Thursday, March 11, 2010

Waomba dawa kwa watoto waathirika vituoni

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeombwa kuvipatia vituo vinavyolea watoto waishio katika mazingira magumu dawa za kurefusha maisha ili viwapatie watoto walioathirika na ambao wamesahaulika na serikali.

Ombi hilo limetolewa jana na Mkurugenzi wa Kituo cha kulea yatima cha Huruma Childrean Trust, Godliver Kugumamu.

Mkurugenzi huyo alikuwa akizungumza wakati wa kupokea misaada mbalimbali kutoka kwa watumishi wanawake wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Manispaa ya Arusha (AUWSA).

Wanawake hao waliotembelea kituoni hapo na kutoa misaada kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani iliyoadhimishwa duniani kote juzi.

Rugumamu alisema vipo vituo vingi ambavyo vinalea watoto walioathirika lakini vimekuwa vikikabiliwa na ukosefu wa dawa hizo kutokana na kutowekwa kwa utaratibu wa kuvipatia dawa hizo.

Alisema imekuwa vigumu kwa vituo hivyo kupatiwa dawa katika vituo maalumu vinavyogawa dawa hizo zikiwemo hospitali kutokana na kutoaminiwa.

Kwa upande mwingine aliwashukuru wafanyakazi hao wanawake wa AUWSA kwa kujitolea kiasi kidogo katika mishahara yao na kuwapatia misaada watoto hao ambao wamekosa misaada baada ya kuwakosa wazazi wao wawili kutokana na majanga mbalimbali.

Kiongozi wa watumishi hao Vick Mgongolwa alisema pamoja na misaada hiyo wataendelea kuhamasisha watumishi wenzao wengine, jamii pamoja na uongozi ili kukisaidia kituo hicho pamoja na kuchukua baadhi ya watoto na kwenda kuishi nao kama mchango wao kwa watoto hao.

Watumishi hao walikabidhi misaada mbalimbali kama vile mchele kilo 50, unga wa ngano kilo 50, sukari kilo 50 mafuta ya kupikia lita 50, sabuni za kufulia katoni 10, kiasi cha Sh 150,000 taslimu kwa ajili ya ununuzi wa kuni pamoja na chakula cha mchana ambacho walikula na watoto hao vyote vikiwa na thamani ya Sh 884,000.

No comments: