Friday, July 16, 2010

Majalada matano yatinga kwa DPP

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imekamilisha uchunguzi wa kesi tano za ufisadi ndani ya Benki ya Taifa ya Biashara (NBC); huku ikikamilisha uchunguzi kama huo ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Raia Mwema limethibitisha.

Habari za uhakika ndani ya TAKUKURU zilizothibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Dk. Edward Hosea, zimeeleza kwamba kwa sasa majalada matano yamekwishafikishwa kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kupata kibali cha kuwafikisha mahakamani wahusika.

Akizungumza na Raia Mwema katika mahojiano maalumu, hivi karibuni, Dk. Hosea alisema kuwa sehemu ya kwanza ya uchunguzi ndani ya NBC imekamilika na majalada matano yamepelekwa kwa DPP kupata kibali cha kuwashitaki wahusika, ambao baadhi ni maofisa waandamizi wa NBC na wafanyabiashara walioshirikiana nao katika wizi wa takriban Sh bilioni 4.

“Ni kweli tunashughulikia tuhuma za ufisadi ndani ya NBC na TRA na tayari kuna majalada matano tumeyafikisha kwa DPP kupata kibali cha kuwafikisha mahakamani wahusika,” alisema Dk.Hosea bila kutaja majina na idadi ya wahusika.

Wakati uchunguzi wa tuhuma za ufisadi dhidi ya wahusika ukiendelea ndani ya NBC na TRA, uongozi wa taasisi hizo mbili umekwisha kuchukua hatua dhidi ya wahusika kupisha uchunguzi dhidi yao.

Ndani ya NBC habari zimethibitisha kwamba maofisa waandamizi wanne (majina tunayahifadhi kwa sasa) wamekwisha kuchukuliwa hatua kufuatia matukio hayo ya ufisadi. Raia Mwema limethibitisha, hata hivyo, kwamba baadhi ya maofisa waandamizi wanaendelea na kazi licha ya kutajwa kuhusika katika ufisadi huo kwa kiasi kikubwa.

Uchunguzi wa Raia Mwema umethibitisha kuwapo mvutano mkali ndani ya NBC kabla ya wenye hisa wakuu wa benki hiyo - benki ya ABSA ya Afrika Kusini, kuingilia kati kutaka kuchukuliwa hatua madhubuti dhidi ya watumishi walioshiriki katika upotevu wa mabilioni ya fedha ndani ya benki hiyo.

Mvutano huo umeelezwa kusababishwa na kuhusika kwa vigogo wa juu wa benki hiyo kabla ya mabadiliko yaliyofanywa hivi karibuni kwa kuingia kwa Mkurugenzi mpya Lawrence Mafuru, ambaye alianza kazi rasmi Juni mosi, mwaka huu, kuchukua nafasi ya raia wa Afrika Kusini, Christo de Vries aliyeondolewa.

Uongozi wa NBC kwa kushirikiana na uongozi wa wafanyakazi, umekwisharidhia kusimamishwa kazi kwa maofisa wandamizi watatu na ofisa mmoja wa ngazi ya chini kuhusiana na kuhusika na upotevu wa zaidi ya Sh bilioni 4 kupitia akaunti hewa zilizofunguliwa katika matawi ya benki hiyo Dar es Salaam.

Uchunguzi dhidi ya ufisadi ndani ya NBC ulihusisha nyaraka za kughushi kutoka taasisi mbalimbali zikiwamo za NBC yenyewe, Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), TRA na za Benki ya CRDB Limited; nyaraka zilizoghushiwa kufanikisha uhalifu huo ambao uliitikisa benki hiyo katika siku za karibuni.

Uchunguzi wa awali ulihusisha pia makachero kutoka kwa wamiliki wa hisa kubwa za benki hiyo, taasisi kubwa ya fedha Afrika Kusini ya ABSA Group Limited, ambao kwa kiasi kikubwa walihakikisha wanasafisha uozo ndani ya benki hiyo.

Habari zaidi zinaeleza kwamba maofisa wanaotuhumiwa kushiriki wizi huo wamekuwa na tabia ya kupoteza hati za dhamana zinazotumiwa na baadhi ya wateja kuchukua mikopo na kusababisha benki hiyo kupata hasara kubwa kwa kushindwa kukamata mali za wateja wanaoshindwa kulipa madeni.

Katika tukio moja wapo la wizi ndani ya NBC, baadhi ya maofisa wa benki hiyo tawi la Corporate walituhumiwa kuhusika na akaunti hewa iliyochotewa kiasi cha Sh milioni 900 ikihusisha akaunti namba 011103033038 iliyodaiwa kumilikiwa na kampuni moja (jina tunalihifadhi kwa sasa).

Benki ya NBC Limited ilibinafsishwa mwaka 2000 baada ya kuendeshwa kwa miaka mingi kama shirika la umma. Ni kati ya mashirika ya umma yaliyozua utata mkubwa wakati wa kubinafsishwa kutokana na kile ambacho hadi leo wengine wanasema iliuzwa kwa bei ya kutupa.

Wakati ABSA Group Limited ya Afrika Kusini inamiliki hisa 55 ndani ya NBC, Serikali ya Tanzania inamiliki hisa 30 na Shirika la Kimataifa la Fedha (International Finance Corporation) linamiliki hisa 15.

Kwa upande wa TRA, tayari bodi ya mamlaka hiyo imeamua kuwachukulia hatua maofisa wake waandamizi kupisha uchunguzi dhidi yao; huku TAKUKURU ikiendelea kukamilisha uchunguzi dhidi yao.

Maofisa wa Idara ya Ushuru wa Forodha waliosimamishwa na Bodi ya TRA kwa tuhuma za ama kushiriki au kufumbia macho vitendo vya ukwepaji kodi, wameamriwa wajieleze huku hatua zaidi zikichukuliwa kwa maofisa wengine wa chini.

Mwenyekiti wa Bodi ya TRA, Dk. Marceline Chijoriga, alilieleza Raia Mwema ya kuwa, aliyekuwa Naibu Kamishna wa Ushuru wa Forodha, Generose Bateyunga, ameondolewa katika nafasi yake kupisha uchunguzi dhidi ya tuhuma zinazomhusu pamoja na wahusika wengine.

“Wapo wahusika ambao ni wafanyakazi wa TRA lakini waajiriwa wa Bodi, hawa ni makamishna na naibu makamishna na hata mameneja, lakini wapo pia wahusika wengine ambao ni walioajiriwa na Menejimenti ya TRA.

“Sasa kwa taratibu za kazi, mimi ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi, nashughulikia hawa ambao mikataba yao ya ajira wamepewa na Bodi na Menejimenti inashughulikia wengine. Hatua tulizokwishakuchukua hadi sasa ni kuitaka Menejimenti imwondoe Kamishna (Naibu) wa Forodha Bateyunga impangie kazi nyingine tofauti wakati uchunguzi unaendelea.”

Akizungumzia uchunguzi ndani ya TRA, Dk. Edward Hosea alisema ofisi yake inafanya uchunguzi mkali kuhusiana na suala la ukwepaji kodi ndani ya TRA na kwamba hatua madhubuti zitachukuliwa.

“Suala la TRA tunalo na tunalifanyia kazi kwa karibu sana. Wakati muafaka tutawaeleza hatua tutakazochukua dhidi ya wahusika... Watu wajue tu tuko kazini wakati wote na hasa kwa mambo ya msingi kama hayo yanayogusa uchumi wa Taifa,” alisema Dk. Hosea katika mahojiano yake na Raia Mwema.

Hatua hizo za Bodi ya TRA na Takukuru zinafuatia taarifa za raia wema ambazo hatimaye zilichapishwa na Raia Mwema zikihusu ufisadi wa kutisha ndani ya Idara ya Forodha ambako, pamoja na mambo mengine, imeelezwa ya kuwa familia moja ya Dar es Salaam inayomiliki kampuni inayojihusisha na biashara ya bidhaa za nyumbani imekuwa ikiendesha uwakala wa forodha kwa ama yenyewe kukwepa kodi au kuwasaidia wafanyabiashara wengine kukwepa kodi huku ikijiwekea kinga kwa wanasiasa.

Taarifa za awali zilizoifikia Raia Mwema na kuandikwa kwa kirefu katika matoleo yake mawili ya nyuma zinaonyesha kuwa biashara hiyo ya uwakala wa ukwepaji kodi imekuwa ikiipotezea Serikali mapato ya mabilioni ya shilingi ambazo zilistahili kukusanywa kutoka kwa wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa mbalimbali kutoka China na Dubai ambako kampuni hiyo imefungua ofisi “kurahisisha” shughuli zake.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, mtandao wa kampuni hii ni mkubwa, unajumuisha baadhi ya watendaji wa TRA, wakubwa kwa wadogo na umevuka mipaka hadi Hong Kong na Guanzhou, China na Dubai. Ofisi za nje ya Tanzania hutumika kupokea mizigo inayoingia nchini.

Imeelezwa kwamba mwagizaji wa mali yoyote kama nguo, hardware au vifa vya umeme hufanya manunuzi kwenye maeneo hayo na hupewa gharama zote za kufikisha mzigo Dar es Salaam pamoja na ushuru wa forodha na gharama nyinginezo hadi kweye bohari yao iliyopo Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa hizo mwagizaji anakabidhi mzigo ofisini China na anakabidhiwa mali yake Dar es Salaam baada ya siku kadhaa kati ya wiki tano hadi sita.

Uchunguzi wa Raia Mwema umebaini viwango vya gharama zao kwa baadhi ya mali ni kama ifuatavyo:

Kusafirisha na kutoa bandarini vifaa vya ujenzi hutoza dola za Marekani 350.00 kwa meta moja ya ujazo (1 cbm).

Kusafirisha na kutoa bandarini bidhaa za nguo ni dola za Marekani 450.00 kwa meta moja ya ujazo (1 cbm).

Kusafirisha na kutoa bandarini bidhaa za umeme kama swichi, circuit breakers na viginevyo ni dola za Marekani 500.00 kwa meta moja ya ujazo (1 cbm).

Mizigo maalumu kama vitenge-mazungumzo hufanyika na bei maalumu hukubaliwa.

“Kinachotisha katika utaratibu huu ni kwamba wakati gharama za usafiri wa meli hupatikana kutegemea uzito na ujazo wa mali, wao wamefika mbali zaidi kwa kukadiria ushuru na kodi za Serikali kwa ujazo (yaani cubic measurements). Kwa kawaida ushuru wa forodha hutozwa kwenye Thamani halisi ya Manunuzi, Bima na Gharama za Usafiri hadi nchini (Cost, Insurance and Freight) na si vinginevyo,” alisema mtumishi mmoja wa TRA mwenye ufahamu wa biashara hiyo akidai kwamba biashara hiyo huwa na ulinzi wa ‘wakubwa’.

Kwa mujibu wa taarifa hizi, kati ya nguvu iliyonazo kampuni hiyo ni ukaribu wake na wanasiasa ikielezwa kwamba kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 kampuni hiyo ilikichangia chama tawala Sh. Milioni 200 na kwamba katika mwaka huu imeahidi kuchangia milioni 500.

Uchunguzi wa Raia Mwema umeonyesha kwamba sehemu kubwa ya fedha hutumika katika kulipia ushuru kidogo, rushwa kwa maofisa sehemu mbalimbali husika, gharama za bandari na usafiri wa bandarini kwenda kwenye maghala yao.

Tuesday, July 13, 2010

Shahidi adai kampuni aliyoleta Basil Mramba ilikuwa feki

Shahidi wa 11 katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka katika ofisi ya umma na kuisababishia hasara serikali, inayowakabili waliokuwa mawaziri, Basil Mramba, na Daniel Yona na aliyekuwa Katibu Mkuu Hazina, Gray Mgonja, ameiambia mahakama kuwa Kampuni ya Alex Sterwart (Assayers) Government Business, ilisaini mkataba na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) miezi miwili kabla haijaruhusiwa na serikali kisheria kufanya biashara zake hapa nchini.

Shahidi huyo, Frank Kanyus, ambaye ni Msajili Msaidizi wa Makampuni wa Wakala wa Serikali wa Biashara na Leseni (Brela), alidai mahakamani hapo jana kuwa kampuni, ambayo imesajiliwa nje ya nchi, ikifanya kazi nchini bila ya kuruhusiwa na serikali kisheria, ni kosa la jinai. Akiongozwa na Wakili Mwandamizi wa Serikali, Frederick Manyanda Frank (37), alidai Kampuni ya Alex Sterwart (Assayers) Government Business, ilisajiliwa nchini Marekani Desemba 13, 2002.

Alidai Juni 14, 2003, kampuni hiyo ilisaini mkataba na BoT na kwamba, iliruhusiwa rasmi na serikali kufanya biashara zake nchini kwa kupatiwa cheti cha usajili (certificate of compliance) Agosti 18, 2003, baada ya kutimiza masharti yote ya sheria za nchi.

Frank, ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alidai kisheria, kampuni iliyosajiliwa nje ya nchi, ikisajiliwa nchini, husajiliwa kama tawi.

Shahidi huyo alidai anaifahamu vyema kampuni hiyo kwa vile alikuwa ni mmoja wa maofisa wa Brela waliohusika katika kuisajili.

Alidai aliajiriwa na Brela mwaka 2001 kama afisa usajili wa makampuni na mwaka 2007 aliteuliwa kuwa msajili msaidizi wa wakala huo anayeshughulikia maombi ya usajili wa makampuni, majina na alama za biashara.

Frank alidai baada ya kuhakiki maombi na vitu hivyo na kujiridhisha kama vimekidhi matakwa ya sheria, huvipeleka kwa viongozi wake wa juu.

“Tulifikia hatua ya kupokea nyaraka za Alex Sterwart (Assayers) Government Business, kuzikagua, kufungua jalada, kuhakiki na kui-foward kwa viongozi wangu wa juu. Jina la hilo jalada nililifungua mwenyewe, ndani yake niliandika kuwa nilipitia nyaraka na kuzihakiki,” alidai Frank kabla ya kulitoa jalada hilo mahakamani kama kielelezo.

Baadaye, shahidi huyo alihojiwa na wakili wa upande wa utetezi, Herbert Nyange na kuieleza mahakama kuwa anuani ya kampuni hiyo iliyomo kwenye mkataba huo inaonyesha kuwa ofisi zake zinapatikana Kitalu namba 1129, Barabara ya Chole, Wilaya ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam. Shahidi huyo alidai kutumika anuani kunatakiwa kufanyika, kuanzia hati ya usajili inapoanza kutolewa na kwamba, ingekuwa ni makosa kampuni hiyo kuanza kutumia anuani ya Tanzania kabla ya kusajiliwa nchini.

Nyange pia, alimhoji shahidi huyo kama hapa nchini zabuni inaweza kutolewa kwa makampuni ya nje na ya ndani na kujibu kuwa anajua. Pia, alimhoji shahidi huyo kama kampuni ya nje inaweza kushiriki kwenye zabuni bila ya kuwa na hati ya usajili na kujibu kuwa hajui.

Shahidi huyo pia alidai kuwa kampuni hiyo ilipoingia mkataba na BoT, ilikuwa inatumia anuani iliyoko Washington DC, Marekani na siyo kampuni iliyosajiliwa Tanzania na kuongeza kuwa kwa kuingia mkataba tu bila kuanza kazi hakuna matatizo.Kesi hiyo inayosikilizwa na jopo la mahakimu watatu wakiongozwa na Mwenyekiti, John Utamwa, Saul Kinemela na Sam Rumanyika, itaendelea leo.

Katika kesi hiyo, Mramba, Yona na Mgonja, wanadaiwa waliruhusu kutolewa kibali cha serikali kilichoisaidia kampuni hiyo kutolipa kodi tofauti na mapendekezo ya Mamlaka ya Mapato (TRA) na uliisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 11,7.


CHANZO: NIPASHE

Monday, July 12, 2010

Dk Bilal mgombea mwenza wa Kikwete

AL I Y E K U W A mgombea wa kinyang’anyiro cha kuwania tiketi ya CCM katika uchaguzi wa urais wa Zanzibar na Waziri Kiongozi mstaafu, Dk. Gharib Bilal, ameteuliwa
na Rais Jakaya Kikwete kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao.

Kabla ya kutamkwa kwa jina la Dk. Bilal jana saa tatu usiku, kura za ndiyo zilipigwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM, kumthibitisha Kikwete kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.

Akitangaza matokeo ya kura hizo jana jioni, Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar,
Rais Amani Abeid Karume, alisema asilimia 99.16 ya wa jumbe walipiga kura za Ndiyo
kumthibitisha Rais Kikwete kuwa mgombea wa urais wa CCM katika uchaguzi mkuu ujao.

Kwa mujibu wa Karume, idadi ya wajumbe wote ni 1,968, waliopiga kura walikuwa 1,909, hakuna hata kura moja iliyoharibika, kura za Ndiyo zilikuwa 1,893 sawa na asilimia 99.16 na kura za Hapana zilikuwa 16 sawa na asilimia 0.84.

Mapema ilipofika wakati wa kupitisha jina la mgombea huyo, Rais Kikwete alilazimika kuondoka katika kiti chake cha uenyekiti na kumkabidhi Rais Karume ili kuongoza mkutano.

Alikwenda kukaa katika sehemu maalumu iliyotengwa kwa viongozi wa juu wa serikali,
wastaafu, wake wao pamoja na wajumbe wa Kamati Kuu.

Baada ya kupitishwa kwa kura hizo, Karume alimpisha Kikwete kurejea katika kiti chake na baadaye kidogo walikwenda katika kikao cha Kamati Kuu kumpitisha mgombea mwenza.
Juzi baada ya mgombea wa urais wa Zanzibar kutangazwa kuwa ni Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Shein, Rais Kikwete aliwashukuru na kuelezea umuhimu wa kila mgombea
katika kuleta maendeleo ya Tanzania.

Rais Kikwete alimwambia Waziri Kiongozi wa SMZ, Shamsi Vuai Nahodha kuwa yeye ni kijana mdogo, ana umri mdogo na Tanzania na Zanzibar bado wanamuhitaji.

Pia alimwambia Dk. Bilal kuwa kuvunjika kwa koleo sio mwisho wa uhunzi na kuwa yeye ni kiongozi makini, mzoefu, mwenye uwezo na Tanzania na Zanzibar wanamuhitaji.

Ulifuata wasaa wa kusoma wasifu wa mgombea ambao ulisomwa na Katibu wa Oganaizesheni, Kidawa Himid Saleh, kabla ya kazi ya kupiga kura kuanza.

Katika wasifu, Saleh alisema Rais Kikwete alijitokeza peke yake katika kuchukua fomu na kurudisha na kwamba alipata wadhamini 14,069 katika mikoa yote ya Tanzania.

Alisema Kamati Kuu pamoja na NEC ziliridhika kwamba Rais Kikwete anazo sifa za kuendelea kuwa Rais wa Tanzania na hivyo kuwaomba wajumbe wote wa Mkutano Mkuu kumpa kura za Ndiyo.

“Chini ya uongozi wake, Serikali imetekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi kwa mafanikio makubwa. Takribani asilimia 80 ya malengo na shabaha za Ilani zimetekelezwa
na mengine yanaendelea kutekelezwa,” alisema Saleh katikawasifu huo.

“Tumefanikiwa hivyo kwa sababu Ndugu Kikwete alihakikisha kwamba bajeti na mipango ya Serikali ya kila mwaka inazingatia malengo ya Ilani ambayo tulimkabidhi mwaka 2005.

“Katika miaka mitano iliyopita, Ndugu Kikwete ameifanya kazi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano kwa bidii kubwa, kwa uadilifu mkubwa, kwa busara kubwa na umakini mkubwa,”
aliongeza Saleh.

Baada ya kusomwa kwa wasifu huo, waasisi wa chama wa Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar, walipata wasaa wa kuongeza maelezo ya ziada kuhusu mgombea huyo.

Balozi Job Lusinde kwa niaba ya waasisi wa Bara, alisema Rais Kikwete ameongoza kwa staili yake ya Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya na mafanikio makubwa yamepatikana.

Alisema wakati serikali ikijivunia kuanzisha chuo kikuu cha aina ya kecha Dodoma, wakazi wa mji huo wana furaha kubwa kwa sababu uchumi wa mji umeimarika.

Kwa upande wake, maelezo ya waasisi wa Zanzibar yaliyotolewa na Hassan Nassoro Moyo, yalieleza kuwa sifa zaidi ya sita zinamfanya Kikwete astahili kupewa muhula mwingine wa
kuongoza Tanzania.

Alizitaja kuwa ni mpendwa wa watu; kiongozi shupavu, mkweli, mtekelezaji na mwadilifu; mtetezi wa Muungano na msimamizi na mtetezi wa Mapinduzi; mpenda maendeleo na
ametekeleza Ilani kwa mafanikio.

Awali, mkutano wa jana ulianza kwa burudani kama ilivyo kawaida, lakini alikuwa wanamuziki wa kizazi kipya, Marima Lawrence maarufu kama ‘Marlow’ aliyekonga nyoyo za
wajumbe akiongozwa na Rais Kikwete.

Alishambulia jukwaa na kuufanya ukumbi mzima kusimama na kucheza baada ya kuimba wimbo wake wenye mahadhi sawa na ule wa ‘Missing my baby’.

Marlow katika wimbo huo alikuwa na mashairi ya kuisifu CCM na Rais Kikwete na haya yalikuwa baadhi ya maneno ya wimbo huo: “Tumeanza kupiga honi now, pipiiii… hawaelewani, hatukuja kupoteza…tunarudi kwa kishindo, na Jakaya ni Rais, Kwa Pamoja tusonge mbele, na CCM ni zaidi.”

Friday, July 9, 2010

Hukumu urais Zanzibar leo

ILE siku ya hukumu kwa wanachama 11 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaowania uteuzi wa kugombea urais wa Zanzibar, imetimia.

Leo Kamati Kuu (CC) ya Halmashauri Kuu ya Taifa pamoja na Halmashauri Kuu (NEC) vinakutana hapa kufanya uteuzi na kisha kupiga kura ya kuchagua mgombea huyo miongoni mwa 11 waliojitokeza.

Awali, Kamati Kuu ilikuwa ikutane jana, lakini sasa itakutana leo kwanza kabla ya kupeleka majina au jina la mgombea mmoja kupigiwa kura NEC.

Tayari Dodoma imepambwa na rangi za kijani na njano zinazotumiwa na chama hicho tawala, huku kambi mbalimbali zikiwamba ngoma upande wao, katika mbio za nani atasimamishwa na CCM kuwania kumrithi Rais Amani Abeid Karume.

Wanachama 11 wamejitokeza kuwania nafasi hiyo wakiwamo vigogo kadhaa ambao ni Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohamed Shein, Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha, Naibu wake ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna na Waziri Kiongozi mstaafu Dk. Mohamed Gharib Bilal.

Pia wamo mawaziri Haroun Ali Suleiman, Naibu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mohammed Aboud, Mohammed Yussuf Mshamba, Balozi Ali Abeid Karume, Hamad Bakari Mshindo, Mohammed Raza na Omar Sheha Mussa.

Miongoni mwao, Dk. Shein, Nahodha na Dk. Bilal wanapewa nafasi kubwa ya kuteuliwa na CCM leo kusimama dhidi ya Maalim Seif Sharrif Hamad wa CUF katika Uchaguzi Mkuu Oktoba 31 mwaka huu.

Dk. Shein anaelezwa kuwa mwanasiasa mwenye kufuata siasa za ustaarabu, muungwana na anayetenda kazi zake bila kuwa na makundi na anatazamiwa kuwa kiungo kikubwa kati ya Pemba na Unguja, hasa baada ya maridhiano ya kisiasa visiwani.

Hata hivyo, tangu ajitose kuwania uteuzi huo, amekuwa akiandamwa na ‘makombora’ kutoka kwa baadhi ya wapinzani wake, waliofikia hatua ya kumwaga vipeperushi Unguja wakimtuhumu kwa mambo kadhaa.

Hata jana jioni, uvumi ulikuwa unaenezwa mjini hapa kuwa Dk. Shein alikuwa ameandika barua ya kujitoa na kuelekeza nguvu zake kumsaidia Nahodha.

Lakini wanaomtetea wanaamini hali hiyo imefanyika kwa sababu mgombea huyo ni tishio miongoni mwa wenzake na ana nafasi kubwa ya kuibuka mshindi leo.

Baadhi ya wasaidizi wa Dk. Shein walithibitisha kuenezwa kwa uvumi wa kujitoa tangu juzi, lakini akaeleza kuwa habari hizo hazikuwa na ukweli wowote.

Mwingine ni Nahodha ambaye kwa umri wake wa miaka 48, anaonekana kuwa chaguo la vijana, kama ambavyo mwenyewe amesema anataka kuleta mabadiliko Zanzibar na kuifanya kuwa kama Dubai.

Huyu naye anaonekana kuwa miongoni mwa wagombea wenye nguvu katika kumrithi Rais Karume na kwa turufu yake ya ujana, na pengine kuwa kwake karibu kama msaidizi wa Rais, ni karata yake nyingine.

Dk. Bilal ambaye aliwahi kuwa Waziri Kiongozi chini ya Dk. Salmin Amour Juma ‘Komandoo,’ ni mgombea mwingine mwenye nguvu miongoni mwa waliojitokeza.

Alijaribu bila mafanikio kutaka kumrithi Komandoo na akabwagwa na Karume na akajaribu tena mwaka 2005 bila mafanikio, lakini tangu wakati huo, ndoto za kutaka kuwa rais wa Zanzibar hazijafutika kwake.

Alitajwa kuwa mtu wa karibu wa Dk. Salmin, lakini yamekuwapo madai mapya hapa na Zanzibar, kuwa wawili hao sasa hawako pamoja katika mbio za mwaka huu za kuingia Ikulu.

Dk. Salmin alitua hapa juzi akifuatana na Nahodha na haijawekwa bayana kama turufu yake ni kwa mwanasiasa huyo kijana, lakini uwepo wake katika vikao hivi viwili vya leo, ni ishara kuwa amekuja na siri moyoni.

Wagombea wengine wanane waliosalia katika kinyang’anyiro hicho, hawapewi nafasi kubwa ya kuteuliwa, kwa sababu mbalimbali, ingawa katika siasa, lolote linaweza kutokea.

Chini ya uenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete, vikao hivyo vinatarajiwa hadi kufikia majira ya jioni leo, vitakuwa vimetoa jina la mgombea na la mgombea mwenza wa Jamhuri ya Muungano.

Rais Kikwete ndiye mgombea pekee wa CCM katika urais wa Muungano na kwa mujibu wa Katiba ya Chama hicho, atapigiwa kura katika Mkutano Mkuu utakaofanyika kwa siku mbili kuanzia kesho.

Katika suala la mgombea mwenza, bado ni siri kubwa kwa Rais Kikwete mwenyewe, ingawa yamekuwapo majina kadhaa yanayotajwa kwa nafasi hiyo.

Majina ya wanasiasa kama Zakia Meghji, Dk. Salim Ahmed Salim, Muhammed Seif Khatib na hata Dk. Shein na Nahodha, yamehusishwa na nafasi hiyo, ingawa ukweli wa mambo utakuwa hadharani majira yoyote leo.

Katika maandalizi ya vikao hivyo, Rais Kikwete jana alitembelea Kizota ambako Mkutano Mkuu utafanyika kesho na keshokutwa, na maandalizi yalikuwa yanaelekea hatua za mwisho kukamilika.

Rais Kikwete alitembelea eneo hilo muda mfupi baada ya kutua mjini hapa na alikuwa Kizota na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Katibu Mkuu wa CCM Yusuf Makamba na watendaji wengine wa CCM na Serikali.