Thursday, June 30, 2011

Zitto mambo magumu

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema), amegonga mwamba katika hatua yake ya kwanza ya utetezi dhidi ya madai mazito aliyoyatoa dhidi ya Baraza la Mawaziri, kwamba lilirubuniwa ili kutaka kuliua Shirika Hodhi la Mali za Mashirika ya Umma (CHC).

Spika wa Bunge la Tanzania , Anne Makinda jana alimbana Mbunge huyo, akisisitiza kuwa awe amewasilisha kwake vielelezo vya ushahidi kuhusu kauli yake hiyo ifikapo Jumatatu.

Kukwama kwa Zitto kunatokana na Spika Makinda kumgomea Mbunge huyo ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, kumwombea serikalini nyaraka alizotaka kuzitumia kutetea hoja yake hiyo, baada ya Spika kusema nyaraka hizo ni za siri.

Akitangaza bungeni mjini Dodoma, Spika Makinda alisema mara baada ya kumtaka Zitto kuwasilisha ushahidi wa kauli yake hiyo aliyoitoa bungeni Juni 23, Zitto alimwandikia barua akimwomba kumwombea serikalini nyaraka mbili ili azitumie katika ushahidi wake.

Spika alizitaja nyaraka alizoomba Zitto kuwa ni Waraka wa Wizara ya Fedha na Uchumi uliowasilishwa kwenye Kamati ya Makatibu Wakuu kuhusu CHC na Waraka uliowasilishwa kwenye Baraza la Mawaziri kuhusu CHC, akitumia kifungu cha 10 cha Kanuni ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

“Taratibu za Baraza la Mawaziri ni za siri na haziwezi kutolewa hapa bungeni. Spika hawezi kumsaidia Mbunge ili aweze kupewa nyaraka hizi za Baraza la Mawaziri kwa vile ni za siri.

“Mheshimiwa Zitto alitamka hapa ndani ya Bunge, kwamba anao ushahidi wa kauli yake hiyo na hata baada ya mimi kumwonya, Mheshimiwa Zitto aliendelea kuzungumza kwa kurudiarudia kwamba ana ushahidi wa kauli hiyo.

“Kutokana na uhakika aliodai kuwa nao, nilimwagiza awe amewasilisha kwangu uthibitisho wa kauli yake hiyo. Sasa kwa vile yeye aliomba nimpe nyaraka hizo ambazo siwezi kumpa, naomba kumwongeza siku awasilishe ushahidi kwa njia zake mwenyewe hadi ifikapo Jumatatu, Julai 4,” alisema.

Spika alitoa mfano wa suala kama hilo ambalo lilitokea bungeni Julai mosi, 2008, ambapo aliyekuwa Mbunge wa Bukoba Vijijini, Nazir Karamagi (CCM), akiwa tayari amejiuzulu nafasi yake ya Waziri wa Nishati na Madini, alisimama bungeni na kudai kuwa kitendo cha Serikali kuiongeza muda Kampuni ya Upakiaji na Uondoshaji Kontena Bandarini (TICTS) kwa miaka mingine 15, kilifanywa na Baraza la Mawaziri.

Kutokana na kauli hiyo, Spika wa Bunge la 10, Samuel Sitta alimtaka Mbunge huyo kutoa uthibititisho kwamba alijuaje Baraza la Mawaziri ndilo lililoamua kuhusu suala hilo wakati yeye hakuwa Waziri wakati huo na wakati taratibu za uendeshaji wa Baraza la Mawaziri ni za siri, hatua iliyomfanya Karamagi kuonywa na Bunge.

Akiwa mchangiaji wa kwanza wa Azimio hilo lililowasilishwa bungeni Juni 23 na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mashirika ya Umma, alisema Azimio hilo liligeuzwa kutoka vile lilivyokuwa awali baada ya mawaziri kushawishiwa.

Hoja ya msingi ya Waziri Mkulo ilikuwa ni kuliomba Bunge kupitisha Azimio hilo ili CHC iongezwe kipindi cha mpito cha miaka mitatu, ili imalize majukumu yake na baadaye majukumu yake yahamishiwe Ofisi ya Msajili wa Hazina, lakini hoja hiyo ilikumbana na upinzani mkali kutoka kwa wabunge wa CCM na upinzani na hatimaye ikafanyiwa marekebisho.

“Mheshimiwa Spika, ndani ya Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma na hata katika Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, tulikubaliana kwamba CHC wapewe muda wa kutosha kukamilisha kazi na majukumu yao, halafu baada ya hapo Waziri alete Azimio hapa na si kuwapa kipindi cha mpito cha miaka mitatu kama Azimio lilivyowasilishwa leo.

“Nawaombeni wabunge wenzangu wote, tukatae uamuzi huu wa Baraza la Mawaziri kwa kuwa yametokana na kurubuniwa na watu wenye lengo la kuiua CHC kwa ajili ya maslahi yao. Ikumbukwe kuwa chombo hiki kinaangalia mali za umma na mashirika, hivyo kutaka kukiua na kupeleka majukumu haya kwa Msajili wa Hazina ambaye uwezo wake wa kulinda mali za umma ni mdogo sana, ni kutaka kuiba mali za Watanzania,” alisema Zitto.

Alisema Azimio la Serikali la kuipa CHC kukamilisha majukumu yake lililenga kusaidia wafanyabiashara walioiba mali za umma ikiwa ni pamoja na kukopa mabilioni ya fedha kutoka iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ambao kesi zao ziko mahakamani, kupata ahueni kwa vile hatua hiyo itapoteza ushahidi.

Baada ya kueleza hayo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), George Mkuchika, aliomba Mwongozo wa Spika akitaka Zitto athibitishe kauli yake kwamba mawaziri walirubuniwa, kwa vile imewadhalilisha mawaziri hao ambao wanafanya kazi kwa maadili na kwa kuzingatia maslahi ya nchi.

Mkuchika alisema kitendo cha kusema uamuzi huo unatokana na kurubuniwa kwa mawaziri kinaleta picha mbaya kwa Watanzania ambao wamewaamini.

Baada ya maelezo ya Mkuchika, Spika alimtaka Zitto kuwa makini na kauli anazotoa anapochangia, ikiwamo ya kudai kwamba mawaziri wanashawishiwa na kurubuniwa; lakini Zitto aliposimama tena ili kuendelea kuchangia alitamka tena kuwa anao ushahidi kwamba mawaziri walikuwa wameshawishiwa na kurubuniwa hadi wakatengeneza Azimio hilo jipya.

“Mheshimiwa Spika, siwezi nikatafuna maneno hapa, nina uhakika na ninachokisema, uamuzi wa Baraza la Mawaziri ni matokeo ya ma-lobbyist (washawishi) na kama Serikali mnabisha, leteni hapa mapendekezo ya awali ambayo yaliwasilishwa katika Kamati ya Makatibu Wakuu na Baraza la Mawaziri ili tuone yalikuwa yanasemaje.”

Kutokana na msimamo huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alimwomba Spika Makinda kumtaka Zitto awasilishe bungeni ushahidi kutokana na kauli yake hiyo, hatua iliyomfanya Spika kumpa Mbunge huyo muda wa kuandaa ushahidi huo na kuuwasilisha bungeni jana.

Shughuli zinazofanywa na CHC ambazo mpaka sasa hazijakamilika ni pamoja na urekebishaji wa TRL baada ya kampuni ya Rites kuondoka, kushughulikia uuzaji wa hisa za Serikali NBC (T) Limited, uperembaji na uhakiki wa vitendo na mashirika yaliyobinafsishwa, urekebishaji wa mashirika 34 yaliyobaki na kukamilisha ufilisi wa mashirika ya umma 24 yaliyobaki.

Pia ukusanyaji wa madeni ya iliyokuwa NBC yenye thamani ya Sh. bilioni 15.8 na urekebishaji wa kampuni ya TTCL baada ya hatua ya awali ya ubinafsishaji kushindikana na mwekezaji wa Airtel kuonesha nia ya kutoka kwenye ubia.

Wednesday, June 29, 2011

Mwanamke wa kwanza kuongoza IMF

Waziri wa Fedha wa Ufaransa Christine Lagarde ameteuliwa kuwa mkurugenzi mkuu wa shirika la fedha duniani IMF. Waziri wa Fedha wa Ufaransa Christine Lagarde ameteuliwa kuwa mkurugenzi mkuu wa shirika la fedha duniani IMF.Kufuatia uteuzi huo Ufaransa itakuwa imeshikilia kiti hicho kwa miaka 26 kati ya miaka 33 iliyopita.


Christine Lagarde mwenye umri wa miaka 55, alikuwa mwanamke wa kwanza kuteuliwa waziri wa fedha katika muugano wa nchi saba zilizostawi maarufu kama G-7.

Lagade anatarajiwa kujiuzulu kutoka serikali ya Ufaransa ili kuandikisha historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwahi kuongoza shirika la fedha duniani IMF.


Uteuzi wake umefuatia kujiuzulu wa mfaransa mwenzake Dominique Strauss Kahn, baada ya kukabiliwa na kashfa ya ubakaji.
Sio wengi walioshangazwa na uteuzi wa wakili huyo wa zamani ambaye ana sifa nzuri kote duniani.

Amekuwa msuluhishi wa matatizo mengi ya kiuchumi yanayokumba mataifa kadhaa barani ulaya katika miaka ya hivi karibuni.


Kabla ya kuteuliwa kwake alikuwa ameungwa mkono na China na India na hivyo kuteuliwa kwake kama mkurugenzi mkuu wa shirika hilo la fedha duniani ilikuwa jambo lililotarajiwa.

Kuna maelewano ambayo hayajanakiliwa kuwa raia wa mataifa ya bara ulaya pekee ndio wanaopaswa kuteuliwa kuhudumu kama mkurugenzi mkuu wa IMF huku raia wa marekani wakipewa nafasi za kuongoza benki kuu ya dunia.
Mataifa yaliostawi yanataka kupewa nafasi kuu katika siasa za dunia, lakini huu ni wakati mgumu kwa mataifa ya ulaya huku mzozo wa kiuchumi wa Ugiriki ukitishia kuathiri mataifa mengine katika kanda hiyo.


Muungano wa ulaya na IMF zimeishurutisha serikali ya Ugiriki kupunguza matumizi yake ili kuendelea kupata msaada kutoka kwao.

Lagarde amekuwa katika mstari wa mbele kujaribu kutatua matatizo hayo ya nchi wanachama wa EU.BBC

Bei petroli yashushwa

WAMILIKI wa vyombo vya usafiri vya moto kuanzia keshokutwa watajisikia afueni baada ya utekelezaji wa mabadiliko ya bei ya nishati ya mafuta kuanza.

Hatua hiyo inatokana na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi kavu na Majini (Ewura) jana kutangaza kushuka kwa bei ya mafuta jamii ya petroli na dizeli.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Haruna Masebu, kuanzia siku hiyo, bei ya dizeli itapungua kwa Sh 215 kwa lita huku ya petroli ikisubiri nayo kushuka kwa kiwango ambacho hakikutangazwa jana.

Lakini wakati hali ni hiyo kwa mafuta hayo,ya taa yatapanda kwa Sh 385, ambapo Masebu aliongeza kuwa, ifikapo Agosti Mosi bei ya mafuta hayo inatarajiwa kushuka zaidi ili kutoa nafuu kwa mtumiaji.

Masebu, alisema hayo Dar es Salaam jana katika mkutano wa wadau wa mafuta na kutaka bei hizo mpya zifuatwe na kuheshimiwa.

Alisema, pia bei ya petroli itapungua na kiwango chake kutangazwa wakati wowote kuanzia sasa baada ya kukamilika ukokotoaji wa tozo zilizopunguzwa, huku akionya kuchukua hatua za kisheria kwa watakaokiuka agizo hilo la kushusha bei.

“Lengo la mkutano wa leo (jana) ni kuwaeleza wadau wa mafuta kuhusu mambo yaliyotokea Dodoma, ambayo yamesababisha sisi Ewura kama wadhibiti, kuwatangazia kuwa kutokana na punguzo la kodi katika mafuta na nyongeza katika mafuta ya taa, bei mpya ya bidhaa hizo itaanza rasmi Julai mosi,” alisema Masebu.

Alisema, kwa sasa kinachosubiriwa ni kusainiwa kwa Sheria ya Fedha yenye makubaliano hayo yaliyopitishwa na Bunge.

Kutokana na mabadiliko hayo, Masebu alisema, tofauti ya bei ya dizeli na mafuta ya taa itakuwa Sh. 15 kwa lita, kwa maana ya mafuta ya taa kuuzwa kwa bei ya chini ya dizeli kwa kiwango hicho ili kuzuia uchakachuaji.

Bei ya zamani ya bidhaa hizo mbili kwa mujibu wa Masebu, mafuta ya taa yaliuzwa kwa bei nafuu pungufu ya Sh. 400 ikilinganishwa na ya dizeli na kusababisha baadhi ya mafuta yaliyokuwa yakiuzwa nchini kuchakachuliwa.

Alisema, pia upo mchakato wa kukokotoa tozo zingine kwa ajili ya kuzipunguza, ili kuifanya bei ya mafuta hayo jamii ya petroli kuwa nafuu zaidi na Agosti mosi, punguzo kubwa linatarajiwa kuanza rasmi kutumika.

Akizungumzia mfumo wa kuweka vinasaba katika mafuta, Masebu alisema, umepitishwa rasmi kutekelezwa nchini ili kudhibiti wafanyabiashara wadanganyifu wanaosingizia kusafirisha mafuta nje ya nchi na baadaye kuyauza nchini ili kukwepa kodi.

“Tumeamua kuwataarifu kuwa mfumo huu wa ‘fuel marking’ tunaendelea nao na tangu uanze, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeongeza mapato yake kutokana na magari mengi kukamatwa, yakifanya udanganyifu na kupigwa faini,” alisema.

Pia mfumo huo umesaidia TRA kupata mapato yaliyokuwa yakivujishwa kwa kukwepa kodi.

Kuhusu mfumo wa uingizaji mafuta kwa pamoja, Masebu alisema, Serikali imekamilisha michakato yote ikiwa ni pamoja na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, kusaini kanuni za mfumo huo na kuzichapisha katika Gazeti la Serikali toleo namba GN 164 la Juni 3.

Kanuni hizo kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, zimetoa wajibu mkubwa kwa wadau wa mafuta zikiwamo taasisi na kampuni za mafuta, ambazo zimetakiwa kuunda Kamati ya Uratibu na Bodi ya Wakurugenzi, katika miezi mitatu ijayo, ili mfumo huo uanze kutekelezwa.

Alisema, vyombo hivyo viwili pamoja na Ewura kuwa msimamizi na mdhibiti, vitasimamia masuala ya zabuni.

“Mfumo huu tunatarajia utasaidia kupunguza gharama kubwa za mafuta, kwa kuwa utashindanisha kampuni za mafuta na hivyo bei itapungua, suala hili sasa si hadithi, bali ndiyo ukweli wenyewe,” alisema.

Wakati akiwasilisha Bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, alisema, katika jitihada za Serikali za kupunguzia mzigo wa gharama za maisha wananchi, imeamua kupunguza baadhi ya kodi za mafuta ili bei ya bidhaa hiyo ipungue.

Akiwasilisha muswada wa Sheria ya Fedha kwa mwaka 2011, Naibu Waziri wa Fedha, Pereira Silima, alisema Serikali imeongeza ushuru wa bidhaa kwa mafuta ya taa kutoka Sh. 52 hadi Sh 400.30 pamoja na mambo mengine, lengo ni kudhibiti uchakachuaji wa mafuta nchini.

Upunguzaji huo wa bei za mafuta, pia una lengo la kudhibiti mfumuko wa bei, ambao umekuwa ukisababishwa na bidhaa hizo kutokana na umuhimu wake katika bidhaa na huduma za kijamii.

Tuesday, June 28, 2011

Mukama-Mafisadi CCM lazima wavue gamba

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilson Mukama, amesema yeye ni sawa na mtu aliyeteuliwa kufanya kazi ya kunyonga mkosaji aliyehukumiwa adhabu hiyo na Mahakama, hivyo hawezi kuogopa kutekeleza hukumu hiyo.

Akifafanua kauli hiyo jana mjini Morogro, Mukama alisema uamuzi wa ngazi za juu wa CCM ukishatolewa kuhusu kuvua gamba watuhumiwa wa ufisadi, hakuna kiongozi atakayepuuza kuutekeleza.

“Ufisadi unasemwa dhahiri na wananchi kwa kuwataja watuhumiwa hadharani wakiwahusisha ana EPA (Akaunti ya Malipo ya Nje ya Benki Kuu), Dowans, ununuzi wa rada na Richmond … na vikao vya chama vimetoa uamuzi.

“Kilichobaki ni utekelezaji tu…na hukumu ikishatolewa na Mahakama hakuna njia nyingine isipokuwa kutekeleza agizo hilo,” alisema Katibu Mkuu huyo alipokuwa akizungumzia madai, kwamba anaogopa kutoa barua za kujivua gamba kwa watuhumiwa wa ufisadi.

Akihutubia mahafali ya wanafunzi wanachama wa CCM wanaomaliza Chuo Kikuu cha Mzumbe Morogoro, Mukama alisema hataogopa kusimamia kikamilifu uamuzi wa chama hicho wa kuwatosa watuhumiwa hao.

Alisema vitendo vyao vimesababisha CCM na Serikali ichafuke mbele ya Watanzania.

Mbali na kuwavua gamba, Mukama alisema CCM pia itashughulikia suala la wafanyabiashara wasio waadilifu wanaojipenyeza ndani ya chama hicho, na itapambana na saratani ya kujilimbikizia madaraka na kukiondoa chama hicho katika utegemezi wa matajiri na wahisani wanaokiweka pabaya.

Alisema, hakuna mwananchi asiyejua kuwa ndani ya CCM wapo viongozi wenye nyadhifa kubwa wanaotuhumiwa kwa ufisadi kuanzia wa EPA, Richmond, Dowans, Rada na kashfa nyingine.

Katibu Mkuu huyo alisisitiza kwamba ili kukisafisha chama hicho mbele ya jamii na kukifanya kikubalike katika uchaguzi wowote, ni lazima watuhumiwa hao watoswe ili kurudisha imani kwa Watanzania.

Mukama alionesha katuni aliyodai imemchora hivi karibuni, akiwa na barua mkononi ikionesha kuwa ameshindwa kutoa uamuzi na kusisitiza kuwa uamuzi huo ni wa chama, hivyo utatekelezwa kama ilivyopangwa.

Awali katika risala ya wanafunzi hao, walitaka viongozi wote wa CCM kujikita kuwaletea maendeleo wananchi, ili baadaye wapimwe kwa kazi zao.

Wanachama hao waliwataka viongozi wahubiri amani badala ya kuendeleza malumbano na vyama vya upinzani na kuwataka watumishi wa Serikali kuachana na siasa wakati wakiwa watumishi wa umma.

Monday, June 27, 2011

Katiba mpya kuzinduliwa Aprili 26,2014

KATIBA MPYA ambayo mchakato wake umeanza inatarajiwa iwe imekamilika na kuzinduliwa rasmi Aprili 26, 2014 wakati wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano, Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema mjini hapa.

Akifungua Semina Elekezi kwa Wakuu wa Mikoa na wa Wilaya kuhusu mchakato wa Katiba Mpya kwenye ukumbi wa Hoteli ya St. Gasper, alisema hayo ndiyo matarajio ya Serikali.

"Ni matarajio ya Serikali kuwa Katiba Mpya itakuwa imekamilika na kuzinduliwa ifikapo tarehe 26 Aprili, 2014 katika Maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar,” alisema.

Waziri Mkuu alisema kwamba kama mambo yote yatakwenda kama yalivyopangwa, Muswada wa Sheria kuhusu Mapitio ya Marekebisho ya Katiba utawasilisha bungeni mwishoni mwa Mkutano wa Nne wa Bunge unaoendelea hivi sasa au mwanzoni mwa Mkutano wa Tano Oktoba mwaka huu.

Aliwataka Wakuu wa Mikoa na wa Wilaya kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Tume ya Kuratibu na Kukusanya Maoni itakayoundwa ili kuwezesha mikutano ya hadhara ya kukusanya maoni
kufanyika kama ilivyokusudiwa kwa kuhamasisha wananchi kuhudhuria na kutoa maoni yao.

“Katika suala hili kubwa na la kitaifa, ni vyema viongozi wasiingize siasa na wajiepushe kuwashawishi wananchi katika kutoa maoni yao, bali wawaache watoe maoni kwa uhuru au pasipo shinikizo lolote,” alisema.

Mchakato huo wa kuelekea uundwaji wa Katiba Mpya, umekwishaanza na katika hatua ya awali, Serikali imeandaa rasimu ya Muswada wa Sheria ya Mapitio ya Marekebisho ya Katiba ya Mwaka 2011.

Waziri Mkuu alisisitiza kuwa hatua ya sasa siyo kutunga Katiba Mpya bali ni kuunda Tume ya Kuratibu na Kukusanya Maoni ya Wananchi kuelekea kutungwa kwa Katiba Mpya.

Ngeleja-Umeme ni janga la taifa, vumilieni

WAZIRI wa Nishati na Madini, William Ngeleja amesema, mgawo wa umeme unaoendelea kote nchini ni janga la kitaifa linaloathiri shughuli za kiuchumi na kijamii kwa taifa.

Hata hivyo, waziri huyo alisema kuna mipango ya Serikali na Shirika la Umeme (Tanesco) yenye tija ya kukabiliana na mgawo huo wa umeme na kuwaomba wananchi waivumilie Serikali na Tanesco wakati inaendelea kutekeleza miradi hiyo.

Ngeleja pia alisema makali ya mgawo huo yatapungua wiki hii baada ya kuhakikishiwa na Wizara ya Fedha kwamba fedha za kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), ili izalishe megawati 100, zimepatikana.

“Hivyo kiwango cha uzalishaji umeme cha mitambo hiyo kitaongezeka kutoka megawati 10 kwa sasa hadi megawati 100 wiki ijayo,” alisema Ngeleja.

Alisema Serikali na Tanesco wanaguswa na kukerwa na adha na usumbufu unaosababishwa na mgawo wa umeme kama wanavyokerwa wananchi wote wa Tanzania.

Hata hivyo licha ya kuwepo kero hizo, amewaomba wananchi wapuuze dhihaka, kejeli na kebehi zinazofanywa na baadhi ya watu wasiothamini juhudi na jitihada za kweli zinazofanywa na Serikali na Tanesco yenyewe.

Alisema Serikali inaamini kwamba watu wote wanapuuza na kubeza jitihada hizi na Serikali na Tanesco wakati wanajua historia iliyopitia shirika la Tanesco kwa kutofanyika uwekezaji wowote kuanzia mwaka 1997 hadi 2005 kuwa wanafanya hivyo kwa makusudi.

Alifafanua kuwa watu hao wanafanya hivyo kwa maslahi yao binafsi, ikiwemo kupata umaarufu wa kisiasa, “tunawaombaa wananchi wawapuuze watu wa namna hii.”

Ngeleja alijitetea kuwa tatizo la mgawo wa umeme kwa nchi yetu ni tatizo halisi kama vile tatizo hilo lilivyoikumba nchi ya Japan kwa sasa kutokana na matatizo halisi ya kuathirika kwa vyanzo vya umeme ambavyo ni mitambo ya nyuklia baada ya kukumbwa na tetemeko la ardhi.

Alisema suluhu ya tatizo hilo siyo kubeza juhudi zinazofanywa na Serikali na Tanesco, bali ni kuunganisha nguvu za wadau wote na kuitia moyo Serikali na Tanesco kwa hatua za dharura zinazochukuliwa na miradi inayoendelea kutekelezwa kukabiliana na mgawo wa umeme nchini.

“Tunawaomba wananchi waendelee kuvumilia, tuimarishe mshikamano, utulivu na amani na tuwaepuke wote wanaobeza juhudi za Serikali na Tanesco kutatua tatizo la mgawo wa umeme kwa maslahi yao binafsi, ikiwa ni pamoja na maslahi ya kisiasa.

Alijitetea kuwa mgawo wa umeme unaoendelea kwa sasa umesababishwa na upungufu wa mvua zilizonyesha mwaka huu, hivyo kutojaza mabwawa yanayozalisha umeme kwa kuzingatia kwamba takribani asilimia 55 ya umeme unatokana na maji.

Alisema, bwawa la Mtera litafungwa mwishoni mwa Agosti kutokana na kina chake kuendelea kuwa chini.

Alisema, suala la Taifa kutegemea umeme wa maji kwa asilimia 55, sio dhambi wala kosa la makusudi wala uzembe, bali ni matokeo ya uwekezaji uliofanywa na Serikali kwa nia njema kama zilivyofanya nchi nyingine duniani.

Alisema, mabadiliko ya tabia nchi katika miaka ya hivi karibuni duniani yamekuwa na changamoto kubwa kwa nchi nyingi zinazotegemea kwa kiasi kikubwa umeme wa maji na akatoa mfano wa nchi ya Ethiopia.

Alizitaja kampuni za Symbion na Aggreko kuwa zimepewa jukumu la kupunguza makali ya mgawo wa umeme katika kipindi hiki cha dharura kwa kuzalisha megawati zaidi ya 200.

Kikao cha Bunge la bajeti kinaendelea tena leo kwa wabunge kuendelea kujadili hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyoiwasilisha Alhamisi iliyopita.

Mara baada ya kipindi cha maswali na majibu, wabunge wataendelea kuijadili hotuba hiyo ambayo itahitimishwa kesho kutwa kwa Waziri Mkuu kufanya majumuisho ya michango ya wabunge.

Friday, June 24, 2011

Wabunge waibue mijadala majimboni mwao

Kona ya Karugendo

Wabunge waibue mijadala majimboni mwao
Privatus Karugendo
22 Jun 2011
Toleo na 191
Raia Mwema

• Wengi hawana mawasiliano na wapiga kura wao

UKISIKILIZA jinsi mjadala unavyokwenda kwenye Bunge la Bajeti linaloendelea Dodoma, utagundua kwamba wabunge wetu hawana mawasiliano na wananchi waliowatuma bungeni.

Wengi wao wanawasilisha maoni yao binafsi badala ya kuwasilisha maoni ya wananchi. Wanaunga mkono hoja zote, kana kwamba hoja hizo zimetengenezwa na malaika. Kama huo ndio ukweli, ya nini basi hoja hizo kuletwa Bungeni?

Kwa nini wabunge wapoteze miezi miwili wakijadili kitu ambacho wanafahamu fika kwamba mwisho wake ni kupitishwa kwa asilimia 100?

Kama mchango wa maoni ya wabunge hauwezi kusaidia kubadilisha chochote ndani ya bajeti inayowasilishwa na serikali, ina maana gani, basi, bajeti hiyo kupelekwa Bungeni? Huku si kufuja fedha za walipakodi wa Tanzania? Kama wabunge hawana mchango wowote kwa bajeti, kwa nini kuijadili?

Ni busara na ni kubana matumizi kama Serikali ingeandaa Bajeti na kutusomea, na maisha yakaendelea kama kawaida kuliko kupoteza muda na fedha nyingi kujadili kitu ambacho kimefanyiwa maamuzi tayari!
Inashangaza jinsi wabunge wetu wanavyoviogopa vyama vyao vya siasa kuliko wanavyowaogopa wananchi waliowatuma Bungeni. Nijuavyo mimi, mbunge anapotangazwa na Tume ya Uchaguzi kuwa mbunge, anakuwa si mbunge wa chama; bali ni mbunge wa wananchi wa jimbo zima; hivyo kukiogopa chama chake wakati wa kujadili masuala ya kitaifa, ni kuwasaliti wananchi waliomtuma Bungeni.

Kwa jinsi Bunge letu lilivyo hivi sasa ambapo lina wabunge wengi wa chama kimoja (CCM) chenye kujali maslahi yake na kuziba masikio kwa kilio cha wananchi walio wengi, hata muswada wa kutunga sheria ambao ni dhaifu mno ukiwasilishwa Bungeni utapitishwa tu; maana ni utamaduni wa “ndiyooo” na “kuunga mkono asilimia 100” bila kutafakari au kuzingatia maoni ya wananchi na maslahi ya Taifa.

Mfano mzuri ni Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano uliopitishwa, wiki iliyopita, Bungeni. Uliletwa Bungeni ujadiliwe; lakini jinsi mjadala ulivyokwenda ilijionyesha wazi kwamba mpango huo ulishapitishwa tayari, na yeyote aliyekuwa na maoni tofauti alionekana kama msaliti.
Swali la kujiuliza ni kama Mpango huo ulishapitishwa tayari, kwa nini ulipelekwa Bungeni? Ili wa wabunge wetu wapate posho? Ili tutambue kwamba CCM ndicho chama tawala?

Hoja hapa si kuupinga Mpango huo, na ni imani yangu kwamba hata wabunge waliokuwa na maoni tofauti si kwamba walilenga kuupinga. Lakini ukweli ni kwamba hata wale waliouandaa si malaika; na si kweli kwamba kabla ya kuuandaa walizunguka nchi nzima kuomba maoni ya wananchi juu ya Mpango huo.
Kuna wananchi wanaoishi pembezoni na hasa wanawake walioulizwa juu ya Mpango huo? Mbona hatuoni vizuri mikakati ya kuwanufaisha walio pembezoni ndani ya Mpango wenyewe?

Mbunge wa Ubungo (CHADEMA), John Mnyika, alihoji juu ya Barabara ya Morogoro ambayo hivi karibuni itapanuliwa na mradi wa mabasi yaendeayo kasi. Lakini ndani ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano haionyeshi kwamba zitatengenezwa barabara mbadala za kuingia katikati mwa jiji wakati barabara ya Morogoro ikijengwa upya.

Pia Mnyika alihoji juu ya huduma ya maji wakati Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano unazungumzia mpango mpya wa huduma ya maji, bado mpango uliokamilika “wa Wachina” bado maji hayajatoka!

Hizo ni hoja za msingi kuzipuuza. Kwa hakika kuzipuuza ni kujitangazia hali ya hatari, kama si leo ni kesho. Maana; kama ni mpango wa maendeleo ya Watanzania, ni lazima Watanzania wote washirikishwe.
Haifai kabisa yawe ni mawazo ya mtu mmoja; kwani siku akiondoka, basi, na mpango mzima unakufa. Usiwe mpango wa chama kimoja; kwani siku kikiondoka madarakani mpango mzima unakufa.

Mpango huu wa miaka mitano, kwa bahati mbaya au nzuri, unakuja wakati Tanzania inasherehekea miaka 50 ya uhuru wake. Lakini pia unakuja wakati tumeshuhudia mipango mingi ya maendeleo na kukuza uchumi ambayo mafanikio yake, kama yanaonekana, basi, ni kwa watu wanaoishi dunia nyingine, na wala si hapa Tanzania.

Ndio maana watu wanakuwa na maswali mengi juu ya tumefanya nini ndani ya miaka 50. Kwamba yaliyoshindikana ndani ya miaka 50 yatawezekana ndani ya miaka mitano?
Kuuliza hivyo haina maana kwamba hatujafanya chochote ndani ya miaka 50. Kuishikia bango hoja hii kwamba kuna watu wanasema Serikali haijafanya chochote ndani ya miaka 50, ni kutaka kuipotosha hoja yenyewe.

Tanzania imefanya mengi ndani ya miaka 50. Ukiachia mbali wimbo wetu wa taifa wa “Amani na Utulivu”, kwenye michezo tunakuwa wa mwisho. Tunaimba “Amani na Utulivu”, uchumi wetu unadidimia. Tunaimba “Amani na Utulivu”, kiwango cha elimu kinashuka. Tunaimba “Amani na Utulivu”, kipindupindu, malaria na magonjwa ya kusendeka yanatuteketeza hadi tunakimbilia Loliondo tukiimba, “Amani na Utulivu”! Aidha, raslimali zetu zinachotwa na wajanja wachache, lakini sisi tunaimba “Amani na Utulivu.

Tulijenga Siasa ya Ujamaa na kujitegemea, ikafa na tukaizika. Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani miaka yote hiyo? Tulianzisha mashirika ya umma yakafa na kuzikwa. Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani miaka yote hii?

Tulianzisha maduka ya vijiji, yakafa yote. Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani miaka yote hii? Tulianzisha viwanda, vikafa vyote na kuzikwa. Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani miaka yote hii?
Tulikuwa na sekondari nzuri zikijulikana ndani na nje ya nchi, kama vile Ihungo, Tabora Boys, Milambo na nyingine nyingi. Ubora wa shule hizo umekwenda wapi? Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani?
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kilikuwa tishio Afrika nzima na duniani kote. Ubora wa chuo hiki umekwenda wapi? Wa kuulizwa ni nani kama si CCM iliyo madarakani miaka yote hiyo 50?

Ndani ya 50 hatuwezi kutengeneza wembe! Hatujavumbua kitu chochote zaidi ya panya wa kutegua mabomu! Tunanunua hata njiti za kuchokonoa meno kutoka nchi za nje. Viongozi wetu wakiugua wanakimbilia nchi za nje na kule wanatibiwa na madaktari wetu walioikimbia nchi.

Ndani ya miaka 50 tumezalisha madaktari wengi na namba kubwa imekimbilia nchi za nje kutafuta maslahi zaidi. Ndani ya miaka 50 tumenunua ndege ya rais wakati tunaomba msaada wa kujenga vyoo kwenye mashule yetu!
Ndani ya miaka 50 tumenunua magari ya kifahari kwa viongozi wetu wakati tunaomba msaada wa fedha za kuiendesha serikali yetu!

Ndani ya miaka 50 Tanzania bado tuna matatizo mengi. Wale maadui tuliowatangaza wakati wa Uhuru: Ujinga, maradhi na umaskini, bado yametuzunguka.
Na ndio maana ninapendekeza kwamba kuna haja wabunge wetu kutengeneza jukwaa la majadiliano ndani ya majimbo yao ili wapate nafasi ya kuwasikiliza watu na kupokea maoni yao.

Hatua hiyo itawasaidia kuondokana na utamaduni huu uliojengeka wa mbunge kuwasilisha bungeni maoni yake binafsi na kuegemea zaidi kwenye chama chake badala ya kuegemea kwa wananchi waliomtuma bungeni.

Wabunge wetu waige mfano wa TGNP. Huu ni Mtandao wa Jinsia Tanzania. Ni shirika la kiraia na kiuanaharakati linalotetea mabadiliko ya kijamii kwa mtazamo wa wanawake; mabadiliko ambayo yanalenga kwenye usawa wa jinsia, ukombozi wa wanawake, haki za kijamii, kufikia na kumiliki raslimali kwa wanawake, vijana na makundi mengine yaliyoko pembezoni.

TGNP ilianzisha jukwaa la majadiliano. Kila Jumatano jioni pale Mabibo, Dar es Salaam kuna mijadala inaendelea. Ni mijadala ya wazi inayomkaribisha kila mtu. Wanajadilia masuala mbalimbali ya kijamii, na siku hizi wanaendesha mijadala juu ya Katiba mpya.

Wabunge wetu wangekuwa wanatembelea jukwaa hili (wabunge wengi wa Tanzania wanaishi Dar es Salaam) wangeweza kupata mengi na kutambua mahitaji ya wananchi.

Aidha, wangeweza kujifunza mbinu za kuanzisha majukwaa kama haya kwenye majimbo yao. Ni kupitia kwenye majukwaa ya majadiliano tunaweza kuwa na uwakilishi wa kweli na wenye tija kwa taifa letu.
Mbali na jukwaa la majadiliano la kila Jumatano, TGNP inaandaa pia matamasha ya jinsia. Kila baada ya miaka miwili kuna tamasha la jinsia pale Mabibo. Tamasha la jinsia ni nafasi ya wazi kwa ajili ya watu binafsi, mashirika na mitandao, walio katika mapambano yanayofanana, kubadilishana uzoefu, taarifa na kujengana uwezo.


Mwaka huu, Septemba 13 hadi Septemba 16, TGNP itaendesha tamasha la jinsia la kumi. Mada kuu ya tamasha hili itakuwa ni Jinsia, Demokrasia na Maendeleo: Ardhi, Ajira na Maisha Endelevu.

Ni tamasha linalokuja wakati kumejitokeza wimbi kubwa la uporaji wa ardhi. Serikali bado ina kigugumizi juu ya wimbi hili na baadhi ya viongozi wa serikali wanashiriki wimbi hili la kupora ardhi.

Kwa maana hiyo, ni wakati mzuri wa kukutana na kujadiliana juu ya suala hili na mengine mengi. Haina maana kukaa na kupanga Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano wakati ardhi inaporwa.

Tunajua kwamba uchumi wetu unategemea kiasi kikubwa sekta ya Kilimo. Kama wananchi wetu hawana uhakika wa ardhi yao, kama ardhi inaporwa na matajiri wakishirikiana na wageni, wananchi watapata wapi ardhi ya kulima na kuzalisha? Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba ardhi ndio uhai wa kila binadamu. Bila ardhi hakuna uhuru!

Ni bahati mbaya kwamba viongozi na wabunge wetu wanalikwepa tamasha hili. Tamasha la jinsia la tisa, sikubahatika kukutana na kiongozi yoyote kwenye tamasha hilo. Hata viongozi wanaojulikana kuwa wapambanaji na watetezi wa haki za binadamu na wapenda maendeleo ya Tanzania, sikuwaona kwenye tamasha hili.

Natumaini mwaka huu viongozi wetu na wabunge watafika kwenye tamasha hili la jinsia; maana kila mwenye akili nzuri na kujali uhai wa taifa letu anaona wazi kwamba, sasa tunayumba. Na bila kuwa na majukwaa kama hili la TGNP na mengine mengi, tutazama kabisa!

Napenda kuwashauri viongozi wetu na wabunge kwamba matamasha kama hili la TGNP na mengine yanayoruhusu mijadala ya wazi, ni muhimu sana kwa maendeleo ya taifa letu.

Ni muhimu kuwasikiliza watu kabla ya kukaa na kuwapangia mipango ya miaka mitano. Unaweza kufikiri wananchi wanahitaji maji, kumbe wao wanahitaji moto!

Bunge kujadili ‘chenji’ ya rada

BUNGE limekubali kujadili msimamo wa Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza kutoa fedha za tozo za rada kwa asasi za kiraia badala ya kuzitoa kwa Serikali ya Tanzania.

Hoja ya kujadili suala hilo ilitolewa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema) na kuungwa mkono na baadhi ya wabunge baada ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kutoa kauli ya Serikali kuhusu suala hilo.

“Tutatafuta muda muafaka wa kulijadili suala hili,” alisema Spika wa Bunge, Anne Makinda. Kampuni hiyo imeamua kutoa pauni milioni 29.5 (Sh bilioni 75) zinazotokana na tozo ya fidia ya mauzo ya rada kwa wananchi wa Tanzania kupitia asasi za kiraia za Uingereza badala ya Serikali ya Tanzania.

Akitoa kauli ya Serikali, Membe alisema Serikali ya Tanzania imetahadharisha kwamba haitaruhusu asasi ya kiraia yoyote ile ya Uingereza itakayonufaika na fedha hizo kuja kuendesha shughuli zake nchini.

“Tanzania ni nchi masikini, lakini haiko tayari kudharauliwa kiasi hicho kwa Serikali yake, taasisi zake na asasi zake kutoaminiwa,” alisema Membe na kuongeza kuwa, “kuruhusu kufanya hivyo ni kuruhusu kuibiwa kwa mara ya pili.” Aliliambia Bunge kuwa “tuwe tayari kupoteza fedha hizo kwa kulinda heshima ya Taifa letu. Tusiwe tayari kudhalilishwa na kuruhusu kampuni iliyotuibia iamue fedha zetu apatiwe nani huko Uingereza na zitumike vipi hapa nchini.”

Waziri huyo alitoa kauli hiyo wakati tayari Bunge limetuma wabunge wanne kwenda Uingereza kukutana na kamati husika iliyoundwa na BAE Systems na kufanya mazungumzo na wabunge wa Bunge la Uingereza.

Wabunge hao ni Naibu Spika Job Ndugai (Kongwa –CCM), Mussa Zungu (Ilala - CCM), Angellah Kairuki (Viti Maalumu –CCM) na John Cheyo (Bariadi Mashariki – UDP).

Wabunge hao pia watakutana na viongozi wengine wenye ushawishi mkubwa nchini Uingereza kuwashawishi waishinikize Kampuni ya BAE Systems kuzitoa fedha hizo kwa Serikali ya Tanzania bila masharti yoyote.

“Kampuni ya BAE Systems ina masikio, lakini haitaki kusikia kilio cha wengi, imeonyesha dharau ya wazi dhidi ya Serikali yetu na watu wake,” alisema Membe.

Alisema iwapo Serikali itapata fedha hizo, imedhamiria kuzielekeza fedha hizo kwenye sekta ya elimu ikiwemo kununua vitabu milioni 4.4 kwa ajili ya wanafunzi wa shule za msingi, kununua vitabu 192,000 vya kufundishia kwa ajili ya walimu wa shule za msingi.

Pia alisema watanunua madawati 200,000 kwa ajili ya wanafunzi 16,000 wa shule za msingi na kujenga nyumba 1,996 za walimu wa shule za msingi vijijini na kujenga vyoo 200,000 kwenye shule za msingi nchini.

Kampuni ya BAE Systems iliamuriwa na Mahakama nchini Uingereza kulipa faini hiyo baada ya kugundulika kwamba ilikwenda kinyume katika kuiuzia Tanzania rada mwishoni mwa miaka ya 1990.

Mahakama yaionya Serikali kesi ya Richmond

HAKIMU anayesikiliza kesi ya kughushi na kutoa taarifa za uongo kuhusu Kampuni ya Kufua Umeme wa Dharura ya Richmond inayomkabili Mfanyabiashara, Naeem Gire, ametoa onyo la mwisho kwa Wakili wa Serikali, Fedrick Manyanda akamilishe ushahidi wake haraka.

Onyo hilo lilitolewa jana na Hakimu Waliarwande Lema wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakati kesi hiyo ilipokuja kusikiliza ushahidi wa upande wa mashitaka.

Alisema, kesi hiyo imekuwa ikiahirishwa mara kwa mara kutokana na upande wa mashitaka kushindwa kuleta mashahidi wake kwa wakati na kuahirisha kwa mara ya mwisho Juni 28 mwaka huu ambapo watakaposikiliza shahidi wa mwisho.

“Nimekubeba vya kutosha mpaka sasa ninaona aibu, ninaomba ulete shahidi wako wa mwisho kabla ya kufunga kesi na mashitakiwa kuandaa utetezi wake,” alisema Hakimu Lema.

Awali wakili wa upande wa utetezi, Alex Mgongolwa aliitaka mahakama kufunga ushahidi wao kwa kuwa ni mara ya tatu wanaahirisha kesi kutokana na shahidi kutofika mahakamani na kumtaka Wakili Manyanda kutaja jina la shahidi huyo.

Juzi kesi hiyo iliahirishwa kwa kuwa shahidi aliyetakiwa kutoa ushahidi wake hakufika mahakamani.

Jambo hilo lilizua mjadala kati ya mawakili hao na Mgongolwa akalalamikia upande wa mashitaka kuchelewesha usikilizwaji wa kesi hiyo.

Inadaiwa kuwa, Juni, 2006 jijini Dar es Salaam, mshitakiwa Gire alitoa taarifa za uongo kwa wajumbe wa timu ya majadiliano ya Serikali, kuwa Kampuni ya Richmond LLC ya Texas, Marekani, ina uwezo wa kuzalisha umeme ili apewe zabuni.

Katika mashitaka mengine inadaiwa kuwa Gire, aliwasilisha hati ya nguvu ya kisheria iliyotolewa Machi 3, 2006 ikimuonesha kuwa ameruhusiwa na Mwenyekiti wa kampuni hiyo, Hemed Gire ambaye ni kaka yake kufanya kazi za kampuni hiyo hapa nchini.

Zitto matatani

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), amedai kuwa Baraza la Mawaziri limerubuniwa na watu wenye maslahi ya kuliua Shirika Hodhi la Mali za Mashirika ya Umma (CHC), hivyo kubadili mapendekezo ya Bunge ya kulipa muda wa kutosha shirika hilo kukamilisha kazi zake.

Kwa kauli hiyo, Zitto ameingia matatani baada ya mawaziri kumtaka athibitishe ukweli wake na Spika wa Bunge, Anne Makinda amempa siku saba awasilishe ushahidi kwamba Baraza la Mawaziri lilishawishiwa kubadili uamuzi huo na watu ambao hakuwataja.

Akiwa mchangiaji wa kwanza wa Azimio hilo lililowasilishwa bungeni jana na Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mashirika ya Umma, alisema Azimio hilo limegeuzwa kutoka vile lilivyokuwa awali baada ya mawaziri kushawishiwa.

Hoja ya msingi ya Mkulo ilikuwa ni kuliomba Bunge kupitisha Azimio hilo ili CHC iongezewa kipindi cha mpito cha miaka mitatu limalize majukumu yake na baadaye majukumu hayo yahamishiwe Ofisi ya Msajili wa Hazina, lakini hoja hiyo ilikumbana na upinzani mkali kutoka kwa wabunge wa CCM na upinzani na hatimaye ikafanyiwa marekebisho.

“Mheshimiwa Spika, ndani ya Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma na hata katika Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, tulikubaliana kwamba CHC wapewe muda wa kutosha kukamilisha kazi na majukumu yao halafu baada ya hapo Waziri ndio alete Azimio hapa na si kuwapa kipindi cha mpito cha miaka mitatu kama Azimio lilivyowasilishwa leo.

“Nawaombeni wabunge wenzangu wote, tukatae maamuzi haya ya Baraza la Mawaziri kwa kuwa yametokana na kurubuniwa na watu wenye lengo la kuua CHC kwa ajili ya maslahi yao. Ikumbukwe kuwa chombo hiki kinaangalia mali za umma na mashirika, hivyo kutaka kukiua na kupeleka majukumu haya kwa Msajili wa Hazina ambaye uwezo wake wa kulinda mali za umma ni mdogo sana ni kutaka kuiba mali za Watanzania,” alisema Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni.

Alisema azimio la Serikali la kuipa CHC kukamilisha majukumu yake limelenga katika kuwasaidia wafanyabiashara walioiba mali za umma, ikiwemo kukopa mabilioni ya fedha kutoka iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ambao kesi zao zipo mahakamani, kupata ahueni kwa vile hatua hiyo itapoteza ushahidi.

Baada ya kueleza hayo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika, aliomba Mwongozo kwa Spika akitaka Zitto athibitishe kauli yake kwamba mawaziri wamerubuniwa kwa vile imewadhalilisha mawaziri hao ambao wanafanya kazi kwa maadili na kwa kuzingatia maslahi ya nchi.

Mkuchika alisema kitendo cha kusema maamuzi hayo yanatokana na kurubuniwa kwa mawaziri yanaleta picha mbaya kwa Watanzania ambao wamewaamini.

Baada ya maelezo hayo ya Mkuchika, Spika alimtaka Zitto kuwa makini na kauli anazozitoa anapochangia, ikiwemo ile ya kudai mawaziri wanashawishiwa na kurubuniwa, lakini Zitto aliposimama tena ili kuendelea kuchangia, alitamka tena kuwa anao ushahidi kwamba mawaziri walikuwa wameshawishiwa na kurubuniwa hadi wakatengeneza Azimio hilo jipya.

“Mheshimiwa Spika, siwezi nikatafuna maneno hapa, nina uhakika na ninachokisema, maamuzi ya Baraza la Mawaziri ni matokeo ya ma-lobbyist na kama Serikali mnabisha, leteni hapa mapendekezo ya awali ambayo yaliwasilishwa katika Kamati ya Makatibu Wakuu na Baraza la Mawaziri ili tuone yalikuwa yanasemaje,” alisema Zitto katika mchango wake.

Kutokana na msimamo huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alimuomba Spika Makinda kumtaka Zitto kuwasilisha bungeni ushahidi kutokana na kauli yake hiyo, hatua iliyomfanya Spika kumpa Mbunge huyo kumpa muda wa kuandaa ushahidi huo na kuuwasilisha bungeni Juni 29, mwaka huu.

Hata hivyo, mjadala kuhusu Azimio hilo, ulionekana kuwa mwiba mkali kwa Serikali kutokana na wabunge ambao mara nyingi wamekuwa wakigawanyika kivyama, kuungana na kuwa kitu kimoja wakiipinga vikali serikali kwa mpango wake huo na kuitaka ichane nao mara moja.

Mbunge wa Mwibara, Alphaxard Lugola (CCM), alisema kitendo cha kuweka muda huo ni kutoa mwanya wa maandalizi ya wizi wa mali za mashirika ya umma ambayo yamekuwa yakitumiwa na wachache kujitajirisha.

“Mheshimiwa Spika mimi ni Mbunge wa CCM, lakini katika hili napingana kabisa kwa kuwa nilipata fursa ya kuchungulia na kuwahoji walioko kwenye mashirika ndio maana nina uchungu kwa kuwa fedha zinaliwa bila sababu ya msingi...hicho kipengele cha majukumu ya CHC kuwa chini ya Msajili wa Hazina ambaye hata ukimuuliza ana mashirika mangapi hajui, wala hajui hisa za serikali zipo wapi na wapi, itakuwa ni kuwafikisha Watanzania mahala pabaya,” alisema.

Alisema kuwa imefikia mahali ambapo maamuzi yanatolewa na Bunge yanapuuzwa na Serikali na kufanya hivyo si kuwatendea haki Watanzania, akaitaka serikali kubadilika na kukubali kutoa muda wa kutosha kwa shirika hilo na lijengewe uwezo.

Pamoja na Lugola, Mbunge wa Kalenga, Dk. William Mgimwa (CCM) na Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), walikomelea msumari wa mwisho katika kupinga hoja hiyo, hatua iliyotosha kuifanya Serikali kupitia kwa Waziri Mkulo, kukubali kulifanyia marekebisho Azimio hilo kwa kuondoa baadhi ya maneno na wabunge kwa kauli moja walilipitisha.

Maneno yaliyoondolewa ni yale yaliyokuwa yakisema kuwa Bunge liipatie CHC ambayo muda wake wa utendaji utakwisha Juni 30, 2011, muda mwingine wa kipindi cha mpito cha miaka mitatu hadi Juni 30, 2014, ili baada ya muda huo kazi za CHC zihamie Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Kutokana na mabadiliko yaliyofanywa, CHC imepewa kipindi hicho cha miaka mitatu, lakini bila kuwepo kipengele kinachosema baada ya muda huo, kazi zake zitahamishiwa kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina, badala yake baada ya muda huo, Serikali itawasilisha tena Bungeni Azimio kuhusiana na kipi kifanyike kama kuiongezea tena muda CHC au vinginevyo.

Shughuli zinazofanywa na CHC ambazo mpaka sasa hazijakamilika ni pamoja na urekebishaji wa TRL baada ya kampuni ya Rites kuondoka, kushughulikia uuzaji wa hisa za Serikali katika NBC (T) Limited, uperembaji na uhakiki wa vitendo na mashirika yaliyobinafsishwa, urekebishaji wa mashirika 34 yaliyobaki na kukamilisha ufilisi wa mashirika ya umma 24 yaliyobaki.

Nyingine ni ukusanyaji wa madeni ya iliyokuwa NBC yenye thamani ya Sh bilioni 15.8 na urekebishaji wa Kampuni ya TTCL baada ya hatua ya awali ya ubinafsishaji kushindikana na mwekezaji wa Airtel kuonesha nia ya kutoka katika ubia.

Thursday, June 23, 2011

‘Wanawake hujamiiana bila ridhaa yao’

WANAWAKE wengi nchini wanadaiwa kujamiiana kwa mara ya kwanza bila ya maridhiano baina yao na wanaume.

Mwezeshaji kutoka Maendeleo ya Jamii ya Shirika lisilo la Kiserikali la Plan International, Geryson Frednand alisema hayo katika washa ya siku mbili ya haki za wasichana na wanawake iliyoandaliwa na shirika la Care International.

Frednand alisema, katika utafiti waliowahi kuufanya, unaonesha kuwa wanawake wengi hasa katika maeneo ya vijijini wamekwa wakishurutishwa kufanya mapenzi au kuozeshwa kabla ya muda wao kufika.

Alisema, katika maeneo ya vijijini ndipo vitendo vya ukatili wa wanawake hufanyika kwa wingi.

Pamoja na mambo mengine, mwezeshaji huyo alisema utafiti unaonesha asilimia kati ya 15 na 71 ya wanawake wananyanyaswa na waume zao huku wakiogopa kutoa taarifa katika ngazi husika kwa kuogopa kuachika.

Alisema, kwa sasa hatuna budi elimu ya uzazi na juu ya haki za msingi itolewe kwa wingi kwa jamii vijijini ili kupunguza ukatili wa wanawake kutoka kwa waume zao.

“Nashangaa kuona wanawake wengi hawatoi taarifa katika ngazi husika pindi wanapofanyiwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia na waume zao, hali ambayo inawafanya kuathirika kisaikolojia na kujikuta wakikosa sehemu ya kukimbiza malalamiko yao kwa wakati,” alisema.

Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari Kuhusu Bajeti Ya Serikali Mwaka 2011/2012 Kutoka Kambi Rasmi Ya Upinzani

Utangulizi

Mnamo tarehe 21/06/2011 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha bajeti ya Makadirio na Matumizi ya Serikali kwa mwaka 2011/2012.

Pamoja na Bajeti ya Serikali kukubali na kuzingatia baadhi ya hoja zilizotolewa na wabunge wa Kambi ya Upinzani na hususani CHADEMA kama vile ;

a) Kupunguza kodi na tozo mbalimbali kwenye mafuta ya petrol na
dizeli.
b) Kupunguza kiwango cha faini za makosa ya barabarani kutoka shilingi
300,000/50,000 hadi kufikia ukomo wa shilingi 30,000.
c) Kufuta leseni za biashara kwenye Majiji,Halimashauri za Wilaya na
Vijiji.
d) Kufuta misamaha ya kodi kwenye makampuni yanayotafuta mafuta na
gesi Nchini.
e) Kuongeza pesa kwenye bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu kwa kuhakikisha
kuwa kodi ya skills development levy 2/3 inapelekwa kwenye bodi kwa
ajili ya Mikopo.

Katika kupitisha bajeti hiyo wabunge wa Kambi ya Upinzani na hususani wa CHADEMA tuliamua kupiga kura za HAPANA kwenye mapendekezo hayo ya Serikali kutokana na sababu mbalimbali na haswa hizi zifuatazo;
1. Serikali haikukubaliana na hoja yetu ya kuondoa posho za vikao (sitting allowances) kwenye mfumo wa malipo ndani ya serikali.

2. Serikali haikukubaliana na hoja yetu ya kuhakikisha kuwa magari yote aina ya “Mashangingi” yanayotumiwa na viongozi na watumishi wa umma yauzwe kwa mnada ndani ya miezi sita na viongozi hao wakopeshwe magari kwa ajili ya kufanya majukumu yao mbalimbali.

3. Serikali haikukubaliana na hoja yetu ya kufuta/kupunguza misamaha mikubwa ya kodi ambayo Makampuni ya Madini yanapata ili kuhakikisha kuwa serikali inapata mapato kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali
ya maendeleo.

4. Serikali imekataa kuingiza pensheni kwa ajili ya wazee wote nchini ya shilingi 20,000 kila mwezi ili kuweza kuwapunguzia ukali wa maisha wazee wetu .

5. Serikali imekataa Kufuta/kuondoa misamaha ya kodi kwa kipindi cha miaka 10 kwenye maeneo maalum ya uwekezaji (EPZ).

6. Serikali haikukubaliana na hoja yetu ya kuhakikisha kuwa tunapunguza gharama za safari na haswa kuhakikisha kuwa ni viongozi wakuu na wenzi wao tuu ndio waruhusiwe kusafiri kwa kutumia daraja la
kwanza (first class) ambao ni ;

* Rais
* Makamu wa Rais
* Waziri Mkuu
* Spika
* Jaji Mkuu

Mawaziri wasafiri kwa kutumia daraja la pili (bussines class) na viongozi wengine wote wa umma na watumishi wa umma wakiwemo wabunge wasafiri kwa kutumia daraja la kawaida (economy class).

Pia misafara ya viongozi wakuu ipunguzwe ili kupunguza gharama za kuhudumia misafara hiyo pindi wanaposafiri nje ya Nchi.

Hitimisho.

1. Tumeamua kumwandikia katibu wa Bunge barua ili aweze kutenganisha fomu kwa ajili ya mahudhurio na kwa ajili ya posho na wabunge wa CHADEMA hawatasaini fomu za posho.

2. Kuhusu magari, kiongozi wa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni (KUB) Mhe. Freeman Mbowe ameamua kurejesha gari yake aina ya “Shangingi” alilopewa na Bunge ili liwe la kwanza kupigwa mnada.

Tunawataka wabunge wengine waunge mkono hoja hizi kwa masilahi ya wananchi na Taifa kwa ujumla.


Imetolewa na ;
Mhe. Freeman A. Mbowe (Mb),
Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni
21 Juni 2011

Wednesday, June 22, 2011

Bajeti yapita, Mbowe asusa shangingi

BAJETI ya Serikali ya Tanzania kwa mwaka wa fedha 2011/12, imepita jana.

Serikali imetangaza kodi na tozo ambazo imezipunguza katika bidhaa ya petrol kuwa ni Sh. 323.5 kwa lita ili kuhakikisha bidhaa hiyo inashuka bei na kutoa ahueni ya maisha kwa wananchi.

Akihitimisha hotuba ya Bajeti ya Serikali bungeni, Waziri wa Fedha, Mustafa
Mkulo alisema, Serikali imekubaliana na ushauri wa Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi na ushauri wa wabunge wengine kuondoa kodi na tozo kwa bidhaa hiyo ya petroli.

Alifafanua kuwa, Serikali imepunguza kodi ya bidhaa ya petroli kutoka Sh. 314 kwa lita hadi Sh. 256 kwa punguzo ambao ni karibia Sh. 100 kwa lita lita na pia imepunguza tozo mbalimbali zinazotozwa kwa lita kwa kiasi cha Sh. 224.50.

Mkulo pia alisema, Serikali pia itapunguza tozo za mamlaka mbalimbali za huduma kama, Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Shirika la Viwango (TBS) na Mamlaka ya Usafiri wa Nchikavu na Majini Sumatra.

Nyingine ambazo tozo zao katika petrol zitapunguzwa ni Kampuni ya Kusafisha Mafuta (Tipper), Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) na Mamlaka ya Udhibi wa Huduma za Maji na Nishati (Ewura).

Lengo la kupunguza tozo hizo kwa mujibu wa Mkulo ni kushusha bei ya bidhaa ya petroli.

Pia Waziri Mkulo alisema, Ewura itakokotoa upya kiwango kinachotozwa na kampuni zinazoagiza mafuta ambacho ni asilimia 7.5 ili kufidia gharama zingine na kushusha gharama kwa mlaji.

Aliwaeleza wabunge kuwa, ushuru kwa upande wa mafuta ya taa utarekebishwa ili kukomesha vitendo vya ukwepaji kodi na uchakachuaji vinavyofanywa na wahujumu uchumi na Ewura imekabidhiwa kazi ya kufanya hesabu ili tozo za mafuta ya taa
zipitiwe upya.

“Lengo letu ni kuondoa uchakachuaji kabisa,” alisema Mkulo. Ingawa waziri huyo
hakutaka kueleza tozo hizo kwa upande wa mafuta ya taa, ni wazi kuwa tozo na ushuru utaongezeka ili viwango vyake viwiane na vile vinavyotozwa kwa mafuta ya petrol na dizeli.

Mkulo alitumia muda mwingi kuzungumzia suala hilo la mafuta alisema hata hivyo Tanzania haipangi bei ya mafuta katika soko la dunia.

Alitoa mfano kuwa ndani ya wiki moja, bei katika soko hilo, bei ya pipa imepanda kutoka dola za Marekani 116 hadi 131.

Pia alisema, kuimarika kwa dola na kushuka kwa thamani ya Shilingi nalo ni tatizo
lingine ambalo linachangia bei ya bidhaa ya petrol kupanda. Alitoa mfano kuwa kwa
sasa dola moja ya Marekani ni Sh. 1,600.

Hata hivyo waziri huyo alitamba kuwa marekebisho yaliyofanywa na Serikali yataleta nafuu na kuchagamsha uchumi wa nchi.

Alisema pia marekebisho hayo yataondoa uharibifu wa magari na yatapunguza bei na kushusha gharama za usafirishaji na Serikali itapata mapato yote yalikuwa yanapotea kwenye uchakachuaji wa mafuta.

Kwa upande wa posho, Waziri Mkulo alisema, uamuzi wa kuzifuta na kuzirekebisha baadhi ya posho hizo umefikiwa na Serikali yenyewe. Alisema katika hotuba yake alisisitiza kuwa ili kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, Serikali itapunguza posho zisizo na tija na safari za nje ambazo hazina tija.

Alisema suala hilo la posho limekuzwa isivyo kawaida na kwa kutumia takwimu ambazo si sahihi. Alisema posho zote zimetengwa Sh. bilioni 312 na si Sh bilioni 980 kama zilivyokuwa zinadaiwa na Kambi ya Upinzani.

Kati ya Sh. bilioni 321.74, posho zilizometengwa kwa ajili ya vikao (Sitting allowance) ni Sh. bilioni 25.68 tu na kati ya hizo wabunge peke yao watatumia Sh. bilioni 4.92 tu.

“Kwa hesabu hizo wabunge pimeni kama tukiamua kufuta posho za vikao kwa wabunge tutaokoa Sh bilioni 4 tu na kama tukifuta kwa Serikali nzima zitaokolewa Sh bilioni 25.68.

Alisema posho zingine haziwezi kuondolewa kwani zipo kisheria hivyo hazifutwi na akatoa mfano wa posho za joho la jaji au posho za madaktari.

Alisema, kwa kuwa umeme ndio kipaumbele kikubwa cha bajeti ijayo, Mkulo ambaye
amekuwa anatuhumiwa kulidanganya Bunge kutokana na takwimu za miradi ya umeme, alibanisha kuwa wizara hiyo imetengewa zaidi ya Sh. bilioni 402 na ya hizo fedha za maendeleo ni Sh. bilioni 325.4 na Sh. bilioni 74 ni matumizi ya kawaida.

Pia alisema, kuna Sh bilioni 536.9 zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya umeme
zikiwemo fedha zilizoko katika miradi ya MCC. “Sijaliongopea Bunge fedha za miradi ya umeme zipo.”

Alikiri kuwa ni kweli misamaha inapunguza mapato ya Serikali lakini akasisitiza kuwa
inatolewa kwa nia njema hivyo ni lazima iendelee kutolewa kwani inasaidia katika
huduma za kijamii.

Alisema, Serikali inapitia upya baadhi ya misamaha hiyo na ile inayotumiwa vibaya itafutwa.

Alifafanua kuwa hata hivyo misamaha hiyo imepungua kutoka asilimia 4.2 ya pato la Taifa katika bajeti iliyopita hadi kufikia asilimia 2.5 ya pato la Taifa katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha.

Wabunge waliopitisha bajeti, 234 walikubaliana na bajeti hiyo,wabunge 81 wakikataa bajeti hiyo.

Pamoja na maelezo hayo ya Mkulo, Kambi ya Upinzani ilikataa Bajeti hiyo kwa madai kuwa hoja zao hazijazingatiwa hata baada ya baadhi kuelezwa na Mkulo kuwa zilikuwa za uongo.

Kutokana na madai hayo, kuwa hoja zao hazikuzingatiwa ikiwemo ya posho, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Freeman Mbowe jana alitangaza kurejesha gari , shangingi alilopewa na Bunge ili lipingwe mnada.

Akizungumza jana na waandishi wa habari baada ya bajeti kupitishwa, Mbowe alisema
wamemwandikia Katibu wa Bunge wakimweleza pia kuwa wabunge wa Chadema hawatasaini fomu za posho pamoja na madai ya juzi kuwa baadhi ya wabunge wa chama hicho hawakupenda kususia posho.

"Tunawataka wabunge wengine waunge mkono hoja hizi kwa maslahi ya wananchi na Taifa
kwa ujumla," alisema Mbowe.

Kujadili mfumo wa Rais katika Katiba hakukwepeki-Jaji Bomani

JAJI mstaafu Mark Bomani, amesema wakati wa kujadili Katiba mpya, Watanzania hawataepuka kuzungumzia mfumo wa Rais, awe Rais mtendaji au asiye mtendaji na nani asimamie mamlaka ya utendaji wa Serikali.

Bomani pia alitaka Watanzania wajadili kwa kina kila kitu bila uoga, ikiwemo muundo wa Muungano, uwe wa Serikali mbili, moja au tatu.

Alisema hayo jijini Dar es Salaam wakati akifungua kongamano la maadili ya wanahabari kuhusu mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lililoandaliwa na Baraza la Habari nchini (MCT).

Pia alizindua vitabu viwili vilivyochapishwa na MCT vilivyohusu kanuni za maadili kwa wanahabari na Mwongozo wa kuandika habari za mahakamani.

Alisema kila kitu kijadiliwe bila uoga kwani Watanzania wana uzoefu wa kutosha kujadili hata aina ya Muungano na kufikia muafaka.

Pia alipendekeza mjadala wa wazi kuhusu idadi na aina ya mihimili kama vile Bunge, Serikali Kuu, Mahakama na asasi nyingine kama vile Tume ya Haki za Binadamu na Tume ya Maadili ya Viongozi.

“Suala la haki za binadamu pia lizungumziwe na kuwekewa vifungu vya kutosha,” alisema na kuongeza: “Unapozungumzia mhimili wa Bunge, je uwe na baraza moja tu la Bunge au labda uwe na zaidi ya baraza moja, na kama ni hivyo mabaraza hayo yapatikaneje na mgawanyo wa madaraka uweje.”

Jaji huyo alitaka wakati wa mjadala wa mhimili wa Bunge, Watanzania waamue suala la upatikanaji wa wajumbe wake na kuwe na aina ngapi za wabunge wa kuchaguliwa kwenye majimbo ya uchaguzi au kwa mtindo wa uwiano au njia zote mbili.

Aidha, Jaji Bomani alitaja masuala mengine muhimu kuwa ni ya wagombea binafsi; waruhusiwe au la; mawaziri wawe wabunge au wasiwe; uwepo uwakilishi wa makundi mbalimbali ndani ya jamii na kama hivyo hayo makundi yafahamike.

Hata hivyo alisema mchakato huo ni lazima mjadala wake uanzie mahali fulani na hadidu za rejea zilizo wazi ziwepo na zijulikane ili mjadala uwe na tija.

Tuesday, June 21, 2011

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Wasichana 40 wa Tanzania kwenda Swaziland kujifunza Reed Dance!!
Huu utamaduni ni kwa faida ya nani?

Sisi Muungano wa Asasi za Kiraia zipatazo 50 zinazotetea Usawa wa Jinsia, Haki za Binadamu, Maendeleo na Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi (FemAct) hapa nchini,tumepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa zilizoandikwa kwenye gazeti la Daily News la tarehe 11 June 2011 , kwamba Mhe, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameridhia mkataba wa makubaliano na Mfalme Mswati 111, wa Swaziland unaohusu wasichana 40 toka Tanzania kwenda Swaziland mwezi Oktoba mwaka huu 2011, kwa ajili ya kujifunza na kusherehekea ‘reed dance’(utamaduni wa Waswaziland ambao unaruhusu wasichana waliyo bikira kucheza dansi hii ya jadi mbele ya mfalme, malikia na viongozi wengine wakiwa nusu uchi. Kila mwaka takribani wasichana 40,000 wa Swaziland husherekea siku hii, ambayo hapo awali ilikuwa ni njia moja ya kumuezi Malkia wa nchi hiyo. Baadaye dansi hii imekuwa ikitumiwa na mfalme kuchagua mke kutoka kwa mabinti hawa ambao kwa hali ya kawaida sheria zetu hapa Tanzania zingalikataza kwani ni ukiukwaji wa haki za watoto wa kike.
Vile vile, dansi hii imekuwa ni kivutio cha watalii nchini Swaziland, hivyo wasichana katika nchi hiyo ya Swaziland wamekuwa wakitumiwa kama kitega uchumi. Wale wanaounga mkono dansi hii wanadai kwamba inajenga utamaduni wa kuthibiti wasichana wasijiingize katika masuala ya ngono kabla ya umri wao. Lakini cha kushangaza ni kwamba Mfalme wa Swaziland amekuwa akitumia nafasi hii kama njia rasmi ya kuchagua mke kutoka kwenye kundi hili la Mabinti wenye umri mdogo wa Kiswazi. Hii inamaanisha kwamba Mfalme hakutaka kuchagua mwanamke wa kuoa ambaye ameshafanya mapenzi na mwanaume mwingine. Mfalme huyu ana wake takribani kumi na moja na watoto ishirini na tatu.


Sisi wanaharakati wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi tumesikitishwa na taarifa hizi zilizochapishwa na gazeti la Serikali “ Daily News” katika makala maalum iliyosomeka” When Tanzania Deserve not the Best” ambapo mwandishi amedai kwamba Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wamekubaliana na Mfalme Mswati 111 kwa kile alichokiita “ Ridance Diplomacy” kwamba wasichana 40 wataenda huko Swaziland kujifunza hii dansi!!! Tunajiliuliza huu utamaduni ni wa nani? Kwa manufaa ya nani? Ni watoto wa nani watakaoenda kujifunza hii dansi na kwa madhumuni gani?.


Huko Swaziland wasichana bikira wakiwa nusu uchi hucheza mbele ya Mfalme na Malkia, na umati wa watu. Kwa nini miili ya wasichana itumike kuwavutia watalii? Kwa nini watanzania tukubali kuiga mambo ya kikoloni ya kuuza watu ili kupata fedha? Je kwa kuingia mkataba na Swaziland tunawatayarisha watoto wetu ili waweze kuwachezea “ wafalme wetu na malkia wao?” Je tunataka kujitayarisha kuuza miili ya watoto wetu wa kike ili wavutie watalii kwa madhumuni ya kitega uchumi wa taifa hili? Je ni watoto kutoka familia zipi watakaotumika?

Ndugu zetu Watanzania, katika karne hii, viongozi wetu wanataka kuwatumia watoto wetu wa kike kama viburudisho na kama vitega uchumi? Hili linaashiria taifa kuelekea kubaya na huenda katika kundi hili wafalme wetu wakapata fursa ya kuchagua wake, vimada, au nyumba ndogo. Wakati “ watalii” wakiweza kupata windo lao kwa njia rahisi kwa ajili ya biashara ya ngono. Matukio kama haya yanafanyika katika nchi nyingi. Kwa mfano Waarabu matajiri huenda India katika familia maskini kununua mabinti wazuri kwa ajili ya kuwatumia kama watumwa wa ngono” Sexual slaves” Je, hiki ndicho tunachotaka kifanyike kwa watoto wetu wa Tanzania katika miaka ijayo?


Tunamtaka Rais wetu Jakaya Kikwete atumie busara katika hili, kama kuna fedha za kudhamini basi fungu hulo litumike kusomesha watoto wanatoka kwenye familia zilizoko pembezoni. Rais asitumie fedha za walipa kodi kuwapeleka wasichana wadogo katika matayarisho ya kuja kutumiwa kama vyombo vya burudani. Huu ni utumwa wa kisasa (modern slavery) na haikubaliki.


Tunataka mkataba uvunjwe mara moja na asitokee binti wa Kitanzania kwenda kufundishwa hiyo ngoma ya unyanyasaji huko Swaziland.Wakati tulio nao sasa mabinti wanatakiwa wapewe elimu ya kuwawezesha kukuza vipaji vyao vitakavyowawezesha kujiendeleza kama binadamu si kujifunza ngoma za tamaduni za watu ambazo hata kwa wao wenyewe hazina tija. Hii ni fedheha wakati huu tunapojaribu kukuza heshima na utu wa watoto wa Afrika na husasani watoto wa kike.


Wanaharakati wa Swaziland, wanapambana na hii mila potofu, yenye kuwadhalilisha watoto wa kike na kuwanyima haki zao za msingi hususani haki za kuendelea na masomo. Sisi wapenda na watetezi wa haki za wanawake na watoto hapa Tanzania, tunapinga vikali kitendo hiki kinachoashiria kuwadhalilisha watoto wetu wa kike, na kutuvunjia heshima wanawake wa Tanzania na Watanzania wote kwa ujumla.


Tunawaomba Watanzania wote tuungane kupinga vikali hatua ya kuingiwa kwa mkataba wa kuwapeleka wasichana 40 kwenda Swaziland kujifunza ngoma ya Reed dance kwa sababu ni udhalilishaji wa watoto wa kike na ni sawa na taifa kuingia katika biashara ya utumwa wa kisasa.

Imetolewa na:

Usu Mallya
Kny. Sekretarieti ya FemAct

Semina: HAKI NA WAJIBU WA RAIA KATIKA KUSHIRIKI MCHAKATO WA KUPATA KATIBA MPYA NCHINI

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII LHRC WATAWASILISHA:

Mada: HAKI NA WAJIBU WA RAIA KATIKA KUSHIRIKI MCHAKATO WA KUPATA KATIBA MPYA NCHINI

Lini: Jumatano Tarehe 22 Juni, 2011

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo


WOTE MNAKARIBISHWA

Simuogopi Mbunge yeyote - Makinda

SPIKA wa Bunge la Tanzania, Anne Makinda, amesema yupo tayari kuhojiwa na Kamati ya Kanuni ya Bunge, kama itamwita kutokana na hatua yake ya kumzuia Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kumuuliza swali Waziri Mkuu, Mizengo Pinda bungeni.

Katika hatua nyingine, Spika huyo mwanamke wa kwanza katika historia ya Tanzania,
amesema hamuogopi Mbunge yeyote anapokuwa anaendesha vikao vya Bunge, zaidi ya
kuwa na hofu na Mungu.

Ameyasema hayo katika viwanja vya Bunge mjini Dodoma, alipozungumza na baadhi
ya waandishi wa habari wanaoripoti habari za Bunge.

“Bado sijaitwa na Kamati ya Kanuni ya Bunge, nikiitwa ingawa mimi ndiye Mwenyekiti, nitajiweka pembeni na Naibu wangu, halafu wajumbe wa Kamati watachagua Mwenyekiti wa kuendesha kikao kitakachonihoji, ili mradi uamuzi huo ufanywe na zaidi ya asilimia 50 ya wajumbe wa Kamati,” alisema Spika Makinda.

Alisema, hadi sasa bado hajaarifiwa na Katibu wa Bunge, Thomas Kashilila, kama
Chadema wamewasilisha barua ya kutaka ahojiwe kwa hatua yake hiyo, kama
walivyoeleza kwa vyombo vya habari.

“Kanuni ya 5 kifungu kidogo cha 4 cha kanuni za Bunge, kinasema Mbunge
asiporidhishwa na jambo lolote kutoka kwa Spika, anaweza kuandika barua ya
kupinga kwa Katibu wa Bunge, ili hatua zingine zichukuliwe ikiwa ni pamoja
na hii ya kutumia Kamati ya Kanuni ya Bunge ili kumhoji Spika.

“Lakini kuhusu hili la Chadema, sijaambiwa, nikiambiwa nitatii kanuni za Bunge
nitaiachia Kamati ifanye kazi yake na mimi na Naibu wangu ambao kimsingi ndiyo
Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti, tutakaa pembeni ili mjumbe mwingine aendeshe
kikao hicho.

“Baadaye uamuzi wa Kamati utaletwa kwangu Spika na nitautangaza mbele ya Bunge
kwa namna uamuzi utakavyochukuliwa na Kamati ya Kanuni,” alisema Makinda.

Akizungumzia mazingira anayokumbana nayo anapoendesha vikao hivyo, alisema:

“Unapokaa katika kiti kile unaongozwa na Mungu na si watu kama inavyodhaniwa,
kabla hujakaa ni lazima umwombe Mungu, vinginevyo unaweza kuharibikiwa, maana
Bunge si chombo cha mchezo.”

Alisema, ni kutokana na kuzingatia kanuni na haki, Bunge la Tanzania limeshinda
katika tathmini iliyofanywa kwa mabunge ya Jumuiya ya Madola, kwa kuendeshwa
kwa uwazi na kuzingatia haki kwa pande husika.

Hivi karibuni, Chadema walieleza msimamo wao wa kumshitaki Spika Makinda kwa
Kamati ya Kanuni ya Bunge, baada ya kumzuia Lissu kumwuliza swali Waziri Mkuu, kuhusiana na mauaji yanayofanywa na polisi katika mgodi wa dhahabu wa North Mara Barrick, Nyamongo wilayani Tarime, wakati kesi kuhusu suala hilo iko mahakamani.

Askofu Wa TAG Aiponda Bajeti Ya Serikali, Asema Haina Lengo La Kumkomboa Masikini

HUKU wabunge wa bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania hasa wa chama cha Demokrasia na maendeleo (Chadema) wakiipinga mapendekezo ya bajeti ya serikali kwwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliyowasilishwa bungeni na waziri wa fedha na uchumi Mustafa Mkulo ,askafu wa kanisa la Tanzania Assembulise Of God (TAG) jimbo la Iringa Jonas Mkane (pichani) ameipinga bajeti hiyo kuwa haijalenga kumkomboa mwananchi wa kawaida.

Pamoja na kuipinga bajeti hiyo pia askofu huyo aliitaka serikali kuwashughulikia vikali mafisadi ambao ndio wanafanya watanzania kuishi maisha magumu.

Katika mahojiano maalum na mwandishi wa habari hizi mara baada ya kufungua semina ya wachungaji wa jimbo la Iringa iliyofanyika TAG Mlandege ,askofu Mkane alisema kwa upande wake anaona kuwa bajeti hiyo haijalenga kumkomboa mwananchi wa kawaida .

Alisema kwa upande wake alifikiri kuwa kabla ya kutenga bajeti hiyo serikali inapaswa kushughulika na watu wachache ambao wamekuwa wakiichakaza nchi kwa kuendekeza ufisadi na baada ya hapo kukaa chini na kutenga bajeti ya wananchi itakayowatoa katika dimbwi laumaskini ila kuendelea kutenga bajeti hiyo na kuwakabidhi mafisadi ni kumkomoa mwananchi.

"Mimi nadhani kabla ya kutenga bajeti hiyo serikali inageanza kushughulika na watu wachache ambao wanafanya ufisadi ndani ya Taifa ambao wanafahamika soma zaidi

Monday, June 20, 2011

TAHLISO yatoa tamko kuhusu UDOM

UMOJA wa Vyuo Vikuu Tanzania (TAHLISO) umeiomba Serikali iangalie kwa kina madai ya wanafunzi wa Chuo Kikuu Dodoma (UDOM) na iyafanyie uchuguzi ili kufikia uamuzi wa msingi utakaowezesha kuwarudishwa chuoni waendelee na masomo.

Mwenyekiti wa Tahliso, Mathias Kipala ambaye pia ni Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) alisoma tamko la umoja huo baada ya kumalizika kwa mkutano mkuu wa siku mbili uliohitimishwa mwishoni mwa wiki.

Jumatano wiki iliyopita, wanafunzi 400 walipewa saa nne wawe wameondoka chuoni hapo eneo la Chimwaga, kutokana na kile kilichoelezwa ni kukithiri kwa vurugu zilizokuwa zikifanywa na wanafunzi.

Licha ya wanafunzi hao kutoka Sayansi ya Sanaa, wengine 1,000 wa Chuo cha Sayansi ya Teknolojia ya Mawasiliano (CIVE) wana zaidi ya mwezi mmoja tangu chuo chao kifungwe kwa muda usiojulikana baada ya kuibuka vurugu zilizoambatana na maandamano ya wanafunzi waliokuwa wakiwasilisha madai mbalimbali.

Katika tamko hilo, Tahliso inayoundwa na Vyuo Vikuu na Taasisi za elimu ya juu 48, imeendelea kuiomba Serikali iridhie kutoa fedha ya chakula na malazi kutoka Sh 5,000 hadi Sh 10,000 kwa wanafunzi wa elimu ya juu.

Mweyekiti huyo alisema wajumbe wa Mkutano Mkuu wameiomba Serikali na Wabunge wapitishe inayozingatia maombi hayo.

“Hapa tunatahadharisha bayana kwamba ongezeko la fedha za chakula na malazi lisije kuwa ndicho chanzo cha kuongezeka kwa karo kwa wanafunzi wa elimu ya juu katika chuo chochote kile, kiwe cha binafsi au cha Serikali…ongezeko hili lipo katika kukidhi mahitaji ya chakula na malazi yaliyopo leo,”alisema Kipala.

Wakati huo huo tamko hilo lililotolewa na TAHLISO, limepinga waraka wa serikali namba 178 unaowalazimisha wanafunzi kubadili muundo wa Serikali bila ridhaa yao ya kubadili katiba zao kama ilivyo desturi ya taasisi yoyote. Walisema hali hiyo inachangia vurugu vyuoni.

Umoja huo ulisisitiza juu ya azma ya wanafunzi wa vyuo vikuu nchini kuendelea kuungana kuhakikisha msingi wa utawala bora unadumishwa nchini.

Friday, June 17, 2011

Kikwete azipasha NGOs

RAIS Jakaya Kikwete amewashutumu watu na hasa asasi zisizo za Serikali (NGOs) kwa kukosa uzalendo na kutangaza mabaya ya nchi zao na kuacha mazuri kwa lengo la kupata ufadhili.

Amesema, mashirika hayo yanayochipuka kama uyoga, yamekuwa yakiainisha mabaya ya nchi zao kana kwamba hakuna kitu kizuri kinachofanyika nchini, huku wengine wakijifanya kutoona mazuri kwa sababu tu hawawapendi viongozi walio madarakani.

Kikwete alisema hayo juzi wakati akizungumza na mamia ya wajumbe kutoka nchi za Afrika waliohudhuria Mkutano Mkuu wa 100 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) unaohitimishwa leo jijini Geneva.

Alikuwa akijibu maswali kutoka kwa baadhi ya washiriki wa mkutano huo muda mfupi baada ya kuhutubia mkutano huo ulioshirikisha nchi 185 wanachama wa ILO.

Miongoni mwa maswali aliyoulizwa, mojawapo ni la mjumbe wa Cameroon, Bissala Isaac, aliyesema vyombo vya habari vimekuwa vikiandika mambo mabaya ya Afrika licha ya kwamba yapo maendeleo, huku viongozi wa nchi husika wakishuhudia bila kuchukua hatua.

Akimjibu, Rais Kikwete alisema hilo lipo, ingawa upo wakati vitakuja kubaini kwamba Afrika haitaendelea kuwa Bara la kuandikwa habari zisizopendeza.

“Afrika si ile ya miaka 30 iliyopita. Angalia nchi zetu; mfano Tanzania, tulikuwa na wahitimu wa chuo kikuu 12, lakini sasa tunazungumzia watu 124,000 wanaosomea shahada vyuo vikuu,” alisema.

Rais ambaye alitumia mifano ya Tanzania kuelezea suala hilo lakini bila
kutaja ama aina ya mashirika au watu wanaofanya hivyo, alisema tatizo
lililopo ni kuangalia mambo kwa kuzingatia NGOs zinazochipuka kutoka Ulaya, zenye mtazamo hasi kwa yanayofanywa na Serikali zao, wakilenga kupata misaada.

Akiendelea kutoa mfano wa maendeleo katika Tanzania, Rais Kikwete alisema, “tulitegemea wahandisi watatu … hadi sasa bado tuna tatizo hilo? Ni kilometa ngapi za barabara za lami tunazo? Wakati ule hazikufika hata kilometa 100 lakini sasa tunazungumzia kilometa zipatazo 7,000.

“Kwa kuwa mwanaharakati mmoja kapigwa na polisi, basi suala hilo linafanywa kuwa la kitaifa. Wanachojaribu kufanya ni kusema mabaya ili wafadhili wawape fedha, ukisema mazuri hupati,” alisema na kuendelea kushangiliwa.

Umati uliendelea kumshangilia kwa kupiga makofi zaidi aliposema, “uzalendo katika nchi zetu unapaswa ujengwe miongoni mwa wananchi. Si kusema mabaya pekee ya nchi. Hebu jaribu kumsema vibaya Obama (Barack-Rais wa Marekani) usikie; magazeti yote na hata yale ya kihafidhina yatakuandama. Lakini kwa Afrika, wanajivunia kusema mabaya”.

Wakati huo huo, Rais Kikwete alisema ipo changamoto kubwa ya kuwa kiongozi katika nchi masikini.

Akijibu swali la mjumbe kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambaye pamoja na mambo mengine, alihoji sababu za viongozi wa Afrika kutoweka mikakati ya uwekezaji, Rais Kikwete alisema ingawa binafsi anataka nchi ikue kiviwanda, vipo vikwazo pia.

Kwa mujibu wake, suala si kwamba hakuna malighafi, isipokuwa uwekezaji mkubwa unahitaji fedha nyingi. Alisema nchini hakuna benki za mitaji na matokeo yake, chache zilizopo ni za biashara hali ambayo inakwaza juhudi za kuhamasisha maendeleo ya viwanda.

Hata hivyo, alizihimiza nchi za Afrika kuwa kinachohitajika ni kuunganisha raslimali na kusaidiana. Alisema ana matarajio makubwa, kwamba katika miongo miwili ijayo, watakaokuwapo, watashuhudia mabadiliko makubwa barani.

Katika hatua nyingine, Rais alipokuwa akihutubia mkutano wa ILO, pamoja na mambo mengine, alisema panahitajika ushirikiano wa Serikali, jamii ya
wafanyabiashara, asasi za kijamii na wabia wa maendeleo kuhakikisha kasi ya
kutengeneza ajira katika nchi zinazoendelea inaongezwa.

Alisema tatizo la ajira linawakumba zaidi vijana katika nchi zinazoendelea na nyingi
zinazotolewa chini ya sekta binafsi hazikidhi mahitaji ya kazi za staha. Alisema wengi wanaingia kwenye sekta binafsi si kwa kuichagua, bali kujikimu.

Suala la posho linakuzwa bure - Pinda

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema suala la posho za vikao hasa kwa wabunge limekuzwa kuliko ukubwa wa jambo lenyewe.

Pinda amebainisha kuwa, zipo baadhi ya posho ambazo haziwezi kutenguliwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria, ikiwamo posho hiyo ya Mbunge hadi sheria na Katiba vitakaporekebishwa.

Pia amewataka wabunge wawe wakweli kuhusu suala la kutaka kufutwa kwa posho zao za vikao, kwa kuwa pamoja na kupewa fedha hizo, bado hazitoshelezi mahitaji na majukumu mengi yanayomkabili Mbunge, jambo ambalo linawafanya wengine kuendelea kukopa.

Amelieleza Bunge mjini Dodoma kuwa, pamoja na kwamba jambo hilo linazungumzwa sana na kushikiliwa kidedea na Mbunge wa Kigoma Kaskazini Kabwe Zitto (Chadema), anafahamu kuwa wapo baadhi ya wabunge wa chama hicho ambao bado wanazimezea mate posho hizo za vikao.

Pinda alikuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mnyaa (CUF)
aliyetaka kujua Serikali ina tamko gani kuhusu posho za vikao, suala ambalo baadhi ya wabunge wamekuwa wakilijadili na kutoa matamko yao dhidi yake na kusababisha kujenga fitna na kadhia kwa wabunge wengine kutoka kwa wananchi wao.

“Katiba Ibara ya 73, inazungumzia masharti ya kazi ya wabunge, kwamba watashika madaraka yao na watalipwa mishahara, posho na malipo mengine kwa mujibu wa kanuni na kwamba kila mbunge ana wajibu wa kufuata sheria hiyo.

“Sasa hivi karibuni kumeibuka kadhia iliyoanzia kwa baadhi ya wabunge na vyombo vya habari na kusababisha fitna na wananchi wetu, naomba jibu mheshimiwa Waziri Mkuu,” alisema Mnyaa.

Waziri Mkuu, alikiri kuwa stahili za wabunge zipo kwa mujibu wa Katiba na Sheria nyingine zilizotungwa na Bunge.

Alianisha kuwa, zipo posho ambazo Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha hana mamlaka ya kuzirekebisha, kwa kuwa zipo kwa mujibu wa Katiba na Sheria, hivyo ili zibadilike, Katiba na Sheria hizo hazina budi kubadilishwa pia.

Lakini pia alisema zipo posho ambazo Katibu Mkuu ana mamlaka ya kuzirekebisha kwa jinsi anavyoona inafaa. “Katika kundi la posho za kwanza ambazo hadi sheria zirekebishwe wapo pia madiwani ambao hawana malipo ya aina yoyote zaidi ya posho ambazo ndizo zinazowawezesha kutimiza majukumu yao, hivyo mnapozungumzia posho mtambue kuwa kuna madiwani,” alihadharisha.

Alitolea mfano pia posho wanazopewa polisi, za chakula, kuwa huo ni utaratibu uliopo ndani ya Jeshi la Polisi ambao hauwezi kubadilishwa, kwa kuwa upo kwa ajili ya kumwezesha askari atimize majukumu yake.

“Jamani tuangalie na posho zenyewe tunazozingumzia, mfano makatibu wakuu wakati wa maandalizi ya Bajeti wamekuwa wakikesha, mimi nikikesha hadi asubuhi sawa, lakini sheria hizi zimeona ni vizuri watu wa aina hii kuwapa motisha, si dhambi hata kidogo kuwapa posho.

“Najua kumekuwa na maneno mengi kama vile kuna jambo kubwa, nashangaa suala hili
lilivyokuzwa, lakini liko wazi kabisa ni masuala ya sheria, Katiba na utaratibu tu wa kufuatwa, kwani hata Spika wa Bunge akitaka kuongeza posho za vikao za wabunge hulazimika kwanza kumwandikia Rais kuomba kibali, huyu mbunge mnayempigia kelele posho hizo hata wakati mwingine hatumii mwenyewe,” alisema Pinda.

Alisema hakuna Mbunge asiyefahamu kadhia wanayoipata ya kushikwa mashati na
kuombwa fedha kila kukicha, hali inayowafanya fedha wanazopata kutowatosheleza na ndiyo maana posho hizo za vikao zinazolalamikiwa na kukuzwa, zimewekwa kwa ajili ya kuwasaidia wabunge hao kutimiza wajibu wao.

Aliongeza kuwa, tamko la Serikali ni kuziangalia fedha hizo namna zilivyowekwa ili angalau zihuishwe na hata ikibidi kuziweka kwenye mishahara ya watumishi wakiwamo wabunge.

Akijibu swali la nyongeza la Mnyaa aliyetaka kujua ni hatua zipi Serikali
inawachukulia wabunge ambao wamekiuka Katiba na Sheria zilizowekwa kwa kukataa
posho hizo za vikao, Pinda alisema hakuna sababu ya kuwachukulia hatua kwa kuwa Zitto si mbunge wa kwanza kutaka fedha zake za posho zitumike katika matumizi mengine na kwamba hakuna mbunge anayekatazwa kuiandikia Hazina kuwa fedha zake za posho ziingizwe katika mipango ya maendeleo.

“Hofu yangu ni kukuzwa sana kwa jambo hili na ninajua hata wabunge wa Chadema
wanazimezea mate fedha hizi za posho za vikao, ila hawana cha kufanya,” alisema
Pinda na kushangiliwa.

Juzi Bajeti Mbadala ya Kambi ya Upinzani iliyosomwa na Naibu Waziri Kivuli wa Fedha na baadaye Waziri Kivuli Zitto, ilibainisha dhamira ya kufuta posho zote za vikao kwa watumishi wa umma wakiwamo wabunge, jambo lililozua mjadala.

Thursday, June 16, 2011

Rushwa bado ni tatizo kubwa nchini

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Utawala Bora , Mathias Chikawe amekiri kuwa tatizo la rushwa limeendelea kuwa kubwa nchini na mbinu za kutenda makosa hayo zinabadilika siku hadi siku.

Kutokana na hali hiyo, Chikawe amewataka wadau wa rushwa nchini kubuni mikakati shirikishi na endelevu ya kukabiliana na adui huyo mkubwa wa maendeleo na ambaye anazifinyanga haki za wanyonge katika jamii.

Alitoa mfano kuwa, wakati wa uchaguzi mkuu, wanasiasa walilazimika kutoa rushwa kutokana na kulazimishwa na wapiga kura kupewa rushwa ili wawachague.

“Katika mchakato wa uchaguzi mkuu uliopita mwaka jana kwa mfano haikuwa wagombea ndiyo waliowashawishi wapiga kura kupokea rushwa bali ilikuwa ni kinyume chake,” alisema Chikawe wakati akizindua kongamano la rushwa lililoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Waziri huyo pia aliwataka viongozi wote katika maeneo yao ya kazi kusimamamia utawala bora na kuhakikisha maadili ya kazi yanafuatwa.

“Kwa kufanya hivi naamini tutapunguza kwa kiasi kikubwa kero ya rushwa katika maeneo yetu ya kazi,” alisema Chikawe.

Pia alitoa mwito kwa viongozi wote wa jamii wakiwemo viongozi wa dini na wanasiasa kukemea rushwa na vitendo vya ufisadi kila wanapopata nafasi ya kuzungumza na wananchi.

Chikawe alisema, jitihada za wadau ni lazima zilenge kuwafikisha wananchi katika kuuona ukweli kwamba rushwa ni adui wa haki na kikwazo cha maendeleo na ni chimbuko la dhuluma na umaskini kwa Mtanzania.

Balozi wa Norway nchini Ingunn Klepsvik alisema, rushwa bado ni tatizo la kidunia na kwa hapa Tanzania imechangia kukithiri kwa umasikini. Alisema Norway itaendelea kushirikiana na Serikali katika kupambana na rushwa nchini.

Mwakilishi mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Phillipe Poinsot alisema, ofisi yake itaendelea kusaidia katika mapambano dhidi ya rushwa na wamekuwa wakitoa mafunzo kwa watendaji wa Taasisi ya Kupamba na Kuzuia Rushwa (Takukuru) na kuwajengea uwezo wa namna ya kufanya kazi zao za kupambana na rushwa.

Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hosea alisema, kauli mbiu ya kongamano la mwaka huu ni ‘Kila sekta kujitafakari na kuchukua hatua madhubuti dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma’.

Alisema, washiriki 200 kutoka sekta zote ambazo takukuru imekuwa inashirikiana nao katika utekelezaji wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kuzuia na Kupambana na Rushwa (UNCAC) wamealikwa kwenye kongamano hilo. Mada 17 ziliwasilishwa kwenye kongamano hilo

Bajeti ya Upinzani yaizidi ya Serikali

KAMBI ya Upinzani Bungeni imewasilisha Bajeti mbadala ya mwaka 2011/12 ya Sh. trilioni 14.16, huku ikipendekeza mchakato uanze ili kila Mtanzania awe anajaza fomu za kodi kila mwaka, kwa sababu kuna wengi ambao wanapata mapato makubwa lakini hawalipi kodi.

Hata hivyo, bajeti hiyo mbadala kwa kiasi kikubwa, imebeba mambo mengi ambayo yamependekezwa na Serikali katika Bajeti ya Mwaka 2011/12 na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 - 2015/16). Bajeti ya Serikali ni ya Sh Trilioni 13.52.

Akiwasilisha bajeti hiyo jana, Waziri Kivuli wa Fedha, Kabwe Zitto, alitoa mfano wa watu wasiolipa kodi, akisema wenye nyumba za kupangisha mijini, wanapata fedha nyingi na wengine hutoza kodi ya pango kwa kutumia dola za Marekani, lakini hawalipi kodi ya mapato.

“Watu hawa hutumia barabara na huduma nyingine za umma ambazo gharama zake zinatokana na kodi lakini hawalipi kodi. Kambi ya Upinzani inapendekeza kuanzishwa kwa Mamlaka ya Udhibiti Majengo (RERA) na kila mwenye nyumba ya kupangisha atambuliwe na kulipa kodi inavyostahili,” alisema Zitto.

Kuhusu kurekebisha kodi, alisema wanapendekeza ushuru wa bidhaa kwenye bidhaa za mafuta upunguzwe kwa asilimia 40 na tozo nyingine zote kwenye mafuta zipunguzwe kwa asilimia kama hiyo pia.

Aidha, walipendekeza kufuta msamaha wa kodi kwenye mafuta kwa kampuni za madini na kampuni za ujenzi, kwani imethibitika kuwa msahama huo unasababisha upotevu mkubwa wa fedha za umma.

Zitto alisema pia wanapinga mapendekezo ya sasa ya kuondoa msamaha wa kodi ya mafuta kwa kampuni za utafutaji wa mafuta na gesi.

“Kambi ya Upinzani inapendekeza pia kuwianisha viwango vya bei ya mafuta ya taa na ya mafuta ya dizeli na petroli, ili kudhibiti uchakachuaji wa mafuta ambao unaligharimu Taifa fedha nyingi na kuleta uharibifu mkubwa,” alisema Mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini kupitia Chadema na Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni.

Eneo lingine walilopendekeza wapinzani ni marekebisho ya kushusha kiwango cha chini cha Kodi ya Lipa kwa Kadri Unavyopata (PAYE) mpaka asilimia 90 na kiwango cha juu mpaka asilimia 27.

Kuhusu ada za leseni za biashara, Zitto alisema wanataka kurejeshwa kwa leseni za biashara ndogo licha ya kuongeza mapato ya halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji, ambako kutarejesha ugumu wa kufanya biashara; hivyo kushauri uamuzi huo uangaliwe upya.

Alipendekeza magogo yote yanayosafirishwa nje ya nchi yalipiwe kodi, huku ikiipongeza Serikali kwa kukubali wazo la kupunguza misamaha ya kodi mpaka kufikia asilimia moja ya Pato la Taifa.

Katika umeme, alisema umefika wakati sasa kutangaza kuwa umeme ni janga la Taifa na Bunge lipitishe Azimio la Uzalishaji wa Umeme kwa viwango vya Mpango wa Maendeleo na kuweka adhabu ya kumfukuza kazi Waziri iwapo miradi hiyo haitakuwa imekamilika kila mwaka.

Kuhusu posho, alisema Kambi ya Upinzani inapendekeza mfumo mzima wa kulipana posho za vikao katika utumishi wa umma uondoke, na kwamba hawapingi posho za kujikimu ambazo viongozi au maofisa wa umma hulipwa wanaposafiri nje ya vituo vyao vya kazi.

“Posho hizi zirekebishwe kuendana na gharama za maisha za sasa. Lakini posho za vikao zifutwe mara moja. Ili kuonesha kuwa viongozi wa kisiasa tunaelewa kilio cha wananchi kuhusu gharama za maisha na kupunguza matumizi ya Serikali, waheshimiwa Wabunge tunaanza na posho za vikao vya Bunge.

“Iwapo sisi tukiendelea kujilipa posho za kukaa humu ndani na kwenye kamati zetu, tunakuwa tunatoa ruhusa kwa watumishi wa Serikali kulipana posho hizi na hatutakuwa na mamlaka ya kuhoji na kuwawajibisha,” alisema Zitto.

Akizungumzia Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), alipendekeza irudi tena katika biashara, huku akishauri Serikali iangalie uwezekano wa kurekebisha umiliki wake kwa kuhusisha taasisi za umma ambazo zinafaidika kwa kuwapo shirika hilo moja kwa moja.

“Kambi ya Upinzani Bungeni inapendekeza ufanyike uchunguzi maalumu kwenye Deni la Taifa ili Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) atwambie madeni haya tunayokopa kwa kasi ya namna hii, tunayapeleka kwenye miradi gani na namna gani tunaweza kudhibiti Deni la Taifa,” alisema Zitto akizungumzia deni hilo ambalo sasa ni dola za Marekani bilioni 11.4.

Katika vipaumbele vya Bajeti, wapinzani wanapendekeza kuondolewa kwa ‘mashangingi’ ya mawaziri na badala yake wakopeshwe magari; kufutwa kwa ada za shule kwa wanafunzi wa kutwa, kuongeza kima cha chini cha mshahara wa mtumishi wa umma hadi Sh 315,000.

Zitto alimpongeza Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, kwa kusikiliza maoni yao kwa baadhi ya mambo na kuyazingatia katika bajeti yake, hivyo kuonesha umma moja ya faida ya mfumo wa vyama vingi.

“Tunatarajia kuwa Serikali itaendelea kusikiliza maoni yetu na kuyafanyia kazi. Changamoto hii ni kwa uzito ule ule pia, ipo kwetu sisi wa Kambi ya Upinzani kusikiliza pia maoni ya Serikali,” alisema.

Wanafunzi 400 watimuliwa UDOM

WANAFUNZI 400 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) jana walipewa saa nne waondoke chuoni hapo kutokana na kukithiri kwa vurugu zilizokuwa wakizifanya.

Uamuzi wa uongozi kukifunga chuo hicho na kuamuru wanafunzi kuondoka eneo la chuo, utawafanya wanafunzi hao kukosa masomo kwa kipindi kisichojulikana kuanzia jana.

Makamu Mkuu wa UDOM, Profesa Idris Kikula, alisema jana kuwa, uamuzi wa kukifunga chuo hicho una lengo la kuepusha baadhi ya wanafunzi na majanga yanayoweza kujitokeza kutokana na baadhi yao kukaidi amri ya kusimamisha mgomo wao.

“Tumefunga chuo na tumewapa muda wa saa nne wawe wameondoka chuoni hapa kuanzia saa tatu asubuhi,” alisema Profesa Kikula.

Akifafanua juu ya uamuzi huo, Makamu Mkuu huyo wa Chuo, alisema wanafunzi wa mwaka wa pili na wa tatu ambao wanachukua kozi ya Sayansi ya Jamii, waliitisha mgomo tangu Jumatatu kwa lengo la kuilazimisha Serikali kuwapa posho za mazoezi kwa vitendo.

“Uongozi wa Chuo umeshangazwa na hatua hii, kwani suala hilo lilishajadiliwa tangu Desemba mwaka jana na kupatiwa ufumbuzi kuwa Serikali itatoa posho hizo kwa muda muafaka na mimi niliongea nao wakakubali kuwa hakuna haja ya kufanya mgomo,” alisema.

Profesa Kikula alifafanua kuwa wanafunzi wanatakiwa waende kwenye mafunzo kwa vitendo katikati ya mwezi ujao, hivyo kwa sasa ni mapema kuilazimisha Serikali kuwapa posho hizo.

Alisema kutokana na uamuzi wa wanafunzi kuandamana kinyume cha sheria Jumatatu hadi kwenye majengo ya Bunge, baadhi yao walikamatwa na uongozi wa chuo ulikubaliana kuwapa barua za kuwasimamisha masomo wanafunzi 400 ambao walishiriki maandamano hayo.

“Habari za kusimamisha wanafunzi hao 400 zilisababisha taharuki miongoni mwa wenzao wakaanza kushambulia kwa mawe magari ya chuo na kuwapiga wanafunzi wengine ambao walionekana hawaungi mkono,” alisema.

Katika hatua nyingine, Profesa Kikula alisema kuanzia leo, uongozi wa chuo utachapisha katika tovuti yake majina ya awamu ya kwanza ya ambao watatakiwa kurudi chuoni.

“Kuna wanafunzi wengi tumewasimamisha, lakini hawana hatia, na baadhi yao walisaini makubaliano kuwa hawatashiriki mgomo, lakini hatukuwa na namna zaidi ya kuwasimamisha wote kutokana na hali ilivyokuwa,” alisema.

Baadhi ya wanafunzi ambao walizungumza na gazeti hili muda mfupi kabla ya kuondoka chuoni hapo, walilaani uamuzi huo na kutaka uongozi uwarudishe haraka masomoni.

“Si haki kutoa adhabu hii kwa watu wote; viongozi wa mgomo wanajulikana, ni vyema uongozi wa chuo ungechukua hatua za kinidhamu dhidi yao,” alisema mwanafunzi ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Wanafunzi hao walikuwa wakidai kuwa walipewa ahadi tangu Februari ya kulipwa posho hizo Juni 7, lakini haikutekelezwa.

Rais wa Wanafunzi wa Chuo cha Sanaa na Lugha, Mwakibinga Phillipo, alisema chuo hicho kimefungwa kutokana na wanafunzi wake kushiriki maandamano juzi wakishinikiza wanafunzi wenzao waliosimamishwa chuo kurudishwa bila masharti.

Philipo alisema, wanafunzi 374 wanasomea Uhusiano wa Kimataifa mwaka wa pili, na wengine 59 ni wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii na ndio walisimamishwa juzi na kusababisha wenzao kuandamana wakiwatetea.

Alisema, katika maandamano yao ya mwanzoni mwa wiki kupitia viwanja vya Nyerere hadi vya Bunge walikokutana na ulinzi mkali wa Polisi, wanafunzi 71 walikamatwa na na kuachiwa kwa dhamana iliyotolewa na Makamu Mkuu wa Chuo.

Wednesday, June 15, 2011

Makinda- Bungeni si sokoni, tunatia aibu

SPIKA wa Bunge la Tanzania, Anne Makinda, amewatolea uvivu wabunge na kuwaeleza kuwa wanajidharaulisha na kukigeuza chombo hicho cha kutunga sheria kuwa kama eneo la sokoni Kariakoo, Dar es Salaam.

Amesema utaratibu wa baadhi ya wabunge kusimama wakati wa vikao vya Bunge na kupaza sauti ya ‘Mwongozo au Utaratibu’, haupendezi na wabunge wanapaswa kurudi kwenye mstari.

Spika Makinda alisema hayo jana bungeni wakati akizungumzia matukio yaliyotokea juzi jioni wakati wa mjadala wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambapo wakati Bunge lilipokaa kama Kamati ya Matumizi, kulikuwa na kukatishana kuzungumza kwa wabunge kwa kutumia kauli za ‘Mwongozo na Utaratibu’.

Wakati huo, Bunge lilikuwa likiongozwa na mmoja wa wenyeviti wa Bunge, George Simbachawene, Mbunge wa Kibakwe (CCM). “Kuhusu hili la ‘Utaratibu na Mwongozo’, kwa kweli sasa tunatia aibu. Waheshimiwa mnajidharau, yaani imekuwa kelele, huku Mwongozo, mara kuhusu Utaratibu, tumegeuka kama watu wa Kariakoo!

“Naomba sana, tunasikilizwa na wananchi, tusikilizane, watu wana hamu sana ya kutazama Bunge … mimi jana nilikuwa natazama kwenye televisheni, lakini sikuona hamu ya kutazama. Naomba sana, sana, tufuate utaratibu,” alisema Spika Makinda.

Alisema, kutokana na hali hiyo ya pengine wabunge kutofahamu vizuri kanuni, kutakuwa na semina kuhusu upitishaji wa vifungu wakati wa mijadala ya Bajeti ambayo inaanza leo kwa Bajeti ya Serikali.

Spika Makinda alifikia hatua ya kuwatolea uvivu wabunge hao, baada ya Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema), kusimama na kutaka mwongozo wake juu ya jibu alilopewa wakati wa kipindi cha maswali.

Makinda alimsifu kiongozi huyo wa Upinzani Bungeni kwa kutafsiri vyema kanuni kwa kuomba mwongozo kwa wakati unaostahili.

“Alichofanya Mbowe ni sahihi kabisa … unasubiri suala linafika mwisho, yaani hadi kitendo kinakamilika, ndio unaomba mwongozo. Si katikati, unasimama na kudai mwongozo, mara mwingine huku kuhusu utaratibu uliovunjwa … hatueleweki wabunge,” alisema Makinda.

Baadaye akifafanua kauli yake kuhusu Kariakoo, Makinda aliomba radhi kwa wakazi na wafanyabiashara wa Kariakoo kuwa hakumaanisha vibaya kutumia neno hilo, ila maana yake ilikuwa ni kwa vile eneo hilo kuna soko kuu, hivyo watu huzungumza bila mpangilio, tofauti na bungeni ambako kuna utaratibu.

“Kariakoo ni sokoni kila mtu anazungumza anavyotaka na hakuna wa kuwazuia, lakini hapa ndani kuna utaratibu si sokoni,” alisema Makinda.

Hii ni mara ya pili kwa Spika Makinda kuonya wabunge kwani hata mkutano uliopita, baadhi ya wabunge walisahau kanuni na kuanza kupiga kelele hadi mwingine akasema “mlango ufungwe tupigane”.

Tuesday, June 14, 2011

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO WIKI HII 15/6/2011

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII Deus Kibamba na Gloria Shechambo WATAWASILISHA:

Mada: KATIBA NA ELIMU, JE BAJETI YA 2011/12 INASEMAJE?

Lini: Jumatano Tarehe 15 Juni, 2011

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo

WOTE MNAKARIBISHWA

RAI YA JENERALI: Hatari ya vurugu inatoka kwa watawala, Slaa asiwape kisingizio



KATIKA kipindi hiki tunapoikazania Serikali ya Rais Jakaya Kikwete isifanye mchezo na suala la Katiba, tunalo jukumu la kutuliza akili zetu na kupima kwa kina kila tunachokisema na kukiandika.

Nasema haya kwa sababu naona kama tunalo tatizo linalotokana na Serikali yetu kuonekana kama vile haina msimamo kuhusu suala hili kubwa na zito. Hakuna dalili za wazi zinazoonyesha kwamba Baraza la Mawaziri limeketi na kulijadili kwa undani na kupata msimamo wa pamoja, na wala hakuna dalili kwamba mkuu wa Serikali hiyo, Rais Kikwete amewapa watu wake maagizo kuhusu nini wafanya na nini waseme kuhusu mada hii ya Katiba.

Kinachojitokeza ni taswira ya kuparaganyika kwa mawazo na kutokuelewana miongoni mwa wale wanaotarajiwa kutuongoza. Kwa bahati mbaya, ingawaje sasa naamini watakuwa wamegundua kwamba walichokifikiria kuwa kitu rahisi, ni kigumu kweli kweli na wanatakiwa wajiandae kukishughulikia kwa umakini mkubwa kuliko huo walioudhihirisha hadi sasa.

Ningependa nirejee jambo ambalo nimekuwa nikilishadidia kwa muda mrefu kidogo: Suala la Katiba mpya limeshika kasi isiyokuwa ya kawaida, na wala haliwezi kuondoka kirahisi. Linahitaji kufanyiwa kazi itakayowaridhisha wananchi, na hiyo kazi haiwezekani ikafanyika ila kwa kuwahusisha wananchi kwa kiwango kikubwa kinachowezekana.

Ukweli ni kwamba, hata kama hatukuwa tumezowea hili, hivi sasa wananchi wanataka mabadiliko makubwa katika maisha yao, na wanataka kuanza na Katiba watakayoiandaa wenyewe.

Ni kwa nini wananchi wamefikia kiwango hiki cha utashi, mimi binafsi sina jibu la haraka, na kila mtu anaweza kuwa na maoni yake. Lakini naamini kwamba wananchi wengi wameanza kung’amua kwamba mambo hayaendi kama ambavyo yanatakiwa yaende.

Wanayaona maisha yao yakiwa hayana matarajio tena. wanaona hali zao za kiuchumi na kijamii zikizidi kuzorota. Wanaona maisha bora waliyoahidiwa kama ni mzaha wamechezewa. Wanawaona watawala wao kama waongo na wanafiki, wasiojali, wala rushwa na wauza nchi. Hawaamini lo lote linalosemwa na watawala kwani wamekwisha kudanganywa mara nyingi.

Sasa wamehamanika na wanataka mabadiliko, tena wanataka mabadiliko makubwa.

Nimekuwa nikifuatilia kwa kiasi fulani maandamano na mikutano ya viongozi wa CHADEMA katika mikoa ya Kusini, na nimekuwa nikiangalia maelfu ya watu wanaoshiriki katika maandamano hayo na mikutano hiyo. Ningekuwa mtawala ningeshitushwa na mikusanyiko ile kwa sababu ningetambua kwamba inabeba ujumbe mzito kwangu.

Ujumbe unaotoka katika maandamano yale na mikutano ile ni kwamba wananchi wamechoka. Ukiona kaumu ya watu kama tuliyoiona katika miji midogo na ya ‘pembezoni’ kama Sumbawanga wanaandamana na kukaa mkutanoni wakisikiliza kama watotot wa shule wanavyokaa darasani kumsikiliza mwalimu, unajua kwamba kuna kitu kimebadilika katika jamii ya Watanzania.

Lakini papo hapo ningependa kutoa angalizo. Kama nilivyowahi kuandika huko nyuma, hii si mara ya kwanza tunashuhudia hamaniko la aina hii la kutaka mabadiliko. Nimeandika kwamba tuliwahi kuona, hapa nchini, hamasa walizozua wanasiasa kama Chistopher Mtikila na Augustine Mrema wakati ule. Watu wengi waliwachukulia hawa kama wakombozi wao. Baadaye bila shaka walikuja kugundua kwamba matumaini yao yalikuwa yamegonga mwamba.

Lakini shauku ikiisha kujengeka kwamba hali iliyopo haifai na ni lazima ibadilike, shauku hiyo haiishi kwa sababu manabii waliotarajiwa kufanya kazi ya ukombozi wamedondoka kando ya njia, bali shauku hiyo huhamishwa na jukumu la ukombozi likatafutiwa manabii wengine. Na kwetu ndivyo ilivyokuwa.

Kikwete alipoingia madarakani mwaka 2005 shauku hiyo ilikuwa imehamishiwa kwake. Bila shaka mwenyewe atakuwa anakumbuka kwamba ilifika mahali wakati wa kampeni ndani ya CCM ikasemwa kwamba hata kama CCM wasingemchagua yeye kuwa mgombea, angepata kuwa rais kwa kupitia chama kingine cho chote. Hayo yalisemwa na wana CCM na wanachama wa vyama vya upinzani pia.

Hili nalisisistiza kwa makusudi mazima: Hizi ni dalili za kuhamanika na kukata tamaa kwa Watanzania wengi. Na hali hii imekuwapo kwa muda mrefu toka utawala wa Rais Ali Hassan Mwinyi hadi ule wa Rais Benjamin Mkapa. Sasa inajirudia katika utawala wa Rais Jakaya Kikwete.

Wananchi wengi wanaona mkombozi wao mpya, nabii wao mpya, ni CHADEMA. Wanachosema katika lugha ya miili yao ambayo naiona kupitia televesheni na kupitia magazeti, ni kwamba wakipata fursa ya kupiga kura na uchaguzi ukawa “huru na wa haki” wanaweza (na uwezekano huo ni mkubwa) watapiga kura kuichagua CHADEMA.

Sasa, kama tunavyojua, uchaguzi mwingine ni mwaka 2015. Bado tunayo miaka minne hadi tupate fursa nyingine ya kupiga kura. Ni vyema kwa wale wanaotaka kufanya mabadiliko katika utawala wa nchi hii kwa njia mbali mbali wakautumia muda uliosalia kujiandaa kwa ajili ya uchaguzi huo, na wale wanaotaka kuiondoa CCM madarakani wafanye kampeni ya nguvu ya kuwahamasisha wapiga kura kimawazo lakini pia na kuwahamasisha wajitokeza siku ya kupiga kura ili watimize azima yao.

Ndiyo maana nilijikuta nikiwa na wasiwasi (wiki chache zilizopita) nilipomsikia Katibu Mkuu wa CHADEMA, Willbrod Slaa akizungumza kama vile anao mpango wa kufanya mabadiliko anayotaka kuyafanya kabla ya uchaguzi ujao. Aliposema kwamba kuiondoa serikali ya Kikwete kabla ya 2015 hautakuwa uhaini anaweza kuwa anasema kweli, kwani uwezekano huo upo.

Kwa mfano Bunge linaweza, katika mazingira mahsusi yaliyoainishwa na Katiba, likamshitaki Rais kwa kosa la kuidhalilisha Ofisi yake, na kama akikutwa na hatia likamvua madaraka. Hiyo imeandikwa katika Katiba tuliyo nayo hivi sasa, na wala halina haja ya kusubiri Katiba mpya. Ndiyo maana nasema kwamba anachosema Slaa ni cha kweli kwa maana ya vifungu vya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano kama ilivyo leo.

Kinachonitia hofu ni kwamba napata hisia kwamba Slaa hakujikita katika vifungu vya Katiba, angalau maelezo niliyoyasoma hayakusema hivyo, jambo ambalo linaweza kuzaa tafsiri kwamba njia mojawapo inayofikiriwa ni kuung’oa utawala wa Kikwete kwa maandamano, kama ilivyokuwa Medani Tahrir.

Kama hivyo ndivyo alivyokusudia kusema Slaa, kuna tatizo. Tatizo hilo, kwa mtazamo wangu, linakuwa kubwa zaidi kwa kuangalia matukio ya siku hizi chache zilizopita.

Tatizo lenyewe si kwamba haiwezekani kuung’oa utawala uliopo kupitia maandamano na bado kitendo cha kuung’oa kikawa si uhaini. Nchi nyingi zimeshuhudia hilo likifanyika, ikiwa ni pamoja na Indonesia, Philippines, Georgia na sasa Tunisia na Misri. Kilichotokea katika nchi hizo ni mapinduzi ya umma uliosimama na kusema “Utawala huu sasa basi!” Ni mantiki ya mapinduzi kama hayo kwamba yanapofanikiwa walioyaongoza wanakwenda moja kwa moja Ikulu, lakini wakishindwa wanatiwa kitanzi.

Ni kwa jinsi hii akina Fidel Castro (Cuba) na Nelson Mandela (Afrika Kusini) walikwenda jela lakini hatimaye waliingia madarakani, lakini Pierre Mulele (Kongo) na Mahjoub (Sudan) walitiwa kitanzi.

Naamini kwamba Katibu Mkuu wa CHADEMA alitaka kupeleka ujumbe mzito kwa wakuu wa nchi, lakini kila siku ujumbe unaohusu mambo kama haya hauna budi uandaliwe kwa uangalifu na weledi mkubwa ili usije ukazaa tafsiri zaidi ya moja.

Ingekuwa vyema kama Slaa angeonyesha subira katika matamko yake. Hivi sasa watu wengi wanamwangalia kama “rais mtarajiwa.” Angechukua muda kujiandaa kwa umakini mkubwa, hasa wa kuyasoma matatizo ya nchi yetu na kufikiria njia mbali mbali za kuyakabili kuanzia na hili la Katiba ambalo sasa naamini kwamba iwapo atachaguliwa kuwa rais mwaka 2015 ( na nasema hili linawezekana kabisa), atalikuta bado lipo kwa sababu sioni dhamira ya kweli ya kulishughulikia.

Akijipa muda wa kujifunza zaidi na kukusanya maoni, na kujenga mitandao ya utafiti itakayowahusisha wataalamu wa kumshauri na kukishauri chama chake, akichukua muda kujadili matatizo ya nchi hii na makundi mbali mbali ya kijamii katika shughuli zao mbali mbali na wakamweleza matatizo yao; naye akajadiliana nao... atakuja kugundua kwamba hakuna muda wa kutosha kwa ajili ya maandalizi hayo.

Najua mara nyingi umefanyika uchokozi dhidi ya vyama vya siasa na wanasiasa wa upinzani. Uchokozi huo unafanywa makusudi ili kipatikane kisingizio na wapinzani waweze kushutumiwa kwamba ndio waliodhamiria kuvunja “amani na utulivu” na misemo mingine ya kuchekesha ukiangalia “amani na utulivu” vinavyotawala shughuli za chama-tawala.

Kwangu ni dhahiri kwamba kama kuna ghasia kubwa zitakazotokea nchini humu, zitaanzia katika vurugu zinazoendelea ndani ya chama hicho tawala. Hata hivyo, Slaa angejiweka mbali na kila kinachoweza kumfanya yeye ama chama chake waonekane, hata kama si kweli, kwamba wao ndio wanaochochea vurugu.

Naandika haya nikijua kwamba sasa kuna hamaniko ndani ya duru za watawala, kwa sababu wanajua wamepoteza nguvu za ushawishi na wanachokiona kwamba kinaweza kuwasaidia ni ushawishi wa nguvu, kama ambavyo wanaonekana kutumia mitulinga isiyokuwa na sababu yo yote alimradi tu waonyeshe kwamba wanazo nguvu, kama vile hatujui kwamba wanazo.

Katika kutapatapa wamewaingiza na wakuu fulani wa dini ambao nao sasa wanatoa ‘onyo’ kwa CHADEMA kama vile wamegeuka kuwa idara ya usalama ya serikali au wasemaji wa Jeshi la Polisi.

Hali hii inatisha, lakini si mpya. Imetokea kila mahali utawala ulipozeeka, ukapoteza njia, ukasahau hata asili yake, ukapuyanga na kubahatisha, ukababaisha na kubangaiza, ukayumba na kutetereka, ukatekwa na waporaji, ukaendelea kujitutumua kwa kuonyesha ukali wa kijeshi kumbe ndani ya roho yake kiini chake kilikwisha kugugunwa na mapanya-buku kwa muda mrefu. Utawala kama huo unao uwezo mkubwa wa kusababisha maafa kutokana na udhaifu wake.

Slaa akae chonjo, apunguze hisia, awe m-rais (presidential). Ajifunze zaidi, kwani kama bado ana nia ya kuwania urais mwaka 2015, kazi iliyo mbele yake ni kubwa. Akumbuke tu kwamba, Rais Jakaya Kikwete alikuwa na (angalau) miaka kumi ya kujiandaa kuwa rais, na hii kumi ni ile tunayoijua sisi.

Hata baada ya muda huo wa miaka kumi kupita, na hata baada ya miaka mitano ya kuendesha Serikali, inaelekea bado hajajifunza mambo mengi ya msingi kabisa yanayohusu uongozi na utawala. Slaa afanye hadhari, asije akawa vivyo hivyo.