Friday, March 30, 2012

Darasa la tano na sita wasomea darasa moja Kisarawe

Baadhi ya wanafunzi wa darasa la pili wa Shule ya Msingi Mengwa wakiwa nje ya darasa lao. Darasa hili kama lilivyoandikwa juu ya mlango wake pia hutumiwa kwa kupokezana na wanafunzi wa darasa la kwanza na la pili.


Hili ni darasa moja ambalo hutumiwa na wanafunzi wa darasa la tano na la sita kwa pamoja wa Shule ya Msingi Mengwa. Kulia walionyoosha mikono ni darasa la sita baada ya mpiga picha kuomba darasa la sita kunyoosha mikono ili niweze watambua.


Hapa walionyoosha mikono juu upande wa kushoto ni wanafunzi wa darasa la tano wa shule ya Msingi Mengwa baada ya kuomba kufanya hivyo ili uweze kuwatenganisha na wale wa darasa la sita.

Na Joachim Mushi, Thehabari-Kisarawe

WAKATI Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi nchini ikijipanga kuanza kufundisha kwa kutumia teknolojia ya kompyuta katika shule mbalimbali, wanafunzi wa darasa la tano na sita wa Shule ya Msingi Mengwa bado wanatumia darasa moja kwa wakati mmoja.

Hali hiyo imejulikana juzi baada ya mwandishi wa habari hizi kutembelea shule hiyo, iliyopo Kata ya Maneromango, Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mengwa, Peter Gadie alisema kitendo cha wanafunzi hao kutumia darasa moja kimefanya wapunguziwe muda wa vipindi wa kawaida ili kupishana kwa zamu kutumia darasa hilo.

Alisema badala ya kila kipindi kufundishwa kwa dakika harobaini walimu wameamua kufundisha kwa dakika ishirini kila kipindi ili kupeana zamu kuwafundisha wanafunzi hao.
Mwandishi wa habari hizi ameshuhudia darasa hilo likiwa na wanafunzi wote yaani wa darasa la tano ambao wapo 24, na darasa la sita wakiwa 29 wakiendelea na masomo kwa pamoja huku wakitenganishwa kwa mistari ya madawati.

Akizungumzia staili ya ufundishaji wa walimu kwa kutumia darasa moja, Gadie alisema mwalimu wa darasa la tano anapoingia darasani huendelea na kipindi kwa dakika 20 huku akiwataka wanafunzi wa darasa la sita kujiinamia na kujisomea ama kuendelea na kazi walizoachiwa na mwalimu aliyetoka punde.

“Anapoingia mwalimu kufundisha darasa moja uwaamuru wanafunzi wa darasa lingine wajisomee ama kuendelea kufanya kazi ambazo wameachiwa na mwalimu aliyetoka…kweli wanapata usumbufu lakini haina namna maana tunaupungufu wa madarasa shuleni kwetu,” alisema Gadie akizungumza na mwandishi wa habari hizi.

Aidha alisema tatizo hilo halipo kwa wanafunzi wa darasa la sita na la tano pekee, kwani wanafunzi wa darasa la kwanza na la pili nao usomea darasa moja kwa kupokezana saa; ambapo darasa la kwanza huingia saa mbili hadi saa sita na baadaye kuwapisha darasa la pili ambao huingia saa sita na kuendelea hadi mchana.

Alisema upungufu wa vyumba vya madarasa umeifanya shule hiyo kukodisha ukumbi wa kuoneshea video kijijini Mengwa na kulifanya darasa la awali kwa wanafunzi wa shule hiyo wanaosoma darasa la awali kabla ya kujiunga na darasa la kwanza.

Habari hii imeandaliwa na Mtandao wa Thehabari.com (www.thehabari.com) kwa kushirikiana na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).

Thursday, March 29, 2012

Wanafunzi 159 wa Shule ya Sekondari Maneromango wakimbia mitihani

Na Joachim Mushi, Thehabari.com-Kisarawe

WANAFUNZI 159 wa Shule ya Sekondari Maneromango wametoroka kufanya mitihani ya majaribio ya robo muhula iliyoanza juzi katika shule hiyo.

Wanafunzi hao ambao ni vidato mbalimbali kuanzia cha kwanza hadi cha nne, ni kati ya wanafunzi 383 wa Shule ya Sekondari Maneromango waliotakiwa kuanzia kufanya mitihani yao Machi 27, 2012 shuleni hapo.

Akizungumza katika mahojiano na mtandao wa Thehabari.com katika shule hiyo iliyopo Kata ya Maneromango, Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani, Mwalimu wa taaluma wa shule hiyo, Jonas Buheruko alisema ofisi yake imebaini utoro huo baada ya kukusanya taarifa kutoka vidato vyote.

Akifafanua alisema hali hiyo ya utoro na hasa wanafunzi kukimbia mitihani hujitokeza mara kwa mara jambo ambalo limekuwa miongoni mwa vikwazo vya shule hiyo kufanya vizuri kitaaluma.

Alisema taarifa zilizokusanywa siku ya kwanza kuanza kwa mitihani hiyo, Machi 27 mwaka huu, zimebaini kidato cha nne ndiyo wanaoongoza kwa utoro wa mitihani kwani kati ya wanafunzi 106 waliotakiwa kuanza kufanya mitihani hiyo ya majaribio ni 45 pekee walifanya huku 65 wakiingia mitini.

“Taarifa zangu nilizokusanya baada ya kuanza tu kwa mitihani zinaonesha kidato cha kwanza wametoroka wanafunzi 10 kati ya 81, kidato cha pili wametoroka 31 kati ya 103, kidato cha tatu wametoroka 53 kati ya 93 waliotakiwa kuanza kufanya mitihani hiyo,” alisema Mwalimu Buheruko.

Hata hivyo alisema kitendo cha utoro wa mithani shuleni hapo sasa kinaendelea kuwa sugu licha ya walimu kufanya jitihada za kuwafuatilia wanafunzi na kutoa adhabu mbalimbali kulingana na taratibu za shule.

Aidha aliongeza mwaka 2011 wanafunzi 34 wa kidato cha nne kati ya 85 walikimbia kufanya mtihani wa majaribio wa Wilaya shule hapo jambo ambalo linawakatisha tamaa walimu katika utoaji wa elimu shuleni hapo.

“Wamekuwa wakikimbia mitihani mara nyingi…tunawapa adhabu lakini wapo radhi kufuraia adhabu unayowapa kuliko kuja kufanya mitihani…wakati mwingine tunapozidiwa tumekuwa tukipeleka majina ya watoro kwa Mwenyekiti wa Kijiji na Ofisa Mtendaji wa Kata lakini bado hatujaweza kudhibiti utoro huu,” aliongeza mwalimu Buheruko.

Akizungumzia hali hiyo, Mratibu wa Elimu Kata ya Maneromango, Nicolaus Lemma amesema wamekuwa wakiwaita mara kadhaa wazazi wa wanafunzi na kuwashtaki pale inapobainika wanachangia utoro wa watoto wao, ila tatizo hilo si kwa sekondari pekee bali hata shule za msingi eneo hilo.

Habari hii imeandaliwa na Thehabari.com kwa kushirikiana na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).