Monday, January 30, 2012

Mama aliridhia mtoto akeketwe ili atambae

MTOTO mwenye umri wa mwaka mmoja (jina tunalo) anateseka katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC ya mjini hapa, baada ya kukeketwa kwa ridhaa ya mama yake mzazi.

Mama wa mtoto huyo, Magdalena Julius (19), amekiri kufanya kitendo hicho, akisema alimpeleka mwanawe kwa mganga wa kienyeji ili akeketwe kutokana na kuchelewa kutambaa na pia kuwa na afya isiyoridhisha.

Hata hivyo, tofauti na matarajio yake, mara baada ya kukeketwa hali ya mtoto huyo ilibadilika na kuwa mbaya zaidi kutokana na kuvuja damu nyingi.

Bibi wa mtoto huyo, Rehema Taraa ndiye aliyegundua tukio la kukeketwa kwa mjukuu wake kutokana na mtoto huyo kulia usiku kucha na ilipofika asubuhi, alimpeleka Hospitali ya Wilaya ya Hai na madaktari kubaini mtoto alikuwa ameishiwa damu na maji mwili, hivyo kutakiwa amhamishie Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi.

Akisimulia, bibi huyo alisema madaktari wa Hospitali ya Mawenzi walimpokea, lakini wakashauri apelekwe KCMC kutokana na hali ya mtoto kuzidi kuwa mbaya.

“Huko ndiko walikothibitisha kuwa amekeketwa na kwamba alidhoofika kutokana na kuvuja damu nyingi. Aliongezewa maji na damu ili kunusuru maisha yake.”

Naye Mratibu wa mtandao wa kupiga vita ukeketaji kwa wanawake na watoto wa kike (AFGEM), Honoratha Raymond, naye alizungumzia kitendo hicho, akilaani na kuiomba Serikali kwa kushirikiana na wadau kuvalia njuga unyanyasaji wa kijinsia hasa kwa watoto ambao bado hawana uwezo kiakili wa kujitetea.

Ingawa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Absalom Mwakyoma hakupatikana kuzungumzia suala hilo, lakini tayari mama wa mtoto huyo amewekwa chini ya ulinzi wa Polisi, huku akiendelea kumuuguza mwanawe.

www.habarileo.co.tz

Madaktari rudini kazini - Pinda aagiza

SERIKALI imewaagiza madaktari wote walio katika mgomo kurejea kazini leo asubuhi na asiyeripoti atakuwa amepoteza ajira serikalini.

Uamuzi huo wa Serikali umetolewa jana jijini Dar es Salaam na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, katika mkutano na waandishi wa habari katika viwanja vya Karimjee baada ya madaktari hao kususa kukutana naye kuzungumzia malalamiko yao.

Pinda pia amewaagiza wakuu wa mikoa, wilaya na waganga wakuu katika hospitali zote nchini kukagua watumishi wao leo na asiyekuwepo kazini jina lake lipelekwe ashughulikiwe.

Alisema Serikali tayari imechukua tahadhari ya kukabiliana na hali hiyo kwa kuagiza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kupeleka madaktari kutoka katika Majeshi ya Ulinzi na Usalama katika hospitali za mkoa wa Dar es Salaam, ili kusaidia wagonjwa walioko hospitalini.
Waziri Mkuu pia ameagiza vyombo vya dola kuzuia mikutano yoyote ya madaktari hao inayoendelea jijini Dar es Salaam.

Wamegoma suluhu

Pinda alisema katika hatua iliyofikiwa, Serikali imetambua kwamba madaktari wanaongozwa na Kamati ya Mpito, hawataki suluhu kwa kuwa imefanya juhudi za kuwaita kwa kuwabembeleza ili kujadili na kushughulikia madai yao bila mafanikio. Alisema baada ya kuwabembeleza kwa muda mrefu ili kupata suluhu ya tatizo hilo bila mafanikio, wameona wasiendelee na mgogoro na kuonekana Serikali haina maana kwani watu wanaumia na madaktari hawataki mazungumzo.

Pinda amekiri kuwa atakabiliwa na changamoto, lakini akasema bora kushughulikia changamoto hiyo mpya kuliko kuendelea na iliyopo sasa. Alisema mbali na kuomba madaktari kutoka jeshini, Serikali pia imewaoamba madaktari wenye utu na ubinadamu kuendelea kutoa huduma wakati jitihada za kuwatafuta madaktari wengine katika taasisi binafsi zikiendelea.


Madai yao kushughulikiwa

Alisisitiza kuwa licha ya uamuzi huo, amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia kuendelea kushughulikia malalamiko ya madaktari hao na kwa yale yanayowezekana yaingizwe kwenye bajeti ijayo ili kuwasaidia watakaokuwepo kazini.

“Madaktari hawa wamefanya kinyume kwa mujibu wa kiapo na sheria za nchi zinazowaagiza wazi kutojihusisha na migomo, hususani katika sekta yao ambayo inahusu uhai wa binadamu kwa kuwa husababisha kupoteza maisha bila sababu,” alisema.

Mikoa 14, wilayani shwari

Waziri Mkuu alisema tangu mgomo uanze, Serikali imekuwa ikifuatilia kutoka katika mikoa yote na hadi kufikia juzi, katika mikoa 14 hospitali za mikoa na za wilaya hazikuwa na mgomo.
Mikoa hiyo ni Ruvuma, Lindi, Mtwara, Shinyanga, Arusha, Tabora, Kagera, Iringa, Mara, Pwani, Kigoma, Singida, Manyara na Rukwa.

Alisema katika mikoa saba, baadhi ya hospitali za mikoa zilikuwa katika mgomo huku hospitali za wilaya zote za mikoa hiyo, zikiendelea kutoa huduma kama kawaida. Mkoani Kilimanjaro Pinda alisema mgomo ulikuwepo katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC ambao ulihusu madaktari waliopo katika mafunzo kwa vitendo.

Mbeya Pinda alisema mgomo ulikuwa kwa madaktari 65 walioko katika mafunzo kwa vitendo, madaktari kumi waliosajiliwa na madaktari bingwa kumi. Hospitali nyingine zilizogoma ni za Mkoa wa Mwanza ambako hata hivyo hakukuwa na mgomo wa wazi licha ya madaktari 46 wa Hospitali ya Rufaa ya Bugando kutoa tangazo la wazi la kushiriki mgomo, lakini dalili za mgomo zikionekana kwa waliopo katika mafunzo ya vitendo.

Alisema Morogoro waligoma madaktari katika Hospitali ya Mkoa wakati Tanga watumishi wote wa kada zote katika Hospitali ya Mkoa ya Bombo walikuwa na mgomo wa chini chini na Dodoma katika Hospitali ya Mkoa na Dar es Salaam mgomo huo ulipoanzia.

Mshahara na mlolongo wa posho wanazodai

Pinda alisema katika barua ya madaktari hao ya Januari 27 mwaka huu kwake, walitoa madai nane wakitaka mshahara wa daktari anayeanza kazi kuwa Sh milioni 3.5 kwa mwezi.
Kwa sasa katika madai hayo walidai wanalipwa Sh 700,000 lakini Pinda alisema wanalipwa Sh 957,700 na ndio wanaoongoza kwa malipo mazuri katika sekta ya umma. Wanaofuata kwa mujibu wa Pinda ni wahandisi Sh 600,000 na wahasibu kati ya Sh 300,000 hadi Sh 400,000.

“Uamuzi wa kuwawekea mshahara mkubwa madaktari ni wa makusudi kwa kutambua umuhimu wao katika kubeba maisha ya watu, inawezekana haitoshi lakini nyongeza ya posho kwa asilimia mia na ishirini hakuna Serikali inayoweza kuongeza,” alisema.

Mbali na mshahara huo, madaktari hao kwa mujibu wa Pinda, wamependekeza kulipwa posho ya kulala kazini ya asilimia 10 ya mshahara wa mwezi. Kwa sasa wanalipwa Sh 10,000 kwa siku. Pia wametaka posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi asilimia 30 ya mshahara wa mwezi na posho ya nyumba asilimia 30 ya mshahara au wapewe nyumba.

Madaktari hao pia wamependekeza walipwe posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu iwe asilimia 40 ya mshahara na posho ya usafiri asilimia 10 ya mshahara au ikishindikana wakopeshwe magari. Baada ya mlolongo huo wa posho, madaktari hao ndio wakaweka pendekezo la kutaka madaktari waliokuwa katika mafunzo ya vitendo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, warejeshwe mafunzoni hospitalini hapo.

Kipato cha Sh milioni 17

Pinda alisema kwa mujibu wa mapendekezo ya madaktari hao, akilipa mshahara wa Sh milioni 3.5 kwa mwezi na posho hizo, daktari anayeanza kazi atalipwa Sh milioni 7.7 kwa mwezi na Daktari Mshauri Mwandamizi atalipwa milioni 17.2 kwa mwezi.

Alisisitiza kuwa ili kutekeleza pendekezo hilo, Serikali italazimika kurekebisha viwango vya mishahara kwa watumishi wote wa kada ya afya na nyingine, ili kuweka uwiano kufuatana na muundo katika utumishi wa umma. “Kwa kuzingatia ukubwa wa gharama hizi, utekelezaji wa mapendekezo ya madaktari utakuwa hauwezekani kwa kuzingatia hali halisi ya bajeti ya Serikali,” alisema Pinda.

Alisisitiza kuwa madai yao ni sawa na nyongeza ya Sh bilioni 301.7 katika bajeti ya mshahara ya mwaka 2011/ 2012 ukijumlisha na nyongeza ya posho kwa watumishi wengine wa kada ya afya kwa miezi mitano iliyobaki, watapaswa kulipwa posho ya Sh bilioni 84.3.

Pinda alisema katika makundi hayo mawili tu; mishahara na posho Serikali itajikuta ikitoa Sh trilioni 2, ambayo ni zaidi ya theluthi mbili ya mishahara ya wafanyakazi wote serikalini ambayo kwa sasa ni Sh trilioni 3.45. Kwa maana hiyo, Pinda alisema madaktari wanataka wapewe theluthi mbili za mishahara ya wafanyakazi wote na waliobakia, wagawane theluthi moja iliyobakia jambo ambalo haliwezekani.

Thursday, January 26, 2012

Madaktari bingwa nao wagoma

MADAKTARI bingwa wasiopungua 12 wa idara mbalimbali za Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) jijini Dar es Salaam wanadaiwa kuwa katika mgomo baridi kwa siku kadhaa sasa, kupinga kuhamishiwa mikoani.

Aidha, Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Dar es Salaam nayo imekumbwa na tatizo kama hilo kutokana na madaktari wake kutotibu wagonjwa, kuanzia Jumatatu, bila kueleza sababu.

Hali hiyo, imeelezwa kuzorotesha kwa kiasi kikubwa utoaji huduma katika hospitali hizo, kiasi cha kuathiri wagonjwa kisaikolojia, kwa hofu kuhusu uhai wao.

Habari kutoka kwa wauguzi, madaktari walioajiriwa kwa mkataba waliomba kutotajwa gazetini na baadhi ya ndugu wa wagonjwa katika hospitali hizo, zilisema madaktari bingwa hao hawajawaeleza chochote kuhusu matibabu yao, licha ya kuonekana hospitalini wakati wote.

Walisema kwa nyakati tofauti, kuwa walitangaziwa kuwa madaktari walikuwa na dharura yenye umuhimu wa juu na hivyo kuombwa warejee nyumbani kusubiri siku nyingine, kwa kuwa wasingewahudumia wakati huo.

Ocean Road tangazo hilo linadaiwa kutolewa na muuguzi wa kike ambaye jina lake halikuweza kujulikana, baada ya wagonjwa siku hiyo kuhudumiwa.

Muhimbili, wagonjwa waliokuwa wakisubiri upasuaji Ijumaa walidai kutangaziwa kuwa waendelee kula kama kawaida kwa kuwa operesheni zao ziliahirishwa kwa muda, bila kupewa maelezo ya ziada.

“Mara ya mwisho kuzungumza na daktari ilikuwa Alhamisi ambapo tuliandaliwa kwa kupewa namba na mashuka na kuelezwa kuwa tusile chakula kwa sababu upasuaji ni asubuhi, cha kushangaza, hakuna kilichoendelea kuhusu operesheni hadi daktari aliyepita kuruhusu wenye nafuu jana kutueleza kuwa tuendelee kula tu.”

Pamoja na maelezo hayo, gazeti hili lilishuhudia MNH ikiwa katika ukimya usio wa kawaida kuanzia jana asubuhi hadi saa 8 huku baadhi ya madaktari walio katika mafunzo wakiwa wamesimama katika makundi kwenye korido lililopo kati ya wadi za Mwaisela na Sewahaji, wakizungumza mambo yao.

Wauguzi waliozungumza na gazeti hili walisema hali si nzuri sana, kwa sababu huduma zinazohitaji wataalamu (mabingwa) zimesimama.

"Kama unavyotuona tunawajibika katika nafasi zetu, tatizo lipo kwa baadhi ya madaktari, huduma zilizo ndani ya uwezo wetu zinaendelea, kwenye upasuaji na tiba nyingine ndio kuna tabu,” alisema muuguzi mmoja na kuungwa mkono na mwenzake wa wadi nyingine, aliyedai kuwa wagonjwa wengi wamekata tamaa ya kutibiwa.

Dodoma nako Naye Sifa Lubasi, anaripoti kutoka Dodoma, kwamba madaktari, wauguzi, wafamasia na watumishi wengine wa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma wameanza mgomo kushinikiza kupatiwa mazingira bora ya kazi na kutaka Waziri wa Afya kujiuzulu.

Huduma zinazoendelea katika hospitali hiyo ni za dharura tu. Kwa hali hiyo, katika hospitali hiyo wameiomba Serikali kusikiliza kilio chao ili kuendelea kutoa huduma za afya kama kawaida.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kuratibu Madai ya Watumishi hao, Dk. Yahya Magaso alisema zaidi ya watumishi 100 wa hospitali hiyo wameingia kwenye mgomo wakiwamo madaktari kuishinikiza Serikali kupitia Wizara ya Afya kusikiliza madai yao na kuyafanyia kazi.

Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dk. Godfrey Mtei alisema uongozi umekaa na kuwashauri waendele na kazi, lakini hata hivyo alisema bado hawajafikia muafaka na majadiliano bado yanaendelea.

Aliyemlawiti mtoto kwenye choo cha Msikiti jela miaka 30

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Dodoma jana ilimhukumu kifungo cha miaka 30 jela mhudumu wa usafi wa Msikiti wa Masjid Ghazal, Bashiri Hassan (36), baada ya kukiri mashitaka ya kumlawiti mvulana wa miaka 11 katika choo cha Msikiti huo.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Adrian Kilimi, baada ya kumtia hatiani mshitakiwa kutokana na kukiri mashitaka.

Kabla ya adhabu hiyo kutolewa, Wakili wa Serikali Godfrey Wambali aliomba Mahakama itoe adhabu kali kwa mshitakiwa kwa kuwa kosa alilofanya ni la kufedhehesha jamii na halifai katika maisha ya binadamu.

Alipopewa fursa ya kujitetea, mshitakiwa alidai hana la kusema na yote anamuachia Mungu ili amtetee; “Namwachia Mungu ili anitetee.”

Akitoa adhabu hiyo Hakimu Kilimi alisema kitendo alichofanya mshtakiwa ni kibaya lakini hata hivyo hakuisumbua Mahakama kuingia gharama kuendesha kesi hiyo na kuepusha muda wa Mahakama kupotea.

Alisema kwa kuwa mshitakiwa amekiri mashitaka, Mahakama inampa adhabu ya kutumikia kifungo cha miaka 30 gerezani, ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.

Awali, ilidaiwa kuwa mshitakiwa ambaye ni mkazi wa Bahi Road, alimlawiti mvulana mwenye umri wa miaka 11 baada ya kumuingiza kwenye choo cha Msikiti huo upande wa wanawake.

Tukio hilo linadaiwa kutokea Januari 23, mwaka huu majira ya jioni.

Wednesday, January 25, 2012

Kamati ya Bunge yaagiza wananchi wapunguziwe gharama za umeme

Na Patricia Kimelemeta

KAMATI ya Hesabu za Mashirika ya Umma(POAC) imelitaka Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma zinazothibitiwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Madini (Ewura -CCC), kuangalia namna ya kupunguza makali ya bei ya umeme kwa wananchi na si vinginevyo.

Agizo hilo la POAC limekuja kipindi ambacho wananchi wengi wamekuwa wakilalamikia ongezeko la bei ya umeme kwa asilimia 40.29 viwango vipya vya bei ya umeme vilivyotangazwa na Ewura na kuanza kutumika Januari 15 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Deo Filikunjombe alisema baraza hilo linapaswa kuangalia hali halisi ya Watanzania, kabla ya kuunga mkono ongezeko la bei hiyo, jambo ambalo lingeweza kuwasaidia wananchi wa kawaida.

“Ewura –CCC liko kwa ajili ya kutetea maslahi ya Ewura, na si kubariki ongezeko la umeme ambalo limesababisha wananchi kulalamika, kutokana na hali hiyo tumelitaka baraza hilo kujiendesha kwa utaratibu wake kuliko kubebwa na Ewura,”alisema Filikunjombe.

Aliongeza kwamba hadi sasa baraza hilo linadhaminiwa na Ewura katika shughuli zake zote zikiwamo malipo, jambo ambalo limesababisha kushindwa kutoa hoja yoyote ya kimaslahi yanayohusu wananchi.

Filikunjombe alisema kutokana na hali hiyo tutaiomba Serikali kurekebisha sheria ili baraza hilo liweze kufanya kazi bila ya kushirikiana na Ewura.

Alisema kutokana na hali hiyo wamelitaka baraza hilo kufanya kazi bila ya kufungamana na upande wowote ili liweze kutenda haki kwa wananchi pindi Ewura na Serikali wanapopanga kuongeza bei ya umeme.

Kwa mujibu wa Filikuonjombe,mbali na suala hilo, kamati hiyo imewaagiza watendaji wake kutumia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya katika matibabu ili kupunguza kutumia gharama kubwa wakati wa matibabu.

Awali, Serikali ilitoa Sh200 bilioni kwa ajili ya kununua umeme, ambazo ni sawa na asilimia 60 ya umeme, huku Tanesco ikichangia asilimia 40 akisema kama ingeshindwa kutoa kiasi hicho, gharama za umeme zingekuwa kubwa kuliko zilizotangazwa hivi karibuni. 



Viwango vipya Katika ongezeko hilo la bei ya umeme ambalo limeanza kutumika Januari 15 mwaka huu, wateja wa hali ya chini wanaotumia chini ya uniti 50 kwa mwezi, wataendelea kulipa Sh60 kwa uniti wakati watumiaji wa majumbani wanaotumia zaidi ya uniti 50, bei hiyo imepanda kutoka Sh195 hadi Sh273 kwa uniti.

Watumiaji wa kawaida wakiwamo wenye biashara ndogondogo, bei imepanda kutoka Sh157 hadi Sh221 kwa uniti wakati watumiaji umeme mkubwa wa kati, bei imepanda kutoka Sh94 hadi Sh132 kwa uniti, wakati watumiaji umeme mkubwa hasa wenye viwanda na migodi, bei imepanda kutoka Sh84 hadi Sh118 kwa uniti.


Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco), litauziwa umeme kwa Sh106 kwa uniti kutoka Sh83 ikiwa ni ongezeko la asilimia 28.21.

Tuesday, January 24, 2012

KUSHUKA KWA THAMANI YA SHILINGI, MFUMUKO WA BEI NA HALI NGUMU YA MAISHA NINI ATHARI ZAKE KWA WANAWAKE NA MAKUNDI YALIYOKO PEMBEZONI?


SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII KYWDP WATAWASILISHA:

MADA: KUSHUKA KWA THAMANI YA SHILINGI, MFUMUKO WA BEI NA HALI NGUMU YA MAISHA NINI ATHARI ZAKE KWA WANAWAKE NA MAKUNDI YALIYOKO PEMBEZONI?

Lini: Jumatano Tarehe 25 Januari, 2012

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni

WOTE MNAKARIBISHWA

UWT- Tutahamasisha wanawake wachaguliwe 2015

KATIBU Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Amina Makilagi amesema watashiriki kikamilifu kuhamasisha wajumbe na wanachama kuchagua viongozi wanawake wanaofaa katika uchaguzi mkuu wa 2015.

Alisema hayo juzi jioni wakati wa mahojiano na gazeti hili mara baada ya kumalizika kwa kikao kazi cha siku mbili kilichohusisha makatibu wa UWT wa mikoa na wilaya kutoka mikoa na wilaya za Tanzania Bara.

Viongozi 152 walihudhuria mafunzo hayo mjini Dodoma ikiwa ni sehemu ya mafunzo kuelekea uchaguzi wa ndani ya CCM na jumuiya zake.

“UWT bado ni imara tutashiriki kikamilifu kuhamasisha wajumbe wanawake kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi,” alisema.

Alisema kuwa UWT wana msimamo tangu wakati wa Chama cha TANU na imeendelea kuwa na viongozi waaminifu na waadilifu wanaozingatia kanuni za chama.

“Hatuwezi kuingia kwenye makundi au kuingizwa kwenye makundi, wanatuogopa kutokana na msimamo wetu ndiyo maana unaona siku zote kwenye chama chetu tuko shwari,” alisema.

Makilagi alisema kuwa baada ya mafunzo hayo watakwenda kuhamasisha wenzao hata katika suala la mchakato wa kupata Katiba mpya ili Tume
ikifika, watoe maoni yao ili ipatikane Katiba mpya inayoendana na wakati wa sasa.

“Bunge lililomalizika Novemba mwaka jana lilifanya vizuri kupitisha Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba mpya ni vyema tukatumia nafasi hiyo vizuri.

“Tupiganie chama chetu na tupiganie haki za wanawake kuanzia ngazi ya shina hadi mkoa. Yote mliyojifunza kwa lengo la kuongeza uwezo muyazingatie ili kuboresha kazi za chama,” alisema na kuongeza kuwa wako tayari kulima hata kwa jembe la mkono ili kufanikisha sera.

Aita wake zake wawili , amuua mmoja kwa kisu

MKAZI wa Kijiji cha Busilima wilayani Musoma Vijijini katika Mkoa wa Mara, Anna Mfungo (26) ameuawa kwa kuchomwa kisu shingoni na mume wake, Shukrani Shaban (32) baada ya kudai kuwa ameoteshwa atapelekwa Polisi.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Robert Boaz alisema Shaban alimuua mkewe Jumamosi iliyopita saa 7 usiku baada ya mtuhumiwa huyo kutoka kwenye ulevi.

Kwa mujibu wa madai ya Kamanda Boaz, Shaban alipofika nyumbani kwake usiku huo, aliwaamsha wake zake wote pamoja na kijana mmoja ambaye alikuwa anaishi naye na kuwaambia aliota kuwa atapelekwa Polisi.

“Mtuhumiwa ni mvuvi na anafanya kazi zake huko Busekela na anakaa hata siku tatu ndipo anarudi nyumbani.

“Anapokuwa nyumbani akitoka kwenye ulevi anawaamsha wake zake wote wawili, wanamletea chakula na akimaliza ndipo wanapotawanyike na kwenda kulala,” alidai Kamanda Boaz.

Alidai kuwa Jumamosi iliyopita, ilikuwa zamu ya mke mkubwa na mtuhumiwa aliporudi kwenye ulevi kama kawaida yake aliwaamsha pamoja na mke kijana ambaye alikuwa anaishi naye na kuwaambia kuwa alikuwa ameota atapelekwa Polisi na kisha kuchukua kisu na kumchoma shingoni mwanamke huyo,” alidai Kamanda Boaz.

Alidai kuwa baada ya kutenda kosa hilo, kijana huyo alikimbia na kutoka nje kuomba msaada lakini watu walipofika, mtuhumiwa alikuwa tayari ameshatoroka na jitihada za kumtafuta zinaendelea.

Wakati huo huo mtoto Emmanuel Joseph (5), alikufa baada ya kamba waliyokuwa wakiitumia kama bembea kumkaba shingoni na kumsababishia kifo.

Kamanda Boaz alisema kuwa ajali hiyo lilitokea Jumapili iliyopita katika Kijiji cha Kabainja wilayani Bunda ambapo Emmanuel na watoto wenzake walikuwa wakibembea.

Monday, January 23, 2012

Hamad Rashid, Kafulila kususwa bungeni

VYAMA vya CUF na NCCR-Mageuzi, vimeamuru wabunge wake kuwasusa wabunge waliovuliwa uanachama pamoja na Mahakama kuzuia uamuzi wa vyama hivyo kwa muda na kutoa fursa kwa wabunge hao kuendelea na kazi yao ya uwakilishi.

CUF ilimvua uanachama Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed lakini Mahakama ikatoa amri ya kuzuia uamuzi huo na kesi ipo mahakamani kuhusu hatima ya mbunge huyo.

NCCR Mageuzi nayo mwishoni mwa mwaka jana, ilimvua uanachama Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye naye alikwenda mahakamani kupinga uamuzi wa chama chake na hivyo kuruhusiwa kuendelea na wadhifa wake.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro katika mazungumzo yake na gazeti hili wiki hii, alisema wabunge wa chama hicho wataendesha mgomo baridi kwa kumsusia Mbunge wa Wawi, Hamad na mambo yake yote hadi atakaposalimu amri mwenyewe.

“CUF hakina ugomvi na Mahakama wala Bunge kwa sababu kilitekeleza matakwa ya Katiba yake ambayo haimzungumzii mbunge bali mwanachama. Kwa maana hiyo, tuliyemwadhibu kwa kumvua uanachama ni Hamad Rashid kama mwanachama na wala sio Mbunge wa Wawi.

“Ubunge wake ni yeye na Bunge na wala chama hakihusiki naye. Akifanya mikutano ataifanya kama ya Hamad sio ya CUF kwa sababu hakuna kiongozi wa CUF atakayekubali kumwandalia mikutano wala ziara kwa sasa kwa kuwa tayari anahesabika kuwa mwasi aliyefukuzwa katika chama,” alisema Mtatiro.

Mtatiro alisisitiza hata wabunge aliowaita halali wa CUF walioko bungeni hawatampa ushirikiano pia.

Hata hivyo Kiongozi wa wabunge wa CUF bungeni na Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Mnyaa alikataa kuzungumzia mkakati wa kumsusa Hamad kwa madai kwamba suala linapokuwa mahakamani, halipaswi kuzungumzwa.

Naye Msemaji wa NCCR Mageuzi na Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali alisema hata kama Mahakama itampa ushindi Kafulila katika kesi iliyopo mahakamani, chama hicho kitaendelea kumtenga na kutompa ushirikiano wa aina yoyote.

“Huyo sio Mbunge sasa tutahitaji kuwa na uhusiano gani wa kibunge huko bungeni? Mimi na NCCR tunamchukulia kama Mtanzania wa kawaida aitwaye David Kafulila,” alisema Machali.
Alionya kuwa NCCR Mageuzi haitahusika na shughuli zote zinazofanywa na Mbunge huyo kwa niaba ya chama ikiwa ni pamoja na kutishia kumfikisha mahakamani kwa kukaidi ukweli kuwa sio mwanachama wa chama hicho.

“Hatutaki atuwakilishe katika jambo lolote na tukimkamata anafanya shughuli za chama tutamchukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kumfikisha mahakamani kwa kuwa kwa sasa yeye ni mwananchi wa kawaida asiye na chama,” alisema Machali.

Naye Kafulila alisema; “naheshimu Mahakama. Siendekezi malumbano. Mimi ni Mbunge na Mjumbe wa Kamati Kuu ya NCCR-Taifa. Sitaki kuzungumza sana, nachapa kazi ili nilete maendeleo kwa walionichagua na taifa. Nawajibika, situkani na sitamtukana mtu wala chama.”

Alidai hata shughuli zote alizozifanya ziliandaliwa na viongozi wa juu wa chama hicho na kwamba hata siku moja hafanyi mambo yahusuyo chama chake bila kushirikishwa.

“Sasa ilikuwaje hawakunikamata nilipofanya ziara na mikutano hivi karibuni baada ya uamuzi wao? Nilizuru kata za Mtego wa Noti, Nguruka, Uvinza, Ilagala, Kazulanimba, Ilalangulu na nyinginezo kwa maandalizi ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Taifa; Stephen Mapunda na Kayombo Kabutali. Wanataka nihitaji ushirikiano gani tena kutoka kwa chama?” Alisema Kafulila.

Hamad kwa upande wake alidai kuwa ataweza yote kwa ushirikiano na wananchi waliomchagua na wala sio viongozi wanaofanya mambo kwa kushinikizwa na kukiuka katika ya chama husika.

“Wananchi walionipeleka bungeni ndio wanaonisapoti na wala sitishiki kwa kutoungwa mkono na viongozi madikteta wa CUF. Wanavunja sheria kwa maneno yao na vitendo visivyozingatia haki lakini mimi nasonga mbele kwa nguvu ya wananchi wangu,” alidai.
,isema hakuna mwenye haki ya kumzuia kuendesha mikutano kwa sababu kama Mbunge anayo nafasi yake ya kufanya shughuli hizo.

Friday, January 20, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ongezeko la bei ya umeme kuongeza makali ya ugumu wa maisha kwa Watanzania masikini!

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), tumekuwa tukifuatilia kwa karibu masuala yanayogusa jamii hapa nchini ikiwa ni sehemu ya kudai mabadiliko ya mfumo wa uchumi, sera, sheria na bajeti katika kampeni yetu ya kudai haki ya uchumi, na hasa ajira na maisha endelevu kwa wote. Lengo ni kuhakikisha mgawanyo sawa wa rasilimali za taifa kwa manufaa ya wananchi wote wanawake, wanaume, wazee, watoto, watu wanaoishi na ulemavu, hususani wale walioko pembezoni.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini (Ewura), Haruna Masebu ametangaza kupanda kwa bei ya umeme kwa asilimia 40.29 kuanzia Januari 15 mwaka huu. Alisema ongezeko hilo halitawahusu wateja wa hali ya chini, wanaotumia chini ya uniti 50 kwa mwezi pamoja na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO)

Swali la kujiuliza ni akina nani hawa wanaotumia umeme chini ya uniti 50 katika hali halisi ya maisha ya Mtanzania wa kawaida? Ni mara chache sana kupata watu wanaoangukia kwenye kundi hili, lakini pia kupanda kwa bei ya umeme hata kwa wale ambao hawatumii umeme mwingi kutawaathiri kwani kunapandisha gharama ya vitu vingine vingi ambavyo kila mtu anatumia.

Wananchi ambao kipato chao kinategemea sana umeme kama vile biashara ya samaki, saluni, kuuza barafu, na vinywaji kama maziwa, juice na soda wataathirika kwa kiasi kikubwa kwa ongezeko hilo. Pamoja na watumiaji wa umeme kuwa wachache, kupanda kwa umeme kuna athari kwa watumiao na wale wasiyotumia, gharama za uzalishaji zitapanda juu, na walaji wote maskini na matajiri watahitajika kufidia wazalishaji.

Tumeambiwa watumiaji wa umeme wa majumbani wanaotumia zaidi ya uniti 50 watalipa shilingi 273. Kundi la wafanyabiashara wadogo wadogo bei imepanda kutoka Shilingi 157 hadi Sh 221 kwa uniti, watumiaji umeme kiwango cha kati, bei imepanda kutoka Sh 94 hadi Sh 132 kwa uniti. Watumiaji umeme mkubwa hasa wenye viwanda na migodi, bei imepanda kutoka Sh 84 hadi Sh 118 kwa uniti na malipo ya huduma kwa kundi hili ni shilingi 14,233 kwa mwezi . ZECO wamepandishiwa kwa asilimia 28.21 kutoka awali ambako, walikuwa wakilipa Sh 83 na sasa watalipa Sh 106 kwa uniti.

Kwa kipindi kirefu sasa Watanzania tumekumbana na hali ngumu ya maisha kutokana na kushuka kwa thamani ya shilingi ya Kitanzania dhidi ya dola ya Kimarekani. Kutokana na takwimu za Shirika la Taifa la Takwimu (National Bureau of Statistic Office ) zinaonesha kupanda kwa mfumko wa bei kwa asilimia 5.6 % (2010), asilimia 8.6 % (hadi Aprili 2011), asilimia 19.2% (Novemba 2011). Mfumko wa bei ulipanda hadi kufikia asilimia 19.8% (Desemba 2011). Hii imepelekea kuendelea kupanda kwa bei ya vyakula na bidhaa muhimu mfano sembe, mchele, maharage, sukari, mafuta ya taa, dizeli na petroli. Vile vile, taifa linapita katika kipindi kigumu kiuchumi kutokana na kukosekana kwa rasilimali muhimu na za msingi kwa jamii kama maji, miundombinu ya usafiri, mafuta, umeme na nyinginezo kwa kipindi kirefu

Pia takwimu za Shirika la Taifa la Takwimu (National Bureau of Statistics) za mwaka 2007, kuhusu utafiti katika kaya kuona idadi ya watu wanaotumia umeme ilikuwa : mwaka 1991/92 asilimia 9 %, mwaka 2000/1 asilimia 12%, hadi kufikia mwaka 2007 ilikuwa asilimia 13% ambayo ni sawa na watu millioni 5 (tano) tu kati ya watu millioni 39 waliotumia umeme. Matokeo haya yanaonesha Watanzania walio wengi hawatumii umeme, hata hivyo kundi hili wanapata athari kubwa kwani gharama za uzalishaji zitapanda juu sambamba na ununuzi wa bidhaa mbalimbali.

Tumeshuhudia katika Wilaya za Ilala, Kinondoni na Temeke jijini Dar es Salaam, ongezeko la bei za vyakula mfano, mfuko mmoja wa sukari wa kilo 25 unauzwa sh 80,000 kwa bei ya jumla kutoka sh 40,000 ikiwa imepanda mara dufu huku kilo moja ikiuzwa kati ya sh 2,000 hadi 2,500.

Katika masoko ya Tandika, Kariakoo na Tandale taarifa inaonyesha bei ya vyakula imepanda kwa kasi katika miezi mitatu iliyopita. Kwa sasa gunia moja la mchele linanunuliwa kati ya sh. 100,000 hadi 120,000 kutoka sh 80,000 hapo awali. Wakati kilo moja ya mchele kwa sasa ni kati ya sh. 2,000 hadi 2,500

TGNP tunahoji sababu za serikali kupandisha bei ya bidhaa muhimu kama umeme hali ikijua kabisa kuwa wananchi wengi, hasa wanawake na wanaume walioko pembezoni na wenye kipato cha chini wanazidi kunyonywa na walafi na mabepari wachache wa ndani na nje ya nchi na kupelekea wananchi masikini walio wengi kukosa maisha endelevu, kunyimwa uhuru na hata kushindwa kutumia na kufaidi rasilimali na utajiri wa nchi yao uliowazunguka, mfano madini, misitu na ardhi. Sisi kama wanaharakati na watetezi wa haki na usawa kwa wote tunapinga kabisa ongezeko la bei ya umeme, kwa sababu ongezeko hilo litaathiri sana maisha na kipato cha mwananchi masikini hasa wanawake walioko pembezoni

TGNP tunaidai serikali, kutekeleza yafuatayo ili kukabiliana na matatizo yaliyopo ikiwemo ongezeko la bei ya umeme:-

  • Kusimamia kwa makini tatizo la mfumko wa bei sambamba na ongezeko la bei ya umeme ili shughuli za uzalishaji ziendelee kwa nia ya kuwanusuru wananchi hasa kutokana na hali ngumu ya kiuchumi
  • Kuwaeleza wananchi, ni lini matatizo haya yatamalizika na mbinu mbadala za kumaliza matatizo haya na kwa kipindi gani. Pia kuwepo na mipango mikakati ya muda mfupi na mrefu kuhakikisha matatizo haya yanatatuliwa
  • Kuwawajibisha wataalamu na watendaji wa serikali wanaoshindwa kutimiza wajibu wao na kusababisha matatizo makubwa kama ya ukosefu wa umeme, maji na mfumko wa bei.
  • Kuchukua hatua za haraka za kufuatilia kwa karibu upatikanaji wa vyanzo mbadala vya umeme ikiwa ni pamoja na kuruhusu watu na makampuni binafsi kuzalisha nishati ya umeme, kama ilivyoruhusu kwa sekta zingine kumilikiwa na watu binafsi ili kuweza kuendelea kuzalisha umeme huo na kuchangia maendeleo mbalimbali ya kiuchumi nchini.
  • Serikali ihakikishe masuala ya ufisadi mfano Richmond, Dowans na mengineyo yamepatiwa ufumbuzi wa haraka na pesa zote zimerudi mikononi mwa serikali na kunufaisha Watanzania wote
  • Tunawasihi viongozi wawe na dhamira ya dhati ya kuwasaidia wananchi, na bila kuingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo hasa yanayohusu maisha na uhai wa Watanzania walio masikini .

Imetolewa na:

Mary Nsemwa
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji

Thursday, January 19, 2012

Urais umeshuka hadhi, wengine wanaiona Ikulu kama kijiwe

Rai ya Jenerali

NAFASI anayopewa mtu ndani ya jamii ili awatumikie wanajamii wenzake, kwa maana kwamba wenzake wanamuomba awatumikie, ni nafasi ya uwakilishi.

Anayepewa nafasi hiyo anakuwa katumwa kazi, amebebeshwa mzigo kwa niaba ya jamii yake kwa sababu jamii imetambua kwamba yeye anao uwezo ambao wengine hawana wa kuifanya kazi hiyo.

Katika mjumuiko wa kisiasa, kama vile chama cha kisiasa, hali ni ile ile. Nafasi ya uwakilishi hupewa mtu anayeonekana kuwa na uwezo mkubwa kuliko wenzake katika kutimiza jukumu fulani. Chama ama kundi jingine lolote lenye nia moja humteua mtu au huwateua watu kwa misingi ya jukumu lililopo wakati huo.

Majukumu hubadilika, au yakachukua sura mpya, na ikiwa hivyo basi chama pia kitabadilisha mtazamo katika uteuzi wa mwakilishi wake. Kwa mfano, tukiangalia historia ya kisiasa ya Tanganyika tutatambua kwamba Julius Nyerere, kijana kutoka shamba, mtu “wa kuja” ambaye hata Kiswahili chake hakikuwa na lafudhi ya kuvutia kwa watu wa mwambao, aliteuliwa kuwawakilisha wazalendo waliotamani kupata Uhuru, wengi wao wakiwa watu wa mwambao, kwa sababu yeye ndiye alikuwa na sifa zilizotakikana ili kumkabili mkoloni.

Nyerere alikuwa kapata elimu kubwa kuliko wenzake wengi; aliwajua Waingereza labda kuliko mwingine yeyote miongoni mwao; alikuwa na uwezo wa kujenga hoja na zikaeleweka kwa Waingereza; pia alikuwa na ujasiri wa kusema anachotaka kusema bila kumung’unya maneno. Alikuwa ndiye mtu mwafaka wa kumtuma kupeleka ujumbe kwa Waingereza.

Alikuwa na sifa nyingine pia, ambayo hatuisemi sana ingawa ni wazi kuwa ilikuwa na umuhimu wake: Alikuwa Mkristo na dola aliyotumwa kupambana nayo ilikuwa ni dola ya Wakristo. Kwa hiyo ilikuwa ni rahisi zaidi kwa wakoloni kumwamini, na hususan kwa sababu katika miaka aliyokaa nchini mwao kama mwanafunzi walikwisha kumtathmini na kumuona kama mwenzi wao ambaye asingewasababishia mashaka makubwa.

Tunaweza kufikiria mazingira mengine, na bila kwenda mbali. Kama Tanganyika ingekuwa na hali ya kisiasa iliyofanana na Kenya ya wakati ule, katikati ya uasi wa Mau Mau, na kama wazalendo wa Tanganyika wangekuwa wameamua kwamba njia pekee ya kumng’oa mkoloni ni mapambano ya kisiasa, labda wasingemteua Nyerere.

Labda wangemteua mmoja wao mwenye uwezo wa kuongoza wapiganaji wenye silaha ili ajenge jeshi la kupambana na Mwingereza, na labda kwa mantiki hiyo wangemteua Ally Sykes, aliyekuwa katoka vitani.

Pia, katika mazingira inapobidi kuchukua njia ya mapambano ya silaha, huyo ambaye angechukua nafasi ya uongozi asingeteuliwa kwa maana ya kuteuliwa kwa wengi wa wanaharakati kumkubali, au kumpigia kura. Angejitokeza tu, akasimama, akwaambia wenzake kwamba maneno yametosha na hayawapeleki kokote; sasa ni mtutu wa bunduki. Na historia ya harakati za kutafuta Uhuru ingekuwa tofauti kabisa.

Hali kama hiyo ndiyo iliyotokea Kenya. Hakuna kumbukumbu zinazoonyesha kwamba Dedan Kimathi, shujaa wa vita ya Mau Mau alichaguliwa na mkutano mkuu wa wapiganaji. Na mapema kuliko wakati huo, hatuna ushahidi wa kuonyesha kama Kinjeketile, shujaa wa vita ya Maji Maji alichaguliwa na mtu yeyote kuwa kiongozi wa harakati hizo.

Katika historia ya Kenya tunajifunza, kama nilivyosema mapema, kwamba mazingira yakibadilika na aina ya mtu anayetafutwa kuwawakilisha wenzake inabadilika. Ndiyo maana wakati Kenya inaandaliwa kupata Uhuru na wazalendo wa nchi hiyo wanatafuta kiongozi wa kupokea mikoba kutoka kwa Waingereza, hawakutafuta mpiganaji wa Mau Mau, mfuasi wa Kimathi. Walimtafuta Jomo Kenyatta, ambaye hakuwa na uhusiano na Mau Mau na alikwisha kuwakana hadharani.

Ninachosema hapa ni kwamba nchi, jamii, chama cha kisiasa au kundi lolote linalokabiliwa na changamoto katika ustawi, usalama ama maendeleo, humteua mtu, au huwateua watu wa kuwakilisha mjumuiko wao kufuatana na hali waliyo nayo, na sifa za hao wanaoteuliwa hubadilika kufuatana na mazingira ya wakati huo.

Tukirudi katika hali yetu nchini Tanzania, leo tunashuhudia kwamba wanasiasa wetu wanapigana vikumbo wakiwania kuchukua nafasi ya urais. Nimekuwa nikijiuliza, hivi hawa wanasiasa wanapendekezwa na wanajamii wenzao kwa sababu wamewaona wanazo sifa za kusaidia ama chama ama nchi katika nyanja walizozichunguza na kuzitathmini? Au ni watu wanaojipendekeza wenyewe na kukusanya mashabiki wa kuwafanyia kampeni kwa sababu tu wanakinyang’anyiro hao wana malengo wasiyoyatamka hadharani na wakipata nafasi wanayoitafuta watawagawia mashabiki wao sehemu ya ngawira watakayoiteka?

Bila shaka urais umeshuka thamani, umechuja, (wako wanaoiona Ikulu kama kijiwe) iwapo kila mtu anajiona anaweza kuwa rais, hata mbumbumbu wa kisiasa wasiojua hata historia ya chama wanachotaka kukiwakilisha, wasiojua historia ya dunia wala Afrika, wasiojua siasa ni nini mbali na kutafuta nafasi za ulaji na ufisadi.

Kwa sababu katika mlo hakuna uwakilishi, kila mtu atataka kwenda mwenyewe mezani. Haiyumkiniki kwamba watu watasema wanamwachia mmoja wao awakilishe kwenye mlo. Hicho ndicho kiini cha mapambano makali tunayoyashuhudia leo hii.

Mimi si bashiri, na wala sipigi ramli, lakini jinsi tunavyoenenda na siasa hizi bandia, watu watatoana roho, kama hawajaanza bado. Yote hii ni kwa sababu nafasi iliyokuwa ya uongozi na kazi ngumu na majukumu mazito sasa imekuwa nafasi ya kujinufaisha mtu na familia yake na watu wa karibu, ‘washikaji’ wasemavyo watu wa mjini.

Hali ya mikanganyiko iliyoikumba Tanzania hivi leo isingeweza kukupa sura ya nchi ambayo watu watauana ili wapate nafasi ya kuitumikia. Umasikini unaozidi kujichimbia nchini katikati ya utajiri wa ajabu; kukata tamaa kwa wananchi wasiouona vyema mustakabali wao kwa jinsi wanavyoendeshwa; dalili za vurugu zinazotuchungulia kama tutaendelea tulivyo; vijana waliojaa ghadhabu kwa sababu wanaona wamenyimwa haki zao za msingi; rushwa, wizi, ulaghai kila pembe…. Hii siyo hali ya kuwafanya watu wajipendekeza kuongoza. Ni hali ambayo, katika mazingira ya kawaida, ingeilazimisha jamii kuwalazimisha wanasiasa na viongozi wenye sifa, wakubali kubeba mzigo wa kuikwamua jamii, siyo wao wajipendekeze na watoane roho kwa tamaa ya kubebeshwa mizigo mizito.

Hatuleti maana, tumekiuka mantiki.

Wednesday, January 18, 2012

Sitta Aitabiria CCM Hali Ngumu

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, ametabiri kuwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, CCM itaendelea kupoteza majimbo ya ubunge, lakini akasisitiza kuwa bado itaongoza kwa idadi ya wabunge.

Alisema hayo juzi katika kipindi cha Monday Agenda kinachorushwa na kituo cha televisheni cha Capital na kufafanua kuwa ni suala la tabia ya asili ya baada ya kuanzisha mfumo wa vyama vingi, kwa chama tawala kupungukiwa wabunge.

"Ukiangalia, tangu mfumo wa vyama vingi ulipoanza, wabunge wanapungua kidogo kidogo na ndivyo mfumo ulivyo, wanatumia udhaifu kidogo uliopo chama tawala kupata viti zaidi," alisema Sitta.

Hata hivyo, alibainisha kuwa CCM bado ina viongozi, wakiwamo wabunge wengi ambao wanaheshimika na hawana upinzani katika majimbo yao, ambao wataendelea kukipa chama hicho nguvu.

"Kwa mfano, mimi katika Jimbo la Urambo Mashariki, nikiamua kugombea, waweke upinzani wasiweke nitashinda, kwa kuwa wananifahamu ni mtu wao na nimefanya mengi," alijinasibu na kuongeza kuwa viongozi wa aina yake wako wengi CCM na wataendelea kuipa nguvu.

Kuhusu urais, Sitta alisema kama CCM itakosea kuteua mgombea urais mwaka 2015, litakuwa jambo la kusikitikia nchi.

Alifafanua kuwa upo uwezekano wa kuwa na mtu ambaye ana nguvu ndani ya CCM, lakini nje anaonekana asiye na maadili na akikubalika kuwa mgombea wa chama hicho, nchi itapaswa kuonewa huruma.

"Kama wataweza kununua mfumo wa chama wa kuteua mgombea urais, litakuwa jambo la kuionea huruma nchi," alisema Sitta.

Kuhusu mvuto wa chama hicho tawala, Sitta ambaye pia ni Spika mstaafu wa Bunge, alisema umepotea kwa vijana, hasa kutokana na kukosekana kwa ajira; tatizo la kiuchumi ambalo kwa upande mmoja, halitokani na uongozi uliopo madarakani, bali hali ya kuyumba kwa uchumi wa dunia.

Sababu ya pili ya kupotea mvuto wa CCM kwa mujibu wa Sitta, ni kukosekana kwa jitihada mpya za kuzalisha ajira na kuwapo watu wanaoishi maisha mazuri kutokana na ufisadi akitoa mfano uliosababishwa na “mikataba mibovu ya bahati mbaya”.

Kuhusu umoja na mshikamano wa wana CCM, Sitta alisema haupo hasa kwa viongozi wa ngazi za juu na kuongeza kuwa ni jambo la kawaida katika vyama vya siasa.

Kwa mujibu wa Sitta, sababu ni kuibuka kwa makundi mawili; la kwanza la viongozi wasiopenda mabadiliko, wanaoweka maslahi binafsi mbele na kuamini kuwa chama kinachotawala hakina tatizo.

Kundi la pili alisema, ni la wanaoona kuwa chama kinapoteza mwelekeo, kimeacha kufuata falsafa za waasisi wa chama hicho akiwamo, Mwalimu Julius Nyerere.

Alisema katika msuguano wa makundi hayo mawili, lazima kundi kubwa liwe la wanaotetea mwonekano mzuri wa chama kwa wananchi na kuonya; "kama chama hakitafanya yale kinachoyaamini basi kutakuwa na ombwe la kimaadili.

Akizungumzia uhuru wa habari, Sitta alisema Tanzania ni kubwa, wanasiasa wanaweza kusema watakalo na katika mitandao ya intaneti hasa blogu, watu wanaweka chochote watakacho bila kuingiliwa na mtu.

Hata hivyo, alisema kibaya ni matumizi mengine ya uhuru huo, ambapo watu wanasema uongo kwa makusudi na kuchafuliwa hasa viongozi aliosema ni rahisi kuchafuliwa na wao kukosa namna ya kujitetea.

Kuhusu utaifa wa Watanzania, Sitta alitilia shaka kuwa unaweza kupotea na kutoa mfano wa Tanzania na Rwanda.

"Wakati wa Mwalimu na hata wa Mzee Mwinyi, ilikuwa rahisi kuwataka wananchi wajitolee na wakafuata mwito wa kiongozi lakini hilo halipo leo.

"Pale Rwanda, kuna siku iliamuliwa watu wote wajitokeze kufagia na kufanya usafi wa mazingira, lakini leo ukiwaambia Watanzania wafanye hivyo, watakucheka na kuhoji unasema nini," alisema Sitta na kuongeza kuwa kutofuatwa kwa mwito wa viongozi kutasababisha siku moja Taifa lipotee.

Kuhusu maendeleo ya ushirikiano wa Afrika Mashariki, Sitta alisema unaendelea vizuri, lakini kwa sasa, hatua ya Umoja wa Sarafu wa kuufanya ushirikiano huo kutumia sarafu moja, umeanza kutiliwa shaka.

Alifafanua kuwa shaka hiyo inatokana na mgogoro wa Umoja wa Ulaya (EU), uliotokana na nchi hizo kuwa katika hatua hiyo ya Umoja wa Sarafu.

Kutokana na hali hiyo, Sitta alisema tayari baadhi ya wataalamu wameondoka kwenda Ulaya kujifunza changamoto inayokabili umoja huo katika hatua hiyo ya kutumia sarafu moja.

Hata hivyo, alitabiri huenda umoja wa kisiasa kati ya nchi za Afrika Mashariki ukafikiwa mwaka 2020 baada ya majadiliano na utekelezaji wa kuingia katika hatua zijazo kutoka hatua ya soko la pamoja lililopo sasa.

Sitta ni mmoja wa wabunge ambao wamekuwa wakijinasibu kupambana na ufisadi nchini na kuwa na kundi ambalo limekuwa kila likipata fursa, huzungumzia ufisadi na kutaka watuhumiwa wawajibishwe.

KUKOSEKANA KWA MWAMKO MIONGONI MWA WAPIGA KURA


SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII TCIB WATAWASILISHA:

MADA: KUKOSEKANA KWA MWAMKO MIONGONI MWA WAPIGAKURA NA UPATIKANAJI WA TAARIFA

Lini: Jumatano Tarehe 18 Januari, 2012

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni

WOTE MNAKARIBISHWA