoyote zilizoripotiwa, na watu wakiendelea na shughuli zao kama kawaida.

Akizungumzia madai ya Polisi kupora maiti kutoka kwa ndugu na kisha kumtelekeza porini, Massawe alisema picha iliyoonekana kwenye baadhi ya vyombo vya habari jana ni ya familia iliyochukua mwili wa ndugu yao na kuupeleka porini.

Alisema ndugu hao walikuwa wakishawishiwa na baadhi ya watu kususia kumzika maiti huyo, huku wakiwa na waandishi wa habari ambao wote walikamatwa kwa madai ya uchochezi.

Katika tukio la Sumbawanga, polisi walilazimika kufyatua risasi dhidi ya wananchi jamii ya wafugaji, waliovamia Kijiji cha Mfinga wilayani humo na kumwua polisi kwa kumchoma mkuki kichwani.

Licha ya kuuawa kwa askari huyo kuna taarifa kwamba raia ambao idadi yao haijajulikana, walijeruhiwa vibaya wengine wakihofiwa kufa kutokana na polisi kuwapiga risasi baada ya kuona mwenzao ameuawa.

Habari za uhakika zilizotufikia na kuthibitishwa na Polisi Mkoa wa Rukwa, zilisema mapigano hayo yalitokea jana, kwenye kitongoji cha Katekela na polisi aliyeuawa ni Sajini Elikana mwenye namba D 2148 na alipoteza maisha wakati akikimbizwa katika hospitali ya wilaya mjini humo.

Mauaji ya polisi huyo yalitokea muda mfupi baada ya kikao cha usuluhushi baina ya wananchi wa kitongoji hicho na wafugaji wanaodaiwa kuvamia baadhi ya maeneo hayo, karibu na Hifadhi ya Taifa ya Katavi wakitokea wilaya za Nkasi na Mpanda.

Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda, alisema mauaji yalitokea baada msako ulioendeshwa na askari wanne wakifuatana na baadhi ya maofisa wa Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga ambao walipata taarifa ya uvamizi huo wa wafugaji katika kijiji hicho.

Kwa mujibu wa Mwaruanda, baada ya askari huyo kuchomwa mkuki na kuanguka chini, katika hali ya kujihami, polisi wengine walifyatua risasi wakielekeza kwenye kundi lililorusha mkuki huo na baadhi ya wananchi walijeruhiwa lakini akaeleza kuwa hakuna taarifa za kuuawa kwa mwananchi yeyote.

“Zipo taarifa kuwa baadhi ya wafugaji walipigwa risasi na kujeruhiwa na askari wetu katika harakati za kujihami … mwenzetu askari mpelelezi wa wilaya Mrakibu Kajala kwa hiyo wapo waliokamatwa, lakini idadi yao bado haijafahamika,” alisema.

Aidha Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Isuto Mantage na Ofisa Upelelezi wa Mkoa, Peter Ngusa, wakiwa na askari zaidi ya 20 walikwenda eneo la tukio umbali wa kilometa zaidi 100 kuendesha msako maalumu ili kuwatia nguvuni watuhumiwa wa mauaji hayo.

Hata hivyo, wengi wao wanadaiwa kukimbia maeneo hayo na kutelekeza mifugo, wake na watoto wao na kujificha kusikojulikana, huku wengine wakibaki eneo la tukio na silaha za jadi tayari kwa kukabiliana na lolote litakalowakabili.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

MADAI YETU KWA MUONGOZO WA BAJETI YA MWAKA 2011/2012- 2015/16

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kupitia kikundi kazi chake cha uchambuzi wa bajeti (Budget Analysis Task Team) wakishirikiana na wanaharakati wengine kutoka ngazi ya jamii wamefanya uchambuzi wa muongozo wa mpango wa miaka mitano wa bajeti kwa mw...aka wa fedha utakaoanza Julai mwaka 2011/2012 hadi 2015/16 . uchambuzi huu umefanywa kwa mtazamo wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi, wakiongozwa na kauli mbiu ya “Haki ya Uchumi: Rasilimali Ziwanufaishe wanawake walioko Pembezoni”.

Uchambuzi huu umefanyika katika muktadha ambapo ndio kwanza nchi imetoka katika uchaguzi na bunge ni jipya pamoja na hali ya vuguvugu la kudai mabadiliko ya katiba mpya ambayo ni homa kubwa kwa serikali pamoja na wananchi. Kwa hiyo mategemeo makubwa yalikuwa kuona msimamo wa serikali katika kutetea haki ya wananchi, kwa kuelekeza rasilimali za kutosha ili kufanikisha mchakato huu wa mabadiliko ya katiba, ambao ndio mhimili kwa wapiga kura walio wengi, hasa wanawake walioko pembezoni. Tumeshangaa kuona kuwa hakuna mikakati mahususi ya kuelekeza rasilimali ktaika eneo la katiba.

Vipaumbele vilivyoainishwa katika muongozo wa bajeti kwa mpango wa miaka mitano vimeelekezwa zaidi kwenye; Kilimo, miundo mbinu, viwanda, uwekezaji katika rasilimali watu,mazingira endelevu,usimamizi wa ardhi, mipango miji na makazi,kuimarisha mahusiano kati ya sekta ya umma na binafsi na kuendeleza mafanikio katika sekta za kijamii. Je vipaumbele hivi vimetokana na mpango wa uibuaji wa fursa na vikwazo kwa maendeleo (O & OD) ambao unatoa nafasi kwa walio wengi kuibua vipaumbele vyao wenyewe? Nani anafunaika zaidi, wawekezaji wakubwa au wawekezaji wadogo.Kwa upande wa kuwekeza katika rasilimali watu, ni kwavipi kila sekta iatongeza ajira kwa watu na ni ajira za namna gani?

Muongozo wa bajeti uliopangwa kwa mwaka 2011/2012 unatarajiwa kuwa Shilingi. 11,970,356 ukilinganisha na 11,609,557 mwaka 2009/2010ambapo bajeti inazidi kuwa kubwa wakati huohuo mapato ya ndani yanazidi kushuka. Ikizingatiwa kuwa bajeti ya serikali ni tegemezi kwa kiasi kikubwa kwa wafadhili na deni la taifa linazidi kukua kutoka Shilingi 7.6 bilioni (2008/2009) hadi Sh10.5 trilioni (2009/2010) ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 38 (Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali), je ni kwavipi serikali inapanga kuongeza ukubwa wa bajeti wakati mikopo na misaada ya wafadhili haitabiriki?Tunadai serikali ipunguze utegemezi wa bajeti kutoka kwa wafadhili kwa kuboresha ukusanyai wa mapato ya ndani na kupunguza ukubwa wa serikali, yaani wizara, mawaziri na manaibu Waziri kufikia kiasi ambacho hakitaathiri sana ukubwa wa bajeti.

Muongozo wa bajeti unasisitiza uimarishaji na uendelezaji wa masuala ya uchumi mpana na siasa kwa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji, kuzuia mfumuko wa bei, kuendeleza sekta binafsi, kusimamia usawa katika bei ya mafuta kwa kuwekeza kupitia rasilimali watu. Sisi kama wanaharakati tulitarajia kuona muongozo huu wa bajeti unaweka kipaumbele katika kusimamia mgawanyo sawa wa rasilimali katika jamii, kurasimisha kazi zisizo na kipato zinazofanywa na wanawake. Pamoja na masuala mengine, suala la ‘mabadiliko ya dhana’ yaani ‘paradigm shift’ na kuipa ‘fursa’ kipaumbele zaidi kuliko ‘mahitaji ya watu’ inatupa wasiwasi sana; tunadai kwamba inatakiwa mdahalo wa kitaifa juu ya mawazo haya, maana inaweza kuwa na matokeo ya ajabu kwa maendeleo ya uchumi wa taifa na wa watu wake.Tunapinga suala la kuweka kipaumbele katika uuzaji wa bidhaa nje ya nchi kwa wawekezaji wakubwa wakatai soko la ndani la bidhaa linakufa.

Tumeshangazwa sana kuona kwamba pamoja na juhudi zote za serikali kuendeleza kilimo na kuwa na mkakati wa mapinduzi ya kijani “Kilimo Kwanza”, ukuaji wa kilimo unatarajiwa kukua na kufikia wastani wa 5.5% tu. Ukuaji huu hauendani kabisa na umuhimu wa kilimo kwa watanzania walio wengi. Halikadhalika pamoja na kilimo kuwekewa kipaumbele, mchango wa kilimo katika pato la taifa unatarajiwa kupungua kutoka asilimia 21.9 (2010) hadi 18.7 (2011) na hii itakuwa na athari kubwa kwa wakulima wadogo wengi wanaotegemea sana kilimo hasa jamii wengi wao wakiwa wanawake.

Tunasikitishwa kuwa bado hakuna mkakati wa wazi au chanzo mbadala cha nishati kama vile gesi, upepo au makaa ya mawe kwa ajili ya kutatua changamoto iliyopo ya umeme. Miaka 50 baada ya uhuru tunadai kwamba kila Mtanzanaia ana haki ya umeme akiwa kijijini au mjini. Pia tulitarajia kuona serikali inaliimarisha shirika la umeme nchini (TANESCO) kwa kulijengea uwezo ili kuondokana na tatizo la ukodishaji mitambo ya uzalishaji umeme, ambapo mara kwa mara mitambo hiyo imekua ikiligharimu taifa kutokana na kuwepo kwa udanganyifu katika manunuzi na ukodishwaji wake. Tunadai uwajibikaji kuanzia kwa Waziri hadi maafisa wengine wanaohusika na suala la nishati ya umeme nchini.

Kwa upande wa sekta ya elimu, serikali kuendelea kubajeti wastani wa shilingi 1,500 kwa kila mwanafunzi kwa siku kwa ajili ya chakula kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari haiendani na hali halisi ya mahitaji ya lishe na kupanda kwa maisha. Asilimia 40 ya “capitation grant” kwa wanafunzi hutolewa kwa ajili ya ununuzi wa vitabu lakini hali halisi iliyopo inaonyesha kwamba shule nyingi za msingi kufikia mwezi Disemba 2010 zimepokea kiasi kisichozidi jumla ya Shilingi 60, 000 hadi 300,000/= kwa ajili ya kununulia vitabu vya kiada na ziada kwa mwaka 2009/2010 (rejea report ya Mkaguzi mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2010). Hali hii tunayoiona ni kwamba shule nyingi hazina vitabu na kila mtoto anaambiwa ajinunulie vitabu. Tunahoji pesa hizi zinakwenda wapi?

Katika Sekta ya Afya muongozo haukueleza ni jinsi gani serikali itakabiliana na changamoto za uzazi salama. Tunakumbuka na kuunga mkono ahadi ya Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii kwamba kila mama mjamzito atapewa vifaa vya kujifungulia bure,tunadai utekelezaji wa ahadi hiyo ya wizara. Tulitarajia kuona muongozo unaelekeza kutengwa kwa bajeti ya Afya inayoanzia 15% kama ilivoelekezwa katika azimio la Abuja pamoja na mikakati mahususi ya kuhakikisha eneo la afya linaboreshwa. Na je pia kuna vivutio gani vitatolewa kwa manesi wakunga wanaofanya kazi katika mazingira magumu?

Kutokana na yaliyojitokeza katika muongozo wa bajeti, sisi kama wanaharakati wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi tunadai yafuatayo:

• Kutengwa kwa rasilimali zakutosha zitakazowezesha mchakato wa mabadiliko ya katiba kufanyika kwa ufanisi zaidi.
• Ushiriki zaidi wa wananchi katika kuainisha vipaumbele vyao.
• Mikakati ya kuimarisha soko la bidhaa za ndani kwa kuimarisha barabara za vijijini zitakazosaidia kuchukua mazao ya wakulima wadogo wadogo ambao wengi wao ni wanawake ili kuinua pato la ndani la taifa na kuimarisha uchumi mkuu.
• Mikakati maalum ya kuongeza ajira, maisha endelevu na kipato kwa wote, wanawake na wanaume, mijini na vijijini.

Hitimisho

Mwongozo wa bajeti ni lazima ulenge namna uchumi wa nchi utakavyojenga maisha ya watu wake kwanza na si kuangalia wageni , suala la ajira na maisha endelevu kwa wote liwekewe kipaumbele. Mahsharti yawekwe kwa wawekezaji ili kila mmoja (awe wa ndani au nje) aongeze idadi ya wafanyakazi kwa asilimia kadhaa kufuatana na sekta husika. Katika utekelezaji wa malengo ya MKUKUTA II lazima muongozo uzingatie masuala ambayo yataleta maendeleo kwa wananchi hasa wanawake walioko pembezoni na si kuangalia masuala ambayo yatawafanya wawe watumwa katika nchi yao. Suala la mahusiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) litazamwe kwa kina zaidi kuona nani anafaidika zaidi, wawekezaji au wananchi? Kwa hiyo tunadai mwongozo wa bajeti ambao utaboresha maisha ya jamii maskini hasa wanawake walioko pembezoni.

Friday, May 20, 2011

Chadema yaratibu mazishi ya waliouawa Tarime

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeamua kusimamia na kuratibu mazishi ya watu waliouawa na polisi wakidaiwa kuvamia mgodi wa dhahabu wa North Mara hivi karibuni.

Hatua hiyo inatokana na kile chama hicho kupitia kwa Mbunge wake wa Arusha Mjini, Godbless Lema inachokiita kulinda haki ya ndugu wa marehemu hao.

Lema, alilieleza gazeti hili jana, kuwa yupo Tarime kusimamia na kuhakikisha haki inatendeka, baada ya vifo vya watu watano waliouawa kwa madai ya kuvamia mgodi huo.

Pia Mbunge huyo alisema, chama chake kinaunga mkono mgomo wa familia za watu hao watano wa kutochukua maiti kwa ajili ya maziko, hadi uchunguzi wa kitaalamu utakapofanyika kubaini sababu za vifo vya watu hao.

Akizungumza kwa njia ya simu Lema alisema, tayari wanasheria wa chama hicho; Mshauri wa Mambo ya Sheria, Mabere Marando na Tundu Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, walikuwa njiani kwenda Tarime kutoa msaada wa kisheria kwa familia hizo.

“Najua watu watasema kuwa hii ni siasa, naweka wazi kuwa mimi Lema niko hapa kama Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi kama alivyo Kagasheki (Hamis -Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi), tunachotaka hapa ni kuhakikisha haki inatendeka kwa watu hawa,” alisema Lema.

Alidai akiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime, alishuhudia polisi akiwamo Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime na Rorya, Constantine Massawe na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi nchini, Paul Chagonja, wakizipa fedha familia za marehemu kwa ajili ya majeneza, chakula na usafiri wa maziko.

“Sasa mimi nashangaa hawa wameuawa na polisi kwa madai kuwa ni majambazi, tangu lini polisi wakahusika na mazishi ya majambazi? Familia zimekataa fedha hizo na sisi tunaunga mkono na tunasisitiza hatoki maiti wala kuzikwa hadi wachunguzwe,” alisema.

Alisema, msimamo uliopo sasa ni mgomo wa mazishi ya watu hao kutoka kwa familia zao, hadi watakapofika madaktari wa kuchunguza miili hiyo, ambayo kwa mujibu wa Lema inaaminika kuwa watu hao waliuawa.

“Hapo ndipo sasa Chadema itatoa msaada wa kisheria kwa wanafamilia hao kupitia kwa Lissu na Marando, watakapojua ni hatua zipi za kisheria za kuchukua kwa kuwa miili hiyo inaonekana kupigwa risasi kichwani na kifuani na hizo ni dalili za mauaji,” alidai.

Hata hivyo, Kamanda Massawe, alikanusha kutoa fedha kwa familia hizo zilizofiwa na ndugu zao.

“Kilichofanyika ni kuhoji wafiwa kwa yeyote anayehitaji msaada wa ama chakula, usafiri na fedha, kwa ajili ya mazishi na tunachojua sisi hawajakataa ila hakuna familia iliyojitokeza.”

Kagasheki juzi alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari akijibu hoja ya Polisi kusaidia mazishi kwa watu hao wanaodaiwa kuuawa wakati wakijaribu kuvamia mgodi huo wa North Mara kuwa, msaada huo unatokana na ukweli kuwa waliokufa ni Watanzania na binadamu kama walivyo binadamu wengine.

Watu zaidi ya 800 wenye silaha walivamia mgodi huo hivi karibuni wakiwa na silaha mbalimbali kwa malengo ya kupora mawe yenye dhahabu na kukabiliana na polisi ambao walitumia mabomu ya kutoa machozi na risasi za mpira kuwatawanya wakashindwa na kisha kutumia risasi za moto na kuua watano.

Juzi Mbunge wa Tarime, Nyambari Nyangwine, akifuatana na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, Amos Sagara, walishambuliwa kwa mawe na wananchi wa Nyamongo, wakati viongozi hao wakienda kuwafariji kutokana na msiba huo.

Thursday, May 19, 2011

Ufisadi Maliasili

-Wanyamapori watoroshewa nje
-Wapelekwa Doha usiku wa manane
-Mlango wa dharura KIA watumika kuwapitisha


NOVEMBA 26, 2010, saa saba usiku, wakati idadi kubwa ya Watanzania wakiwa usingizini, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kulikuwa na pilikapilika kubwa ya kupakia mizigo kwenye ndege ya jeshi la anga la Qatar (Qatar Emir Air Force).

Mizigo iliyokuwa inapakiwa usiku huo mkubwa katika ndege hiyo haikuwa ya kawaida. Wahudumu walikuwa wanapakia wanyamapori hai 130 wa aina 14 tofauti na shehena kubwa ya nyamapori iliyokaushwa, mizigo hiyo yote ni inayotambuliwa kuwa kati ya rasilimali muhimu za Taifa.

Kwa mujibu wa wafanyakazi wa uwanja huo na raia wema kadhaa, wanyama hao hai 130 pamoja na shehena ya nyama zilizokaushwa vilikuwa vinatoroshwa kwenda Doha, Qatar.

Kwa mujibu wa sheria za Tanzania, mizigo hiyo ilikuwa inaondoka nchini kinyume cha sheria kwa kuwa haikuwa na kibali wala nyaraka sahihi za kiserikali na walioshiriki katika kuratibu na hatimaye kusafirisha mizigo hiyo nao walifanya makosa ya kuhujumu Taifa.

Kati ya wanyamapori hai 130 wakiwa wa aina 14 tofauti, walikuwamo twiga wanne. Twiga hutambuliwa kama alama ya Taifa, sheria za Tanzania zinaharamisha mnyama huyo mpole kuuawa au kusafirishwa kibiashara nje ya nchi.

Shehena ya viroba vya nyamapori zilizokaushwa inaelezwa kuwa ni ya wanyama wengi waliouawa “kijangili” na mtandao wa watu wanaoendesha biashara haramu ya nyamapori.

Ndege hiyo ya Jeshi la Qatar iliwasili KIA Novemba 24, mwanzo ikionekana kama ndege iliyokuwa katika safari za kawaida hadi Novemba 26 usiku wafanyakazi uwanjani hapo waliposhuhudia ikipakia mizigo wakiwamo wanyama hai.

Taarifa zaidi zinaeleza kuwa baada ya kuwasili kwa ndege hiyo wafanyakazi wake na marubani walikwenda kupumzika kwa siku mbili katika hoteli ya Naura Springs ya mjini Arusha.

Vinara wa uporaji huo wa wanyama hai wanatajwa kuwa ni raia wawili wa kigeni ambao wameshirikiana na Watanzania wanne ambao walifanikisha kuwatorosha wanyama hao wenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 170.

Kati ya vinara hao mmoja ni raia wa Pakistan, Ahmed Kamran, mkazi wa Arusha na mwingine ni mwanamke, raia wa Kenya, Jane Mbogo, mfanyakazi katika kampuni ya Equity Aviation Service inayotoa huduma katika Uwanja wa KIA ambaye anaishi katika nyumba za uwanja huo.

Raia Mwema limefanikiwa kupata majina ya wahusika wengine, lakini haitayataja sasa kwa kuwa haikuweza kuwasiliana nao.

Raia Mwema imefahamishwa pia kwamba washiriki wengine wa mpango huo wa uhujumu ni Watanzania wanne, ambao taarifa zisizotia shaka zilizokusanywa na gazeti hili kwa muda zinaonyesha kuwa ndio waliofanikisha mkakati wa kuwasadia wageni hao kutorosha wanyama hai hao pamoja na shehena ya nyama zilizokaushwa.

Kati yao ni mwanamke mmoja mkazi wa Dar es Salaam ambaye anamiliki kampuni ya kukamata na kumiliki wanyamapori, mtumishi mmoja mwanamke wa idara ya ulinzi ya kampuni ya KADCO inayosimamia shughuli zote za uwanjani KIA, mtumishi wa Serikali katika Idara ya Mifugo KIA na mtumishi mmoja mstaafu wa Idara ya Ushuru wa Forodha.

Wanyama hao walitoroshwaje?

Duru na taarifa zilizokusanywa na Raia Mwema zinaonyesha kuwa kinara wa usafirishaji wa wanyamapori hao ni Kamran ambaye amekuwa akifanya kazi hiyo kwa kutumia leseni ya kuwakamata wanyamapori hai ya kampuni ya mwanamke mmoja wa Dar es Salaam.

Taarifa hizo zinasema wanyamapori waliotoroshwa walikamatwa katika mapori ya akiba na sehemu mbalimbali za mikoa ya Arusha na Kilimanjaro na kuhifadhiwa katika nyumba anayoishi Mpakistan huyo katika eneo la Baraa, Manispaa ya Arusha.

Taarifa zinaeleza kuwa Mpakistan huyo amekuwa akiwahifadhi wanyama wa aina mbalimbali kwa muda mrefu katika nyumba hiyo ambayo imejengewa ukuta mrefu unaokadiriwa kufikia futi tisa, na kwamba ndani ya nyumba hiyo kuna zizi kubwa la kuhifadhi wanyama na ndege pori.

Ni kutoka ndani ya nyumba hiyo, Novemba 26, mwaka jana, usiku wa saa tatu, malori matatu aina ya Fuso yaliyokuwa yamesheheni wanyamapori hao hai na viroba vya nyamapori zilizokaushwa, yalisafirisha shehena hiyo hadi uwanja wa ndege wa KIA kabla ya kusafirishwa kwenda Doha, Qatar.

Katika uwanja huo, magari hayo yaliyokuwa na wanyama hao yalipitia lango namba 5B ambalo kwa kawaida hutumika kama lango la dharura, hadi ndani ya uwanja ambamo kazi ya kuwapakia ilianza bila vibali kutoka mamlaka za kiserikali zinazohusika.

Kwa utaratibu, wanyama hao walipaswa kupitishwa kupitia lango namba 5A ambako kuna wakaguzi wa Idara za Ushuru wa Forodha, na idara nyingine za kiserikali ambako vibali vyote vingekaguliwa na kupigwa mihuri kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.

Wakati magari hayo yalipowasili, Jane Mbogo, kwa makusudi, hakuwa ameandaa taarifa za mzigo huo (cargo manifest) kwa kuwa kampuni yake hairuhusiwi kisheria kuhudumia ndege inayozidi tani 40, badala yake alitumia vifaa vya kuazima kutoka kampuni ya kuhudumia ndege ya Swissport kufanikisha kazi hiyo.

“Hawa Equity Aviation Serevice kisheria wanaruhusiwa kuhudumia mizigo ya ndege ndogondogo, na kwa kufahamu hilo, mtuhumiwa alifanya mipango ya kuazima vifaa vya kampuni ya Swissport ili kuwapakia wanyama hao lakini pia alikacha makusudi kuanisha aina ya mizigo iliyokuwa inasafirishwa ili kuharibu kumbukumbu,” alieleza mtoa taarifa wetu.

Aidha, taarifa zinaeleza zaidi kuwa yule mtumishi wa Serikali wa Idara ya Mifugo naye akifahamu fika kuwa wanyamapori hao hawakuwa na vibali na walikuwa wanatoroshwa nje ya nchi, hakukagua vibali vinavyotakiwa katika usafirishaji.

“Kwa kawaida mizigo inayosafirishwa kwenda nje ya nchi, hasa wanyama hai, lazima wawe na nyaraka zote sahihi za kiserikali na nyaraka hizo hukaguliwa na mamlaka zote zinazohusika na usalama na mambo mengine muhimu katika uwanja lakini wakati wanyama hao wakipakiwa mambo hayo muhimu hayakuzingatiwa,” alieleza mtoa taarifa wetu aliyeshuhudia tukio hilo.

Taarifa zinasema kuwa wakati watu hao wakifanikisha mpango huo, askari mmoja aliwasili uwanjani hapo na kuhoji akitaka kuona vibali vya kusafirisha wanyama hao, lakini wahusika walimweleza kuwa “mzigo unaosafirishwa ulikuwa wa kiserikali”.

Mtoa taarifa wetu anaeleza zaidi kuwa juhudi za askari huyo kutimiza wajibu wake ziligonga ukuta baada ya kujibiwa kwa ukali na afisa wa mifugo, ambaye ni afisa mwenzake serikalini, aliyekuwa akisimamia zoezi hilo kuwa “asiingilie kazi zisizomhusu”; huku pia akimtukana matusi ya nguoni.

Akimkariri afisa huyo mtoa habari wetu alieleza: “Wewe mpumbavu? Una akili? Unaingilia kazi zisizo zako na hivi nakuambia kuwa nitakufukuzisha kazi. Huu ni ugeni wa Serikali usipende kuhoji kitu kisichokuhusu na kama hunielewi mfuate huyo Mhindi (Kamran) hapo akupatie vibali.”

Taarifa zinasema askari polisi huyo alipomwuliza mtuhumiwa huyo kuhusu vibali vya kusafirisha wanyama alidai kuwa asingeweza kudurufu (kutoa kopi) vibali hivyo kwa kuwa ni usiku wa manane na kuahidi kuwa angempatia asubuhi yake, lakini hata hivyo vibali hivyo havikuwahi kuwasilishwa hadi leo.

kwa mujibu wa taarifa hizo, askari huyo alikwenda kutoa taarifa kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi cha KIA, lakini kwa muda huo tayari ndege hiyo ilikuwa imekwishakuondoka na hakukuwa na hatua zilizoweza kuchukuliwa kuzuia mpango huo.

Habari zaidi zinasema ya kuwa baada ya kukamilika kwa kazi ya kuwapakia wanyamapori hao, wahusika waliwapatia wafanyakazi walioshiriki kupakia mzigo kiasi cha shilingi 150,000 za Kitanzania ili wagawane, mgawo huo ukifanyakia uwanjani hapohapo.

Taarfa za karibuni zaidi kuhusu suala hilo zinasema tayari Polisi walikuwa wamefungua jalada la upelelezi wa shauri hilo na kupendekeza watuhumiwa wote waliotajwa wafikishwe mahakamani, lakini katika mazingira yanayotia shaka hadi sasa suala hilo limekaliwa. Miezi mitano baada ya tukio hilo, hakuna hatua zilizochukuliwa.

Kauli za watuhumiwa

Rai Mwema wiki hii ilizungumza na Kamran kwa njia ya simu ikimtaka kuzungumzia suala hilo, lakini alikana kuhusika na akaongeza kuwa hafanyi biashara hiyo.

“Sihusiki na jambo unaloniuliza. Nafikiri umepiga namba isiyo sahihi (wrong number). Si mimi,”alisema na kisha kukata simu yake.

Kwa upande wake, Jane Mbogo alidai kuwa yeye ni mtumishi wa kampuni ya Equity Aviation Services; hivyo masuala yote hayo aulizwe Mkurugenzi wake na akatoa namba ya simu ambayo hata hivyo, ilipopigwa ilionyesha ya kuwa haitumiki.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Swissport, Gaudance Temu, alithibitisha vifaa vya kampuni yake kutumika kupakia mzigo huo na kuongeza kuwa walifanya hivyo baada ya kukodishwa na kampuni ya Equity Aviation Service na walilipwa fedha kiasi cha dola 3,000 za Kimarekani kwa kazi hiyo.

Alisema Temu kuhusu suala hilo: “ Ndiyo, nakumbuka Polisi walikuja kuhoji kuhusu ushiriki wetu katika madai ya kutoroshwa kwa wanyama hao. Lakini tumewaeleza kuwa hatuhusiki, ila vifaa vyetu vilikodishwa na wenzetu wa Equity na walitulipa kwa kazi hiyo. Nafikiri ukienda ofisi yetu ya KIA pale kuna risiti ya malipo hayo kuthibitisha”.

Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya KADCO ambayo ndiyo inayoendesha Menejimenti ya KIA, Marcus Van De Kreeke, alithibitisha madai ya kutoroshwa kwa wanyamapori hao na kuongeza kuwa hata hivyo menejimenti haihusiki na suala hilo.

“Kazi yetu kama KADCO ni kulinda usalama wa abiria na ndege zinazotumia uwanja huu kwa safari zao, lakini sisi hatuhusiki na usafirishaji wa mizigo inayopita katika uwanja. Hiyo ni kazi ya mamlaka nyingine,” alisema Van De Kreeke.

Aliongeza: “Polisi tayari wameanzisha uchunguzi. Nafikiri tuwaache wafanye kazi yao na tuone uchunguzi wao utaleta majibu gani. Ila kwa upande wetu hatuna tatizo. Tutawapa ushirikiano wa kutosha.”

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Lukas Ng’omboko naye alithibitishia Raia Mwema kuwapo kwa tukio hilo, na kufafanua kuwa upelelezi wa kesi hiyo ulikuwa unaendeshwa na maafisa wa timu maalumu ya Polisi kutoka Makao Makuu ya jeshi hilo.

“Tukio hilo ni la kweli lakini tafadhali wasiliana na Makao Makuu ya Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam. Wao ndio waliounda timu maalumu ya askari wa upelelezi na kwa ufahamu wangu walikuwa wameanza kazi ya kuwahoji watuhumiwa,”alisema Kamanda huyo.

Raia Mwema haikufanikiwa kumpata Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) Robert Manumba kuelezea hatua walizofikia katika upelelezi wa tukio hilo.

Utorashaji wa raslimali za nchi katika sekta za madini na maliasili umekuwa moja ya matatizo sugu ambayo Tanzania inakabiliana nayo na sababu kubwa inaelezwa kuwa ni kushamiri kwa vitendo vya kifisadi miongoni mwa maafisa wa serikali waliopewa mamlaka ya kusimamia rasilimali hizo kwa niaba ya wananchi.

Chanzo: Raiamwema

Mbunge apigwa mawe, Chadema yadaiwa kuhusika

MSAFARA wa Mbunge wa Tarime mkoani Mara, Nyambari Nyangwine na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Tarime, Amos Sagara, umeshambuliwa kwa mawe na wananchi wa Nyamongo na baadhi ya walinzi wa viongozi hao kujeruhiwa.

Wakati hali ikiwa hivyo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Balozi Hamis Kagasheki, amesema fujo hizo zilizotokana na mauaji ya wananchi wanne waliovamia mgodi hivi karibuni, zinachochewa kisiasa.

Akisimulia vurugu hizo, Nyangwine alisema yeye na Sagara, walikwenda kuwafariji wananchi wa Nyamongo ambao ndugu zao waliuawa na Polisi wakidaiwa kutaka kuvamia mgodi wa North Mara mwanzoni mwa wiki hii.

Kwa mujibu wa Nyangwine, walipanga kufanya mkutano na wananchi katika eneo la kituo cha mabasi cha Kewanja, Nyamongo.

"Tulifika na kukaa, lakini kabla hatujaanza kuhutubia, lilijitokeza kundi la vijana zaidi ya 100 na kudai kuwa wanachama tilioongozana nao wakiwa na sare za CCM wavue sare hizo na kuondoka maeneo hayo nikiwamo mimi na Mwenyekiti wa Halmashauri.

“Walitushambulia kwa mawe na walinzi wangu sita wakiongozwa na Godfrey Francis na Sutwa, walipambana nao nikafanikiwa kuingia ndani ya gari na kuondoka huku wakiturushia mawe na kujeruhi baadhi ya walinzi hao na kuharibu magari yetu," alisema Nyangwine.

Magari yaliyoharibiwa kwa kuvunjwa vioo katika vurugu hizo ni pamoja na gari la Idara ya Elimu aina ya Toyota Land Cruiser namba STK 8411, Toyota RAV4 namba T 299 ASW na Toyota Prado, namba T 239 DNW.

Nyangwine alisema, walishambuliwa saa tano asubuhi Kewanja na kuwataka wananchi wa Nyamongo wasikubali kutumiwa na baadhi ya wanasiasa wa vyama vya upinzani kuvamia mgodi huo na kushambulia viongozi wa umma kwa mawe.

“Suluhu inapatikana kwa kukaa pamoja wala si kurushiana mawe, tumekuja kwa nia njema kukufarijini, lakini baadhi ya wanasiasa wamegeuza maafa haya mtaji wa kupandikiza, jambo ambalo ni hatari kwa jamii ya Tanzania, nakemea na kulaani kitendo hiki," alisema Nyangwine

Alisema, katika mkutano huo, alitaka kuzungumzia mauaji ya mara kwa mara ya wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi huo na sababu za kuvamiwa mgodi huo na baada ya hapo, walikuwa waungane kwenda kumpokea Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.

Moja ya sababu za kuvamia mgodi huo kwa mujibu wa madai ya Nyangwine, ni malalamiko ya wananchi wa maeneo hayo kutolipwa fidia za mali zao na maeneo yao yaliyochukuliwa na mgodi wakikosa eneo la wachimbaji wadogo.

Malalamiko mengine ni vijana kukosa ajira na vifaa vya kisasa kwa wachimbaji wadogo, hali inayochangia ugumu wa maisha katika maeneo yanayozunguka mgodi huo.

Alisema, Serikali itaunda Tume huru itakayoshirikisha Wananchi, viongozi wa vijiji, wa Serikali, wazee wa kimila na wamiliki wa mgodi huo.

Wakati Polisi wilayani hapa, ikisaka watuhumiwa wa uhalifu huo, umati mkubwa wa zaidi ya watu 200 walikusanyika nje ya mochari ya hospitali ya Wilaya ya Tarime, wengi wao wakiwa ni wafuasi wa Chadema, wakizuia miili ya waliouawa kuchukuliwa na ndugu zao tangu mwanzoni mwa wiki.

Katika vurugu hizo za kutupiana mawe, Mwandishi wa ITV, George Marato, aliporwa kamera yake.

Kwa mujibu wa Lucy Lyatuu, Balozi Kagasheki akifafanua kuhusu tukio hilo, alisema mapambano hayo kati ya Polisi na raia yameanza kuchukua sura ya kisiasa, baada ya chama cha kisiasa kuanza uchochezi kikishawishi wanafamilia kutozika miili hiyo.

Serikali pia imepinga kufanyika kwa maandamano yaliyoandaliwa na chama hicho, bila kukitaja jina kutokana na ishara kuwa ni ya shari na yasiyo salama.

Balozi Kagasheki alisema hayo jana Dar es Salaam na kuongeza kuwa Serikali itagharimia mazishi ya wananchi waliokufa.

Kuhusu uchochezi wa kisiasa, alisema kuna shinikizo la kisiasa ambapo chama hicho kinataka kufanya maandamano katika eneo hilo na mkutano wa hadhara.

Alisema, chama hicho kimetuma ombi la kibali cha kufanya hivyo, lakini Serikali imekataa kutokana na ishara hizo na kauli za viongozi wa chama hicho, kuwaambia wananchi waliofiwa wazike baada ya maandamano na mkutano wa hadhara.

“Masuala ya siasa hadi kwenye maiti … kibali cha maandamano hakitokuwapo, tumieni muda huo kutatua matatizo mengine ya wananchi, ambayo yatasaidia kuleta maendeleo,” alisema Balozi.

Akizungumzia mgodi huo, alisema yamekuwepo matukio mbalimbali katika eneo hilo na Mei 7 mwaka huu wananchi walianzisha ghasia na kuvamia mgodi na kupora.

Mbali na siku hiyo, Kagasheki alisema Mei 14 wananchi pia walirudi katika eneo hilo na kuvamia na kupora ingawa walipambana na Polisi.

Kutokana na tukio hilo, Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema ametuma timu ya maofisa wake kuchunguza na kuzungumza na familia hizo, ili ziache siasa na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, atalitolea tamko suala la wachimbaji wadogo.

Kuhusu sababu za Serikali kuzika watuhumuwa wa uhalifu, Kagasheki alisisitiza kuwa pamoja na kwamba ni wahalifu waliovunja sheria, bado ni Watanzania.

Wakati huo huo, Namsembaeli Mduma, anaripoti kwamba kampuni ya African Barrick Gold (ABG) inayomiliki mgodi huo, imesema itatoa elimu zaidi kwa jamii inayouzunguka kuhusu umuhimu wa machimbo hayo kwa maendeleo yao na ya nchi.

Kampuni hiyo imesema hiyo ndiyo njia salama ya kushawishi kuacha uvamizi, wizi na uharibifu dhidi ya migodi nchini.

Msemaji wa Kampuni hiyo, Teweli Teweli, aliliambia gazeti hili Dar es Salaam, kuwa licha ya uvamizi wanaofanyiwa na wananchi hao kila mara, hawataki kuendelea kuona vifo vikitokea au damu ikimwagika.

Akieleza sababu za kuvamiwa huko kila wakati, Teweli alisema ni kutokana na wananchi kufahamu siri ya ulinzi uliopo katika mgodi huo ambayo kwa asilimia 100 hawauogopi.

“Kampuni yetu ilikula kiapo cha kulinda haki za binadamu kwa mujibu wa matakwa ya Umoja wa Mataifa (UN), hivyo hairuhusu walinzi wake kuwa na silaha za moto au kutumia nguvu inayoweza kuhatarisha maisha ya mtu.

“Suala hilo limefahamika kwa kila mwanakijiji katika eneo la mgodi, na hivyo kuwafanya wasihofie kufanya uvamizi wakati wowote,” Teweli alisema.

Serikali yatoa tamko kashfa ya rada

Serikali ya Tanzania imepinga vikali uamuzi wa kampuni ya silaha ya Uingereza –BAE Systems wa kulipa fidia ya Paundi milioni 29.5 za Uingereza kwa Tanzania kupitia asasi isiyo ya kiserikali badala ya kulipa fedha hizo moja kwa moja serikalini kufuatia kukamilika kwa kesi ya rushwa ya ununuzi wa Rada.
Mwanzoni mwa miaka ya 2000, Kampuni ya BAE System iliiuzia Tanzanai Rada kwa gharama ya Paundi milioni 41 za Ungereza wakati gharama halisi ilikuwa Paundi milioni 12.
Akitangaza msimamo wa serikali leo jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Bernard Membe amesema, uamuzi huu unaenda kinyume na msimamo wa serikali yetu uliotaka fidia hiyo irejeshwe serikalini.“Fedha hizo ziliibwa kutoka serikalini na hazina budi kurejeshwa serikalini,” amesema.

Tamko la Serikali limekuja miezi sita baada ya uamuzi uliotolewa na Jaji Bean wa mahakama ya Southwark ya Uingereza Desemba 21,2010 kutoa uamuzi kuwa BAE kulipa Paundi milioni 29.5 kwa wananchi wa Tanzania.

Jaji Bean alitoa uamuzi huo baada ya kutorishika na na maelezo ya makubaliano ya Ofisi ya Makosa makubwa ya jinai ya Uingereza SFO na BAE.
Kwa mujibu wa Waziri Membe, kampuni ya BAE system badala ya kulipa fedha hizo moja kwa moja kwa wananchi wa Tanzania, imeamua kuunda jopo litakalojumuisha watu kutoka ndani mwake kuishauri jinsi itakavyotumia fedha hizo kupitia kwa asasi isiyo ya kiserikali ya uingereza na sio kwa serikali ya Tanzania.

“Msemaji wa BAE amenukuliwa na Ubalozi wa tanzania nchini Uingereza akisema kampuni yake inaongozwa na sera ya kutoa misaada ya kihisani kwa asasi zisizo za kiserikali tu. Kwa msingi wa sera hiyo, kampuni hiyo haitaweza kulipa fidia hiyo moja kwa moja kwa serikali ya Tanzania,” amesema.

Waziri Membe amesema kuwa uamuzi hu wa BAE unalengo la makusudi kuonyesha sura ya kutokuamini mpango wa pamoja wa Serikali za Tanzania na Uingereza ulioelezea jinsi fedha hizo zitakavyotumika.

“Serikali ya Tanzania ilikusudia kutumia fedha hizo kununua jumla ya vitabu milioni 4.4 kwa ajili ya shule za msingi, vitabu vya miongozo ya mitaala 192,000 kwa ajili ya masomo 12 katiak shule 16,000, kununua madawati 200,000 kwenye shule zilizo na upungufu wa madawati na kujenga nyumba 1,196 za walimu katika wilaya zote nchini, kujenga vyoo 2,900’ amesema.

“BAE wanajaribu kujikosha mbele ya asasi mbalimbali zisizo za kiserikali za Uingereza baada ya kukosolewa sana kwa kashfa ya rushwa na kutoka sasa kuonekana kwamba inawajali zaidi Watanzania kukliko serikali yetu,” ameseam.
Waziri Membe ameeleza kuwa kampuni hiyo silaha ikikaidi kutoa fedha hizo moja kwa moja kwa serikali ya Tanzania, hakuna asasi isiyo ya Kiserikali ya Uingereza itakayopewa fedah hizo na kuruhusiwa kuja nchini.

Imeandikwa na Joseph Ishengoma
MAELEZO, DAR ES SALAAM

Tuesday, May 17, 2011

Vyama vya siasa vyaonywa, atayekaidi kufungwa

OFISI ya Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini imevionya vyama hivyo kuacha kupenyeza siasa kwenye taasisi za umma zikiwamo shule, vyuo na sehemu za kazi kwa kuwa ni kosa kisheria.

Aidha, imeiandikia barua Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kuifahamisha kuhusu tatizo hilo na kuiomba ichukue hatua za dhati kwa kuwakumbusha wakuu wa vyuo na wahadhiri nchini, juu ya sheria inayozuia siasa kuendeshwa vyuoni na shuleni, ili waitekeleze pia.

Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake Dar es Salaam jana, Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Ibrahim Mkwawa, alisema, hatua hiyo ilitokana na kuzuka kwa tabia ya baadhi ya vyama vya siasa kuendesha siasa katika taasisi hizo na hivyo kukiuka sheria ya vyama vya siasa inayokataza jambo hilo katika maeneo hayo.

Kwa mujibu wa Naibu Msajili huyo aliyekuwa akijibu swali kuhusu kujipenyeza kwa vyama vya siasa katika taasisi za umma hasa shuleni na vyuo vya elimu ya juu na hatua zilizochukuliwa na ofisi yake kulizuia, alisema waliamua kuviandikia barua ya onyo vyama 18 vyenye usajili wa kudumu.

Kwa maelezo yake, barua hiyo ya Aprili 16 iliyojibiwa na baadhi ya vyama, licha ya kutotakiwa kufanya hivyo kwa kuwa ilikuwa ni onyo na taarifa ya kuwakumbusha wajibu wao, ililenga pia kuvikumbusha vyama vingine juu ya umuhimu wa kutoendesha siasa katika taasisi hizo ili visiige mambo hayo baadaye.

“Siasa vyuoni ni tatizo kubwa tuliloliona na kujiridhisha, kuwa linasababishwa na vyama vyetu vya siasa vinavyokiuka sheria na hivyo kupandikiza nyanja hiyo katika taasisi hizo za umma kwa kutumia vijana shuleni, mahali pa kazi na katika taasisi za elimu ya juu.

“Vyama vilipaswa kusubiri vijana hao mitaani na mahali pengine nje ya vyuo au shuleni na kuwaimbisha kuhusu siasa. Kufanya mikutano ya hadhara ya kisiasa kwenye taasisi hizo na kampeni za uchaguzi katika majengo ya vyuo pia, ni kinyume cha sheria ya vyama vya siasa,” alisema.

Mkwawa alifafanua kuwa kitendo cha kupandikiza siasa za vyama katika vyuo ambavyo hata hivyo sheria ya vyuo inakataza, ni kusababisha machafuko ya amani na kuchanganya wanafunzi, kwa kuwa wengi hubadilika na kuegemea kwenye itikadi za vyama badala ya elimu waliyoifuata kwenye taasisi hizo.

“Sheria inaeleza wazi, kuwa ni kosa na ndiyo maana tumeviandikia vyama vyote kuvionya na kuvikumbusha ili matatizo hayo yakijirudia visiseme kuwa havikujua. Adhabu kwa mujibu wa sheria iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2009 ni Sh. milioni moja au kifungo cha miezi sita jela au adhabu zote mbili kwa pamoja, kwa mtu au chama kitakachoendesha siasa mahali pasiporuhusiwa, ikiwa ni pamona na vyuoni na kwenye nyumba za ibada,” Mkwawa alisema.

Alitaja sheria hiyo kuwa ni kifungu cha 12 (2) cha sheria ya vyama vya siasa iliyoongezwa uzito mwaka 2009 kwa kifungu A kinachovitamka vyama vya siasa pia badala ya mtu mmoja mmoja kama kifungu cha 2 kinavyoeleza.

Kwa pamoja, vifungu hivyo vinakataza shughuli za siasa kufanywa na mtu au vyama katika taasisi za serikali, shule, vyuo na ofisi za umma.

Kipindi cha nyuma, Profesa Idrissa Kikula wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) naye aliwaonya wanafunzi wa chuo hicho kuacha kuingiza siasa katika chuo hicho, kwa kuwa ni kosa na hivyo kuwataka washiriki wakiwa mitaani au mahali pengine nje ya chuo.

Five Day Workshops to Prepare Students for University Life

RAIDA HIGH SCHOOL P. O. BOX 35128 TELEPHONE: +255 22 2807605 EMAIL: Raida_high@yahoo.com www.raidahighschool.sc.tz
________________________________________

Five Day Workshops to Prepare Students for University Life

Venue: RAIDA High School and Learning Center
Time : 6th June – 11th June 2011
20th June – 25th June 2011
July 11th -16th 2011

RAIDA High School and Learning Center is organising a series of workshops targetting individuals who are entering University or tertiary education for the first time.
Purpose : The purpose is to support first year students to manage challenges of the transition from a very protected environment of high school to an independent life and its challenges.
Some of the topics will include:

• Setting your learning goals
• Time management
• Balancing social life and academics
• Managing peer pressure
• Stress management
• Nurturing your spritual, mental and physical health

Mode of Delivery
Each topic will be facilitated by experienced facilitators who will use animation and participatory approaches .

Program cost : 50, 000 Tshs only
For more details: call us at these numbers : 0786 122471, or 0688425652, 0754 82824723, 0784 622235

Monday, May 16, 2011

Mkurugenzi Mkuu IMF adaiwa kubaka

MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Fedha Duniani (IMF), Dominique Strauss-Kahn amefunguliwa mashitaka na Polisi wa New York nchini Marekani kwa tuhuma za kumshambulia na kutaka kumbaka mhudumu wa hoteli jijini humo.

Strauss-Kahn (62) alishushwa ndani ya ndege ya Air France kwenye Uwanja wa Ndege wa John F. Kennedy (JFK) dakika chache kabla ya ndege hiyo kuondoka kwenda Paris, Ufaransa.

Polisi wamesema, kiongozi huyo anakabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kutaka kubaka.

Wakili wake ameliambia Shirika la Habari la Uingereza (Reuters) kuwa kiongozi huyo atakana mashitaka hayo.

Bosi huyo wa IMF mwenye mke na watoto ambaye amewahi kuwa Waziri wa Fedha wa Ufaransa, alikuwa pia akitajwa kuwa mmoja wa wagombea urais nchini kwake mwenye mvuto mkubwa kupitia chama cha Socialist.

Kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza ( BBC) Paris, Strauss-Khan alikuwa akiongoza kwenye kura za maoni na alikuwa akionekana kuwa nafasi kubwa ya kumshinda Rais Nicolas Sarkozy.

Kiongozi wa chama cha Socialist nchini Ufaransa, Martine Aubry, alielezea habari za kutiwa nguvuni kwa bosi huyo wa IMF kuwa ni kama “radi” iliyomwacha katika “mshangao” mkubwa.

Strauss-Khan alitarajiwa kupanda kizimbani katika mahakama moja ya New York jana, kwa mujibu wa mtandao. Alikuwa amepanga kukutana na Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel jana, lakini mkutano huo ulifutwa.

Katika taarifa yake fupi jana kwenye tovuti yake, msemaji wa IMF, alithibitisha kutiwa nguvuni kwa bosi wao, na kueleza kuwa taasisi hiyo haitaeleza lolote kuhusu kesi hiyo.

“IMF iko imara kiutendaji na katika operesheni zake,” ilieleza IMF. Kabla ya kushushwa kwenye ndege hiyo, alikuwa safarini kwenda katika mkutano wa Mawaziri wa Fedha wa Umoja wa Nchi za Ulaya (EU) jijini Brussels, Ubelgiji unaotarajiwa kuanza .

Msemaji wa Kitengo cha Polisi cha uwanja huo wa ndege, alisema Strauss-Kahn aliweka chini ya ulinzi kutokana na ombi la polisi wa New York (NYPD) ambapo baada ya kukamatwa, alihojiwa na polisi hao na alielezwa aliwapatia ushirikiano mkubwa.

Msemaji wa NYPD, Paul Browne alisema kiongozi huyo amefunguliwa mashtaka ya kutaka kubaka, kukiuka sheria dhidi ya ubakaji katika tukio lililomhusisha mwanamke mwenye umri wa miaka 32 katika Hoteli ya Manhattan.

Alisema tuhuma dhidi ya Strauss-Kahn zilitolewa na mwanamke huyo ambaye alikuwa mfanyakazi katika hoteli hiyo.

“Tulipokea simu kutoka eneo la wahudumu wa Hoteli ya Manhattan kuwa ametendewa vibaya na mtu aliyekuwa amekodisha chumba cha kifahari ndani ya hoteli hiyo na baada ya hapo mtu huyo alikimbia,” alieleza ofisa huyo wa Polisi.

Mhudumu huyo alieleza kuwa alilazimishwa kwa kufungiwa ndani ya chumba hicho na kutaka kubakwa.

Akizungumza na Reuters, Browne alitoa maelezo zaidi ya kina juu ya tuhuma zinazomkabili Strauss-Khan.

“Aliwaeleza wapelelezi kwamba (Strauss-Khan) alitoka bafuni akiwa uchi, alikimbilia katika kibaraza cha hoteli ambako alikuwapo mwanamke huyo, alimsukumiza chumbani na kuanza kumfanyia shambulio la kumtaka kimapenzi, kulingana na mwanamke huyo.”

Baada ya kuripoti tukio hilo polisi walijaribu kumtafuta aliyekodisha chumba hicho chenye kugharimu Dola za Marekani 3,000 (takriban Sh milioni 4.5) kwa siku na kubaini kuwa ni kiongozi huyo wa IMF.

“Tulibaini kuwa wakati huo alikuwa tayari Uwanja wa Ndege wa JFK na tuliwasiliana na mamlaka za uwanja huo na ndege aliyopanda ilizuiwa na kiongozi huyo alitiwa nguvuni, wakati huyo yule mhudumu alipelekwa hospitali kwa matibabu,” alisema Brown.

Inadaiwa kuwa kiongozi huyo wa IMF aliondoka hotelini hapo kwa haraka na kusahau simu yake ya mkononi na vitu vyake vingine binafsi.

Hadi sasa IMF haijatoa tamko lolote kuhusu tukio hilo. Mwaka 2008, kiongozi huyo alikuwa akichunguzwa na shirika hilo juu ya uhusiano wake wa kimapenzi na mfanyakazi mwenzake ambapo alikutwa na hatia na kuomba msamaha kwa Bodi ya shirika hilo.

Thursday, May 12, 2011

Ufisadi IPTL sasa waibua kizaazaa

-Kigogo ahamishwa kufunika ulaji wa mabilioni
-Kauli ya Ngeleja bungeni utata mtupu
KASHFA mpya inayohusisha mafuta ya kuendeshea mitambo ya kufua umeme ya kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) imepamba moto na sasa Msimamizi rasmi wa kampuni hiyo, Teophili Rugonzibwa, amehamishwa, Raia Mwema imeelezwa.

Kuhamishwa kwa Rugonzibwa, ambaye ni mteule wa Mahakama aliyekabidhiwa jukumu la kusimamia mali na madeni ya IPTL, kunahofiwa kuwa na malengo ya kufunika tuhuma za ulaji wa mabilioni ya fedha katika tenda za mafuta na kuvuruga kesi iliyorindima kwa miaka tisa ambayo nayo inahusisha mabilioni.

Rugonzibwa, ndiye ambaye amekuwa akiendesha kesi kati ya Mechmar - kampuni ya Malyasia iliyoingia ubia na VIP ya mfanyabiashara Mtanzania, James Rugemalila kuanzisha IPTL kabla ya pande hizo mbili kutofautiana na VIP kuiomba Mahakama kuingilia kati na kisha Mahakama kumteua yeye kutoka Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) kuwa msimamizi wa IPTL.

Pamoja na kuendesha kesi hiyo, Rugonzibwa akiwa mfilisi, ndiye ambaye amekuwa akisimamia shughuli karibu zote za IPTL akiiwakilisha Serikali katika shauri la ufilisi ambalo linaendelea kusikilizwa Mahakama Kuu, sasa likiwa limeahirishwa bila kupangiwa tarehe maalumu.

Kauli ya Rugonzibwa

Wiki hii, Rugonzibwa - wakili mwandamizi wa Serikali daraja la kwanza, akizungumza katika mahojiano ya simu, aliiambia Raia Mwema kwamba ni kweli alikuwa amepewa uhamisho kutoka RITA kwenda Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi ambako alisema hajajua atapangiwa kazi gani.

“Ni kweli siku ya Ijumaa (Mei 6, 2011) Mtendaji Mkuu wa RITA , Philipo Saliboko, aliniita ofisini kwake kama saa 10 hivi jioni na kunipa barua ya uhamisho kwenda Wizara ya Ardhi. Hivi ninavyozungumza na wewe nimeambiwa nikabidhi ofisi na nyaraka zote ndani ya wiki mbili,”alisema Rugonzibwa akikataa kueleza nani atasimamia shughuli za IPTL.

Baada ya uhamisho huo IPTL sasa itaongozwa na raia wa Malaysia, mhasibu kwa taaluma na mwakilishi wa Standard Chartered Bank ya Hong Kong, Magesvaran Subramaniam, ambaye alikuja nchini kama mwajiriwa wa Mechmar mwaka 1998.

Tuhuma za rushwa

Uhamisho wa Rugonzibwa umekuja huku kukiwa na tuhuma za ufujaji mkubwa wa fedha za mafuta ya kuendesha mitambo ya IPTL kwa kipindi cha kuanzia Novemba mwaka jana hadi Februari mwaka huu, ambazo zilitajwa bungeni na Waziri William Ngeleja kuwa ni karibu shilingi bilioni 15 kila mwezi.

Taarifa zinasema kwamba mtandao wa ulaji fedha hizo ni mpana ukigusa uongozi wa juu wa RITA, wafanyakazi wageni wa IPTL na wakubwa ndani ya Wizara ya Nishati na Madini na wizara nyingine kadhaa, ambao kwa sasa hatutawataja kwa sababu za kitaaluma.

Taarifa zinasema wakubwa ndani ya Wizara ya Nishati na Madini wamekuwa wakihusika kikamilifu katika mchakato wa uagizaji mafuta ya IPTL na malipo yake kwa kampuni za Oryx na Total ambazo ndizo pekee zilizopitishwa katika tenda ya mafuta hayo.

Gazeti hili likikariri habari za uhakika kutoka vyanzo mbalimbali vya habari, liliandika wiki iliyopita, kwamba tayari vyombo vya dola vimeanza kufuatilia matumizi ya fedha hizo zinazotolewa serikalini kabla ya kuingia katika mfuko mkuu wa Hazina.

Ni utata wa matumizi ya fedha hizo ambao ulimsukuma hivi karibuni, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe, kuliomba Bunge kupitia Kamati ya Nishati na Madini, kufanya uchunguzi wa matumizi ya fedha hizo kwa kushirikiana na vyombo vya dola na ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG).

TAKUKURU kuchunguza

Kuna taarifa pia kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) nayo imekuwa ikichunguza matumizi ya fedha hizo. Raia Mwema imethibitishiwa ya kuwa maofisa wa TAKUKURU walifika RITA katikati ya wiki iliyopita, mara ya mwisho ikiwa mwanzoni mwa wiki hii, pamoja na mambo mengine, wakihoji uhamisho wa Rugonzibwa katikati ya mchakato wa uchunguzi.

Kinachogomba katika suala hilo ni wingi wa fedha zinazoelezwa kuwa zimetumika katika miezi hiyo kama alivyoeleza katika majibu ya Waziri Ngeleja bungeni, wakati wa Mkutano wa tatu, Aprili 6, 2011, kuwa Serikali ilitumia zaidi ya shilingi bilioni 46 kununua mafuta ya kuendeshea mitambo ya IPTL tangu Novemba 2010 hadi Februari 2011.

Maelezo ya Ngeleja Bungeni

Katika maelezo yake bungeni, Waziri Ngeleja alisema shilingi bilioni 46.4 au wastani wa shilingi bilioni 15.62 kwa kila mwezi zilihitajika kwa ajili ya kugharamia ununuzi wa tani 36,800 za mafuta mazito kwa kipindi cha miezi mitatu, kuanzia 15 Novemba, 2010 hadi 14 Februari, 2011 sawa na tani 400 kwa siku.

Alisema kampuni mbili za Oryx na Total ndizo pekee zinazofanya biashara ya mafuta mazito nchini (Raia Mwema imearifiwa kuwa zipo kampuni nyingine zenye uwezo wa kufanya biashara hiyo) na ndizo zilizoombwa kushiriki katika mchakato wa ununuzi wa mafuta hayo.

“Utaratibu uliotumika kupata kampuni za Oryx na Total ni kwa restricted tendering ambapo, kampuni za mafuta zilitakiwa kufikisha mafuta katika maghala ya IPTL mwezi Novemba, 2010. Katika hali ngumu kama hiyo, maamuzi ya Serikali yalihitajika kufanyika haraka ili kupunguza ukali wa mgawo wa umeme kwenye mfumo wa grid ya Taifa. Fedha za kununua mafuta ya kuendeshea mitambo ya IPTL zimetoka kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali,” alisema Ngeleja.

Lakini taarifa ambazo Raia Mwema inazo na takwimu za jinsi mafuta yalivyokuwa yakitumika IPTL na umeme uliokuwa unafuliwa katika miezi hiyo yote, zinaonyesha kuwa gharama yake ni karibu nusu ya shilingi bilioni zaidi ya 46 alizotaja bungeni Waziri Ngeleja.

Utata wa gharama za mafuta

Kwa mujibu wa takwimu hizo, kwa Novemba mafuta yaliyotumika IPTL ni meta za ujazo 3,670.09 ambazo ni sawa na lita za ujazo 3,670,090 ambazo kwa mauzo ya fedha za kigeni wakati huo yanaweza kufikia gharama ya shilingi 3,934,336,480 (Tsh. bilioni 3.9).

Takwimu zinaonyesha pia kwamba kutokana na mgao kuwa mkali sana Desemba mwaka jana, IPTL ilizalisha zaidi umeme na hivyo kutumia mafuta mengi zaidi yaliyofikia meta za ujazo 8,146.80 sawa na lita 8,146,800 zenye gharama ya shilingi 8,733,369,600 (sh. bilioni 8.7).

Matumizi ya Januari 2011 hayakuwa makubwa sana na takwimu zinaonyesha kwamba mafuta yaliyotumika IPTL yalikuwa ya meta za ujazo 2,021.43 sawa na lita 2,021,430 ambazo gharama yake iliyoko katika nyaraka ni karibu shilingi 2,166,972,960 (Sh.bilioni 2.1).

Huku mgao ukiendelea kupungua na sababu nyingine, ikiwamo ya Subramaniam kuzima mitambo katikati ya mgao ili kushinikiza apewe mkataba mpya baada ya mkataba wake wa awali kwisha (alikwishakuandika notisi ya miezi mitatu ya kuacha kazi) uzalishaji mwezi Februari ulishuka, IPTL ikiwa imetumia mafuta ya meta za ujazo 1,876.94 ambayo ni sawa na lita 1,876,940 kwa gharama ya shilingi karibu 2,012,079,680 (Sh.bilioni 2.0).

Kwa mujibu wa Waziri Ngeleja bungeni, jumla ya shilingi bilioni 46.4 zilitumika kununuliwa mafuta ya mitambo ya IPTL kwa miezi mitatu kati ya Novemba 15 2010 na Februari 2011, takwimu ambazo ziko juu mno kulinganisha na hali halisi kwani kwa miezi hiyo mitatu takwimu za matumizi ya mafuta IPTL zinaonyesha kwamba mafuta yaliyotumika ni lita 15,715,260 sawa na shilingi 16,846,758,720 (Sh.bilioni 16.8).

Taarifa zinasema hata kama Waziri Ngeleja angezungumzia IPTL kuendelea kutumia mafuta hadi Machi 2011 na Aprili 2011 bado kwa mujibu wa takwimu za kweli ambazo Raia Mwema imefanikiwa kuziona mafuta hayo yasingefikia gharama ya shilingi bilioni 46.4.

Raia Mwema imefahamishwa kwamba kwa Machi, IPTL ilitumia mafuta ya meta za ujazo 4,368.08 ambazo ni sawa na lita 4,368,000 zenye gharama ya shilingi 4,642,496,000 (Sh.bilioni 4.6).

Aidha, imefahamika kwamba kwa Aprili, mafuta yaliyotumika IPTL ni meta za ujazo 2,818.20 ambazo ni sawa na lita 2,818,200 zenye gharama ya shilingi 3,021,110,400 (Sh.bilioni 3.0).

Ukiongeza gharama hizo za Machi na Aprili katika jumla ya miezi mitatu ya mwanzo hesabu ya miezi yote inafika shilingi bilioni 24,510,365,120 ambayo dhahiri ni pungufu chini ya nusu kwa hesabu aliyotoa Waziri Ngeleja katika Bunge.

Mgawo wa fedha

Taarifa za uchunguzi zinaonyesha kuwa mpango wa ulaji ukubwa kiasi hicho, unaoweza kuingiza fedha nyingi kiasi hicho katika mifuko binafsi unaweza tu kufanikishwa na ushiriki mkubwa wa wakubwa, tena katika ngazi ya watendaji wakuu au makatibu wakuu.

“Mnajisumbua bure. Huo ni mpango wa wakubwa. Na si unaona hizo ni fedha nyingi. Ni mabilioni. Hata hizo takwimu mlizonazo watazibadili, si tayari aliyekuwa akizitunza amehamishwa,” alisema ofisa mmoja katika Wizara ya Nishati na Madini ambaye aliomba jina lake lisitajwe.

Ajira tata ya Meneja IPTL

Hali ya utata anayoizungumzia ofisa huyo wa Wizara ya Nishati na Madini inachangiwa zaidi na hatua ya Mtendaji Mkuu wa RITA, Philipo Saliboko kuongeza mkataba wa kazi wa Subramaniam, ambaye sasa ni Kaimu Meneja Mkuu wa IPTL pamoja na ukweli kwamba ni mwakilishi wa Standard Chartered Bank ya Hong Kong iliyoishitaki Serikali ya Tanzania na ambaye kibali chake cha kuishi nchini, cha daraja la B, kiliisha tangu Februari 19, 2011.

Taarifa zinasema hata mkataba wake wa kufanya kazi IPTL ulikwisha Januari 31, 2011 na kwa karibu miezi mitatu, mpaka alipopewa mkataba mpya na Saliboko alikuwa hafanyi kazi kutokana na notisi yake ya miezi mitatu ya Novemba mwaka jana ambayo ingemfikisha katika kuacha kazi Februari 2011.

Imeelezwa kwamba baada ya Saliboko kumpa mkataba, sasa RITA inamtafutia kibali cha kuishi nchini kupitia Kituo cha Uwekzaji (TIC).

Kwa kupata mkataba mpya, na baada ya mfilisi wa IPTL Rugonzibwa kutimuliwa, sasa Subramaniam ni kati ya wahasibu wanaolipwa vizuri sana nchini.

Taarifa zinaonyesha kwamba anapata dola za Marekani 10,500 (karibu sh. Milioni 15) kwa mwezi kama mshahara baada ya makato; ana gari la kisasa kabisa GX Landcruiser analowekewa mafuta kila mwezi; ana dereva wa kuhudumia familia, analipiwa gharama za simu, maji, intaneti, umeme, gesi, na watoto wake wanasomeshwa kwa gharama zaidi ya dola za Marekani 10,000 (Sh.milioni 15) katika shule za kimataifa, na amepewa nyumba ya IPTL yenye samani.

Taarifa zinasema ni fedha hizo nyingi zinazomfanya kuwa karibu sana na uongozi wa juu wa RITA, Wizara ya Nishati na Madini na benki ya Standard Chartered ambayo imekuwa ikifanya jitihada kutaka ilipwe zaidi ya dola za Marekani 117,000 katika shauri lililoko Mahakamani lililokuwa likisimamiwa na Rugonzibwa ambaye habari zinasema Mahakama ilimteua binafsi.

Pengo la Rugonzibwa RITA

Taarifa za ndani ya RITA zinasema kuondoka kwa Rugonzibwa, ambaye uhamisho wake unaelezwa kuwa wa aina yake wa kutoka katika Mamlaka kwenda Serikali Kuu, kutaiacha kesi iliyoko Mahakamani wazi kwa vile ndani ya RITA si Mtendaji Mkuu, Saliboko au wafanyakazi wengine waliobaki, mwenye uwezo wa kusimamia kesi hiyo mahakamani.

Sifa za kazi ya ufilisi kwa mujibu wa Sheria ya Kabidhi Wasii Mkuu sura ya 27 na Sheria ya Mawakili sura ya 341, zinamhitaji mfilisi kuwa si tu mwanasheria, bali awe pia wakili, sifa ambazo Saliboko na timu yake iliyobaki haina.

Wiki iliyopita Saliboko aliliambia Raia Mwema kwamba hakuwa na taarifa za uchunguzi unaofanywa na TAKUKURU ofisini kwake kuhusu ununuzi wa mafuta ya IPTL.

Alisema pamoja na RITA kusimamia IPTL, haina mamlaka na wala fedha zinazotolewa na Serikali hazipitii ofisini kwake na kwamba hata taratibu za ununuzi na maamuzi yote mazito hufanywa na Serikali kuu moja kwa moja baada ya ofisi yake kutoa taarifa za upungufu wa mafuta katika mitambo ya kuzalisha umeme.

Sakata la IPTL limekuwa la kihistoria tokea kuingia kwa kampuni hiyo nchini, ikihusishwa na ulaji rushwa wa kutisha ambao hadi sasa hakuna hatua zozote za kisheria zilizochukuliwa dhidi ya wahusika pamoja na kuwapo kiapo cha Patrick Rutabanzibwa, ambaye wakati huo alikuwa Kamishna Nishati. Rutabanzibwa sasa ni Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, anakopelekwa Rugonzibwa.

Bilioni 160 za ESCROW Account

Wakati hayo yakiendelea, bado kuna taarifa za kuwapo wanasiasa na watendaji ambao wanazinyemelea fedha ambazo zinawekwa kwenye akaunti maalumu Benki Kuu ya Tanzania (ESCROW Account) ambapo zimefikia zaidi ya Shilingi bilioni 160, fedha zinazosubiri uamuzi wa kisheria wa masharuri yanayoendelea kuhusiana na IPTL.

Hivi karibunini katika kikao cha Bunge, Zitto alisema TANESCO wanalipa capacity charge ya zaidi ya shilingi bilioni 3.6 kwa IPTL, na kuhoji zinakotoka fedha za kuilipa IPTL kutokana na kutokuwapo bajeti ya fedha hizo, swali ambalo Waziri Ngeleja alilikwepa kwa kutoa majibu ya jumla jumla.

Katika swali lake Zitto alihoji akianza kwa kusema;

“Ni dhahiri kwamba shilingi bilioni 15 kwa mwezi ni fedha nyingi sana. Wakati tunapitisha bajeti ya Serikali mwaka 2010/2011 hapakuwa na provision yoyote ya bajeti kwa ajili ya mafuta kwa mitambo hii. Waziri alithibitishie Bunge ni katika vote gani na kama ni ya Wizara yake au Wizara nyingine yoyote ambayo tunapata fedha (mabilioni) haya kwa ajili ya kulipia mafuta haya?”

“Kumekuwa na malalamiko na maombi na hoja mbalimbali za kutaka mitambo hii igeuzwe kuwa gas na imilikiwe na Serikali. Lakini mpaka sasa hakuna lolote ambalo limefanyika. Waziri haoni kwamba kuendelea mitambo hii kutumia mafuta kama hivi na bila utaratibu ambao labda mitambo hii imilikiwa na Serikali ni kuwa ni mradi wa watu wachache ambao wanafaidika na mafuta haya?”

Katika majibu yake, Waziri Ngeleja hakuwa na maelezo ya kutosha kuhusu zinakotoka fedha hizo na badala yake alisema, “nimuombe Zitto Kabwe kama anavyofahamu vizuri ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge suala hili ni la takwimu tunayo ofisi inayosimamia mambo yote ya Fedha, chini ya Wizara ya Fedha mimi na yeye tukutane baada ya kikao hiki ili tupeane taarifa kupitia Wizara ya Fedha.”

Ngeleja alisema kwa utaratibu uliopo fedha inayopaswa kulipwa kwa IPTL inalipwa kwenye akaunti maalum ESCROW kwa sababu ya kuwapo mgogoro wa kisheria mahakamani na kwamba ni lazima kuwe na utaratibu maalum hadi hapo mgogoro utakapokuwa umekwisha.

“Kwa nini hatujaweza kufanikisha azma ya Serikali ya kubadili ile mitambo kutoka kwa kutumia mafuta mazito kutumia gesi asili kilichotuchelewesha hapa ni huo mgogoro ulioko mahakamani kwa sababu ya mgogoro hatuwezi kuendelea zoezi hilo linahitaji kufanywa baada ya kupatikana hatma ya mambo ambayo yanabishaniwa mahakamani,” alisema Ngeleja.

Sekta ya nishati nchini imeendelea kugubikwa na kashfa na baada ya IPTL iliibuka kashfa nyingine katika miradi kama hiyo ikihusisha kampuni za Richmond Development LLC na Dowans Holding Limited, kashfa ambazo ziliwagharimu wanasiasa kadhaa akiwamo aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri wawili, Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi, ambao wote waliwahi kuongoza Wizara ya Nishati na Madini.

Wednesday, May 11, 2011

Wanajeshi, raia wapambana Dar es Salaam, Mwanamke mjamzito ajeruhiwa

ASKARI wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kambi ya Kunduchi, Dar es Salaam wanadaiwa kuvamia makazi ya wananchi na kuwapiga na kuwajeruhi vibaya baadhi ya watu, mmoja wa majeruhi hao ni mwanamke mjamzito.

Mwanamke huyo kwa sasa amelazwa katika hospitali ya Mwananyamala, Dar es Salaam, majeruhi mwingine amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Chanzo cha vurugu hizo hakijawekwa bayana kwa kuwa wanajeshi wanadai kuwa wananchi ndiyo walioanza kupanga mipango ya kuwavamia askari waliokuwa doria eneo hilo la machimbo ambalo wananchi wamepigwa marufuku wasiendele na uchimbaji.

Lakini wananchi wamekanusha madai ya askari hao na kudai kuwa, wanajeshi waliwavamia kwenye makazi yao baada ya kuzozana na baadhi ya wachimbaji ambao walikuwa wanachimba kokoto eneo ambalo si la jeshi.

Tukio hilo lilitokea Jumapili saa nne asubuhi Kunduchi wilayani Kinondoni mkoani Dar es Salaam.

Katika eneo hilo la machimbo ya kokoto kwa sasa baadhi ya watu wameligeuza makazi yao, lakini pia eneo hilo liko liko karibu na Kambi ya JWTZ Kunduchi.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mvutano kati ya wachimbaji na wanajeshi kuhusu uchimbaji wa kokoto unaofanywa eneo hilo.

Uchimbaji kwa kutumia baruti ulikatazwa na jeshi na kuwataka wananchi wafanye shughuli zao nje ya mita 500 kutoka kambi ya JWTZ.

Mmoja wa majeruhi, John Kadengu aliliambia gazeti hili kuwa wakati tukio hilo linatokea, alikuwa nyumbani kwake mara akavamiwa na kundi la wanajeshi na ndipo akashitukia anapigwa kirungu begani na baadaye akapigwa ngwala na kuanguka chini.

“Mimi nimeumia na hivi natoka hospitali Muhimbili wameniambia kuwa bega langu limeteguka,” alisema Kadengu aliyedai wanajeshi waliwatesa kwa kuwarusha kichura kwenye matope na pia kuwaamuru wapande kilima huku wakiruka kichura.

Alidai kuwa, wakati anaruka kichura kwa vile alishapigwa, alijisikia vibaya akawaomba wanajeshi wampumzishe; lakini wakaendelea kumtaka aruke kichura na baadaye hali yake ikawa mbaya akakimbizwa kwenye zahanati ya kijeshi kabla ya kupelekwa Muhimbili.

Diwani wa Kata ya Kunduchi, Janet Rithe alisema, yeye alipigiwa simu wakati tafrani hiyo inaanza na alipoenda eneo la tukio alishuhudia wanajeshi wakivamia makazi ya wananchi na kuwapiga virugu na mikanda hali iliyomfanya akimbilie kambini ili kutoa taarifa kwa mkuu wa kambi.

“Nilishuhudia kwa macho yangu wakiingia kwenye nyumba moja iliyoko eneo hilo la machimbo wakampiga mwanamke mjamzito ambaye baadaye tulimkimbiza Hospitali ya Mwanyamala; lakini bahati mbaya ile mimba imetoka,” alisema Janet.

Alidai alipofika kambini alipokewa kwa lugha za kejeli kutoka kwa wanajeshi waliokuwa getini. “Waliniambia usilete siasa hapa au wewe ndio unaowatuma watu wako waje kutufanyia fujo,” alidai diwani huyo.

Alisema, alikuta watu 32 wanashikiliwa na baada ya kuruhusiwa kuonana na mkuu wa kambi, aliwasihi wawaachie wananchi waliokuwa wanashikiliwa ili zifanywe taratibu za kuwashitaki kiraia.

Alisema baada ya kuwaachia na kupelekwa ofisi ya kata ndipo walipowakimbiza watu wanne ambao walijeruhiwa vibaya hospitalini ambako wawili wameruhusiwa kutoka; lakini wengine wawili akiwemo mama huyo mjamzito bado wamelazwa.

Ofisa Habari wa JWTZ, Meja Joseph Masanja alikanusha wanajeshi kuwapiga raia na akasisitiza kuwa, walioumia ni waliojaribu kukimbia kwa hofu baada ya kuwaona wanajeshi wakienda eneo hilo.

Akielezea tukio hilo kwa kina, Masanja alisema, wananchi waliokutwa katika eneo hilo hawakuumizwa wala kupigwa na askari wao.

Alisema siku hiyo, wanajeshi waliokuwa doria katika eneo hilo waliwakamata baadhi ya watu wakiwa wanachimba kokoto. Alisema wakati wakiwahoji, walijitokeza kundi la wananchi ambao waliwaambia wanajeshi hao kuwa hawawezi kuliachia eneo hilo.

Alisema wananchi hao huku wakiwa wamebeba silaha waliwazingira askari hao wawili waliokuwa doria tayari kuwazuru wanajeshi hao.“Baada ya kuona hivyo wale wanajeshi hawakuwa na namna ya kufanya hivyo wakaomba msaada kwa wenzao waliokuwa kambini.”

Masanja alisema, kundi hilo la wanajeshi walipofika eneo hilo walitumia mbinu za kijeshi za kuwaokoa wenzao; hivyo wananchi baada ya kuliona kundi hilo walikimbia ovyo na wengine wakaumia.

Alisema, baadhi ya wananchi walikamatwa na kupelekwa kambini na wakati huo tayari viongozi wa wananchi hao akiwemo diwani walikuwa tayari wameshafika kambini hapo kwa ajili ya kufanya mazungumzo na viongozi wa kambi.

“Uongozi wa kambi ulifanya mashauriano na diwani na kuamriwa kuwa wahusika waliokamatwa wapelekwe kwenye vyombo vya sheria kupitia ofisi za serikali za mitaa,” alisema Meja Masanja.

Alisema wananchi hao walikamatwa na vifaa vya kuchimbia kokoto pamoja na malori mawili . Alisema eneo hilo ni la jeshi kwani liko ndani ya mita 500 kutoka kambi ya jeshi.

Tuesday, May 10, 2011

Kikwete awataka mawaziri wajivue magamba

RAIS Jakaya Kikwete amewataka viongozi na hasa mawaziri wasiowajibika kwa pamoja katika Baraza la Mawaziri na Bungeni, kujiondoa ili watakaobakia wajenge umoja katika kuwatumikia wananchi.

Rais Kikwete alisema , bila umoja katika Wizara au Serikali, kutakuwa na udhaifu mkubwa na viongozi watapingana tena mbele ya watumishi wa Serikali na huwa mbaya zaidi wakipingana katika vyombo vya habari.

Alikuwa akifungua semina elekezi kwa viongozi na watendaji wakuu wa Serikali mjini Dodoma jana.

"Tuepuke kauli za kuchonganisha mawaziri...wakati wote tuzingatie wizara ni moja, Serikali ni moja hivyo tuwe na kauli moja na lengo moja...si vizuri kuona Waziri na Waziri, Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, wanasemana, wanapingana.

"Si maadili mema katika Wizara wala taasisi yoyote, hata katika kampuni yako binafsi wewe na msaidizi wako mkishindana hadharani, kuna kampuni hapo?" Alihoji katika semina hiyo ya siku nne.

Kwa mujibu wa Rais Kikwete, uzoefu umeonesha kuwa hali ya kupingana kwa mawaziri na viongozi wengine huchangiwa na kuingiliana majukumu ya kazi na kutokuwepo kwa maadili ya utendaji kazi.

"Lazima ikubalike, tukishaamua katika Baraza la Mawaziri, ni uamuzi wetu sote, tunawajibika kuunga mkono na kuutetea, kama unaona huwezi kuwajibika, hapo si mahali pako, toka utatupunguzia mzigo wa kukutetea," alionya Rais Kikwete.

Aliwataka mawaziri pia kuacha utoro katika vikao vya Baraza la Mawaziri na vya Bunge na kwa pamoja waunge mkono miswada inayopelekwa bungeni kwa kuwa huo ndiyo utaratibu wa uendeshaji wa Serikali.

“Muswada wa Sheria ukiletwa na Waziri mmoja, kila Waziri anao wajibu wa kuunga mkono na kuutetea. Haitegemewi na ni kinyume cha maadili cha hali juu kwa Waziri kupinga muswada wa Waziri mwenzake. Kwa kweli, tabia hii haivumiliki na anayetenda hayo amejitenga mwenyewe na Serikali,” alisema na kuongeza:

“Jambo lingine muhimu kwa Mawaziri ni kutambua kuwa kuhudhuria vikao vya Bunge ni jambo la lazima kama ilivyo kwa vikao vya Baraza la Mawaziri. Si jambo la hiyari. Ni lazima Waziri ahudhurie vikao vya Bunge bila ya kukosa labda awe na sababu kubwa inayoelezeka na kukubalika.

“Kutembelea jimbo lako la uchaguzi ni jambo la lazima, lakini siyo sababu ya kukufanya ukose vikao vya Bunge au Baraza la Mawaziri.”

Rais Kikwete pia aliwataka mawaziri na makatibu wakuu kuwapangia kazi na kushirikisha naibu mawaziri na naibu makatibu wakuu katika shughuli za wizara ili wote wajue kinachoendelea na pasitokee atakayekosa kazi.

Aliwataka kutonuniana ikiwa atatokea mwananchi kwenda kumuona Naibu Waziri au Naibu Katibu Mkuu, badala yake wapeane habari kila mara na ikibidi hata kutengeneza sehemu ya kunywa chai pamoja na kupeana habari za utendaji kazi.

"Sio unasikia mtu kaenda kwa Naibu Waziri unasema kwa nini asije kwangu, au yuko ziarani unasema nani kamtuma huko... kumbukeni aliyekuteua kuwa Waziri au Katibu Mkuu ndiye aliyemteua Naibu," alisema.

Katika hilo, alisema Waziri Mkuu mstaafu, Cleopa Msuya na Spika mstaafu wa Bunge, Pius Msekwa watatoa mada kwao kwa kuwa wana uzoefu wa uofisa wa Serikali, ukatibu mkuu, uwaziri mkuu, uspika na umakamu wa Rais.

Pia aliwataka wajumbe wa semina hiyo ambao ni mawaziri, naibu mawaziri, makatibu wakuu na naibu makatibu wakuu kuwa mfano mwema kwa jamii inayowazunguka katika kuchapa kazi na maadili, ili watu watamani kufanikiwa kama wao na kuishi kama wao.

"Waziri na Naibu Waziri usinyooshewe vidole vya uvivu, unafika saa tano, unatoka saa saba unaenda kulala...kazi yako uzembe, wizi, kuchonga laini, kutumia ofisi kujinufaisha," alionya Rais Kikwete.

Aliwataka kuheshimiana kwa cheo na umri na kushirikiana kutimiza wajibu wao uliopo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2010-2015 huku akisisitiza zaidi maadili.

"Nafasi hizi kuna vitu utavikosa kutokana na maadili ya viongozi... hupaswi kuonekana mbabe, muonevu, mdhulumaji, mzinzi, mlevi kupindukia.

"Hizi si sifa za uwaziri, haiwezekani unaenda baa unakunywa mpaka chupa ya mwisho, wakisema tunataka kufunga, unasema hujui mimi ni Waziri," alisema Rais Kikwete.

Aliwataka viongozi hao kukubaliana na ukweli kuwa katika nafasi walizokabidhiwa, kuna vitu watavikosa na wakitaka vyote, kuna moja litawaponyoka na hasa la uongozi.

Kuhusu kuwatumia wananchi, Rais Kikwete, alisema “Lazima tukumbuke kwamba Serikali yetu imewekwa madarakani na wananchi kwa ajili yao na siyo kwa ajili ya viongozi tuliopo madarakani. Serikali ipo kwa ajili ya kuwahudumia na kutatua matatizo yanayowakabili wananchi na kuwaletea maendeleo.

“Wananchi wanapenda kuona Serikali yao ina viongozi na watumishi waadilifu, wachapakazi hodari, wanaowasikiliza, wanaojali shida zao na wepesi wa kushughulikia na kutekeleza maamuzi mbalimbali ya Serikali. Ni wajibu wetu kama viongozi wakuu na watendaji wakuu kutimiza matarajio hayo ya wananchi.”

Kuhusu mchakato wa Katiba mpya, Rais Kikwete alisema, “Tuliazimia pia kuwa tuanzishe mchakato wa kuipitia Katiba yetu. Tumeanza, lakini kuna upotoshaji mkubwa, lakini wajibu wetu sote tuliopo hapa kukabili hila na njama hizo chafu. Naamini tutafika salama. Kinachotakiwa ni mshikamano na umoja miongini mwetu.”

Mbali na Msuya na Msekwa, pia viongozi wa ulinzi na usalama, wawakilishi wa Benki ya Dunia, CAG na wataalamu wengine wa ndani na nje ya nchi watatoa mada na kujadiliwa.

Monday, May 9, 2011

Wajawazito kupatiwa vifaa vya kisasa

Mkurugenzi wa Idara ya Kinga kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Donan Mmbando, amesema serikali imeandaa mkakati mpya kwa ajili ya kuwahudumia akina mama wajawazito ili kupungaza tatizo la vifo kwa wajawazito.

Aliyasema hayo jijini Dar es Salaam, wakati alipokuwa akisoma hotuba yake katika maadhimisho ya siku ya wakunga duniani yaliyokuwa na kauli mbiu ‘Dunia inahitaji wakunga sasa kuliko wakati wowote’ ambayo yalitanguliwa na maandamano yaliyoanzia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii hadi Viwanja vya Mnazi Mmoja.

Alisema mkakati huo unalenga kuwapatia wajawazito mikoba pamoja na makasha maalum yenye vifaa vya kutoa huduma ya uzazi.

Dk. Mmbando alisema vifaa hivyo vitawasaidia akinamama wajawazito kupata huduma bora na hata kama watajifungulia majumbani itawasaidia.

Alisema mikoba hiyo itasambazwa katika vituo mbalimbali vya afya nchini na kwamba mpango huo umepangwa kutekelezwa katika bajeti ijayo ya serikali.

Alifafanua kwamba serikali imepanga kutoa bure vifaa hivyo ili kila mmoja aweze kunufaika na mpango huo katika maeneo yote nchini.

Kwa upande mwingine, Dk. Mmbando alisema pamoja na matatizo yanayowakabili wajawazito, serikali imefanikiwa kupunguza vifo ambapo utafiti wa mwaka 2005 unaonyesha kuwa kati ya wanaojifungua 100,000 wanaopoteza maisha ni 578. Aidha, alisema utafiti wa mwaka 2010 umeonyesha kuwa kati ya akinamama wanaojifungua 100,000 ni 454 wanaopoteza maisha hivyo idadi imeshaanza kupungua.

Naye Makamu Rais wa Chama cha Wakunga (Tama), Feddy Mwanga, alisisitiza kuwa pamoja na wakunga nchini kukabiliwa na changamoto mbalimbali wanatakiwa kufanya kazi kwa kufuata maadili.

Alisema endapo mkunga atakuwa hana maadili kwa mgonjwa anatakiwa kuchukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria la sivyo atakuwa akiharibu taaluma ya ukunga katika jamii.

Friday, May 6, 2011

Vigogo wabanwa ufisadi mpya IPTL

-Zitto awatuhumu kupata mabilioni
-TAKUKURU yaanza kuchunguza

KUNA taarifa ya kuwa kuna kashfa mpya ya ufisadi inayonukia kuhusu mafuta ya mitambo ya umeme ya kampuni ya Independent Power Limited (IPTL) inayoweza kuwa inawahusisha vigogo serikalini.

Kashfa hiyo ambayo tayari vyombo vya dola vimeanza kufuatilia kwa karibu, inahusisha matumizi yenye utata ya Sh bilioni 15 kila mwezi, fedha zinazotolewa serikalini kabla ya kuingia katika mfuko mkuu wa Hazina.

Tayari Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe, ameliomba Bunge kupitia Kamati ya Nishati na Madini, kufanya uchunguzi wa kashfa hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya dola na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali (CAG).

Wakati Zitto akitaka Bunge liunde kamati ya kuchunguza suala hilo, Raia Mwema limefahamishwa kwamba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imekwisha kuanza kuchunguza suala hilo kwa kina.

Imeelezwa kwamba TAKUKURU inachunguza taarifa za kwamba baadhi ya vigogo wakiwamo wanasiasa na watendaji serikalini wananufaika na mradi huo ambapo baadhi wanatajwa kupata bakshish ya fedha zinazotolewa kila mwezi na serikali kwenda IPTL.

Vyanzo vya habari ndani ya Bunge vimeliambia Raia Mwema kwamba Zitto ameandika barua hiyo Aprili 11 mwaka huu, kwenda kwa Spika akipendekeza Bunge kuunda kamati teule kuchunguza suala hilo.

Kumbukumbu za Bunge (Hansard) zinaonyesha kwamba suala hilo lilianzia Bungeni ambapo katika Mkutano wa tatu wa Bunge, Aprili 6, 2011, Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja alilithibitishia Bunge kwamba Serikali ilitumia zaidi ya Shilingi Bilioni 46 kununua mafuta ya kuendeshea mitambo ya IPTL tangu Novemba 2010 hadi Februari 2011.

Katika barua yake kwa Spika Zitto alisema;

“Waziri alikiri kwamba serikali ilitumia mfumo wa zabuni dharura na hivyo kuyapa makumpuni mawili ya
Oryx na Total Zabuni ya kuagiza Mafuta mazito kwa ajili ya kuendesha mitambo ya IPTL. Fedha hii ni wastani wa Tsh 15bn kila Mwezi.

“Kumekuwa na Manung’uniko kuhusiana na zabuni hii na hata kuletea hisia za rushwa miongoni mwa Maafisa wa Wizara ya Nishati na Madini na Kabidhi wasii Mkuu aliyeko Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) ambaye ndiye msimamizi wa IPTL kwa sasa
kufuatia amri ya Mahakama. Inawezekana kabisa kwamba kuna watumishi wa Umma ambao wanafaidika na tatizo la mgawo wa umeme kwa kuhongwa kutokana na zabuni hii ya mafuta mazito kwa ajili ya mitambo ya IPTL.”

Mtendaji Mkuu wa RITA Philip Saliboko, ameliambia Raia Mwema jana kwamba hana taarifa za kuwapo uchunguzi unaofanywa na TAKUKURU, pamoja na kuwa wakala unahusika katika mchakato wa kuisimamia IPTL.

Saliboko alisema pamoja na RITA kusimamia IPTL, hawana mamlaka na wala fedha zinazotolewa na serikali hazipitii katika kwao na kwamba hata taratibu za ununuzi na maamuzi yote mazito hufanywa na serikali kuu moja kwa moja baada ya wao kutoa taarifa za upungufu wa mafuta katika mitambo ya kuzalisha umeme.

Katika maelezo yake Zitto alisema kuna mashaka kuhusiana na utaratibu wa zabuni kama ulifuata sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004.

“Ninaleta kwako ombi kwamba Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ifanye uchunguzi maalumu kuhusu zabuni ya uagizaji mafuta ya kuendesha mitambo ya IPTL. Uchunguzi huo, pamoja na mambo mengine, uzingatie malipo yote ambayo Kampuni za Oryx na Total zinafanya kwa watu mbalimbali kuhusiana na biashara hii. Malipo yote ya Kampuni hizi ya ndani ya nchi na nje ya nchi yachunguzwe na Maafisa wa TRA na CAG wakisaidiwa na PCCB (TAKUKURU),” inaeleza sehemu ya barua ya Zitto kwa Spika wa Bunge.

Katika maelezo yake bungeni, Waziri Ngeleja alisema shilingi bilioni 46.4 au wastani wa shilingi bilioni 15.62 kwa kila mwezi zilihitajika kwa ajili ya kugharamia ununuzi wa tani 36,800 za mafuta mazito kwa kipindi cha miezi mitatu, kuanzia 15 Novemba, 2010 hadi 14 Februari, 2011 sawa na tani 400 kwa siku.

Alisema kampuni mbili za Oryx na Total ndizo pekee zinazofanya biashara ya mafuta mazito nchini na ndizo zilizoombwa kushiriki katika mchakato wa ununuzi wa mafuta hayo, kauli ambayo imepingwa na baadhin ya wadau wa mafuta wakizitaja kampuni nyinginezo zinazofanya biashara ya mafuta hayo na kampuni za madini zinazoendesha mitambo ya umeme wa mafuta.

“Utaratibu uliotumika kupata kampuni za Oryx na Total ni kwa restricted tendering ambapo, kampuni za mafuta zilitakiwa kufikisha mafuta katika maghala ya IPTL mwezi Novemba, 2010. katika hali ngumu kama hiyo, maamuzi ya Serikali yalihitajia kufanyika haraka ili kupunguza ukali wa mgawo wa umeme kwenye mfumo wa grid ya TAIFA. Fedha za kununua mafuta ya kuendeshea mitambo ya IPTL zimetoka kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali,” alisema Ngeleja.

Hata hivyo, Raia Mwema limethibitishiwa kwamba fedha hizo hutolewa katika akaunti ya makusanyo hata kabla ya kuingia katika mfuko mkuu, jambo ambalo linazidi kuibua utata kutokana na fedha hizo kutofuata taratibu za fedha za serikali na kuwapo ugumu wa kufanyiwa ukaguzi.

Katika swali la nyongeza, Zitto alihoji; “Ni dhahiri kwamba shilingi bilioni 15 kwa mwezi ni fedha nyingi sana. Wakati tunapitisha bajeti ya Serikali mwaka 2010/2011 hapakuwa na provision yoyote ya bajeti kwa ajili ya mafuta kwa mitambo hii. Waziri alithibitishie Bunge ni katika vote gani na kama ni ya Wizara yake au Wizara nyingine yoyote ambayo tunapata fedha (mabilioni) haya kwa ajili ya kulipia mafuta haya?”

Zitto alisema kila mwezi Tanesco wanalipa capacity charge ya zaidi ya shilingi bilioni 3.6 kwa IPTL, fedha ambazo zinawekwa kwenye ESCO Account ambapo zimefikia zaidi ya shilingi bilioni 160.

“Kumekuwa na malalamiko na maombi na hoja mbalimbali za kutaka mitambo hii igeuzwe kuwa gas na imilikiwe na Serikali. Lakini mpaka sasa hakuna lolote ambalo limefanyika. Waziri haoni kwamba kuendelea mitambo hii kutumia mafuta kama hivi na bila utaratibu ambao labda mitambo hii imilikiwa na Serikali ni kuwa ni mradi wa watu wachache ambao wanafaidika na mafuta haya?” alihoji Zitto.

Katika majibu yake, Waziri Ngeleja hakuwa na maelezo ya kutosha kuhusu zinakotoka fedha hizo na badala yake alisema, “nimuombe Zitto Kabwe kama anavyofahamu vizuri ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge suala hili ni la takwimu tunayo ofisi inayosimamia mambo yote ya Fedha, chini ya Wizara ya Fedha mimi na yeye tukutane baada ya kikao hiki ili tupeane taarifa kupitia Wizara ya Fedha.”

Ngeleja alisema kwa utaratibu uliopo fedha inayopaswa kulipwa kwa IPTL inalipwa kwenye akaunti maalum ESCO kwa sababu ya kuwapo mgogoro wa kisheria mahakamani na kwamba ni lazima kuwe na utaratibu maalum hadi hapo mgogoro utakapokuwa umekwisha.

“Kwa nini hatujaweza kufanikisha azma ya Serikali ya kubadili ile mitambo kutoka kwa kutumia mafuta mazito kutumia gesi asili kilichotuchelewesha hapa ni huo mgogoro ulioko mahakamani kwa sababu ya mgogoro hatuwezi kuendelea zoezi hilo linahitaji kufanywa baada ya kupatikana hatma ya mambo ambayo yanabishaniwa mahakamani,” alisema Ngeleja.

Sekta ya nishati nchini imekuwa ikigubikwa na kashfa za mara kwa mara na mradi wa IPTL ndio mkubwa wa kwanza kuhusishwa na ufisadi ambao hadi sasa hakuna maelezo wala hatua zilizowahi kuchukuliwa dhidi ya wahusika kabla ya kuibuka kashfa nyingine katika miradi kama hiyo ikihusisha kampuni za Richmond Develepoment LLC na Dowans Holding Limited.

Kikwete atakiwa mahakamani

RAIS Jakaya Kikwete ameombwa kutoa ushahidi kumtetea aliyekuwa Balozi wa Tanzania
nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na aliyekuwa Ofisa Tawala wa ubalozi huo, Grace Martin katika kesi inayowakabili ya uhujumu uchumi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Wakili wa washitakiwa hao, Mabere Marando alidai jana kuwa wamewasilisha barua kwa Katibu Mkuu Kiongozi Mei 2, mwaka huu, kuelezea nia ya kumuita Rais Kikwete kama shahidi wa upande huo wa utetezi.

Marando alidai sheria inawataka kufanya hivyo kwa kutoa taarifa kwa Katibu Mkuu Kiongozi, naye anaweza kufika mahakamani ama kuwasilisha hati ya kiapo kama iliyowasilishwa na Rais mstaafu Benjamin Mkapa.

Alidai ushahidi wa Rais Kikwete unahitajika kwa kuwa mshitakiwa anadaiwa kufanya makosa wakati ambao Rais Kikwete alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

“Tumemfahamisha Katibu Mkuu Kiongozi pia kwamba Rais kama hatoweza kufika mahakamani, kusimama kizimbani na kutoa ushahidi, basi hati yake ya kiapo itatosha,”
alisema Marando.

Marando alisema mashahidi wengine wanaotarajia kuwaita ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Fedha wa wakati huo, Basil Mramba na mashahidi wengine saba kufanya idadi ya mashahidi wao kuwa 10.

Hati ya kiapo ya Mkapa iliwasilishwa mahakamani hapo na wakili huyo juzi na kukabidhiwa mawakili wa Serikali.

Katika hati hiyo, Mkapa amedai kuwa kwa kipindi chote alichofanya kazi na Mahalu katika nyadhifa mbalimbali za kiserikali, mshitakiwa huyo alionesha tabia nzuri.

Mkapa amedai Mahalu alikuwa mnyenyekevu, mwaminifu na mfanyakazi hodari aliyezawadiwa heshima ya juu na Rais wa Italia Siku ya Taifa la nchi hiyo kipindi kirefu tangu aondoke nchini humo.

Pia Rais mstaafu alidai kuwa jengo ambalo Profesa Mahalu anatuhumiwa kununua la ofisi ya Ubalozi wa Tanzania mjini Rome, lilinunuliwa kipindi ambacho alikuwa Rais wa Tanzania na kudai manunuzi ya jengo hilo yalikuwa kwa mujibu wa sera ya Serikali.

Amedai katika hati hiyo kuwa sera hiyo ni ya kumiliki au kujenga ofisi za kudumu na makazi kwa mabalozi wa nje ya nchi na ililenga kupunguza gharama.

Profesa Mahalu anakabiliwa na kesi ya kuisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni mbili kwa kununua jengo la Ubalozi wa Tanzania nchini Italia katika Jiji la Roma.

Wednesday, May 4, 2011

Jaji ataka uhuru wa habari uwe katika Katiba

JAJI Mkuu mstaafu, Augustine Ramadhani , amelitaka Baraza la Habari Tanzania (MCT) na
wadau wote wa habari nchini kukusanya nguvu zao na wanasheria kuhakikisha Katiba mpya inatambua uhuru wa vyombo vya habari.

Amesema, Katiba ya sasa haitambui uhuru wa vyombo vya habaribadala yake inatambua uhuru wahabari wa mtu mmoja mmoja.

Akizungumza katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani Dar es Salaam jana, Jaji Ramadhani alisema, kwa sasa mchakato wa kuunda Katiba mpya unaendelea hivyo ni vyema wadau hao kuhakikisha uhuru wa vyombo vya habari unakuwemo.

“Ingawa leo wanahabari wote wanasherehekea siku hii na miaka 20 ya Maazimio ya Windhoek, suala la uhuru wa vyombo vya habari halimo katika Katiba, nawashauri hii iwe
ajenda yenu kubwa katika mjadala wa Katiba mpya,” alisema Jaji Ramadhani.

Alitolea mfano uhuru wa Mahakama kuwa hata nao haukuwemo kwenye Katiba lakini sasa ni miaka 10 tu imepita tangu uhuru huo uingizwe kwenye Katiba, “nasisitiza kuwa bado hamjachelewa anzeni mchakato wenu sasa”.

Alisema inasikitisha Serikali kuhusishwa kuingilia uhuru wa vyombo vya habari au uhuru wa kitu chochote jambo ambalo pamoja na kuwa lina ukweli, lakini sababu kubwa ya ukosefu wa uhuru huo ni wanataaluma wenyewe wakiwemo wanasheria na wanahabari.

“Naomba tukubaliane hapa hakuna Serikali yoyote duniani inayotoa maelezo ya kila kitu chake, lazima kuwapo kufichaficha lakini jambo lililowazi ni kwamba wanahabari uhuru wao wanatakiwa uwe dhidi ya waajiri wao, dhidi ya wale wanaowaandika, dhidi ya umma na
nafsi zao wenyewe,” alisema.

Alisema mwanataaluma yeyote lazima awe na nafsi inayomlinda katika kufuata maadili na kwa waandishi wa habari aliwataka kujiepusha na vitendo vya rushwa ambavyo moja kwa
moja huwanyima uhuru kuandika dhidi ya aliyewapa rushwa.

Naye Kaimu Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari vya Kusini mwa Afrika upande wa Tanzania (MISA-TAN), Bujaga Kadago, aliiomba Serikali kupitia maudhui ya Azimio
la Windhoek ili kuweka mazingira mazuri ya kazi ya uandishi wa habari.

Alisema kwa kufanya hivyo kutawezesha waandishi wa habari kufanya kazi yao bila uoga kwani kuwapo kwa mazingira magumu kwao kunajenga hali ya uoga, kutojiamini na hatimaye wananchi hupatiwa habari zisizokamilika na kunyimwa haki yao ya msingi kikatiba.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (MOAT), Reginald Mengi, aliwataka waandishi wa habari kufuata maadili ya kazi yao na kuandika habari zinazohamasisha maendeleo na demokrasia na kuacha kushabikia habari za wanasiasa zinazoweza kuleta uchochezi katika jamii.

Tuesday, May 3, 2011

Kikwete atoa ahadi nzito kwa watoto, wajawazito


RAIS Jakaya Kikwete amesema atahakikisha vifo vya watoto chini ya miaka mitano na wajawazito vinapungua mpaka asilimia sifuri ifikapo mwaka 2015.

Alielezea nia hiyo katika mkutano wa waandishi wa habari uliohusu maazimio ya Tume ya Umoja wa Mataifa ya Habari na Uwajibikaji wa Afya ya Wanawake na Watoto, iliyomaliza kikao chake cha pili na cha mwisho Dar es Salaam Jumatatu.

“Kwa Tanzania tumepiga hatua kidogo katika kupunguza vifo vya watoto na wajawazito...lakini tunataka tufikie chini ya moja, maana yake tunataka tufikie vifo sifuri,” alisema Rais Kikwete anayeongoza tume hiyo na Mwenyekiti mwenza, Waziri Mkuu wa Canada, Stephen Harper.

Akifafanua mafanikio yaliyopatikana Tanzania ambayo yamepongezwa na Tume hiyo, Rais Kikwete alisema mwaka 2000, kati ya wajawazito 100,000, wajawazito 578 walikufa wakati wakijifungua ambao kwa mwaka ilikuwa ni sawa na vifo vya wajawazito 8,000.

Lakini kufikia 2010, baada ya Serikali kufanya juhudi za makusudi kukabiliana na hali hiyo, vifo hivyo vya wajawazito vilipungua na kufikia 454 kati ya wajawazito 100,000 sawa na vifo vya wajawazito 6,800 kwa mwaka.

Kwa watoto, Rais Kikwete alisema, katika vizazi 100,000, walikufa watoto 81 mwaka 2000, lakini juhudi za Serikali zilisaidia kupunguza vifo hivyo na kufikia watoto 51 mwaka 2010.

“Mtu anaweza kufikiri kuwa ni vifo vichache kwa nchi yenye watu milioni 40, lakini ujauzito si maradhi, ni utaratibu tu wa Mungu kuendeleza vizazi hatutaki afe hata mmoja,” alisema Rais Kikwete.

Katika mkutano huo, waliazimia kuhakikisha habari za wanaozaliwa na vifo zinapatikana haraka ili hatua stahiki zichukuliwe katika eneo husika hasa katika nchi 74 zinazoendelea ambako zaidi ya asilimia 92 ya vifo hivyo duniani hutokea huko.

Pia wamekubaliana kutengeza utaratibu wa kufuatilia rasilimali fedha zilizoahidiwa na mataifa tajiri zaidi ya Doloa za Marekani bilioni 40 kwa ajili ya kupunguza vifo hivyo na kuhakiki matumizi yake katika nchi zitakakopelekwa.