Monday, December 22, 2008

Seif: Hakuna sheria inayoagiza Serikali ya Tanganyika ifutwe

Desemba 4, mwaka huu, Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Seif Sharif Hamad, alitoa mada mjini Zanzibar iliyokuwa ikichambua hatma ya Zanzibar na mustakabali wa Muungano. Mwandishi Wetu ARISTARIKO KONGA, ameipata mada hiyo anapitia baadhi ya hoja na msimamo wa mwanasiasa huyo.

“[President Nyerere] managed half the work of a python… He swallowed Zanzibar all right but he did not crush its fighting force first. The live animal is a long time digesting, and its kicks are being felt hurtfully, and possibly even fatally, deep inside Tanganyika’s body politic.”

‘The Perils of Nyerere’ in The Economist of June 1964

SEIF Sharif Hamad amekichagua, nadhani kwa umakini mkubwa, kifungu hicho kutoka jarida la The Economist la mwaka 1964, akielezea mtazamo wake kwamba Tanganyika na mamlaka zake, tangu muda mrefu ilikuwa imepangilia kuimeza Zanzibar, si kwa bahati mbaya bali kwa makusudi, tena wakati mwingine kwa kutumia katiba na sheria.

“Mtafiti mmoja kutoka Argentina, Boaventura Santos de Sousa, aliwahi kuandika kwamba ‘mwandishi ingawa huandika kuhusu yaliyopita huwa anajaribu kueleza yaliyopo, si yaliyopita. Lakini, kwa kufanya hivyo, huwa pia anajiweka mbali na hali ya sasa na kwa hakika anaandika kwa ajili ya siku zijazo’.”

Kwa mujibu wa Seif, Muungano wa Zanzibar na Tanganyika umepita katika masaibu kadhaa tokea uasisiwe takriban miaka 45 iliyopita, lakini mtikisiko ulioukumba katika siku za karibuni ni mkubwa sana. Kwamba ni mkubwa kwa sababu umegusa kiini cha Muungano huu ambapo suala linaloulizwa ni iwapo kwa kule kukubali kushirikiana katika baadhi ya mambo, je, Zanzibar na Tanganyika zimejifuta na hivyo kupoteza hadhi zake kama nchi?

“Hilo limekuwa ndiyo swali kubwa linaloulizwa na Wazanzibari, hasa baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutamka bungeni kwamba Zanzibar si nchi.”

Seif anasema kwamba tangu kuasisiwa kwake, Muungano umejengeka kwa misingi ya hofu, kutiliana shaka na kutokuaminiana baina ya pande mbili zinazouunda, na wakati mwingine kumezua hata kutishia uhai wa Muungano wenyewe.

“Muungano umekuwa gumzo kuu katika takriban kila mjadala wa katiba na siasa katika nchi yetu. Umejitokeza na kujionyesha hivyo katika mwaka wa mwanzo wa Muungano kuhusiana na sakata la kuwa na Ubalozi wa iliyokuwa Ujerumani Magharibi kwa upande wa Tanganyika, na Ubalozi wa iliyokuwa Ujerumani Mashariki kwa upande wa Zanzibar; kuhusiana na uwakilishi wa Zanzibar katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki na uanzishwaji wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mwaka 1964 – 1966; wakati wa kuunganisha vyama vya ASP na TANU kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwaka 1977; katika mjadala wa Marekebisho ya Katiba wa 1983/84 na hatimaye kujiuzulu kwa Rais wa pili wa Zanzibar Sheikh Aboud Jumbe; wakati wa kuondolewa katika Uwaziri Kiongozi kwa mwandishi wa makala haya na hatimaye kufukuzwa katika CCM na wenzake sita mwaka 1988; katika harakati za madai ya kutaka kura ya maoni kuhusiana na Muungano huo mwaka 1989/90; wakati wa mjadala wa kuanzishwa vyama vingi mwaka 1991; katika sakata la Zanzibar kujiunga na Umoja wa Nchi za Kiislamu (OIC) mwaka 1993; wakati wa mjadala wa G-55 kudai kuanzishwa kwa Serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano mwaka 1994; katika mjadala wa marekebisho ya 11 na 14 ya Katiba ya Muungano mwaka 1994/95; wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 1995 na ule wa 2000 na karibuni kabisa kuhusiana na suala la matarajio ya ugunduzi wa mafuta visiwani Zanzibar na harakati za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki.

“Ukiondoa kuibuka kwake katika mijadala mikubwa ya kikatiba na kisiasa nchini, kwa upande mwingine katika uendeshaji wa shughuli za Serikali za kila siku, ‘matatizo na vikwazo kadhaa vya kiutawala na kiutendaji’ vimekuwa vikiripotiwa kila mara kwamba vinakwamisha uimarishaji wa Muungano.

Seif anasema tume na kamati kadhaa zimeundwa kuainisha matatizo ya Muungano na kupendekeza njia za kuyatatua. Serikali ya Jamhuri ya Muungano imeunda tume na kamati kadhaa, miongoni mwa nyingi, kuhusiana na masuala haya, ikiwamo Kamati ya Mtei, Tume ya Jaji Francis Nyalali ya mwaka 1991, Kamati ya Shellukindo ya mwaka 1994, Kamati ya Shellukindo 2 ya kuandaa muafaka juu ya Mambo ya Muungano baina ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT), Kamati ya Jaji Mark Bomani ya mwaka 1995, Kamati ya Jaji Robert Kisanga ya mwaka 1998, Kamati ya 'Harmonization', na Kamati ya Masuala ya Simu (Kamati ya Kussila).

Kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) Seif Sharif anasema nayo iliunda kamati zake kwa madhumuni hayo hayo, ikiwamo Kamati ya Baraza la Mapinduzi (Kamati ya Amina) ya 1992, Kamati ya Rais ya Kupambana na Kasoro za Muungano (Kamati ya Shamuhuna) ya 1997, Kamati ya Rais Kuchambua Ripoti ya Jaji Kisanga (Kamati ya Salim Juma Othman), Kamati ya Kuandaa Mapendekezo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar juu ya Kero za Muungano (Kamati ya Ramia) ya 2000, Kamati ya Baraza la Mapinduzi juu ya Sera ya Mambo ya Nje, Kamati ya Rais ya Wataalamu juu ya Kero za Muungano ya 2001, Kamati ya Baraza la Mapinduzi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kamati ya Mafuta, Kamati ya Madeni baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano wa Tanzania, Kamati ya Suala la Exclusive Economic Zone (EEZ), Kamati ya Masuala ya Fedha na Benki Kuu, Kamati ya Rais ya Masuala ya Simu ya mwaka 1996 hadi 1999, Kamati ya Baraza la Mapinduzi juu ya matatizo na kero za Muungano na taratibu za kuyaondoa ya 2004.

“Ukiacha tume, kamati na ripoti hizo, kuanzia mwaka 1985 kulianzishwa utaratibu wa Kamati ya Pamoja ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano na Waziri Kiongozi wa Zanzibar pamoja na Mawaziri wa Serikali zetu mbili ambao ulitarajiwa uwe ndilo jukwaa la kuzungumzia matatizo kutoka kwa washiriki wakuu wa Muungano huu na kuyapatia ufumbuzi unaofaa.

Utaratibu huu uliachwa kwa muda mrefu lakini sasa umerejeshwa upya kufuatia agizo la Rais Jakaya Kikwete, alilotoa katika mkutano na mawaziri na watendaji wakuu wa Serikali yake huko Ngurdoto, Arusha, Februari, 2006.

“Mikutano, makongamano, semina na warsha vimefanywa kujadili masuala haya na kupendekeza hatua za kuchukuliwa. Wasomi na wanafunzi wamefanya tafiti kadhaa na kujipatia shahada na stashahada hadi ngazi ya Ph.D juu ya Muungano lakini bado matatizo yako pale pale na yanaongezeka kila kukicha.

“Yanayoonekana na kuelezwa kama matatizo, mapungufu, dosari, kasoro na, kwa msamiati wa sasa, kero, yamekuwa ndiyo yale kwa yale. Nini basi kiini cha haya? Na vipi tutayatatua?

“Mimi nimeamua kutoa changamoto kupitia waraka huu kwa kuitazama historia ya Muungano, jinsi ulivyoundwa, matatizo yanayoukabili, nafasi na hadhi ya Zanzibar katika Muungano na nini hatma ya Zanzibar na mustakbali wa Muungano huko tuendako.

Nitakayoyaeleza yanaweza yakaonekana ni machungu kwa wakati huu wa sasa, lakini kama asemavyo Santos de Sousa yanaweza yakawa ndiyo ufumbuzi kwa siku zijazo.”

Katika mada yake Seif Sharif anajaribu kueleza asili na sababu za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ingawa anakiri hakuna jibu la moja kwa moja kuhusu chanzo hicho kwa kuwa kuna maelezo mengi.

“Maoni yanayotolewa kuhusu asili na sababu za Muungano yamekuwa yakitofautiana mno. Wapo wanaouleza Muungano huu kuwa ni wa pekee katika Bara la Afrika, kwani ndiyo pekee ulioweza kudumu katika kutimiza azma na malengo ya kuleta umoja wa Afrika (Pan-Africanism), na pia wapo wanauona kuwa ni jaribio la ukoloni mdogo wa nchi moja ya Kiafrika kuiteka na kuitawala nchi nyingine ya Kiafrika.

“Kutokana na maelezo na hoja nyingi na zinazokinzana kuhusu asili na sababu za Muungano, si rahisi kusema moja kwa moja kuwa maelezo yepi au hoja ipi ni sahihi. Utangulizi wa Mkataba wa Muungano wenyewe unataja sababu kuu ya kuunganisha nchi za Zanzibar na Tanganyika kuwa ni ‘maingiliano ya muda mrefu ya watu wa nchi mbili hizi na mahusiano yao ya kidugu na kirafiki … na … kuendeleza umoja wa watu wa Afrika.’ Lakini miaka 45 sasa baada ya uzoefu wa Muungano huu, Wazanzibari wanajiuliza kweli haya ndiyo madhumuni ya Muungano huu?

“Wazo la kuungana linaweza kurudishwa nyuma tokea zama za harakati za ukombozi wa nchi za Afrika. Waasisi na wakuu wa harakati za kupigania uhuru waliiona mipaka ya nchi zao iliyowekwa na wakoloni kuwa ni ‘mbinu za kibeberu’ zilizotekelezwa kwa ajili ya manufaa na maslahi yao. Kutokana na hisia hizo, mazungumzo ya kuanzisha aina fulani ya umoja miongoni mwa nchi huru za Afrika yalitawala duru za siasa katika miaka ya 50 na 60.

“Nadharia mbili zilijichomoza. Ya kwanza, ikishadidiwa na Kwame Nkrumah wa Ghana, ilikuwa ikitaka kuasisiwa kwa nchi moja tu ya Afrika nzima iliyoungana ikiwa na Serikali moja kwa bara zima. Nadharia hii ilipingwa na baadhi ya viongozi, wakiongozwa na Julius Nyerere wa Tanganyika, ambao walisisitiza haja ya kuanza na miungano ya maeneo (regional unions) chini ya mfumo wa Shirikisho badala ya kuwa na mpango wa Serikali moja.

“Katika kulifikia lengo hilo, viongozi wa kisiasa wa nchi tatu za Afrika Mashariki – Kenya, Uganda na Tanganyika – walikuwa wakifanya mikutano ya mara kwa mara kipindi chote cha kati ya mwaka 1961 na 1963 kuona jinsi gani wanaweza kutimiza ndoto hiyo. Mfumo wa Muungano uliokuwa ukiandaliwa ulikuwa ni ule wa Shirikisho. Tamko la Pamoja la viongozi hao lilisema: ‘Sisi, viongozi wa wananchi na Serikali za nchi za Afrika Mashariki … tunayakinisha nia zetu kuhusu kuwepo kwa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki. Mkutano wetu wa leo unasukumwa na hisia za umoja wa Afrika (Pan-Africanism), na siyo tamaa za maslahi binafsi ya eneo hili. … Ijapokuwa Zanzibar haikuwakilishwa katika mkutano huu, tunapaswa kuweka bayana kwamba nchi hiyo inakaribishwa kushiriki kikamilifu katika mikutano yetu kwa ajili ya uundwaji wa Shirikisho.’

“Lakini Umoja wa Afrika (Pan-Africanism) hauonekani kuwa ndiyo dhamira pekee au kama ndiyo dhamira halisi ya Muungano. Wengi wanaamini, na mimi nikiwa mmoja wao, kwamba dhana hiyo ilitumiwa tu kuficha njama za muda mrefu za Nyerere kutaka kuimeza na kuitawala Zanzibar. Katika mwaka 1961, wakati Tanganyika inakaribia kupata Uhuru wake, Nyerere alinukuliwa akisema: ‘Kama ningekuwa na uwezo wa kuvikokota visiwa vile [Zanzibar] na kuvitupa nje kabisa, katikati ya Bahari ya Hindi, basi ningefanya hivyo … Nahofia vitakuja kuniumiza kichwa sana.’

“Imani hii inatiliwa nguvu na mahusiano ya karibu na ya muda mrefu yaliyokuwepo kati ya chama kilichokuwa kikitawala Tanganyika, TANU, na ASP ambacho kilishika hatamu za utawala baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964, mwezi mmoja tu baada ya Zanzibar kupata uhuru wake kutoka Uingereza hapo Desemba 10, 1963. Zilikuwepo taarifa tokea mwaka 1959 kwamba TANU na ASP zitakaposhika madaraka zitaziunganisha nchi mbili hizi kuwa Jamhuri moja.

“Wakati juhudi za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki zikiwa zinafifia, Nyerere aliona fursa Zanzibar ambayo hakutaka kuipoteza. Katika mazungumzo ya siri kati yake na Rais Abeid Amani Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, wakakubaliana kuziunganisha nchi mbili hizi. Hakukuwa na ushirikishwaji wa aina yoyote ule wa wananchi wa nchi hizi mbili katika maamuzi haya makubwa. Usiri uliogubika hatua hii kubwa unafichuliwa na si mwingine bali Nyerere mwenyewe pale aliposema: ‘[Tanganyika] tulipeleka polisi wetu Zanzibar. Baada ya kuyashinda matatizo kadhaa tukaungana. Sisi wenyewe kwa hiari zetu tulikubaliana kuungana. Karume na mimi tulikutana. Peke yetu wawili tu tulikutana. Nilipomtajia wazo la Muungano, Karume hakufikiri hata mara mbili. Pale pale alinitaka kuita mkutano wa waandishi wa habari kutangaza azma yetu. Nilimshauri asubiri kidogo kwani ilikuwa bado ni mapema mno kuweza kuviarifu vyombo vya habari’.’’

Kwa mujibu wa Seif Sharif Hamad, taarifa hizo ziliendelea kubaki kuwa siri hadi Aprili 26, 1964 pale Redio ya Tanganyika ilipotangaza kwamba siku hiyo marais wawili hao wangekutana katika Bunge la Tanganyika kubadilishana Hati za Muungano ambazo zimeunganisha Zanzibar na Tanganyika kuwa Jamhuri moja. “Hivyo inaonekana wazi kwamba tokea awali Muungano huu ulikosa ridhaa ya watu. Haukuwa Muungano wa watu, ulioundwa na watu, kwa maslahi ya watu. Bali ulikuwa na umeendelea kuwa ni Muungano uliosimamishwa kwa ridhaa ya watawala pekee. ’’

Katibu huyo mkuu wa CUF katika mada hiyo anaelezea mtazamo wake na hata kutumia maandiko na mitazamo ya watu wengine kuhusu kiini na matatizo ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kuanzia tafsiri ya mkataba wenyewe na hasa kuhusu mfumo wa muungano na mambo ya muungano yaliyomo kwenye mkataba.

“Ukitazama kwa jicho la sheria, kiini cha matatizo ya Muungano kinatokana na tafsiri ya Mkataba wa Muungano wa 1964. Hizi ndizo hati zinazounda, kupitia mkataba wa kimataifa, Jamhuri ya Muungano. Suala kubwa lililoumiza na linaloendelea kuumiza vichwa vya wengi na hivyo kuendelea kuulizwa ni mfumo gani wa Muungano ulikusudiwa kuwekwa na Mkataba huu? Ni muungano wa moja kwa moja (unitary) au wa shirikisho (federal)?

“Mfumo uliopo sasa ambao ulianza kutekelezwa 1964 ni ule wa serikali mbili – ile ya Jamhuri ya Muungano na ile ya Zanzibar. Tanganyika haikuwekewa serikali yake tofauti; madaraka yake kwa yale mambo yasiyo ya Muungano yalielezwa kwamba yatasimamiwa na kuendeshwa na Serikali hiyo hiyo ya Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo, uhalali wa kisheria wa muundo huu umeendelea kuhojiwa na hata kupingwa kwamba hauwakilishi ipasavyo makusudio yaliyomo katika Mkataba ulioanzisha Muungano wenyewe.

“Mkataba wa Muungano wenyewe hauelezi bayana aina au mfumo wa Muungano inaouanzisha lakini uko wazi kuhusiana na mgawanyo wa madaraka inaouweka na idadi ya mamlaka (number of jurisdictions) zitakazokuwepo. Ibara ya (iii) (a) ya Mkataba huo inaanzisha ‘Bunge na Mamlaka ya Utendaji’ (Parliament and Executive) ndani ya na kwa ajili ya Zanzibar ikiwa na mamlaka kamili kuhusiana na mambo yote yasiyo mambo ya Muungano kwa Zanzibar. Kwa upande mwingine, ibara ya (iv) ya Mkataba huo inaanzisha ‘Bunge na Mamlaka ya Utendaji’ (Parliament and Executive) ya Jamhuri ya Muungano ikiwa na mamlaka kamili katika eneo lote la Jamhuri ya Muungano kuhusiana na mambo ya Muungano na, pia, ikiwa na mamlaka kamili ndani ya, na kwa ajili ya Tanganyika kuhusiana na mambo yote yasiyo mambo ya Muungano kwa Tanganyika. Kwa hivyo, katika sehemu ya pili, mamlaka mbili tofauti zimechanganywa pamoja.

“Mjadala mkubwa na mkali umekuja kuhusiana na tafsiri ya ibara hiyo ya (iv) na kule kuchanganya kwake mamlaka mbili hizo. Haya si masuala ya kisheria tu kama ambavyo baadhi yetu wanataka tuamini (ingawa nayo ni muhimu mno kama ilivyodhihirika hivi karibuni), bali pia ni masuala ya kisiasa kwa vile yanahusisha uwezo wa maamuzi, madaraka na mamlaka, na zaidi mchango wa gharama za uendeshaji na mgawanyo wa raslimali na mapato kati ya wahusika wakuu. Mambo haya, katika uzoefu wa nchi za wenzetu, ndiyo yaliyopelekea kuvunjika kwa miungano yao kwani huzaa kutiliana shaka na kutokuaminiana. Kwa vile yanachukua sura ya kisiasa (kutokana na sababu nilizozitaja), haya hayana chama wala itikadi kama nitakavyoonyesha huko mbele. Kama alivyowahi kusema Profesa Issa Shivji: ‘Mwisho wa yote, suala la Muungano linabakia kimsingi kuwa ni suala la kisiasa, na inapofikia kwenye siasa hasa, hotuba na kauli kali za jazba kuhusiana na mahusiano ya damu na ya kidugu, zote hazitafaa kitu.

“Kwa hakika, kinyume na inavyojaribiwa kuonyeshwa na wengi kwamba Tanganyika imepoteza kila kitu katika muundo huu wakati Zanzibar imekabidhi sehemu tu ya madaraka yake, muundo wa Serikali mbili umepelekea wengi kuamini kwamba kilichofanyika ni kiini macho tu kwani ni Zanzibar iliyokabidhi sehemu muhimu ya mamlaka yake (mahusiano ya nchi za nje, ulinzi na usalama, uraia, kodi na ushuru, sarafu, nguvu kuu za kuendeshea uchumi na mengineyo) kwa Tanganyika na kisha Tanganyika ikajigeuza jina na kujiita Jamhuri ya Muungano. Na haya si maoni ya ngumbaru (kwa lugha ya Mwalimu Julius Nyerere) bali ni maoni ya watu wazito wakiwemo aliyekuwa Spika wa Bunge na ambaye sasa ni Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa, ambaye alisema kwa jinsi mambo yalivyofanyika, Zanzibar inaonekana kama vile ni ‘invited guest’ (mgeni aliyealikwa) katika Muungano. Naye msomi mashuhuri ulimwenguni, Profesa Ali Mazrui alisema baada ya Muungano Zanzibar imepoteza kila kitu muhimu wakati Tanganyika imebadilika jina tu na kuwa Tanzania huku ikiwa na mamlaka zaidi lakini ikibaki na Rais wake, nembo yake ya Taifa, wimbo wake wa Taifa na hata kiti chake katika Umoja wa Mataifa.”

Seif Shariff Hamad anazungumzia pia kwamba Mkataba wa Muungano haukufuta Serikali ya Tanganyika, kwa kuwa hakuna kifungu chochote kilichotoa maagizo ya kufutwa kwa serikali hiyo.

“Katika makubaliano ya kimataifa yaliyounda Muungano, ambayo hata hivyo katika muda wote wa uhai wa Muungano yamekuwa hayafuatwi, hakuna kifungu hata kimoja kilichotoa au kuagiza kwamba Serikali ya Tanganyika ifutwe kwa mujibu wa makubaliano hayo. Serikali ya Tanganyika, kama ilivyo ile ya Zanzibar, imelindwa na kifungu cha (v) kinachosomeka kwamba: “The existing laws of Tanganyika and of Zanzibar shall remain in force in their respective territories”. Kinachosemwa hapa ni kwamba ‘Sheria zilizopo za Tanganyika na za Zanzibar zitaendelea kufanya kazi na kuwa na nguvu katika maeneo yao.’

“Wataalamu wa katiba na sheria wanafahamu kwamba katiba ndiyo sheria mama ya sheria zote za nchi. Hivyo Katiba ya Tanganyika imelindwa na inapaswa kuwepo na Serikali yake iwepo, pamoja na viongozi wake kuwepo na kusimamia mambo yasiyo ya Muungano. Katiba na sheria za Tanganyika ndizo zilizotakiwa zitumike katika eneo la Tanganyika kwa yale mambo yaliyokuwa hayamo kwenye Muungano kama ambavyo Katiba (au kabla ya hapo Matangazo ya Kikatiba – Constitutional Decrees) na sheria za Zanzibar zinavyotumika katika eneo la Zanzibar kwa yale mambo ambayo si ya Muungano. Hiyo ndiyo tafsiri ya ‘maeneo yao’.

“Wazanzibari wanafahamu kwamba Serikali ya Tanganyika imefutwa kwa makusudi na Bunge la Tanganyika kinyume na Makubaliano ya Muungano ili kujipa nafasi kuitumia Serikali ya Muungano, kama kwamba ndiyo Serikali ya Tanganyika. Lengo ni hatimaye kuiua Serikali ya Zanzibar na kufanya Tanganyika mpya ikiwa na jina jipya la Tanzania lenye mipaka mipya, yaani kuwa nchi moja yenye Serikali Moja.

Itaendelea..

Raia Mwema
Disenba 17, 2008

Ufisadi mkubwa vyama vya siasa

PAMOJA na vyama vya siasa kuwa mstari wa mbele kupiga vita rushwa na ufisadi, imebainika kwamba ndani ya vyama karibu vyote vya siasa kuna ufisadi mkubwa katika mapato na matumizi ya mabilioni ya fedha za vyama hivyo.

Uchunguzi wa muda mrefu wa Raia Mwema umebaini kwamba vyama vya siasa vinakiuka Sheria ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992 kuhusiana na masuala yanayohusu fedha hali inayoeleza kuwa hakuna uadilifu katika matumizi ya mabilioni yanayoingia katika vyama hivyo ikiwa ni pamoja na ruzuku na fedha kutoka kwa wafadhili wa ndani na nje.

Kumekuwa na matumizi makubwa ya fedha katika medani ya siasa katika miaka ya hivi karibuni, fedha ambazo baadhi zimebainika kuwa zinatoka nje ya nchi lakini hazitolewi maelezo kama sheria inavyoelekeza huku kiasi kingine kikubwa cha fedha kikitolewa na wafanyabiashara wa ndani wakiwamo ambao si raia wa Tanzania.

Kifungu cha 13 (1) cha Sheria ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992 kinabainisha vyanzo vya mapato kwa vyama vya siasa kuwa ni pamoja na ada za wanachama, michango ya hiari, miradi ama hisa katika kampuni, ruzuku ya serikali na michango ama misaada kutoka vyanzo vingine lakini kwa sharti kwamba hesabu zake zinakuwa wazi.

Sehemu ya pili ya kifungu hicho inaelekeza vyama vya siasa kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kuhusu michango kutoka nje ya nchi na pia kutoka kwa watu ambao si raia wa Tanzania hata kama wanaishi ama wanafanya biashara halali nchini lakini pia vyama vya siasa vinalazimika kuwasilisha hesabu sahihi kila mwaka.

Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, amekiri kuwapo kwa udhaifu mkubwa katika eneo la fedha kwa vyama vyote vya siasa, ingawa hakupenda kutaja jina la chama chochote cha siasa.

“Vyama vyote havizingatii sheria, hakuna hata chama kimoja kinachowasilisha chanzo cha mapato yake ya nje na ndani. Kama Jeetu Patel anawapa fedha TLP au chama chochote hawasemi, na kwa sheria yetu CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali) hakagui hesabu za vyama vya siasa kwa kuwa si taasisi za umma,” alisema Tendwa wiki katika mahojiano ya simu na Raia Mwema.

Tendwa alizungumzia pia kuhusiana na udanganyifu mkubwa unaofanywa na vyama vya siasa ikiwa ni pamoja na kutowasilisha taarifa sahihi za mapato yao, jambo ambalo amesema limetokana kwa kiasi kikubwa na udhaifu wa Sheria ya Fedha za Umma ambayo haivitaji vyama vya siasa kama taasisi za umma.

“Hesabu za vyama zinaletwa kwa Msajili lakini ujue Msajili hakagui ila yeye anakaguliwa na CAG. Sisi tukisha kuwapa fedha (vyama vya siasa) wanakwenda huko wanatumia halafu wanaajiri mkaguzi wao wanayemjua wanakuja wanatudanganya kwamba wamekwenda vijijini, wamenunua sijui vitu gain, kumbe wengine uongo mtupu,” alisema Tendwa katika mahojiano hayo.

Alisema kwa sasa inaonyesha wazi kwamba kuna haja ya CAG kukagua hesabu za vyama vya siasa kwa maelezo kwamba udhaifu wa kisheria uliopo unatoa mwanya kwa fedha za umma zinazoingizwa katika siasa kupotea na lakini pia unatoa mwanya wa kuimarika kwa rushwa na ufisadi mwingine.

Katika kipindi cha bajeti ya miaka mitatu pekee 2005/2006 hadi mwaka 2008/2009, Serikali imetoa jumla ya Shilingi bilioni 72 kama ruzuku kwa vyama vya siasa, fedha ambazo hazijakaguliwa na CAG bali wakaguzi wanaoteuliwa na vyama husika na baadaye kuwasilishwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa.

Mwaka 2005/2006 zilitolewa Shilingi bilioni 39, mwaka 2006/2007 Shilingi bilioni 15 na mwaka 2008/2009 zimetengwa Shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ruzuku kwa vyama vya siasa vyenye uwakilishi katika dola.

Juhudi za kumpata CAG Ludovick Utouh, hazikufanikiwa hadi tunakwenda mitamboni jana Jumanne huku simu yake ya mkononi ikiendelea kuita bila majibu.

Kumekuwapo na manung’uniko makubwa miongoni mwa wana jamii kuhusiana na matumizi makubwa ya fedha katika siasa na wananchi wengi wamekuwa wakihoji mahali hasa yanakotoka mabilioni ya fedha zinazotumika katika shughuli za siasa nchini, baadhi zikiwa zinatumiwa na wagombea na sehemu nyingine ikitumika na vyama husika.

Mara baada ya kukabidhiwa kuongoza chama, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, alidhihirisha wazi kukwerwa kwake na jinsi fedha ilivyogeuzwa kuwa kigezo muhimu cha mtu kupata wadhifa wa kisiasa, hisia ambazo amezigusia katika hotuba zake mbalimbali.

Tayari kuna habari kwamba Kikwete amekuwa akipata wakati mgumu katika kutekeleza dhamira yake hiyo ya kuhakikisha kwamba fedha zinakuwa si kigezo cha kuwa kiongozi kutokana na kuguswa na matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni za chama chake zilizomuingiza Ikulu lakini pia kuzungukwa na wasaidizi ambao au wameingia madarakani kwa kutumia fedha nyingi ama wanajiimarisha kwa kutumia fedha.

Baadhi ya wachunguzi wa kimataifa wamekuwa wakihoji hatima ya Tanzania kama Taifa kutokana na matumizi hayo makubwa ya fedha katika siasa na katika moja ya taarifa zake, Benki ya Dunia (WB), imeonyesha wazi kushitushwa na wingi wa fedha katika mchakato wa kisiasa nchini kutokana na kwamba vyanzo vya fedha hizo nyingi vina utata.

“Pamoja na nchi kuingia katika mfumo wa vyama vingi, bado kuna udhaifu mkubwa katika mfumo wa utawala unaochangia kukwama kwa vita dhidi ya rushwa katika siasa. Fedha za kuendeshea siasa zinaonyesha kuwa chanzo kikuu cha rushwa na ufisadi,na hii ni pamoja na kuwa Sheria ya Vyama vya Siasa inataka vyama vya siasa kueleza vyanzo vyote vya mapato na kukaguliwa kila mwaka, utekelezaji wake ni kitendawili,” inaeleza sehemu ya ripoti ya WB ya hivi karibuni kuhusiana na hali ya rushwa
nchini.

Ripoti hiyo inabainisha kwamba suala la vyanzo vya mapato ya fedha za kuendeshea siasa limekuwa tatizo sugu kwa nchi nyingi duniani na inapendekeza kuunda chombo ama mfumo wa kuhakiki fedha za kuendeshea siasa.

“Inawezekana kufanikiwa kwa kuwapo kwa majadiliano kati ya vyama
vinavyoshiriki uchaguzi, ama kuwapo kwa Tume ya Bunge, ambayo itakuwa inaangalia na kuhakiki fedha za kampeni na pia ikiwezekana vyombo husika viweke ukomo wa kiwango kinachopaswa kuchangwa,” inaeleza sehemu ya ripoti hiyo.

Katika kauli za kiaiasa zinazozungumzwa sasa kuhusiana na fedha katika siasa za Tanzania, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Zitto Kabwe alidai majuzi kwamba ufike wakati CAG akague hesabu za vyama vya siasa kama njia ya kuvisafisha vyama vya siasa kutoka katika tuhuma za ufisadi.

katika kauli iliyokikera chama tawala, Chama cha Mapinduzi (CCM), Zitto amenukuliwa akitaka CAG afanye ukaguzi maalumu wa hesabu za CCM wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005.

"Njia pekee itakayowatoa CCM katika hili ni kwa wao kuruhusu uchunguzi maalumu kufanywa na CAG. Baada ya uchunguzi, Mkaguzi ataueleza umma CCM walitoa wapi fedha zao na walizitumia namna gani. Yeye pekee ndiye anayeweza kuwasafisha kama hawahusiki na fedha za EPA, na si maneno ya baadhi ya viongozi wa CCM ya kujaribu kujitakasa," amenukuriwa Zitto akisema.

"Kesi ya Kisutu haitatuambia ukweli juu ya kikao cha baadhi ya viongozi wa CCM na Gavana wa Benki Kuu mara baada ya kugundua kuwa CCM hawakuwa na fedha za kutosha za kampeni baada ya Kikwete kuteuliwa kuwa mgombea wa CCM," aliongeza mbunge huyo.

Akizungmza na Raia Mwema kwa njia ya simu jana, Zitto alisisitiza umuhimu wa CAG kukagua hesabu za vyama vya siasa kwa kuwa ni fedha za umma ambazo zinapaswa kukaguliwa kwa mujibu wa Katiba na sheria ya fedha za umma.

“Fedha zote hata za misaada kwa vyama vya siasa zinapaswa kukaguliwa na kwamba wakati wa uchaguzi vyama vyote viweke wazi taarifa za mapato na matumizi ya fedha zao za uchaguzi. Haya ni matakwa ya kikatiba na kisheria kwani fedha za ruzuku ni fedha za umma zinazotokana na kodi zetu,” alisema katika mazungumzo hayo ya simu.

Baadhi ya watu waliotoa maoni yao juu ya matakwa ya Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992, kuhusu umuhimu wa vyama vya siasa kutaja vyanzo vya mapato kutoka nje ya nchi, waliiambia Raia Mwema ya kuwa utaratibu huo haufuatwi na umejaa usiri mkubwa karibu katika vyama vyote.

Mhadhiri wa Idara ya Uchumi ya Chuo kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Lenny Kasoga alisema ni kweli sheria inavitaka vyama vya siasa kutaja vyanzo vya mapato au misaada yao kutoka nje ya nchi, lakini utaratibu huo ni mgumu kuufuatilia kwa kuwa hakuna chama ambacho huweka wazi masuala ya fedha.

Mkurugenzi wa Utawala na Fedha wa Chadema Anthony Komu alisema kuwa kutaja vyanzo vya mapato kutoka nje kunategemea zaidi utashi wa wanasiasa, lakini kwa ufahamu wake viongozi wengi ni wadanganyifu.

“Chama chetu kinapendekeza kuwa ukaguzi wa hesabu za vyama ufanywe na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ili vyanzo hivyo vijulikane,” alisema.

Kwa upande wake, Msemaji wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Chama cha Wananchi (CUF) Suleiman Khalifa alisema ni mapungufu hayo ya ukaguzi yanayosababisha suala hilo lizungumzwe sasa na kwamba maoni ya wabunge wengi ni kwamba uletwe bungeni muswada wa kumpa uwezo zaidi CAG kukagua vyama vya siasa. Huenda muswada ukafikishwa bungeni mapema mwakani.

Huku hayo yakiendelea, Raia Mwema imeambiwa kwamba suala hilo la fedha za vyama, ni kati ya sababu zilizoutungua Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa mwaka 2008 uliokuwa uwasilishwe bungeni mwaka huu.

Sababu nyingine suala linaloonekana kutofurahiwa na baadhi ya vyama hivyo la muungano wa vyama kabla ya uchaguzi na sababu nyingine za kiufundi.

Hoja nyingine inayotajwa kusababisha kuahirishwa ghafla kuwasilishwa
bungeni kwa muswada huo ni suala la vyama vya siasa kuruhusiwa kuwa na vitengo vya ulinzi na usalama, hoja ambayo ilielezwa kuzua mjadala wakati muswada huo ulipojadiliwa na Kamati ya Sheria na Katiba ya Bunge.

Raia Mwema
Disemba 17, 2008

Wednesday, December 17, 2008

Miaka Mitatu Ikulu: Rais akipunguza kasi, hatokwepa lawama

NAENDELEA na tathmini yangu ya Uongozi wa Awamu ya Nne wa Rais Jakaya Kikwete. Katika miaka mitatu tunaona, kuwa pamoja na dhamira njema ya Rais aliye madarakani, dhamira ya kutaka kutuongoza Watanzania ili tujitoe hapa tulipo, na kupiga hatua za maana na za haraka za kimaendeleo, bado anakwamishwa na baadhi ya watendaji wanaomzunguka.

Watendaji walio mbali na uhalisia, na baadhi ya watendaji walio chini, ni wale wenye kuiga matendo maovu ya watendaji waandamizi, baadhi ni wenye kumzunguka Rais.

Kama Rais aliye madarakani atapunguza kasi ya kuwashughulikia watenda maovu, basi, hataepuka lawama. Wengine tutabaki kuwa 'wapiga zumari'. Mwenye wajibu wa mwisho wa kukamata fagio na kusafisha uchafu unaomzunguka ni yule anayezungukwa na uchafu huo, maana yu karibu na fagio.

Wiki iliyopita nilimalizia kwa sentesi yenye kuhoji na kuwaachia wasomaji swali la kujiuliza na kutafakari. Niliandika; wenye kutumia madaraka yao vibaya na kufuja mali ya umma wanafanya hivyo kila siku. Hivi hawana uchungu na nchi yao? Na labda ni kwa kufanya mambo kwa mazoea tu, lakini katika karne hii ya 21, je, bado hatuoni kuwa msafara wa kiongozi mwandamizi wenye magari 30 ni ufujaji mkubwa wa rasilimali za nchi?

Nitasimulia kisa cha mzungu mmoja Mkurugenzi wa Shirika la Misaada la Kigeni. Mheshimiwa huyu alipata kunipa maelezo mafupi na kisha kuniuliza kwa kushangaa; Mheshimiwa yule alitoka kwenye moja ya nchi zinazotufadhili. Alikubaliana na afisa mmoja wa asasi isiyo ya Kiserikali ya Kitanzania, wakutane wakiwa safarini kwenda ughaibuni. Asasi ile ilipata misaada kutoka Shirika la misaada analoliongoza mheshimiwa huyo.

Kilichomshangaza Mkurugenzi yule ni kushindwa kwa wawili wale kufanya mazungumzo kwa vile yule Mkurugenzi wa Asasi isiyo ya Kiserikali ya Tanzania alipanda ndege daraja la kwanza na yule mzungu alibaki daraja la kawaida (Economy Class).

" Hivi unaweza kunifafanulia mantiki ya kitendo cha Mtanzania mwenzako yule?" Aliniuliza Mkurugenzi yule wa Shirika la Misaada.

Na hapa kuna mfano mwingine. Mwaka jana nikiwa mitaa ya jiji la Dar es Salaam nililiona barabarani gari la Mkuu wa Mkoa ulio mpakani kabisa na nchi ya jirani. Nikasoma magazetini kuwa mteule huyo alikuwa jijini kuhudhuria harambee ya kuchangisha fedha za elimu kwa mkoa wake.

Nilijiuliza; hivi ni kweli Mkuu huyo wa Mkoa alisafiri kwa gari lake hilo kwa siku mbili au zaidi kutoka makao makuu ya mkoa wake hadi Dar es Salaam? Kwa uchache, gharama za kuendesha gari lile hadi lifike Dar es Salaam ni shilingi milioni moja kwa kwenda na kurudi. Hapo hatujapiga hesabu ya gharama nyingine ikiwamo posho za njiani za mteule na dereva wake.

Na yawezekana kabisa, kuwa Mkuu wa Mkoa yule alipanda ndege kwenda Dar es Salaam na kumwamuru dereva wake aendeshe gari kutoka mkoani hadi Dar es Salaam alimradi tu mteule akiwa jijini avinjari akiwa na gari lenye kutambulisha cheo chake. Kwa mteule huyu, hajawa Mkuu wa Mkoa kama gari lake halijawa na sahani ya namba yenye kusomeka " RC XX"!

Naam! Mteule anaruka angani kwa ndege kutoka mkoa wa pembezoni na shangingi lake linakata mbuga kuitafuta Dar es Salaam! Je, kama mteule ametuma gari na kukaanga mafuta ya thamani ya shilingi milioni moja na zaidi kwa safari ya kwenda Dar es Salaam na kurudi kuchangisha fedha za elimu ya watoto wa mkoa wake, haoni kwamba milioni hizo zinazoteketea barabarani ni kodi za wananchi ambazo zingesaidia kuwasomesha watoto wa mkoa wake? Je, haikutosha kwake kupanda ndege kwa gharama isiyozidi shilingi laki tano kwa safari ya kwenda na kurudi na kwa saa chache?

Kwamba akiwa jijini ingekuwa nafuu kuazima gari jingine la serikali au hata kupanda teksi. Lakini, huu ni zaidi ya uzumbukuku. Na wala si kwa mteule niliyemtolea mfano tu, hali hii imezoeleka kwa baadhi ya wateule wetu. Ni hulka ya kupenda sana utukufu. Lakini inachangiwa pia na hulka ya kupenda kujipendelea, kuendekeza ubinafsi na kutokujali maslahi mapana ya taifa. Maana, mteule huyu, kama ni kwa fedha za mfukoni mwake asingekubali kusafiri kwa ndege kwenda Dar es Salaam na kisha kumwamuru dereva wake apeleke gari binafsi la mteule ili aje kulitumia akiwa Dar es Salaam! Asingeweza kufanya hivyo hata kama angeahidiwa kuchangiwa nusu ya gharama.

Naam. Majuzi hapa tumemsikia Waziri Mkuu Mizengo Pinda akikemea vitendo vya watendaji wa Wilaya na Mikoa kutokukaa ofisini. Alikemea pia semina zisizoisha. Alikuwa sahihi, lakini hata hapa tunaona umuhimu wake kukemea urefu wa misafara kwenye ziara zake za kikazi. Misafara mirefu ina maana ya watendaji wengi walioziacha ofisi zao kwenda kushuhudia kiongozi mwandamizi anapofanya kazi zake.

Katika taratibu za sasa, tuchukue mfano wa ziara ya kikazi ya siku mbili ya Waziri Mkuu kwenye moja ya mikoa yetu. Hata kama ziara hii tutaiita ni ya kikazi, lakini kuna uwezekano mkubwa wa kazi kusimama katika baadhi ya idara za serikali. Kama mheshimiwa atatua kwa ndege saa nne asubuhi, basi, hakuna huduma zitakazotolewa kwa wananchi siku hiyo. Kila mtendaji unayemtaka akusaidie atakujibu " leo tuna ugeni wa mheshimiwa!".

Kwa ufupi siku hiyo imekatika bila watu kuwa ofisini. Tuje sasa kwenye shughuli nzima ya kumpokea mheshimiwa. Kwa kawaida viwanja vingi vya ndege katika mikoa yetu hujengwa kiliomita 15 au zaidi kutoka makao makuu ya mkoa. Kwa uchache, msururu wa magari 20 utaanza kwenda kumpokea mheshimiwa saa moja au mbili kabla ya mheshimiwa kutua. Kwa safari ya kwenda uwanjani na kurudi, kila gari litatumia kwa uchache shilingi 50,000 za mafuta.

Na hapa inafuatwa kanuni ya kila mteule na dereva wake na pengine kabendera kake. Hakuna mteule atakayekuwa tayari kukaa kiti cha nyuma kwenye gari la mteule mwenzake wakati serikali imempa gari na dereva wake wa kumwamrisha twende huku , twende kule! Akiomba lifti, wateule wenzake watamshangaa.

Kwa uchache, orodha ya wateule watakaoumlaki mheshimiwa inaweza kuwa na Mkuu wa Mkoa, Kamanda wa Polisi wa Mkoa, DED, DAS, Meya, Ma-DC wa Wilaya zote za Mkoa, Wakurugenzi wa Idara, Madiwani wa Halmashauri, na wakati mwingine wakuu wa mikoa ya jirani nao hufunga safari kutoka kwenye vituo vyao vya kazi kwenda kwenye mkoa wa jirani "kumlaki" mheshimiwa.

Katika hali hii ngumu ya kiuchumi tumefika mahali kama zinavyofanya nchi nyingine zinazoendelea na zilizoendelea, tuangalie uwezekano wa serikali na mashirika ya umma kuwa na aina mbili tofauti za magari; yale yanayotumika mijini na yenye kubana matumizi ya mafuta na gharama za uendeshaji na yatakayotumika kwa safari za nje ya miji.

Kuwepo na "pool" ama yadi ya magari ya serikali kwa shughuli za nje ya miji ambapo watendaji watalazimika kwenda kuchukua magari hayo kwa safari hizo na kuyarudisha kwenye yadi baada ya ziara zao za kikazi. Kwa mantiki hiyo, kutakuwapo na idadi ya kutosha ya magari yatakayokuwa chini ya udhibiti wa serikali na kutumika na idara yeyote ile ya serikali pindi yatakapohitajika kwa safari za nje ya miji.

Hatua kama hiyo, itaipunguzia serikali mzigo wa gharama za uendeshaji na hivyo kuokoa kiasi kikubwa cha fedha kitakachotumika kuwasaidia Watanzania. Na katika kuyaandika haya, kuna watakaojisemea moyoni na kuniuliza kwa kunidhihaki; " Kwani hiyo diseli unalipia wewe bwana?"

Itaendelea.



0754 678 252
mjengwamaggid@gmail.com
http://mjengwa.blogspot.com

Haki za Binadamu hazijui mipaka

"NAAMINI katika usawa na utu wa binadamu wote, na wajibu wa kuwatumikia waishi vizuri pamoja na uhuru wao katika jamii ya amani na ushirikiano," Julius Nyerere.

Juzi, Desemba 10 watu wa Marekani wanaungana na jamii ya kimataifa kusherehekea Azimio la Haki za Binadamu na wanaume na wanawake wa kila utamaduni na imani, kila rangi na dini, katika nchi ndogo na kubwa, zilizoendelea na zinazoendelea.

Maneno ya Mwalimu yanagonga ukweli kwa Wamarekani. Tunaamini kwa dhati kwamba haki za binadamu na haki za msingi zilizomo katika Azimio la Haki za Binadamu zinaanzia kwenye kuzaliwa kwa binadamu wote.

Zaidi ya miaka sitini tokea lipitishwe azimio hilo Desemba 10, 1948, kumekuwa na maendeleo yanayoonekana katika kila bara kwa haki zilizoorodheshwa. Lakini, pamoja na kupita miongo sita, mamilioni ya watu bado wananyimwa haki za msingi na serikali zao.

Leo, karibu duniani kote, wanaume na wanawake wanafanya juhudi kupata haki za msingi ili kuishi kwa utu, kuzungumza bila woga, kuchagua watu wa kuwaongoza, kuwawajibisha viongozi wanaoshindwa kuwajibika na kupata haki sawa chini ya sheria.

Katika nchi nyingi, watu wanaojitolea kwa ujasiri kudai kwa njia ya amani haki za wananchi wenzao ndio wanaolengwa kuchukuliwa hatua na kufungwa na vyombo vya serikali.

Azimio la Haki za Binadamu ni zaidi ya orodha za haki kama zilivyoandikwa ni mwito wa kuchukua hatua. Azimio hilo linamtaka “kila mtu na kila chombo cha jamii ... kuheshimu haki hizi na uhuru kwa kuchukua hatua, kitaifa na kimataifa kupata kutambuliwa..."

Kama ahadi kubwa ya Azimio la Haki za Binadamu itatimizwa, jumuiya ya kimataifa na hasa zile nchi za kidemokrasia duniani, hazitakaa kimya huku kuna watu katika dunia hii ambao wanaishi bila kuwa na utu au chini ya utawala mbaya.

Kutokana na kuendelea kuwapo kwa wanaume na wanawake katika dunia hii ambao wanaendelea kunyimwa haki zao za msingi, sisi, ambao tunafaidi kujaaliwa uhuru lazima tuendelee kuunga mkono jitihada za kupata haki za msingi kwa wote na kuwaunga mkono wote ambao wanaupigania.

Kama Rais George Bush alivyosema: "Uhuru unaweza kupingwa, na uhuru unaweza kucheleweshwa, lakini uhuru hauwezi kunyimwa." Kwa muda, madikteta wanaweza kutawala, lakini hatimaye, wale wanaojitolea kupigania haki, huru na demokrasia watashinda, kama Havels na akina Mandela walivyofanya kabla yao.

Mara nyingi, watetezi wa leo wa uhuru wanashutumiwa na kushitakiwa na serikali zao wenyewe. Lakini katika historia, mashujaa hawa wanaume na wanawake watatambulika kwa wanayoyafanya. Wataheshimika kama wazalendo wenye uvumilivu ambao si tu wanahamasisha wananchi wenzao, lakini pia mfano wao unatoa matumaini kwa watu kila sehemu ambako wanapigania haki za msingi.

Kupamba moto kwa matakwa ya kuwa na haki za binadamu na demokrasia si matokeo ya juhudi binafsi za baadhi ya wasomi au uhamasishaji wa serikali za nje. Ukweli ni kwamba mwito huu unatokana na matakwa yenye nguvu ya binadamu ya kuishi kwa utu na uhuru na ushujaa binafsi wa wanaume na wanawake katika kila umri katika kila jamii ambao wanajitolea mhanga kwa ajili ya uhuru.

Tunaamini ya kuwa demokrasia ndiyo mfumo pekee wa serikali wenye uwezo kupata na kulinda haki za binadamu na uhuru wa msingi wa muda mrefu. Nchi ambazo utawala uko mikononi mwa viongozi wasiowajibika ndizo ambazo zinaongoza kwa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.

Lakini hakuna utawala ambao hauna kasoro. Demokrasia ni mfumo wa serikali ya watu na kwa ajili ya watu ambao unatokana na misingi ya binadamu kuwa na haki ya kuamua juu ya hatima ya maisha yao ya baadaye. Lakini sisi binadamu ni viumbe wenye kuweza kufanya makosa hivyo ni lazima kuwa na njia za kujisahihisha na kujipima kwenye serikali ya demokrasia.

Kujisahihisha na kujipima kunahitaji kuwa na asasi zenye nguvu za kiraia, vyombo huru vya habari vyenye nguvu, bunge na mahakama ambavyo vinafanya kazi yake bila kuhofia au kuipendezesha serikali na kuwapo kwa utawala unaoonekana wa sheria.

Demokrasia ya Marekani, kama zilivyo nyingine si nzuri kwa asilimia zote. Wananchi wetu wanajivunia historia ya kupambana katika kila kizazi tokea kuanzishwa kwa taifa hilo ili kuleta demokrasia hiyo karibu na msimamo unaoliliwa hata pale tunapopambana na mambo yasiyo na haki katika kila zama mpya.

Tunayachukulia kwa umakini mkubwa majukumu yetu ya Haki za Binadamu na katika nia thabiti ya kutimiza majukumu hayo tunaenzi kazi kubwa inayofanywa na na asasi za kiraia na vyombo huru vya habari.

Huwa hatuchukui maoni ya jinsi tunavyotekeleza demokrasia yetu kama kuingiliwa kwa mambo yetu ya ndani, na serikali nyingine nazo zisijisikie vibaya zinapoelezwa kuhusu demokrasia zao.

Serikali ya Marekani itaendelea kusikiliza na kujibu hapo hapo maoni mbalimbali kuhusu tunavyotimiza demokrasia yetu ikiwa ni pamoja na hatua tuliyochukua ya kulinda taifa letu kutokana na tishio la dunia la ugaidi. Sheria zetu, sera na jinsi tunavyofanya mambo vimebadilika sana katika miaka ya hivi karibuni.

Tunaendelea kulinda raia wasio na hatia wasishambuliwe wakati tunaendelea na jukumu letu la muda mrefu la kuheshimu haki za binadamu na uhuru wa msingi. Kama sehemu ya juhudi hizi, Marekani inawasilisha ripoti kwa vyombo vya kimataifa kwa mujibu wa jukumu lake chini ya mikataba mbalimbali ya haki za binadamu.

Kujenga demokrasia makini dunia nzima ni kazi ya zama na vizazi mbalimbali, lakini kila mara ni kazi ya dharura ambayo haiwezi kusubiri. Demokrasia yetu wenyewe inajizungusha. Safari ya Marekani kuelekea kwenye uhuru na haki kwa wote imekuwa ndefu na ngumu, lakini tunajivuna kwamba tunaendelea kufanya maendeleo muhimu, matawi huru ya serikali, vyombo vya habari huru, uwazi wetu kwa dunia, na muhimu zaidi uvumilivu wa kiraia wa wazalendo wa Marekani umesaidia kuweka imani na matakwa ya kuanzishwa kwa taifa na jukumu letu la kimataifa la haki za binadamu.

Januari 20, mwakani demokrasia yetu wenyewe itaadhimisha tukio la kihistoria – kuapishwa kwa Mmarekani wa kwanza mwenye asili ya Afrika kama Rais wa Marekani.

Martin Luther King, Jr., aliita tukio kama hilo "kutimiza ndoto nyingine isiyopata kutimizwa." Bado, tunatambua kwamba safari yetu ya kitaifa kuelekea kwenye umoja imara uliotabiriwa na waasisi wa taifa letu ni ndefu kuimaliza.

Njia ya demokrasia huwa si nzuri na mara nyingi haikunyooka, lakini ni ya uhakika. Njiani lazima kutakuwa na vizingiti na hata kukata tamaa. Mataifa mengine bado yana asasi dhaifu za serikali ya demokrasia na yanaendelea kuhangaika. Mengine yamejidhatiti kwa dhati kwenye demokrasia. Hatua za kusonga mbele zinaweza zikakwamishwa na mambo yasiyofaa. Kunaweza kuwa na kurudi nyuma kupita kiasi. Serikali zilizochaguliwa kwa njia ya kidemokrasi mara nyingi hazitawali kwa demokrasia zinapokuwa madarakani.

Mambo ya kuyazingatia kwa ajili ya kusonga mbele yako wazi: Wape raia uhuru mkubwa zaidi ili waweze kuutumia kwa ajili ya kusahihisha mapungufu yanayojitokeza ambayo yanakwamisha kuwapo kwa hali nzuri ya baadaye.

Katika dunia ya leo, matatizo yanayokabili mataifa ni nyeti hata kwa mataifa makubwa kuyakabili peke yake. Mchango wa asasi za kiraia, mawazo huru na habari katika kujadili matatizo ya kila nchi na ya kimataifa ni muhimu. Kuziwekea mpaka wa kisiasa asasi zisizokuwa za kiraia (NGO) na majadiliano ya umma ni vitendo ambavyo madhara yake ni kukwamisha maendeleo ya jamii yenyewe.

Katika kila eneo la dunia, kuna serikali ambazo zinaitikia miito ya kuwa na uhuru wa watu na wa kisiasa kwa kutowajibika kwa watu wao bali kuwanyanyasa wale wanaokuwa msitari wa mbele kupigania haki za binadamu na kuanika maonevu ya kila aina. Hivyo wananyanyasa asasi zisizokuwa za kiraia, vyombo huru vya habari ikiwa ni pamoja na intaneti.

Kwa asasi za kiraia na vyombo huru vya habari, uhuru wa kuzungumza, kukutana na watu na mkusanyiko wa amani ni oksijeni. Bila ya kuwa na vitu hivyo vya uhuru wa msingi, demokrasia inaminywa pumzi yake ya kupumua.

Cha kusikitisha ni kwamba baadhi ya serikali zinatumia madaraka vibaya dhidi ya NGOs, waandishi wa habari na wanaharakati wa vyama vingine vya kiraia.

Wakati demokrasia inapounga mkono kazi za wanaharakati wa haki za binadamu asasi za kiraia, tunawasaidia wanaume na wanawake katika nchi duniani kote kurekebisha mustakabali wao wenyewe katika uhuru. Na kwa kufanya hivyo, tunasaidia kujenga dunia nzuri zaidi na yenye usalama kwa watu wote. Lazima tuwalinde walindaji kwa sababu wao ni mawakala wa amani na mabadiliko ya demokrasia.

Kuna matakwa makubwa duniani yanayotaka kuwapo kwa uhuru mpana zaidi wa mtu na wa kisiasa kwa ajili ya kuwa na serikali yenye misingi ya demokrasia. Marekani inaunga mkono juhudi za wanaume na wanawake duniani kote kupata na kuonyesha haki zao.

Kuunga kwetu mkono kunaonyesha thamani kubwa ya watu wa Marekani. Kama Rais Bush alivyosema: "Uhuru ni haki ambayo haina mjadala wa kila mwanamume, mwanamke na mtoto na njia kuelekea kwenye amani ya kudumu katika dunia yetu ni uhuru."

Katika Marekani, tuko katika mchakato wetu wa demokrasia ya mpito wa kupata utawala mpya. Kazi ya Marekani ya kupigania uhuru duniani inazidi ile ya siasa zetu za ndani kwa sababu kuendelezwa kwa haki za binadamu na misingi ya demokrasia kuna thamani kubwa kwa wananchi wetu.

Utakapoingia madarakani utawala wa Barack Obama utakapoignai Januari hii, kazi hii muhimu ya uhuru wa binadamu itaendelea, itaimarishwa kwa kuungwa mkono na Bunge machachari lenye ushabiki wa masuala ya kimataifa na ya nyumbani kama ulivyo utamaduni wa watu wa Marekani.

Mwandishi wa makala hii, Mark Green, ni Balozi wa Marekani nchini Tanzania. Hii ni tafsiri isiyo rasmi ya makala yake ya Kiingereza kuhusu Haki za Binadamu ya kudhimisha siku ya Azimio la Haki za Binadamu lililotangazwa miaka 60 iliyopita.

Tuesday, December 2, 2008

Zitto: CCM ichunguzwe ilivyochota mapesa EPA


MBUNGE wa Kigoma Kaskazini (Chadema) mwenye ushawishi mkubwa nchini, Zitto Kabwe, anataka uchunguzi maalumu ufanywe na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu matumizi ya CCM wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ili ukweli wote ufahamike.

Sambamba na hilo, Zitto, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, amependekeza iundwe mahakama maalumu (Special Tribune) kwa ajili ya kesi zinazohusu Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) iliyopo katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Katika taarifa yake kwa Raia Mwema, Zitto anasema: "Njia pekee itakayowatoa CCM katika hili ni kwa wao kuruhusu uchunguzi maalumu kufanywa na CAG. Baada ya uchunguzi, Mkaguzi ataueleza umma CCM walitoa wapi fedha zao na walizitumia namna gani. Yeye pekee ndiye anayeweza kuwasafisha kama hawahusiki na fedha za EPA, na sio maneno ya baadhi ya viongozi wa CCM ya kujaribu kujitakasa."

Kwa mtazamo wa Zitto, kesi za Kisutu hazitaonyesha ukweli wote juu ya nini hasa kilitokea mwaka 2005 Benki Kuu. "Kesi ya Kisutu haitatuambia ukweli juu ya kikao cha baadhi ya viongozi wa CCM na Gavana wa Benki Kuu mara baada ya kugundua kuwa CCM hawakuwa na fedha za kutosha za kampeni baada ya Kikwete kuteuliwa kuwa mgombea wa CCM," anasema Zitto katika taarifa yake hiyo.

Zitto anasema: "Suluhisho nililonalo mimi ni kuundwa kwa mahakama maalumu (special tribunal) ambayo panelists wake watakuwa Watanzania waliotumikia nchi kwa uadilifu kama majaji wastaafu, wanasheria wakuu wastaafu, magavana wastaafu wa Benki Kuu au wakuu wa taasisi za umma wastaafu, wahadhiri waliobobea katika masuala ya fedha na sheria.”

Mbunge huyo amependekeza kuwa mahakama hiyo maalumu iundwe kwa sheria ya Bunge. “Mahakama hii iweke mazingira ambayo watu waitwe na kusema kweli, ukweli wote. Mahakama hiyo maalumu iwe na uwezo wa kutoa amnesty kwa watu ambao itaridhika na ushahidi wao na ushirikiano wao katika kufikia ukweli wa matatizo yote yanayohusu rushwa kubwa kubwa zilizopata kutokea hapa nchini.”

Kwa mtazamo wake, mahakama hiyo isiwe ya EPA tu, bali pamoja na masuala kama ya Meremeta, IPTL na Deep Green. “Iwe mahakama ambayo ikimaliza muda wake itatufanya, kama Taifa, tujiangalie na kusema haya yasitokee tena. Tusonge mbele."

Anasema Zitto: "Ndio maana nikiwaona hawa Watanzania waliofikishwa mahakamani na wale watakaofikishwa siku za usoni kuhusiana sakata la EPA, nafsi yangu inasema mahakama haitakata mzizi wa fitina. Kesi zitaenda, wenye kufungwa watafungwa, lakini hatutamaliza tatizo la EPA au tatizo kama hilo siku za usoni".
Anaamini kwamba hilo lisipofanyika, EPA itajirudia kwa njia mbali mbali na kwamba EPA haitaisha kwa judicial approach. "EPA itaisha kwa juhudi za pamoja za kimahakama na za kisiasa. Lazima kama nchi tufikie mahali na kusema haitatokea tena kwa chama chochote cha siasa au wanasiasa kutumia fedha za umma kwa manufaa yao kisiasa."

"Hatuwezi kuwa taifa ambalo kila siku tunajadili mambo yale yale na kurudia makosa yale yale. Hatuwezi kuwa Taifa ambalo vichwa vya habari vya magazeti vinapambwa na habari za ufisadi tu. Tunapaswa kutoka hapo kwa kusahihisha makosa, na kama tukifanya makosa mengine yawe makosa mapya," anasema mbunge huyo kijana.

Waziri Mkuu ni sahihi, achaneni na semina hizi !


MWANZONI mwa wiki iliyopita Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alisema kile ambacho tumekuwa tukikiamini kwa muda mrefu – kwamba idadi kubwa ya semina, warsha na makongamano yanayofanyika nchini yanalenga katika ulaji, na hayawasaidii wananchi wa kawaida; hususan wanavijiji.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wilayani Mpwapwa, Waziri Mkuu alisema kwamba ameshitushwa na kiasi kikubwa cha fedha ambacho wizara nyingi hutenga kwa ajili ya kuendesha semina, warsha na makongamano.

Lakini si tu kwamba Pinda aliishia katika kukemea uandaaji wa semina, warsha na makongamano hayo ya ulaji, lakini pia alisema kwamba kuanzia sasa hakuna wizara itakayoziandaa bila kwanza kupata kibali cha ofisi yake.

Tunapenda kumuunga mkono Waziri Mkuu kwa hatua hiyo sahihi aliyoichukua. Ingawa huko nyuma waliomtangulia walipata kukemea jambo hilo; lakini yeye amekwenda mbali zaidi kwa kuagiza kwamba semina, warsha na makongamano hayo yafanyike tu baada ya kupata kibali kutoka ofisi yake.

Tunadhani hiyo ni hatua murua itakayodhibiti ufanyaji holela wa semina, warsha na makongamano hayo ambayo, kama tulivyoeleza mwanzo, asilimia kubwa yanalenga katika ulaji na si kuwanufaisha walipa kodi wa nchi hii.

Kwa hakika, baadhi ya wizara zimekuwa zikirudia aina zile zile za semina, warsha na makongamano mwaka hadi mwaka. Matokeo yake ni kwamba makabati ya wizara hizo yamesheheni mada na maazimio ambayo hayafanyiwi kazi, na ndiyo maana tunasema kuwa hazina manufaa makubwa kwa walipa kodi wa nchi hii.

Ni matarajio yetu kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu itatoa vibali vya kufanya semina, warsha na makongamano hayo baada ya kufanyia maombi itakayopokea uchambuzi yakinifu na kuridhika kwamba mwisho wa yote kuna manufaa yatakayopatikana kwa kwa wananchi.

Tunamuunga mkono Waziri Mkuu tukitambua kuwa hatua hiyo ya kudhibiti warsha, semina na makongamano imekuja katika kipindi muafaka; kwani athari za anguko la uchumi wa dunia zimeshaanza kupiga hodi nchini mwetu.

Katika kipindi hiki cha anguko la uchumi wa dunia ambacho tunatarajia mapato ya Taifa ya nje na ndani kupungua kwa kiasi kikubwa, ni muhimu mno kwa Serikali yetu kuwa makini na matumizi yake ya pesa, kuwa makini na matumizi ya kila senti ya walipakodi nchini.

Ni matumaini yetu, hivyo basi, kwamba Waziri Mkuu Pinda, baada ya kuzishushia rungu semina, warsha na makongamano, pia ataangalia maeneo mengine yanayoteketeza fedha za Serikali na kuziba mianya hiyo haraka.

Mramba, Yona wasota rumande


MAWAZIRI wawili waandamizi wa Serikali ya Awamu ya Tatu iliyoongozwa na Rais Benjamin Mkapa, Basil Pesambili Mramba na Daniel Ndhira Yona, wamepandishwa kizimbani wakituhumiwa kutumia madaraka vibaya wakiwa madarakani.

Mramba na Yona wote kwa pamoja wameshitakiwa kwa kuibeba kampuni ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation ya Washington DC, Marekani ambayo ilikuwa ikifanya kazi ya uhakiki wa mapato ya madini ya dhahabu nchini.

Mawaziri hao wawili walisomewa mashitaka yao na waendesha mashitaka kutokaTaasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Hezron Mwankenja, kukiwa na ulinzi mkali wa makachero na askari magereza wenye silaha.

Pamoja na kutoa upendeleo wa kuongeza mkataba wa kampuni hiyo ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation, Mramba na Yona wakiwaWaziri wa Fedha na Waziri wa Nishati na Madini, waliisababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh. bilioni 11 kutokana na kusamehe kodi kampuni hiyo kinyume cha sheria.

Makosa hayo yameelezwa mahakamani hapo kutendwa katika kipindi cha mwaka 2002 na mwaka 2007, ambako Mramba aliandaa na kutoa matoleo ya Gazeti laSerikali (GN) yenye namba 423/2003, 424/2003, 497/2004, 498/2004, 377/2005 na 378/2005 ambayo yalilenga kutoa msamaha wa kodi kwa Alex Stewart (Assayers) Government BC uliofikia kiwango cha Sh 11, 752, 350, 148/- bila kuzingatia sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Kwa mamlaka yao na nafasi zao, Mramba na Yona wamedaiwa mahakamani hapokwamba bila kuzingatia wajibu wao waliokabidhiwa na serikali waliingia mkataba ulioisababishia serikali hasara ya Sh 11, 752, 350, 148/- kutokana na kampuni hiyo ya uhakiki wa dhahabu.

Imedaiwa kwamba Mramba kupitia matoleo mbalimbali ya Gazeti la Serikali amewezesha kutolewa kwa msamaha wa kodi ya mapato iliyopaswa kulipwa na kampuni hiyo ya Alex Stewart kinyume cha sheria ya Kodi ya Mapato.

Kwa mujibu wa maelezo ya waendesha mashitaka hao, Mramba anadaiwa alitumia vibaya madaraka yake kwa kudharau ushauri wa TRA waliomtaka kutokubali kutoa msamaha wa kodi ya mapato kwa kampuni hiyo ya kigeni ambayo ililalamikiwa sana kwa kumega mapato ya dhahabu nchini.

Mawaziri hao wa zamani wanatuhumiwa pia kudharau maelekezo ya kamati ya ushauri ya serikali ambayo ilipendekeza kupelekwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mkataba wa Alex Stewarts na badala yake waliongeza muda wa mkataba wa kampuni hiyo bila kuzingatia suala la kupitia upya ada iliyokuwa ikilipwa kwa kampuni hiyo na hivyo kuiingizia serikali hasara.

Katika kuongeza mkataba huo, Mramba na Yona wanadaiwa kutumia vibaya madaraka yao kwa kumshirikisha Dk. Enrique Segura wa Alex Stewarts katika kuingia naye mkataba wa nyongeza ya miaka miwili kuanzia Juni 14, 2005 hadi Juni 23, 2007 bila kuzingatia Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2002 na Sheria ya Madini ya mwaka 2002.

Mashitaka dhidi ya watuhumiwa hao yamefuatia kibali kilichotolewa na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) Elieza Feleshi kutoa kibali, juzi Jumatatu akisema kwamba viongozi hao waandamizi wametumia vibaya madaraka yao na wamesababisha hasara kwa mamlaka husika.

Watuhumiwa wote wawili walilazimika kupelekwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana ikiwa ni pamoja na kuwasilisha mahakamani fedha taslimu Sh. bilioni 3.9 kila mmoja, kwa kuzingatia kiwango cha fedha kilichopotea kwa makosa waliyoshitakiwa nayo.

Mramba na Yona walifikishwa Kisutu kwa gari maalumu la TAKUKURU aina ya Toyota Land Cruiser T319 ATD likisindikizwa na Toyota Rav 4 lenye namba T 528 AQQ likiwa na mawakili wa TAKUKURU na makachero huku kukiwa na magari mengine kadhaa yenye walinzi wa ziada.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi leo Desemba 2, 2008 itakapotajwa tena.

Raia Mwema
November 26, 2008

Friday, November 28, 2008

Tukemee Ukatili wa aina hii !


Mimba Mashuleni, nini chanzo? Jamii iwajibike kupambana na hali hii!

Thursday, November 27, 2008

UKATILI HUU DHIDI YA ALBINO UTAISHA LINI?

Pichani Mwajuma Hassan ambaye anaulemavu wa ngozi (ALBINO) akibubujikwa na machozi baada ya kuona mchoro wa msichana albino aliyekatwa mikono hivi karibuni. Mchoro huu ni mojawapo wa michoro mingi ambayo ipo katika banda la maonyessho ya maadhimisho ya siku 16 za uanaharakati zinazoazimishwa katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Tanzania(TGNP. Maonyesho hayo yanaendela mpaka tarehe 10 Desemba 2008, karibu ujionee michoro inyoeleza hali halisi ya ukatili wa kijinsia. Usisubiri kusimuliwa!


(Picha Kwa hisani ya The Guardian, 27/11/2008.)

KILA KITUO CHA POLISI KUWA NA DAWATI LA KUHUDUMIA WAHANGA WA UKATILI WA KIJINSIA

Jeshi la Polisi nchini limejiandaa kikamirifu kuanzisha dawati (chumba) maalum la kushughulikia makosa ya ukatili wa kijinsia nchini. Kwa majaribio, kuanzia mwezi ujao (Desemba, 2008) kila kituo cha polisi kanda maalum ya Dar es Salaam kutakuwa na dawati hilo, na baadae mwakani kwa vituo vyote nchini. Hayo yalisemwa na Katibu wa Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania, Kamishna wa Polisi Elice Mapunda, ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Maafisa wa Polisi Kurasini Dar es Salaam, wakati akitoa tamko la Jeshi la Polisi kuhusu ukatili wa kijinsia kwenye tamasha la kuadhimisha siku 16 za Uanaharakati wa kupambana na ukatili wa kijinsia. Tamasha hilo liliandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na kufanyika katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Mabibo, Dar es Salaam.

Aliwataka wananchi na hasa wanawake wasiwe na wasiwasi na wawe na imani na polisi. “Najua wanawake wamekata tamaa na jinsi askari walivyokuwa wanawa-treat (wanawahudumia) wakifanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia. Awali tulikuwa hatujui nini maana ya ukatili wa kijinsia, lakini kwa jitihada za Mtandao wa Wanawake Polisi na Mashirika ya Wanaharakati mbali mbali, Polisi karibu wote wamepata mafunzo ya kupambana na ukatili wa kijinsia, kwa sasa tunaongea lugha moja. Tutumieni, tushirikiane tuweza kupunguza na hatimaye kutokomeza kabisa vitendo hivi”, alisema Kamishna Mapunda.

Aliwakumbusha wanaharakati kuwa ni haki ya kila mmoja kuhudumiwa na polisi pale anapofanyiwa ukatili wa kijinsia, na kuwataka kuakikisha kuwa watumia fursa hiyo ipasavyo. Pia alikariri tamko la mgeni rasmi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Utawala Bora, Mheshmiwa Sophia Simba kuwa mapambano ya kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia ni jukumu la jamii nzima. “Ukatili wa kijinsia ni suala la jamii nzima, si la mtu mmoja mmoja. Hivyo ili tuweze kutokemeza vitendo hivyo lazima jamii nzima tushirikiane. Polisi hawatoshi, jeshi lina takiribani polisi elfu thelathini na idadi ya watanzania ni takribani milioni arobaini kwa sasa; ambayo ni uwiano wa askari mmoja kwa watu mia nne hamsini!. Jamii nzima lazima ipambane” alisisitiza kikamanda.

Kamishna Mapunda alimalizia kwa kutoa changamoto kuwa kuwepo na dawati la kuhudumia wahanga wa ukatili wa kijinsia katika kila kituo cha polisi sio dawa, bali jamii bado inatakiwa kuelimishwa na kuamasishwa ili iweze kuona kuwa suala la ukatili wa kijinsia halifai na halina nafasi katika jamii yetu.

Tamko hilo lilipokelewa kwa furaha na mamia ya wanaharakati walioudhuria maadhimisho hayo kutoka mikoa yote ya Tanzania.

Wednesday, November 26, 2008

Pinga Ubakaji kwa Wanawake na Watoto


Wanawake na watoto wataendelea kubakwa mpaka lini? Usikae kimya, hakikisha sheria inachukua mkondo wake!

Tuesday, November 25, 2008

KONGAMANO KONGAMANO KONGAMANO

KATIKA KUADHIMISHA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA NCHINI TANZANIA NA MIAKA SITINI TANGU KUTOLEWA KWA TAMKO LA DUNIA LA HAKI ZA BINADAMU, MTANDAO WA JINSIA TANZANIA (TGNP), KWA KUSHIRIKIANA NA MASHIRIKA YANAYOTETEA MASUALA YA KIJINSIA, HAKI ZA BINADAMU NA UKOMBOZI WA MWANAMKE KIMAPINDUZI YAANI FEMACT, WAMEANDAA KONGAMANO KUBWA LITAKALOJADILI HATUA AMBAZO TANZANIA IMEFIKIA KATIKA KAMPENI YA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA NA JUU YA NINI KIFANYIKE KUBORESHA HALI ILIVYO SASA

KAULI MBIU YA MWAKA HUU NI: SISI KAMA JAMII TUNA UWEZO NA NIA YA KUZUIA UKATILI WA KIJINSIA

JOPO LA WAZUNGUMZAJI:
- TAMWA
- WLAC
- WOFATA
- KIWOHEDE / HOUSE OF PEACE
- WD
- TGNP

LINI: Jumatano Tarehe 26 Novemba 2008

Muda: Saa 8:00 Mchana – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo
Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni



WOTE MNAKARIBISHWA!!

Monday, November 24, 2008

AJIRA KWA VIJANA MUHIMU BARANI AFRIKA- JK

Jakaya Mrisho Kikwete amesema Mahitaji ya ajira kwa vijana ni makubwa zaidi katika nchi za Afrika , hivyo suala la kutengeneza ajira kwa vijana hao ni changamoto kubwa ya maendeleo inayolikabili Bara hilo na dunia kwa ujumla hivi sasa.

Rais kikwete ameyasema hayo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Afrika uliofanyika kwa siku moja tarehe 20 Novemba, 2008 Addis Ababa nchini Ethiopia ambao Mwenyekiti wake alikuwa Bwana Anders Fogh Rasmussen ambaye ni waziri Mkuu wa Denmark.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha Rose-Migiro.

Akifungua rasmi Mkutano huo uliofanyika katika Hoteli ya Sheraton Addis, Bwana Rasmussen amesema ajira ndiyo injini muhimu kwa maendeleo ya Bara la afrika na kwamba ongezeko la idadi ya vijana linawakilisha fursa pekee kwa Bara hilo ambayo inatakiwa kutumiwa kikamilifu katika harakati za kuleta maendeleo.

Amesema hatua madhubuti zinatakiwa kuchukuliwa ili kutoa msukumo katika kutekeleza Maendeleo ya Milenia (MDGs).Aidha amesema ukuaji wa uchumi hauna budi kuwanufaisha raia wote na ndiyo maana jitihada za Tume zimelenga, pamoja na mambo mengine, katika masuala ya ajira.
Kwa upande wake, Rais Kikwete amesema kwa zaidi ya asilimia 89 ya vijana duniani wanaishi katika nchi zinazoendelea na kwamba idadi ya vijana wanaoishi katika nchi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara ni asilimia 13 ya vijana wote duniani.

Amesema ajira kwa vijana zinahitaji ongezeko kubwa la uzalishaji na utengenezaji wa fursa zaidi za ajira kwa kuongeza kiwango cha uwekezaji wenye tija zaidi.

Ameainisha mambo muhimu katika kukabiliana na tatizo la ajira kuwa ni pamoja na utekelezaji wa dhana ya ushindani, ukuaji wa uchumi, ujasiriamali, maendeleo katika biashara pamoja na maendeleo ya elimu, mafunzo na ujuzi.

Mambo mengine ni uwezeshaji na kuwepo kwa fursa za kupata mikopo na kutumia vema fursa za sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano. Amesema ujasiriamali unatoa fursa kubwa zaidi za ajira kwa vijana na wanawake na hivyo kupunguza kiwango cha umaskini.

Hata hivyo amesema changamoto zilizopo ni namna ya kuwawezesha vijana kuwa wajasiriamali kati ya mamilioni ya vijana waliopo ambao kwa sasa hawana ajira, namna ya kuwasaidia wale ambao tayari wameanzisha biashara zao na namna ya kuwafanya wajasiriamali wadogo kukua hadi kufikia ngazi ya kati ya ujasiriamali.

Amevitaja vikwazo viwili vikubwa vya ujasiriamali kuwa ni kukosekana kwa ujuzi wa ujasiriamali na uhaba wa fursa za kupata mitaji.

Wednesday, November 19, 2008

EPA: Kama vile mchezo wa kuigiza

Baadhi ya watuhumiwa walalamika wanasiasa kuwatosa

WAKATI baadhi ya watuhumiwa wakiwa wamekwisha kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa fedha katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) ndani yaBenki Kuu (BoT), mbinu chafu zilizotumika na vigogo katika kuchota mabilioni ya fedha katika akaunti hiyo sasa zimebainika.

Mbinu hizo ni pamoja na kughushi nyaraka mbalimbali na kutumia kivuli cha siasa katika kupitisha nyaraka husika bila kufanyika kwa uhakiki wa kina wa uhalali wa nyaraka hizo, kazi iliyofanyika kwa kasi iliyowashangaza hata wakaguzi wazalendo na wale wa kimataifa waliopitia hesabu za BoT.

Mfano wa dhahiri uliotolewa tokea mwanzo ni ule wa kampuni ya Kagoda Agricultural Limited, ambayo ilithibishwa tokea mwanzo jinsi vigogo walivyoghushi nyaraka za kampuni 12 za kigeni kuweza kujichotea kiasi cha Sh bilioni 40.

Katika mchakato huo, Kagoda ilighushi nyaraka mbalimbali kuweza kujichotea kiasi cha Dola za Marekani 30,732,658.82 (takriban Sh bilioni 40), ikiwa ni pamoja na nyaraka hizo kupitishwa na maofisa wa BoT bila kufanyiwa uhakiki.

Waliowasha moto wa wizi huo walikuwa ni wakaguzi wa kimataifa wa kampuni ya Deloitte & Touche, ambao walitimuliwa na serikali baada ya kutokea kutokuelewana katika ukaguzi wa akaunti hiyo ambayo sasa inazidi kuisakama Serikali.

Deloitte & Touche, ambayo ilipewa kazi ya kukagua akaunti za BoT, ilikumbana na utata mkubwa katika akaunti ya EPA namba 99915091 01, na hivyo kuwa kiashirio cha kwanza cha utata mkubwa katika akaunti hiyo.

Maelezo yaliyoibua utata huo yanaonyesha kwamba aliyekuwa Gavana wa BoT, Marehemu Dk. Daudi Ballali, alianza kujulishwa mapema kuhusiana na wizi huo akipewa mfano wa dhahiri jinsi Kagoda Agriculture Limited ilivyoghushi nyaraka.

Mfano uliotolewa kudhihirisha uhalifu huo ni jinsi ambavyo mikataba ya ununuzi wa madeni kwa kampuni 12 ilivyosainiwa katika kipindi kifupi cha kati ya Septemba 10, 2005 na Novemba 5, 2005, kipindi ambacho kilielezwa kuwa ni vigumu kwa wahusika kutembelea mbalimbali duniani kutiliana saini.

Aidha, imefahamika kwamba nyaraka zote zilisainiwa na wakili mmoja tu B.M. Sanze, na kati ya hizo mikataba minne ilisainiwa Oktoba 18, 2005 na mitano ilisainiwa siku moja baadaye Oktoba 19, 2005, jambo ambalo lilitia shaka jinsi wawakilishi wa kampuni hizo za kigeni walivyoweza kusafiri kwa wakati mmoja wakitofautiana kwa saa chache, jambo ambalo lilishindwa kuthibitishwa kwa kutumia kumbukumbu za Uhamiaji.

Katika nyaraka hizo, mikataba miwili iliyosainiwa Oktoba 18, 2005 kuhusiana na kampuni mbili za Ujerumani, Lindeteves J Export BV na Hoechst ikionyesha kwamba kulikuwa na deni la Euro 1,164,402.76 badala ya fedha za Ujerumani (Deutsche Marks.)

Wachunguzi na wakaguzi wameshitushwa na kasi ya ajabu ya jinsi marekebisho ya makosa hayo yalivyofanyika kwa kipindi kifupi baada ya BoT kuifahamisha Kagoda Agriculture Limited; huku barua ya kutaka marekebisho yafanyike ikiwa na maelekezo ya kuidhinisha malipo ya Sh 8,196,673,600.53 kwenda kwenye akaunti ya Kagoda. Kampuni hiyo iliwasilisha mkataba uliorekebishwa siku mbili tu baada ya kujulishwa.

"Haiwezekani hata kidogo kwa kampuni ya kigeni inayodai kuandika fedha zisizo sahihi huku BoT ikiendelea kuidhinisha malipo bila kuhakiki mikataba yote 12 ambayo imeonekana kufanana kwa kila kitu ikiwa ni pamoja na maneno," inaeleza sehemu ya waraka wa wakaguzi.

Pamoja na kubainika kuwa mikataba na nyaraka zote hazikuwa na nembo ya kampuni huusika, nyaraka zote zilisainiwa katika ukurasa mmoja pekee wa mwisho tofauti na nyaraka za kisheria zinavyopasa kuwa.

Uchunguzi wa kina umebaini kufanana kwa mihuri ya kampuni zote zilizopitishwa ikiwa inalandana kabisa na muhuri wa kampuni za Kitanzania, tofauti ikiwa ni majina na anuani ya kampuni husika.

Mfano uliotolewa ni wa kampuni za Kitaliano za Fiat Veicoli Industriali na Adriano Gardella S.P.A pamoja na kampuni ya Kimarekani ya Valmet ambazo zote zimeonekana kuwa na mihuri na lugha zilizofanana katika nyaraka zote.

Utata mwingine uliodhihirika kughushi ni katika mkataba wa kampuni ya Valmet ya Marekani uliohusu Dola za Marekani 2,398,439.96 kusainiwa na Patrick Kevin, aliyetajwa kuwa Mhasibu wa kampuni hiyo, jambo ambalo limeelezwa kwamba ingekuwa vigumu kwa mhasibu kuachiwa kufanya kazi hiyo.

Utata mwingine uliobainika ni katika mkataba wa kampuni ya Daimler Benz AG ambao ulionyesha kusainiwa na Mkurugenzi aliyetajwa kwa jina la Christopher Williams, huku sahihi yake ikisomeka 'W Christopher'.

Uchunguzi wa ziada ulithibitisha kwamba baadhi ya kampuni zilikwishakufa wakati mikataba hiyo ikisainiwa na kampuni za Kitanzania, jambo ambalo linaendelea kuthibitisha wizi mkubwa wa kutumia maandishi uliofanywa katika akaunti ya EPA.

Mifano hai ni kampuni za Hoechst AG iliyobadilika na kuwa Aventis mwaka 1999, Daimler Benz AG iliyobadilika na kuwa Daimler Chrysler AG mwaka 1998 na Fiat Veicoli Industriali iliyobadilishwa na kuwa Industrial Vehicle Corporation (IVECO) tokea Januar1 1, 1975.

Kampuni nyingine zilizobadilika ni Mirrlees Blackstone kuwa MAN B&W Diesel Limited mwaka 2002/03 na Valmet iliyobadilishwa na kuwa Metso Paper kuanzia Mei 10, 2000. Utata huo uliwafanya wachunguzi na wakaguzi kujiuliza ilikuwaje kampuni zote hizo kuingia mikataba mwaka 2005 kwa kutumia majina ya zamani.

Pamoja na kuingiwa kwa mikataba hiyo na kampuni zilizokwisha badilishwa majina na umiliki wake, kampuni za sasa zenye uhusiano na kampuni zilizoingia mkataba zimekanusha kufahamu watu waliotajwa kuziwakilisha katika mikataba hiyo.

Kagoda ambayo ilisajiliwa Septemba 29, 2005, na kujichotea Sh bilioni 40 katika kipindi cha mwezi mmoja tu, jambo ambalo limewashangaza wengi kuona kampuni ngeni isiyofahamika inawezaje kuaminiwa kiasi kikubwa cha fedha bila kuhakikiwa.

"Inashangaza jinsi BoT ilivyoweza kuamini kampuni mpya kuwasilisha nyaraka za mabilioni ya fedha kwa kuingia makubaliano na kampuni za kigeni katika nchi za Ujerumani, Italia, Yugoslavia, Uingereza, Marekani na Japan kwa muda mfupi kiasi hicho bila kutilia shaka," wamehoji wakaguzi waliokagua hesabu za BoT.

Tayari kampuni ya Kagoda Agricultural Limited imekuwa gumzo katika sakata zima la EPA. Inafahamika kwamba kati ya shilingi bilioni 90 zilizoibwa katika akaunti ya EPA, sehemu kubwa ilichukuliwa na kampuni ya Kagoda Agricultural Limited ambayo hadi sasa wahusika wake hawajaguswa pamoja na kujitokeza kwa vigogo wawili kurejesha fedha zilizoibwa na kampuni hiyo.

Vyanzo vya uhakika vinaeleza kwamba sehemu kubwa ya Shilingi bilioni 90 zilizothibitika kuchukuliwa kihalifu zilichukuliwa na makundi mawili tu, kundi la kwanza likiwa chini ya Jeetu Patel na lingine likiwa chini ya usimamizi wa vigogo wawili waliotumia kampuni ya Kagoda.

Imefahamika kwamba kwa sasa kuna hekaheka kubwa za kutaka kuzuia kushitakiwa kwa wahusika wa Kagoda, lakini vyanzo vya ndani ya Serikali vimeeleza kwamba kwa sasa Serikali haitabiriki na lolote linaweza kutokea wakati wowote kabla ya mwisho wa mwaka.

Kumekuwa na utata kuhusiana na ilipo na umiliki wa Kagoda Agricultural Limited. Hakuna anayeweza kubainisha hasa zilipo ofisi na wahusika wa kampuni hiyo tata.

Kumbukumbu za BRELA zinaonyesha kwamba ofisi zake zipo Kipawa Industrial Area Plot namba 87, Temeke, Dar es Salaam lakini eneo hilo lina makampuni tofauti jirani lakini namba iliyotajwa haionekani na badala yake eneo lenye ofisi na kampuni viwanja vyenye namba 77, 86 na 88 katika eneo hilo la viwanda.

Katika ukaguzi wake wa awali wa mkaguzi wa nje Samuel Sithole kutoka kampuni ya Kimataifa ya Deloitte & Touche yenye makao yake Afrika Kusini alionya kuhusu matendo ya kihalifu ndani ya Kagoda kabla ya kuandikiwa barua na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji kwamba fedha hizo zilienda katika mambo "nyeti" ya kiusalama.

Hata hivyo siku nne baada ya kuandika barua hiyo, Meghji alifuta barua hiyo akielezea kupotoshwa na aliyekua Gavana, Dk. Daudi Ballali, uamuzi ambao ulimgharimu kwa kiasi kikubwa mwanamama huyo makini ambaye alijikuta akiachwa nje ya Baraza la Mawaziri.

Wakati Rais Jakaya Kikwete akisema serikali yake haitomuingilia Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), watuhumiwa wengi walikamatwa na kufikishwa mahakamani walikuwa wamejiaminisha kuwa wamekwishapona na sasa waliobaki "hawalali" kuhofia kushitukizwa na kupandishwa kizimbani.

Tayari watu 20 wamekwisha kufikishwa mahakamani baada ya wafanyabiashara watatu kufikishwa mahakamani Jumatatu wiki hii wakitanguliwa na watuhumiwa wengine wakiwamo watumishi wa BoT waliohusika katika mchakato wa wizi huo.

Waliopandishwa kizimbani ni Ajay Somani na Jai Somani wanaodaiwa kula njama ya wizi wakiwa na watu wengine ambao hawajafahamika kuiibia BoT na kwamba Septemba 2, 2005 waliiba Sh. bilioni 5.9 mali ya benki hiyo.

Mtuhumiwa mwingine aliyefikishwa mahamani ni mfanyabiashara Mwesiga Lukaza, aliyepandishwa kizimbani akiunganishwa na mshtakiwa mwingine Johnson Lukaza, ambaye alishapandishwa kizimbani mapema wiki hii.

Watuhumiwa wengine ambao tayari wamefikishwa mahakamani ni Farijala Hussein, Rajab Maranda, Japhet Lema, Bahati Mahenge, Davis Kamungu, Godfrey Mosha, Manase Mwakale na Eddah Mwakale, Devendra Vinodbhai Patel, Amit Nandy, Ketan Chohan, Jayantkumar Chandubahi Patel na Johnson Lukaza.

Wengine ni wafanyakazi wa BoT ambao ni Mkuu wa Idara ya Madeni ya Biashara, Iman David Mwakyosa, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Madeni, Ester Mary Komu na makaimu Katibu wa benki wawili ambao ni Bosco Ndimbo Kimela na Sofia Joseph Lakila.

Raia Mwema
November 19, 2008

Monday, November 17, 2008

Policy and Budget Analysis training

TGNP through ALC is conducting a training on policy and budget analysis for its partners and stakeholders (IGNs Networks/Movement Building Groups and GDSS). The training will be conducted for four days between 17th - 18th and 20th- 21st November 2008 at TGNP Mabibo Dar Es Salaam from 8.30 am.

The objectives of this session are:

-To share key gender/transformative feminist issues in policy and budgeting

-Enhance participants on policy and budget analysis from Transformative Feminist outlook

-To share tools of analysis with participants to be used in their own areas

-To share experiences/information and Networking

We are banking on your collective collaborations in organizing for this training.

Monday, November 10, 2008

Mrejesho wa Semina ya GDSS ya Tarehe 05/11/2008.

Mrejesho wa Semina ya GDSS ya Tarehe 05/11/2008.

Mada katika semina ya Jumatano ya tarehe 05/11/2006 ilikuwa ni, Mrejesho wa Wanaharakati kutoka katika vikundi mbalimbali ambao walikwenda kufuatilia kero zilizopo katika maeneo yao. Vikundi ambavyo vilifanikiwa kutoa mrejesho ni pamoja na; Kigamboni clusters, Kigogo, Makuburi, Mwananyamala, Kinondoni, na Kawe.

Baadhi ya Kero ambazo zilitajwa na wanaharakati wengi ni pamoja na;

- Haki ya kushiriki katika ngazi mbalimbali za maamuzi hasa ngazi ya Kata na Serikali ya mtaa. Katika Maeneo mengi bado wananchi hawapati fursa ya kushiriki katika vikao vya serikali za mitaa, hivyo kushindwa kufuatilia ama kutoa maamuzi ya mambo mbalimbali ya maendeleo katika maeneo hayo.

- Haki ya kupata maji safi na salama. Bado katika maeneo mengi jijini Dar es Salaam maji safi na salama limekuwa ni tatizo sugu, wakazi wengi bado hawapati maji safi na salama ya kunywa na ya matumizi ya kawaida, hivyo wanawake wamekuwa wakitumia muda mwingi kutafuta maji maeneo ya mbali hivyo kuwazidishia mzigo wa kazi wanawake.

- Haki ya kuendelea na masomo kwa watoto wa kike wanaopata mimba wakiwa shuleni. Bado watoto wanaopata mimba wakiwa mashuleni hawaruhusuwi kuendelea na masomo, kitu ambacho kinawanyima haki watoto wa kike kuendela na masomo. Pia wahalifu wanaowapa mimba watoto wa kike hawachukuliwi hatua kali za kisheria kitu ambacho kinaongeza wigo wa tatizo hili.

- Rushwa katika vituo vya polisi na ukatili wa kijinsia. Katika baadhi ya vituo vya polisi hapa nchini vimekuwa vikituhumiwa kwa vitendo vya rushwa; ambapo askari wanawadai rushwa watuhumiwa wa kesi mbalimbali na kusababisha kupindishwa kwa haki za wadai. Pia askari wa wanaume wamekuwa wakilalamikiwa kwa kuwatendea watuhumiwa wanawake vitendo vya unyanyasaji wakijinisa kwa kuwadai rushwa ya ngono.

- Ajira kwa watoto wa kike hasa wale wanaoachishwa shule ili waende kutumika katika kazi za ndani, katika mabaa, ama katika madanguro.

Changamoto.
Harakati hizi za kutatua kero za wananchi zinakabiliwa na changamoto zifuatazo;

- Changamoto kubwa iliyopo ni kuweza kuunganisha nguvu ya pamoja ya wanaharakati katika ufuatiliaji kero mbalimbali, kwa mfano wanaharakati wameshindwa kuunganisha nguvu za pamoja katika kudai maswala mbalimbali ya kijamii, jambo ambalo limesababisha nguvu nyingi kupotea inapotokea vikundi viwili ama zaidi kupigania swala moja na kuacha sekta zingine bila utetezi.

- Kukosekana kwa mbinu shirikishi katika ufuatiliaji wa mambo mbalimbali katika ngazi ya mtaa, jambo amblo limesababisha wanaharakati kufanya kazi pekee yao badala ya kuwatumia wanajamii hivyo kuweza kuongeza ushiriki mkubwa zaidi katika kufuatilia mambo. Pia hii itasaidia jamii kudai mambo ambayo wanahisi wanayahitaji zaidi kuliko wanaharakati kupambana pekee yao.

- Changamoto nyingine kwa wanaharakati ni katika kutambua kiini cha tatizo ambacho kinasababisha kuwepo kwa kero nyingi katika jamii. Kwa mfano badala ya wanaharakati kupambana na huduma mbovu za afya hasa katika swala la afya ya uzazi kwa kuwatupia mpira waauguzi wa afya pekee na kuacha mfumo mzima ambao unasababisha huduma ziwe mbaya, kwa mfano kuna hospitali zina waaguzi wawili wa afya na wanahudumia zaidi ya wazazi 50 kwa siku, kwa hali hiyo lazima huduma itakuwa si nzuri. Hivyo changamoto kwa wanaharakti ni kuongeza wigo wa mapambano na kuungalia kiini halisi cha tatizo.

Mwanaharakati unafanya nini cha ziada kuhakikisha kwamba serikali inatatua kero hizi? Kwa maoni yako, Serikali imefanya vya kutosha katika kutatua kero hizi?

Monday, November 3, 2008

Tunataka haki, si kafara za kisiasa

WIKI na miezi imepita, na sasa umepita ule muda ambao Rais Jakaya Kikwete aliwapa mafisadi waliokwiba fedha za umma za EPA, kuzirejesha.

Wakati akilihutubia Bunge, mjini Dodoma, Agosti 21, 2008, Rais Kikwete aliiongezea muda kamati yake maalumu inayochunguza wizi huo na kuipa hadi Oktoba 31 kuikamilisha kazi hiyo; hatua iliyolenga kuwapa mafisadi hao fursa nyingine ya kurejesha fedha hizo na mpaka hivi juzi wakati akilihutubia taifa katika utaratibu wake wa wa kila mwezi aliueleza umma wa watanzania kuwa muda aliowapa wanaotuhumiwa kuiba fedha hizo wazirudishe baadadhi yao hawajafanya hivyo na kusema ambao hawajarejesha watafikishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa.

Tulipata kusema huko nyuma, na hatuoni haya kurudia kusema tena na tena; kwamba haki haipo katika kurejeshwa kwa fedha hizo; bali ipo katika kuwachukulia hatua za kisheria wezi hao.

Tulisema huko nyuma na tunasisitiza kusema tena kwamba Serikali itakuwa haisimamii haki kama itaacha kuwafikisha mafisadi hao mahakamani; eti kwavile tu wamerejesha pesa walizoiba.

Na kama ndivyo itakavyotokea hiyo Novemba mosi; yaani mafisadi waliorejesha fedha hizo kutoshitakiwa, basi, ingekuwa vyema pia kwa Serikali kuwatangazia msamaha wezi wote wa pesa za umma walioko vifungoni kama nao watarejesha fedha walizokwiba.

Maana; hatuwezi kukubali kuiachia nchi yetu kuwa na sheria mbili – moja kwa wanyonge na nyingine kwa vigogo na mafisadi. Kwa usalama na amani yetu sote na ya wanetu, ni lazima tuendelee kujenga nchi ambayo raia wote ni sawa mbele ya sheria.

Aidha, wananchi walitarajia kwamba mafisadi walioghushi na kuiba fedha za EPA watakaofikishwa mahakamani, ni vigogo hasa wa wizi huo wa pesa za umma, na si watu waliotafutwa kutolewa kafara za kisiasa; ilhali vigogo wenyewe wa ufisadi wa EPA wamefichwa nyuma ya pazia.

Labda tumkumbushe tena Rais wetu, Jakaya Kikwete kwamba wizi huo wa kihistoria wa pesa za EPA, umemweka yeye binafsi katika majaribu makubwa.

Wizi huo wa EPA ni mtihani mkubwa ambao Rais anapaswa kuuvuka kwa kutenda haki, na hiyo ni kama hataki wananchi waendelee kupoteza imani na namna anavyoiendesha vita dhidi ya ufisadi nchini.

Yeye mwenyewe Rais ni shuhuda, wakati wa ziara zake mikoani, jinsi wananchi wanavyoilalamikia kero hiyo ya kushamiri kwa ufisadi nchini. Wasiwasi wetu ni kwamba kama atashindwa kuchukua hatua za kuridhisha dhidi ya wahusika, atapoteza imani ya wananchi wake, na wakati mwingine itadhaniwa kuwa kuna kundi la mafisadi nchini ambalo “halishikiki”.

Na ili hilo lisitokee, ni vyema basi, kwa Rais Kikwete kujipa ujasiri wa hali ya juu na kuwafikisha mafisadi wote wa EPA mahakamani; bila kujali walirejesha fedha walizoiba au la, na bila kujali ni wafadhili au si wafadhili wa chama chake CCM.

Thursday, October 30, 2008

Mfululizo wa Semina za GDSS.

Mada ya Jumatano hii ya tarehe 29/10/2008 ilikuwa ni mrejesho wa Mwenge wa Kampeni ya Lengo la Tatu la Milenia: Kupunguza Vifo Vya Watoto wachanga na akina Mama Wajawazito. Mapema mwaka huu FemAct walikabidhiwa mwenge kama ishara ya kupewa jukumu la kuhakikisha utekelezaji wa Lengo la Tatu la Millenia.

Wawasilishaji wakuu walikuwa ni dada Jesca Mkuchu(Pichani) Mwenyekiti wa FemAct na Ussu Mallya- Mkurugenzi wa TGNP. Lengo la Mrejesho huu ni; kukabidhi mwenge kwa wanaharakati na kupata fursa ya kutandaa na kupashana habari zaidi juu ya utekelezaji wa lengo la namba tatu la malengo ya millenia.

Katika kufanya uchambuzi yakinifu wanaharakati walinabaini kuwa lengo hilo la millenia linakabiliwa na changamato kadhaa wa kadha baadhi ni kama zifuatazo: Lengo hilo lina ufinyu wa dira, kwa sababu halilengi kumkomboa mwanamke katika kila nyanja, pili Malengo haya hajatilia mkazo maazimio ya Beijing ya mwaka 1995, kwa sababu katika maazimio Kumi na mbili ya Beijing ni azimio moja tu ndio lililochukuliwa.

Wanaharakati waliangalia uwezekano wa serikali yetu kutimiza malengo hayo kabla ifikapo mwaka 2015 kama ilivyoahidiwa, na kujaribu kuangali ni kwa kiasi gani malengo hayo yamekamilishwa.

Dada Halima Mselem kutoka TAMWA aliangalia uwezo wa serikali katika kudhibiti unyanyasaji wa kijinsia na upatikanaji wa haki sawa katika elimu kati ya watoto wa kike na wakiume. Na alishauri pawepo na mpango maalumu wa serikali wa kutenga fedha kwa ajili ya kukomesha unyanyasaji wa kijinsia.

Dada Jonoveva Katto kutoka TAWALA, yeye aliangalia utekelezaji wa lengo la tatu hasa katika upande wa sheria, ambapo alitanabaisha vipengele kadhaa vya sheria ambavyo bado vinaendeleza ukandamizaji kwa wanawake. Sheria hizo ni zile za Mirathi, kwa mfano, sheria ya mirathi ya kimila ya mwaka 1963 hamruhusu mwanamke kurithi na kumiliki mali. Na sheria ya ndoa ya mwaka 1971, kifungu cha 60, kinaeleza wazi kwamba mali zinazopatikana katika ndoa zinapaswa kuandikishwa kwa jina la mwanaume, sheria hii mara nyingi huleta msuguano hasa pale mwanaume anapoamua kuoa mke mwengine na kumfukuza mwanamke bila kumpa kitu chochote walichochuma wote.

Dada Festa Andrew kutoka UTU Mwanamke yeye aliongelea juu ya hali ya afya ya Uzazi ambapo alitabanaisha kwamba hali bado si nzuri nchini Tanzania ambapo kwa wastani kila baada ya lisaa limoja mwanamke mmoja mazazi anafariki dunia kutokana na matatizo ya uzazi salama. Hivyo bado kuna haja ya wanaharakati kuendelea kuisisitiza serikali kuongeza fedha zaidi katika swala hili la afya ya uzazi, tofauti na ahadi za sasa za wanasiasa ambazo zinaendeleza kuleta madhara kwa wazazi.

Changamato kwa wanaharakati ni pamoja na kuishinikiza serikali ili iweze kuongeza nguvu na kutekeleza makubaliano ya lengo la tatu la milenia kama lilivyoafikiwa na wakuu wa maataifa 189. Kwa sasa bado serikali inasusua katika utekelezaji wa lengo hilo kutokana na kutoa kipaumbele kidogo katika sekta hiyo.

Je Wanaharakati wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba lengo hili la tatu linafanikiwa kwa wakati husika? Je, takwimu zinazotolewa na maofisa wa serikali zina ukweli ndani yake? Nini kifanyike ili kuboresha kampeni hii ya utekelezaji wa lengo la tatu la millenia?

Monday, October 27, 2008

MWENGE WA KAMPENI YA LENGO LA TATU LA MILENIA, KUPUNGUZA VIFO VYA AKINAMAMA WAJAWAZITO NA WATOTO WACHANGA

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS)

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO AMBAPO WIKI HII JESCA MKUCHU MWENYEKITI WA FemAct NA USU MALYA MKURUGENZI WA TGNP WATAWASILSHA MREJESHO KUHUSU:

MWENGE WA KAMPENI YA LENGO LA TATU LA MILENIA: Kupunguza vifo vya Watoto Wachanga na Kina Mama Wajawazito

LINI: Jumatano Tarehe 29 Oktoba 20

Muda: Saa 9:00 – 11:00 Jioni


MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo

Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni


Tafadhali dhibitisha ushiriki wako kupitia
info@tgnp.org



KARIBUNI SANA !!!!!!

Friday, October 24, 2008

Mrejesho wa Semina za kila Jumatano (GDSS): Ushawishi na Utetezi

Idadi ya washiriki ilikuwa 128 kati yao wanawake walikuwa 72 na wanaume 56 kutoka sehemu tofauti kama vile Asasi za kiraia, vikundi vya kujitolea kupambana na maambukizi ya Ukimwi na VVU, wanafunzi kutoka taasisi za elimu ya juu, waandishi wa habari, FemAct, taasisi za walemavu, makundi maalumu na jamii kwa ujumla.

Kwa kuongozwa na mtoa mada (Anna Sangai), washiriki walijadili maana, mikakati / nyenzo, aina, madhumuni na taratibu katika ushawishi na utetezi ili kushawishi watunga sera na watekelezaji kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii iliyokandamizwa kwa kubadilisha sheria na kanuni.

Mada kuu mbili (mikakati na nyezo) zilijadiliwa kwa kina na kuwekwa bayana kutokana na umuhimu wake katika ushawishi na utetezi

Kuhusu mikakati, mtoa mada alikubaliana wazi kuwa lazima kuwepo dira ili kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii. Ili kukabiliana na changamoto kutoka kwa watunga sera na watekelezaji, yafuatayo lazima yazingatiwe: - Ufahamu / Elimu ya sheria, sera na mipango lazima vizingatiwe ili kufikia na kutekeleza mchakato mzima wa ushawishi na utetezi.

Kuhusu nyenzo, mtoa mada aliainisha njia tofauti kama vile mawasilianao ya nje na ndani kwa wadau wenyewe, elimu kwa makundi yanayostahili, jamii kuwa na ufahamu wa elimu, sanaa na michezo bila kusahau vyombo vya habari.

Mtoa mada aliendelea kuhafiki kwamba njia zote zilizotajwa na nyingine nyingi zinaweza kutumika kusaidia kupinga aina yoyote ya ukandamizaji.

Washiriki walipewa nafasi ya kujadili katika makundi, zikachaguliwa mada tano (5) ili kutathmini kiwango cha uelewa wa suala la ushawishi na utetezi. Mada zilizochaguliwa ni:- Ukimwi na VVU, Afya ya uzazi, Maji, Elimu na Unyanyasaji wa kijinsia.

Mwezeshaji na makundi yote kwa pamoja yalihitimisha kwa kupendekeza kuchagua ujumbe mbalimbali na kuwasilisha kwa mwezeshaji kwa kuupitia na kisha kupeleka kwenye vyombo vya habari kama njia mojawapo ya ushawishi na utetezi ili kuleta mabadiliko ya kweli.

Thursday, October 23, 2008

Mwalimu Nyerere: Mwanaharakati mchochezi wa maasi matakatifu

Wiki jana Oktoba 14, Watanzania waliadhimisha miaka tisa ya kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas, Mjini London, Uingereza kwa ugonjwa wa kansa ya damu.

Ni kwa yapi Mwalimu anapaswa kukumbukwa? Ni kwa yapi anastahili kuigwa na jamii ya Kitanzania na Jumuiya ya kimataifa kwa ujumla?

Ukiachilia mbali ushupavu wake na heshima aliyojipatia kwa kupigania na kuleta Uhuru, Mwalimu ni mtu wa ngano na simulizi nyingi, kuanzia staili ya maisha yake, tabia na fikra zake.

Hakuna mazingira wala hali yoyote ya kuonyesha kwamba Mwalimu alijilimibikizia utajiri kihalali au vinginevyo wakati na baada ya utumishi wake, aliporejea na kuishi kijijini kama raia wa kawaida, mwaka 1985.


JK Nyerere
Mwalimu J.K. Nyerere

Nyumba yake ndogo imejengwa sehemu ile ile ilipokuwa nyumba ya baba yake, Chifu Nyerere Burito, imetuama juu ya miamba ya kilima cha asili cha Mwitongo, kijijini Butiama. Ni ndogo mno kutostahili hadhi ya mtu aliyekuwa kiongozi wa kimataifa.

Baada ya kuona kwamba kijumba hicho kidogo hakikustahili hadhi ya rais mstaafu kama Mwalimu, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWT) lilijitoleaa kuipanua, kama alivyopata kusema yeye mwenyewe: “Vijana waliona vyema Amiri Jeshi wao Mkuu anastahili nyumba ya wageni, lakini ni masikini, hana fedha”, akimwambia mwandishi wa makala haya, alipomtembelea nyumbani kwake Butiama, Februari 1999, miezi kadhaa kabla ya kwenda London kwa matibabu.

Kuna kipindi kufuatia kupinduliwa kwa Rais Kwame Nkurmah wa Ghana, mwaka 1966, Dar es Salaam ilionekana kuchukua nafasi ya Accra kama “Makkah” ya Afrika kwa wanaharakati Weusi; na kwa kufuta mwangwi wa hotuba za nguvu na za kiimahiri za Nkurumah, Tanzania, chini ya Rais Nyerere, ilishika hatamu za fikra za kimapinduzi kwa ladha ya ukurasa wa Afrika ya kale.

Mwalimu hakupenda makuu, kujikuza au urasimu mwingi, alichukia utajiri: “Kimsingi mimi ni mkulima (mdogo) na Mjamaa. Hakuna mtu anayeweza kutajirika kwa kazi yake. Milionea hawi milionea kwa jasho lake; lazima atakuwa amewanyonga wengine; mpe mtu huyo kisiwa chake uone kama atatajirika”, alipata kusema.

Kuhusu wanasiasa wanaojikweza majukwani na kutoa misaada ya mamilionoi ya pesa kwa wengine, Mwalimu, katika kitabu “Binadamu na Maendeleo” , akimnukuu Mtakatifu Ambrose, anasema, “ Humpi masikini sadaka ya mali yako, unampa kilicho chake, maana wewe umenyakua na kukifanya chako peke yako. Kile kilichopo kitumiwe na watu wote”.

Anaendelea: “Hakuna yeyote mwenye haki ya kutumia mali (rasilimali za taifa) hiyo anavyotaka. Hakuna yeyote mwenye haki ya kulimbikiza mali, au kitu asichokihitaji akitumie peke yake, wakati wengine hawapati hata mahitaji ya lazima….”

Mwalimu aliwahi kutamka wazi kuwa hakuhitaji utajiri, alisema:
“Nihitaji utajiri kwa ajili gani? Nilikuja duniani uchi na nitarudi uchi; sioni sababu kwa nini nijihangaishe na mambo ya utajiri; natimikia watu wangu, utajiri kwangu wa nini?”

Mwalimu alikufa fukara, lakini kwa utumishi uliotukuka. Katika enzi hizi za ufisadi, mafisadi wangapi wanao ujasiri wa kuwaza au kusikiliza ujumbe wa Mwalimu? Na wameadhimishaje siku hiyo?.

Mwalimu alianza kufikiria juu ya “Ujamaa” alipokuwa Chuo Kikuu Nchini Uingereza, lakini hakuwa muumini wa sera za Ki-Karl Marx kwa sababu, anasema, Karl Marx alitawaliwa na nadharia za kibaguzi za ki – Darwin, zilizomwona Mwafrika kama binadamu wa daraja la pili.

Hakutaka kuigiza Ujamaa wa Ki – Ulaya kwa sababu ulijikita zaidi katika dhana ya migongano ya kitabaka, wakati huo Afrika haikuwa na matabaka, anasema, “Ujamaa wa ki – Ulaya (Socialism) ni matokeo ya upepari uliokomaa… (lakini) lengo letu lilikuwa ni kuleta maendeleo wakati huo huo tukibakiza moyo wa jumuiya asilia”.

Baadhi ya watu walihoji ni vipi Mwalimu aliweza kuchanganya harakati za kisiasa, dhana za Karl Marx, ibada na hata dhana ya kuwapo Mungu bila kuathiri kimojawapo.

Kwa hili Mwalimu alipata kusema: “Kama ningeziogopa harakati kwa kisingizio cha kulinda imani yangu ya dini, nisingeweza kuongoza mapambano ya Uhuru wa nchi hii; ingekuwa ni sawa na kudhalilisha Ukristo wangu na Kristo, ambaye yeye mwenyewe alikuwa mwanaharakati na mwanamapinduzi”

Msimamo huu wa Mwalimu umewekwa wazi katika kitabu chake “Binadamu na Maendeleo”, kwamba: “Kanisa likubali kuwa maendeleo ya watu maana yake ni maasi… watu hufikia hatua ya kuyakataa mambo yanayowabana katika Uhuru wao kama binadamu”

Mwaliimu aliasa, “Ikiwa hatutashiriki kwa vitendo katika mapambano ya kuondoa utaratibu wa maisha na wa uchumi unaowadidimiza watu kwenye umasikini, uonevu na unyonge, basi Kanisa litakuwa halina uhusiano na maisha ya binadamu, na dini itakuwa kama ni mkusanyiko wa imani za ushirikina zinazokubaliwa na wenye hofu tu”.

Mwalimu aliamini kuwa maendeleo lazima yamaanishe maasi matakatifu, kwa sababu ya kuleta mabadiliko, alisema: “Tunasema kwamba, binadamu ameumbwa kwa mfano wa Mungu. Mimi nakataa kumfikiria Mungu aliyefukara, mjinga, mshirikina, mwoga, dhalili, ambayo ndiyo hali ya walio wengi kati ya wale aliowaumba kwa mfano wake mwenyewe”.

Mwalimu aliamini pia kwamba yote hayo yanasababishwa na binadamu kwa binadamu mwenzake, alisema: “ Lakini tulivyo hivi sasa tu viumbe, tena si viumbe wa Mungu, bali wa binadamu wenzetu… Kanisa lazima lishambulie wazi wazi mtu au kikundi chochote kinachosaida kudumisha unyonge huo wa mwili na roho, bila ya kujali misukosuko inayoweza kutokea kwa kanisa au kwa wafuasi wake.”

Mwalimu alichukia tabia ya kuiga kila kitu bila kuhoji sera, mifumo ya maendeleo na demokrasia ya kigeni kwa kutozingatia mazingira na hali halisi ya nchi yetu: “Angalia wanavyoishi kule Marekani; ni fujo na uhuni mtupu. Kama wanakuvutia kwa gharama ya watu wetu, fungasha mizigo uende ukaishi huko kama wao. Hapa lazima jicho lako liwe kijijini kwa wanavijiji; usiangalie hizo gari mbili na majokofu na vitu vyote katika nchi za kibepari, bado wanaendelea kutunyonya. Sisi tunataka kujenga jamii yenye usawa, jamii iliyostaarabika, tukipewa muda”, alisema.

Juu ya demokrasia na Maendeleo, Mwalimu aliona kuna mambo mawili muhimu: la kwanza, ni uongozi wa kueleza, na la pili, ni demokrasia katika kuamua mambo: “Maana uongozi si kukemea watu; maana yake si kuwatukana watu au kikundi cha watu usiokubaliana nao; wala maana yake si kuamuru watu kutenda lile wala hili. Uongozi maana yake ni kuzungumza na kushauriana na watu ukawaeleza na kuwashawishi. Maana yake ni kuwa mmoja wao na kutambua kwamba wao ni sawa na wewe”

Mwalimu aliamini kwamba uongozi hauwezi kuchukuwa nafasi ya demokrasia; uongozi lazima uwe sehemu ya demokrasia. Alihuzunika baada ya kustaafu kubaini kwamba rushwa serikalini ilianza kuchukua umbo la kulitaifisha Taifa.

Ni wakati huo pia alipong’amua kwamba chama tawala Chama cha Mapinduzi (CCM), kilikuwa kimekoma kuwa chama cha wanachama na kuwa chama cha viongozi. Na kwa sababu hiyo alianzisha mjadala juu ya mfumo wa vyama vingi nchini.

Mwalimu alinukuliwa akisema: “ Kiitikadi, mimi ni mtu wa Chama kimoja. Lakini nimeanzisha mjadala huu kwa sababu ile dhana kwamba ni mwiko kuhoji Katiba yetu si ya kidemokrasia…. Siwezi kukubali; nasema, kama hawa jamaa (watu) wanataka mfumo wa vyama vingi, waache waanzishe….”

Mwalimu alikwisha kututoka. Ni kweli alikuja mtupu duniani na amerudi mtupu, lakini fikra zake zinaishi. Hata hivyo, tumejionea jinsi fikra hizo zinavyopigwa vita na vikosi vya nyang’au wa uchumi na siasa ili washike hatamu za nyanja hizo kwa maangamizi ya uchumi, Taifa na watu wake.

Ilivyo sasa uzalendo unatoweka haraka, maadili yanayoyoma. Uongozi umenyakuliwa na wasomi wachache wanaojifanya kuyaelewa matatizo yetu, wakati ni kinyume chake. Wameunda mtandao na mabwana wa ubepari wa kimataifa; viongozi wamepungukiwa hisia za kitaifa zinazozaa uzalendo, ushujaa, kujitoa mhanga kwa nchi. Wamekuwa kama watu wanaojiaandaa kustaafu na kuishi ughaibuni.

Kwa tabaka hili dogo, lakini lenye nguvu, demokrasia sasa maana yake ni kukamata mawazo ya watu wasio na elimu ya demokrasia kwa kuwanunua kwa nguvu ya pesa na kunyakua madaraka ya kisiasa.

Viongozi wamebweteka na kubugia sera zinazowakamua masikini kuwatajirisha mabepari wachache. Badala ya kuwa watumishi wa watu wamegeuka kuwa mabwana zao. Wasomaji watajiuliza: Kwa nini Watanzania, kila wanapokerwa na jambo, wanaimba, “ Kama si juhudi zako Nyerere… x 3; … na uhuru, elimu, amani… tungepata wapi?”.

Ni kwa sababu Nyerere, kama mwanaharakati na mwana mapinduzi, alichochea moto wa maasi yasiyozimika, hadi ushindi upatikane kwa “Wasakatonge”.