Monday, October 21, 2013

TGNP na juhudi za ukombozi wa kijinsia Tanzania






MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) ni taasisi huru inayotoa chachu ya ujenzi wa tapo la harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi nchini Tanzania, barani Afrika na kwingineko duniani.

Mtandao ulianzishwa wakati kuna mabadiliko makubwa ya kiuchumi duniani na nchini Tanzania kati ya miaka ya 1980 na1990.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa TGNP, Usu Mallya, mabadiliko hayo yalitoa msukumo mkubwa wa kuanzishwa kwake na kipindi hiki kilitawaliwa na mikakati ya maendeleo iliyoongozwa na Benki ya Dunia (World Bank) na Taasisi ya Fedha ya Kimataifa (IMF) katika kurekebisha uchumi.

Mallya alisema hayo hivi karibuni katikia Tamasha la 11 la Jinsia 2013 lililofanyika katika viwanja vya TGNP vilivyopo Mabibo Septemba 3 hadi 6, mwaka huu na kusisitiza kuwa malengo makuu ya urekebishaji huu yalikuwa kulegeza masharti ya biashara na kupunguza nafasi ya Serikali katika kusimamia uchumi na rasilimali za taifa.

Mallay alisema malengo mengine “Ni kuweka kipaumbele kwa uwezeshaji wa sekta binafsi ; kuondokana na siasa na itikadi ya ujamaa na kujitegemea na kasumba ya kukumbatia upepari na uliberali mamboleo.”

Anasema, “Mabadiliko haya yalikuwa na taathira nyingi hasi nchini zikiwemo kupunguza wafanyakazi hasa kwenye mashirika ya umma; kukosa uhakika wa ajira kwa wengi wakiwamo wanawake, pamoja na rasilimali za umma zilizojengwa kwa jasho la wengi kuchukuliwa na wachache wengi wakiwa wageni na makampuni makubwa ya kibepari, hivyo kujengeka kwa kasi kwa tabaka na wenye nacho na wasio nacho.”

Mkurugenzi Mtendaji huyo wa TGNP anasema athari nyingine zilikuwa majukumu  ya huduma za kijamii kurudishwa katika ngazi ya familia mzigo ambao umeendelea kubebwa na wanawake kwa kiwango kikubwa hadi sasa.

“Hadi leo kulikuwepo na adhari nyingi zilizowakuta wananchi maskini wakiwemo wanaume na hasa wanawake, athari hizi zilijumuisha kukosekana kwa huduma muhimu kama afya/afya ya uzazi, elimu na mengine kutokana na sera zinazoelekeza kuwa serikali kupunguza nguvu ya kuwekeza kwenye sekta kama afya na elimu tofauti kubwa zimeendelea kujengeka kati ya miji na vijiji, kimikoa, kikanda, kiumri, wenye ulemavu wenye kuishi na VVU/Ukimwi na tofauti nyingine zote.”

MATOKEO YAKE NI NINI?

Mkurugenzi huyo nasema, “Tunaendelea leo kuona athari nyingi hususan katika kuporomoka kwa dhana ya uwajibikaji kwa jamii, ufisadi na rushwa zilizokithiri, kuzorota kwa ufikiaji na ubora wa huduma mbalimbali zikiwemo za maji, elimu, afya na nishati,”
Kadhalika, “Kuongezeka kwa ukatili dhidi ya wanawake na watoto, kukua kwa uchumi bila ajira, na uporaji mkubwa wa ardhi, madini, maji, gesi, na rasilimali nyinginezo.”

Anasema kwa mantiki hii “Kuanzia mwanzo Mtandao ulijengwa katika misingi ya kupambana na mfumo wa uliberali mamboleo (yaani utandawazi wizi) na mfumo dume ambayo ndiyo kiini cha tofauti za kijinsia kati ya wanawake na wanaume na  kusukuma makundi mengi pembezoni.”

Uchunguzi wa makala yaha umebaini kuwa, muktadha huu wa ujenzi wa kitabaka, uliojengeka katika mifumo mingine kandamizi ikiwemo mfumo dume, fursa ya kuanzishwa kwa Mtandao iliyoelekeza wakati wa  maandalizi ya wanawake wa  Tanzania kushiriki , Mkutano wa Beijing mwaka 1995.

Semina tatu za maandalizi ziliongozwa na timu ya wanaharakati. Dhana ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi na mbinu za uraghbishi katika kuibua masuala na wanawake na kuyaainisha katika muktadha wa soko huria na mfumo dume ulitoa hamasa ya kipekee na Madai ya umuhimu wa kuanzishwa kwa taasisi itakayoendeleza kutandaa na kupashana habari kuhusu masuala ya haki za wanawake na usawa wa kijinsia na haki ya jamii nchini.

Ndipo Mtandao wa Jinsia ukaandikishwa rasmi mwaka 1993 kama shirika lisilo la kiserikali lenye   dira ambayo ni kuona jamii ya kitanzania inayojali na kuhakikisha haki za wanawake, usawa wa kijinsia na haki za kijamii.

DHIMA NA DHAMIRA YA TGNP

 Katika mada iliyotolewa kwa ushirikiano na Profesa Marjorie Mbilinyi pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Mary Rusimbi isemayo “MIAKA 20 YA HARAKATI ZA UKOMBOZI WA WANAWAKE NCHINI TANZANIA: TUKO WAPI NA TUNAKWENDA WAPI?”  Mallya anasema, “Mabadiliko tunayotaka katika mifumo kandamizi na sera zake hayawezi kutokana na vitendo vya mtu mmoja wala taasisi au kikundi kimoja pekee, bali tunahitaji kujenga nguvu za pamoja.”

“Kwa kutumia dhana na nadharia ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi katika misingi uraghbishi na UTATU yaani Utambuzi, Uchambuzi, Utatuzi/Utekelezaji, TGNP Mtandao umetoa mchango wa kipekee nchini Tanzania, barani Afrika na kwingineko duniani.”

Mkurugenzi huyo anajivunia mafanikio ya TGNP akisema, “Taasisi hii pia imetukuka katika kuwa na msimamo usiotikisika kuhusu umuhimu wa kubomoa mifumo yote kandamizi ili kufikia maendelo endelevu kwa kizazi cha sasa na vijavyo.”

Anafahamisha akisema, “Msingi wa dhana ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi ni mahusiano ya kijinsia na tabaka, hatutenganishi, bali tunaunga masuala haya kwa maana nia yetu ni kubomoa mifumo ya ubepari na ubeberu na kwa maneno mengine, utandawazi wizi na mfumo dume.”

NAMNA YA KUIBOMOA MIFUMO KANDAMIZI

TGNP inasema, “Dhana ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi inatuongoza jinsi taasisi yetu inavyofanya kazi, mfumo wake wa uongozi shirikishi, mipango yetu ya utafiti shirikishi na wanaharakati wa ngazi ya jamii, jinsi tunavyounganisha utafiti shirikishi na vyombo vya habari ili kuwezesha madai ya wananchi yawafikie wengi pamoja na  viongozi wa serikali za mitaa na serikali kuu.”

Mallya anasema kuwa, mchakato huu ni fursa ya wanajamii kukutana, kutafakari, kutafuta taarifa mbalimbali na kujenga nguvu za pamoja katika kudai haki na fursa sawa kwa rasilimali zote yaani ardhi, madini, gesi, maji, fedha/bajeti, ajira, taarifa pamoja na uwajibikaji wa huduma muhimu za kijamii kama afya, elimu, maji, malezi, malazi, nishati, usafiri na hasa, na kukataa ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

MTANDAO ULIPO SASA
TGNP inasema muktadha wa sasa hauna tofauti kubwa na ule wa miaka 20 iliyopita kwani azma ya awali ya soko huria, upepari na uliberali mamboleo bado uko pale pale. 

“Kilichobadilika ni kuongezeka kwa kasi kwa utekelezaji wa azma hiyo hususan kutokana na mtikisiko wa uchumi duniani hasa kuanzia 2008, kuporomoka kwa mfumo wa fedha na mtikisiko wa mfumo mzima wa ubepari wa kibwanyenye duniani,” anasema Mallya.

Anaongeza, “Matokeo yake ni  zahma mpya za kiuchumi ambapo tunashuhudia  mbinu za wazi na za kikatili zaidi za kutekeleza azma hiyo zikiwemo uporaji wa wazi wa maliasili, ardhi, madini, gesi na maji.”

Kwa mujibu wa TGNP,  kumekuwa na badiliko ya kisera kutoka kwa nchi wahisani  toka mwelekeo walau kidogo wa kushughulikia masuala ya umaskini na kuendeleza uwekezaji na biashara kama msingi mkuu wa kuleta maendeleo, bila kusahau uwekezaji mwingi ni wa makampuni kutaka nchi iwape maeneo yao.”
NINI KIMEFANYIKA?
Mtandao wa Jinsia umetoa mchango mkubwa katika michakato mbalimbali ikiwa na malengo ya kutoa fursa za kuhoji/kutafakari, kujenga nguvu za pamoja katika ngazi ya taifa, kikanda na kimataifa.yanayojitokeza  hapo chini  ni kati ya yale mengi yaliyotekelezwa katika kipindi cha miaka 20 iliyopita.

Kadhalika, Muungano wa Taasis takribani 50 zinazotetea haki za binadamu,demokrasia na maendeleo (Fem Act) katika ngazi ya kitaifa ilianzishwa kama jukwaa lenye mrengo wa harakati za ukombozi wa wanawake linalounganisha mashirika yanayotetea haki za binadamu, harakati za rasilimali, utawala bora na demokrasia, haki za huduma za jamii.

Kutambua nguvu ya kila taasisi na kutoa sauti na kujenga nguvu za pamoja katika masuala mbalimbali ya mstakabali wa Taifa, uongozi, ufisadi, harakati za Sheria ya Makosa ya Kujamiina (SOSPA), iliyoongozwa na TAMWA, na sheria ya Ardhi .

“Mtandao wa Jinsia kutoa mchango katika mapambano mapana mfano ya ardhi na ya kuhakikisha suala la jinsia linapewa kipaumbele katika mchakato mzima; ndivyo hivyo hata katika mchakato wa sasa wa Katiba,” anasema Mallya.
                                                
Katika kipindi hiki TGNP inasema, imeendelea kujitahidi kutoa sauti na msimamo katika kuzungumzia maeneo yenye ukimya ikiwemo mfumo dume na mwingiliano wake na mfumo wa kiliberali mamboleo; pamoja na soko huria; suala la UKIMWI na VVU kuwa ni la rasilimali na jinsia.

“Ndio maana tunatumia fursa mbalimbali kuvunja ukimya kuhusu suala la rushwa ya ngono, tukihusisha masuala ya mifumo ya kugawa rasilimali inayowapa  wachache nafasi zaidi, huku ikipokonya uwezo wa wengi kujipatia ajira endelevu na zenye hadhi wengi kukosa huduma,” Mallya anasema.

Anaongeza, “Hiki ndicho kiini kinachozaa rushwa ya ngono kwa mfano, wanafunzi kutokana na ufinyu wa mabweni ya kutosha wanafunzi hutozwa hela wakati wa kutaka vyumba kwenye vyuo na wanafunzi wa kike kudaiwa rushwa ya ngono.”

Mtandao huo kwa mujibu wa Mallya, unasema lengo hasa ni kudai rushwa ya ngono ili izungumzwe kama sehemu ya mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi nchini Tanzania, uwajibikaji kuhusu rushwa ya ngono hususan kupitia kamati za maadili katika taasisi serikalini, sekta binafsi na nyingine zote ambazo hatuoni zikielekeza nguvu katika suala hili.

“Lingine ni kuanzishwa kwa bajeti ya kijinsia kama nyenzo ya kudai na kuelekeza rasilimali fedha katika kushughulikia haki za wanawake na usawa wa kijinsia. Hii ni nyenzo ya wanaharakati kudai uwajibikaji, kupata taarifa za mapato na matumizi na kufuatilia bajeti katika ngazi ya taifa, sekta na serikali za mitaa.”

KURASIMISHA HARAKATI ZA UKOMBOZI WA WANAWAKE KIMAPINDUZI
Ili kuhakikisha kwa itikadi na dhamira ya TGNP Mtandao inakuwa endelevu, jitihada kubwa zilifanyika tangu mwanzo kurasimisha misingi ya harakati hizi katika Sera, mipango, utaratibu wa utendaji kazi, uwajibikaji wa pamoja na kwa binafsi na zaidi ya yote katika uongozi wa TGNP Mtandao.
KUNA CHANGAMOTO GANI?
Changamoto zilizopo ni pamoja na kuendelea kuzungukwa na muktadha kimfumo, kisera, kisiasa na kuitamaduni unaoendeleza itikadi ya ubabe, kuendeleza kwa kasi kwa nadharia ya uzuri wa soko huria wakati upo msimamo wa kuwawezesha wanyonge na hususan wanawake walioko pembezoni kunufaika zaidi.

Mkurugenzi Mtendaji huyo wa TGNP anasema, “Muktadha huu unaongeza nafasi ya kukua kwa mfumo dume katika ngazi zote na kupunguza fursa za wanaharakati kuleta mabadiliko ya kweli.”

Anasema, “Kwa mfano, kujengeka kwa tabaka, kuwa wabinafsi zaidi kila mmoja akijaribu kujitafutia fursa mwenyewe na familia yake, kushusha maonevu kati ya sisi kwa sisi na kuanza kupigana wenyewe kwa mfano wafugaji na wakulima wadogo wadogo kuchinjana badala ya kutambua adui mkubwa na kutokutumia fursa za kujenga nguvu za pamoja kumkabili adui.”

“Kukosekana kwa ajira endelevu, na kipato cha uhakika na kurudisha majukumu nyumbani kumepelekea hasira na kuendelea kwa ukatili dhidi ya wanawake hususan kutoka kwa waume au wapenzi wao.”

Wednesday, October 2, 2013

TATHMINI YA TAMASHA LA JINSIA 2013

SEMINA ZA JINSIA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (GDSS) 25/09/2013 ILIYOFANYIKA VIWANJA VYA TGNP MTANDAO

MADA:                      Tathmini ya Tamasha la Jinsia 2013
MWEZESHAJI:         Mary Nsemwa kutoka TGNP
WASHIRIKI:             66       (39 Ke/27 Me)

Mchakato:
Mwezeshaji aliwapitisha washiriki kwenye malengo makuu ya Tamasha la Jinsia 2013, na kisha kuwapitisha kwenye kazi za Kamati mbali mbali zilizokuwa zimeundwa zifanye kazi kabla na wakati wa Tamasha, ili kuhakikisha malengo ya Tamasha yanafikiwa.
Kisha, washiriki waligawanyika kwenye vikundi vinne kujadili Kamati nne tofauti kwa kuangalia mambo yafuatayo:
·        Mafanikio makubwa matatu kwa Kamati husika
·        Maeneo ya kuboresha na njia mahsusi tatu za kuboresha
·        Ushiriki wa wana GDSS kwenye Tamasha lijalo uboreshwe vipi.
Kamati za Tamasha la Jinsia 2013 zilizofanyiwa uchambuzi ni:
·        Kamati Kuu
·        Kamati ya Utafutaji Rasilimali na Utawala
·        Kamati ya Ushiriki
·        Kamati ya Habari, Taarifa na Mawasiliano
Kwa ujumla wa Kamati zote nne zilizojadiliwa, mambo yafuatayo yalijitokeza kutoka kwenye vikundi hivi vinne kama mafanikio:
·        Kwa kuingiza Bunge la Wananchi na Mahakama ya Wazi; maudhui ya Tamasha la mwaka huu yalikuwa  tofauti  yenye ubunifu  uliohamasisha ushiriki wa hali ya juu  tofauti na  miaka mingine;
·        Watoa mada za msingi (plenary) walikuwa mahiri, na warsha zilitumia mbinu shirikishi (uraghbishi) zilizofanya ushiriki kuwa mkubwa na mpana.
·        Washiriki wote kupatiwa chakula ilisaidia kutulia  na  bila kupoteza muda kwenda kutafuta chakula.
·        Washiriki wote kushiriki kikamilifu na kuchangia mijadala
·        Vikundi vya sanaa  vilifanya sanaa zenye maudhui  yanayoendana na mada  na  kuibua  mjadala mkubwa.
·        Tamasha lilifanikiwa kutangazwa sana kwenye redio, televisheni, mitandao ya kijamii, magazetini n.k. kabla, wakati na baada ya Tamasha
Maeneo yafuatayo yalitajwa kuhitaji maboresho kwenye matamasha yajayo:
·        Idadi ya warsha ipunguzwe maana inaleta mkanganyiko kwa washiriki na zinapungua ufanisi
·        Muda wa majadiliano ya plenary na kwenye warsha uongezwe
·        Huduma ya chakula  iboreshwe; na washiriki wapakuliwe chakula cha kutosha na maji ya kunywa yatolewe wakati wa chakula
·        Wana GDSS wajulishwe mapema kutokuwepo kwa uwezeshwaji wa nauli ili wajiandae
·        Taarifa za Tamasha zitolewe na kusambazwa miezi mitatu au zaidi kabla
·        Gharama za mauzo ya vikoi, tshirt, begi n.k. zijulikane mapema ili washiriki wajipange mapema kununua.



Ushiriki wa wana GDSS kwenye Tamasha lijalo uboreshwe vipi?:

·        Ratiba itoe nafasi zaidi kwa vikundi vya GDSS  kushiriki kuto mada  na kuonesha sanaa zao
·        Fursa za kujitolea (volunteers) zichukue wana GDSS w wengi zaidi
·        Kazi za maandalizi ya Tamasha kama vile usafi, kupaka rangi, useremala, mama lishe n.k. zitangazwe mapema ili wana GDSS wajipange na kuomba kuzifanya.
Makubaliano kuelekea Tamasha la Jinsia 2015:
·        Kuwe na  maandalizi ya mapema kwa wana GDSS  hususan semina maalum kwa wana GDSS kabla ya Tamasha ili waelewe vizuri mada kuu ya Tamasha, warsha zitakazokuwepo n.k ili ushiriki wao uwe na ufanisi zaidi

·        Tamasha la mwaka 2015, litakuwa mwaka wa Uchaguzi Mkuu Tanzania na huenda tukawa na Katiba mpya tayari, tutumie fursa hizi kuhakikisha linafana zaidi.

MWISHO


TAMKO LA SERIKALI JUU YA SABABU ZA KUYAFUNGIA MAGAZETI

 TAMKO LA SERIKALI KWA KUYAFUNGIA MAGAZETI YA MWANANCHI NA MTANZANIA

Serikali imeyafungia  kutochapishwa Magazeti ya MWANANCHI na MTANZANIA kuanzia 27 Septemba,2013  kutokana na mwenendo wa magazeti hayo kuandika habari na makala  za uchochezi na uhasama kwa nia ya kusababisha wananchi wakose imani kwa vyombo vya dola hivyo kuhatarisha amani na mshikamano ulipo nchini.


Gazeti la MWANANCHI limefungiwa kutochapishwa kwa siku kumi na nne(14) kuanzia 27 Septemba,2013.Adhabu hii imetangazwa kwa Tangazo la Serikali(Government Notice )Namba 333 la tarehe 27 septemba,2013.


Gazeti la MWANANCHI limepewa adhabu hiyo kutokana na hivi karibuni kuchapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na uvunjifu wa amani,mfano tarehe 17 Julai,2013 katika toleo Namba 4774 ilichapisha habari isemayo “MISHAHARA MIPYA SERIKALINI 2013”  kwa kuchapisha waraka uliozuiliwa kwa matumizi ya vyombo vya habari waraka huo ulikuwa wa Siri  haukupaswa kuchapishwa Magazetini.


Aidha, katika toleo la Jumamosi,tarehe 17 Agosti,2013 lilichapisha habari yenye kichwa kisemacho “WAISLAM WASALI CHINI YA ULINZI MKALI”  habari hiyo ilikolezwa na picha ya mbwa  mkali mwenye hasira.Habari na picha hiyo ilitoa tafsiri ya kuwa Jeshi la Polisi lilipeleka Mbwa katika maeneo ya ibada ya waumini wa dini ya kiislam.Jambo ambalo halikuwa la  ukweli.


Jeshi la Polisi katika doria siku hiyo halikupeleka mbwa katika maeneo ya Misikiti.Serikali na jeshi la Polisi linaheshimu na kuzingatia maadili ya dini ya Kiislamu na kwa hiyo Jeshi lake haliwezi kupitisha au kuingiza mbwa katika maeneo ya ibada.

Hivyo basi,kwa gazeti hili kuchapisha habari iliyokolezwa na picha ya mbwa ni uchochezi wa kulichonganisha Jeshi la Polisi na waumini wa dini ya kiislam  mbwa ni najisi hapaswi kuingia  katika maeneo ya ibada.

Gazeti la MTANZANIA limefungiwa kutochapishwa kwa siku tisini(90) kuanzia tarehe 27 Septemba,2013 kwa kuchapisha habari zenye uchochezi.Gazeti hili limeonywa mara nyingi  lirekebishe mtindo wake wa uandishi wa  kichochezi na lizingatie maadili na Sheria na Kanuni za  fani ya Habari.

Pamoja na kuonywa gazeti hili halikuonyesha kuzingatia maelekezo ya Msajili wa Magazeti, mfano ;katika toleo na 7262 la 20 Machi,2013 liliandika habari yenye kichwa kisemacho “URAIS WA DAMU”,tarehe 12 Juni,2013,toleo Namba 7344 lilichapisha makala isemayo “MAPINDUZI HAYAEPUKIKI”.

Aidha, siku ya Jumatano,tarehe 18 Septemba,2013 katika toleo Namba 73414 ukurasa wa mbele lilichapisha Kichwa cha habari kisemacho “SERIKALI YANUKA DAMU” taarifa hiyo ilikolezwa na picha zilizo unganishwa kwa ustadi mkubwa kwa kutumia kompyuta  kutapakaza rangi nyekundu mithili ya damu nyingi kumwagika .Katika habari hiyo gazeti hilo limedai bila uthibitisho kuwa Jeshi la Polisi linahusika  na wahanga waliomizwa na watu wasiojulikana kwa kumwagiwa tindikali na  waliyovamiwa na kujeruhiwa vibaya.

Vile vile gazeti hilo limeishtumu serikali kuwa goigoi katika kushughulikia matukio yenye sura ya kigaidi.

Kwa ujumla wake habari hiyo ni ya kichochezi ina lengo la kuwafanya wananchi wavichukie vyombo vya ulinzi na usalama  wavione kuwa haviwasaidii.

Kutokana na makosa yalitajwa hapo juu serikali imelifungia gazeti la Mtanzania  kutochapishwa kwa muda wa siku tisini(90) kwa Tangazo la Serikali Namba 332(Government Notice No.332) la tarehe 27 septemba,2013,.

Serikali inawataka wamiliki,wahariri na wanahabari kwa ujumla kuwa makini,kuzingatia weledi,miiko na madili yataaluma uandishi wa habari.

Serikali inawataka wamiliki na hasa wahariri kuhakisha kuwa habari wanazoziandika na vipindi wanavyoviandaa vinazingatia taaluma,kuweka mbele maslahi ya taifa letu kwa kuwa na uzalendo wa hali ya juu.

Serikali inavionya vyombo vya habari vinavyoutumia uhuru wa habari bila wajibu kuwa haitasita kuvichukulia hatua kali ikiwemo ya kuvifungia .Serikali haitakubali kuona vyombo vya habari kuwa chanzo cha uvunjifu wa amani  nchini.

Imetolewa na



MKURUGENZI IDARA YA HABARI

WIZARA YA HABARI,VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO

28 SEPTEMBA,2013