Monday, November 30, 2009

`Uagizaji mitambo mipya ni Richmond nyingine`

-Yadaiwa kuna wanaotaka kufukuzia asilimia 10

Mtego mwingine wa kuingiza Serikali katika hasara kubwa ya mabilioni ya fedha unanukia baada ya kudaiwa kuwa maofisa wake wamekataa ushauri wa watalaamu wa masuala ya umeme na kung'ang'ania kuagiza mitambo mikubwa miwili ya kufua umeme kutoka nje ya nchi.

Wataalamu hao waliishauri serikali kuongeza mkataba na iliyokuwa kampuni ya kufua umeme ya Aggreko baada ya kuonekana kufanya kazi nzuri kwa kipindi cha miaka miwili lakini ushauri huo ukapuuzwa.

Baada ya ushari huo kupuuzwa, kampuni ya Aggreko iliamua kung'oa mitambo yake na kuihamisha nchini wiki kadhaa zilizopita.

Mwaka 2006 Serikali iliingia hasara kubwa kwa kuingia mkataba na kampuni hewa ya Richmond LLC ya Marekani, baada ya nchi kukumbwa na ukame uliosababisha kukauka kwa maji katika mabwawa ya kuzalisha umeme.

Hali hiyo ililazimu Serikali kuipa zabuni kampuni hiyo tata kufua umeme wa dharura wa megawati 100 kwa mkataba wa miaka miwili, mradi ulioigharimu takribani Sh. bilioni 200.

Kwa mujibu wa habari za uhakika zilizolifikia gazeti hili, mpango wa kuishauri Serikali ikatae kuongeza mkataba uliandaliwa na watendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

Vyanzo vyetu vimesema kuwa watendaji wa Tanesco waliishauri Serikali ikatae kuongeza mkataba na kutaka iagizwe mitambo mipya bila sababu za msingi.

Habari hizo zilidai kuwa gharama ya kuagiza mitambo hiyo zinafikia dola za Marekani milioni 82 (Sh. 107,281,000,000) mara mbili ya ile ya kampuni ya Aggreko ambayo ilikuwa Dola za Marekani milioni 42 (Sh. 28,782,600,000).

Gharama hizo hazijumuishi zile za mafuta ambayo yatakuwa yanatumika kwa kila mwezi kwa ajili ya uendeshaji.

Mitambo ya Aggreko ilikuwa inatumia mafuta ya Sh. bilioni tisa ambayo ni nusu ya gharama za uendeshaji wa mitambo ya Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).

Katika mkutano wa watalaam wa umeme uliofanyika jijini Dar es Salaam mwaka 2008, waliitahadharisha serikali kuwa kutatokea tatizo la upatikanaji wa umeme nchini na kutaka mikataba ya makampuni binafsi ya kufua umeme yaliyokuwepo yaongezewe mkataba.

Inadaiwa kuwa kampuni ya Aggreko ilitaka iongezewe muda na ilikuwa tayari kufanya kazi na serikali ili kukabiliana na tatizo la umeme linalolisumbua taifa hivi sasa, lakini haikuwezekana.

Kampuni ya Aggreko iliingia mkataba na serikali ili izalishe umeme wa megawati 40 mwaka 2006 ikiwa ni miongoni mwa kampuni tatu za kuzalisha umeme.

Kampuni nyingine ni Dowans, ambayo ilirithi zabuni ya Richmond, baada ya kubainika kuwa ni bandia. Dowans ilikuwa inazalisha megawati 100 kabla mkataba wake kusitishwa rasmi mwaka jana kutokana na mapendekezo ya Bunge.

Kampuni ya tatu iliyoingia mkataba na Tanesco ni Alstom Power Rentals iliyofanyia kazi zake mkoani Mwanza.

Licha ya kuonekana kuwa mitambo ya kampuni ya Aggreko haikuwa na dosari zozote, lakini maofisa wa Tanesco walishinikiza ile yenye matatizo ya Dowans inunuliwe na serikali kwa gharama kubwa.

Imedaiwa kuwa watu waliokuwa wanashinikiza kununuliwa mitambo mipya na kuacha ile ya Aggreko walitarajia kujipatia asilimia 10 kwa njia ya rushwa.

Akizungumzia madai hayo, Msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini, Alyoce Tesha, alithibitisha kuwepo kwa mipango ya kuagiza mitambo hiyo mipya na kwamba zabuni imeshatangazwa.

Tesha alisema Serikali inataka kununua mitambo hiyo ambayo itakuwa na uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 160 ambazo zitaingizwa katika gridi ya taifa.

Tesha aliiambia Nipashe hivi karibuni kuwa watatumia Sheria ya Manunuzi ya Umma (PPRA) ya mwaka 2004 katika kutangaza zabuni hiyo kati ya siku 45 hadi 60.

Alihakikishia Nipashe kuwa hakutakuwa na njia ya mkato katika kuchagua kampuni itakayopewa jukumu la kuagiza mitambo hiyo kutoka nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Tesha, baada ya kupatikana kwa kampuni itakayoshinda zabuni hiyo, itapewa muda wa kuomba kutengenezewa mitambo hiyo kutoka nchi watakayoamua wenyewe

Tesha alisema ni bora nchi kukaa gizani kuliko kujiingiza katika mtego kama ulivyotokea mwaka 2006 baada ya kuipa zabuni kampuni ya kitapeli ya Richmond, ambayo kila siku ilikuwa ikilipwa Sh. milioni 152 hata kama haikuzalisha umeme.

Kashfa ya Richmond ilimlazimisha aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kujiuzulu sambamba na mawaziri wengine wawili walioiongoza Wizara ya Nishati na Madini kwa nyakati tofauti, Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi..

CHANZO: NIPASHE

Maalim Seif atoa ya moyoni

KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Seif Sharrif Hamad, amesema, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar utavunjika kama migogoro ya visiwani haitamalizika.

Kauli hiyo aliisema mwishoni mwa wiki wakati wa Baraza la Idd lililoandaliwa na chama hicho, mjini hapa.

Hamad alisema hatua waliyoichukua yeye na Rais Dk. Amani Abeid Karume, ina lengo la kuondoa migogoro ya Zanzizar ili kuimarisha zaidi Muungano.

Alisema amefurahishwa na hotuba mbalimbali za Rais Karume tangu wafanye mazungumzo rasmi na kumaliza tofauti zao hivi karibuni.

“Mpaka leo (juzi) sijasikia kitu chochote kinachokatisha tamaa kutoka katika kinywa cha Rais Karume katika juhudi mpya za kuunganisha Wazanzibari,” alisema.

“Tumedhamiria kuimarisha amani; hatuna ajenda nyingine yoyote ile iliyojificha.

Watanzania dharauni madai eti mimi na Rais Karume tuna ajenda dhidi ya Muungano. Wazanzibari wote wanaupenda muungano na utadumu,” alisema Hamad na kuendelea kumuomba Rais Jakaya Kikwete kuunga mkono juhudi zao.

Alisema wale wote ambao wana husuda na muungano wa Karume na Hamad ni lazima wadharaulike.

Aliwataka Wazanzibari kusameheana kwa maslahi ya utaifa ili kuwa katika nafasi ya kudai haki zao kirahisi katika Muungano.

Akizungumza katika baraza hilo, Makamu Mwenyekiti wa CUF, Machano Khamis Ali alisema Wazanzibari wote wanatakiwa kuwa na matumaini mema hasa kwa sababu Karume na Hamad wana nia njema.

Machano alitaka kuwapo na umoja miongoni mwa Wazanzibari bila kubaguana.

Wakati huo huo, mmoja wa mashehe wa Zanzibar amesema, ni vyema viongozi wa Zanzibar wakajifunza kutoka kwa rais wa kwanza Mwafrika wa Afrika Kusini, Nelson Mandela aliyewaunganisha wananchi wote wa Afrika Kusini bila kujali rangi wala kabila.

Akihutubia baraza hilo, Shehe Saidi Mwinyi alisema viongozi wengi wa Afrika wangeiga mfano wa kiongozi huyo kungelikuwa na utulivu.

Friday, November 27, 2009

Uzinduzi wa Siku 16 Za Kupinga Ukatili Dhidi ya Wanawake Duniani tarehe 25 na 26 Novemba 2009 - Viwanja vya Mnazi Mmoja na Karimjee.

Wasemavyo Waliohudhuria Katika Uzinduzi wa Siku 16 Za Kupinga Ukatili dhidi ya Wanawake Duniani - Viwanja vya Mnazi Mmoja na Karimjee.


Said Nyanja – GDSS Mabibo.
Mambo yanayozungumziwa katika makongamano kama haya ni yale ni yale, inabidi wanaharakati kuweka mikakati zaidi ya kuweza kuboresha matukio kama haya. Watu waliohudhuria ni wachache na wahusika wakuu -wanawake wanaonyanyaswa- hawapo katika kongamano hili. Hivyo kupelekea ujumbe kuwafikia watu wachache, ambao pia sio wahusika wakuu wa manyanyaso hayo tunayoyapinga! Wanaharakati wanatakiwa wajipange zaidi ili waweze kuwafikia na kuzishirikisha taasisi za mikoani hasa zinazotetea haki za akina mama, pia ni vyema tukafikilia kuwashirikisha wanafunzi na camp -vikundi vya vijana vya mitaani- ili kuweza kufikisha taarifa na ujumbe huu majumbani na mitaani kwa watu wengi zaidi.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Prudenciana Otaro – House of Peace.

Jamii haijafahamu umuhimu wa kushiriki katika matukio kama haya, ipo haja ya kuzishirikisha zaidi jamii na familia. Wanaharakati tuna kazi ya kutoa elimu zaidi, badala ya kuendelea kugawa vipeperushi ambavyo pia ni nadra kwa wanajamii kuvisoma. Ni vyema kama wanajamii wanao hudhuria katika maonyesho kama haya wangepata bahati ya kueleweshwa juu ya kazi za mashirika mbalimbali kabla ya kugawiwa vipeperuhi, ambavyo vingi vimekuwa vimeandikwa katika lugha ya kigeni. Ipo haja ya kuongeza elimu zaidi kwa jamii juu ya siku hizi 16, matangazo mitaani na mashuleni ili wananchi wengi waelewe zaidi juu ya harakati hizi zinazoendelea. Pia ni muhimu sana kwa wanaharakati kuanza kubadilisha mtazimo wao na kuangalia jinsi ya kufanya harakati kama hizi katika mikoa mingine tofauti na sasa ambapo harakati hizi zinafanyika Dar es salaam peke yake na huku watu wenye shida hizi za manyanyaso wapo mikoani zaidi ya hapa mjini. Huku mijini mahudhurio sio mazuri ukilinganisha na shughuli kama hizi zikifanyika mikoani.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Mama Nuru Mtewele na Mama Jona Jonas - WOFATA

Watu wengi hawana taarifa za kitu kama hiki, hata wanaokuja hapa katika mazimisho haya hawajui kwa nini wanakuja katika kitu kama hiki. Pia kwa sisi, wajasiriamali ni kazi ngumu kufika katika maeneo kama haya. Ni vizuri waandaji wakafanya utaratibu kuandaa matukio kama haya maeneo ambayo ni karibu na wananchi ili iwe rahisi kwa wajasiriamali kuwakilisha bidhaa zao. Pia ni vyema siku hii ijulikane kitaifa kama zilivyo siku ya UKIMWI au siku ya akina mama duniani ili iweze kuwa na heshima tofauti na sasa ambapo bado haijapewa hadhi wakati ni siku muhimu sana katika harakati za kuwakomboa akina mama na wajasiriamali kama sisi.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Dickens Mwakibolwa na Isabela Nchimbi – NOLA

Uzinduzi umefanikiwa kwa maana ya kuweza kukusanya watu wengi katika viwanja vya mnazi mmoja, lakini inaonekana watu wengi waliohudhuria walishindwa kutumia fursa zilizopo katika uzinduzi huo. Kwa mfano kwa sisi tunaotoa huduma za kisheria tulitegemea kupata watu wengi wa kuwasaidia katika uzinduzi huu, lakini badala yake tumepata watu watatu tu kwa kutwa nzima na tunaamini wapo watu wengi sana wenye shida ya huduma ya kisheria. Wananchi wengi hawana uelewa juu ya kitu kama hiki. Wanafunzi waliletwa katika maandamano bila kuelimishwa wanakuja kufanya nini, ni vyema wakaelimishwa kabisa mashuleni kabla ya kuja katika shughuli kama hizi ili waweze kutumia fursa watakazokutanazo huku. Pia jana katika uzinduzi makada wa chama cha mapinduzi(CCM) walikuja kwa wingi ambao kwa kweli hawakufahamu umuhimu wa siku hii. Ni vyema kwa wakati ujao wanaharakati wakaangalia aina ya wageni rasmi wa shughuli kama hizi, na kuepukan na wageni wa kisiasa ambao wanakuwa na itifaki nyingi.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Pia Chinyele na Edna Lushaka -LHRC
Uzinduzi umefanikiwa kwa kiasi chake, siku ya kwanza kulikuwa na watu wengi zaidi, hivyo wengi tunatarajia meseji iliweza kuwafikia watu wengi zaidi. Mapungufu yalikuwepo hasa baada ya mgeni rasmi Mh. M Pinda kuchelewa kufika uwanjani na kusababisha wanafunzi na wanaharakati kukaa juani kwa muda mrefu sana jambo ambalo ni hatari hasa kwa wototo wa shule. Pia watu wengi hawafahamu juu ya siku hizi 16 za ukatili dhidi ya wanawake, ama ukatili dhidi ya wanawake una maana gani na ni nini umuhimu wa kutomeza ukatili huu. Upo umuhimu wa kuwafundisha zaidi watoto na wanafunzi kuliko kuwavalisha ma-tshirt. Pia watu walishindwa kutumia fursa za misaada ya kisheria zilizokuwepo katika viwanja vya uzinduzi kwa sababu walishindwa kufahamu kwamba kuna huduma kama hizo katika viwanja hivyo. Wanaharakati tunahitaji kutumia mbinu mbadala kuweza kufikisha ujumbe kwa jamii juu ya siku kama hizi, badala ya kutumia luninga, redio na magazeti peke yake, ni vyema kama tukitumia vitu kama matarumbeta na midundiko ambavyo vinaweza kuwavuta wananchi wengi zaidi na kufikisha ujumbe kwa urahisi na kwa gharama nafuu zaidi.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Immaculata Moria na Joel Swebe -Tawla

Mwamko wa jamii bado ni mdogo sana na bado shughuli kama hizi zinafanyika Dare s salaam pekee wakati watu wengi wenye shida za ukandamizaji wapo mikoani na vijijini, ipo haja kwa wanaharakati kuangalia zaidi maeneo hayo ya vijijini. Ipo haja ya kubadilisha mfumo wa kutangaza shughuli kama hizi, badala ya kutumia vyomba vya habari kam magazeti, redio au luninga ni vyema tukatumia mbinu za maigizo na ngoma za asili kama midundiko na mdumange. Pia ni bora shughuli kama hizi tukazizindulia maeneo ya watu wa chini badala ya viwanja kama hivi vya mnazi mmoja na karimjee ambapo wananchi wa hali ya chini hawawezi kuhudhuria kwa urahisi.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Hadija Zuberi, Kuruthum Rashid, na Fatuma Kandambovu - SIYODE Manzese, Sisi kwa Sisi.

Kwetu sisi, siku hii ni muhimu sana kwa ajili ya kujifunza zaidi juu ya harakati hizi za ukombozi wa wanawake Tanzania, kwani sisi ni wanaharakati wageni na tumeunda kikundi chetu baada ya kuja mara kwa mara pale katika semina za GDSS Mabibo. Tunatarajia tutakachokipata hapa tutakipeleka kwa wenzetu ambao hawajapata bahati ya kuja katika viwanja hivi. Ila wenzetu wengi hawana habari juu ya semina hizi ni vyema waandaaji wakatoa matangazo zaidi hasa maeneo ya kwetu ambapo watu wengi hawasomi magazeti wala kuangalia taarifa za habari mara kwa mara. Sisi wenyewe hatuna uelewa wa kutosha juu ya siku hii, kitu ambacho kinafanya tushindwe kushiriki kikamilifu zadi. Lakini tunashukuru kama tutahudhuria vitu hivi mara kwa mara vinaweza kutufungua akili zetu zaidi na zaidi na kuweza kuwakomboa pia na wenzetu, kwani kwa kweli bado wanawake tunanyanyaswa bila kujua!

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Nuru Lukusasi – Mwanachama wa GDSS

Muda wa siku mbili kwa ajili ya uzinduzi ni mdogo ukilinganisha na matatizo wanayokutana nayo wanawake katika jamii hii. Ni vyema waandaaji wakaangalia jinsi ya kutafuta rasilimali ya kutosha ili waweze kufanya kongamano la muda mrefu zadi, hata wiki moja na wanawake wengi waweze kutoa visa mkasa vyao na kuchangia hoja mbalimbanli na machungu wanayokutana nayo katika jamii kuliko ilivyo sasa, ambapo katika muda wa siku mbili tu uzinduzi unafanyika. Wanawake hawafahamu juu ya taarifa hizi za Karimjee na faida ya kuhudhuria sehemu kama hizi, kwa mfano, mimi mwenyewe nimeambiwa leo kuhusu kufanyika kwa kitu kama hiki. Kama ningefahamu mapema ningeweza kuwachukua na wanawake wenzangu na kuja nao hapa kwa sababu wao ndio wanaofahamu hasa manyanyaso wanayoyapata! Maeneo na shughuli kama hizi ni muhimu kwa wanawake kuhudhuria kwani pamoja na kujifunza mambo mengi pia yanapunguza uoga na kuongeza ujasiri hasa kwa sie wanawake tuliosoma zamani!

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Dai, Chukua Hatua, Pinga Ukatili wa Kijinsia.

Vuguvugu hili jipya la wanawake liungwe mkono!

Na Padri Privatus Karugendo

HARAKATI za ukombozi wa mwanamke zimepiga hatua mpya baada ya wanaharakati wa kupigania haki za wanawake kuamua kuanzisha vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi.

Hatua hii imefikiwa baada ya jitihada za miaka mingi. Tunafahamu mengi yaliyofanyika kwenye Mpango wa Mwanamke katika Maendeleo na ule wa Jinsia na Maendeleo. Pamoja na mambo mengi na mazuri yaliyofanyika kupitia mipango hiyo niliyoitaja hapo juu, wanaharakati wa kupigania haki za wanawake walihisi mapungufu katika mchakato mzima wa kutetea haki za wanawake.

Bado mwanamke anakandamizwa, bado anawekwa pembeni katika uongozi, mfano chama tawala cha CCM uongozi wa juu umeshikiliwa na wanaume; mwenyekiti, makamu wenyeviti na katibu mkuu ni wanaume; uongozi wa kitaifa; rais, makamu wa rais, waziri mkuu, spika n.k. ni wanaume.

Kule vijijini mwanamke analima, anachanja kuni, anapika, anachota maji, analea watoto n.k. Upande mwingine mwanaume anafanya kazi kidogo lakini ndiye anayenufaika zaidi. Baada ya mavumo mwanaume ndiye anayepokea fedha, hasa zile za mazao ya biashara kama vile kahawa, korosho, chai na pamba.

Kuna habari kwamba kule Mbozi wanawake walifikia hatua ya kujinyonga baada ya kuona wanafanyishwa kazi kubwa ya kulima, kuvuna na kutunza kahawa na chai, lakini fedha zinaingia kwenye mifuko ya wanaume.

Mashirika ya kutetea haki za wanawake kama vile TGNP, TAMWA na mengine mengi, yameona kuna haja kubwa ya kuanzisha vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi ili kwenda sambamba na mipango mingine inayoendelea ya kumkomboa mwanamke kama vile Mwanamke katika Maendeleo na Jinsia na Maendeleo.

Inafahamika kwamba kumwelimisha mama ni kuielimisha familia nzima, ni kuielimisha jamii na ni kulielimisha taifa zima. Hivyo ukombozi wa mwanamke kimapinduzi ni kulenga katika kulikomboa taifa letu la Tanzania.

Changamoto iliyo mbele ya wanaharakati wa vuguvugu la Ukombozi wa Mwanamke Kimapinduzi, ni kuliangalia jambo hili kwa upana zaidi. Badala ya kuendesha vuguvugu la Ukombozi wa Mwanamke Kimapinduzi, waendeshe vuguvugu la Ukombozi wa Mwanadamu Kimapinduzi.

Hoja kubwa hapa ikiwa kwamba hata wale wote wanaoendeleza mfumo dume, wale wanaowanyanyasa na kuwatesa wanawake, wale wanaowaweka pembeni wanawake katika mfumo wa uongozi wa taifa letu, wanakuwa hawajakombolewa. Hawa nao wanahitaji ukombozi wa kimapinduzi.

Mwanadamu akikombolewa kimapinduzi ni wazi kutajitokeza usawa katika jamii zetu. Kuweka nguvu kubwa katika kuwakomboa wanawake na kuwaacha wanaume pembeni, ni kulishughulikia tatizo nusunusu na kesho na keshokutwa tutajikuta tukihitaji kubuni mbinu mpya za kuwakomboa wanaume kimapinduzi.

Kama inawezekana sasa hivi (kuendesha ukombozi wa mwanamke na mwanaume) kwa nini yote yaya yasifanyike kwa pamoja? Ingawa kuna ukweli kwamba akikombolewa mwanamke, taifa zima linakombolewa, bado kuna wanaume waliobobea katika mfumo dume; kuna haja ya kuubomoa mfumo huu kwanza ndipo tufuate ule wa kumkomboa mwanamke kwa lengo la kulikomboa taifa lote.

Changamoto nyingine ambayo ni ya hatari zaidi ni kule kuyaangalia mapambano ya ukombozi wa mwanamke kama uhasi ndani ya jamii: Kwamba wale wote wanaopigania haki za wanawake hawako kwenye ndoa; kwamba wanaharakati hawa wanaunga mkono ndoa za jinsia moja, kwamba wanaharakati wanaunga mkono maisha ya dada poa na kaka poa.

Mawazo haya hasi yanalenga kuvuruga jitihada zote zinazofanywa na wanaharakati wa ukombozi wa mwanamke kimapinduzi.

Ni wazi jamii yoyote ile inahitaji familia nzuri na zenye maadili bora. Hili wala halina mjadala. Lakini swali ni je; ni familia gani nzuri na yenye maadili bora?

Familia inayoongozwa na unafiki na kuonekana bora mbele ya macho ya watu wakati ndani ya familia kuna moto - mama anateswa, ananyanyaswa, hana furaha na wala hana hata dakika moja ya kuyafurahi maisha yaliyoumbwa na Mwenyezi Mungu, ndiyo familia bora?

Au ni ile ambayo mwanaume ana haki zote hata na ile haki ya kutafuta virusi vya ukimwi na kuvipandikiza kwa mke wake? Familia bora ni ukimya wa mwanamke? Familia bora ni kubeba msalaba?

Wateja wa kaka poa na dada poa wanatoka wapi? Wateja wa “vibustani” wanatoka wapi? Kama familia zetu zingekuwa bora na zenye maadili mazuri; kaka poa na dada poa wangepata wateja?

Mbona hatuwanyoshei vidole wale wote wanaovuruga maadili na kuyaharibu maisha ya watoto wetu? Mtu asiyekuwa katika ndoa hawezi kuweka misingi ya maadili bora? Kama masista na watawa wanakuwa msitari wa mbele kuweka misingi ya maadili bora, kwa nini akina mama wanaharakati wanyoshewe vidole pamoja na ukweli kwamba ndoa zao zilivurugwa na mfumo dume?

Uamuzi wa kuanzisha vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi, unawapatia nguvu wanaharakati kujitambulisha kama wanaharakati wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi.

Utetezi wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi ni dhana ya kisiasa, hivyo dhana hii inawaweka wanaharakati kwenye msimamo ulio wazi kiitikadi; kwa maneno mengine vuguvugu la ukombozi wa wanawake kimapinduzi kunaliweka suala la ukombozi wa wanawake katika nafasi ya wazi kiitikadi na kisiasa.

Kwa njia hii wanaharakati wanaweza kuhoji uhalali wa mifumo mbalimbali iliyopo ambayo inamkandamiza mwanamke na kuibua nyenzo kwa ajili ya uchambuzi na utendaji ambao ni wa kimageuzi.

Uchambuzi wa kina unaelekezwa kwenye miundo na mfumo dume wa mahusiano ya kijamii ambayo imejengeka kwenye miundo mingine mipana kandamizi na ya kinyonyaji.

Mfumo dume ni mfumo wa mamlaka ya kiume ambao unahalalisha ukandamizaji wa wanawake kupitia taasisi na mifumo ya kisiasa, kijamii, kiuchumi, kisheria, kitamaduni, kidini na hata kijeshi. Mamlaka ya umiliki na udhibiti wa rasilimali na marupurupu na dhawabu nyingine kwa wanaume katika ngazi binafsi na kijamii unatokana na itikadi na mfumo dume uliotawala.

Mfumo dume unatofautiana kulingana na majira na wakati na unabadilika kutokana na tabaka, rangi, jamii/kabila, asili ya mtu, imani/dini na mahusiano yaliyopo katika miundo ya kimataifa ya ubeberu. Pia, kwa hali halisi ya wakati tuliomo, mfumo dume haubadiliki tu kulingana na sababu hizi bali una mahusiano na unachangia katika mahusiano ya kitabaka, rangi, kabila dini na ubeberu wa kimataifa.

Hivyo basi, ili kutoa changamoto stahiki kwa mfumo dume ni budi pia kuichambua mifumo mingine iliyo kandamizi na ya kinyonyaji ambayo mara nyingi hutegemeana.

Hivyo basi jukumu la kiitikadi la wanaharakati wa vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi ni kuielewa mifumo yote kandamizi, na jukumu lao la kisiasa ni kuibomolea mbali mifumo yote kandamizi ukiwemo mfumo dume. Mwelekeo ni kupambana dhidi ya mfumo dume kama mfumo kandamizi na sio dhidi ya wanawake na wanaume kama watu binafsi.

Kwa upande wa Afrika, mapambano ya ukombozi wa wanawake yana uhusiano wa karibu na hali iliyopita ya bara letu, kama vile muktadha wa kabla ya ukoloni, utumwa, ukoloni, mapambano ya ukombozi, ukoloni mambo leo, utandawazi n.k.

Mataifa ya kisasa ya Kiafrika yamejengwa ka kupitia migongo ya wanaharakati wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi ambao walikuwa wanapambana bega kwa bega na wanaume katika ukombozi wa bara hili. Baada ya uhuru mfumo dume ulisimika mizizi na kuwarudisha wanawake jikoni.

Ipo mifano mingi hapa Tanzania, inayoonyesha jinsi wanawake walivyosalitiwa na mfumo dume ulipofika wakati wa kushika madaraka ya kuliongoza taifa letu. Akina Bibi Titi Mohamed na wenzake ni mifano michache.

Hivyo wanaharakati wanaona kwamba wakati huu tunapojaribu kujenga Mataifa mapya ya Kiafrika katika milenia mpya, kuna haja ya kujenga pia utambulisho mpya wa wanawake wa Kiafrika, utambulisho wa kuwa raia huru wasioathiriwa na ukandamizaji wa mifumo ya uonevu na kandamizi.

Wanataka wanawake wawe na haki ya kupata, kumiliki na kudhibiti rasilimali, miili yao na kutumia vema sehemu chanya za utamaduni wao kwa malezi bora nakatika kuleta ukombozi wa kimaendeleo.

Ili vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi lifanikiwe, panahitajika maadili binafsi na maadili ya kitaasisi. Maadili binafsi ni pamoja na wanaharakati wa ukombozi wa mwanamke kimapinduzi wa kiafrika, mmoja mmoja, kudhamiria na kuamini katika msimamo wa usawa wa kijinsia wenye misingi ya ukombozi wa wanawake.

Pia kutambua kwamba haki za binadamu za wanawake hazigawanyiki, hazitenganishwi na zinafungamana na haki za binadamu duniani kote.

Aidha, kujenga mazoea yasiyoruhusu ukatili wa aina yoyote ile na kufikia jamii isiyokuwa na ghasia na kutokomezwa kabisa kwa ukatili wa kijinsia; haki ya wanawake wote kuishi bila kukandamizwa, kubaguliwa wala kunyanyaswa na mfuno dume; Haki ya wanawake wote kuwa na maisha endelevu na ya usawa, na kupata huduma bora za ustawi zikiwemo Afya, Elimu, Maji salama na usafi wa mazingira.

Kingine ni uhuru wa kufanya uchaguzi na mamlaka juu ya masuala ya miili ya wanawake ikiwemo haki ya uzazi, kutoa mimba, utambulisho na utashi wa utambulisho wa aina jinsia na mahusiano kijinsi; kujihusisha katika majadiliano ya masuala ya imani/dini, utamaduni, mila na hasa yale yanayolenga katika kuhalalisha kutawaliwa kwa wanawake kwa kutetea msimamo na mtizamo wa msingi wa haki za wanawake.

Maadili ya kitaasisi ni pamoja na kila taasisi ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi kudhamiria kutetea uadilifu, usawa na uwajibikaji kwa taasisi na mashirika yanayoongozwa na misingi ya ukombozi wa wanawake, kusisitiza na kutambua kuwa taasisi ya ukombozi wa wanawake haimaanishi isiwe ya kitaalamu, yenye ufanisi, nidhamu na yenye misingi ya uwajibikaji.

Mashirika ya wanaharakati wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi wa Kiafrika yawe mfano wa kuigwa miongoni mwa jamii na mashirika ya kiraia, yakihakikisha kuwa raslimali fedha na vitu zilizopatikana kwa kusudi la kuwaendeleza wanawake wa Kiafrika zinatumika kwa kusudi hilo, na sio kwa maslahi binafsi.

Vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi ni chachu mpya katika jamii yetu. Tunawajibika kuliunga mkono vuguvugu hili ili tuweze kujenga jamii yenye usawa na kuheshimu haki za binadamu.


Simu:
0754 633122

Mtikisiko wazuka Baraza la Mawaziri

-Kikwete yaanza kumshinda
-Sasa hata Dk. Shein azoza

SIKU chache tu baada ya kutuma ujumbe kwamba akipita mwakani hatabeba mawaziri wazee, Rais Jakaya Kikwete ameanza kutekeleza azma hiyo kwa kuwatangazia mawaziri wake kwamba amechoshwa nao kwa kuwa hawamsaidii, imefahamika.

Habari ambazo Raia Mwema imepata zinasema kwamba Rais Kikwete na hata wasaidizi wake, Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wamekuwa wakali isivyo kawaida yao katika vikao vyao vya kazi.

Kwa mujibu wa habari hizo, katika kipindi kiasi cha wiki mbili zilizopita, Rais Kikwete amekutana na mawaziri wake mara mbili na katika vikao hivyo amesema waziwazi kwamba mawaziri wake hawamsaidii kama alivyotarajia wakati akiwateua.

"Hakikua kikao cha baraza, lakini alizungumza kwa ukali akiwaambia kwamba alipowateua alikuwa na matumaini makubwa nao kwamba atakuwa amepunguza kwa kiasi kikubwa uzito wa kazi.

"Akawaambia amekuwa akilazimika kufanya mambo mengi ambayo yangeweza kufanywa na mawaziri wake aliowaamini na akawapa dhamana," anaeleza ofisa mmoja wa serikali aliyezungumza na Raia Mwema wiki kwa masharti ya kutotajwa gazetini.

Mtoa habari huyo amesema wiki iliyopita Rais Kikwete alikuwa mkali kwa wasaidizi wake kuliko ilivyopata kutokea tangu aingie madarakani mwishoni mwa mwaka 2005.

Imefahamika kwamba kabla ya kikao cha wiki iliyopita, kilichofanyika nje ya Dar es Salaam, Rais Kikwete aliwaita mawaziri wake ghafla katika hatua ambayo ilizua hofu miongoni mwao wakiamini kwamba huenda alitaka kuvunja Baraza lake.

Habari zaidi zinasema katika kikao cha awali waziri mmoja mwanamke alikwepa kuhudhuria baada ya kupata fununu kwamba Rais Kikwete alikuwa amekerwa na baadhi ya kauli zake za hivi karibuni.

Habari zinaeleza kwamba, hata Dk. Shein ambaye anafahamika ya kuwa mara nyingi hana hulka ya ukali amebadilika, na sasa naye ameanza kuwa mkali waziwazi katika vikao vya utendaji.

"Kuna kikao kimoja ambacho baada ya Rais kumbana waziri mmoja kutokana na kuwasilisha waraka uliokuwa umejaa mapungufu, Makamu naye alizungumza kwa ukali akimtaka waziri huyo kuacha kufanya mambo bila kufuata taratibu," anasema mtoa habari huyo.

Anaongeza: " Katika kikao hicho Rais alimkatiza waziri huyo mara kwa mara akitaka ufafanuzi na wakati mwingine kumlazimisha waziri huyo kubadili baadhi ya mambo ambayo aliona yana makosa mengi katika waraka wake.”

Ukali wa ghafla wa Rais Kikwete, Dk. Shein na Pinda unatajwa kuwa umechochewa na utendaji usioridhisha wa mawaziri wengi unaosababisha viongozi hao wa juu kabisa kulazimika kufanya kazi ya ziada.

Katikati ya habari hizo ni hali kwamba mawaziri wengi wanashindwa kuitetea na kuisimamia Serikali ndani na nje ya Bunge, mbele ya umma na katika shutuma nyingi zinazotajwa kwenye vyombo vya habari.

Anasema mtoa habari huyo: "Rais alieleza wazi kwamba anakerwa na taarifa za mara kwa mara katika vyombo vya habari zikionyesha udhaifu mkubwa wa Serikali yake huku wasaidizi wake wakiwamo mawaziri wakishindwa kutoa hoja zenye nguvu au mkakati mahususi wa kukabiliana na taarifa hizo.”

Japo tathmini inaonyesha kwamba si rahisi katika muda mfupi uliobaki kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu kuwa na mabadiliko katika Baraza la Mawaziri, Raia Mwema imearifiwa ya kuwa tayari mchakato umeanza ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa wa kuchunguza mienendo ya watu wakiwemo wajumbe wa sasa wa Baraza la Mawaziri na wajumbe watarajiwa ikibidi kufanyika kwa mabadiliko.

Habari zaidi zinaeleza kwamba yamekuwapo mapendekezo kwa Rais Kikwete ya kutaka abadili baadhi ya mawaziri waliopo kwa baadhi ya wabunge ambao wamekuwa wakitajwa kuwa wako msitari wa mbele katika inayotajwa kuwa ni vita ya ufisadi katika hatua ya kukisafisha Chama cha Mapinduzi (CCM) katika tuhuma za ufisadi na migawanyiko ya dhahiri ili kuvutia kura katika uchaguzi wa mwakani.

Mbali ya kuingiza sura mpya na kupunguza baadhi ya mawaziri, kuna taarifa kuwa yapo mapendekezo kwa Rais ya uwezekano wa kupandisha ngazi naibu mawaziri walioonyesha uwezo mkubwa.

Haya yakiendelea zimekuwapo taarifa za wizara mbalimbali ambako wafanyakazi wanawalalalimikia mawaziri wao kwa utendaji kazi usioridhisha.

Kati ya waliotajwa na wafanyakazi hao ni pamoja na Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, John Chiligati; Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na Naibu wake, Dk. Makongoro Mahanga; Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Sophia Simba.

Lakini akizungumza na Raia Mwema wiki iliyopita Chiligati alisema “hawezi kufanya mtihani na kujisahihishia mwenyewe.”

“Hayo maoni ya watu siwezi kuyaingilia, mimi siwezi kufanya mtihani na kujisahihisha mwenyewe lakini naamini watendaji ofisi wanajua naingia ofisini saa ngapi na natoka saa ngapi,” alisema Chiligati na alipoulizwa kuhusu shughuli za chama kuingilia majukumu ya serikali, alisisitiza kutotaka kujisahihishia mtihani.

Katikati ya mwezi huu akizungumza na vijana wa kutoka nchi mbalimbali za Afrika mjini Dar es Salaam, Rais Kikwete alituma salamu za mwanzo kwa wateule wake kwa kuwaambia vijana hao ya kuwa endapo atajaliwa kuongoza tena Tanzania mwakani, atafanya jitihada kubwa kuondokana na sura za wazee ambao atawabadilisha na vijana.

Akizungumza katika mkutano wa vijana hao wa kulea viongozi wa Afrika, Rais Kikwete alisema atafanya mabadiliko makubwa kwenye Serikali yake akshinda uchaguzi ujao.

Alisema Kikwete: “Wale viongozi wa rika langu, lazima waanze kuwaachia nafasi vijana. Tunahitaji wakuu wa wilaya vijana zaidi, wakuu wa mikoa vijana zaidi na hata mawaziri vijana zaidi. Ndivyo ilivyotokea kwetu sisi wakati tukiwa vijana.”

Thursday, November 26, 2009

'Mahari zinasababisha wanawake wanyanyaswe' - Pinda

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema, mahari ni jambo zuri lakini zinasababisha wanawake wanyanyaswe kijinsia.

Waziri Mkuu amesema, watanzania wanapaswa kutafuta namna ya kuacha utaratibu wa kulipa mahari ili wanawake wasinyanyaswe.

Pinda amesema, zinahitajika juhudi za kulitazama suala hilo taratibu na kwa makini sanjari na kuanzisha vilabu katika shule za msingi na sekondari ili kutoa elimu kuhusu vitendo hivyo kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Waziri Mkuu ametoa changamoto hiyo, Dar es Salaam, wakati wa ufunguzi wa siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia, kwa kutumia Kauli mbiu isemayo ‘Siko peke yangu mwenye nia binafsi , uthubutu, na utayari wa kuzuia na kupambana na ukatili wa kijinsia’

Amewataka Maofisa Maendeleo wa jamii kuwasaidia wanafunzi kuanzisha vilabu hivyo kwa kuwa ni kuna umuhimu wa kulielimisha kundi hilo ili jamii inufaike.

Pinda amesema, Serikali itaendelea kupambana na mila , desturi na imani zozote zenye madhara kwa jamii ikiwemo mila ya kukeketa, na mauaji ya Abino.

Amesema, Serikali itahakikisha kuwa utaratibu uliowekwa kisheria ,Kiutawala,kimila na kijadi vinalenga kulinda haki , utu na heshima ya wananchi.

“Kuwepo kwa vipengele vya kisheria na kiutawala vinavyokataza ukatili wa kijinsia hakutakidhi haja endapo jamii hatutakuwa tayari kupiga vita imani, mila, desturi, tabia na mienendo inayosababisha kuwapo kwa vitendo hivyo” amesema Pinda.

Wednesday, November 25, 2009

Amuua kwa sumu mtoto wa 'mtalaka'

POLISI wamemkamata kijana mkazi wa Kijiji cha Ufala, Kata ya Kilago wilayani Kahama mkoani Shinyanga, akituhumiwa kumuua mtoto kwa kumnywesha dawa ya kuua wadudu wanaoshambulia zao la pamba.

Inadaiwa kuwa, kijana huyo, Juma John (19),alifanya hivyo baada mama mzazi wa mtoto huyo, Limi Midone, kukataa kufanya nae mapenzi, walikuwa na uhusiano wa kimapenzi zamani.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Daudi Sias, amesema, mtoto huyo, Coletha Simoni (3) alinyeshwa sumu jana saa mbili usiku katika kijiji cha Tulole.

Kwa mujibu wa kamanda Sias, kabla ya kumnyesha sumu mtoto, John alikuwa na ugomvi na mama wa mtoto huyo, unaosadikiwa kuwa ni ulisababishwa na wivu wa mapenzi.

Sias amesema, siku ya tukio, mtuhumiwa huyo na rafiki yake, Maganga Tanganyika,walitoka katika Kijiji cha Ufala na kwenda Kijiji cha Tulole, walipofika wakakaa baa iliyopo jirani na makazi ya mpenzi wake wa zamani.

Kwa mujibu wa polisi,John alimuacha rafiki yake hapo baa,akaenda nyumbani kwa Limi, hakumkuta, alimkuta mtoto huyo, akamnywesha dawa hiyo ya kuua wadudu.

Sias amesema, baada ya kumnywesha dawa hiyo, aliondoka na kurudi baa ili yeye na rafiki yake waondoke kurudi kijijini kwao Ufala usiku ule ule ili watu wasifahamu kilichofanyika.

Polisi wamesema, baada ya mama wa mtoto huyo kurudi nyumbani, Coletha alilalamika tumbo linamuuma, aliaga dunia wakati anapelekwa katika kituo cha afya.

Baada ya mtoto kufariki dunia wanakijiji wa Tulole walipiga simu kwa wenzao wa Kijiji cha Ufala kuwaeleza kuhusu tukio hilo, msako ulifanywa usiku huo huo, mtuhumiwa alikamatwa akiwa ana harufu ya dawa ya kuulia wadudu wa pamba katika nguo zake.

John amekiri polisi kuwa ni kweli alimnywesha Coletha dawa ya kuua wadudu wanaoshambulia pamba, mchakato wa kumpandisha kizimbani unaendelea.

Jiji lanusa mchezo mchafu stendi ya Ubungo

MAPATO katika Kituo cha Mabasi yaendayo Mikoani cha Ubungo (UBT), yameongezeka kutoka sh milioni moja kwa siku hadi sh milioni nne.

Wakati Kampuni ya Smart Holdings ilipokuwa ikikusanya mapato kituoni hapo ilidaiwa kuwa ilikuwa inakusanya sh milioni moja kwa siku, lakini baada ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kuchukua jukumu hilo sasa zinapatikana sh milioni nne kwa siku.

Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji, Ahmed Mwilima, alitoa taarifa hiyo jana katika Baraza la Madiwani la Jiji na kusema kutokana na ongezeko hilo, inaonesha kulikuwa na mizengwe katika taarifa zilizokuwa zikitolewa awali kuhusu mradi huo.

Mwilima ambaye alikuwa akizungumzia juu ya mapato yatokanayo na mradi huo wa ukusanyaji mapato UBT, alisema halmashauri imegundua kuwa mapato yaliyokuwa yakidaiwa kukusanywa awali yalikuwa ni kidogo.

Alisema halmashauri haijaamua imkabidhi nani mradi huo kwa kuwa wanaendelea kufanya uchunguzi wa utendaji wake na vielelezo vyote muhimu kwa ujumla ili kuepuka utata kama uliotokea awali.

“Suala hili ni nyeti, linahitaji umakini wa hali ya juu katika kulitekeleza na kabla ya kukabidhi mradi huu kwa yeyote. Ni vizuri halmashauri iendelee kuuendesha kwa sasa ili kujua uhalisia wa makusanyo yake na utendaji wake ili kabla ya kukabidhi au kutafuta mkusanyaji mwingine, halmashauri iwe tayari na maelezo yote muhimu yanayotakiwa kuhusu mradi huo ili kuepuka mtafaruku mwingine kama wa awali,” alisema Mwilima.

Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ilianza kazi ya kukusanya mapato katika kituo hicho Novemba mosi mwaka huu kutokana na kumalizika kwa mkataba wa Kampuni ya Smart Holdings inayomilikwa na familia ya mwanasiasa mkongwe na Mbunge wa Kuteuliwa, Kingunge Ngombale-Mwiru.

Wakati wa usimamizi wa kampuni hiyo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliwahi kutembelea kituoni hapo na kubaini kuwepo kasoro katika ukusanyaji wa mapato.

Alimwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua mapato na matumizi ya makusanyo katika kituo hicho pamoja na Soko Kuu la Kariakoo.

Tayari CAG ametoa ripoti zake na kumkabidhi Waziri Mkuu ambaye wataalamu wake wanaendelea kuzifanyia kazi.

Bodi ya BOT yazidi kukaangwa kesi ya Liyumba

SHAHIDI wa tano katika kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala Benki Kuu Tanzania (BOT), Amatus Liyumba, amedai kuwa Bodi ya Wakurugenzi ya benki hiyo ilikuwa ikijadili katika vikao vya dharura mradi wa ujenzi wa majengo pacha ya benki yaliyopo Dar es Salaam.

Liyumba anadaiwa kutumia madaraka vibaya na kuisababishia Serikali hasara ya Sh Bilioni 200. Kwa mujibu wa shahidi huyo wa Serikali, Dk.Natu Mwamba (48), bodi hiyo haikuwahi kujadili mradi huo katika vikao vya kawaida vya bodi.

Mjumbe huyo wa bodi ya BOT na Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwa, mradi huo ulikuwa ukijadiliwa katika vikao vya dharura na si vya kawaida vinavyofanyika kila baada ya miezi mitatu.

Dk Mwamba ameieleza mahakama kuwa, hata kama katika ajenda za siku hiyo katika mikutano ya kawaida kulikuwa na suala la mradi huo, liliwekwa la mwisho na baada ya ajenda zote kwisha wajumbe ambao hawakuwa wakihusika na mradi walitakiwa kuondoka.

Alipoulizwa kama wajumbe hawakuona ni ajabu kwa nini iwe hivyo, alisema, mwenyekiti wa vikao hivyo ambaye ni Gavana wa BOT ndiye aliyekuwa akiamuru iwe hivyo.

Dk. Mwamba alidai kuwa, mabilioni hayo ya benki yanayodaiwa kuisababishia Serikali hasara yalikuwa yakitumika kwa ridhaa ya Gavana kwa kuwa ndiye mtendaji mkuu.

Amesema mahakamani kuwa,vikao hivyo vya bodi vilikuwa vikiandaliwa na BoT,wajumbe waliitwa katika mikutano ili kuidhinisha malipo, na kwamba, jambo halikuwa sahihi.

Alipoulizwa kwa nini wajumbe wa bodi hawakujiuzulu walipobaini utaratibu unakiukwa alisema,walilifikiria hilo ingawa hakufafanua ni kwa nini hawakufanya hivyo.

Amedai kuwa,walimtumia mjumbe mmoja kuwasilisha malalamiko kwa Waziri wa Fedha wa wakati huo, Basil Mramba, kuhusu matumizi mabaya ya fedha.

Katika mahojiano na mawakili wa mshitakiwa Dk. Mwamba amedai kuwa wajumbe wa bodi hiyo iliwabidi waidhinishe malipo hayo ya mabilioni kuhofia kuvunjwa kwa mkataba jambo ambalo lingesababisha Serikali ishitakiwe.

Hata hivyo amedai kuwa, hana kumbukumbu kamili kuwa ni Shilingi ngapi kwa sababu karatasi za taarifa ya mradi huo zilikuwa zikisomwa na kuachwa pale pale.

Amesema, kwa mujibu wa utaratibu ilitakiwa kuwa kabla matumizi hayajafanyika bodi ipitie na kutoa idhini ndipo jambo lianze kufanyika, na kwamba utaratibu ulikiukwa.

Dk Mwamba amesema, fedha zilitumika, na kisha bodi ya BOT iliombwa ridhaa ya malipo maada ya matumizi.

Amesema, aliyekuwa akiwasilisha taarifa hiyo alikuwa msimamizi wa mradi huo kwa niaba ya kurugenzi ya utumishi na utawala baada ya kupata idhini ya mwenyekiti wa kikao, taarifa ambayo ni ya menejimenti kuja kwenye bodi.

Monday, November 23, 2009

‘Maslahi binafsi yanachochea mgogoro Loliondo’

UONGOZI wa Kampuni ya Ortello Business Corporation (OBC), umesema, maslahi binafsi yakiwemo ya wanasiasa na baadhi ya watendaji serikalini, ndiyo chanzo cha mgogoro unaoendelea katika eneo tengefu la ardhi la Loliondo wilayani Ngorongoro ambako kampuni hiyo imepewa kibali cha kuwinda.

Mkurugenzi wa OBC Tanzania, Isaac Mollel, amesema, maslahi hayo binafsi yanachangia kuwepo kwa mgogoro huo, lakini kama sheria zikifuatwa, hakutakuwa na mgogoro katika eneo hilo ambalo Ortello imekuwa ikiendesha shughuli zake kwa kibali cha serikali tangu mwaka 1993.

Mollel alihoji ni kwa nini mgogoro katika kitalu hicho hutokea kila wakati serikali inapotaka kugawa vitalu na kila watanzania wakijiandaa kwa Uchaguzi Mkuu, akitolea mfano wa mwaka 1993 na sasa miezi kadhaa kabla ya uchaguzi wa mwakani.

"Hili suala lina maslahi binafsi. Kwa nini linajitokeza kila tunapoelekea Uchaguzi Mkuu na ugawaji wa vitalu vipya? Mwaka 1993 ilikuwa vivyo hivyo, ingawa na mwaka huu kuna suala pia la ukame. Lakini pia msije kuidharau issue (suala) la ardhi kwa nchi za Afrika Mashariki,” alieleza Mollel.

Alisema,kwa kuwa Kenya ardhi ni tatizo, wapo baadhi ya watu kutoka nchi hiyo ambao wengi ni wa jamii ya wafugaji wa Kimasai, wameingia Loliondo na kuchukua ardhi, na kusababisha mtafaruku kwa jamii ya wenyeji.

Akifafanua zaidi suala la maslahi, alisema mgogoro huo pia ni baina ya Wazungu na Waarabu, akihoji kuwa kama kuna vitalu zaidi ya 100 nchini, kwa nini kitalu kimoja cha OBC tu kinachomilikiwa na Mfalme wa Dubai, Shehe Mohamed Rashid bin Maktoum kiwe na matatizo na siyo vingine.

“Suala ni la maslahi, kwa sababu hiki kitalu ni cha kipekee, kinapata wanyama wa aina zote, wanaenda na wanarudi. Sasa kuna watu wamevamia pale, hawana kibali chochote, sijui kama wanalipa fedha wapi, lakini wapo ndani ya eneo la OBC ambayo inalipia kila kitu serikalini na hawajachukuliwa hatua.

“Ndio maana tunahoji, inawezekanaje mtu akavamia eneo la mwenzake, akaachwa tu. Humuulizi, unachouliza wewe ni hela tu, na sijui kama hela hiyo inakwenda serikalini. Ziko kampuni zaidi ya kumi zinafanya kazi ndani ya kitalu chetu, lakini serikali imekaa kimya,” alihoji Mkurugenzi wa OBC.

Alisema kampuni hiyo inaamini kuwa kama sheria zikifuatwa, Loliondo hakuna tatizo wala mkanganyiko wa sheria kama inavyodaiwa na baadhi ya watu wakiwemo wanasiasa na mashirika yasiyo ya kiserikali, hasa kwa sababu eneo hilo la OBC ni ardhi ya uhifadhi na wanafanya hivyo kwa mujibu wa sheria.

Alisema wao wako tayari kubaki na eneo la hekta za mraba 1,200 kati ya 4,600 za Loliondo, hasa baada ya kuipa Serikali ya Mkoa wa Arusha, Sh milioni 156 kwa ajili ya kupima eneo hilo kwa matumizi ya wakazi wake.

Kauli ya Mollel imekuja wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira leo inaanza kazi yake ya kufanya tathmini ya hali halisi huko Loliondo kutokana na kuwepo kwa madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu baada ya wananchi waliovamia kitalu cha OBC kuondolewa kwa nguvu na Serikali ya Mkoa.

Karume anguruma

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Amani Abeid Karume ameeleza kwa undani yaliyojiri katika mkutano kati yake na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad na kumtaja kiongozi huyo wa CUF kuwa ni jasiri kutokana na uamuzi wake wa kwenda kuwatangazia wafuasi wake kwamba anamtambua kuwa ni Rais.

Rais Karume alisema hayo jana katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa lengo la kuelezea mazungumzo hayo ya kisiasa yaliyofikiwa. Mkutano huo uliofanyika Unguja, ulihudhuriwa na umati mkubwa wa wananchi.

Alisema Maalim Seif alimtumia salamu za kumuomba wakutane. “Nikamkaribisha nikasema njoo bwana tena tukazungumza sana.Kuna baadhi wakasema sijui nilimpa chai ya maziwa. Maneno yale siyo ya kweli,” alisema Karume na kufafanua kwamba kila mmoja alikunywa glasi moja ya maji, hali iliyosababisha kelele za kushangilia kutoka kwa mamia ya watu waliojitokeza katika mkutano huo.

Kwa mujibu wa Karume, Katibu Mkuu huyo wa CUF alimwambia kwamba chama chake kimeyaona maendeleo na akasema kama wakishirikiana, wataleta maendeleo zaidi.

Aliueleza umati huo kuwa Maalim Seif alisema, “sisi CUF tumewakosa, nanyi mmetukosa. Imefika wakati tusameheane. Tusahau yaliyopita, tugange yajayo. Hayo ndiyo maneno tuliyozungumza,” alisema Rais Karume.

Alisema kutokana na kauli ya kiongozi huyo wa CUF, alizingatia ubinadamu kwamba hata kama mtu amekosana na mwingine kwa miaka 100, mmoja akienda na kuomba kusamehewa, lazima anayeambiwa aseme yameisha.

Alisema baada ya mazungumzo hayo, Hamad alimwambia Rais Karume amuombee dua wakati akienda kuwaeleza wanachama juu ya tamko la Baraza Kuu la CUF la kumtambua rasmi.

“Akasema niombee dua, nami nikasema nakuombea kila siku,” alisema Karume na kuendelea kushangiliwa.

Karume ambaye kila mara hotuba yake ilikatishwa na vigelegele na sauti za kushangilia, alisema, “kwa niaba yenu wote na wapenzi wa CCM, nataka nimpongeze saana, mheshimiwa Seif kwa ujasiri wake. Maana halikuwa jambo rahisi kama hivi kuzungumza na watu wake ambao siku zote walishaelekezwa hivyo.” Aliendelea kusisitiza, “alikuwa jabali na jasiri. Si jambo jepesi. Kiongozi ye yote wa siasa lazima afike pahala aseme njia hii haifai.”

Rais Karume ambaye alisisitiza anawapenda wapinzani na kuwaona kama vile ni askari Polisi, alisema kitendo hicho kilichofanywa na CUF na CCM kisiwani humo, kitaleta mustakabali mpya katika siasa. Alisema upinzani si ugomvi na wala vita.

“Nawapenda sana hawa wapinzani. Ni kama askari Polisi. Kazi moja kubwa ya wapinzani ni kuwachunga walio madarakani wasipoteze njia. Ndo maana napenda wawepo watuongoze ongoze,” alisema na kusisitiza kwamba anaamini kwamba sasa amani ya kudumu imefika Zanzibar.

Alisema matokeo ya mazungumzo hayo, ni mafanikio ya vyama vyote na Watanzania kwa ujumla na wala hakuna mshindi katika hilo. “Huu si uchaguzi. Ushindi unapatikana kwenye uchaguzi. Amani na utulivu ni wa sisi sote,” aliongeza Rais Karume.

Wakati huohuo, Rais alisema baada ya mazungumzo hayo, wapo waliosema lipo jambo lingine lililozungumzwa. Bila kutaja jambo hilo, alihoji, “jipi lingine tuzungumze jamani? Hili la amani na utulivu ni dogo?” Ingawa hakuweka wazi, miongoni mwa mambo ambayo baadhi ya watu walikuwa wakihisi kwamba huenda yamezungumzwa ni suala zima la uundwaji wa Serikali ya Mseto (ya pamoja).

Karume alisema, “suala la amani tumehangaika nalo miaka mingapi? Wale wanaobeza ebu tuachieni. Kama kuna jambo jingine, milango iko wazi tutazungumza. Kama kuna lingine lenye mustakabali wa nchi, tutazungumza. Kila jambo lina wakati wake, waamuzi wake na mazingira yake. Wananchi wa Zanzibar msidanganyike waamuzi ni nyie wenyewe.”

Alisema Zanzibar wana utaratibu wao waliojiwekea. Alisema wakubwa wanaweza kupanga, lakini hatimaye uamuzi unatakiwa ufanywe na wananchi. “Naamini jambo lolote zuri la mustakabali hamtakataa, lakini msilazimishwe.”

Friday, November 20, 2009

Mrejesho wa GDSS: Mjadala juu ya Uchimbaji wa Madini Unaendelea.

Katika mfululizo wa semina za GDSS wiki hii ya tarehe 18.11.2009, mjadala juu ya uchimbaji wa madini uliendelea na muwasilishaji mkuu wa mada alikuwa ni mchungaji Magafu kutoka Chama cha Wachungaji Tanzania, ambaye aliwasilisha mada yake kwa kutumia video juu ya mgogoro wa mgodi wa North Mara unaomilikiwa na Barick. Katika mgogoro huo, madini ya sumu aina ya Sodium Cyanide yanayotumiwa kuchimbia dhahabu yalitiririka kutoka katika mgodi huo wa North Mara na kuingia katika mto Tegete, na kusababisha madhara makubwa kwa wananchi, wanyama, na mazingira ya maeneo hayo. Wananchi wa maeneo hayo wanatumia maji ya mto huo kwa shughuli zao za kila siku, pamoja na mifugo yao. Wananchi wengi wamedhurika na mifugo kadhaa imeshakufa mpaka sasa, na mimea imikauka kabisa.

Washiriki wa semina baada ya kuangalia video hiyo, waliweza kuchangia na kutoa maazimio kadhaa ambayo walipendekeza yafanyiwe kazi na wanaharakati kutokana na madhara yaliyopatikana katika mgodi huo. Hapa chini ni baadhi ya michango na mapendekezo ya wanaharakati kutokana na mgogoro huo.

• Ipo haja kwa mawaziri wahusika –waziri wa usalama wa raia, waziri wa madini, na waziri wa mazingira– kuchukuliwa hatua kwa sababu ingawa walikuwa wanafahamu juu ya uchafuzi huu wa mazingira lakini hawakuchukua hatua yoyote na kuwaacha wananchi kupata matatizo yanayoendelea. Hata baada ya kuambiwa hawakuchukua hatua yoyote ya msingi dhidi ya wahusika wakuu, ambao ni Barick.
• Wanaharakati walihoji kwa nini mgodi huo wa North Mara bado haujafungwa mpaka sasa? Na kwa nini serikali imeendelea kukaa kimya bila kuchukua hatua yoyote kwa wawekezaji hao? Ipo haja kwa wanaharakati kuweka maazimio ili rais aweze kupata taarifa juu ya uchafuzi na uonevu huu dhidi ya wananchi wake. Kwa sababu wanaharakati tayari wanao ushaidi wa kutosha juu ya uchafuzi huu ni vyema rais akaambiwa.
• Ipo haja kwa wanaharakati kutambua wale wote waliopo katika mapambano haya, ili iwe rahisi kwao kuunda mtandao wa pamoja wa kupigania madini na urithi wa nchi yetu, kwani kwa sasa ni vigumu kuunda mtandao wa pamoja wa kupambana na uvamizi wa nchi yetu.
• Wanaharakati waingie barabarni na kufanya maandamano ya kupinga uonevu huu wa watu wa Mara, kwani bila kuingia barabarani si rahisi kwa watu wengi kupata taarifa juu ya uvamizi huo. Serikali yenyewe imejaribu kuficha taarifa hizi mara nyingi lakini wameshindwa!
• Vyombo vya habari vilinyimwa kuonyesha picha kama hizi ili wananchi wengi zaidi wasiweze kupata taarifa juu ya uchafuzi huo. Hivyo serikali ilikuwa inajua juu ya hali halisi inavyoendelea kule North Mara lakini ikachagua kukaa kimya na kuendelea kuwakumbatia wawekezaji wale, hivyo kuna haja kwa wanaharakati kusambaza taarifa juu ya uchafuzi ule ili watu wengi zaidi wapate taarifa juu ya hali halisi inavyoendelea kule North Mara ili waweze kuingia katika harakati hizi za utetezi wa rasilmali zetu ili ziweze kuwanufaisha wananchi wa kawaida.
• Pawepo na maandalizi ya mjadala wa kitaifa juu ya unyonyaji na uonevu unaondelea juu ya rasilimali zetu hasa katika sekta ya madini. Semina za GDSS kama hizi ni sehemu mojawapo ya mijadala hiyo inayotakiwa endeshwe nchini nchi nzima. Mijadala hii itasaidia wananchi kufahamu juu ya uharibifu unaoendelea katika migodi, pamoja na wananchi wanavyopata tabu katika nchi yao.
• Wanaharakati walipendekeza iundwe kamati ndogo ambayo itafuatilia mambo ya madini, ikiwa na pamoja na kuandaa maandamano makubwa ya amani yenye lengo la kupeleka taarifa kwa wananchi kwa wingi zaidi, na kuibua hisia za kutetea rasilimali zetu.

Wanaharakati tuungane kupinga uonevu huu dhidi ya raia wanyonge.

Kutoka Frederick Lugard hadi leo

Na Jenerali Ulimwengu.

NIMEKUWA nikijadili suala la watu kukimbia kutoka maeneo ya shamba na kukimbilia mijini. Tumekwisha kuona kwamba watu hawa wanakimbilia mijini kwa sababu kadhaa, moja miongoni mwao ikiwa ni kwamba miji ndiyo imekuwa na ukirtimba wa hata hayo maendeleo haba yaliyopo, na pili kwa sababu viongozi wao wamehamia mijini kwa sababu maisha ya kijijini ni adha tupu.

Kwa ye yote anayefuatilia masuala ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii na ukuaji wa jamii zetu katika historia ya nchi za Kiafrika takriban zote, hali hii haiwezi kumshangaza, kwani inatokana na historia tuliyoipitia. Hatutakiwi kusahau hata siku moja kwamba katika mambo mengi yaliyotuathiri na ambayo yamesababisha tuwe kama tulivyo, uzoefu wetu chini ya utawala wa kikoloni umekuwa na nafasi kubwa mno, kiasi kwamba kila tukifurukuta tunajikuta tunalazimika kukirejea kipande hicho cha historia yetu.

Kabla ya ukoloni jamii zetu zilikuwa ni makundi ya kikabila ambayo kwa kiwango kikubwa yalijitegemea na kujitosheleza, yakifanya kazi za jamii kulingana na mahitaji ya jamii kwa wakati ule. Makundi haya yalikuwa na mahusiano na maingiliano na makundi mengine ya karibu, mara nyingi uhusiano huu ukitokana na nasaba zilizokaribiana za makundi haya au historia ya ujenzi wa makusudi wa udugu minajili ya kumaliza vita na kujenga amani baina ya makundi haya.

Katika mkundi ya kikabila uzalishaji uliamuliwa na kutekelezwa kufuatana na utashi wa jamii, na matunda ya uzalishaji huo yalikuwa ni mali ya jamii iliyoyazalisha, kuanzia chini kabisa kwenye familia mahsusi iliyotekeleza majukumu yake vyema na kupanda hadi jamii nzima ambayo kwa pamoja imetimiza malengo iliyojiwekea.

Maamuzi yalikuwa yakifanywa karibu kabisa na wanajamii na sababu za maamuzi hayo zilieleweka vyema. Watawala walikuwa watu wanaojulikana na kila mwanajamii kwa sababu waliishi ndani ya jamii yao, wakifanya kazi bega-kwa-bega na jamii na wakishiriki katika kila tukio la jamii, katika msiba na katika faraja.

Inawezekana ninachora picha isiyo sahihi sana kwa kurahisisha mambo na kuyaremba kwa waridi na yasmini. Ni kweli kwamba jamii zetu hazikufanana zote; zilipishana, tena wakati mwingine kwa viwango vikubwa, na ama kwa hakika, zipo jamii zilizoishi kwa vipindi virefu kama jamii za watumwa na vijakazi wa jamii nyingine.

Itoshe tu hapa kusema kwamba kwa jamii iliyotamanika, jamii mwanana ambayo makabila mengine yangeiona kama jamii ya kupigiwa mfano, hivyo ndivyo ilivyokuwa: Jamii inayofanya kazi kwa kupanga yenyewe, kusimamia yenyewe utekelezaji wa kazi ilizojipangia, ugawanaji wa mazao kwa haki (siyo lazima usawa), na kutathmini shughuli zote hizo kwa pamoja, kwa uhuru, kama jamii.

Ujio wa ukoloni ulifanya jambo moja ambalo limetuathiri hadi leo. Jamii zetu zilifanywa ziache kuzalisha kwa ajili ya mahitaji yao na badala yake zifanye kazi kwa lengo la kukidhi mahitaji ya wakoloni. Tunajua kwamba hayo mahitaji ya wakoloni mara nyingi hayakusadifu na mahitaji ya jamii zetu, kwani hili halikuwa lengo la ukoloni. Wao walikuwa mabwana, nasi tulikuwa watawana wa kuwatumikia, basi.

Kama mahitaji ya wakoloni wakati huo yalikuwa ni mazao ya mafuta, au mazao ya mbao au vipusa vya ndovu, watu wetu walilazimishwa kuzalisha vitu hivyo, hata kama kufanya hivyo kulikinzana moja kwa moja na mahitaji ya jamii zetu. Hii ilikuwa ni imla ya watawala wetu nasi hatukuwa na chaguo katika uzalishaji tuliotakiwa kuufanya, wala hatukuwa na uhuru wa kupanga bei za mazao yaliyotokana na jasho letu, au hata kujua huko yanakokwenda mazao hayo yanakwenda kufanya nini na kwa faida ya nani.

Wale waliopitia historia ya mapambano dhidi ya ukoloni watakumbuka kwamba wakati wote harakati zilihusiana na suala la uzalishaji, nini kinazalishwa, kwa ajili ya kukidhi haja gani, na nani anufaike kutokana na uzalishaji huo.

Ziko jamii zilizokataa kulima mazao ambayo hayakuwa na faida kwao; ziko nyingine zilizong’oa mazao zilipoona kwamba zinanyonywa kwa kulipwa bei ndogo sana; na ziko zilizogoma ili kupinga kuchukuliwa ardhi yao kwa ajili ya kilimo cha mazao yaliyotakiwa ughaibuni badala ya mazao yaliyokidhi mahitaji ya jamii hizo.

Kuondoka kwa wakoloni na kuingia kwa utawala mpya kungetarajiwa kuleta mabadiliko makubwa katika jinsi maamuzi yanavyofanyika kuhusu uzalishaji ili jamii zetu zizalishe kwa mpangilio niliouleza hapo juu, yaani kwa mpangilio wao na kwa manufaa yao.

Kilichotokea ni kwamba utaratibu ule ule wa ukoloni uliendelea kama vile hakuna kilichotokea, na wananchi wakaendelea kupokea maagizo kutoka Dar es Salaam na kuyatekeleza, kama walivyokuwa wakifanya chini ya mkoloni.

Ili kuhakikisha kwamba matakwa yao yanatimizwa, katika uzalishaji na masuala mengine, wakoloni walikubali aina fulani ya utawala wa wenyeji ndani ya “serikali za mitaa”, kwa utaratibu wa “indirect rule” ulioasisiswa na mkoloni Frederick Lugard nchini Nigeria na baadaye ukasambazwa katika makoloni mengi ya Uingereza.

Soma zaidi

Zaidi ya Bil 14/- zatafunwa TRA

-Wakaguzi mbioni kukamilisha ripoti
-Kigogo mtuhumiwa ajiuzulu kwa notisi ya saa 24
-Baadhi ya mabenki yahusishwa

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) sasa ipo kwenye wakati mgumu baada ya kuwapo kwa taarifa za wizi wa zaidi ya Sh. bilioni 14 uliofanyika kwa awamu ndani ya miaka tisa.

Raia Mwema linaweza kuripoti kwa uhakika kwamba kwa sasa wakaguzi wa ndani ya mamlaka hiyo wanahakiki wizi huo ili hatimaye kuchukua hatua mahususi.

Uhakiki huo mahsusi pia umethibitishwa kwa gazeti hili na Mwenyekiti wa Bodi ya TRA, Dk. Maceline Chijoriga ambaye, hata hivyo, alisisitiza kutoa fursa kwanza kwa kamati ya uhakiki (auditing committee) kuachwa kufanya kazi yake. Wizi huo uligundulika Julai mwaka huu.

Lakini wakati Mwenyekiti huyo akiwa na mtazamo huo, tayari mfanyakazi mmoja mwandamizi (jina linahifadhiwa) anayedaiwa kuhusishwa na wizi huyo amejiuzulu kwa notisi ya saa 24, miezi michache iliyopita lakini kukiwapo madai kutoka kwa maofisa wengine waandamizi kuwa kigogo huyo ameshirikiana na mtandao mpana wa viongozi serikalini na baadhi kwenye mamlaka hiyo na baadhi ya benki nchini, ikiwamo mojawapo maarufu iliyowahi kubinafsishwa kutoka mikono ya umma.

Taarifa za uhakika kutoka kwa maofisa watatu waandamizi kwenye menejimenti ya mamlaka hiyo zinaeleza kuwa mabilioni hayo yaliyoanza kuchotwa taratibu kuanzia mwaka 2000 yanatoka katika makato ya kodi maarufu kama Pay As You Earn (lipa kadiri unavyopata) ambayo hukatwa kwenye mishahara ya wafanyakazi na kupaswa kuingizwa kwenye pato la taifa.

Inaelezwa kuwa makato hayo na hasa kutoka kwa wafanyakazi wa TRA nchi nzima yamekuwa yakichotwa taratibu na kuingia mifukoni mwa mtandao (syndicate) huo wa uhujumu na wizi na wakati mwingine TRA imekuwa ikilipa mishahara hewa kwa wafanyakazi waliokufa au kutokuwapo kazini kwa sababu nyingine za kawaida, kama kuacha au kuachizwa kazi.

Kwa mujibu wa habari hizo zilizofikishwa katika gazeti hili na jopo la maofisa watatu wa TRA, inadaiwa kuwa mbinu za kufanikisha uchotaji huo zilianza pale mamlaka kuandaa, kuidhinisha na kusaini ulipaji mishahara kutolewa kwa ofisa mmoja pekee, utaratibu unaotajwa kuwa ni kinyume kwa mujibu wa watalaamu wa masuala ya uhasibu na fedha.

“Huyu (anatajwa jina) aliandaliwa na kupewa mamlaka ya kuwa muandaaji mishahara na signatory. Ndiye aliyekuwa na sauti kwa chochote kuhusu malipo iwe mishahara au malipo mengine kwa hiyo imekuja kubainika na hasa baada ya ukaguzi wa hesabu kufanywa kwamba, kuna upotevu wa zaidi ya Sh. bilioni 14.

“Upotevu huo umetokana na wizi katika makato ya pay as you earn ya wafanyakazi wa TRA nchini na nyongeza ya mishahara kwa baadhi ya wafanyakazi nyongeza ambayo hata hivyo haiendi kwa wahusika lakini pia kumekuwapo na malipo ya mishahara hewa kwa watu waliokufa au kuacha kazi,” alisema ofisa mmoja aliyekuwa akiungwa mkono na wenzake wawili ambao Raia Mwema ilithibitisha kwa utaratibu mahsusi kuwa ni wafanyakazi wa TRA makao makuu.

“Alikuwa na uwezo wa kufanya chochote katika system ya mishahara kwenye kompyuta na hata baada ya kutoa notisi ya 24 baada ya mambo kutibuka, system ilishindwa kuendeshwa kama kawaida na ililazimu aitwe kazini na alifanya kazi kwa siku mbili kuweka mambo tena sawa,” anasema ofisa mwinginen kwenye jopo hilo.

Inadaiwa kuwa kutokana na kushirikiana na baadhi ya vigogo TRA makao makuu na hata baadhi ya vigogo serikalini, mhusika huyo alijihakikishia usalama katika kuendeleza hujuma hizo hadi pale ukaguzi uliofanywa na kampuni moja ya ukaguzi wa hesabu kubaini kasoro hiyo ambayo awali, licha ya ukaguzi kufanyika taarifa zinadaiwa kutozaa matunda ikiwa ni pamoja na kuzuia tatizo kuendelea.

Katika mazungumzo yake na Raia Mwema kuhusu sakata hilo, Mwenyekiti wa Bodi ya TRA Dk. Chijoriga alisema: “Ni kweli kuna auditing committee (kamati ya uhakiki) ndani ya TRA na hiyo inaripoti taarifa zake kwenye bodi kila baada ya miezi mitatu.”

Lakini kuhusu sakata hilo, alieleza: “Bado hatuwezi kutoa taarifa halisi juu ya nini kimetokea na hatua zitakazochukuliwa. Ni lazima kwanza tupishe kamati ifanye kazi yake na iwasilishe ripoti kwetu (bodi), tukianza kusema sasa nadhani si vizuri…kwa hiyo tuachie tufanye kazi yetu kikamilifu bila kuingiliwa.”

Raia Mwema pia iliwasiliana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Ramadhani Kija ambaye hakutaka kuzungumzia kwa kina suala hilo la ujpotevu wa mabilioni ya fedha akitaja aulizwe Waziri wake, Mustafa Mkulo.

Hata hivyo, Katibu Mkuu huyo alikiri kushuka kwa kiwango cha ukusanyaji mapato TRA, lakini akishindwa kuweka bayana kuwa sababu ni kushuka kwa uaminifu miongoni mwa maofisa wa TRA na badala yake akitetea kuwa anachofahamu sababu ni mtikisiko wa uchumi duniani.

“Hilo suala la wizi aulizwe waziri ambaye ripoti hufikishwa kwake kwa hiyo kama amepewa ripoti rasmi ya ukaguzi atakueleza, lakini kuhusu kushuka kwa mapato kwenye miezi mitatu hii ni kweli yameshuka kwa asilimia 10 hivi na sababu siwezi kusema moja kwa moja ni uaminifu mdogo kwa watendaji hilo la uaminifu wanaweza kuzungumza TRA wenyewe, isipokuwa nafahamu sababu mojawapo ni mtikisiko wa uchumi duniani,” alisema Kija, ambaye aliteuliwa na Rais Kikwete kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Graye Mgonja. Awali kabla ya uteuzi huo, alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo.

Thursday, November 19, 2009

Mtoto wa kike anaweza

Mawaziri wanane wazidiwa

-Maofisa wa wizara husika wawalalamikia
-Mmoja adaiwa kujikita zaidi CCM kuliko serikalini
-Kikwete atakiwa kusuka au kunyoa

WAKATI Rais Kikwete ametimiza mwezi huu miaka minne kamili tangu alipoingia madarakani, hali ya utendaji kazi wa baadhi ya mawaziri wake si nzuri na angalau wanane wanalalamikiwa na wafanyakazi wa wizara hizo.

Raia Mwema limetajiwa na wafanyakazi hao jina la waziri mmoja, John Chiligati ambaye inadaiwa hutumia muda mwingi zaidi wa kazi katika shughuli za chama (CCM) ambako ana wadhifa wa kitaifa.

Mawaziri wanaozungumzwa na watendaji waandamizi kwenye wizara zao katika tafsiri ya kutakiwa kuwajibika mbali na Waziri huyo wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, John Chiligati, ni Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na Naibu wake, Dk. Makongoro Mahanga, Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Sophia Simba.

Uchunguzi wa Raia Mwema uliohusisha mazungumzo na baadhi ya watendaji waandamizi wa wizara hizo na baadhi ya wabunge, kwa wiki kadhaa sasa, umebaini kuwa Waziri John Chiligati ndiye mwenye wakati mgumu zaidi mbele ya watendaji kwa kuwa kabla yake, Wizara hiyo ilikuwa na Waziri John Magufuli ambaye anatajwa na watendaji wa chini kuwa ni mchapakazi hodari na alikuwa kipenzi kwa watendaji wengi wizarani.

Kwa mujibu wa mazungumzo hayo kati ya Raia Mwema na watendaji wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, ambayo inasimamia Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Chiligati anatajwa kutumia muda wake mwingi zaidi katika shughuli za Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambako ni Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) ya chama hicho-Itikadi na Uenezi.

“Kwetu hapa wizarani na hata wenzetu wa NHC (Shirika la Nyumba la Taifa) tunamwona Mheshimiwa Chiligati kama mwanasiasa zaidi na anatumia muda mwingi kwenye vikao na safari za CCM. Si mtu wa ku-concentrate na masuala ya wizara kama ilivyokuwa kwa Waziri Magufuli, isipokuwa mara chache tu.

“Mambo yamerejea kuwa ya kawaida mno baada ya Magufuli kuondolewa hapa. Kwa kweli Magufuli alikuwa kipenzi cha wafanyakazi wazalendo waliojitoa mhanga kutumikia nchi…hapa mambo yamekuwa ya kawaida sana,” alisema ofisa mmoja mwandamizi Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye kwa sababu zilizo wazi hakutaka jina lake kuandikwa gazetini.

Kwa upande wake, ofisa mwingine kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) amelieleza gazeti hili kuwa ili mambo yaweze kwenda sawa na kwa uhakika ndani ya shirika hilo anahitajika Mkurugenzi mpya wa shirika ambaye ni mzalendo na mchapakazi kwa kuwa tayari kuna pengo la kuwa na waziri mfuatiliaji wa karibu wa majukumu yake katika shirika hilo.

“Tunaye Waziri anayefanya kazi yake kwa kawaida mno bila kasi yoyote na kwa kweli tunazo sababu za kufanya hivyo na hasa tunapomlinganisha na Magufuli. Sasa katika mazingira kama haya ni wazi shirika linahitaji mtu makini na mzalendo zaidi ili aweze kuipa image (taswira) wizara,” alisema ofisa huyo.

Hata hivyo, Raia Mwema ilizungumza na Chiligati kuhusu maoni hayo na alisema ya kuwa “hawezi kufanya mtihani na kujisahihishia mwenyewe.”

“Hayo maoni ya watu siwezi kuyaingilia, mimi siwezi kufanya mtihani na kujisahihisha mwenyewe lakini naamini watendaji ofisi wanajua naingia ofisini saa ngapi na natoka saa ngapi,” alisema Chiligati na alipoulizwa kuhusu shughuli za chama kuingilia majukumu ya serikali, alisisitiza kutotaka kujisahihishia mtihani.

Kutokana na maoni haya, tayari kuliwahi kujitokeza mapendekezo kutoka kwa baadhi ya wabunge na viongozi wa CCM kwamba, viongozi wa serikali, na hususan mawaziri wasiwe viongozi wa chama na hata wajumbe wa Halmashauri Kuu au Kamati Kuu ya chama hicho.

Kati ya wabunge waliowahi kutoa ushauri au mapendekezo hayo kupitia mahojiano na gazeti hili ni Mbunge wa Kishapu, Fred Mpendazoe ambaye aliweka bayana kuwa kuna mgongano wa maslahi kwa waziri kuwa kiongozi wa kitaifa wa chama.

Kwa mujibu wa mbunge huyo, ripoti za utendaji wa mawaziri hupaswa kuwasilishwa kwenye kamati kuu au halmashauri kuu ya chama hicho na huwasilishwa na waziri na kwa hiyo mjadala hauwezi kuwa wa haki au ukosoaji kwa kuwa waziri ni sehemu ya uongozi wa chama aliyeteuliwa na Rais.

Lakini maoni mengine nje ya hayo ya Mpendazoe yaliyowahi kutolewa ni kwamba hata na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapaswi kuwa Mwenyekiti wa chama tawala kwa maslahi na ustawi wa chama hicho kwani akiwa kama mwenyekiti hataweza kuongoza kwa uhuru vikao vya kamati kuu au halmashauri kuu vinavyoweza kuibua ukosoaji mkali dhidi yake au serikali yake.

Mbali na Chiligati, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja naye upepo ndani ya wizara yake na hususan Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) haumwendei vizuri mbele ya wananchi. Anaonekana kutotimiza wajibu wake kwa kasi inayostahili na msingi mkuu ni kuonekana kushindwa kuzuia kitisho cha Mkurugenzi wa TANESCO, Dk. Idriss Rashid kuwa nchi itaingia gizani, kitisho ambacho Rais alikipuuza lakini kilitimia; huku Ngeleja akiendelea kuwa waziri hadi sasa.

“Tunamwona Ngeleja kama Waziri ambaye amechangia kuwapo kwa mgawanyiko na hata mgongano baina ya wajumbe fulani wa bodi ya TANESCO na menejimenti ya TANESCO. Kuna mpasuko fulani kwenye bodi na wajumbe wengi wa bodi wako upande wake kuliko kuwa karibu na shirika.

“Ni waziri ambaye si mhimili wa wafanyakazi wa TANESCO, tunamwona kama yuko karibu zaidi na miradi ya umeme ya kampuni binafsi kuliko kuwekeza juhudi na maarifa yake karibu na wataalamu wa TANESCO ili kubaini kuikoa nchi na janga la ukosefu wa umeme. Ameridhika kukimbia huku na huko kwenye miradi midogo ya umeme lakini ukweli ni kwamba hakuna dira ya wazi zaidi ya mikakati kwenye makaratasi kuhusu umeme wa uhakika nchini.

“Watalaamu wanasema mabwawa yetu ya kuzalisha umeme yanahitaji ukarabati madhubuti lakini umesikia hivi karibuni huko Tanga mtambo umepata hitilafu ambayo chanzo chake ni uchakavu. Hii maana yake ama hakuna uratibu mzuri wa taarifa kati ya menejimenti ya TANESCO na Wizara au wizara na hasa waziri hana hamasa ya masuala ya umeme,” alisema mmoja wa maofisa waandamizi wa TANESCO.

Lakini mbele ya wananchi, kitisho cha Dk. Rashid kuwa nchi itaingia gizani na hatimaye ikaingia licha ya ahadi ya Rais kuwa haitafikia hali hiyo ni pigo kubwa kwa Waziri Ngeleja, ambaye pia anaonekana mbele ya wananchi kukimbia huku na huko kutokana na kile kinachotajwa kuwa shinikizo la Rais, kuwasha mitambo ya kampuni binafsi ya IPTL, jijini Dar es Salaam.

Kwa upande wa wabunge, wanashindwa kuelewa ni kwa nini Waziri Ngeleja anashindwa kuwasilisha kwa wakati mapendekezo ya iliyokuwa kamati ya Jaji Mark Bomani kuhusu marekebisho ya mikataba na mambo mengine kwenye sekta ya madini nchini.

Kamati ya Bomani iliyoteuliwa na Rais kutoa mapendekezo kwenye sekta ya madini ili taifa linufaike kama ilivyo kwa wawekezaji wa kigeni (win-win situation) iliwashirikisha wabunge makini, kutoka CCM akiwamo Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe na wabunge wa kambi ya upinzani, Zitto Kabwe wa Kigoma Kaskazini na John Cheyo wa Bariadi Mashariki.

Inaelezwa kuwa katika mapendekezo hayo, kamati iliweka bayana namna ambavyo taifa linapoteza kiasi kikubwa cha mapato na namna ambavyo hali hiyo inavyoweza kuzuiwa. Kwa kadiri muda unavyopotea ndiyo mapato hayo yanazidi kupotea mikononi mwa taifa.

Jinamizi la mgodi wa North Mara kutiririsha maji ya sumu kwenye Mto Tigithe, Tarime mkoani Mara bado linazidi kumtafuta Waziri Ngeleja akionekana kutojipanga au kupanga Wizara yake kuhakiki mara kwa mara usalama wa migodi na wakazi wanaozunguka, ingawa lawama hizi anapaswa kushirikiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, Dk. Batilda Burian.

Hata hivyo, Waziri Ngeleja hakupatikana kupitia simu yake ya mkononi lakini Raia Mwema ilizungumza na Naibu Waziri wake, Adam Malima, ambaye hakuwa tayari kuelezea hayo akitaka aulizwe Katibu Mkuu wa wizara hiyo.

Waziri wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa, naye anatajwa na baadhi ya watendaji makini wa wizara hiyo kuwa anaongoza ofisi yake katika utaratibu wa ‘business as usual” na hasa kushindwa kutoa mwongozo wa haraka katika masuala tata kama ya Shirika la Reli Tanzania (TRL) ambako wafanyakazi waliamua kuchukua hatua ya kutangaza kutomtambua mwekezaji kutokana na kile kinachoelezwa kuwa ni ubabaishaji wa mwekezaji huyo na hasa baada ya kutokuwapo kwa mabadiliko yoyote baada ya mwekezaji Railways Infrastructure, Transport and Economic Services (RITES) ya India, kusaini mkataba wa kuwekeza.

Mbali na reli, utata wa muda mrefu katika Bandari ya Dar es Salaam na hasa suala la msongamano wa bidhaa ni kati ya mambo yaliyomchukua muda mrefu Waziri Kawambwa kuamua kwa maslahi ya Taifa kiasi cha baadhi ya wasafirishaji wanaotumia bandari hiyo kudaiwa kuanza kutumia bandari jirani ya Mombasa, nchini Kenya.

Ingawa tayari wizara imefuta ukiritimba wa Kampuni ya Kupakua na Kupakia Mizigo (TICTS) kwa kuruhusu kampuni nyingine binafsi kufanya kazi hiyo, lakini bado wabunge wamekuwa wakipiga kelele kuwa kazi ya kuongeza ufanisi bandarini ni lazima iende sambamba na kuimarisha usafiri wa reli ili mizigo inayokwenda nchi jirani na maeneo mengine nchini iondoke kwa wakati na kasi inayohitajika na hasa ikizingatia kuwa Tanzania imezungukwa na nchi kadhaa zisizo na bandari.

“Waziri wetu na naibu wake ni watu wanaofanya kazi zao kwa kawaida mno, tangu kuwapo kwao hapa hakuna changamoto za wazi walizokuja nazo. Hakuna hamasa yoyote mpya. Hii wizara ndiyo inashughulika na barabara wakati wa awamu ya tatu, iliitwa Wizara ya Ujenzi na alikuwa Magufuli wewe mwenyewe unakumbuka utendaji makini na mbwembwe za Magufuli alipendwa na wahandisi karibu wote wizarani na hata mikoani,” anasema mmoja wa wafanyakazi waandamizi wa wizara hiyo tangu awamu ya tatu. Waziri Kawambwa naye alishindwa kupatikana kupitia simu yake ya mkononi.

Wimbi la vijana kuhama kutoka vijijini kuja maeneo ya miji mikubwa nchini kama Dar es Salaam, Mwanza, Arusha na hasa maeneo ya migodi kunatajwa kuwa ni ishara ya kutosha ya Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya kuongoza wizara yake ili iwe kinara na mwongozo kwa vijana nchini.

Na katika hali isiyo ya kawaida, Wizara hiyo inayoongozwa na msomi kwa kiwango cha ‘profesa’ na naibu wake kiwango cha shahada ya uzamivu (Dk. Makongoro Mahanga), imepachikwa jina la Wizara ya Kuwasha na Kuzima Mwenge, kwa maana kwamba shughuli za mbio za Mwenge wa Uhuru huratibiwa na wizara hiyo.

Baadhi ya wabunge wameilalamikia wizara hiyo kuwa licha ya kuwa na fungu la fedha kwa ajili ya kukopesha vijana, lakini fedha hizo zimekuwa hazina matunda ya wazi kwa taifa na kinyume chake, vijana wamekuwa wakijiongoza wenyewe bila mwongozo wa wizara katika kujikimu kimaisha na kwa hivyo, wizara imechangia kukata mawasiliano kati ya serikali na vijana nchini.

“Naweza kusema bado wizara hii haijapata waziri anayejua awafanyie nini vijana wa Tanzania. Mawaziri na naibu wao karibu wote wamekuwa kama wapita njia wanaosubiri muda au siku yao ya kuondoka ifike, waondoke. Huyu Kapuya alikuwapo hapa awamu ya tatu, migogoro ya kazi ilikuwa mingi na vijana walikuwa wakijifanyia mambo yao wenyewe kwa kadiri ya uwezo wao, wakifika hapa labda wanahitaji sahihi au muhuri wa wizara.

“Umesikia Serikali ya Awamu ya Nne imetoa mikopo ya mabilioni kwa wajasiriamali bila kubagua iende kwa vijana au watu wa rika jingine lakini hapa Wizara na hasa Waziri hashituki na pengine hajui ni vijana wangapi na wa maeneo gani wamenufaika na hadi sasa maendeleo yao yamefikia wapi. Je, wamerejesha fedha au mkasa gani umewapata na msaada gani unatolewa na vijana kwao,” alisema mmoja wa wafanyakazi wa ngazi ya chini wizarani hapo.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrance Masha, naye si kiongozi wa kujivunia mbele ya watendaji wa chini yake, ikielezwa kuwa amekuwa akikabiliwa na upuuzwaji wa chini kwa chini na baadhi ya makamanda waandamizi kwenye Jeshi la Polisi, Magereza na Uhamiaji na kwamba Naibu Waziri, Balozi Khamis Kagasheki ndiye mwenye mvuto kwa kile kinachotajwa kuwa ‘ustaarabu na uungwana’ wake .

Hata hivyo, wakati mawaziri hawa wakionekana kufifia kiutendaji imebainika kuwa taswira bora ya wizara hiyo kwa sasa inabebwa kwa kiasi kikubwa na umakini wa Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Saidi Mwema. Baadhi ya maofisa waandamizi wa polisi wamekuwa wakimtii Mwema kwa nafasi ya Waziri kwa kuwa juhudi zake zimelenga kwa dhati kuboresha jeshi hilo.

Wizara nyingine ambazo mawaziri wake wapo kwenye hali tete ni Sophia Simba wa Utawala Bora, wizara ambayo vyombo vya Usalama wa Taifa, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) viko chini yake.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa tayari kuna mpasuko katika Idara ya Usalama wa Taifa na hasa mpasuko wa maslahi hali ambayo inatajwa kuhitaji Waziri madhubuti tofauti na Simba ambaye anadaiwa kufikia hatua ya kutetea baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi.

Inaelezwa kuwa kupasuka kwa Idara ya Usalama wa Taifa kunathibitishwa na wizi wa mabilioni katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), na wizi katika wizara za serikali na taasisi nyingine.

Inadaiwa kuwa baadhi ya maofisa waandamizi wa idara hiyo wamebainika kuwamo katika kashfa nzito nchini, zikiwamo za wizi BoT na kwamba hali inaweza kuwa tete kama watafikishwa mahakamani kwa kuwa wanafahamu siri za vigogo wengine waandamizi walioshirikiana nao kwenye wizi.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, anaonekana kuwa makini zaidi akitumia vema Idara zenye mamlaka huru kama Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) na ile ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ambapo amekuwa akisisitiza ni ofisi huru kufikisha kesi mahakamani hali inayomwondoa kwenye kitanzi cha lawama kwa baadhi ya kesi za ufisadi kutofikishwa mahakamani.

Hata hivyo, alikuwa akibanwa na suala la nchi kujiunga na Umoja wa Nchi za Kiislamu (OIC), ambalo nalo limemalizwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwamba katiba ya OIC inafanyiwa mabadiliko. Pia Waziri Chikawe amejivua kitanzi cha Mahakama ya Kadhi kwa maelezo ya serikali kwamba ni suala linalopaswa kuundwa ndani ya mfumo, uratibu na usimamizi wa waislamu.

Utata upo kwa Wizara ya Maliasili na Utalii, ambako Waziri wake Shamsha Mwangunga amewahi kukumbwa na ‘gharika’ la Bunge mara tatu. Mara ya kwanza, aliwahi kubanwa na Mbunge wa Kwela, Chrisant Mzindakaya kuwa amekiuka maazimio ya Bunge kuhusu vitalu vya uwindaji, na ilipendekezwa apewe karipio, mara ya pili, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela, kutishia kupinga bajeti yake kutokana na maofisa wake kughushi nyaraka na kuruhusu pembe za ndovu kutoroshwa kwa kutoa vibali kuwa ni kilichobebwa kwenye makontena ni taka za plastiki.

Tatu, ni suala la mgogoro kati ya mwekezaji kampuni ya Ortelo Business (OBC) na wananchi wa Loliondo, ambako Waziri huyo aliunda tume ya kuchunguza na alipotoa taarifa ya tume hiyo bungeni, Mbunge wa Simanjiro alitamka bungeni kuwa ripoti yake (waziri) kwa sehemu kubwa imejaa uongo.

Kutokana na ‘uongo’ huo, Spika wa Bunge, Samuel Sitta amekwishaunda timu kwenda Loliondo kupata ukweli kwa kulinganisha na taarifa ya Waziri na hali halisi.

Waziri huyo sasa anaishi katika hofu akisubiri kamati ya bunge na bila shaka kama itabainika alitoa taarifa ya uongo bungeni, wito wa kuwajibika utaanza kumwandama.

Waziri wa Kilimo na Chakula, Stephen Wasira, naye mbele ya wananchi yuko kwenye hali ngumu kwa kuwa licha ya Serikali kutimiza miaka minne bado nchi inakabiliwa na njaa ingawa pia Waziri huyo hakuingia moja kwa moja kwenye wizara hiyo ambayo awali katika serikali ya sasa ilikuwa ikiongozwa na Joseph Mungai. Wasira binafsi aliwahi kuzungumza na televisheni moja nchini na katika kujibu lawama kwamba kwa nini nchi inaingia kwenye njaa akasema; “mimi si waziri wa mvua.”

Kwa ujumla hali ni tete ndani ya wizara hizo na jambo la hatari zaidi watendaji waandamizi wameanza kutilia shaka uwezo wa baadhi ya mawaziri wao na wengine wakibaini kuwa tatizo si mawaziri wao bali ni bajeti finyu.

Hata hivyo, suala la bajeti finyu linapingwa na baadhi ya watendaji wanaodai kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayoongozwa na Magufuli pia ina bajeti finyu lakini licha ya upya wake imefanya kazi inayoonekana tayari.

Chanzo: www.raiamwema.co.tz

Wednesday, November 18, 2009

‘Zanzibar undeni Serikali ya Mseto’

ZANZIBAR imeshauriwa kuunda Serikali ya Mseto ikilazimika kufanya hivyo, kwa sababu si jambo la aibu, bali ni sehemu ya demokrasia.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Balozi Juma Mwapachu, alisema jana kuwa watu hawatajisikia vibaya kuhusu uundaji wa Serikali ya Mseto kutokana na kuwa sehemu ya kuundwa kwa demokrasia ya kweli.

“Nafikiri rafiki zetu wa Zanzibar wakifikiria kuwa na Serikali ya Umoja si mbaya,” alisema Balozi Mwapachu na kuongeza: “Ingawa wanasiasa wengi katika nchi za Afrika Mashariki hupendelea serikali inayoendeshwa na chama kimoja.”

Alizungumza hayo baada ya kufungua mkutano wa demokrasia katika nchi za Afrika Mashariki ulioandaliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kusherehekea miaka 10 tangu kuundwa kwa EAC Novemba 1999.

Alisema Serikali ya Mseto imefanikiwa katika nchi nyingine kama za Ujerumani na Italia, huku akiunga mkono makubaliano yaliyofikiwa hivi karibuni kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF), akisema ni mwanzo mzuri wa upatikanaji wa amani Zanzibar.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala, alisema sababu ya watu wachache kujitokeza katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliopita inatokana na wananchi kuamini kuwa viongozi wanaochaguliwa hawaleti tofauti yoyote.

Alisema ni jambo la kawaida duniani uchaguzi unapofanyika kama wa mitaa, unakuwa na matokeo duni mpaka Uchaguzi Mkuu ambao wananchi wanaamini kuwa kura zao zinaweza kuleta mabadiliko.

Profesa Mukandala alishauri katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu ufanyike kwa wakati mmoja ili kuhamasisha wananchi wengi kujitokeza kupiga kura katika kuchagua viongozi wa mitaa.

Monday, November 16, 2009

Wanafunzi Elimu ya Juu wageuka ombaomba

WANAFUNZI katika vyuo vikuu kadhaa nchini wanadaiwa kuishi maisha ya kubahatisha kutokana na fedha wanazozitegemea kutoka Bodi ya Mikopo kutowafikia kwa wakati mwafaka.

Ingawa taarifa zimedai kwamba vyuo vingi wanafunzi wake wamekumbwa na adha hiyo, Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na Tumaini, mkoani Iringa, ni miongoni mwa vyuo ambavyo baadhi ya wanafunzi walitoa taarifa kulalamikia hali hiyo.

Wanadai kwamba baadhi ya wanafunzi wanaotegemea mkopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) wamekuwa wakipata mlo mmoja na wengine wakiomba msaada kutoka kwa wanafunzi wenzao.

“Watu wanaishi kwa mlo mmoja. Wengine wanaishi kwa kusaidiwa. Tunasaidiana kwa kukopeshana. Kwa kweli hali ni mbaya. Tunashindwa kuelewa tatizo ni bodi au chuo,” alisema mwanafunzi wa Udom, ambaye hakutaka jina lake litajwe.

Taarifa kutoka chuoni hapo, zinasema wiki iliyopita, wanafunzi walianza kushawishiana kufanya mgomo. Lakini baadhi ya viongozi wa wanafunzi waliwasihi kwa kuwataka wawe na subira.

Makamu Mkuu wa Udom, Profesa Idris Kikula, alisema chanzo cha tatizo ni wanafunzi wenyewe kutokana na baadhi kusuasua kufanya udahili huku wengine akaunti zao walizopaswa kuingiziwa fedha kuwa na utata.

Profesa Kikula alisema katika wiki ya kwanza ya Septemba, wanafunzi 4,500 ambao ilikuwa wapatiwe fedha zao, kati yao, wanafunzi 3,900 akaunti zao zilikuwa na matatizo.

Pia wiki iliyopita, wanafunzi 500 walianza kuingiziwa fedha zao lakini baadhi yao ilibainika pia akaunti zao zilikuwa na utata.

“Tulikaa na serikali ya wanafunzi na tatizo hili limetatuliwa,” alisema Profesa Kikula na kusisitiza kwamba wiki hii, kundi hilo pia litapatiwa fedha hizo.

Alithibitisha kwamba wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza, wa pili na tatu wanaostahili kupata mkopo huo wa Heslb, fedha zao zimeshatolewa na bodi.

Akizungumzia kusuasua kwa wanafunzi kufanya udahili, Profesa Kikula alisema, “wanafunzi wengi walisuasua kufanya udahili kwa sababu sisi ni chuo tunajiendesha, kwa hiyo tulisema lazima walipie vyumba. Wengi wamechelewa kufanya hivyo.”

Hata hivyo, alisema chuo kinataka kijenge utaratibu kwa kushirikiana na bodi ili fedha hizo za mkopo ziwe zinapelekwa moja kwa moja kwa wanafunzi kwa kuwa licha ya usumbufu, ni hatari pia kwa chuo kuingiziwa mabilioni ya fedha ambazo si zake.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Heslb, Cosmas Mwaisobwa, alisema hadi kufikia Novemba 6, vyuo mbalimbali kikiwemo Udom na Tumaini, vilishapelekewa fedha kwa ajili ya wanafunzi walioidhinishwa kupata mkopo.

Kufikia tarehe hiyo, Sh bilioni 12.7 zilipelekwa kwa ajili ya wanafunzi wapya 5,363 katika Chuo Kikuu cha Dodoma na Sh milioni 698 kwa ajili ya wanafunzi wapya 291 wa Chuo cha Tumaini.

Wakati Tumaini ilifunguliwa Oktoba 3 na Udom ilifunguliwa Oktoba 17, gazeti hili limebaini kwamba wazazi na wanafunzi wengi ambao majina yao yaliwekwa kwenye tovuti ya Heslb kuonesha madaraja ya mkopo, walidhani kwamba wangeweza kupatiwa fedha mara baada ya kuripoti chuoni.

“Walipofungua chuo, tulidhani kwamba baada ya kuwasili vyuoni, fedha hizo zingepatikana ndani ya muda mfupi.Lakini hali imekuwa tofauti, mtoto anasema wanaishi kwa shida sana nasi imebidi tusake japo hela kidogo kumtumia,” alisema mzazi wa mtoto anayesoma Tumaini, aliyejitambulisha kwa jina la Mama Mushi.

Wakati huo huo, Mwaisobwa alisisitiza kwamba majina yaliyotolewa kuonesha madaraja ya mkopo na asilimia zinazotakiwa kutolewa kwa waliofuzu vigezo katika mwaka huu wa masomo, siyo kigezo cha mwanafunzi kuingia chuoni na kukaidi kulipa gharama zinazotakiwa kwa kuwa huo siyo uthibitisho kwamba ameshapewa mkopo.

Aliliambia gazeti hili kwamba upo uwezekano wa baadhi ya wanafunzi wakawa wanalalamika wakati hawako kwenye orodha ya waliokwishaidhinishiwa kupewa fedha hizo.

Vile vile alitahadharisha kwamba malalamiko ya wanafunzi yanaweza kuwa yanatolewa na wale ambao bodi haijaidhinisha kama watapewa au la.

Wapo baadhi ya wanafunzi ambao hadi sasa fedha zao hazijatolewa kutokana na majina yao kuendelea kufanyiwa kazi na bodi.

Kundi lingine ni la wanafunzi ambao walichagua chuo zaidi ya kimoja. Hawa wanatakiwa wadahiliwe kwanza kwenye vyuo walivyoamua na kisha namba zao za udahili zipelekwe kwenye bodi ishughulikie mchakato wa kuwapa mkopo.

Friday, November 13, 2009

Mrejesho wa Semina za GDSS

Utetezi Kuhusu Masuala ya Madini Katika Mtizamo wa Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi

Mada ya jumatano ya tarehe 11.11.2009 iliwakilishwa na Silas O’lang kutoka taasisi ya Revenue Watch Institute (RWI) na mchungaji Magafu kutoka Chama cha wachungaji Tanzania. Taasisi ya RWI inajenga uwezo kwa asasi za kiraia na kamati za bunge.

Wawakilishi walianza mada yao kwa maswali sita ya uchokozi kwa washiriki. Rasilimali ya madini ni ya akina nani? Ni nani anayefaidika na madini hayo? Ni jukumu la nani la kuhakikisha rasilimali ya madini inawanufaisha wananchi? Je uamuzi wa uchimbaji wa madini yetu ulifanyika kwa wakati muafaka? Je, usimamizi ukoje? Na sera zetu zipoje?

Katika kujibu maswali hayo, washiriki waliweza kuweka wazi kwamba, madini na uchimbaji wa madini hapa Tanzania haunufaishi wananchi wa kawaida, bali hunufaisha makampuni ya nje na baadhi ya viongozi wachache wa serikali.

Kaka O’lang alisema, Tanzania kuna matatizo makuu matatu ambayo yanasababisha sekta ya madini isitoe mchango mkubwa katika pato la taifa. Matatizo hayo aliyaeleza ni;

1. Sekta hii ya madini ilitarajiwa kuleta mapato kwa serikali kutokana na kodi ambayo ingesaidia kuinua huduma za jamii kama shule, hospitali, afya, nk Lakini kutokana na mfumo wetu wa sheria umetowa mwanya kwa makampuni haya kukwepa kodi, hivyo kuchangia kiasi kidogo sana katika pato la taifa.

2. Taraji la serikali ni kwamba sekta hii ya madini ingeweza kuongeza ajira kwa wananchi wa hapa nchini. Lakini kampuni hizi zinatumia teknolojia ambayo haihitaji wafanyakazi wengi sana na wanaohitajika ni watu ambao wanaujuzi maalumu. Pia walitarajia kutakuwepo na uwiano kati ya sekta hii na sekta zingine, lakini sekta hii haijakuza sekta zingine. Wawekezaji wamekuwa wakitumia malighafi zote kutoka nje. Na zaidi ya hayo, wananchi wengi walihamishwa kutoka katika maeneo yao ili kupisha uanzishwaji wa migodi hiyo, bila kulipwa fidia ya kutosha, kitu kinachozua migogoro isiyoisha katika maeneo hayo ya migodi.

3. Shughuli za uchimbaji wa madini zimekuwa na athari kubwa sana kwa mazingira na raia. Kwa mfano katika mgodi wa dhahabu wa Buhemba wawekezaji wameondoka na kuacha mashimo bila kuyafukia, na katika mgodi wa North Mara ambapo sumu kali ya migodini ilititirika hadi mto Tegete na kudhuru mamia ya raia na mifugo. Mapaka sasa serikali bado hajatowa tamko la wazi kuhusiana na uchafuzi huo, huku ikiendelea kuwatetea wawekezaji. Hali hii imekuwa ikisababisha migogoro ya mara kwa mara katika maeneo ya migodi.

Ukiachilia mapungufu hayo makubwa bado kuna swali la kujiuliza, ni kiasi gani cha mapato kinachopatikana katika sekta hii kinachokwenda kugharamia sekta ambazo zinagusa maisha ya kila siku ya akina mama, kwa mfano afya ya uzazi, maji, na nishati mbadala?

Washiriki wakichangia hoja hizo walipendekeza kupata tathimini ya mali iliyopo katika ardhi yote ya Tanzania na kufahamu itawanufaisha vipi raia wa kawaida?

Pia kupendekeza sheria ya madini iangaliwe upya. Wanaharakati wamepigia kelele mara nyingi bila mafanikio yoyote, na serikali imeendelea kushikilia msimamo wake wa kuifanya mikataba hii kuwa siri, pamoja na kuendelea kutoa misamaha ya kodi kwa wawekezaji katika sekta ya madini.

Swala la kuwasemehe kodi wageni bado liliibua majadiliano makubwa. Washiriki walisisitiza kwamba hakuna umuhimu wowote wa kuwasamehe kodi wageni kwa miaka mitano katika sekta ya madini, kwani hakuna ulazima huo kwa vile sekta hii aina ushindani ukilinganisha na sekta zingine.

• Wanaharakati walipendekeza kelele kuhusu uporaji wa madini ziendelee kupigwa zaidi. Inavyooenekana kwamba wananchi hawana sauti ya kutosha juu ya madini yao na serikali imewekwa mfukoni na wawekezaji katika sekta ya madini. Wanaharakati waandike zaidi katika magazeti, kuelimishana zaidi juu ya umuhimu wa kutetea rasilimali zetu ambazo ndio urithi wetu.
• Yaandaliwe Maandamano kwa wazira ya madini na kueleza haja yetu ya kutaka kuwa na sera ya madini ambayo itawanufaisha wananchi wote kwa usawa bila upendeleo wowote, ukilinganisha na sasa.
• Tujenge nguvu ya pamoja katika kudai haki za wananchi ambazo zinavunjwa na serikali kwa kushirikiana na mashirika ya kimataifa.kwa sababu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko tunayoyakusudia!

Mwisho, Wanaharakati wana nafasi ya kuleta mabadiliko kama wakiunganisha nguvu kwa pamoja.

Serikali mseto Z’bar yanukia

MAPATANO ya ghafla kati ya Rais wa Zanzibar, Aman Abeid Karume na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad, yakihusisha kumtambua rasmi Karume, na Hamad kudai hatua hiyo inafungua makubwa zaidi, ni hatua za awali kuandaa serikali ya mseto, Raia Mwema imeelezwa.

Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari kutoka vyama vya CCM na CUF, serikali ya mseto itaundwa ikiwa ni moja ya mkakati wa vyombo vya usalama kujipatia fursa ya kubaini kasoro na namna ya kuzifanyia kazi kwa kipindi hiki cha miezi kadhaa kabla ya Uchaguzi Mkuu, mwakani.

Mara baada ya Uchaguzi Mkuu mwakani, vyama vya CCM na CUF vilikubaliana rasmi kuwa Zanzibar itakuwa ikiendeshwa kwa mfumo wa serikali ya mseto, lakini sasa imebainika kuwa ni vizuri zaidi kufanyia kazi wazo hilo ili kupunguza msuguano utakaoweza kujitokeza baada ya uchaguzi mkuu.

Baada ya mkutano wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM uliofanyika kijijini Butiama, mkoani Mara, Machi, mwaka jana, CCM kimsingi ilikubali kuanzishwa kwa Serikali ya mseto lakini mvutano kati ya chama hicho na CUF ulijitokeza kwa swali kwamba lini mseto uanze.

CCM walitaka mseto uanze baada ya Uchaguzi Mkuu mwakani, lakini CUF wakataka uanze sasa. Wakati mvutano huo ukiendelea kulijitokeza hoja ndani ya CCM kwamba yatafutwe maoni ya Wazanzibari wote kuhusu suala hilo kwa kuwa Zanzibar si ya CCM wala CUF pekee.

Kati ya watu wanaoamini kuwa serikali ya mseto inawezekana kuundwa Zanzibar ili kumaliza mpasuko wa kisiasa ulioibuka tangu uchaguzi wa mwanzo wa vyama vingi uliofanyika mwaka 1995.

Viongozi waliokwishaweka msimamo wao wazi tangu Agosti mwaka jana ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhan Ferouz, alipozungumza na moja ya magazeti ya kila siku nchini.

Mapema wiki hii, Rais Karume alikutana na Maalim Seif, Ikulu ya Zanzibar katika kikao cha faragha ambacho baada ya kukamilika, Seif alifanya mkutano wa hadhara wa wanachama wa chama chake na kuwaeleza kuwa wanamtambua rasmi Karume kwa kuwa hatua hiyo inafungua milango ya makubwa zaidi, ambayo hata hivyo hakuyataja.

Hatua ya viongozi hao imetanguliwa na kauli ya Rais Jakaya Kikwete alipozungumza na wananchi miezi michache iliyopita kuwa suala la ufumbuzi wa migongano ya kisiasa Zanzibar bado halijamashinda Rais Karume kiasi cha yeye kuingilia kati.

Hata hivyo, wakati hayo yakijiri hali imekuwa tete katika vyama vya CCM na CUF. Wakati CCM na hususan wahafidhina ndani ya chama hicho wakianza kuratibu mikakati ya kupinga suala hilo, CUF wanaitazama hatua ya kiongozi wao kumtambua Karume kwa hadhari kubwa baadhi wakiamini hiyo ni ‘janja’ ya CCM kuweka utulivu wa nchi hususan kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.

Tayari viongozi mbalimbali wa kitaifa wa vyama hivyo wameunga mkono uamuzi wa CUF kumtambua Karume. Viongozi hao ni pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, na Kingunge Ngombale-Mwiru ambaye alishiriki kwenye timu ya mazungumzo ya muafaka ya makatibu wakuu wa vyama hivyo.

Suala la utatuzi wa mpasuko wa kisiasa Zanzibar lilizungumzwa na Rais Kikwete katika hotuba yake ya kuzindua Bunge, Desemba 30, mwaka 2005, akisema mgogoro wa Zanzibar unamsononesha na kuahidi kuufanyia kazi.

Chanzo:www.raiamwema.co.tz

Baraza la Mawaziri la Kikwete lagawanyika

-Mawaziri kumi wataka watuhumiwa waadhibiwe
-Wanane wanawatetea, waliosalia hawana msimamo
-Sophia Simba asonywa na wenzake

BAADA ya Kamati inayoongozwa na Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi kuzungumza na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi na kuibuka malumbano, kejeli na matusi kwenye mkutano huo, imebainika kuwa sasa mpasuko si tu miongoni mwa wabunge; bali umesogea hadi kwenye Baraza la Mawaziri na kugawa mawaziri hao.

Uchunguzi wa Raia Mwema, ukihusisha mazungumzo na baadhi ya wabunge na mawaziri, umebaini kuwa mpasuko katika baraza la mawaziri kwa kiasi fulani umechukua sura tofauti na ule wa wabunge wa CCM.

Katika Baraza la Mawaziri, hali ni tofauti. Siku kadhaa mara baada ya mkutano wa Mwinyi, Dodoma, wapo mawaziri walioanza kuwapuuza manaibu mawaziri wao, lakini pia wapo manaibu mawaziri walioanza kuwapuuza mawaziri wao, hali inayotajwa kuwa huenda ikasogea hadi kwa watendaji wa chini kwenye wizara na hatimaye kugawa watendaji wote.

Lakini pia katika mazungumzo hayo ya Raia Mwema, pia imebainika kuwa kuna baadhi ya wizara zenye mawaziri wanaofanana kimtazamo wakiwa kundi moja kwenye mpasuko huo; hali inayotajwa kuwa huenda ikazua mvutano kama watendaji wengine waandamizi wizarani watakuwa na misimamo pinzani.

Mpasuko huo chanzo chake kinatajwa kuwa kashfa ya Richmond, na hususan kuhusika kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kwenye sakata hilo ambapo mawaziri na manaibu mawaziri wanaodaiwa kuwa karibu naye wameendelea kumtetea kwa siri na hadharani; huku wengine wakitafsiri hatua hiyo kuwa ni upuuzi na hata kuwaona wenzao wanaoendesha harakati hizo ni wapuuzi.

Mmoja wa mawaziri hao ni Sophia Simba, ambaye sasa si tu imedaiwa anatazamwa kwa jicho tofauti na baadhi ya mawaziri wenzake, lakini pia CCM imeanza kukana baadhi ya shutuma alizotoa kwa baadhi ya watu katika juhudi zake za kutetea watuhumiwa wa kashfa mbalimbali. Simba anadaiwa kueleza kuwa Mfanyabiashara Reginald Mengi, si mwanachama wa chama hicho.

Taarifa zaidi zinaeleza kuwa kati ya mawaziri 26 waliopo ukimwondoa Waziri Mkuu, 10 wamedaiwa kuwa na msimamo unaofanana na baadhi ya wabunge wapambanaji wa ufisadi wakiwa na msimamo watuhumiwa wa ufisadi waadhibiwe, wakati mawaziri wengine wanane wakiwa katika kundi la utetezi.

Mawaziri wanaodaiwa kuwa na msimamo wa kupinga ufisadi ukiwamo wa Richmond ni pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Uvuvi, John Magufuli, Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Mary Nagu, Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Profesa Mark Mwandosya na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Bunge, Philip Marmo.

Wengine ni Waziri wa Afya, Profesa David Mwakyusa ambaye anatajwa kuwa na msimamo wa chini chini, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Celina Kombani, Waziri wa Afrika Mashariki, Diodorous Kamala na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Margaret Sitta.

Mawaziri wanaodaiwa kuwa msimamo wao haueleweki katika sakata la Richmond ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, dk. Hussein Mwinyi, Waziri wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe na Waziri wa Kilimo, Stephen Wasira.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa kundi la mawaziri wenye msimamo mkali wanaotaka hatua kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa, wengi wao wamekuwa na rekodi nzuri kiutendaji ikilinganishwa na wale watetezi wa watuhumiwa.

Baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema wamedai kuwa mawaziri wengine wanane msimamo wao umeshindwa kubainika moja kwa moja kutokana na kuwapo katika kila kundi.

Katika mkutano uliopita wa Bunge, utekelezaji wa lala salama wa mazimio ya Bunge kuhusu Richmond ulipaswa kutolewa taarifa na serikali lakini haikuwa hivyo, bila kuelezwa sababu za wazi.

Uchunguzi huo wa muda mrefu wa Raia Mwema bungeni pia umebaini kuwa athari za makundi kwa kiasi fulani zimekuwa zikimgusa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye ndiye aliteuliwa na Rais baada ya Lowassa kujiuzulu.

Uchunguzi huo umebaini kuwa katika mkutano wa 16 wa Bunge na baadhi ya vikao vya mkutano wa 17 uliokwisha, hivi karibuni, wakati akitoa hoja au kujibu maswali ya papo kwa papo yenye utetezi wa Serikali ni sehemu ya mawaziri wachache tu wamekuwa wakimpongeza kwa kumpigia makofi na wengine wakibaki kuduwaa, wengine wakiwa katika mazungumzo yao.

Kutokana na hali hiyo, mmoja wa wabunge amedai kuwa wapo mawaziri wasiompa nafasi ya heshima na utiifu unaostahili Waziri Mkuu Pinda na kwamba, wameendelea kuwa watiifu zaidi kwa kundi lao kuliko kwa waziri mkuu.

Wizara ambazo zimejipambanua kuwa na waziri mwenye msimamo wa utetezi kwa Lowassa na watuhumiwa wengine ni Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais – Utawala Bora, inayoongozwa na Sophia Simba.

Wizara nyingine ambazo zimebainika kuwa na mawaziri wenye misimamo ya makundi ni pamoja na Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, inayoongozwa na Profesa Juma Kapuya, na Naibu wake Dk. Makongoro Mahanga.

Kapuya alitajwa na kundi mojawapo kwenye mpasuko huo kuwa ni kati ya watu wanaopaswa kuchukuliwa hatua akidaiwa kumtetea Lowassa kwa gharama za wanasiasa wengine akiwamo Spika wa Bunge, Samuel Sitta. Naibu wake, Makongoro naye pia alijipambunua kuwamo kwenye kundi la Lowassa, wakati wa mkutano wa Mwinyi.

Baadhi ya wabunge pia wanaitazama Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuwa inaongozwa na viongozi wenye mgongano wa makundi, japokuwa ikidaiwa kuwa Naibu Waziri Khamis Kagasheki, amejitahidi kwa muda mrefu kuficha hisia zake tofauti na Waziri wake, Lawrance Masha, anayedaiwa kuwa kundi la Lowassa.

Katika hatua nyingine, baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema kutoka makundi yote wamebainisha matarajio yanayozidi kukinzana mara baada ya kukamilika kwa mkutano kati yao na Kamati ya Mwinyi.

Wakati upande mmoja ukiendelea kusisitiza kuwa watuhumiwa wenye nyadhifa katika chama hicho wang’olewe, wenzao wamekuwa na msimamo tofauti.

Hata hivyo, kundi la wabunge wanaotaka wenzao watuhumiwa watimuliwe ndilo linaonekena kuwa na nguvu zaidi hata mbele ya wananchi na taasisi nyeti zikiwamo za elimu ya juu nchini kama ambavyo imekuwa ikiandikwa na baadhi ya magazeti nchini.

Kwa upande mwingine, hali ya kuwapo kwa kile kinachoelezwa kuwa ni mvutano huenda ikaendelea. Kuwapo kwa dalili hizo kunatokana na kuendelea kukinzana kati ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta na baadhi ya wanasiasa wa kundi linalomwandama, akiwamo Kingunge Ngombale-Mwiru.

Kingunge katika mkutano uliopita wa NEC-CCM Dodoma aliripotiwa kutaka Spika Sitta ang’olewe kwa kuwa anaendesha Bunge vibaya kwa kuruhusu mijadala ya ufisadi na hivyo kuhatarisha chama na serikali na kuimarisha hoja yake kwa kusema ubaya wa Spika unathibitishwa na hatua yake ya kuandika kitabu kinachoitwa “Bunge lenye Meno” akishirikiana na wabunge wengine machachari, akiwamo Dk. Harrison Mwakyembe.

Inaelezwa kuwa Kingunge alirejea msimamo wake huo katika mkutano wa Mwinyi lakini akionyesha kukejeli msimamo huo, Spika wa Bunge wakati akizungumza bungeni muda mfupi kabla ya kuahirishwa kwa Bunge, alijigamba kuwa Bunge lake bado lina meno.

Sitta alitamka; “Ni Bunge lenye meno” wakati akielezea uamuzi wa kuwatuma wabunge kwenda eneo la Loliondo lenye mgogoro kati ya wananchi na mwekezaji, mgogoro ambao serikali kupitia Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga, iliwasilisha ripoti yake iliyotokana na kamati aliyounda kubaini kama kulikuwa na vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu.

Ripoti hiyo ya Mwangunga ilikataliwa na Bunge baada ya Waziri kueleza kuwa hapakuwa na haki za binadamu huku wananchi walioathirika wakieleza kuwa haki zao zilikiukwa, ikiwa ni pamoja na kuchomewa makazi na karaha nyingine zikiwamo za vitendo vya udhalilishaji wa wanawake.

Awali, kabla ya Spika kuingia bungeni kikao cha Bunge kilikuwa kikiongozwa na Mwenyekiti, Job Ndugai ambaye ni Mbunge wa Kongwa CCM, ambaye alionekana kutaka kuikubali ripoti hiyo ya Serikali kabla ya Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka kusimama na kueleza Bunge kuwa kwa sehemu kubwa ripoti ya Waziri Mwangunga imejaa uongo na hivyo kuomba mwongozo wa Spika ili kutoa uamuzi utakaolinda maslahi ya wananchi.

Kutokana na uamuzi huo, Ndugai alikubali na kueleza kuwa atalifikisha suala hilo kwa Spika ambaye atatoa uamuzi na ilipofika kikao cha jioni siku hiyo, Spika akatoa msimamo kuwa atatuma timu ya wabunge kwenda Loliondo, hatua ambayo bila shaka mbele ya kina Kingunge itaendelea kumtafsiri Sitta kama kikwazo kwa mambo ya serikali kupita bila kujali yana maslahi ya wananchi au la.

Ripoti ya kamati ya Mwinyi inatarajiwa kuwasilishwa katika mkutano ujao wa NEC-CCM bila shaka baada ya kupitia mikononi mwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye ni Mwenyekiti wa chama hicho.

Kwa muda mrefu kumekuwa na wito wa kutaka Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba aenguliwe katika wadhifa huo kutokana na tuhuma mbalimbali zikiwamo za kuendelea siasa za makundi kwenye chama hicho. Kati ya matukio yanayomuhukumu Makamba ni kitendo chake cha kumlaani kada machachari wa CCM, Nape Nnauye, aliyejitokeza hadharani na kudai kuwa mkataba wa ujenzi katika jengo la Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Upanga Dar es Salaam ni wa wizi na unaonyonya jumuiya hiyo.

Katika shutuma zake hizo, Nape alitaka baadhi ya viongozi wa Baraza la Wadhamini wa UVCCM akiwamo Edward Lowassa, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na kujiuzulu kwa kashfa ya Richmond , awajibike. Makamba aliwatetea wadhamini hao akishirikiana na aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM, Dk. Emmanuel Nchimbi.

Hata hivyo, suala hilo lilifikishwa kwenye NEC-CCM na uamuzi ulitolewa kuwa iundwe kamati kuchunguza na ikibidi kurekebisha mkataba huo. Kamati hiyo ilifanya marekebisho makubwa, uamuzi ambao kwa namna fulani unaathiri umakini wa Makamba katika utetezi wake kwa baadhi viongozi wanaodaiwa kuwamo katika kundi lake ndani ya CCM.

Source:www.raiamwema.co.tz