Tuesday, June 30, 2009

Polisi Wavunja harusi ya binti wa miaka 17 Tanga!


Tukio lisilo la kawaida limeripotiwa leo kupitia TBC 1 kwamba polisi mkoani Tanga wameingilia kati na kuvunja shughuli ya harusi kwenye moja ya vijiji vya mkoa huo. Kwa mujibu wa taarifa hiyo, polisi wameingilia kati kwa vile ndoa hiyo ilihusu msichana wa miaka 17 na aliyekatishwa masomo yake kuolewa na bwana wa umri wa miaka 50.

Polisi waliingia mahali hapo wakati Bi. Harusi, ndugu na waengine walioudhuria walipokuwa... soma zaidi; http://www.kwanzajamii.com

MEREMETA: Wananchi wanataka ukweli

NI jambo la kukatisha tamaa kwamba Serikali yetu, kwa mara nyingine, imeendelea kuwaficha wananchi ukweli kuhusu madai ya ufisadi uliotendeka katika mradi wa Meremeta ambao inaaminika umeteketeza fedha za umma Sh. bilioni 155.

Mwanzoni mwa wiki hii, si tu kwamba Serikali (kupitia waziri wake) ilishindwa, bungeni, kumjibu ipaswavyo mbunge wa CHADEMA, Dk. Willbroad Slaa, kuhusu mradi huo; lakini pia, kwa namna ya kushangaza, ilimtaka aachane na hoja hiyo.

Kauli hiyo ya kumtaka mbunge wa wananchi aachane na hoja hiyo, ni sawa na kuwaambia wananchi (ambao yeye mbunge anawawakilisha), kwamba hawana haki ya kujua ukweli ni upi kuhusu mabilioni ya pesa zao yanayodaiwa kutafunwa kupitia mradi huo wa Meremeta.

Hatukubaliani na hoja kwamba mradi wa Meremeta ni mradi unaohusisha jeshi letu la ulinzi (JWTZ), na hivyo ni jambo nyeti lisilostahili kujadiliwa bungeni! Hakuna jambo nyeti linalohusu madai ya uchotaji wa mabilioni ya pesa za umma ambalo halistahili kujadiliwa bungeni.

Tunaamini hivyo, kwa sababu, kama alivyosema Dk. Slaa, hapa tunazungumzia madai ya wizi, na wala hatuzungumzii siri za ndani za jeshi kama vile tuna kambi ngapi, tuna wanajeshi wangapi, tuna zana gani za kivita nk. Hapa tunazungumzia fedha za umma zilizochotwa, tunazungumzia madai ya wizi, na si siri za jeshi.

Isitoshe, kama serikali yetu ilijua kwamba jeshi ni asasi nyeti katika usalama wa taifa; ni kwa nini ililiruhusu lijitose katika biashara ya kununua dhahabu kupitia Meremeta? Tena katika zama hizi ambapo biashara duniani zinaendeshwa kwa uwazi?

Kwa hiyo, serikali bado ina deni kwa wananchi. Na deni hilo ni kuelezwa ukweli kuhusu madai kwamba mapesa hayo ya umma yaliyochotwa kupitia Meremeta.

Akizungumza katika kikao cha Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Saerikali (CAG), alipata kusema kwamba Meremeta haimo katika makampuni ya mashirika ya umma, na hivyo ofisi yake haijawahi kukagua mahesabu yake.

Kama hivyo ndiyo, na hasa ikizingatiwa kuwa benki ya kigeni ilihusishwa katika mradi huo, wananchi wanataka kujua, miongoni mwa mambo mengine, ni nani hasa waliokuwa na hisa katika kampuni hiyo?

Kwa hakika, kiu hii ya wananchi ya kutaka kuujua ukweli kuhusu Meremeta, haitamalizwa kwa serikali kuwakatisha tamaa kina Slaa kwa kuwaambia watafute hoja nyingine. Itamalizwa tu kwa ukweli kuwekwa hadharani.

Kwa hiyo, bado tunaamini kuwa suala hilo linaweza kujadiliwa bungeni kwa namna ambayo siri nyeti zinazohusiana na masuala ya ndani ya jeshi letu hazitaguswa.

Ni hapo tu hilo litakapotendeka, kiu ya wananchi itatulizwa.

Maana; haingii akilini serikali yetu kulishirikisha jeshi katika uanzishaji wa kampuni (Meremeta) ya kufanya biashara ya dhahabu na hata kuwasiliana na mabenki ya nje ( Nedcor Trade Service ya Afika Kusini na Deutshe Bank AG ya Uingereza) kwa ajili ya mkopo, na kisha wananchi kuambiwa suala hilo ni siri baada ya pesa kutafunwa!

Tunafahamu kwamba demokrasia yetu haijakomaa vya kutosha; lakini tuige, basi, kwa wenzetu (kama Afrika Kusini) ambako skandali za manunuzi hata ya silaha za jeshi hujadiliwa bungeni.

Hakika; mzimu wa Meremeta utatulia tu kama wananchi, hatimaye, wataelezwa ukweli wote na sheria kuachiwa ifuate mkondo wake.

Chanzo: www.raiamwema.co.tz

Bajeti ya safari za Kikwete nje yapaa

-Vinywaji, vitafunio Ikulu Sh. mil 201
-Pesa za mavazi, mashuka na viatu zabanwa

MCHANGANUO wa mgao wa fedha katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha wa 2009/2010 unaonyesha kuwa Ikulu imetengewa Shilingi milioni 115 kwa ajili ya safari za nje ikilinganishwa na Sh. mil 82 ilizotengewa kipindi kilichopita.

Hiyo maana yake ni kwamba, bajeti ya safari za nje za Ikulu imeongezeka kwa takriban Sh. milioni 34.

Bajeti ya Ikulu ya safari za ndani ya nchi nayo imeongezeka kutoka Sh. 608,419,000 kwa bajeti ya mwaka 2008/2009 hadi Sh 723,360,000 kwa mwaka 2009/2010, ikiwa ni ongezeko la Sh. milioni 114.9.

Miongoni mwa mambo ambayo Rais Kikwete amekuwa akishutumiwa nayo na wananchi, ni wingi wa safari zake za nje ambapo inadaiwa kwamba zinachota mapesa mengi ya walipakodi; ilhali manufaa yake hayaonekani wazi.

Rais Kikwete ameingia katika rekodi ya kuwa rais wa kwanza wa Tanzania kusafiri mara nyingi kwenda Marekani katika kipindi kifupi tu cha utawala wake. Mpaka sasa ameshakwenda Marekani mara sita. Aidha ni nadra kumaliza mwezi mmoja bila kufanya safari ya nje; huku wananchi wakilalamika pia kwamba msafara wake mara nyingi unakuwa mkubwa.

Wiki iliyopita Waziri wa Mambo ya Nje na na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, aliliambia Bunge kwamba serikali inaangalia uwezekano wa kupunguza idadi ya watu wanaosafiri na viongozi wa juu kwenda nje ya nchi baada ya kupata maelekezo kwa Rais Kikwete mwenyewe, jambo linalodhihirisha ujumbe kumfikia.

Mchanganuo unaonyesha pia kwamba bajeti ya Ikulu kwa ajili ya ununuzi wa mavazi, mashuka na viatu, imepunguzwa kutoka Sh. milioni 127,400,000 kwa mwaka wa fedha 2008/2009 hadi Sh. 116,400,000 mwaka wa fedha wa 2009/2010, ikiwa ni punguzo la Sh. milion 11.

Lakini Ikulu imeongezewa takriban Sh. milioni 201.6 katika bajeti yake ndogo ya vinywaji, vitafunio na huduma nyingine za malazi (hospitality supplies and services), ikilinganishwa na bajeti inayokwisha ya mwaka 2008/2009 kwa upande wa masuala ya utawala.

Katika bajeti ya mwaka wa fedha 2008/2009, Ikulu ilipangiwa kutumia Sh 242,710,000 kwa ajili ya vinywaji na huduma nyingine za namna hiyo, lakini katika bajeti ya safari hii, yaani 2009/2010, imetengewa Sh 444,350,000 za huduma hizo.

Kwa mujibu wa mchanganuo wa Bajeti Kuu ya Serikali, matumizi katika kipengele hicho yanaonyesha kuongezeka kila mwaka wa bajeti, kuanzia mwaka wa fedha 2007/2008, ambapo matumizi halisi yalikuwa Sh. milioni 190.44, ikiwa ni ongezeko la Sh milioni 51.3.

Hali ni tofauti kidogo kwa Makamu wa Rais ambako gharama kwa ajili ya ununuzi wa mavazi, mashuka na viatu ni Sh 30,296,000, ikiwa kuna ongezeko ikilinganishwa na mwaka jana, ambako Sh. 22,840,000 zilitengwa. Hapa ni ongezeko la Sh. milioni 7.5 hivi.

Kwenye safari za ndani pia fungu la fedha limeongezwa na katika mwaka huu zimepangwa kutumika Sh. 344,200,000, ikilinganishwa na mwaka jana ambapo zilitengwa Sh. 256,970,000, ikiwa ni ongezeko la takriban Sh. milioni 87.2.

Safari za nje ya nchi za Makamu wa Rais zimetengewa Sh. milioni 25, tofauti na mwaka unaokwisha wa bajeti ambao zilitengwa Sh. milioni 2 ikiwa ni ongezeko la Sh. milioni 23.

Kwa upande wa bajeti ya Makamu wa Rais kuhusu vinywaji na vitafunio, zimetengwa kutumika Sh. milioni 214, ikiwa kuna ongezeko kwa kulinganisha na bajeti ya mwaka wa fedha unaokwisha ambayo ni Sh. milioni 137, hapa kukiwa na ongezeko la Sh. milioni 77.

Wakati takwimu hizo zikiwa kwa ajili ya Makamu wa Rais, kwa upande wa ofisi yake (Ofisi ya Makamu wa Rais) fedha zilizotengwa kwa ajili ya vinywaji baridi na moto, chai na vitafunio, ni Sh. milioni 12.5, tofauti na mwaka jana ambako hapakuwa na bajeti ya aina hiyo.

Maofisa katika ofisi hiyo wamepangiwa kutumia Sh 331,270,000 kwa ajili ya safari za nchini, fedha ambazo ni zaidi ya walizopangiwa mwaka uliopita Sh. 273,215,000, kukiwa na nyongeza ya kitita cha Sh. milioni 58.

Lakini wakati hesabu zikiwa hivyo kwa ajili ya safari za ndani, mambo ni tofauti kwa upande wa safari za nje za maofisa wa ofisi hiyo zikiwa zimepangwa kutumika Sh. milioni 331, ikiwa ni tofauti ya Sh. 270,000 na kiasi kilichotengwa kwa ajili ya safari za ndani ya nchini, lakini pia ni kiasi kikubwa zaidi kwa kulinganisha na fedha zilizotengwa kwa ajili ya shughuli hiyo kwa mwaka jana ambazo ni takriban Sh. milioni 145.6.

Kwenye mavazi (mfano sare), viatu na mashuka zimetengwa Sh milioni 37.5, ikilinganishwa na Sh milioni tano za mwaka uliokwisha.

Kwa Waziri Mkuu, safari za ndani ya nchi zimepangwa kutumika Sh. milioni 636.6 ikiwa ni pungufu ya kiasi kilichotengwa mwaka jana ambacho ni Sh. milioni 842.34, kukiwa na upungufu wa Sh. milioni 205.7.

Kwa ufupi, Ikulu ni moja ya taasisi za serikali zilizoongezewa fedha za matumizi kama ya vinywaji na vitafunio, mambo ambayo yanapingwa na baadhi ya wabunge.

Wabunge hao wanaopinga ni pamoja na wa Karatu, Dk. Wilbroad Slaa ambaye aliliambia bunge, juzi jioni, kuwa matumizi hayo si kipaumbele cha matatizo mengi yanayoikabili nchi kwa sasa, kauli ambayo ilipata upinzani mkali kutoka kwa wabunge wa CCM.

Spika wa Bunge Samuel Sitta, aliingilia kati kwa kuwataka wabunge wenzake wa CCM kumuacha Dk. Slaa aendelee kutoa maoni yake na kwamba ana haki ya kufanya hivyo na hakuwa amevunja kanuni yoyote hadi hapo Bunge litakapokaa kama kamati kupitisha vifungu vya bajeti hiyo.

Kwa ujumla Ikulu imepangiwa matumizi ya Sh. bilioni 7.23 katika bajeti iliyopitishwa na bunge wiki iliyopita itakayoanza kutumika Julai mosi hadi Juni 30 mwakani.

Monday, June 29, 2009

KAULI YA (FEMACT NA SAHRINGON) KUHUSU TAMKO LA SERIKALI JUU MJADALA WA UFISADI UNAOHUSU MAKAMPUNI YA MEREMETA , TANGOLD NA DEEP GREEN FINANCE LTD

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Sisi mashirika yanayotetea Usawa wa jinsia, haki za binadamu na maendeleo na ukombozi wa wanawake kimapinduzi (FEMACT)na mtandao wa mashirika yanayotetea haki za binadamu kusini mwa Afrika tawi la Tanzania (SAHRINGON) tumeshangazwa na kauli iliyotolewa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samwel Sitta na Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda kwamba tuhuma za ufisadi na/au wizi mkubwa wa fedha za umma unaoyahusu makampuni ya Meremeta Ltd., Tangold Ltd. na Deep Green Finance Co. Ltd. haziwezi kuzungumziwa ndani ya Bunge la Jamhuri kwa sababu tuhuma hizo zinahusu mambo ya jeshi na/au usalama wa taifa. Aidha tunapenda kuweka msimamo wetu wazi kwamba hatukubaliani na kauli na/au msimamo huo wa Spika wa Bunge na Serikali kwa sababu zifuatazo:

Kwanza hatuamini kwamba ufisadi mkubwa unaotuhumiwa kufanywa kwa kutumia kivuli cha makampuni haya una uhusiano wowote na mambo ya jeshi na/au usalama wa taifa. Taarifa zilizoko hadharani zinaonyesha kwamba Meremeta Ltd. na Tangold Ltd. ni au yalikuwa makampuni ya kigeni na wala sio ya Kitanzania. Taarifa hizo zinaonyesha kwamba wakati Meremeta Ltd. iliandikishwa nchini Uingereza mnamo tarehe 19 Agosti 1997 na kufilisiwa huko huko Uingereza tarehe 10 Januari 2006, Tangold Ltd. iliandikishwa nchini Mauritius mnamo tarehe 8 Aprili 2005 na kupewa hati ya kutimiza masharti ya Tanzania mnamo tarehe 20 Februari 2006. Zaidi ya hayo makampuni hayo yalianzishwa na kuendeshwa kama makampuni binafsi ijapokuwa inaelezwa kwamba Serikali ya Tanzania kwa kupitia Hazina ilikuwa na hisa katika kampuni ya Meremeta Ltd.

Hakuna hata moja katika makampuni haya mawili ambayo imewahi kuwekwa katika orodha ya makampuni na/au mashirika ya umma na wala hesabu zake kukaguliwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kama ilivyo sheria kuhusu hesabu ya fedha za umma. Aidha Meremeta Ltd. kwa kipindi chote cha uhai wake iliendeshwa na wamiliki wa kampuni ya Triennex (Pty) Ltd. ya Afrika Kusini iliyokuwa na hisa 50 katika Meremeta wakati Serikali ya Tanzania ikiwa na hisa nyingine 50 na makampuni mawili ya Kiingereza yakiwa na hisa moja kila kampuni. Msimamo wa Spika Sitta na Serikali una walakini mkubwa kwa sababu unaweza kutafsiriwa kuwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania na Idara ya Usalama wa Taifa ni kichaka cha kufichia ufisadi na wizi wa mali ya umma.

Kuhusiana na kampuni ya Deep Green Finance Co. Ltd., nyaraka zilizoko hadharani zinaonyesha kwamba Deep Green Finance iliandikishwa mnamo tarehe 18 Machi 2004 kwa madhumuni ya, pamoja na mengine, kufanya biashara ya wakopeshaji fedha. Licha ya kutokuwepo kwa ushahidi wowote wa kuonyesha kwamba Deep Green Finance iliwahi kufanya biashara yoyote na Serikali ya Tanzania, katika kipindi cha miezi minne tu kati ya tarehe 1 Agosti na 10 Desemba 2005, Benki Kuu ya Tanzania ililipa jumla ya shilingi 10,484,005.39 katika akaunti ya Deep Green Finance iliyokuwa NBC Corporate Branch, Dar es Salaam. Aidha, kuanzia tarehe 11 Desemba 2005 hakuna fedha yoyote iliyoingizwa katika akaunti hiyo hadi tarehe 27 Februari 2007 kampuni hiyo ilipovunjwa ‘kwa hiari’ ya wanahisa wake. Inasemekana kuwa jumla ya fedha bilioni 155 ziliibiwa kupitia makampuni hayo.

Kwa miaka mingi kumekuwa na taarifa za utatanishi kuhusu umiliki wa makampuni haya. Kwa mfano, Serikali imekuwa ikitoa taarifa kwamba Meremeta Ltd. ilikuwa ni kampuni ya Kitanzania iliyokuwa ikimilikiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa ajili ya mradi wake wa magari ya deraya ya Nyumbu, Kibaha, Mkoa wa Pwani. Hata hivyo, nakala ya usajili iliyotolewa na Msajili wa Makampuni wa Uingereza na Wales inaonyesha kwamba kampuni hiyo iliandikishwa nchini Uingereza tarehe 19 Agosti 1997 na ilifilisiwa huko huko Uingereza tarehe 10 Januari 2006. Aidha, taarifa ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) ya tarehe 31 Mei 2005 inaonyesha kwamba Meremeta Ltd. ni tawi la kampuni ya kigeni iliyosajiliwa Tanzania kama tawi tarehe 3 Oktoba, 1997. Taarifa hiyo inaonyesha kwamba hisa 50 za Meremeta Ltd. zilikuwa zinamilikiwa na Kampuni ya Triennex (Pty) Ltd. ya Afrika Kusini, hisa 50 nyingine zilikuwa zinamilikiwa na Serikali ya Tanzania kwa kupitia kwa Msajili wa Hazina katika Wizara ya Fedha wakati makampuni mawili ya Kiingereza – London Law Services Ltd. na London Law Secretarial Ltd. - yalikuwa yanamiliki hisa moja moja za Meremeta Ltd. Kwa mgawanyo huu wa hisa za Meremeta Ltd., ni wazi kwamba makampuni binafsi ya kigeni yalikuwa yanamiliki sehemu kubwa zaidi ya hisa za kampuni hiyo.

Bunge limepewa wajibu wa kusimamia Serikali na Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, 1977. Namna pekee ya Bunge kutekeleza wajibu wake wa kikatiba ni kutumia fursa ya wabunge kuuliza maswali kwa mawaziri na vile vile kwa kuunda Kamati Teule za Uchunguzi au kutumia Kamati za Kawaida za Bunge kuchunguza masuala mbali mbali yanayohusu uendeshaji wa Serikali. Masuala yanayohusu makampuni ya Meremeta Ltd., Tangold Ltd. na Deep Green Finance Co. Ltd. yamejadiliwa sana na Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali tangu mwaka 2007. Kwa muda wote huu, Serikali ya Tanzania haijawahi kuzikanusha rasmi tuhuma za ufisadi zinazoyahusu makampuni haya. Kauli za Spika Sitta na Waziri Mkuu Pinda zinadhihirisha kwamba matumaini hayo ya Serikali hayajafanikiwa. Msimamo wao wa sasa ni dhahiri unalenga kutumia kivuli cha usalama wa taifa au jeshi ili kuzima mjadala huu ndani na nje ya Bunge. Iwapo watafanikiwa kwenye jambo hilo hapana shaka kwamba watatumia kivuli hicho hicho kuzima mijadala mingine ndani na nje ya Bunge na uwezo wa Bunge wa kusimamia Serikali na uhuru wetu wa kushiriki katika mijadala inayohusu masuala mbali mbali muhimu kwa wananchi utafifishwa.

Ni dhahiri kuwa upotevu wa fedha bilioni 155 kupiti makampuni hewa ya Meremeta, Tangoald na Deep Green umeongeza kufukarishwa kwa wananchi walio wengi katika nchi yetu. Fedha hizo zingetosha:

•kujenga visima vya maji safi elfu kumi na tano (15,000) kwa thamani ya shilingi milion kumi (10 milioni) kila kimoja. Nchi yetu ina vijiji visivyozidi elfu kumi na mmoja. Kwa maana hiyo kila kijiji kingepata karibu visima viwili;
•Fedha hizi zinaweza kusomesha zingewezesha watoto zaidi la laki tano (500,000) kusoma bure shule za sekondari kwa gharama ya shilingi laki tatu kila mmoja;
•Kujenga zahanati 1,550 kwa gharama ya shilingi milioni mia moja kila zahanati. Kwa maana hiyo vijiji 1,550 hapa nchini vingepata zahanati;
•Fedha hizo zingeweza kutoa motisha kwa kulipa madaktari na watoa huduma katika sekta ya afya ili waweze kuwahudumia vizuri wagonjwa na hivyo kupunguza vifo visivyo vya lazima. Kwa mfano fedha hizo zingetosha kuajiri madaktari 6,458 kwa mwaka na kuweza kuwalipa shilingi milioni mbili kwa mwezi kila mmoja;
•Kadhalika fedha hizo zingeweza kujenga madarasa 17,222 kila moja kwa gharama ya shilingi milioni tisa. (9,000); au
•Kuajiri wauguzi 12,917 kwa mwaka na kila mmoja akiwa analipwa shilingi milioni mmoja (1,000,000) kwa mwezi

Kwa vile inaelekea Serikali haijawa tayari kuchukua hatua dhidi ya waliohusika na ufisadi uliofanywa kwa kutumia makampuni ya Meremeta Ltd., Tangold Ltd. na Deep Green Finance, tunadai mambo yafuatayo :

i.Bunge la Jamhuri liunde Kamati Teule ya Uchunguzi wa makampuni haya kama lilivyofanya kuhusiana na Kashfa ya Richmond;
ii.Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Muungano atumie uhuru na mamlaka aliyopewa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 kufanya uchunguzi maalumu (special audit) ya taarifa za fedha na/au mahesabu ya makampuni ya Meremeta Ltd., Tangold Ltd. na Deep Green Finance kwa nia ya kuhakikisha kwamba fedha zote zilizotolewa na Benki Kuu ya Tanzania kwa makampuni hayo ziliidhinishwa kisheria na kwamba zilitumiwa kwa ajili ya shughuli iliyoidhinishwa kwa mujibu wa sheria;
iii.Watakaogundulika kuhusika na kashfa hii ya fedha za umma wachukuliwe hatua zinazostahili; kisheria na kinidhamu
iv.Waziri Mkuu Mizengo Pinda achukuliwe hatua za kinidhamu kwa kupotosha bunge juu ya umiliki wa meremeta
v.Tunawahimiza wanachi wote wa Tanzania wadai uwajibikaji wa wabunge wao na serikali yao kwa ujumla kuhusiana na wizi/ufisadi uliyofanywa na makampuni ya Meremeta, Tangoald na Deep green kwa sababu ni wizi mkubwa unaochangia kwa kiasi kikubwa wananchi wengi kuwa na maisha magumu hivi sasa

Imetolewa na FemAct na kusainiwa na
1.Tanzania Gender Networking Programme (TGNP)
2.Legal and Human Rights Centre (LHRC)
3.Concern for Development Initiatives in Africa (ForDIA)
4.Youth Action Volunteers (YAV)
5.The Leadership Forum (TLF)
6.Coast Youth Vision Association (CYVA)
7.Walio Katika Mapambano na AIDS Tanzania (WAMATA)
8.Tanzania Media Women’s Association (TAMWA)
9.Youth Partnership Countrywide (YPC)
10.Tanzania Human Rights Fountain (TAHURIFO).
11.HakiArdhi
12.Women in Law and Development in Africa (WILDAF
13.Women Legal Aid Centre (WLAC)
14.Lawyers’ Environmental Action Team (LEAT)
15.Tanzania Ecumenical Dialogue Group (TEDG)
16.Life Skills Association (LISA)
17.Women Fighting Against Aids in Tanzania Trust Fund (WOFATA)
18.Taaluma Women Group (TWG)
19.Marcus Garvey Foundation (MGF)

28 June 2009

Enzi za uhai wa Prof. Haroub Othman


Profesa Haroub Othman (kati) akiwa na Profesa Saida Yahya Othman(ambaye ni Mke wake) (shoto) na Profesa Amandina Lihamba enzi za uhai akiwa kwenye moja ya shughuli zake.

Wanazuoni wamlilia Profesa Haroub Othman, kuzikwa leo alasiri zanzibar


Hayati Profesa Haroub Othman

Mazishi ya Hayati Profesa Haroub Othman yamepangwa kufanyika kesho shambani kwake Chuini, Unguja. Kwa mujibu wa mwana wa marehemu, Tahir Othman, mazishi yatatanguliwa kumuombea katika swala ya alasiri katika msikiti wa Masjida Salaam uliopo Michenzani Msufini jirani na Quality Supermarket.
------------------------------------------------------
Dear brothers, sisters and comrades:

This is so devastating. I have no words. And here I am sitting in Toronto in transit to Dar tomorrow arriving Dar on July 1st afternoon. I have no one here to share my sorrow with except Parin and amil. Don't know what to do.

Feeling so helpless.
I am with you in spirit.

Collectively express my profound shock to Saida, my dear friend.
Give the best farewell ever to my dear dear friend of over 40 years.

Buriani rafiki yangu,
ndugu yangu,
kamaradi Haroub Issa

Wako,
Issa Shivji

Friday, June 26, 2009

Vita vya wenyewe kwa wenyewe Barani Afrika


Vita vya wenyewe kwa wenyewe barani Afrika imekuwa na madhara makubwa hasa kwa Wanawake na Watoto, kama picha hii inavyoonyesha mtoto huyu akiteseka kwa njaa na kuhatarisha maisha yake kama picha inavyosomeka.

Wadau mnasemaje?

Thursday, June 25, 2009

Mgongano huu wa maudhui kati ya Ikulu na wizara!

KWA mara nyingine, Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 imekuwa na kasoro kadhaa. Kasoro ambazo ni dhahiri si za bahati mbaya.

Kasoro hizo ni pamoja na kufutwa kwa misamaha ya ushuru wa mafuta ya petroli kwa kampuni mpya za uchimbaji dhahabu nchini, huku zile za zamani zikipewa fursa ya kipekee ya kujadiliana kwanza na serikali.

Mara kwa mara tumekuwa tukisikia serikali, kupitia kwa viongozi wake wakiwamo mawaziri na wakati mwingine Rais, wakisisitiza kuwa kazi kubwa ya serikali ni kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Huu ni wimbo wa muda mrefu, ulioanza kuchukua nafasi kubwa zaidi katika Serikali ya Awamu ya Tatu na kuendelezwa na serikali ya sasa.

Kwa kuzingatia wimbo huo, milango na hata madirisha ya uwekezaji nchini yalifunguliwa. Wawekezaji wa sekta ya madini wakaanzisha shughuli zao bila bughudha yoyote na zaidi, wakapatiwa misamaha mbalimbali ya kodi.

Wakafutwa machozi hata pale walipoigiza tu kulia. Wakati mwingine ilipojitokeza wakazi wa jirani na migodi wameingia katika mgogoro na wawekezaji hao, basi serikali ilisimama upande wao dhidi ya wananchi. Mifano iko mingi na sehemu ya ushahidi ni kesi zilizowahi kufunguliwa kuhusu migogoro hiyo.

Wapo wananchi waliohamishwa bila fidia inayostahili ilimradi tu wapishe ardhi waliyokuwa wakitumia ili mwekezaji achimbe dhahabu. Hapa, wakazi wa Nyamongo, wilayani Tarime wanafahamu suala hili kwa undani zaidi.

Lakini pia nani amesahau kiwewe cha uhusiano wa shaka, kati ya wawekezaji wa sekta ya madini na baadhi ya viongozi wa serikali kiliwahi kumtia matatani aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, baada ya kutia saini mkataba wa uchimbaji madini hotelini mjini London, ilimradi tu asikwamishe ‘mipango.’

Kashfa Buzwagi ndiyo ile iliyochangia kumtia katika msukosuko Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, ambaye mwishowe alisimamishwa kuhudhuria vikao vya mkutano wa Bunge.

Kimsingi, uzoefu unaonyesha kuwapo kwa upendeleo wa muda mrefu kwa kampuni za uchimbaji dhahabu ambao wakati mwingine hata hutishia usalama wa nyadhifa za viongozi wa serikali. Upendeleo huo ulianzia katika misamaha ya kodi ya mapato hadi katika ushuru wa mafuta ya petroli.

Soma zaidi

Wednesday, June 24, 2009

Mollel, Selelii, Mpendazoe wawasha moto


-Wizara za Miundombinu, Nishati zasubiriwa kwa hamu
-Mawaziri watatizwa na namna ya kuitetea bajeti

HALI ya mambo ndani ya Bunge si shwari. Kuna mgawanyiko wa dhahiri kati ya mawaziri na wabunge na mwelekeo wa hoja za baadhi ya wabunge dhidi ya Serikali unaonekana kuwaelemea mawaziri, Raia Mwema imebaini.

Wakati hali ikiwa hivyo, tayari Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ameahidi kulinda uhuru wa kuzungumza bungeni lakini kwa kuzingatia matakwa ya kanuni zinazosimamia mijadala.

Hali ya mambo kuwa magumu kwa upande wa Serikali ilianza kujitokeza mwanzoni mwa wiki hii, wakati Mbunge wa Nzega, Lucas Selelii (CCM), alipoonyesha kukerwa na uamuzi wa mawaziri kwa kushirikiana na watalaamu serikalini.

Salelii alionyesha kukerwa na uamuzi wa kukarabati na kupanua barabara kutoka Same hadi Korogwe ambayo inapita kwa urahisi na yenye kiwango cha lami wakati maeneo mengine muhimu ya nchi yakikosa huduma hiyo.

Katika kuonyesha kukerwa na suala hilo, mbunge huyo alisema anashangazwa na uamuzi huo akiamini kuwa ungeweza kuwa na tija zaidi kama ungelenga kupanua kipande cha barabara kati ya Dar es Salaam hadi Chalinze, hatua ambayo ingepunguza msongamano wa magari hasa ikizingatiwa kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa uchumi wa nchi kwa kuwa hutumika kupitisha mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam hadi katika nchi za Malawi, Zambia na hata Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Lakini pia Salelii alionyesha kukerwa na uamuzi huo ambao pia ungeweza kuelekezwa katika barabara inayounganisha Mkoa wa Tabora na mikoa mingine, pia akiamini kuwa ni hatua ambayo ingechangamsha uchumi katika mikoa ya Magharibi mwa nchi.

Baada ya kuonyesha kukerwa huko mbunge huyo alijikuta akitumia maneno makali bungeni, na akitangaza kutaka mawaziri walaaniwe na kudai kuwa wamekuwa na hila na roho mbaya dhidi ya baadhi ya wabunge kwa kuwa wanapendelea miradi ya maeneo wanakotoka na mingine ambayo iko kwa baadhi ya wabunge vipenzi vyao.

Hatua hiyo ya Selelii kutumia maneno hayo ilimfanya Mbunge wa Pangani, Rished Abdallah, kuingilia kati akiomba mwongozo wa Spika akilenga kumtaka Spika kumwelekeza Selelii afute kauli yake ya kulaani mawaziri kwa kuwa ni ya kukera, ambayo ni kinyume cha kanuni za Bunge zinazosimamia mijadala.

Mbali na kulaani, Selelii aliwataka wabunge kusoma makaburi ambayo alidai yana maandishi yanayosema “Sisi tuliolala hapa tulikuwa kama ninyi” wengine wakitafsiri kauli hiyo kuwa uwaziri waliokuwa nao umetokana na ubunge na hivyo wanaweza kurudi kubaki wabunge na kwamba uwaziri si wa milele.

Lakini Spika Sitta hakuwa tayari kufanya hivyo na badala yake alisema haamini kama kauli hiyo ya Selelii ilifikia kiwango cha kukera kama ambavyo kanuni ya Bunge inavyotamka isipokuwa akasema ilikuwa ni kauli inayoonyesha hisia halisi za mbunge huyo.

Soma zaidi

Mpango wa Kikwete ni EPA 'namba mbili' - Mbunge

-Hoja yawasilishwa utungiwe sheria maalumu

MPANGO wa Serikali wa kuhami na kunusuru uchumi dhidi ya mtikisiko wa uchumi duniani, uliotangazwa na Rais Jakaya Kikwete, umetiliwa shaka na kambi ya upinzani ambayo imesema unaweza kuleta "EPA namba mbili".

Makombora dhidi ya mpango huo yalitoka Kambi ya Upinzani Bungeni kupitia kwa kiongozi wake, Hamad Rashid Mohamed. Kambi ya Upinzani imependekeza mpango huo kutungiwa sheria maalumu ya udhibiti kwa kurejea uzoefu wa baadhi ya nchi za Asia.

Mapendekezo hayo yanatajwa kulenga kuinusuru nchi na kile kilichoelezwa kuwa ni “EPA namba mbili”, hasa ikizingatiwa kuwa katika wizi wa fedha za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), takriban Sh bilioni 133 zililipwa kwa kampuni nyingine hewa. Ikihofiwa kuwa huenda katika kufanikisha mpango huo na hasa suala la kufidia hasara za baadhi ya kampuni, zipo kampuni hewa.

Katika hotuba yake bungeni wiki hii, mjini Dodoma , Hamad Rashid Mohamed, kwa niaba ya wabunge wenzake kutoka vyama vya CUF, CHADEMA na UDP, alihoji masuala mbalimbali kuhusu matumizi ya fedha hizo za stimulus package, zipatazo Sh. trilioni 1.7, zilizotangazwa na Rais Kikwete.

“Tunataka sheria ya Appropriation Act iwe na Schedule maalumu ya Stimulus Package na iseme waziwazi nani atapata nini, kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge iwe inapata taarifa kila miezi 3 ya utekelezaji wa hiyo stimulus package.

“Ni ukweli uliowazi kuwa stimulus package inazinufaisha benki tu, kwa kuzipa mwanya wa kufanya biashara nzuri na Serikali kwa kutumia fedha za Serikali yenyewe, na ndio maana katika nchi nyingine serikali imelazimika kuwa na hisa ili kuhakikisha kuwa fedha iliyotolewa ambayo inatokana na kodi za wananchi inadhibitiwa na kurudi kwa walipa kodi na wapiga kura.”

Hamadi alisema katika bajeti ya mwaka 2007/08 na ile ya 2008/09 serikali ilijizuia kukopa kwenye mabenki, kwa kigezo kikubwa kuwa mabenki yaweze kufanya biashara ya kukopesha sekta binafsi na kuwa zuio hilo liliongeza ufanisi kwa mabenki kukopesha sekta binafsi kwani mikopo kwa sekta binafsi ilipanda hadi kufikia asilimia 40.

Stimulus Package itapunguza mikopo ya benki kwenda kwenye sekta binafsi, na yale mafanikio yaliyokwishafikiwa yatayeyuka, vinginevyo mabenki yawekewe viwango vya kufikia katika kutoa mikopo nje ya stimulus package.

“Kwa mujibu wa taarifa ya Sera ya Fedha ya BoT serikali itazikopesha benki Sh bilioni 270 kwa ajili ya kuzikopesha sekta binafsi. Itatoa Sh bilioni 205 ili kukopa kwenye benki hizo.

Je, benki hizo zikishindwa kutumia fedha zile ambazo serikali imeziweka ili kukopesha sekta binafsi kutumia fedha hizo kufanya biashara na serikali kwa fedha za serikali? Hili litadhibitiwa vipi? Waziri atueleze,”, alihoji Hamad na kuongeza kuwa;

“Mwaka huu wa bajeti ni ya kuongeza matumizi na madhara yake ni mpango huo wa kuhami uchumi kuongeza mfumuko wa bei.

“Serikali imeamua kufidia vyama vya ushirika na kampuni zinazonunua mazao ya wakulima na kuyauza kwa hasara. Katika soko huria kuna kupata faida na kupata hasara. Wafanyabiashara makini wa mazao hupanga bei zao za kununulia mazao kwa kuzingatia bei walioipata katika soko la baadaye.

“Hata hivyo wengine hawapendi kuchukua tahadhari kwa kutegemea kwamba bei itapanda na kwa hiyo watapata faida kubwa. Bei imeshuka kwa hiyo wamepata hasara.Ó Alihoji akisema; Je, hakuna wafanyabiashara wa mazao waliolipa mikopo waliokopa kwa kujibana. Serikali ina uhakika gani kuwa mikopo hii ilitumiwa vizuri?”

Pia alipendekeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua kampuni zitakazopewa fedha kutoka katika mpango wa kuhami uchuni.

Alitaka CAG kwanza kuthibitisha kuwa hasara waliopata haikutokana na matumizi mabaya ya mikopo na kwamba, gharama ya ukaguzi huu ilipwe na benki zilizokopesha. Alionya kuwa, la sivyo serikali inaweza kuliingiza taifa katika EPA namba mbili.

Kwa upande mwingine, Hamad katika hotuba yake hiyo alihoji kama serikali iko tayari kusaidia wafanyabiashara, kampuni na benki zilizopata hasara lakini bia kuwapo kwa hatua zozote za kuwasaidia wakulima wanaopata bei mbaya ya mazao isiyorudisha gharama.

“Hivi sasa wakulima wa pamba hawavuni pamba yao kwa kuwa bei ya pamba ni ya chini sana na hakuna soko la uhakika. Si hotuba ya Rais wala ya Waziri wa Fedha iliyotoa matumaini kuwa walalahoi pia wanakumbukwa na watafidiwa hasara na athari walizozipata kutokana na mtikisiko wa uchumi duniani.

“Serikali imeamua kutoa udhamini wa madeni ambayo wakopaji kwa sababu ya msukosuko wa uchumi wa dunia wanapata matatizo kulipa kwa wakati. Madeni hayo yanafikia Shs.270 bilioni.

“Kuna hatari ya serikali kujiingiza katika kudhamini madeni ambayo hatimaye yatabidi yalipwe na serikali. Serikali inajiongezea mzigo wa madeni yanayoweza kutokea (Contigent Liabilities).

Serikali imeamua madeni haya yadhaminiwe kwa miaka miwili na siyo mwaka mmoja ili shughuli za Uchaguzi Mkuu wa 2010 ziwe zimemalizika. Hii itatoa mwanya kwa wanaodhaminiwa madeni wachangie kwenye kampeni na baada ya uchaguzi mzigo wa madeni ubebwe na serikali.

“Kuna hatari ya EPA nyingine kuzinduliwa. Ukaguzi wa kina wa mahesabu ya makampuni husika ufanywe na CAG kwa gharama za mabenki yaliyokopesha kabla ya serikali kuyadhamini makampuni haya,” alionya Hamad.

Kutokana na maelezo yake hayo, katika mazungumzo yake na Raia mwema nje ya ukumbi wa Bunge, Hamad alisema endapo Waziri wa Fedha na Uchumi hatatekeleza mapendekezo hayo na hasa suala la kutungia sheria stimulus package, basi wataamini kuwa huo ni mpango wa kuchota fedha ili zitumike katika uchaguzi kama ilivyo mabilioni ya fedha za EPA.

“Endapo serikali haitakubali haya na hasa suala la kuwapo kwa sheria ya usimamizi wa fedha hizo Sh trilioni 1.7 na pia kama haitakubali kampuni zitakazopewa fedha za kufidia hasara kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, ni wazi kuwa tutakuwa tumethitisha mpango huo ni “EPA namba mbili” alisema Hamad.

Waziri Mkulo anatarajiwa kutoa majibu ya hoja hizo pamoja na hoja nyingine za wabunge kesho wakati atakapokuwa akijumuisha mapendekezo ya bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010. Ijumaa wiki hii, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, anatarajiwa kuwasilisha bajeti kwa ajili ya ofisi yake kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amefanya uteuzi wa Naibu Makatibu Wakuu wa Wizara kama ifuatavyo kwa lengo la kujaza nafasi zilizokuwa wazi pamoja na kuongeza ufanisi wa kazi kwenye Wizara kama ifuatavyo:-

Bwana ELIAKIM CHACHA MASWI
- ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, (TAMISEMI) atakayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kabla ya uteuzi huo, Bwana Maswi alikuwa Kamishna Msaidizi wa Bajeti, Wizara ya Fedha na Uchumi.

Bwana JUMANNE ABDALLAH SAGINI – ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI atakayeshughulikia Elimu ya Msingi na Sekondari. Kabla ya uteuzi huu Bwana Sagini alikuwa Mratibu wa Mradi wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Dr. SHAABAN RAMADHANI MWINJAKA – ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko. Kabla ya uteuzi huu Dr. Mwinjaka alikuwa Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Ofisi ya Makamu wa Rais.

Bi. ELIZABETH JOKTAN NYAMBIBO – ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kabla ya uteuzi huu Bi. Nyambibo alikuwa Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko.

Bwana ULEDI ABBAS MUSSA – ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kabla ya uteuzi huu Bwana Mussa alikuwa Mkurugenzi wa Biashara na Uwekezaji kwenye Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Dr. PATRICK S. J. J. MAKUNGU – ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia. Kabla ya uteuzi huu Dr. Makungu alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa ‘Centre for Agricultural Mechanization and Rural Technology’, Arusha.

Uteuzi huu unaanza tarehe 13 Juni, 2009.

(Phillemon L. Luhanjo)
KATIBU MKUU KIONGOZI

Tuesday, June 23, 2009

Takrima marufuku mwakani

Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 itafanyiwa marekebisho ambapo vipengele vinavyoruhusu takrima katika uchaguzi, vitaondolewa. Akiwasilisha hotuba ya makadirio ya matumizi ya ofisi yake bungeni jana, Pinda alisema hatua hiyo ni sehemu tu ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwakani.

Pia alisema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) itaandaa vigezo na utaratibu utakaotumika kugawa majimbo ya uchaguzi nchini. “Mapendekezo mengine (ya marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi) ni kuongeza muda wa kufungua kesi za kupinga matokeo na kuweka kikomo cha mgombea kujitoa katika uchaguzi,’’ alisema Pinda.

Vilevile katika marekebisho hayo, NEC itapewa mamlaka ya kuandikisha wapiga kura wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuwa na kipindi maalumu cha kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga kura angalau mara mbili kati ya uchaguzi mmoja hadi mwingine.

Alitaja mapendekezo mengine kuwa ni kuipa NEC, mamlaka ya kufanya uchaguzi mdogo wa madiwani angalau mara mbili kwa mwaka, badala ya kila wakati kutokana na kumalizika kwa kesi mahakamani. Mapendekezo mengine kwa mujibu wa Pinda, yanalenga kubadilisha kipindi cha kufanya uteuzi wa wagombea, endapo mgombea urais au mgombea mwenza atafariki dunia. Kutokana na mabadiliko hayo, Pinda aliiomba jamii kuipa ushirikiano NEC wakati wa kutekeleza majukumu yake, ili wapiga kura wasikose haki yao ya msingi ya kuchagua viongozi.

Mzindakaya :Wanaopinga ufisadi ni mafisadi

Mbunge wa Kwela, Dk Chrisant Mzindakaya amewashambulia wanaowatuhumu wenzao kuwa ni mafisadi kwa kusema kuwa nao ni mafisadi na wana roho mbaya.

Mbunge huyo pia amewatuhumu wanaomlaumu Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa kuwa wana roho za kishetani.

Mzindakaya amesema bungeni leo kuwa, wanaosema wenzao ni mafisadi wana roho za kifisadi na amehoji kwa nini wawaandame wenzao. “Na kwa nini wewe umezaliwa kuandama wenzako tu?” amehoji Mzindakaya wakati anachangia hoja ya bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Amesema, watu hao wana roho mbaya, na wanajifanya wazuri kwa kuwa hawana moyo wa kuthubutu. “Binadamu ana kasoro moja, ukifanya mema kumi, ukakosea moja atafuta yote” amesema mbunge huyo katika kikao cha 11 cha mkutano wa 16 wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma.

Amejisifu kwa kuwa na moyo wa kuthubutu uliomuwezesha kuwa mkulima bora mkoani Rukwa, anajivunia hilo na hahitaji kusifiwa. Naye Mbunge wa Same Mashariki, Anne Killango Malecela jana jioni aliwaponda wanaotaka kuwanyamazisha wanaopinga ufisadi akiwamo yeye.

“Kama wewe ni fisadi kwa nini nisikuseme, na ninaomba wananchi watambue kwamba hatutanyamaza hata siku moja” alisema wakati anachangia hoja ya bajeti hiyo.

Ameitaka Serikali ilichukulie hatua kali gazeti lililotangaza kuwa jimbo lake na majimbo mengine manne yapo wazi bungeni na isipofanya hivyo bungeni patakuwa hapatoshi. Mbunge huyo aliwaonyesha wabunge gazeti hilo lilitwalo Nipe Habari, na kusema kuwa ni gazeti uchwara na linaandika mambo ya kihuni.

Kwa mujibu wa Mbunge huyo, gazeti hilo limeandika kuwa, majimbo matano yapo wazi, na kwamba, waliokuwa wabunge wa maeneo hayo ni mgambo katika vita dhidi ya ufisadi nchini.

“Patakuwa hatatoshi tena hapa, katika hili sitakubali” amesema Mbunge huyo aliyetangazwa kuwa ni mwanamke jasiri zaidi Tanzania. Alimtaka Waziri Mkuu atapokuwa anajibu hoja za wabunge wanaochangia hoja ya bajeti ya ofisi yake amweleze gazeti hilo limechukuliwa hatua gani kali.

“Jambo hili limenikera sana, jambo hili limeniudhi”alisema Killango Malecela bungeni wakati anachangia katika hoja ya bajeti ya ofisi Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Alitaka vyombo vya habari viache kuandika mambo ya kihuni na akadai kuwa, magazeti kama hayo yanaweza kuiingiza nchi kwenye vurugu.

“Hakuna dhambi kubwa kama hii, Mheshimiwa Spika kesho asubuhi litasema kiti cha Rais kipo wazi” alisema na kutoa kauli iliyoashiria kuwa habari hiyo iliandikwa na wanaounga mkono ufisadi.

Naye Mbunge wa Viti Maalum, Grace Kiwelu amewatuhumu watendaji wa Halmashauri wakiwamo wanasheria kuwa ni wala rushwa, hawanna maadili, na wanawakandamiza wananchi kwa maslahi yao.

“Sijawahi huona hata siku moja tajiri ananyang’anywa ardhi, masikini ndiyo wananyang’anywa ardhi” amesema Mbunge huyo leo wakati anachangia bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu.

Amewatuhumu pia watumishi wa umma kuwa ni watoro, wanatumia muda wa kazi kufanya shughuli zao binafsi, wanaacha makoti na mikoba ofisini kama kiini macho. Wakati anachangia, amesema pia kuwa Tanzania inahitaji wawekezaji kwenye sekta ya viwanda na si wa kujenga migahawa au kuuza maua.

Amesema, kuna raia wengi wa China nchini wanaofanya biashara zinazoweza kufanywa na watanzania hivyo wachunguzwe kwa madai pia kwamba, wanawanyanyasa wananchijiriwa katika biashara hizo na wanalipa mishahara midogo.

Monday, June 22, 2009

'Kilimo Kwanza' iwe Kilimo Kwanza kweli kweli

WIKI iliyopita Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, akiwasilisha bungeni taarifa ya hali ya uchumi na malengo kwa kipindi cha mwaka wa fedha wa 2009/2010, alitangaza kuanzishwa kwa kaulimbiu mpya ya Kilimo Kwanza.

Katika kile kinachoonekana kuwa Serikali yetu, hatimaye, sasa imekikumbuka kilimo, Waziri Mkulo pia aitangaza nguzo kuu 10 zitakazotuwezesha kufikia mapinduzi ya kilimo nchini.

Alizitaja nguzo hizo kuwa ni Dira ya Kilimo Kwanza, Ugharimiaji wa Kilimo Kwanza, Mabadiliko ya Mkakati wa Kushughulikia Kilimo, Kuhuisha Muundo wa Asasi za Kilimo, Ardhi, Vivutio vya Kilimo, Sayansi na Teknolojia, Mageuzi ya Viwanda vya Kilimo, Raslimali Watu, Miundombinu na Uhamasishaji Watanzania juu ya dhana ya Kilimo Kwanza.

Tunapenda kuipongeza Serikali yetu kwa kukikumbuka kilimo na kwa kuibuka na kaulimbiu hiyo ya Kilimo Kwanza.

Lakini pamoja na pongezi hizo, tunatahadharisha kwamba kaulimbiu ya Kilimo Kwanza itabakia tu ni kaulimbiu; kama haitaandamana na matendo ya dhahiri katika kuzishughulikia hizo nguzo 10 zinazolenga kutuletea mapinduzi hayo ya kilimo nchini.

Tunatoa tahadhari hiyo tukikumbuka kwamba ukosefu wa kaulimbiu halijapata kuwa tatizo katika sekta ya kilimo nchini. Tumewahi kuwanazo nyingi tu; kama vile “Siasa ni Kilimo”, “Kilimo cha Kufa na Kupona”; lakini zote hazikutuwezesha kuyafikia Mapinduzi ya Kilimo tunayoyataka.

Kinachokosekana nchini si kaulimbiu za kilimo bali vitendo; yaani uchapaji kazi wa kweli kweli katika kutekeleza mipango ya kunyanyua kilimo hicho, na pia utoaji wa pesa za kutosha kutekeleza mipango hiyo.

Kwa hiyo tunataraji kwamba “Kilimo Kwanza” si ahadi tu ya makaratasi kama zilivyopata kuishia ahadi nyingine walizopewa wakulima wetu.

Na mfano mzuri ni CCM yenyewe. Katika ilani ya uchaguzi ya chama hicho ya mwaka 2005, wakulima waliahidiwa kwamba Serikali ya CCM itasambaza kilimo cha matrekta katika wilaya zote nchini. Leo hii, miaka minne baadaye, kilimo cha matrekta hakijasambazwa hata katika wilaya 15 tu nchini!

Kwa hiyo wakati tunaipongeza Serikali yetu kwa kuikumbuka sekta ya kilimo, inayohusisha asilimia 75 ya Watanzania, tunaitahadhirisha kuhusu utendaji. Tunataka Kilimo Kwanza iwe Kilimo Kwanza kweli kweli, na si ahadi nyingine tena kwenye makaratasi tu.

SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO AMBAPO WIKI HII LILIAN LIUNDI NA VENANT WILLIAM (TGNP) WATAWEZESHA MAJADILIANO YA WANAGDSS KUHUSU:

MAPITIO YA NUSU MWAKA YA GDSS; JANUARI-JUNI 2009!

LINI: JUMATANO TAREHE 24 JUNI 2009

Muda: SAA 9:00 – 11:00 JIONI

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni

WOTE MNAKARIBISHWA!!

Thursday, June 18, 2009

Tamasha la Jinsia 2009


Mtandao wa Mashirika Watetezi wa Haki za Binadamu na Jinsia nchini Tanzania (FemAct), Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) tunayo furaha kubwa kutangaza rasmi Tamasha la Jinsia la Mwaka 2009.

Mahali:Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Mkabala na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT)

Tarehe: 8 Septemba - 11 Septemba 2009

Mada Kuu: "Rasilimali Ziwanufaishe Wanawake Walioko Pembezoni"

Mada zitakazojadiliwa:

(1)Heshima ya Mwili na Ujinsia
(2)Haki za uchumi na maisha endelevu
(3)Maarifa, Sanaa na Utamaduni
(4)Siasa, Uongozo na uwajibikaji
(5)Virusi vya Ukimwi na Ukimwi: Zaidi ya Uhai

Malengo ya Tamasha la Jinsia 2009
1.Kusisitiza na kuimarisha vuguvugu la ukombozi wa wanawake kimapinduzi, kutengeneza nafasi kwa ajili ya: kuibua, kubadilishana, na kuanzisha fikra, uchambuzi na kutengeneza mikakati ya pamoja kwenye suala la rasilimali kuweza kunufaisha wanawake walioko pembezoni;

2.Kusherekea nguvu zetu za pamoja, kupanua na kuimarisha ushirikiano katika vuguvugu la kuwakomboa wanawake kimapinduzi katika ngazi na sekta zote za kijamii;

3.Kuimarisha kujinoa na kuongeza uwezo wa kuchambua, kutafiti na kutathamini masuala yahusuyo Jinsia na harakati za ukombozi wa wanawake na wanyonge wengine kote duniani na

4.Kuandika nyaraka na kusambatisha maarifa kuhusu harakati za ukombozi wa wanawake dunia na kuchangia kwenye mjadala wa mada kuu ya Tamasha la Jinsia 2009 na ile ya la Jinsia, Demokrasia na Maendeleo.

Ushiriki wako wako unaweza kuwa katika:
•Kuandaa mada na mawasiliano mbalimbali kwa njia tofauti (sanaa, wimbo, shairi, mjadala, paneli, n.k) kwenye warsha kutokana na masuala yaliyo tajwa hapo juu;
•Kuandaa na kuratibu warsha na mijadala ya kujenga uwezo;
•Kualika na kuwezesha ushiriki mtu mmoja mmoja au vikundi kwa ajili ya kuhudhuria Tamasha;
•Kutengeneza na kufanya maonesho ya vitabu, picha, kazi za mikono n.k;
•Kuandaa maonesho ya sanaa, tumbuizo, ngoma, michezo ya kuigiza n.k;
•Ushiriki katika mijadala ya warsha na semina za Tamasha;
•Kuchangia gharama za wale watakaohudhuria, na/au waandaaji wa Tamasha.

Tutafarijika sana endapo mtajiandikisha kwa wingi mapema iwezekenavyo kwa kulipa ada ya ushiriki TGNP mapema. Lugha rasmi za Tamasha ni Kiswahili na Kingereza. Kwa taarifa zaidi wasiliana nasi kupitia barua pepe: gf_coordinator@tgnp.org Simu: +255 754 784050, +255 715 784050 na +255 22 2443450/2443205/2443286 au tembelea tovuti yetu www.tgnp.org

JK amaliza Mgogoro

SERIKALI imesitisha mpango wake wa kuyafutia misamaha ya kodi mashirika ya dini na asasi zisizo za kiserikali (NGOs) kama ilivyopanga.

Hatua hiyo ya serikali inatokana na hatua ya Rais Jakaya Kikwete kuridhia ushauri alioupata kutoka kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye juzi alikutana na viongozi wa dini na kujadiliana nao kwa kina kuhusu mpango huo wa awali wa serikali.

Waziri Mkuu aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa jana, kuwa Rais Kikwete aliridhia mashirika hayo ya dini na NGOs kuendelea kupewa misamaha ya kodi jana.

Alisema serikali imefikia uamuzi huo baada ya kuona kuwa mpango huo umepokelewa kwa upinzani mkali na Wabunge, viongozi wa mashirika ya dini, wananchi na wahisani wa nje ambao wanasaidia miradi ya maendeleo kupitia mashirika ya dini.

Alisema serikali imeona mpango huo haujaeleweka vizuri kwani azma ya serikali ilikuwa si kufuta misamaha ya kodi hata kama huduma muhimu za jamii kama afya, maji na elimu kama ilivyoeleweka.

Alisema lengo kubwa lilikuwa ni kujaribu kubana mianya ya matumizi mabaya ya misamaha hiyo kwa baadhi ya viongozi wa mashirika ya dini ambao wamekuwa wakitumia misamaha ya kodi kujinufaisha.

“Baada ya kuona kuwa suala hili limekuwa na mjadala mkubwa hasa kwa Wabunge wa CCM, ambao wametushauri tulitazame kwa upana wake kutokana na mchango mkubwa wa mashirika haya kwa wananchi, serikali tumeona ni vizuri tukawasikiliza.

“Kutokana na usikivu wa serikali, jana (juzi) nilikutana na viongozi wa dini na tukalijadili suala hili kwa kina ili kuona nini cha kufanya.

Alikuwepo Baba Askofu Malasusa, Baba Askofu Mokiwa, Baba Askofu Mwamasika, Shiekh wa Mkoa wa Dodoma aliyekuja na Masheikh wengine na viongozi wengine wa dini ambao walitueleza atahiri za kuendelea na mpango huu,” alisema Waziri Mkuu.

Alisema rai ya viongozi hao wote kwa serikali ilikuwa ni kuisihi serikali kusitisha azma hiyo kwa vile ingeweza pia kuleta sura mbaya kwa wahisani wa nje ambao wanatumia fedha za walipakodi wao kuwasaidia wananchi wa Tanzania.

“Niliwaelewa ingawa pia niliwaeleza nia nzuri iliyokuwa nayo serikali katika mpango huu ya kubana maeneo ya misamaha kwani fedha hizo zikikusanywa zinaweza kuleta mchango mkubwa kwa maebdeleo ya wananchi wetu,” alisema.

Alisema kwa pamoja viongozi hao wa mashirika ya dini wameahidi kuisaidia serikali katika kuwasaka na kuwadhibiti viongozi wa dini wanaotumia mianya ya misamaha hiyo ya kodi kwa manufaa yao.

Alisema pia pande hizo mbili zimekubaliana kukutana ili kujadiliana mfumo mzuri utakaowezesha mashirika ya dini kuendelea na mfumo wa kutolipa kodi lakini wakati huohuo kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi.

Alisema ili kuziba nakisi ya makusanyo ya kodi itakayotokana na uamuzi huo wa serikali, Waziri Mkuu alisema tayari serikali imeainisha vyanzo vingine vya fedha vitakavyoweza kuziba pengo la mapato hayo ambayo yangepatikana kwa mashirika ya dini kulipa kodi.

Alisema Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo atakapomaliza shughuli za kuwasilisha bajeti yake bungeni, atakutana na wataalamu wa Wizara yake na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Harry Kitilya ili kuunda kamati itakayosimamia marekebisho ya mfumo ili kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi kwa mashirika ya dini na NGOs

Wednesday, June 17, 2009

TRA goigoi

Wabunge wameishambulia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwa ndiyo kikwazo cha kuboresha huduma katika bandari ya Dar es Salaam na imesababisha mrundikano wa shehena kutokana na urasimu wa kushughulikia nyaraka za waagiza bidhaa. Wakichangia bajeti ya Serikali jana, baadhi ya wabunge walisema licha ya Kampuni ya Kitengo cha Kuhudumia Kontena (TICTS) kuwa na matatizo yake, lakini urasimu wa wafanyakazi wa TRA wa kutaka kuthibitisha bei ya bidhaa ilikotoka kunachangia mrundikano wa shehena bandarini.

Mbunge wa Solwa, Ahmed Salum (CCM), alisema mifumo iliyowekwa na TRA katika kutoza ushuru bandarini, inakoroga mambo kuliko ilivyokuwa awali kwani ina michakato mirefu ya kushughulika mzigo wa mteja mmoja. Alisema TRA imechangia asilimia 70 ya mrundikano huo na ndio maana baadhi ya wafanyabiashara wameamua kupitishia shehena zao Mombasa, kutokana na kuchoshwa na urasimu huo unaosababisha mizigo kukaa muda mrefu bandarini.

“Kule wafanyabiashara wanafuata uharaka, kwani mzigo unakaa siku mbili licha ya kulipa gharama mara mbili ya ushuru unaotozwa na bandari ya Dar es Salaam,” alisema Salum. Mbunge huyo alisema bandari imewashinda viongozi waliopewa jukumu za kuisimamia na akapendekeza iundwe wizara maalumu ya kushughulikia bandari hiyo, badala ya kuiachia Wizara ya Miundombinu ambayo kila siku inaonyesha kushindwa.

Alisema TRA na wizara wamekuwa wakitupiana mpira kuwa kuna upande hauwajibiki, huku huduma zikiendelea kudorora kila siku bandarini hapo. Mbunge huyo alisema kama bandari ingesimamiwa vizuri, ina uwezo wa kuingizia nchi zaidi ya Sh trilioni 14 kwa mwaka, lakini kilichopo sasa ni porojo tupu. Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo (Chadema), alisema msongamano uliopo bandarini unasababishwa na TRA, kwani wafanyakazi wake wanatengeneza fursa ya rushwa kwa kuchelewesha nyaraka za wateja kwa makusudi.

“Tuna matatizo makubwa pale bandarini kwa sasa, enzi za Nyerere, mzigo ulikuwa unamaliza siku mbili, leo unachukua wiki tatu hadi mwezi maendeleo yatatoka wapi?” alihoji Ndesamburo. Alisema mtindo wa ofisa wa forodha kurudisha nyaraka katika nchi ambako mzigo umetoka ili kujiridhisha bei, ndio unachangia mrundikano wa shehena bandarini na kujitengenezea ‘ulaji’.

Alishangaa kuwa wakati Kenya wanapanua bandari yao, mipango ya Tanzania ni kutaka kujenga bandari nyingine Bagamoyo. Pia alishangaa kuwa wakati uwanja wa ndege wa Dar es Salaam haujapanuliwa, kuna mpango wa kujenga uwanja mwingine mpya Bagamoyo. “Hivi kama hatujaimarisha hii miundombinu iliyopo sasa, kwa nini tunataka kwenda Bagamoyo kujenga bandari na uwanja mwingine wa ndege, kwa nini au kwa vile Rais Kikwete (Jakaya) na Waziri wa Miundombinu wanatoka Bagamoyo?” alihoji mbunge huyo.

Mbunge wa Tabora Mjini, Siraji Kaboyonga (CCM), alisema bandari ya Dar es Salaam ni mgodi ambao kama Taifa litaamua kuelekeza nguvu zake huko, nchi itaondokana na umasikini na kuombaomba wakati wa bajeti. Alisema Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Zambia na nyinginezo, zinategemea bandari hii kupitisha shehena zao, hivyo akataka Serikali ifanye kila linalowezekana kuimarisha bandari hiyo.

“Tuondoe ukiritimba kwa TICTS ili uwepo ushindani wa kupakia na kupakua kontena pale bandarini, itasaidia kupunguza mrundikano wa shehena,” alisema Kaboyonga. Mbunge wa Viti Maalumu, Khadija Salum Al Qassmy (CUF), alisema kutojiamini kwa wafanyakazi wa TRA kumechangia kudhoofisha huduma ya bandari ya Dar es Salaam na akatoa mfano kuwa bandari ya Mombasa mzigo unachukua siku tatu, lakini Dar es Salaam ni siku 21. Alisema ‘long room’ ya TRA ambayo kila siku inaundiwa mtandao tofauti tofauti pia haijaleta ufanisi uliotarajiwa.

“Kwa mfano mtu unatuma nyaraka zako kwa mtandao, ukienda pale, unaambiwa hazijafika hii ni ajabu sana.” Alisema nchi kama Hong Kong, uchumi wake unategemea bandari, lakini nchini maneno ni mengi kuliko vitendo, ndiyo maana bandari ya Dar es Salaam imeelemewa na shehena, kutokana na watendaji wazembe kutochukuliwa hatua za kisheria.

Alipendekeza Serikali ipunguze maneno badala yake ifanye kwa vitendo kuboresha bandari ya Dar es Salaam ili nchi jirani zisiendelee kuchukua mipango ya Tanzania na kuiendeleza. “Ni kweli wenzetu wanachukua mipango yetu wanaifanyia kazi, ndiyo maana Mombasa inazidi kupanuka.” Mbunge wa Kwamtipura, Zuberi Ali Maulid (CCM) alisema wakati magari yameshuka ushuru Japan, maofisa wa TRA bado wanang’ang’ania kuwatoza ushuru wananchi kwa bei zao za miaka ya nyuma.

Wabunge wazidi ‘kung'ata’ mawaziri

Baadhi vya wabunge wamedai kuwa baadhi ya mawaziri hawana uzalendo, ndiyo maana baadhi yao wanatetea na kubeza vita dhidi ya ufisadi na wakati mwingine wanapitisha mikataba isiyo na maslahi kwa Taifa, hali inayoliingiza katika hasara kubwa.

Wakichangia hotuba ya Bajeti jana, wabunge hao walisema licha ya kuwa wataalamu nchini wana udhaifu mkubwa wa kujadiliana na kuingia mkataba na kampuni za wawekezaji, lakini kitendo cha Serikali kutochukua hatua kinaonyesha wazi kuwa kuna harufu ya ufisadi ndani ya Serikali. Mbunge wa Kishapu, Fred Mpendazoe (CCM), aliwafananisha mawaziri hao na mawe yaliyoko chini ya bahari ambayo hayawezi kusikia kilio cha mti wa mtende ulio jangwani.

Mpendazoe alihoji kama kweli Serikali iko makini kupambana na ufisadi, kwa nini wataalamu walioshiriki kuingiza nchi katika hasara kwa kuingia mikataba mibovu bado wanaendelea na kazi tena ndani ya Serikali. Alisema wakati Wizara ya Fedha inakiri kuwa Watanzania wengi wanaishi chini ya Sh 1,720 kwa siku, lakini kuna watu wachache ambao wananufaika na nchi hii na kusababisha umasikini mkubwa kwa wananchi wa kawaida.

Alitaja baadhi ya mifano ambayo wataalamu wa Serikali wameboronga kuwa ni kwenye ubinafsishaji wa mgodi wa Kiwira, Reli ya Kati, ATCL, Richmond, madini, IPTL, lakini wamekuwa wanaendelea na kazi. Mbunge huyo aliitaka Serikali isikilize kilio cha wananchi ambao wanaitaka ichukue hatua dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi. Mbunge wa Maswa, John Shibuda (CCM), alisema ukosefu wa uzalendo miongoni mwa mawaziri umekuwa chanzo cha mikataba mibovu kupitishwa na baadaye kuiweka nchi katika hali ngumu ya kiuchumi.

“Nyie mawaziri mnatupeleka wapi, si hii mikataba mibovu huwa inapitia kwenu, kama ni wazalendo kwa nini msiikatae?” alihoji Shibuda na kusema kukosekana huko kwa uzalendo ndani ya Serikali ndiko kumefanya nchi iendelee kuibiwa fedha nyingi na kampuni za uwekezaji. Mbunge huyo alisema ukosefu huo wa uzalendo ndio umekuwa kikwazo cha kukamilika kwa vitambulisho vya kitaifa, kwani kilichopo ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa sasa ni malumbano na kazi imekwama.

Alipendekeza Wakala wa Vitambulisho vya Taifa aondolewe kwenye Wizara ya Mambo ya Ndani ili kuharakisha mchakato wa kutengeneza vitambulisho hivyo, viisaidie nchi kupata kodi sahihi kutoka kwa wananchi wake. Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu (CCM), alisema nchi hii ni nzuri na ina raslimali nyingi ambazo zinaweza kuisaidia kuondokana na umasikini, lakini baadhi ya viongozi wanashiriki kuibomoa.

Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Mnyaa (CUF), alishangaa kuona hata Waziri wa Fedha na Uchumi na manaibu wake, hawajui jinsi rasilimali za nchi zinavyonufaisha nchi nyingine na badala yake wanatangaza mbele ya umma kuwa Serikali haina takwimu za nchi zinazonufaika. Mnyaa alitoa mifano ya namna misitu ya Tanzania inavyoinufaisha Kenya na sasa wamesitisha kuvuna misitu yao kwa kutegemea misitu ya Tanzania. Pia alitoa mfano wa Kenya inavyonunua ng’ombe Mara badala ya kununua nyama.

Tuesday, June 16, 2009

Serikali:Umasikini unapungua

Wizara ya Fedha na Uchumi imesema, siasa za Tanzania ni nzuri na kuna mipango mizuri ya maendeleo ndiyo maana umasikini wa kipato unapungua. Hata hivyo Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Omar Yussuf Mzee amesema, bungeni mjini Dodoma kuwa, kuna watanzania wengi wanaishi kwa kula mlo mmoja. Kiongozi huyo wa Serikali amesema leo kuwa, umasikini ni mchakato, unapungua siku hadi siku.

Mzee ameyasema hayo wakati anajibu maswali ya Mbunge wa Viti Maalum, Magdalena Sakaya aliyetaka kufahamu ni kwa nini watanzani wengi bado ni masikini wakati nchi imepata uhuru miaka 48 iliyopita.

Mbunge huyo pia alidai bungeni kuwa, watanzania wengi bado ni masikini kabisa kwa kuwa hakuna siasa safi, na pia hakuna mipango mizuri ya kuwawezesha wananchi wapate maendeleo.

Naibu Waziri Mzee amewaeleza wabunge kuwa kuna umasikini wa aina tatu ukiwamo wa elimu, afya na kipato.Amesema, kama Tanzania isingekuwa na siasa safi na mipango mizuri ya maendeleo, takwimu zisingeonyesha kupungua kwa umasikini wa kipato nchini.

Amewaeleza wabunge kuwa, mwaka 1991, asilimia 21.6 ya watanzania wote milioni 24.8 walikuwa masikini kabisa. Kwa mujibu wa kiongozi huyo, mwaka 2001, Tanzania ilikuwa na watu milioni 31.9, asilimia 18.7 kati yao walikuwa masikini kabisa, na mwaka 2007, asilimia 16.5 ya watanzania milioni 38.3 walikuwa masikini kabisa.

Mzee amelieza Bunge kuwa, watanzania wengi bado ni masikini kwa kwa wengi wao ni wakulima wanaotumia jembe la mkono, bei za pembejeo za kilimo zimepanda, na pia mabadiliko ya hali ya hewa yanathiri uzalishaji kwa kuwa sehemu kubwa ya kilimo nchini hutegemea mvua. Ametaja sababu nyingine kuwa ni ukuaji mdogo wa sekta ya viwanda, wakulima kukosa mitaji, na pia ukosefu wa ajira.

Serikali kuwasaka wanaowatumia watoto wa kike kufanya biashara ya ngono

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto itawasaka watu wanaowatumia watoto wa kike kufanya biashara ya ngono na kuwachukulia hatua za kisheria.Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dk Lucy Nkya amesema, Serikali imepata taarifa kuhusu kuwapo kwa biashara hiyo haramu inayofanywa hasa na wanawake wanaojipatia fedha kwa kuwauza watoto wa kike kwa wanaume ili wafanye nao ngono.

Dk Nkya ametoa onyo kwa wanaofanya biashara hiyo waache mara moja, na yupo tayari kushiriki kuwasaka wahusika ili wachukuliwe hatua.Ameyasema hayo katika ofisi za Bunge mjini Dodoma muda mfupi baada ya kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika kesho.

Kiongozi huyo wa Serikali amesema, kuwatumia watoto kufanya biashara ya ngono ni unyama hivyo Wizara hiyo itafanya utafiti kubaini maeneo walipo watoto hao, wahusika wanaofanya biashara hiyo, na maeneo wanapotoka watoto hao.Amewataka wazazi wawe waangalifu ili kuhakikisha watoto wanapata haki wanazostahili ikiwamo ya kulindwa, na ameziagiza pia kamati za shule zifuatilie maendeleo ya watoto shuleni.

Dk Nkya amesema, watoto watakaokamatwa watapelekwa kusoma katika vyuo vya maendeleo ya jamii ili wapate stadi za kazi zitakazowasaidia kujiajiri.Kuna taarifa zinazodai kuwa, kuna watu hasa wanawake wanaochukua watoto wa kike vijijini na kuwapeleka mjini na kuwafanyisha biashara ya ngono.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, watoto hao wamewekwa sehemu moja chini ya uangalizi wa wanawake hao, na kwamba kazi ya wasichana hao ni kufanya ngono na wanaume wanaotoa fedha kwa ajili ya huduma hiyo.Inadaiwa kuwa, ngono hiyo ni biashara, kiasi cha fedha wanazotozwa wanaume hutokana na makubaliano ya mwanaume mwanamke anayemiliki watoto hao, na kwamba, sehemu kubwa ya mapato anachukua mwanamke huyo na si mtoto.

Watoto wanaoishi katika mazingira ya hatari ni miongoni mwa changamoto zinazoikabili Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto.Dk Nkya ametaja changamoto nyingine kuwa ni kuwapo kwa watoto wanaoishi mitaani, kuongezeka kwa idadi ya watoto yatima katika jamii, na kuongezeka kwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji watoto majumbani, shuleni na mitaani.

Amesema, Serikali inaandaa mpango mkakati wa jamii kudhibiti watoto wanaoishi mitaani ili kusaidia upatikanaji wa mahitaji ya watoto hao kama vile chakula, mavazi, malazi, matibabu na elimu.Dk Nkya pia amewaeleza waandishi wa habari kuwa, Serikali inaendelea na mchakato wa kuandaa muswada wa sheria ili itungwe sheria moja kuwahusu watoto ili kuwawezesha watoto wapate haki zao kwa urahisi.

Maabara kujengwa shule zote za sekondari

Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ipo kwenye mchakato wa kuandaa utekelezaji wa mradi mkubwa wa ujenzi wa maabara katika shule zote za sekondari nchini unaotarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 592.

Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Gaudentia Kabaka amesema bungeni leo mjini Dodoma kuwa, mradi huo utahusisha pia ununuzi wa vifaa vya maabara hizo.Kwa mujibu wa Kabaka, mradi huo unatarajiwa kutekelezwa katika awamu ya pili wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari(MMES) kwa kuwashirikisha wadau wa maendeleo.

Mradi huo mkubwa utakuwa muendelezo mkakati wa serikali wa kuboresha elimu ya sekondari nchini ikiwa ni pamoja na kutoa ruzuku kwa ajili ya ujenzi wa maabara za sayansi kwenye shule hizo. Kati ya mwaka 2008/2009, Serikali ilipanga kutoa ruzuku za kujenga maabara 230 katika shule za sekondari, 182 zimejengwa, ujenzi wa maabara nyingine unaendelea na kwa mujibu wa Kabaka, utakamilika haraka iwezekanavyo.

Licha ya kujenga maabara hizo, ruzuku hiyo imelenga pia kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Kabaka amewaeleza wabunge kuwa, ili kutekeleza lengo hilo, katika kipindi hicho cha mwaka 2008/2009 Serikali ilitenga sh bilioni 3.9 kujenga maabara hizo na kuzinunulia vifaa vya kufundishia na kujifunzia.

Amesema, fedha hizo hazitoshi kujenga maabara na kununua vifaa katika kila shule hivyo Serikali imezishauri shule zifanye hivyo kwa awamu. Kikao cha sita cha mkutano wa 16 wa Bunge kinaendelea Dodoma, baada ya kipindi cha maswali na majibu, wabunge wataendelea kujadili bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Monday, June 15, 2009

Serikali yajitwisha mzigo bajeti mpya

BAJETI ya serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 iliyopangwa kugharimu Sh trilioni 9.5 ikilinganishwa na bajeti iliyopita ya Sh trilioni 7.3, imeelezwa kuwa mzigo mzito zaidi kwa serikali kutokana na kubebeshwa vipaumbele vingi zaidi ya uwezo halisi wa kiuchumi.

Bajeti hiyo ambayo itasomwa na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, imebebeshwa vipaumbele sita. Kuna maoni kwamba bajeti hiyo na hasa uchumi halisi wa nchi hauna uwezo wa kumudu kutekeleza kwa ufanisi idadi hiyo ya vipaumbele kwa wakati mwafaka.

Baadhi ya wabunge wametoa maoni tofauti na mmojawapo ameonya kuwa, uchumi ni mdogo na haumudu idadi kubwa ya vipaumbele na kwamba unaweza tu kumudu kutekeleza kwa kiwango cha juu cha ufanisi vipaumbele kama vitatu.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na Raia Mwema wiki hii, Mbunge wa Ulanga Magharibi (CCM) na aliyepata kuwa Waziri wa Uchumi, Mipango na Uwezeshaji katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Dk. Juma Ngasongwa anaamini kwamba uchumi wa Tanzania, na hasa baada ya mtikisiko wa uchumi wa dunia, unamudu vipaumbele viwili hadi vitatu tu, na si zaidi ya hapo.

Dk. Ngasongwa, ambaye alishiriki kuandaa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2005, anasema katika mahojiano hayo, yaliyochapishwa katika kurasa za katikati za toleo hili, kuwa kwa uchumi wa Tanzania kubebeshwa vipaumbele zaidi ya vitatu hakutaweza kutoa matokeo ya wazi ya juhudi za Serikali katika sekta muhimu.

Kwa mujibu wa Dk. Ngasongwa, ambaye pia alishiriki kuandaa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000, kuweka vipaumbele vingi katika bajeti kunatokana na kuwapo kwa mahitaji mengi nchini.

‘‘Najua kwa nini watu wanaamua hivyo. Wanaamua hivyo kwa sababu mahitaji yako mengi. Lakini mahitaji ya binadamu hayawezi yote yakatekelezwa kwa wakati mmoja na ndiyo maana ya msingi wa vipaumbele. Mkishakuwa na vipaumbele zaidi ya vinne mna matatizo, si vipaumbele tena hapo.

Soma zaidi

Uamuzi huu wa Serikali wastahili pongezi

KIKAO cha bajeti cha Bunge la Jamhuri ya Muungano kilianza wiki iliyopita mjini Dodoma. Kwamba safari hii kikao hicho kitachukua mwezi mmoja na wiki tatu tu kumalizika badala ya miezi mitatu, ni kitu cha kufurahisha.

Ni kwa msingi huo tunapenda kuipongeza Serikali yetu na Bunge letu, kwa kuchukua hatua hiyo ya kupunguza siku za kikao cha bajeti; hatua ambayo wananchi wamekuwa wakiisubiri kwa muda mrefu.

Tunatambua kwamba hatua hiyo ni moja ya mikakati ya Serikali ya kupunguza matumizi katika kipindi hiki ambacho uchumi wa dunia umeporomoka. Ni matarajio yetu, hata hivyo, kwamba Serikali itaendelea kuchukua hatua nyingine za kubana matumizi katika sekta nyingine.

Ni matarajio yetu vilevile kwamba kupunguzwa kwa siku za kikao hicho cha bajeti, hakutapunguza umakini wa Bunge letu; na kwamba wabunge wetu hawatatumia hatua hiyo kama kisingizio cha kutojadili vyema bajeti za wizara wakianzia na bajeti yenyewe ya Serikali.

Wiki iliyopita Serikali iliwasilisha bajeti yake ya mwaka wa fedha wa 2009/2010. Ni jukumu la wabunge kuhakikisha bajeti hiyo inaendana na hali ya sasa ya anguko la uchumi wa dunia; kwa maana kwamba kila senti inakwenda tu katika matumizi ambayo ni ya lazima.

Ni wajibu wa wabunge wetu kuisoma kwa makini bajeti hiyo ya Serikali na kuichambua ili wajiridhishe kama kweli inaweza kutuvusha katika kipindi hiki kigumu cha anguko la uchumi wa dunia. Na kama hawaridhiki nayo, basi, ni wajibu wao kuionyesha Serikali mapengo yanayostahili kuzibwa katika bajeti hiyo.

Kwa ufupi, wananchi wanatarajia, safari hii, kuuona umakini wa wabunge wao katika kuijadili bajeti ya Serikali yao kuliko ilivyopata kuwa tangu waingie bungeni miaka minne iliyopita.

Tunatarajia kwamba, kwa mara ya kwanza, wabunge wetu wataweka siasa za vyama pembeni na kujadili kwa umakini bajeti hiyo ambayo, kwa kiasi kikubwa, inaamua mustakabali wa Taifa letu katika kipindi hiki kigumu cha anguko la uchumi wa dunia.

Hatutarajii kuwaona baadhi yao wakisinzia bungeni wakati wa kuwasilishwa bajeti hiyo na wakati wa kujadiliwa. Tunatarajia kuona Bunge lililo hai kweli kweli lililosheheni wabunge wenye hoja nzito za kuisaidia Serikali namna ya kuwavusha Watanzania masikini katika kipindi hiki kigumu cha anguko la uchumi wa dunia. Kila la heri.

Friday, June 12, 2009

Bajeti 2009/2010


Waziri wa fedha na mipango Mh. Mustafa Mkullo akiingia bungeni jana na mkoba wake tayari kusoma bajeti ya mwaka 2009/2010. Bajeti hiyo itaanza kujadiliwa jumatatu.

Serikali imewasilisha bungeni mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha wa 2009/2010. Katika bajeti hiyo ya serikali iliyowasilishwa na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, bungeni mjini hapa jana, maeneo mbalimbali yamefanyiwa marekebisho huku wigo wa kodi ukitanuliwa. Katika mwaka wa fedha wa 2009/2010, matumizi ya serikali yatakuwa Sh trilioni 9.5, matumizi ya kawaida yakiwa Sh trilioni 6.7 na matumizi ya maendeleo ni Sh trilioni 2.8.

Kwa mujibu wa bajeti hiyo, katika matumizi ya maendeleo, kiasi cha Sh trilioni 1.9 zitatokana na fedha za wahisani kupitia miradi pamoja na mifuko ya kisekta na kiasi kilichobaki cha Sh milioni 968,028 zitatokana na mikopo ya ndani na sehemu ya mchango wa wahisani kupitia misaada ya kibajeti.

Kama ilivyotarajiwa bajeti hiyo ya serikali ya mwaka ujao wa fedha, ina mabadiliko makubwa yenye lengo la kutaka kukabiliana na msukosuko wa fedha ulioziathiri nchi nyingi duniani. Bajeti hiyo imezigusa sekta mbalimbali ambapo zipo zilizofutiwa kodi, kupandishiwa au ushuru kurekebishwa.

Katika hatua hiyo, serikali imeamua kupunguza kiwango cha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kutoka asilimia 20 ya mauzo hadi asilimia 18 ili kupunguza makali ya athari za mdororo wa uchumi. Bidhaa zilizopandishiwa ushuru Waziri Mkulo alisema serikali imeamua kurekebisha kwa asilimia 7.5 viwango maalumu kwenye bidhaa zinazotozwa ushuru wa bidhaa isipokuwa zile za mafuta ya petroli.

Alisema marekebisho hayo yamezingatia kiasi cha wastani wa mfumuko wa bei. Viwango vya sasa na vile vinavyopendekezwa ni pamoja na vinywaji baridi ambavyo ushuru unapanda kutoka Sh 54 hadi Sh 58 kwa lita. Ushuru wa bia inayotengenezwa na nafaka ya hapa nchini na ambayo haijaoteshwa, umepanda kutoka Sh 194 hadi Sh 209 kwa lita, huku bia nyingine zote ushuru wake ukipanda kutoka Sh 329 hadi Sh 354 kwa lita.

Mvinyo uliotengenezwa kwa zabibu inayozalishwa nje ya nchi, kwa kiwango kinachozidi asilimia 25, ushuru umepanda kutoka Sh 1,053 hadi Sh 1,132 kwa lita na vinywaji vikali umepanda kutoka Sh 1,561 hadi Sh 1,678 kwa lita.

Serikali pia imerekebisha viwango vya ushuru wa bidhaa kwenye sigara ambapo sigara zisizo na kichungi na zinazotengenezwa kutokana nba tumbaku inayozalishwa hapa nchini umerekebishwa kwa kiwango cha asilimia 75 kutoka Sh 5,348 hadi Sh 5,749 kwa sigara 1,000. Sigara zenye kichungi na zinazotengenezwa kutokana na tumbaku inayozalishwa hapa nchini, umerekebishwa kwa asilimia 75 pia kutoka Sh 12,618 hadi Sh 13,564 kwa sigara 1,000.

Sigara nyingine zenye sifa tofauti na hizo, ushuru wake umerekebishwa kutoka Sh 22,915 hadi kufikia Sh 24,633 kwa sigara 1,000, wakati tumbaku ambayo iko tayari kutengeneza sigara ushuru umerekebishwa kutoka Sh 11,573 hadi Sh 12,441 kwa kilo na ushuru wa Cigar unabaki kuwa asilimia 30.

Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) Kwa upande wa sheria za Kodi ya Ongezeko la Thamani, Mkulo alisema imependekezwa kufanya marekebisho katika sheria ya kodi ya VAT kwa kusamehe VAT kwenye matangi maalumu ya kuhifadhia maziwa na vipipa vya aluminium vya kukusanyia maziwa ili kuhamasisha matumizi yake.

Pia kusamehe kodi ya VAT kwenye huduma za kilimo za kutayarisha mashamba, kulima, kupanda na kuvuna ili kupunguza gharama za uzalishaji kwenye kilimo na kupanua wigo wa msamaha maalumu wa kodi ya VAT kwenye maduka yasiyotoza kodi ya JWTZ. Serikali pia imepunguza wigo wa msamaha maalum wa kodi ya VAT kwa asasi na Mamlaka za maji safi na maji taka nchini ili msamaha huo uhusishe vifaa na huduma zitakazohusika katika ujenzi wa miundombinu ya maji safi na taka pekee.

Imeondoa msamaha wa VAT kwenye huduma za kukodi ndege, kwani huduma hizo hutolewa kibiashara kama huduma za kukodi vyombo vingine vya usafiri na kuondoa msamaha wa VAT kwenye chai na kahawa iliyozalishwa na kusindikwa nchini ili kuleta usawa na mazao mengine yanayosindikwa nchini.

Alisema pia serikali imeamua kutoza kodi ya VAT kwenye muda wa maongezi kwenye simu kwa kutumia bei halisi inayoonyeshwa kwenye vocha badala ya bei nafuu anayotozwa muuzaji wa jumla. Imepunguza pia wigo wa msamaha maalumu wa Kodi ya VAT kwa kampuni za madini, mafuta ya petroli na gesi ili msamaha huo uhusishe shughuli na utafutaji pekee ambao hufanywa na mwekezaji kabla ya kuanza uzalishaji.

Imeondoa msamaha maalumu wa VAT kwa asasi zisizo za kiserikali (NGOs) na kwa mashirika ya dini na kwamba hatua hiyo itahusisha madhehebu yote ya dini ambayo ni Waislamu, Wakristo, Wahindu, Mabohora na mengine na kuwa vifaa vya kiroho na ibada vitaendelea kupata msamaha wa kodi.

Soma zaidi

Thursday, June 11, 2009

Mrejesho wa GDSS; 10th June 2009.

“Ajira Bila Ujira! ”

Maendeleo ya nchi yoyote hutegemea wazalishaji mali. Kuna mahesabu anuai yanayofanywa ili kupata pato halisi la nchi husika. Pato la taifa -GDP- hupimwa kwa nguvu kazi inayolipwa. Katika jamii kuna kundi la wafanyakazi ambao pamoja na kufanya kazi nyingi mchango wao ni mdogo katika pato la taifa. Kwa sababu ajira zao hazina ujira rasmi. Kundi hili ambalo mara nyingi hutunza nguvu kazi ya taifa inayotumika katika kuzalisha, limepewa jina la “uchumi wa matunzo na kazi bila malipo” yaani kwa tafsiri (sio rasmi) “Home Based Care Economy”. Wafanyakazi waliopo katika kundi hili ni wanawake na watoto wa kike na mara nyingi kazi wanazozifanya ni pamoja na; kupika, kufua, kusafisha nyumba, kutafuta maji na kuni, kulima shamba la familia kutunza watoto na wagonjwa n.k.

Hali halisi ya pato la taifa limeweka kipaumbele katika uchumi wa uzalishaji viwandani na madini. Sera mbalimbali za nchi zimeendelea kuwekezwa katika maeneo haya mawili muhimu. Mifano ya baadhi ya sera za taifa zinazowekea mkazo katika hili; zimetajwa kwa uchache ni pamoja na Sera ya nishati; Afya; Maji; Miundombinu; Elimu; na pia bajeti ya nchi.

Sera ya nishati haiweki wazi mikakati ya kuwarahisishia wananchi kupata nishati nafuu na mbadala kwa matumizi ya nyumbani, na kwa sababu wanawake ndio watafutaji wakubwa wa nishati hutumia muda mwingi katika kutafuta nishati hiyo hasa kuni katika maeneo ya vijijini. Pia sera ya matunzo ya wagonjwa nyumbani “Home Based Care Policy” ni nzuri kama ilivyoainishwa, lakini serikali imeshindwa kutenga kiasi cha fedha za kutosha kuwahudumia wagonjwa, hivyo mzigo mkubwa wa kuwalea wagonjwa unarudi kwa wanawake na watoto. Eti wanasema kwa kuwa wao –wanawake na watoto- wanaupendo tangu awali. Sijui kama ni kweli?!

Katika sera ya maji serikali imeshindwa kabisa kusaidia wananchi wake kupata maji safi na salama, badala yake maji yamepelekwa katika viwanda vikubwa na migodi. Wanawake na watoto wa kike ndio wanaotafuta maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani; katika maeneo ya vijijini wanawake hutembea zaidi ya kilomita 20 kwa siku kutafuta maji. Katika kilimo hali ni iyo iyo, wanawake ndio wazalishaji wakubwa wa chakula cha nyumbani na kinachobaki kinauzwa kwa ajili ya kujipatia vijisenti kidogo. Katika elimu pia watoto wa kike wanashindwa kwenda shuleni kutokana na kuzidiwa na mzigo wa kazi za nyumbani na uzalishaji mashambani. Ili mradi katika kila sekta wanawake hawana afadhali!

Katika tafiti za karibuni zilizofanywa na mashirika ya wanaharakati zinazoonyesha wanawake wanatumia muda mwingi zaidi katika ajira zisizo na malipo kuliko wanaume (Takwimu zinaonyesha uwiano wa 24% - 6%). Na katika ajira zisizo na malipo wanaume wanatumia muda mwingi zaidi ya wanawake (uwiano upo 39% -24%). Wanaharakati wa utetezi wa usawa katika jamii wameshafanya chambuzi mbalimbali za sera, bajeti ya nchi, na kutoa machapisho na mafunzo mbalimbali ili kuweza kusambaza dhana hii ya “ajira zisizo na ujira” -ingawa ajira hizo ni muhimu- kwa wananchi walio wengi hasa wa vijijini ambao wanaoathiriwa sana na mfumo huu na kuitisha mjadala wa kitaifa katika kuondoa kabisa hali hii na kuleta usawa ama kuzipa ajira hizi hadhi yake katika mchango wa pato la taifa.

Wanaharakati bado wanauliza; Je, ni mikakati gani itumike katika kuboresha hali hii ikiwemo bajeti pamoja na kuimarisha harakati za ukombozi wa wanawake wa Tanzania?

HOTUBA YA JK WAKATI AKIWAHUTUBIA WANANCHI WA DODOMA, NA WABUNGE KWENYE UKUMBI WA KILIMANI, DODOMA TAREHE 10 JUNI, 2009


Waheshimiwa Wabunge;
Ndugu wananchi;
Nawashukuru kwa dhati wazee wangu, Waheshimiwa Wabunge na wananchi wenzangu wa Dodoma, kwa kuitikia wito wangu wa kuja kukutana na kuzungumza nanyi. Nakushukuru Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na Katibu wa Baraza la Wazee kwa maandalizi mazuri.

Mara kadhaa katika hotuba zangu za siku za nyuma, nimekuwa nikielezea jinsi ambavyo uchumi wa dunia unavyopita katika misukosuko mikubwa na jinsi ambavyo mtikisiko huo unavyoweza kuathiri uchumi wetu pia. Tayari athari zake tumezipata na tunaendelea kuathirika nazo.
Nilifanya uamuzi siku za nyuma wa kuunda kikundi kazi cha
watalaam chini ya uongozi wa Gavana wa Benki Kuu, Profesa Benno Ndulu, kufanya uchambuzi wa hali ilivyo ili kubaini athari tulizopata na kushauri hatua za kunusuru uchumi wetu na kujenga uwezo wa kujihami na kukuza uchumi.

Ndugu Wananchi;
Wenzetu hao wamemaliza kazi yao na taarifa yao imeshajadiliwa na Baraza la Mawaziri na maamuzi kufanywa. Matokeo yake ni kuwepo kwa mkakati wa Kunusuru Uchumi wa Tanzania dhidi ya Msukosuko wa Uchumi wa Duniani. Katika mkakati huo mpango wa utekelezaji wa malengo na hatua mbalimbali za kuchukua zimeanishwa.

Soma zaidi

Raza: Kama fisadi ni fisadi, huo si ubaguzi wa rangi

ALIYEWAHI kuwa mshauri wa masuala ya michezo wa Rais wa Zanzibar Dk. Salmin Amour, Mohamed Raza, amezidi kusikitishwa na mwenendo wa baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi, na hasa suala la kuporomoka kwa maadili, akihoji “iko wapi CCM ya mwaka 1977 iliyotokana na TANU na ASP?”

Raza ambaye wiki iliyopita jijini Dar es Salaam, alimzawadia vifaa vya michezo Mbunge wa Same Mashariki kwa ajili ya shughuli za michezo jimboni kwake baada ya mbunge huyo kutunukiwa Tuzo na Marekani, wiki hii alizungumza na Raia mwema na kueleza masikitiko yake hayo.

“Wizi unatisha serikalini tena ukihusisha baadhi ya viongozi…zamani CCM ilikuwa haitaki mchezo wa namna hiyo na yeyote anayehusika hatua zilichukuliwa hata kama kiongozi anatuhumiwa tu, aliwekwa kwanza nje ya uongozi wa chama na serikali ili kupisha uchunguzi,”

“Lakini leo hii hili halifanyiki ndani ya CCM wapo viongozi watuhumiwa lakini wameachwa hawajasimamishwa, sisemi kwamba wana makosa moja kwa moja lakini kama mtu unatuhumiwa na kama unakipenda chama chako na huna shaka yoyote na huna uroho wa madaraka kwa nini usikae pembeni kupisha uchunguzi?

“Iko wapi CCM ya mwaka 1977 iliyozaliwa baada ya kuunganishwa kwa vyama vyenye uadilifu na uzelando wa TANU na ASP?” alihoji Raza.

Katika jitihada za kumwondoa katika lawama hizo Rais Jakaya Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, Raza aliwatupia lawama wasaidizi wa kiongozi huyo mkuu wa nchi, akiamini kuwa hawezi kufanya mambo yote mazuri kwa nchi peke yake bila mwongozo mzuri na bora kutoka kwa wasaidizi wake.

“Kwanza, Rais ameonyesha utayari mkubwa wa kupiga vita ufisadi na ubadhirifu wa aina yoyote na ndiyo maana leo tunaweza kuzungumza hivi lakini utayari huu wa Rais unaonekana kupingwa kwa chini chini na baadhi ya wasaidizi wake. Kuna hali ya kulindana kuanzia katika chama hadi serikalini na taasisi nyingine.

“Kama chama kingekuwa kinamuunga mkono Rais bila shaka yoyote ni lazima watuhumiwa wengine wenye nyadhifa na ambao bado wako katika chama kama viongozi wangesimamishwa kwanza kupisha uchunguzi na kama watabainika safi warejeshwe huu ndiyo utaratibu bora wa chama bora au serikali bora,” alisema Raza.

“Leo hii utasikia au kuona baadhi ya viongozi wanashindwa kutembea mitaani mchana kwa kuhofia kuzomewa kuwa ni mafisadi…wengine wakitajwa wanajidai kuwa huo ni ubaguzi wa rangi…mimi nasema hakuna ubaguzi wa rangi katika suala la ubadhirifu.”

“Mtu utahukumiwa kwa matendo yako kama ni mwizi utaitwa mwizi na kama ni fisadi utaitwa fisadi hakuna cha ubaguzi wa rangi hapa…tusipotoshe watu. Matendo yenu ndiyo yanayotumiwa na wananchi kuwahukumu,” alisema Raza.

Soma zaidi

Tuesday, June 9, 2009

Utata uhamishaji mabilioni BoT


- Ni Sh bilioni 137 za Tanesco na IPTL
- Gavana Ndullu asema hajajulishwa

TAKRIBAN Sh. bilioni 137.8 zilizohifadhiwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) katika akaunti ya pamoja ya Serikali na kampuni ya kufua umeme ya IPTL, zimeandaliwa mpango wa kuhamishwa kwa utaratibu unaoibua maswali mengi zaidi, Raia Mwema imedokezwa.

Uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kwamba kuna mpango wa kuhamisha fedha hizo kutoka BoT kwenda kwenye akaunti tofauti bila maelezo ya kuridhisha.

Haikuweza kufahamika mara moja fedha hizo zitahamishiwa kwenye akaunti ipi kutokana na nyaraka husika kutobainisha taarifa muhimu kuhusiana na uhamishaji huo.

Mpango huo umekuwapo kutokana na kile kinachoonekana kuwa ni fedha hizo ‘kuzubaa’ BoT baada ya mali za IPTL kuwekwa chini ya mfilisi, ambaye ni Wakala wa Usajili, Vizazi na Vifo (RITA) bila kujumuisha fedha hizo.

Ikiwa mpango wa kuhamisha fedha hizo utafanikishwa kabla ya mwaka 2010, itakuwa ni mtikisiko mwingine mkubwa kutokea ndani ya BoT baada ya ule wa fedha zilizoibwa katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005. Fedha zilizothibitishwa kuibwa EPA mwaka 2005 ni Sh bilioni 133.

Fedha hizo ambazo ziliwekwa kwenye akaunti maalumu (Escrow account) ndani ya BoT hadi kufikia Sh 137, 769, 763, 052.84, zilitokana na malipo yaliyokuwa yalipwe kwa kampuni ya IPTL kutokana na kuliuzia umeme Shirika la Umeme nchini (Tanesco), kabla ya kubainika kuwapo udanganyifu uliofanywa na kampuni hiyo tata kuhusiana na gharama halisi za uwekezaji.

Raia Mwema imefanikiwa kupata mawasiliano ya awali ambayo yanaonyesha kuwapo kwa barua kutoka RITA kwenda kwa Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndullu, kwa lengo la kuomba mfilisi huyo, kwa niaba ya IPTL, apatiwe udhibiti wa fedha hizo.

Barua hiyo, ambayo Raia Mwema imepata nakala yake, ni yenye kumbukumbu namba ADG/OR/IPTL/GEN/009, ya Mei 6, mwaka huu.

Nakala za barua hiyo pia zimepelekwa kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mtendaji Mkuu wa Tanesco.

“…Mfilisi wa IPTL ameamua kutumia mamlaka yake kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa kifungu cha 188 ya sheria za makampuni ili kudhibiti kikamilifu akaunti ya pamoja (Escrow account) ya IPTL Tegeta ambayo ipo BoT,” inasema barua hiyo ambayo pia inaweka bayana kuwa wenye mamlaka ya kutoa fedha hizo katika akaunti hiyo ni watu wawili tu.

Watu hao wawili waliotajwa katika barua hiyo ambayo sahihi zao ndizo zinazoweza kutoa mabilioni hayo ni Theophil Rugonzibwa na Dk. Magesvaran Subramaniam anayetajwa kuwa raia wa kigeni.

Imeelezwa na barua hiyo kwamba watu hao ndio wenye mamlaka ya kutoa maelekezo kwa BoT na kutoa fedha hizo kutoka katika akaunti hiyo ya pamoja, wakimtaka Gavana Ndullu kutekeleza matakwa ya mkataba huo.

Gavana wa Benki Kuu, Profesa Ndullu, ameliambia Raia Mwema kwamba hadi jana Jumanne alikuwa hajapokea maelekezo yoyote kuhusiana na kutolewa kwa fedha hizo akikwepa kufahamu lolote kuhusiana na barua ya RITA.

Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja na Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk. Idrissa Rashidi, hawakuweza kupatikana jana ikielezwa kuwa walikuwa na mikutano muhimu, lakini habari za ndani ya ofisi zao zimethibitisha kufahamu kuwapo kwa mawasiliano ya kutaka kuchukuliwa fedha hizo.

Habari zaidi zinasema kwamba wakati kukiwa na mkakati wa kuhamisha fedha hizo kumekuwapo Azimio la Bunge linalotaka suala hilo kumalizwa haraka nje ya mahakama ili fedha hizo kutumika katika kumaliza madeni ya Tanesco na kuichukua mitambo ya IPTL ili ibadilishwe na kutumia gesi na hivyo kupunguza makali ya bei na uhaba wa umeme nchini.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Zitto Kabwe, ambaye kamati yake ndiyo iliyowasilisha mapendekezo yaliyotoa azimio hilo, alisema “uamuzi wowote utakaofikiwa kuhusiana na IPTL unapaswa kuzingatia azimio la Bunge.”

Kwa mujibu wa kumbukumbu rasmi za Bunge (hansard) azimio ambalo linahusu IPTL lilitolewa Aprili 29, 2000 likiwa na maelezo ya kuitaka Serikali na wadau wengine wa suala hilo kuzingatia zaidi maslahi ya Taifa katika maamuzi yao.

“Suala la IPTL limalizwe kwa haraka nje ya Mahakama ili kuharakisha ubadilishaji wa mtambo huo ili utumie gesi na hivyo kuongeza uzalishaji wa umeme wa megawati 100 ambao unatakiwa hivi sasa ambapo kuna nakisi kubwa ya umeme na hivyo kupelekea mgawo unaoumiza uchumi wa nchi,” inaeleza sehemu ya azimio hilo la Bunge na kuendelea;

Soma Zaidi

Monday, June 8, 2009

Gender and Development Seminar Series.

You are invited to the weekly Gender and Development Seminar Series (GDSS) in which this week, Mary Nsemwa and Marjorie Mbilinyi (TGNP) will give feedback on

Care Economy and Unpaid Labour from a Transformative Feminist Perspective!

Date: 10th June, 2009

Time: 3:00 pm - 5:00 pm

Venue: TGNP Grounds / Adj.NIT

Please confirm your participation through

info@tgnp.org

Come One Come All !!!!!!

Friday, June 5, 2009

Wosia wa Baba wa Taifa


Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere

BABA WA TAIFA AMBAYE ALIKUWA ANAONA MBALI KULIKO INAVYODHANIWA. HII NI NUKUU YAKE WADAU TUCHANGANUE NA KUCHANGIA;

"DOLA LAZIMA ISIMAMIE SHERIA ILI KULINDA HAKI NA KUHIFADHI AMANI. WAJIBU HUU USIPOZINGATIWA, WATAIBUKA MANABII WENYE KUIHUBIRI HAKI KWA KUWAHUKUMU WENGINE. HAMTABAKI SALAMA MKIFIKIA HAPO"

J.K. NYERERE

Waziri Mkulo kitanzini

Wabunge wameitaka serikali ifanye marekebisho makubwa kwenye bajeti ya mwaka ujao kwa maelezo kuwa inategemea zaidi fedha za nje na kuwapo upendeleo kwenye ujenzi wa barabara. Wabunge wa Kamati ya Uchumi na Fedha ambao walikuwa wanajadili mfumo wa mapato na matumizi ya serikali katika mwaka ujao wa fedha, walisema kama bajeti hiyo itaenda bungeni kama ilivyo, kuna uwezekano mkubwa wa kutopita.

Mbunge wa Mvomero, Suleiman Sadiqq (CCM) alisema kama Wizara ya Fedha na Uchumi haitarekebisha bajeti hiyo kwa kuingiza sehemu ya barabara iliyoko jimboni kwake ili ijengwe kwa kiwango cha lami, ataenda kulalamika kwa Rais Jakaya Kikwete.

Barabara hiyo inatokea Kilosa kwenda Dumila na kupitia Mvomero kwenda Handeni hadi Korogwe. “Rais alishaahidi kuwa barabara hii mwaka ujao itajengwa kwa lami, lakini angalia kule ilikotokea Kilosa ambako ni kwako wewe Waziri umeweka lami.

Mlipofika Mvomero mmeruka hadi mkaenda kuanzisha lami Handeni kwa Dk. Kigoda ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati hii hadi Korogwe, hii inamaanisha nini, nasema sitakubali nitaenda kulalamika kwa Rais,” alisema.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), alishangazwa na bajeti hiyo kutotenga fedha kwa barabara za Magharibi badala yake fedha nyingi zimerundikwa kwenye barabara za Mashariki mwa Tanzania.

“Kwa nini Magharibi ambako kuna shughuli nyingi za kiuchumi tunaendelea kuwasahau…angalia Chalinze mnapanua barabara ya lami lakini Kigoma, Rukwa, Tabora hawajui lami inafananaje?” Alisema.

Mbunge wa Viti Maalumu, Devota Likokola (CCM) alishutumu mpango wa serikali wa kupendelea baadhi ya mikoa katika ujenzi wa barabara wakati wakazi wa Mbamba Bay, Mbinga, Tunduru, Mangaka hadi Masasi tangu wazaliwe hawajawahi kuona lami.

“Wananchi wetu wanayaona haya na wanatuhoji, kuna barabara inaenda Iringa kila mwaka inabadilishwa lami, lakini huko kwetu wananchi hawajui lami kwa nini mnataka kuleta matabaka ya maendeleo katika nchi hii?” Alisema na kuongeza kuwa wakati umefika Wizara ya Fedha na Uchumi itenge keki ya taifa kwa kuangalia uwiano wa maeneo.

Mbunge wa Ilemela, Anthony Diallo (CCM), alisema bajeti hiyo kwa sura iliyonayo kama itaenda bungeni itakuwa ya kwanza kukataliwa na wabunge kutokana na kuwa na upendeleo kwenye ujenzi wa barabara.

Soma zaidi

Thursday, June 4, 2009

Mfumo wa bajeti ulenge kukomboa wanyonge

Wiki ijayo serikali itawasilisha bungeni bajeti yake ya mwaka wa fedha wa 2009/2010 ikiwa ni ya nne tangu serikali ya awamu ya nne iingie madarakani Desemba 2005.

Bajeti hii inaiacha awamu hii na bajeti moja tu kukamilisha kipindi chake cha utawala cha miaka mitano ambacho kinahitimishwa Oktoba 2010.

Wakati wananchi wakitarajia kusikia bajeti hiyo kwa matumaini tofauti, tayari makundi mbalimbali ya kijamii yameanza kutoa maoni yao jinsi ambavyo wangependa ijielekeze.

Miongoni mwao ni Mtandao wa Kijinsi (TGNP) ambao jana walitoa maoni yao ambayo pamoja na mambo mengine wametaka serikali izibe matundu katika misamaha ya kodi ambayo imekuwa mingi na kuikosesha mapato mengi.

Kadhalika, wametaka juhudi ziongezwe ili bajeti inufaishe makundi yote katika jamii, ikiwa ni pamoja na kuwepo uwazi katika mipango na matumzi ya rasilimali za taifa kwa faida ya wananchi wote.

Maoni ya TGNP ni sehemu tu ya hisia na matamanio ya wananchi walio wengi ya kutaka kuwepo na bajeti inayolenga kunufaisha jamii kwa ujumla na si kusaidia waliopewa dhamana ya kupanga mipango kwa niaba ya wananchi.

Kwa hali hiyo basi, ni matarajio ya kila mwananchi kwamba serikali ya awamu ya nne inatambua kwamba iliahidi mambo mengi kwa wananchi wakati wa kuomba kura, ingawa yapo mazuri yaliyotekelezwa, lakini bado ahadi nyingi hazijaguswa.

Bajeti hii kama tulivyosema hapo juu ni ya nne ya serikali ya awamu ya nne, kwa maana hiyo sasa wananchi wanataka kuona walau ahadi zao zikitekelezwa kwa kiwango zaidi ya asilimia 70 sasa, kwa sababu muda uliobakia ni mfupi mno.

Hata hivyo, sisi tunatambua kwamba uchumi wa dunia umeyumba katika kipindi cha takribani mwaka mmoja uliopita. Mataifa makubwa na yenye nguvu kama Marekani na mengine ya Ulaya kama Uingereza ambao ni wafadhili wa miradi mingi nchini nayo yameyumba.

Pia tunatambua kuna uwezekano mkubwa kwamba misaada kutoka kwa mataifa hisani itapungua kwa kiwango kikubwa mwaka huu kwa sababu zilizo wazi kabisa; kwa maana hiyo tunaamini nguvu ya kutuvusha kama taifa katika bajeti ya mwaka 2009/2010 ni kwa kuongeza juhudi na mikakati ya kujitegemea.

Miaka nenda rudi kumekuwa na kilio juu ya matumizi bora ya rasilimali zetu kama kwenye uvuvi, uvunaji wa mazao ya misitu, uwindaji wa kitalii na mapato yanayotokana na madini yetu.

Maeneo haya yameanishwa mara nyingi kwamba kama mipango mizuri ikiwekwa na umakini ukawepo katika kuisimamia ni dhahiri Tanzania haitahitaji hata senti moja ya msaada kutoka kwa wafadhili.

Kila Mtanzania ni shahidi kwamba hoja juu za utajiri tulionao katika sekta ya uvuvi ilipokuwa inaelezwa, watu wachache sana walikuwa wanafahamu hadi pale Waziri wa Mifugo na Uvuvi, John Magufuli, alipofanikisha operesheni ya kukamata meli ya uvuvi iliyokuwa inavua bila kibali ikiwa na shehena ya samaki wenye thamani ya Sh. bilioni tatu!

Uvuvi wa namna hiyo umefanyika miaka na miaka, hakuna hatua inayochukuliwa; hali ni hiyo hiyo kwenye uwindaji wa kitalii na uvunaji wa wanayama wetu; kadhalika ndiyo hali katika uchimbaji wa madini yote ya nchi hii kuanzia dhahabu hadi kwenye vito vyote hasa Tanzanite.

Tunapoyakumbuka haya na tukitafakari hali ya kuyumba kwa uchumi wa dunia, na hisia kwamba wafadhili safari hii wataota mbawa, tunaona njia ya kujikomboa sasa ni kuwa makini katika matumizi ya rasilimali zetu.

Ni kwa njia hii tu tutaweza kuwa na bajeti ya maana ya mwaka ujao wa fedha kwa hali hiyo kuipa serikali nguvu ya kutekeleza ahadi ambazo wananchi walipewa mwaka 2005 wakati wa kuomba kura lakini bado hazijatekelezwa.

CHANZO: NIPASHE