Monday, October 31, 2011

Mbunge: TGNP saidieni wagombea wanawake majimboni

Wajumbe wa kamati ya Bunge ya kudumu ya Huduma za Jamii wakimsikiliza Mkurugenzi wa TGNP Usu Mallya ( hayupo pichani)

Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii Mhe. Juma Mtanda akizungumza

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Usu Mallya akiwaelezea Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wajumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma za jamii shughuli za TGNP

MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) umetakiwa kuwawezesha wanawake wanaojitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi hasa Ubunge na Udiwani majimboni ili washinde.

Wakizungumza katika ofisi za TGNP wabunge wa kamati ya Bunge ya Kudumu ya Maendeleo ya jamii wamesema TGNP inalojukumu la kuwasaidia kwa kuwajengea uwezo wagombea wanawake watakaojitokeza kugombea ili waweze kujiamini na hata ikiwezekana kwapatia rasilimali za kuwawezesha kuwashinda wanaume.

Idadi ya Wabunge waliochaguliwa kwenye majimbo imengozeka kutoka 12 mwaka 2000, hadi 17 mwaka 2005 na katika uchaguzi wa mwaka 2010 wamefikia wabunge 20. Sawa na asilimia 36 ya wabunge wote.

Mbunge wa Jimbo la Nkenge,MKoani Kagera Mchangaji Asumpta Mshana (CCM) amesema kuwa hata yeye binafsi ameshinda katika jimbo hilo kwa taabu kutokana na kupambana na mgombea aliyekuwa waziri na mwenye nguvu kubwa.

“Wanawake tunapomua kugombea tunashindwa kutokana na tatizo la rasilimali hasa fedha, unakuta wanaume wanatumia fedha nyingi wakati sisi hatuna kitu, tutawezaje kushinda? TGNP wekeni mkakati wa kuhakikisha Mwanamke atakayesimama kugombea anapata msaada wa kujengewa uwezo na hata raasilimali”

“Mimi nilisimama na Waziri, ilikuwa kazi kwelikweli, wanawake wachache tumeshinda kwasababu wananchi walipima ni kitu gani tutakipata tukimpa huyu mwanamke,…”alisema Mshana

Mshana aliitaka TGNP kwa kupitia Chuo chake cha Mafunzo ya Jinsia (GTI) kuwaelimisha wabunge wanawake juu ya uchambuzi wa bajeti kwa mtazamo wa kijinsia ili wakati wa Bajeti ya serikali wabunge wote wanawake wasimame kudai bajeti yenye usawa wa kijinsia ambayo haimbagui mwanamke na mwanamme masikini.

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Usu Mallya aliwaeleza wabunge hao kuwa TGNP ni shirika huru lisilofungamana na siasa wala dini, na ni shirika la mfano kwa hapa nchini ambalo mwanachama wake akijihusisha na siasa anaacha kuwa mwanachama mara moja.

Mallya alitoa mfano wa Mbunge wa Viti Maalum (Chadema) na Waziri Kivuli wa Wizara ya Jinsia, wanawake na watoto Naomi Kaihula, na Naibu waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mkangala, ambao kwa Pamoja mwishoni mwa mwaka jana walijitoa kwenye Bodi ya Shirika baada ya kujiingiza kwenye siasa na kuchaguliwa kuwa Wabunge.

Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Said Mtanda, aliomba TGNP kutoa mafunzo elekezi kila mwaka mara moja kwa wabunge kwaajili ya kujifunza masuala ya bajeti, sera na mauala mengine ya kijamii yanayoweza kuwasilishwa Bungeni.

“Ipo haja ya TGNP kukutana na kamati hii na kupatiwa semina elekezi, mtupatie mafunzo ya jinsia, tunapokaa Bungeni tuweze kuyaelezea, mtupatie maarifa ili tuweze kutoa maoni ya wadau.

Sunday, October 30, 2011

WANAWAKE WATAKIWA KUTUMIA NAFASI WANAZOPEWA NA UNIFEM

Na Anna Nkinda- Perth Australia
30/10/2011 Wanawake wametakiwa kutumia nafasi zinazotolewa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Wanawake (UNIFEM) katika kujiletea maendeleo yao na ya mataifa yao kwani lengo kuu la kuanzishwa kwa shirika hilo ni kumuinua mwanamke na kuleta usawa wa kijinsia.

Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo Dk. Noeleen Heyzer wakati akiongea na wake wa wakuu wa nchi wanachama wa Jumuia ya Madola katika mkutano wao uliofanyika Perth nchini Australia.

Dk. Heyzer alisema kuwa hivi sasa katika nchi nyingi Duniani wanawake wanapewa nafasi za kupata elimu, kuwezeshwa kiuchumi, usawa wa kijinsia , kupata afya bora kwa mama na mtoto na upatikanaji wa ajira hii yote ni kumfanya mwanamke aweze kujiinua kiuchumi kwani hapo zamani wanawake walikuwa wameachwa nyuma kimaendeleo tofauti na wanaume.

“UNIFEM inashughulika na masuala ya usawa wa jinsia na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi, kisiasa na kijamii hivyo basi ni jukumu lenu kuwahamasisha wanawake katika nchi mnazotoka ili waweze kuzitumia nafasi wanazopewa hii itawasaidia kujikwamua kiuchumi”, alisema

Baada ya Mkurugenzi Mtendaji wa UNIFEM kumaliza kuongea na wake hao wa wakuu wan chi akiwemo Mke wa Rais Mama Salma Kikwete walitembelea Halmashauri ya jiji la Perth upande wa Sekta ya Nishati na Madini na kuelezwa jinsi sekta hiyo ilivyochangia kutoa ajira na kuinua uchumi wa nchi hiyo.

Viongozi kutoka makampuni ya uchimbaji wa madini ambao ni Mtendaji Mkuu wa Chamber of Minerals and Energy of West Australia Reg Howard-Smith, Mkurugenzi Mtendaji wa Argyle Diamonds Kevin McLeish na Josephine Archer ambaye ni meneja biashara kutoka Argyle Pink Diamonds walisema kuwa kutokana na jiografia nzuri mji huo umejaliwa kuwa na madini mengi ukilinganisha na miji mingine.

“Upande wa Magharibi wa Nchi yetu kuna miji minne ambayo ni Kimberley, Pilbara, Yilgarn na Kusini Magharibi ambako kunapatikana madini zaidi ya aina 50 baadhi yakiwa ni dhahabu, almasi, chuma, mchanga mzito wenye madini aina tofauti, base metals, chumvi, chuma cha pua, Ilmenite, Rutile, Alumina, Zircon, Garnet na Tantaluma”, walisema.

Wake wa wakuu wan chi wanachama wa Jumuia ya madola waliweza kujionea aina mbalimbali za madini yanayopatikana katika nchi hiyo pamoja na vito vya thamani na bidhaa zinazotengenezwa kutokana na madini hayo.
Aidha waliweza kutembelea bustani ya kutunza mimea na wanyama wa asili nakuona jinsi viumbe hai vya kale vinavyotunzwa ili visiweze kupotea kwa ajili ya kumbukumbu ya vizazi vijavyo na wageni wanaotembelea nchi hiyo.

Mkutano wa wakuu wa Nchi wanachama ya Jumuia ya madola umemalizika leo na Kaulimbiu ya mwaka 2011 ya Jumuia hiyo ni “Wanawake ni wakala wa mabadiliko”.

Thursday, October 27, 2011

Ongezeko la watu Duniani ni zaidi ya bilioni 7

Bi. Christine Mwanukuzi kutoka UNFPA akiwasilisha mada

Martha Samwel akichangia mjadala

Ongezeko la watu linakadiriwa kufikia bilioni 7. Hayo yalisemwa jana na mtoa mada wa shirika la kimataifa la watu Duniani (UNFPA) Bi. Christine Mwanukuzi kuhusu ongezeko la watu Duniani katika semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS) zinazofanyika kila siku ya jumatano katika ofisi za Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).

Akizungumzia ongezeko hilo Bi. Christine Mwanukuzi amesema Tanzania kuna idadi ya watu milioni 44.4 na ongezeko hili la idadi ya watu haiendi sambamba na mgawanyo wa rasilimali uliopo, ni wachache wanaofaidi na kuna tofauti kubwa kati ya walionacho na wasionacho, vifo vya wakinamama wakati wa kujifungua na watoto chini ya miaka 5 kuzidi kuongezeka.

Bi. Christine aliweka bayana matokeo ya utafiti wa UNFPA unaoonyesha kuwa idadi ya watu ni milioni 3.7, watu bilioni 1 hulala njaa kila siku, watu bilioni 2 katika bilioni 7 wanaishi chini ya kipato cha dola 1 ya kimarekani kwa siku, inakadiriwa watu 7,000 hufa kila mwaka kutokana na matatizo haya na vifo 578 ikiwa ni vya wakinamama wakati wa kujifungua nchini Tanzania

Akichangia mjadala huo wa wazi Bi Martha Samwel ambaye ni mshiriki wa semina hizo alisema kulingana na maazimio ya sera ya Maputo, ifikapo mwaka 2015 bajeti ya kila nchi inatakiwa iwe imewekeza asilimia 15 katika sekta ya afya, mpaka sasa katika nchi ya Tanzania hatujafikia hata asilimia 10 na ongezeko la vifo vya wanawake wakati wa kujifungua ni kubwa, je tukifika bilioni 7 huduma za afya zitakuwaje? Vifo vya wanawake wajawazito vitakuwa kwa wingi kiasi gani? Serikali iliangalie hili kwa umakini ili kuwekeza katika rasilimali watu

Wengi wa waliochangia mjadala huo hawakuridhishwa na jinsi serikali inavyolipa umuhimu suala zima la afya ya uzazi na sekta nzima ya afya na kuitaka serikali kuchukua jukumu lake la kutoa huduma za msingi kwa jamii ambayo ni walipa kodi.

Semina za jinsia na maendeleo ni za wazi kwa yeyote na hufanyika kila siku ya jumatano saa tisa kamili alasiri mpaka saa kumi na moja jioni katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na kushirikisha wadau wote katika kada mbalimbali.

Wakuu wa nchi CHOGM waombwa kuwasaidia wasichana wanaoozeshwa kwa nguvu

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Commonwealth Business Forum, Dk. Mohan Kaul mjini Perth, Australia ambapo anahudhuria mkutano wa wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Madola

WAKUU wa nchi Wanachama wa Jumuia ya Madola wameombwa kuchukua hatua na kuwasaidia mamilioni ya wasichana wanaoozwa kilazima huku wakiwa na umri mdogo na hivyo kukosa haki zao za msingi.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya Habari vilivyohudhuria maandalizi ya mkutano wa Viongozi wa Nchi wanachama wa Jumuia ya Madola (CHOGM) unaotarajia kuanza tarehe 28 hadi 30 mjini Perth nchini Australia inasema kuwa hivi sasa kuna mamilioni ya wasichana wananyanyasika kijinsia kutokana na ndoa za utotoni.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa leo na Plan International na Royal Commonwealth Society inasema kuwa ndoa za lazima na za utotoni ni moja ya vikwazo vikubwa kwa wasichana katika elimu, afya ya uzazi, na uchumi wa mwanamke hivyo basi kuna ulazima kwa jumuia ya madola kuchukua hatua zaidi ili kuzuia wasichana wasilazimishwe kuolewa wakiwa bado au wakiwa tayari kuolewa.

“Jumuia ya madola inatetea haki za binadamu na kaulimbiu yake ya mwaka 2011 ni “Wanawake ni wakala wa mabadiliko” hivyo basi viongozi wa Jumuia hiyo wafanye haraka kuhakikisha kuwa yanapatikana mabadiliko makubwa kwa wanawake na si kubaki kama walivyo,” ilisema taarifa hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa Plan Internationa nchini Australia Ian Wishart alisema kuwa ndoa za lazima na za utotoni zinamuweka msichana katika umaskini, kutokuwa na afya njema na ukosefu wa elimu.

“Hivi sasa katika Dunia takwimu zinaonyesha kwamba kuna wasichana milioni 10 wenye umri wa chini ya miaka 18 ambao wanaolewa kila mwaka hii inamaana kuwa kila msichana mmoja anaolewa kila baada ya sekunde tatu”, alisema Wishart.

Aliendelea kusema kuwa wasichana wanaoolewa mapema wanauzoefu wa ukatili wa kijinsia, wanadharauliwa na kulazimishwa kufanya mapenzi hii inawasababishia matatizo ya kijinsia na afya ya uzazi na zaidi wanakosa elimu na hivyo kuwa wajinga.

Wishart alisema, “Ndoa za utotoni na za kulazimishwa ni moja ya vitu vinavyozuia kufika malengo ya milinia ya kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na watoto, upatikanaji wa elimu ya msingi kwa wote, kupunguza umaskini, usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Royal Commonwealth Society Peter Kellner alisema kuwa Jumuia ya madola iko makini kuhusiana na maendeleo ya wanawake na haki za binadamu, na ina mipango kazi ya kuhakikisha kuwa suala la ndoa za lazima na za utotoni linachukuliwa hatua za haraka na linapata ufumbuzi.

“Wanachama wote wa Jumuia ya Madola wamekubaliana kulinda haki za watoto na wanawake kwani nchi 12 kati ya 20 ambazo zilikuwa na kiwango kikubwa cha ndoa za lazima na za utotoni ni nchi za Jumuia ya madola,” alisema Kellner.

Mwenyekiti huyo aliendelea kusema kuwa mamilioni ya wasichana kila mwaka kupitia Jumuia ya madola wanapata nafasi ya kuondokana na matokeo ya ndoa za lazima na za utotoni hii si kwao tu bali katika familia zao, jamaa zao na jumuia ya madola.

Jumla ya viongozi wa nchi 53 ambao ni wanachama wa Jumuia ya Madola wanatarajiwa kuhudhuria mkutano huo ambao utafunguliwa na Malkia Elizabeth wa pili akiwemo Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Serikali nchini Tanzania kupitia wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Taasisi mbalimbali za Kiserikali na zisizo za Kiserikali zinafanyakazi ya kuelimisha jamii ili kuhakikisha kuwa tatizo la ndoa za lazima na za utotoni linamalizika.

Wednesday, October 26, 2011

Wahadzabe wapewa hatimiliki ya ardhi

JAMII ya Wahadzabe waishio katika Bonde la Yaeda chini, wilayani Mbulu mkoani Manyara, wamepatiwa hatimiliki ya kimila kwa ajili ya matumizi yao ya asili ikiwamo kurina asali, kuwinda na kuchimba mizizi.

Tukio hilo ni la kwanza na la kihistoria tangu Tanzania kupata Uhuru wake kutoka Uingereza miaka 50 iliyopita ambapo lilihusisha pia kukabidhiwa kwa hatimiliki 50 za kimila kwa wakazi wa vijiji vya Domanga na Mongo wa Mono vilivyopo ndani ya bonde hilo.

Mbali na jamii hiyo ya Wahadzabe makabila mbalimbali yanaishi ndani ya bonde hilo ambayo ni Wasukuma, Watatoga na Wairaq ambao kiasili ni wafugaji na wakulima.

Akikabidhi hati hizo mwishoni mwa wiki iliyopita Kamishna Msaidizi wa Ardhi, Kanda ya Kazkazini, Doroth Wanzala alisema kuwa upatikanaji wa hati hizo utawasaidia wakazi hao kuepukana na migogoro ya ardhi inayowakumba mara kwa mara.

Alisema kuwa hati hizo zitawasaidia pia kutambua mipaka yao ya ardhi, hivyo kupunguza tatizo la migogoro katika maeneo hayo na kurahisisha mipango ya matumizi bora ya ardhi.

Awali,akisoma risala mbele ya mgeni rasmi, kwa niaba ya Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Endeko Endeko alisema kuwa mwaka 1998 vijiji vya Mongo wa Mono na Domanga vilianzisha mpango wa matumizi bora ya ardhi uliokamilika mwaka 2000.

Alisema kuwa baada ya mpango huo kukamilika, vijiji vyao vilitunga sheria ndogondogo za vijiji kwa lengo la kulinda mpango huo, shughuli ambazo zilifanywa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu kwa kushirikiana na Shirika la Ujamaa Community Resource Team(UCRT) kama mwezeshaji.

Hatahivyo, Endeko alisema kuwa zipo changamoto zinazowakabili katika vijiji vyao na kutaja uvamizi wa maeneo aliodai unafanywa na watu kutoka mikoa ya jirani ya Singida na Shinyanga.Mratibu wa UCRT, Edward Loure alisema kuwa upatikanaji wa hatimiliki hizo za kimila utawasaidia wakazi wa maeneo hayo kuondokana na tatizo sugu la migogoro ya ardhi linalowakabili kwa muda mrefu.Zoezi la kukabidhi hati hizo lilifadhiliwa na shirika hilo la UCRT lenye makao makuu yake mkoani Arusha.

Sitta:Sigombei urais uchaguzi 2015

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta amesema hana ndoto ya kuwania urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu ujao mwaka 2015.Kauli hiyo ya kwanza ya Sitta ambaye pia ni kada wa CCM, imekuja wakati ambao kuna mpasuko mkubwa ndani ya chama chake hicho ambao unahusishwa na mbio za urais wa 2015, huku yeye akitajwa kuwa mmoja wa wenye nia ya kushiriki mbio hizo.

Kauli yake imeingia katika orodha ya kauli za makada wengine kadhaa ambazo zimetikisa siasa za CCM huku nyingi zikiwa na sura ya mvutano tena zikitolea nje ya vikao rasmi vya chama hicho tawala nchini.

Hata hivyo, juzi usiku akijibu swali kama ana ndoto ya kuwania urais au la, Sitta alisema: "Hapana! Sina ndoto ya kuwania urais kwa sasa, wapo vijana watajitokeza, wapo wazuri, tutawaunga mkono tu".

Sitta alifafanua kwamba matumaini yake mwaka 2015 watakuwapo wagombea wenye uwezo wakiwemo vijana, na kuongeza, "wale wazalendo wenye maadili wataungwa mkono".

Ingawa, Sitta amesema hana ndoto ya kuwania urais kwa sasa, lakini amekuwa akitajwa kama mmoja wa watu wanaoutaka baada ya Rais Jakaya Kikwete mwaka 2015, kutokana na nguvu zake kubwa alizojijengea kwa umma.

Sitta aliweza kujipatia umaarufu mkubwa kisiasa baada ya kuongoza kwa mafanikio Bunge la Tisa ambalo alikuwa na kauli mbiu yake ya Bunge la Kasi na Viwango.

Kuhusu chuki ya watu aliowaita mafisadi, Sitta alisema watuhumiwa hao walifanya mbinu mbalimbali kuhakikisha hafanikiwa katika malengo ya kurejea kwenye uspika wa Bunge la Kumi kwani waliendesha hujumu nzito dhidi yake.

Sitta aliwatuhumu watu hao akisema: "Mafisadi hawanitaki, wananichukia wako tayari hata kuniua".

Mwelekeo wa CCM
Akizungumzia mustakabali wa chama hicho kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015, Sitta alisema CCM kitaweza kushinda kutokana na mabadiliko yanayotarajiwa kufanywa katika vikao vijavyo vya chama hicho baadaye mwaka huu, pamoja na uchaguzi wake mkuu wa mwakani.

Sitta aliongeza:, "Uchaguzi Mkuu ndani ya CCM wa mwaka 2012, utatuonyesha sura ya chama. Nina imani watapatikana wanaofuata maadili yale aliyosimamia Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere".

Hata hivyo, Sitta alionya kwamba chama hicho kinahitaji timu ya ushindi na kwamba hakiwezi kufanya hivyo ikiwa kitaendelea kuwa na watu wanaojitajirisha kwa nafasi zao za uongozi.

"CCM inastahili kufanya mabadiliko, inahitaji timu ya ushindi ili kuweza kufanya hivyo, lakini hakiwezi kufanya hivyo kama itaendelea kuwa na watu wanaojitajirisha kupitia fursa za uongozi. 2012 CCM iwe safi zaidi, tusiache watu wanunuane," alionya Sitta.

Alisema mwaka 2012, CCM itashuhudiwa ikirejea katika mstari wake, kupitia vikao vyake na falsafa ya kujivua gamba ambayo itashuhudiwa ikiwashughulikia wanaopinga kurejesha maadili na kuzaliwa upya.

Lakini, alisema katika hilo wapo wanaopinga kurejeshwa kwa maadili hayo kwa kutumia fedha zao kununua wapambe aliowaita wenye roho za kuku ambao watakuwa wakitumika kuzuia mpango huo kwa malengo ya kisiasa.

"Katika hilo wapo wenye roho ya kuku, wakionyeshwa pesa tu, basi wanabadilika. Wanaosema hawataki dhana ya kujivua gamba hawataki CCM izaliwe upya,"alisema.

Malipo ya Dowans
Sitta alirerejea msimamo wake kuhusu malipo kwa kampuni hiyo, huku akisema kuwa anaridhishwa na hatua ya kukata rufaa na kusisitiza umuhimu wa vijana kuwa na uzalendo wa kufanya maandamano kupinga mambo yasiyo ya msingi.

"Sisi zamani tulikuwa mstari wa mbele katika maslahi ya taifa. Ila kwa sasa naona vijana wako nyuma sana hawaandamani kupinga vitendo vya kifisadi katika Serikali yao, maandamano ya kizalendo yenye kuonesha hisia zao juu kupinga ufisadi huu,’’alisema Sitta.

Alisema angefurahi siku kuona kama vijana wa CCM na wengine wenye maadili wakiandamana kwa pamoja kupinga vitendo vya kifisadi, ikiwemlo kuilipa Dowans, lakini kwa sasa akasema suala hilo linashughulikiwa kisheria.

Sitta ambaye alikuwa akizungumza katika kipindi cha dakika 45 kinachorushwa na kituo cha luninga cha ITV, alisema Sh 110 bilioni za kuilipa Dowans zina uwezo wa kujenga shule za kisasa 300 mbazo kila moja ingegarimu Sh300 milioni.

Sitta alisema huo ni ulafi na kuongeza kwamba yeye kama angekuwa na fedha nyingi au sehemu angekuwa tayari mafisadi wangemchafua.

“Mimi kama ni ngekuwa hata na tuhuma ya shilingi moja ni lazima wangeniumbua maana wananitafuta sana na kama vitisho nimevipata sana kwenye simu ndiyo maana nabadilisha sana namba ya simu,’’ alisema.

Alisema stahiki anazolipwa na Serikali kama nyumba na magari si ufahari, kwani kama ni benzi aliyokuwa akitumia kipindi akiwa mbunge si lake.
Waziri Sitta alisema gari kama hilo alinunuliwa pia Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) na hata Gavana wa Benki Kuu (BoT) na kuhoji, "sasa kwanini nitajwe mimi tu?"

Kauli za makada CCM
Wiki iliyopita Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa naye alivunja ukimya kwa kuzungumzia tuhuma mbalimbali zinazoelekezwa kwake, huku akisisitiza kuwa amechoka kukashifiwa na sasa kamwe hatawavumilia wanaomzulia mambo.

Lowassa ambaye pia amekuwa akitajwa kuwa na mpango wa kuwania urais wa 2015 alisema ni jambo lisiloingia akilini kumhusisha yeye na kile kinachodaiwa mkakati wa kumhujumu Rais Kikwete au CCM, wakati yeye ni mbunge anayetokana na chama hicho.

Siku moja kabla ya Lowassa kuzungumza na vyombo vya habari, Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Millya aliingia katika malumbano yanayoendelea miongoni mwa makada wa chama hicho pale aliposema “watoto wa viongozi wa CCM na Serikali wamejitwika madaraka ya wazazi wao kinyume cha sheria za nchi”.

Kama ilivyokuwa kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Onesmo Ole Nangole na Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Benno Malisa, pia Millya alimshambulia Katibu wa Itikadi na Uenenzi wa chama hicho, Nape Nnauye kwamba amekuwa akikivuruga chama.

Nape anatuhumiwa na kundi mojawapo ndani ya CCM kutokana na jinsi anavyosimamia utekelezaji wa maazimio ya NEC ya CCM hasa falsafa ya kujivua gamba, na hilo limekuwa likihusishwa na mbio za urais wa 2015.

Hata hivyo, Nape aliwahi kuliambai gazeti hili kwamba anashamgazwa na wale wanaopotosha utekelezaji wa maazimio hayo ya NEC kwa kuhusisha utekelezaji wake na Uchaguzi Mkuu ujao, wakati muda wa uchaguzi wenyewe bado haujafika.

Tuesday, October 25, 2011

Wanasiasa, matajiri wakwepa deni Posta

MWENYEKITI wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Kabwe Zitto, amesema baadhi ya wanasiasa wanakopa na kutumia nyadhifa zao kushawishi wafutiwe madeni yao, ilhali wana uwezo wa kuyalipa.

Zitto alisema hayo jana wakati Kamati hiyo ilipokutana na watendaji wa Benki ya Posta (TPB) Dar es Salaam, walioelezea mpango wa benki hiyo wa kufuta deni la Sh bilioni 1.1 kwa wateja inaowadai.

Mbali na wanasiasa, Zitto alisema mchezo huo pia umekuwa ukifanywa na matajiri na watumishi wenye vyeo vya juu katika mashirika na taasisi mbalimbali nchini.

Kutokana na hali hiyo, Kamati hiyo ilimwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), apitie upya deni hilo ili kujiridhisha, endapo linastahili kufutwa.

Pia Kamati hiyo iliiagiza benki hiyo kutoa orodha yote ya majina ya wadaiwa waliokopa kuanzia Sh milioni 50 na kuendelea, waliowekwa katika mpango wa kufutiwa deni hilo kwa mwaka 2009/10, ili iyapitie na kufanya uamuzi, iwapo walio orodheshwa wanastahili kutodaiwa tena au kuwaanzishia deni upya.

“Kamati inaagiza iletewe orodha ya majina yote ya wadaiwa walioainishwa kuwa wafutiwe madeni ya jumla ya Sh bilioni 1.1 ili iyapitie na kuyachambua kuona kama kuna anayeweza kudaiwa upya, ili hilo lifanyike.

“Hatuwezi kukubali kirahisi tu kwamba wadaiwa hao wafutiwe madeni kwa sababu kufanya hivyo ni kuiathiri benki na kumnufaisha mdaiwa anayejineemesha kwa njia ya ubadhirifu.

“Tuna uzoefu na mambo haya kutokana na tuliyoyaona kipindi cha nyuma. Madudu ni mengi kwenye mashitaka ya umma, wanasiasa na wenye nyadhifa wanatumia mashirika ya umma kujineemesha kwa sababu ya ubinafsi,” alisema Zitto.

Alisema, Bunge kupitia Kamati hiyo ndilo lenye uamuzi wa mwisho wa ama kufutwa kwa madeni au la, na kwamba wadaiwa watakaothibitika kuwa na uwezo wa kulipa madeni yao watadaiwa, hata kama ni kwa kutumia madalali.

Aliiagiza benki hiyo iipe Kamati orodha hiyo wakati itakapokutana nayo tena kupitia hesabu zake za kuishia Desemba.

Zitto pia aliitaka TPB iwasilishe kwa Kamati hesabu za deni la Sh milioni 375 inaloidai Western Union kwa kipindi hicho cha 2009/10 ili ijiridhishe pia kama linastahili kufutwa au la.

Fedha hizo ni malipo ya matumizi ya huduma mbalimbali za benki hiyo. Uamuzi huo ulitolewa baada ya Mtendaji Mkuu wa TPB, Sabasaba Moshingi, kuiambia Kamati hiyo kuwa deni hilo lilionekana kwa makosa baada ya maandalizi ya hesabu za fedha zilizopokewa na benki hiyo na zinazodaiwa kutoainishwa sawasawa.

“Tumeweka deni hilo katika orodha ya yanayostahili kufutwa kwa sababu limetokana na makosa yetu wenyewe katika kuoanisha fedha tulizolipwa na Western Union na tunazodai, deni hilo lililipwa, hivyo halikustahili kuonekana katika hesabu zetu,” alisema Moshingi.

Katika hatua nyingine, POAC imemwita Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, na wajumbe wa Bodi ya Utalii nchini (TTB) wafike mbele ya Kamati hiyo Oktoba 31, kuieleza ni kwa nini haijateua Bodi ya Wakurugenzi wake hadi sasa. Bodi ya awali ilimaliza muda wake wa kazi tangu mwaka 2009, ikiwa ni zaidi ya miaka miwili.

Zitto alimtaka Mkurugenzi Mkuu wa TTB, Dk. Aloyce Nzuki, aeleze ni nani aliyekuwa akiidhinishia fedha za matumizi ya kila siku ya Bodi hiyo ambayo ni zaidi ya Sh bilioni saba, wakati wenye uwezo huo kisheria ni Bodi ya Wakurugenzi ambayo haipo.

Pia alihoji ni vipi matumizi hayo yalikuwa yakiangaliwa kutokana na ukweli kwamba hakuna mwenye uwezo wa kumhoji mwingine, kati ya Menejimenti na TTB, juu ya matumizi ya fedha hizo, jambo ambalo Kamati iliona kama linatoa mwanya wa matumizi yasiyostahili.

kijibu, Dk. Nzuki alisema wamekuwa wakiomba kibali cha kutumia fedha hizo kutoka wizarani na kati ya hizo, Sh bilioni nne zinatoka serikalini, huku Sh bilioni tatu zikiwa ni makusanyo kutoka kwa wakala mbalimbali wakiwamo Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA).

Kamati ilimwagiza Msajili wa Hazina asiidhinishie TTB fedha nyingine hadi hapo majibu ya kuridhisha yatakapotolewa na Waziri kuhusu Bodi ya Wakurugenzi au atakapoiunda.

SEMINA: KAMPENI YA ONGEZEKO LA WATU DUNIANI

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO


UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII UNFPA WATAWASILISHA:


MADA: KAMPENI YA ONGEZEKO LA WATU DUNIANI: 7 BILLION ACTIONS GLOBAL CAMPAIGN


Lini: Jumatano Tarehe 26 Oktoba, 2011


Muda: Saa 09:00 – 11:00 Alasiri


MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni


WOTE MNAKARIBISHWA

Monday, October 24, 2011

Mtoto albino awafukuza waliokata mkono wake

MLEMAVU wa ngozi aliyekatwa mkono wake wa kulia na watu wasiojulikana, Kulwa Lusana (16), amesimulia alivyojikuta akiwafukuza wavamizi hao, huku akilia na kuwaomba wamrudishie mkono wake.

Kulwa ametoa maelezo hyao Polisi jana na kuongeza kuwa juhudi hizo za kudai kurudishiwa mkono wake, hazikuzaa matunda, kwani wakataji hao walizidi kutokomea gizani na kumuacha akitapatapa.

Baada ya kupoteza matumaini ya kuupata mkono wake, Kulwa alisimulia kwamba akiwa anagugumia kwa maumivu makali, alikimbilia kwenye nyumba ya baba yake ambapo aligongana naye mlangoni na wote kuanguka chini.

Mlemavu huo alifanyiwa unyama huo juzi saa 7 usiku katika Kijiji cha Mbizi, Kata ya Segese wilayani Kahama katika Mkoa wa Shinyanga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Diwani Athumani alisema watuhumiwa hao walivunja mlango na kuingia ndani kwa albino huyo na kuanza kumshambulia na kumjeruhi sikio na baadaye wakakata mkono wake wa kulia na kuondoka nao.

Kwa mujibu wa Kamanda Athumani, albino huyo alipiga kelele ya kuomba msaada kwa baba yake, Lusana Nkola ambaye hata hivyo wakati akitoka katika harakati za kumuokoa mtoto wake huyo, alipigwa jiwe kichwani akaanguka chini.

Alisema baada ya kufanyiwa unyama huo, watu hao waliufunga mkono huo kwenye mfuko na kuanza kukimbia nao na kutokomea pasipo julikana na kumuacha albino huyo akigugumia kwa maumivu makali.

Kutokana na tukio hilo, Polisi inamshikilia Petro Nkola mkazi wa kijiji cha Mtukula Runzewe wilayani Bukombe ambaye ni baba mdogo wa mlemavu wa ngozi, Kulwa Lusana (16).

Hata hivyo, Kamanda Athumani hakutaka kueleza kwa undani sababu za kumshikilia baba huyo zaidi ya kufafanua kuwa ni kwa mahojiano zaidi na uwezekano wa kuwapata watuhumiwa wengine waliotoroka na mkono wa mlemavu huyo.

Kulwa kwa sasa yupo katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama akiuguza jeraha lake na hali yake inaendelea vizuri.

Kamanda Athumani aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa watu wote watakaowadhani kuwa ni washiriki wa tukio hilo la kinyama alilofanyiwa mtoto huyo.

Tukio hilo limetokea ikiwa ni siku chache tu baada ya mlemavu mwingine wa ngozi, Adam Robert (14) kujeruhiwa kwa kukatwa na sime mkono wa kushoto na kunyofolewa vidole vya mkono wa kulia huko katika Kijiji cha Nyaruguguna wilayani Geita, mkoani Mwanza.

Katika tukio hilo la Geita, baba mzazi na mama wa kambo wa mtoto huyo, wanashikiliwa kwa tuhuma hizo.

Friday, October 21, 2011

Gaddafi: Mwanzo na mwisho

ALIYEKUWA kiongozi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi ameripotiwa kuuawa na wapiganaji wanaoongozwa na Baraza la Mpito nchini humo (NTC), baada ya mji wa nyumbani kwake, Sirte kunyakuliwa na vikosi hivyo jana.

Kifo cha Kanali Gaddafi (69) kilitangazwa rasmi na Waziri Mkuu wa Serikali ya mpito nchini humo, Mahmoud Jibril, muda mfupi baada kiongozi huyo aliyeitawala Libya kwa miaka 42 kuuawa.

Awali, msemaji wa NTC nchini Libya, Kanali Ahmed Bani alisema Kanali Gaddafi aliuawa na mwili wake ulipelekwa katika mji wa Misratah, bila kutoa ufafanuzi kamili kuhusu mazingira ya kifo hicho.

Taarifa za kuuawa kwake zilitolewa huku zikiambatanishwa na picha zinazoonyesha sura inayoonekana kuwa ni ya kiongozi huyo, katika muonekano wa nywele zake laini na ndefu wastani na uso uliotapakaa damu na majeraha.

Kanali Gaddafi anakuwa kiongozi wa kwanza kuuawa tangu kuanza vuguvugu la mageuzi katika mataifa ya kiarabu mwanzoni mwa mwaka huu, yaliyowaondoa madarakani Rais Ben Ali wa Tunisia na Hosni Mubarak wa Misri.

Kifo hicho kimetangazwa ikiwa ni miezi tisa tangu kuanza kwa upinzani mkali dhidi ya Serikali yake Februari mwaka huu, ambapo aliapa kwamba asingeondoka nchini Libya na kwamba yeye na wafuasi wake wangepambana hadi tone la mwisho la damu.

Kanali Gaddafi ambaye wakati wa utawala wake aliwahi kujipa wadhifa wa “mfalme wa wafalme wa Afrika” alikuwa akisifika kwa ukali wa sauti yake na maneno makali ya kuhamasisha na kueleza misimamo yake katika hotuba zake.

Mapambano hayo yameishia katika mji wa nyumbani kwake, Sirte ambao umekuwa na upinzani mkali kwa vikosi vya wapiganaji wa NTC ambavyo vililazimika kupambana kwa miezi kadhaa hadi waasi walipofanikiwa kuuteka jana.

Kanali Bani alisema mtoto wa Kanali Gaddafi, Mutassim ambaye walikuwa pamoja katika mji wa Sirte aliuawa na wapiganaji hao wa NTC.

Msemaji huyo aliwaambia waandishi wa habari kuwa kiongozi huyo alifariki dunia baada ya kujeruhiwa vibaya katika miguu yake yote na kichwani.

“Aliuawa katika mapambano na wapiganaji wetu. Kuna picha zinazoonyesha hayo,”alisema.

Alijificha kwenye karavati

Kwa mujibu wa taarifa za vyombo mbalimbali vya habari vya kimataifa, Kanali Gaddafi alidhibitiwa baada ya kukutwa amejificha katika karavati la barabarani, yeye pamoja na baadhi ya walinzi wake.

Kwa upande wake, kamanda wa wapiganaji wa baraza hilo, Abdul Hakim Belhaj pia alithibitisha kuwa Kanali Gaddafi alifariki dunia kutokana na majeraha aliyoyapata baada ya kukamatwa.

Makamu Mwenyekiti wa NTC, Abdul Hafiz Ghoga alithibitisha mbele ya waandishi wa habari kuwa Gaddafi aliuawa katika mji wa Sirte.

“Tunatangaza kwa dunia kuwa Muammar Gaddafi aliuawa katika mikono ya wanamapinduzi,” alisema Ghoga.

Katika mtiririko wa matukio yaliyokuwa yakirushwa katika vituo mbalimbali vya televisheni, kituo cha televisheni cha al-Jazeera kilionyesha picha za mwili wa Kanali Gaddafi ukiburuzwa katika eneo alilouawa.

Filamu za video zilizochukuliwa kwa simu za mkono zilionyesha kile kilichoonekana kuwa maiti ya Gaddafi iliyolowa damu. Mwili wake baadaye uliburuzwa na wapiganaji na kupakiwa nyuma ya gari aina ya pick-up.


Nato na Marekani zilieleza kuwa haziwezi kuthibitisha taarifa za kuuwawa kwa kiongozi huyo ambaye hajaonekana tangu NTC ilipoikamata Tripoli.

Watu washangilia mitaani

Wakati huohuo, katika mji wa Benghazi na miji mingine nchini humo, watu walionekana kukusanyika mitaani na kushangilia taarifa hizo za kuuawa kwa Gaddafi.

Viongozi mbalimbali duniani pia wamezungumzia kuhusu taarifa hizo za kuuawa kwa Kanali Gaddafi ambaye amewahi kuwa mpinzani mkubwa wa mataifa ya Ulaya na Marekani kutokana na misimamo yake dhidi ya mataifa hayo.

Miongoni mwa viongozi hao ni Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameroon ambaye alisema ni siku maalum ya kukumbuka maovu yote yaliyofanywa na Gaddafi.

Alisema watu wa Libya wako katika nafasi nzuri ya kujenga nchi imara na yenye demokrasia.

“Ninafurahi kazi ambayo Uingereza imesaidia katika kuuondoa utawala wa Gaddafi,”alisema.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Alain Juppe amepongeza kufikiwa mwisho kwa utawala wa miaka 42 ya Gaddafi.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon pia alisema kwamba kifo cha Kanali Gaddafi kinatoa mwanya wa “historia mpya kwa Libya”.

“Watu wanatakiwa watambue kuwa huu ni mwisho wa mwanzo. Sasa ni wakati wa Walibya wote kushikamana na kuwa kitu kimoja. Ni wakati wa kuponya majeraha na kujenga upya taifa. Si wakati wa visasi,” alisema Ki-Moon.

Balozi wa Libya nchini Uingereza, Mahmud Nacua alisema kuwa kuawa kwa Gaddafi kunamaanisha Libya inaelekea kwenye mustakhabali bora wa baadaye.
Wasifu wa Kanali Muammar Gaddafi

Alikuwa mtoto wa wafugaji wa Kibedui, mwenye maisha ya utata, lakini ambaye alitukuzwa sana, huku mataifa ya Magharibi yakimuona mtu wa hatari wakati wote.

Muammar Muhammad Gaddafi aliitawala Libya kwa zaidi ya miaka 40. Hadi mwanzoni mwa Machi 2011, alikuwa akiamini ndani ya moyo wake kwamba watu wake walikuwa wakimpenda na kwamba walikuwa tayari kumlinda hadi kufa kwa ajili yake.

Lakini wakati huo, tayari Gaddafi alikuwa ameshatumia njia za kikatili kuyazima maandamano dhidi yake, maandamano ambayo baadaye yaligeuka vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Kwa mujibu wa taarifa, watu zaidi ya 30,000 waliuawa kwenye vita hivyo. Mara nyingi sana, Gaddafi alitoa matamko makali wakati wa vita hivyo, ila linalojuilikana zaidi ni lile la kuwaita wapinzani wake kuwa ni panya.

Kwa kila hali, yaliyotokea ni mambo ambayo Gaddafi hakuyatarajia asilani. Mtoto huyu wa wafugaji wa Kibedui aliyezaliwa mwaka 1942, alikuja kuibuka kama mkombozi wa Walibya, alipompindua Mfalme Idriss hapo mwaka 1969.

Kuanzia hapo akaanza kujenga kile alichokiona mwenyewe kuwa ni mfumo wa kidemokrasia wa moja kwa moja. Alianzisha kamati za umma zilizoamua juu ya mustakabali wa umma na wa Serikali. Aliuita mfumo wake wa kisiasa na kiuchumi kuwa ni wa kisoshalisti, alioufafanua kwenye kijitabu chake cha Kijani.

Historia yake kiufupi

Alizaliwa mwaka 1942 katika eneo la Jangwa, kwenye mji wa Sirte, katika familia ya baba Mohamed Abdulsalama Abuminiar na mama Aisha Ben Niran. Alijiunga na Jeshi la Libya mwaka 1965.
Alifanya mapinduzi ya Serikali yasiyo ya umwagaji damu na kumuondoa mfalme Idris katika utawala wake mwaka 1969 na kuwa mtawala wa Libya akiwa na umri wa miaka 27.

Alikuwa maarufu kwa nguo anazopenda kuvaa na walinzi wa kike wenye kubeba silaha, kiongozi huyo wa Libya pia anadhaniwa kuwa na mbinu nzuri za kisiasa kwa kuweza kuirejesha Libya kutokana na kutengwa kidiplomasia duniani.

Baada ya miongo miwili ya kutengwa katika jamii ya kimataifa, mwaka 2003, Tripoli ilikiri kuwa walifanya shambulio la Lockerbie kwa kuiangamiza kwa mabomu ndege ya Pam Am. Umoja wa Mataifa (UN) ulikubali kuondoa vikwazo dhidi ya Libya.

Baada ya miezi kadhaa, Serikali ya Kanali Gaddafi ilisitisha mipango yake ya kuunda silaha za maangamizi na hii ikarejesha ushirikiano na nchi za Magharibi.

Gaddafi ni mtu wa kipekee katika kauli zake, mienendo yake, tabia zake na mikakati yake, kwa mujibu wa Saas Djebbar, mtaalam wa siasa za Libya.
Alipokuwa kijana alivutiwa na kiongozi mzalendo wa Misri, Gamal Abdel Nasser, alipokuwa akishiriki katika maandamano dhidi ya Israel wakati wa mtafaruku wa Suez mwaka 1956.

Alipanga njama ya kupindua utawala wa kifalme alipokuwa mwanafunzi wa kijeshi alipokuwa mafunzoni Uingereza kabla ya kurejea nyumbani Libya. Alipanga mapinduzi ya Septemba 1, 1969 akiwa katika mji wa Benghazi.

Alianza kujenga itikadi zake za kisiasa mwaka 1970 na kuziandika katika kitabu chake cha kijani kibichi.
Alikitumia kitabu chake kuanzisha mfumo wa kisiasa uliojumuisha kanuni za Kiislamu na mfumo ulio tofauti na siasa za ujamaa au ubepari.

Mwaka1977 aliasisi mfumo ujulikanao kama 'Jamahiriya' au 'Taifa la Umma' ambapo raia ndio wanaoendesha uongozi wa nchi yao kupitia 'kamati za umma'.

Mfumo huo wa Gaddafi umevuka mipaka na hauhusishi mambo ya siasa tu, bali pia mambo mengine.
Akiwa safarini ng'ambo, alikuwa akitumia makazi maalum kwenye kambi iliyojengwa na hema yake ya kifahari ya Kibeduwi akiwa amefuatana na walinzi wanawake ambao, inasemekana, huwa hawapotezi umakini kazini kama walinzi wanaume.Hema hiyo pia ilitumiwa kuwalaki wageni wa Libya na Kanali Gaddafi huendesha mikutano na mahojiano yake humo humo akipepea usinga au tawi la mitende.

Rais wa zamani wa Marekani Ronald Reagan alimwita Gaddafi 'mad dog' yaani 'mbwa kichaa' na Marekani ililipiza kisasi dhidi ya Libya kwa madai ya kuhusika na mashambulio ya anga barani Ulaya kwa kuvamia miji ya Tripoli na Benghazi mwaka 1986.Aliposhindwa katika jitihada zake za kuzipatanisha nchi za Uarabuni katika miaka ya 90, Kanali Gaddafi alielekeza nguvu zake barani Afrika na kupendekeza 'Muungano wa Nchi' za bara la Afrika.

Alianza kuvaa mavazi yake binafsi, sare za michezo zilizo na ngao za Bara la Afrika au picha za viongozi kutoka bara hilo.Aliwahi kuvunja na kufuta Wizara za nchi hiyo pamoja na bajeti zao, isipokuwa Wizara chache ikiwemo ya Ulinzi, Fedha na Mambo ya Nje.Licha ya uchumi wa Libya kutoa fursa kwa wawekezaji wa nje, mabadiliko bado yanakwenda taratibu.

Vuguvugu la mageuzi dhidi yake lilipoanza mwanzoni mwa mwaka huu, aliapa kuwafuata wanaompinga nyumba hadi nyumba, mlango kwa mlango, hatua iliyoibua hasira na kuchochea harakati za kijeshi dhidi yake.

Baada ya baadhi ya askari kutangaza kujitoa katika jeshi lake na kuanzisha uasi, aliapa kwamba atapambana hadi tone la mwisho la damu litakapomwagika. Alisisitiza kwamba kamwe hatakimbia kutoka katika ardhi ya Libya, atafia katika ardhi ya mababu zake.

Taarifa zilieleza jana kwamba aliuawa baada ya kukutwa akiwa amejificha katika daraja dogo kwa ajili ya kupitisha maji barabarani (karavati).

Mara baada ya kuuawa, wapiganaji wa Baraza la Mpito waliokuwa katika mapambano dhidi yake walibaini kwamba alikuwa na bastola iliyotengenezwa kwa dhahabu tupu.

Thursday, October 20, 2011

Wananchi watakiwa kusimamia kesi za ukatili zifike mahakamani

Na Ananilea Nkya Mkurugenzi Mtendaji TAMWA.

WANANCHI wa Mkoa wa Kusini Unguja wameshauriwa kusimamia kesi zao zinazohusu ukatili wa kijinsia kuhakikisha zinafikishwa katika vyombo vya sheria. Mkuu wa upelelezi na makosa ya jinai, mkoa wa Kusini Unguja SSP Makaran Khamis Ahmed amesema kesi nyingi za ukatili hazifikishwi Mahakamani kutokana na wananchi kuanzisha tabia ya kuhukumu kesi katika ngazi za shehia, kijiji na familia pamoja na kukubali kuzifuta katika vituo vya polisi.

Makarani alitoa ushauri huo ofisini kwake Mwera alipokutana na wanaharakati kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa mashtaka ya jinai (DPP) na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Zanzibar kufuatia wimbi la ongezeko la kesi za ukatili ambazo hazifikishwi mahakamani.

Alisema kuna matatizo katika vituo vya polisi katika mpango mzima wa kushughulikia kesi za udhalilishaji wa kijinsia lakini jamii pia ina tatizo kubwa la kuchelewa kufikisha kesi katika vituo vya polisi kutokana na kuzifanyia maamuzi katika ngazi zisizo rasmi.

“Tatizo hili la jamii wakati mwengine pia huchangia kuharibika kwa uchunguzi, kwa hivyo ni vizuri kuripoti kwa wakati muafaka na kuwabainisha askari wakorofi ambao wanazuia haki kuchukua mkondo wake”, alisema Ofisa huyo wa upelelezi mkoa wa Kusini Unguja.

Ofisa wa TAMWA anayeshughulikia mabadiliko ya jamii Zanzibar Asha Abdi alisema tangu mwaka 2009 hadi sasa zaidi ya kesi 10 zilifikishwa katika vituo mbalimbali vya polisi lakini ni kesi tatu tu ndizo zilizopelekwa mahakamani.

Alisema kutokana na hali hiyo waliamua kufuatilia kesi hizo kwenye ofisi ya Mwendesha mashtaka ambapo pia walielezwa kuwa hazikufikishwa huko na ndipo walipoamua kuzifuatilia kesi hizo katika polisi ya mkoa huo.

Kesi nyingi za ubakaji na watoto wenye umri chini ya miaka 18 kubebeshwa mimba zimetokea katika shehia za Mzuri, Kidimni, Michamvi, K/dimbani, K/mkwajuni, Unguja Ukuu, na Mtende.

Lowassa: Uvumilivu sasa basi

WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa amevunja ukimya na kuzungumzia tuhuma mbalimbali zinazoelekezwa kwake, huku akisisitiza kuwa sasa amechoka kukashifiwa.Alisema kuanzia sasa hatakubali kuchafuliwa jina lake na mtu yeyote au chombo chochote cha habari na atakayefanya hivyo, ajiandae kukabiliana na mkono wa sheria.

Lowassa alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake katika Kijiji cha Ngarash Wilaya ya Monduli, Arusha kuhusu tuhuma mbalimbali zinazoelekezwa kwake, ikiwamo ya kuandaa na kuongoza mpango mkakati wa kumhujumu Rais Jakaya Kikwete.

“Imetosha. Sasa nimeamua kukabiliana na yeyote atakayenichafulia jina na kunizulia mambo ya uongo. Nitatumia vyombo vya sheria na tayari nimewaelekeza mawakili wangu kufanya hivyo,” alisema,

“Baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu sasa, nimeamua kuanza kuchukua hatua mbalimbali za kisiasa na kisheria ambazo naamini zitatoa majibu sahihi dhidi ya wale wote walio nyuma ya ajenda hizi chafu kwa lengo la kuweka kumbukumbu sawia ndani ya chama changu na kwa jamii nzima ya Watanzania ambao kwa muda mrefu wamelishwa mambo mengi ya kizushi na wakati mwingine ya hatari dhidi yangu,” alisema.

Alisema tayari amepanga kuanza kuwasiliana na kuwasilisha malalamiko yake kwa mamlaka husika zinazosimamia mienendo ya kimaadili na weledi wa kitaaluma wa vyombo vya habari kama vile Msajili wa Magazeti na Baraza la Habari Tanzania (MCT).

“Kama hiyo haitoshi, baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu nimeshaanza kufikiria na kujipanga kuanza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waandishi wa habari na wahariri ambao kwa makusudi wameamua kutumia vibaya uhuru wa habari ambao serikali imeutoa. Naamini sote tunakubaliana kuwa uhuru usio na nidhamu ni fujo.

Katika mkutano huo, Lowassa pia alikanusha madai kuwa hivi sasa yeye na baadhi ya wanaCCM, wanakusanya taarifa na vielelezo vya mabaya ya Rais Kikwete ili kuyawasilisha kwenye vikao vya chama.

Alisema katika mkakati huo, mahasimu hao wamekuwa wakivitumia baadhi ya vyombo vya habari na kufikia hatua ya kudai kuwa ameanza kuandaa orodha ya kile anachokiita madhambi ya Rais Kikwete ambayo wanadai kuwa amepanga kuyasoma wakati wa kikao kijacho cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM.

Alisisitiza kuwa ni jambo lisiloingia akilini kumhusisha yeye na kile kinachoitwa mkakati wa kumhujumu Rais Kikwete au CCM ambacho alisema ni mbunge anayetokana na chama hicho na kiongozi wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

“Kuhusu hili, napenda kusema kwa uwazi kwamba, mbali ya ukweli kuwa sijapata kufikiria hata mara moja kuhusu hicho wanachokiita mabaya au madhambi ya Rais, sina na wala siijui hiyo wanayoitaja kuwa ni orodha ya mabaya ya namna yoyote dhidi ya Rais Kikwete,” alisema na kuongeza:

“Siyo kweli. Nampenda, namwamini na kumheshimu Kikwete ambaye urafiki wetu haukuanzia barabarani kama baadhi wanavyodhani. Kwanza sijui mabaya ya mheshimiwa Rais. Najua mazuri yake mengi lakini siyo mabaya, hivyo sina nia ya kuyatafuta. Siwezi kumhujumu Rais wala chama changu. Naamini hata mheshimiwa Kikwete pia hawezi kuamini uongo huo.”

Alisema awali, alikuwa akiyapuuza madai mengi yanayoelekezwa kwake lakini amelazimika kuvunja ukimya kwani uongo ukizungumzwa mara nyingi bila maelezo sahihi kutolewa, unaweza kugeuka kuwa ukweli na watu wakauamini.

Richmond na kujivua gamba

Kuhusu tuhuma za kampuni ya kufua umeme ya Richmond na falsafa ya kujivua gamba, Lowassa alisema atazizungumzia muda mwafaka ukifika lakini, akasisitiza kuwa atafanya hivyo kupitia vikao rasmi vya chama.

“Mimi nimetumikia CCM kwa takriban maisha yangu yote tangu nilipohitimu Chuo Kikuu Mlimani mwaka 1977. Ni kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja pekee ndicho nimekuwa nje ya mfumo wa chama nilipokuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC). Najua kuwa kupitia vikao ndiyo mtu unaweza kujenga hoja kukabiliana na zile usizozikubali,” alisema.

Alisema hataki kuzungumzia masuala hayo nje ya vikao kukwepa kufanana na baadhi ya viongozi wanaofanya hivyo kwa kutumwa na maslahi na utashi binafsi kwa lengo la kujipatia umaarufu na kuchafua wengine.

Maandamano ya UVCCM Arusha

Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli alikana kuhusika kwa namna yoyote na maandamano na malumbano yanayoendelea sasa ndani ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), unaomhusisha Mwenyekiti wa Mkoa wa Arusha, James Ole Millya na makundi mengine akisema kipindi yanatokea alikuwa Ujerumani kwa matibabu.

Hata hivyo, alishauri sauti za vijana zisipuuzwe kwani kufanya hivyo ni hatari kwa chama na taifa kwa ujumla kutokana na uwezo wa kundi hilo katika kufikiri, kuamua na kufanya mambo.

“Mzee Kingunge (Ngombale) alitufundisha kuwa vijana damu yao inachemka haraka na uamuzi na matendo yao yanafanyika kwa mtindo huohuo damu yao inavyochemka. Jambo muhimu ni kuwasikiliza, kujadiliana nao na kuwarekebisha kwa amani pale wanapokosea, kamwe wasipuuzwe wala kukaripiwa na kukandamiza mawazo yao,” alisema Lowassa.

Alitoa mfano wa maandamano waliyofanya enzi zao za ujana kupinga ziara ya mmoja wa mawaziri wa Marekani aliyetembelea nchini akisema licha ya kusukwasukwa na polisi, Mwalimu Julius Nyerere na Serikali yake haikupuuza hata kidogo hisia, mawazo na kitendo chao.

Alisema iwapo kuna uvunjifu wa sheria uliotokea katika harakati za vijana hao kuwasilisha mawazo na kutekeleza majukumu yao ni vyema sheria ikachukua mkondo wake bila kuonekana wanatiwa kashkashi, kwani hakuna aliye juu ya sheria.

Ugumu wa maisha na ukosefu wa ajira

Akirejea kauli yake aliyowahi kuitoa kuhusu ugumu wa maisha na ukosefu wa ajira kwa vijana nchini, Lowassa alisema tatizo hilo ni bomu linalosubiri muda wa kulipuka, iwapo hatua madhubuti na za haraka hazitachukuliwa.

“Kama taifa tufanye uamuzi mgumu wa kukopa fedha kutoka taasisi za ndani na nje, tujenge viwanda badala ya kusubiri uwekezaji kutoka nje ambako nako kuna tatizo sawa na hili linalotukabili. Waasisi wetu walifanya hivyo na kufanikiwa. Naamini sisi pia tunaweza tukiwa na nia thabiti ya kukuza uchumi wetu na kuongeza ajira kwa vijana wanaohitimu katika taaluma mbalimbali.”

Alisema hata Marekani na nchi za Ulaya zinazohimiza na kutekeleza sera ya uchumi wa kibepari, zimeanza kuchukua hatua zinazofanana na zinazotekelezwa katika ujamaa kwa kusaidia taasisi na kampuni za nchini mwao ili kukuza uchumi wao na kulinda ajira za wananchi.

Kampeni za urais 2015

Akionyesha kushangazwa na kitendo cha mjadala wa mrithi wa Rais Kikwete kutawala duru za siasa nchini sasa mwaka mmoja tu tangu kufanyika uchaguzi mkuu, Lowassa alisema hiyo: “Si salama kwa nchi wala amani yetu kila jambo nchini kutawaliwa na mjadala wa urais mwaka 2015.”

“Tumeacha kujadili mustakabali wa taifa kwa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yanayoikabili jamii yetu na hili ni changamoto kubwa kwa vyombo vyetu vya habari ambavyo vinawajibu wa kuendeleza mijadala yenye tija kwa taifa, badala ya kukubali kutumika na wanasiasa wenye malengo yao binafsi.”

Alivitaka vyombo vya habari kuchukua jukumu la kuongoza mijadala ya kusaidia jamii kutafuta ufumbuzi wa ajira kwa vijana, uchumi na kulinda amani, utulivu na mshikamano alioeleza kuwa umeanza kutikiswa kwa vitendo na maneno ya watu wachache wenye malengo binafsi dhidi ya maslahi ya umma.

Wednesday, October 19, 2011

Lowassa Kutoa Ya Moyoni Leo

MILLYA ACHAFUA HALI YA HEWA CCM, ASEMA MAISHA YAKE YAKO HATARINI

WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa leo anatarajiwa kuzungumza na vyombo vya habari katika mkutano ambao utazungumzia mambo makuu matatu likiwamo suala la Kampuni ya kufua umeme ya Richmond ambalo lilisababisha ajiuzulu wadhifa huo, Februari 2007. Mkutano huo wa Lowassa unafanyika siku moja tangu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Arusha, James Millya atoe matamshi makali akiwatuhumu aliowaita watoto wa vigogo kwamba wanavuruga umoja huo huku akilalamika kwamba: “Maisha yake yapo hatarini.” Habari zilizopatikana jana kupitia kwa watu walio karibu na Lowassa zinasema, katika mkutano huo, Mbunge huyo wa Monduli (CCM), pia atazungumzia taarifa zinazomhusu ambazo zimekuwa zikichapishwa katika baadhi ya vyombo vya habari nchini.

Suala jingine ambalo linatarajiwa kuzungumzwa na kiongozi huyo ni kuhusu mgogoro ndani ya CCM mkoani Arusha, ambao unatokana na mgawanyiko miongoni mwa makada na viongozi wa chama hicho. “Pia anasema kwamba ataanzia pale alipoishia, siku ile alipozungumza bungeni kuhusu Serikali kufanya uamuzi mgumu lakini hakutakuwa na kumshambulia mtu,” alisema mmoja wa watu hao na kuongeza:

“Anasema (Lowassa) kwamba lazima aweke kumbukumbu sahihi kwa baadhi ya mambo ambayo yametamkwa na baadhi ya viongozi wa kisiasa na viongozi wengine kwani amebaini kuwa uongo ukisemwa sana na kwa muda mrefu hugeuka kuwa ukweli.”

Soma zaidi www.kwanzajamii.com

Tuesday, October 18, 2011

Zitto, January wamkalia kooni Ngeleja

- WASEMA KAMA AMESHINDWA UWAZIRI AACHIE NGAZI

WENYEVITI wa Kamati za Bunge za Nishati na Madini, January Makamba na Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Zitto Kabwe wamesema ikiwa hali ya umeme itaendelea kuwa mbaya nchini, itamlazimu Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja kujiuzulu.Kadhalika, wenyeviti hao wamesema hakutakuwa na uhalali wa Serikali kuzilipa kampuni zilizopewa jukumu la kuzalisha umeme wa dharura ikiwa umeme huo hautapatikana katika muda uliotarajiwa.

Wakizungumza Dar es Salaam juzi usiku kwenye mdahalo kuhusu ‘Hali ya Umeme nchini na Tanzania tunayoitaka’ ulioandaliwa na Kampuni ya Vox Media, wabunge hao waliuponda mpango wa dharura wa Serikali wa kukabiliana na mgawo wa umeme wakisema hautekelezeki.Katika mdahalo huo uliorushwa moja kwa moja na Kituo cha Televisheni cha Star, January alisema: “Bora kutokuwa Waziri kuliko kuwa waziri ambaye kauli zake haziaminiki kwa umma.”

Alisema kwa kushindwa kutekeleza ahadi zake za kuondoa mgawo wa umeme, lazima waziri husika awajibike kama ambavyo imekuwa ikifanyika katika nchi za magharibi.

Hata hivyo, January ambaye ni pia Mbunge wa Bumbuli (CCM) na Katibu wa Mambo ya Nje na Siasa wa CCM, alisema suala la kujiuzulu kwa waziri linategemea zaidi uadilifu wake na mamlaka iliyomteua kushika wadhifa huo.

Kwa upande wake, Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema) alisema: “Niliwahi kusema bungeni kwamba kila waziri aandike barua ya kujiuzulu ‘in advance’ (mapema) ili pale anaposhindwa kutekeleza wajibu wake, kazi ya Spika inakuwa ni kuchukua ile barua na kumkabidhi Rais.”

Alisema katika hali ya sasa, Serikali imeshindwa kutimiza ahadi iliyoitoa bungeni kuhusu utekelezaji wa mpango wa dharura wa kuzalisha umeme ili kuwezesha nchi kuondokana na mgawo na kwamba hilo tu linatosha kumfanya waziri ajiuzulu wadhifa wake.

Mpango wa dharura Wabunge hao walisema kuna kila dalili kwamba huenda mpango wa dharura wa kukabiliana na giza nchini ambao uliwasilishwa na Serikali bungeni usitekelezeke.

Mpango huo ni ule uliowasilishwa bungeni na Waziri Ngeleja Agosti 13, mwaka huu akiliomba Bunge liidhinishe kiasi cha Sh523 bilioni kwa ajili ya utekelezaji wake. Mpango huo unaonyesha kuwa kutokana na dharura hiyo, Tanesco lilitarajiwa kukusanya kiasi cha Sh115 bilioni kutoka kwa wateja wake, hivyo kubakisha pengo la Sh408 bilioni ambazo Serikali iliahidi kwamba ingezitafuta katika vyanzo vingine.

Zitto alisema kutokana na hali hiyo, wabunge wanatarajia kuhoji katika Mkutano wa Tano wa Bunge la 10 unaotarajiwa kuanza Novemba 8, mwaka huu mjini Dodoma na kuitaka Serikali iwe na majibu.

“Kuna masuala ya ‘procurement’ (ununuzi), sheria lazima ifuatwe sasa ukiangalia mfano watu wa NSSF (Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii) ambalo linatakiwa kuzalisha megawati 150, hadi sasa bado hawajaanza kuingiza umeme kwenye gridi ya taifa, lakini Serikali ilileta mpango wake na wakasema wana uwezo wa kuutekeleza, kazi yetu ni kusubiri majibu,” alisema Zitto.

Alisema katika mchakato wa kutafuta mashine za kuzalisha umeme, NSSF lilinusurika kutapeliwa pale wataalamu wake walipofika Marekani na kubaini kwamba mtu waliyekuwa wakiwasiliana naye kwa ajili ya kupata mtambo huo, hakuwa na mashine wala kampuni ya aina hiyo.

Kauli hiyo iliungwa mkono na January aliyesema: “Kwanza ukiangalia mpango wenyewe wa dharura, vyanzo vyote ni vya mafuta au mafuta mazito ya dizeli au ya ndege. Huu umeme ni ‘very expensive’ (ghali mno), kwa nchi ambayo ni tajiri wa makaa ya mawe, gesi asilia na rasilimali nyingine.

Ni ‘scandal’ (kashfa) kutumia umeme huu,” alisema January na kuongeza: “Nasema ni ‘scandal’ (kashfa) kwa sababu kitaalamu umeme unaotokana na makaa ya mawe gharama yake ni senti 10 hadi 12 za Marekani kwa megawati moja, gesi ni kati ya senti za 8 hadi 12 za Marekani wakati umeme wa mafuta ni senti kama 42 za Marekani, sasa mtaona jinsi tunavyopoteza fedha nyingi kwa sababu zisizo za msingi.”

Alisema ukodishaji wa mitambo ya umeme wa dharura inayotumia mafuta ni mzigo kwa walipa kodi ambao ni maskini na kwamba fedha zinazotumika zingeweza kugharamia shughuli nyingine za maendeleo.

Alisema kwa taarifa alizonazo, kampuni ambazo tayari zimeingiza umeme wa dharura ni Symbion (megawati 37), IPTL (megawati 80) na Agrreko (megawati 50) na kwamba kiasi hicho cha umeme hakifikii nusu ya kile kilichoahidiwa na Serikali bungeni ambazo ni megawati 572 hadi Desemba mwaka huu.

Mbunge huyo alisema ikiwa umeme huo wa dharura hautapatikana wote ifikapo Desemba, basi hakutakuwa na maana ya dharura na kwamba hapo Serikali itabidi ipitie upya suala la malipo kwa kampuni husika.

“Dharura maana yake ni kutupatia umeme ‘within’ (kati ya) sasa na Desemba, sasa kama hadi leo NSSF hawajaweza kutupa zile megawati 50 tulizoahidiwa kwamba zitakuwa tayari Septemba na tunawadai na hizi nyingine za Oktoba, sidhani kama wanaweza kutimiza ahadi hiyo, hivyo lazima hili tuliangalie na hii ni kazi yetu sisi wabunge,” alisema January.

Chini ya mpango wa dharura, NSSF wanatarajiwa kuingiza katika gridi ya taifa megawati 150 za umeme, Symbion megawati 205, Agrreko megawati 100 na IPTL megawati 80 ambazo tayari zimeingizwa baada ya kupatikana kwa mafuta mazito.

Vyanzo mbadala Kutokana na athari za mgawo wa umeme, wabunge hao waliitaka Serikali kuchukua hatua za kutekeleza ushauri ambao umekuwa ukitolewa na wabunge na wataalamu wa nishati.

Katika matamshi yao, wabunge hao kutoka kambi mbili tofauti bungeni, walikubaliana kwamba kimsingi suala la matumizi ya gesi na makaa ya mawe ndiyo suluhisho la matatizo ya nishati ya umeme nchini lakini wakaiponda Tanesco kwamba haina uwezo wa kusimamia sekta hiyo peke yake.

Kwa mujibu wa takwimu za kitaalamu, miradi ya makaa ya mawe ya Ngaka mkoani Ruvuma, Kiwira mkoani Mbeya na Mchuchuma mkoani Iringa, ina uwezo wa kuzalisha megawati 1,500 za umeme kwa miaka 150, hivyo kulisaidia taifa kuondokana na giza.

Zitto alisema suala la Tanesco kufanyiwa marekebisho kwa maslahi ya Taifa halina mjadala ili kuliwezesha kufanya kazi kwa ufanisi tofauti na sasa ambako limeshindwa kukidhi matakwa ya umma.

“Shirika hili linaweza kugawanywa sehemu mbili, kukawa na uzalishaji peke yake na sehemu ya usafirishaji na usambazaji nazo zikawa peke yake maana hivi sasa haliwezi kufanya kazi yake ipasavyo,” alisema Zitto.

Hata hivyo Naibu Kiongozi huyo wa upinzani Bungeni na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, aliwalaumu wanasiasa kwa kuingilia utendaji wa Tanesco na kwamba matatizo mengi ya shirika hilo la umma, yamechangiwa na kutolewa kwa maelekezo ya kisiasa yanayopingana na utaalamu.
“Lazima sasa kila mtu atekeleze wajibu wake, Tanesco tuwaachie wataalamu, Serikali ibaki na masuala ya kisera na sisi wabunge tubaki na ‘role’ (nafasi) ya usimamizi, hapo tutasonga mbele,” alisisitiza Zitto.

Katika maoni yake, January alisema Tanesco haiwezi kumudu kusimamia miradi mikubwa ya umeme na kwamba ipo haja ya kugawanywa katika sehemu tatu kwa maana ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme ili kuongeza ufanisi wake.

Alisema kugawanywa kwa shirika hilo kutapunguza upotevu wa umeme ambao kwa takwimu za mwaka jana, ulipotea kwa asilimia 25, kiwango ambacho ni sawa na umeme wote uliotumiwa viwandani au asilimia 75 ya umeme wote unaozalishwa na kampuni ya Songas.

“Kuna matatizo mengi sana ambayo yanapaswa kutatuliwa, kwani upotevu wa umeme mwingi kwa kiasi hiki na ni hatari sana, nadhani marekebisho yatakayofanywa yanaweza kusaidia kuondoa matatizo hayo,” alisema.

Ngeleja, Tanesco Katika mdahalo wa juzi, viongozi wa Serikali waliingia mitini kwa maelezo kwamba Waziri pamoja na watendaji wote wa sekta ya umeme katika Wizara ya Nishati na Madini wako safarini.

Mwenyekiti wa Mdahalo huo, Rosemary Mwakitwange alisema, Waziri Ngeleja alikuwa amealikwa na kwamba kulikuwa na ahadi kwamba lazima Serikali ingewakilishwa lakini akashangazwa na kutoshiriki kwao katika tukio hilo.
Kwa upande wake, Tanesco liliwakilishwa na Mkurugenzi wake wa Uwekezaji, Katyega Maneno ambaye alipata wakati mgumu pale alipotakiwa kujibu hoja za washiriki wa mdahalo huo.

Katyega alisema Tanesco linafanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa umeme wote wa dharura unaanza kuzalishwa kabla ya Desemba mwaka huu kama Serikali ilivyoahidi.

“Tumeshajiandaa hata kama itatokea kampuni moja ikashindwa kutimiza mahitaji yetu, basi tuko tayari kila kitu kitakwenda sawa. Hata sasa kuna unafuu kwani makali ya mgawo yamepungua,” alisema Katyega.
Jana, gazeti hili lilimtafuta Ngeleja kupitia simu zake mbili za kiganjani ili kufahamu msimamo wake kuhusu kuelekea kushindwa kwa mpango wa dharura bila mafanikio.

Hata hivyo, waziri huyo aliwahi kukaririwa akisema hayupo tayari kujiuzulu kwa maelezo kwamba yeye si chanzo cha matatizo ya umeme nchini.
Alisema hayo Julai 19, mwaka huu mjini Dodoma, siku moja baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuondoa bungeni bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ili iandaliwe upya baada ya kuwa imekataliwa na wabunge.

Kukataliwa huko ndiko kulikozaa mpango wa dharura ambao sasa unaonekana kutotekelezeka hivyo kumweka waziri huyo kwenye wakati mgumu zaidi Bunge litakapokutana tena mwezi ujao.

Ngeleja katika maelezo yake, alisema tatizo la nishati ya umeme ni la Serikali nzima na si yeye peke yake anayepaswa kulaumiwa.

Thursday, October 13, 2011

Kisa cha Julius Kambarage Nyerere, 1952 - 7

Harakati za TAA na baadaye TANU ziliendelea. Katika sehemu hii ya makala, mwandishi MOHAMED SAID ambaye amefanya utafiti wa mambo yalivyokuwa Tanganyika kabla na baada ya uhuru, anaendelea kusimulia harakati zilivyokuwa…

INASEMEKANA kwamba ilikuwa wakati huu Abdulwahid kwa mara ya pili alimshauri Nyerere kujiuzulu kufundisha ili ashughulike na kazi za TAA.

Wazo hili halikumvutia Nyerere kama vile ambavyo halikumvutia Chifu Kidaha Makwaia miaka minne iliyopita. Lakini Nyerere alipiga hatua moja mbele kuliko Chifu Kidaha. Angalau Nyerere alikuwa amekubali kuiongoza TAA.

Nyerere alikuwa anajua vyema wakati huo kwamba TAA ilikuwa ikiendeshwa kutoka mifuko ya wazalendo ambao idadi yao haikuzidi watu wanne. Ni dhahiri kuwa Nyerere hakutaka kuishi kwa kutegemea msaada hata ikiwa wafadhili wake walikuwa na nia njema.

Kilichosukuma ule uongozi wa ndani wa TAA kusisitiza juu ya Nyerere kujiuzulu kazi na kuchukua uongozi wa TAA ilikuwa kwanza, ule ukweli kuwa TAA ilikuwa ikifanya kazi kama chama cha siasa na Gavana alikuwa akifahamu hivyo.

Pili, mpango ulikuwa mbioni kusajili chama cha siasa kabla ya mwisho wa mwaka wa 1954.

Wakati huo huo TAA ilikuwa ikishughulikia rasimu ya katiba ya chama kipya na mipango ilikuwa ikiendelea kwa rais wa chama cha siasa kilichokuwa kikitarajiwa kusafiri kwenda Umoja wa Mataifa, New York kutoa madai ya Tanganyika mbele ya Baraza la Udhamini kama Japhet Kirilo alivyofanya miaka miwili iliyopita.

Vilevile ilikuwa muhimu uongozi wa TAA uwe na rais aliyekuwa anafanya kazi ya chama kwa muda wote wakati chama kipo mbioni kuundwa.

TAA ilikuwa inafungua ukurasa mpya, ikijiondoa kutoka zile siasa za baada ya vita, za mapambano; na kuelekea katika siasa za mazungumzo na mapatano. Kulikuwa hakuna wasiwasi wowote kuwa TAA ilikuwa na udhibiti kamili wa siasa nchini kote.

Katika miaka yote 25 ya kuweko kwa TAA hakuna chama chochote kilichozuka kuipinga. Kwa miaka mingi TAA ilidhihirisha uhalali wake wa kuwapo kama mwakilishi wa kweli wa Waafrika.

TAA ilikuwa na mpinzani mmoja tu wa kupigana naye, nayo ilikuwa ni serikali ya kikoloni ya Uingereza.
TAA iliunda itikadi na uongozi wake wenyewe kuwaunganisha watu wote kama chama cha Waafrika kilichoungwa mkono na umma dhidi ya utawala wa Kiingereza.

Sasa Tanganyika ilikuwa ikichemka pole pole kutokana na kampeni za TAA, manungíuniko ya wananchi yakitumika dhidi ya serikali.

Hili lilikuwa jambo jipya kwa serikali ya kikoloni. Kutokana na hali hii ya manungíuniko ya wananchi wa Tanganyika, Gavana Twining katika hotuba yake kwa Baraza la Kutunga Sheria mnamo Mei, 1954 aliwashambulia viongozi wa TAA kwa maneno haya, “Nimefahamishwa juu ya mambo yanafanywa katika baadhi ya sehemu humu nchini na watu wanaojitafutia makuu.

Hawa ni watu wakorofi, ambao baada ya kujiteua wao wenyewe kuwa viongozi wa siasa, wanajaribu kuwachochea watu dhidi ya tawala za kienyeji na wakati mwingine dhidi ya Serikali Kuu, kwa kutumia malalamiko ya sehemu hizo ya kweli au ya kubuni...

Jambo hili haliwezi kuruhusiwa kuendelea na serikali haitavumilia vitendo kama hivyo ambavyo viko kinyume na maslahi ya watu na vimekusudiwa kuiharibu ikiwa siyo kuiangamiza serikali. Heshima kwa serikali, ambayo ni tabia ya asili katika silika ya Waafrika lazima idumishwe…”

Hotuba hii ilijaa vitisho. Baada ya hotuba hii serikali ilichukua mfululizo wa hatua za ukandamizaji na vitisho dhidi ya viongozi wa TAA, ikitumia mbinu zote, zilizokuwa dhahiri na za siri. Wakati huu na hususan baada ya kuchapishwa kwa ile Sekula ya Serikali No.5 ndani ya Government Gazette mwaka wa 1953 na kufuatia kuvunjika kwa Pan African Congress ambao wajumbe kutoka Tanganyika walikuwa Ally Sykes na Denis Phombeah, walikamatwa Rhodesia na kurudishwa nchini.

Serikali ya kikoloni sasa iliimarisha Special Branch kwa kumwaga mitaani makachero na vibaraka. Ally Sykes tayari alikuwa akijulikana kwa msimamo wake wa kupinga ukoloni na Abdulwahid kwa uongozi wake katika TAA waliandamwa na hawakuwa na pa kujificha, walifuatwa fuatwa na makachero kokote walikokwenda.

Makachero walikuwa na kazi kutafuta habari mjini na baadhi yao waliwekwa nje ya ofisi ya Abdulwahid pale katika soko la Kariakoo.

Katika kipindi hiki Abdulwahid alianza kutumia hati mkato katika kumbukumbu zake za mikutano ya TAA na katika kuandika shajara (diary) yake mwenyewe. (Hizi shajara ziko hadi leo na zimehifadhiwa).

Joto la siasa lilikuwa katika kiwango kama hiki wakati wajumbe kumi na saba wa TAA kutoka kwenye matawi majimboni na makao makuu walipokutana mjini Dar es Salaam tarehe 7 Julai, 1954, kujadili katiba mpya ya chama kipya cha siasa - TANU.

Jimbo la Mashariki ambalo lilikuwa na wajumbe wengi kushinda yote liliwakilishwa na, ndugu wawili Abulwahid na Ally Sykes, Dossa Aziz, Tewa Said Tewa, Patrick Kunambi, Kasella Bantu, John Rupia, Julius Nyerere na C. O.Milinga; Jimbo la Kaskazini liliwakilishwa na na Joseph Kimalando na Japhet Kirilo; Jimbo la Ziwa liliwakilishwa na Abubakar Kilanga, L. M. Makaranga.

Katika wanachama kumi na saba waasisi, tisa kati yao walitoka makao makuu, watano kutoka Jimbo la Ziwa, mmoja kutoka Jimbo la Magharibi na wawili kutoka Jimbo la Kaskazini.

Uwakilishi huu wa wajumbe kutoka kwenye majimbo na makao makuu unatoa picha ya hali ya harakati za siasa nchini Tanganyika kabla ya kuundwa kwa TANU.

Mkutano Mkuu wa Mwaka wa TAA ulikuwa na ajenda ndefu. Siku ya kwanza mkutano ulichukua masaa matano na nusu. Siku hiyo ilitumiwa kuondoa matatizo yaliyokuwa yakikiathiri chama.

Ajenda ya kwanza ya mkutano huo ilikuwa idhinisha kufukuzwa kazi kwa Alexander Tobias aliyekuwa katibu mtendaji tangu Juni, 1953. Tobias alikuwa amepoteza majalada na nyaraka muhimu sana za chama zilizokuwa chini ya mamlaka yake kama katibu mtendaji. Kulikuwa na tetesi kwamba majalada hayo aliyakabidhi kwa Special Branch baada ya kupewa fedha.

Ilikuwa katika siku ya pili ndipo wajumbe walikaa chini kuanza kazi hasa ya kujadili ya kuigeuza TAA na kukifanya chama cha siasa TANU bila ya kuficha madhumuni yake na kutangaza dhamiri ya chama ya kuwatayarisha Waafrika wa Tanganyika kujitawala. Julius Kambarage Nyerere, mwanasiasa mgeni katika TAA pale makao makuu akiwa amejiunga na uongozi wa chama miezi 15 tu iliyopita, alichaguliwa Rais wa kwanza wa TANU na John Rupia Makamo wa Rais.

Waziri Mkulo akumbwa na kashfa

AVUNJA BODI YA CHC KABLA HAIJAPOKEA RIPOTI YA UFISADI KUTOKA KWA CAG, ZITTO KUZUNGUMZA LEO

WAZIRI wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ameivunja Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma (CHC), wakati ambao bodi hiyo ilikuwa ikisubiri kupokea ripoti ya ukaguzi uliofanywa na Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ukilenga kubaini tuhuma za kuwapo kwa ufisadi katika shirika hilo.

Msingi wa uchunguzi ndani ya CHC, ni maombi ya Bodi ya shirika hilo hodhi kwa CAG, kufuatia kuwapo kwa tuhuma kwamba menejimenti yake ilihusika na vitendo vya ufisadi, hivyo kusababisha kusimamishwa kwa Kaimu Mkurugenzi wake, Methusela Mbajo.

Ofisi ya CAG ilifanya uchunguzi kwa kutumia kampuni ya kimataifa ya ukaguzi wa hesabu ya Ernst&Young, ukaguzi ambao pia ulilenga kubaini tuhuma dhidi ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), inayoongozwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.

Katika Mkutano wa Nne wa Bunge, Mkulo aliingia katika mvutano na Zitto baada ya waziri huyo kumtuhumu mbunge huyo na Kamati yake kwamba walihongwa ili kutetea nyongeza ya muda wa CHC, tofauti na mawazo ya Serikali ya kutaka kufutwa kwa shirika hilo.

Baada ya tuhuma hizo, Zitto aliapa bungeni kwamba kama uchunguzi utathibitisha yeye au wajumbe wa POAC wamehongwa, angejiuzulu uenyekiti na ubunge na kumtaka Waziri Mkulo nae atoe kiapo chake bungeni kama atajiuzulu akibainika amefanya ufisadi ndani ya CHC.

Mkulo akijibu swali hilo alishindwa kula kiapo na Spika wa Bunge, Anne Makinda akamkumbusha kuhusu kula kiapo kama atajiuzulu, lakini waziri huyo aligoma kufanya hivyo.

Lakini wakati CAG akiwa katika hatua za mwisho kukamilisha ripoti yake ambayo kimsingi ilipaswa kukabidhiwa kwa bodi ya CHC, uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa Mkulo amevunja bodi hiyo kabla ya kumaliza muda wake wa nyongeza ambao ulipaswa kumalizika Desemba 31, mwaka huu.

Uhai wa Bodi ya CHC
Awali bodi ya CHC ilikuwa imalize muda wake Juni 30 mwaka huu, lakini Mkulo aliiongezea muda hadi Desemba 31, mwaka huu na barua ya hatua hiyo ilitumwa kwa wajumbe wa bodi hiyo kuwajulisha hatua hiyo ya waziri Julai 29, 2011.

Hata hivyo, ghafla Mkulo alibadili uamuzi wake Oktoba 10, 2011, kwa kumwandikia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC kwamba awaarifu wajumbe wa bodi kuhusu uamuzi huo.

Sehemu ya barua kutoka Wizara ya Fedha kwenda CHC ambayo Mwananchi imeiona inaeleza: “Nimeelekezwa nikuarifu kwamba Waziri wa Fedha, Mh. Mustafa H. Mkulo (Mb), ametengua uamuzi wake wa kuongeza muda wa Bodi ya CHC hadi tarehe 31 Desemba, 2011 au hapo Rais atakapoteua Mwenyekiti wa Bodi hiyo kuanzia tarehe ya barua hii (10, Oktoba, 2011).”

Barua hiyo iliyosainiwa kwa niaba ya Katibu Mkuu Hazina na Geoffrey Msella pia inasema; “Kwa barua hii unatakiwa kuwaandikia barua waliokuwa Wajumbe wa Bodi ukiwashukuru kwa michango yao kwa Shirika hili katika kipindi walichotumikia CHC.”

Kufuatia barua hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC, Dome Malosha siku hiyo hiyo ya Oktoba 10, 2011 aliwaandikia barua wajumbe hao wa Bodi akiwaarifu kuhusu uamuzi wa Waziri Mkulo kuvunja bodi hiyo.

Ukaguzi wa CAG
Uchunguzi wa Mwananchi umebiani kuwa hatua ya Mkulo kuvunja bodi ya CHC ilifanyika muda mfupi tu, tangu alipojibu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utuoh kuhusu kile ambacho kinaonekana kuwa ni matokeo ya awali ya ukaguzi uliofanywa na Ernst & Young.

Uchunguzi wetu unaonyesha kuwa kulikuwa na mawasiliano baina ya Mkulo na Utouh kati ya Oktoba 6 na 8, 2011, na baadaye kuvunjwa kwa bodi Oktoba 10.

Oktoba 8, 2011, Mkulo alimwandikia barua Utouh akikanusha kwamba hahusiki na ufisadi wowote ndani ya CHC, kauli inayothibitisha kwamba alitajwa katika taarifa yake hiyo.

Katika barua hiyo ambayo pia Mwananchi imeiona, Mkulo anakanusha kile alichosema kuwa ni tuhuma za kuhusishwa na uuzwaji wa mali za CHC kinyume cha sheria.

Barua hiyo ya Mkulo kwenda kwa CAG ina kumbukumbu Namba TYC/B/70/03 na kichwa cha habari, YAH: UKAGUZI WA CONSOLIDATED HOLDING CORPORATION ikirejea mazungumzo ya simu baina ya viongozi hao wawili Oktoba 7, mwaka huu, pia ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa Utouh kwenda kwa Mkulo Oktoba 6, 2011.

Soma zaidi