Tuesday, August 31, 2010

TENDWA KUTOA MAAMUZI PINGAMIZI LA CHADEMA BAADA YA SIKU TANO


Msajili wa Vyama Vya Siasa Nchini John Tendwa amesema atatoa uamuzi wake dhidi ya malalamiko yaliyowasilishwa ofisini kwake jana na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuhusu mgombea wa urais kupitia chama cha mapinduzi (CCM) baada ya siku tano.

Bwana Tendwa ameyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es salaam baada ya kupokea malalamiko hayo rasmi leo.

‘’Nitatoa maamuzi hayo baada ya kupokea maelezo kutoka kwa mlalamikiwa dhidi ya mlalamikaji yaliyowasilishwa,na nitatoa nakala ya maamuzi kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi,Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi na Katibu Mkuu wa chama cha CHADEMA’’,Alisema Tendwa.

Akifafanua suala hilo Tendwa amesema baada ya maamuzi yake mlalamikaji na mlalamikiwa kama hawataridhika na uamuzi wake wanayo haki ya kwenda kutafuta haki yao kwenye vyombo vya sheria.

Soma zaidi

Monday, August 30, 2010

NEC kuamua rufani wiki hii

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imesema taarifa kuhusu rufani za udiwani na ubunge zilizopokelewa zitaanza kutolewa wiki hii.

Rufani hizo ziliwasilishwa kwa NEC na baadhi ya wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge siku chache baada ya uteuzi.

Mkurugenzi wa NEC, Rajabu Kiravu, alisema bado wanaendelea kuzijadili rufani hizo na kwamba taarifa kamili watazitoa kuanzia wiki ijayo. “Tunaendelea kuzifanyia kazi rufani tulizozipokea, hivyo siwezi kutoa taarifa nusu, wiki ijayo tunaamini tutakuwa tumekamilisha na tutatoa maelezo yake,” alisema.


Hadi kufikia Ijuma, rufani 152 zilikuwa zimepokelewa na NEC.

Friday, August 27, 2010

Lipumba: Nipeni urais nikomeshe mafisadi

-Azindua ilani ya CUF

Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, amezindua Ilani ya uchaguzi ya chama hicho na kuahidi kuwa iwapo atafanikiwa kuingia Ikulu atapambana vikali na 'mchwa' wanaotafuna fedha za umma.

Vile vile, Profesa Lipumba alisema ataimarisha mfumo wa ukusanyaji wa kodi ili kupunguza utegemezi wa wahisani katika bajeti ya serikali kwani ni aibu nchi kuendelea kuwa omba omba.

Akizindua ilani hiyo jijini Dar es Salaam jana kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu, Profesa Lipumba alisema hakuna sababu ya kuendelea kutegemea nchi wahisani wakati taifa lina rasilimali nyingi na vyanzo vingi vya mapato ambavyo vikisimamiwa vyema nchi inaweza kujitegemea.

Alisema asilimia 30 ya mapato ya serikali yanaishia mikononi mwa mafisadi hivyo kuifanya nchi kuendelea kuwa tegemezi wakati fedha hizo zingetosha kabisa kuiwezesha serikali kujiendesha.

Alisema mapato ya fedha za mfuko wa barabara ambayo yanapatikana kupitia makato katika mafuta ni makubwa, lakini yamekuwa yakipotelea mikononi mwa mafisadi wachache hivyo kukwamisha maendeleo ambayo yangepatikana kupitia fedha hizo.

Alisema akiingia Ikulu, CUF itahakikisha uchumi wa taifa unakuwa kwa angalau asilimia saba hadi 10 kwa mwaka, hali itakayowezesha huduma nyingi za jamii kupatikana kwa urahisi tofauti na ilivyo sasa.

Katika Ilani hiyo, Lipumba alisema chama chake kitahakikisha asilimia 25 ya mapato ya serikali yanakwenda kuboresha sekta ya elimu nchini.

Alisema asilimia 15 ya mapato hayo ya serikali yatatumika katika kuboresha kilimo, asilimia 15 sekta ya afya na sekta nyinginezo zitapewa asilimia 20 hadi 25 ya mapato hayo.

Aidha, Profesa Lipumba alisema serikali yake itaongeza uzalishaji wa chakula kwa kiwango kikubwa ili wananchi wapate lishe nzuri tofauti na sasa ambapo wananchi wengi wanaishi kwa kubahatisha na hawana uhakika wa chakula.

Alisema idadi ya Watanzania maskini imeongezeka kutoka milioni 11 mwaka 2005 hadi kufikia watu milioni 12.5 mwaka huu na kwamba CUF itahakikisha inabadili hali hiyo kwa kuongeza ajira na kuwawezesha watu kujiajiri hivyo kuondokana na lindi la umaskini.

Alisema atajikita katika kupambana na ufisadi na rushwa kwani serikali ya sasa imeshindwa kabisa kukabiliana na vitendo hivyo na kwamba kesi zilizopelekwa mahakamani ni geresha tu.

Alisema Tanzania ina vyanzo vingi vya umeme ambavyo ni gesi, upepo na jua ambavyo vinaweza kutumika kuimarisha miundombinu ya nishati ya umeme na kuondokana kabisa na umeme wa kubahatisha.

Alisema katika suala la teknolojia, CUF itahakikisha somo la kompyuta linakuwa la msingi kuanzia chekechea na kila mwanafunzi anakuwa na kompyuta yake wakati wa masomo.

“Ukizungumzia suala hili watu wanakuona kama unaota, lakini si kitu kigumu na kinawezekana kabisa tukidhamiria kuleta mapinduzi katika teknolojia ...kuna watafiti wamegundua kompyuta ndogo (laptop) ambazo zitakuwa zikiuzwa kwa dola 100 hivyo tutazinunua kwa wingi na kuzitumia,” alisema Profesa Lipumba ambaye pia ni mwenyekiti wa CUF taifa.

Alisema CUF imesimamisha wagombea ubunge katika majimbo 139 Tanzania Bara na katika majimbo 50 ya Zanzibar.

CHANZO: NIPASHE

Wednesday, August 25, 2010

Tendwa aongeza siku za kujaza gharama za uchaguzi


Msajili wa vyama vya siasa- John Tendwa

Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, ameongeza muda wa siku kumi kwa wagombea kuwasilisha fomu za gharama za uchaguzi watakazotumia wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu na kwamba watakaoshindwa kufanya hivyo ndani ya muda huo wa ziada, atawafuta kwenye kinyang’anyiro hicho.

Muda wa kurejesha fomu za tamko la gharama za uchaguzi zitakazotumika unaishia kesho, lakini Tendwa ameuongeza hadi Septemba 6 baada ya baadhi ya vyama vya siasa kulalamika kuwa wagombea wake hawajapewa fomu hizo na wakurugenzi wa halmashauri, ambao ndio wasimamizi wa uchaguzi huo.

Msajili huyo alithibitisha kuwa baadhi ya wakurugenzi wa halmashauri ambao ndio wasimamizi wa uchaguzi wamekuwa wakiwakatalia kuwapa fomu hizo wagombea wa ubunge na udiwani wa vyama vya siasa wanapokwenda kuziomba.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Tendwa alisema wakurugenzi hao hawana sababu yoyote ya kuwanyima wagombea fomu hizo kwani tayari zilishapelekwa kwa wingi katika kila ofisi ya halmashauri kwa ajili ya kuzigawa.

Alisema hata vyama vya siasa havipaswi kulalamika kwani navyo vilishapatiwa fomu hizo muda mrefu hivyo viliwajibika kuwa vimeshawapatia wagombea wao wajaze na kuzirejesha katika ofisi ya msajili kwa wakati.

“Sitaongeza muda tena na mgombea yeyote atakayeshindwa kuwasilisha fomu inayoelezea gharama atakazotumia katika kampeni ajue nitamwondoa na hatagombea maana sheria inanipa mamlaka ya kufanya hivyo, nimeamua kuongeza muda baada ya kuridhika kuwa baadhi ya sehemu fomu zilikuwa hazijafika,” alisema Tendwa.

Alisema hata wagombea ambao wamepita bila kupingwa wanapaswa kujaza fomu hizo na kuziwasilisha kwa ofisi ya msajili kama sheria inavyosema.

“Hata Waziri Mkuu nimemwambia leo (jana) kuwa kupita bila kupingwa si sababu ya kutojaza fomu ya gharama za uchaguzi atakazotumia, nimemwambia kuwa Sheria inamtaka ajaze na aiwasilishe kwangu, na wabunge wengine ambao hawakupingwa nimewaeleza hivyo hivyo,” alisema Tendwa.

Alisema siku kumi alizoongeza sio nyingi hivyo vyama vya siasa vinapaswa kufanya haraka kuwapa wagombea wao fomu hizo wazijaze na kisha kuzirejesha ili wasipoteze sifa za kugombea.

Alisema wagombea wanaweza kutumia zaidi ya gharama walizojaza katika fomu, lakini baadaye watawajibika kuelezea matumizi ya nyongeza yalivyofanyika.

“Kuna vitu vingi ambavyo vinaweza kutokea bila kutarajia kama mfumuko wa bei, watu wakakuta njia mbovu wakakwama wakatumia fedha zaidi, kinachotakiwa ni kuelezea matumizi yaliyozidi basi, lakini mgombea hakatazwi kutumia zaidi ya alichoandika kwenye fomu,” alisema.

Kuhusu malalamiko ya Chadema kuwa wagombea wake wamenyimwa fomu za kujaza gharama hizo, Tendwa alisema ofisi yake ilishatoa fomu hizo kwa chama hicho siku nyingi hivyo anashangaa malalamiko yanatoka wapi.

Alisema wajibu wa kuwapa wagombea fomu za kujaza ni la vyama vya siasa kwa kuwa vyenyewe ndivyo vinawania madaraka na si ofisi yake.

Katika fomu hizo, wagombea wanatakiwa wajaze matarajio ya mapato yao na gharama wanazotarajia kuzitumia wakati wa kampeni.

Sheria inawataka wagombea hao kujaza fomu hizo ndani ya siku saba baada ya kuthibitishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kugombea.

Tuesday, August 24, 2010

JK achanja mbuga, amwaga ahadi

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, ameahidi kununua kivuko cha Maisome katika jimbo la Buchosa mkoani Mwanza ili kuwaondolea adha wananchi wanapotaka kuvuka maeneo hayo.

Aliyasema hayo jana mjini hapa akiwa katika siku yake ya pili ya ziara yake mkoani Mwanza ya kuomba ridhaa ya wananchi kumchagua kwa kipindi kingine cha miaka mitano.

Rais Kikwete alisema serikali ya Marekani nayo imeahidi kununua meli maalum ya doria kwa ajili ya kuimarisha usalama katika Ziwa Victoria.

Rais Kikwete aliahidi kutoa Sh. milioni 530 kama malipo kwa wafanyakazi wa Chama Cha Ushirika cha Mkoa wa Mwanza (Nyanza) ili walipwe baada ya chama chao kufa kutokana na ubadhirifu.

Rais Kikwete aliahidi pia kutoa Sh. bilioni tano kukifufua chama hicho na kuendelea na shughuli zake kama kawaida.

Rais Kikwete aliahidi kuendelea kuimarisha miundombinu ya maji katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Mwanza ili kuwaondolea adha wananchi.

Akiwa katika Jimbo la Buchosa, Rais Kikwete alimsimamisha mgombea ubunge kupitia CCM aliyeshika nafasi ya pili katika kura za maoni, Eric Shigongo, na wananchi wakalipuka kwa shangwe na nderemo.

Baada ya kupewa nafasi ya kuzungumza, Shigongo aliahidi kuvunja makundi ya wakati wa kura za maoni na kumuunga mkono mgombea aliyeshinda.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza, Clement Mabina, jana alinogesha mikutano ya kampeni hizo kwa kueneza sera kwa lugha ya Kisukuma.

Alikuwa akizungumza Kisukuma wakati wa kampeni za CCM Jimbo la Buchosa na Sengerema hali iliyoonekana kuwakuna wananchi wengi na kumshangilia mara kwa mara.

Akiwa wilayani Geita, Kikwete alisema mgodi wa Geita Gold Mine GGM), utatoa Sh. bilioni 9 kwa ajili ya mradi wa maji wilayani humo na serikali kwa upande wake itatoa Sh. bilioni sita kwa ajili ya shughuli za usambazaji wa maji.

Alitangaza kuwa kuanzia Januari mwakani wilaya ya Geita itakuwa mkoa rasmi na kwamba shughuli za ujenzi wa makao makuu ya mkoa huo yanaendelea vizuri.

Rais Kikwete pia alisema wachimbaji wadogo wadogo wa Geita wasiingiliwe na wachimbaji wakubwa katika maeneo yao ya uchimbaji.

Akiwa Geita na Sengerema, aliahidi kuwa maeneo ya wilaya hizo yatapatiwa umeme.

Friday, August 20, 2010

Aliyetaka kumuuza albino afungwa miaka 17

RAIA wa Kenya aliyeianza safari yake nchini mwao akifuatana na rafiki albino kwa kumrubuni kumtafutia kazi jijini Mwanza, lakini badala yake akataka kumuuza kwa Sh milioni 400, amehukumiwa kifungo cha miaka 17 jela.

Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani hapa jana ilimhukumu Nathan Mtei (28) kifungo hicho na faini ya Sh milioni 80, baada ya kupatikana na hatia ya kumsafirisha na kumtorosha binadamu kwa lengo la kumuua.

Awali akimsomea maelezo ya mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Angelo Rumisha, Mwanasheria wa Serikali, David Kakwaya, alisema mshitakiwa alitenda makosa hayo Agosti 15 mwaka huu kwa kudhamiria kumuua Robinson Mtwana (20) raia mwenzake wa Kenya ambaye ni albino.

Baada ya mshitakiwa kusomewa maelezo, Kakwaya alisema kitendo cha kusafirisha binadamu ni kosa la kisheria hivyo kuiomba mahakama ifikirie adhabu dhidi ya mshitakiwa kwa kuwa makosa hayo yanadhalilisha utu wa binadamu.

“Vitendo vya kusafirisha binadamu kwa lengo la kumuuza vilikuwa vikifanyika enzi za biashara ya Utumwa, kwa kuwa vilikuwa vikidhalilisha utu wa binadamu … biashara hiyo ilizuiwa,” alisema Mwanasheria wa Serikali.

Aliongeza kuwa mwathirika wa tukio hilo ni mlemavu wa ngozi, watu ambao wamekuwa wakiandamwa nchini na matukio ya kuuawa na inaonesha wazi lengo la mshitakiwa lilikuwa ni kuua.

“Madhara ambayo yangetokea endapo mshitakiwa angetekeleza azma yake ni makubwa na yangesababisha mwathirika huyo kuuawa, hivyo tunaiomba Mahakama itoe adhabu kali dhidi ya mshitakiwa,ili liwe fundisho kwa watu wengine wenye nia kama ya mshitakiwa,” alisisitiza Kakwaya.

Akisoma hukumu, Hakimu alisema tukio hilo limeleta picha mbaya kwa Tanzania, kwani imekuwa na matukio kama hayo.

Aliongeza kuwa adhabu aliyopewa mshitakiwa kwa kosa la kwanza atatumikia kwa miaka tisa jela au kulipa faini ya Sh milioni 80 na kwa kosa la pili atatumikia miaka minane.

Lakini kama atalipa faini adhabu zote zitatumika tofauti. Alibainisha kuwa adhbu hiyo imetolewa dhidi ya mshitakiwa ili liwe fundisho kwa watu wengine wenye uroho na tamaa ya fedha kama aliyonayo mshitakiwa.

Kabla ya kutoa hukumu, Hakimu alimtaka mshitakiwa ajitetee.

Aliiomba Mahakama imsamehe au iruhusu kesi ikasikilizwe Kenya kwa kuwa anategemewa na familia yake.

Mshitakiwa aliongeza kuwa mganga wa kienyeji alichangia kutenda kosa hilo, kwani anahisi alimfanyia dawa hata kuingia tamaa.

Hata hivyo, Hakimu alisema mshitakiwa anaruhusiwa kukata rufaa Mahakama Kuu ndani ya siku 45 kuanzia jana, ikiwa hajaridhishwa na hukumu iliyotolewa dhidi yake.

Mtikila, Kyara waenguliwa kugombea urais

KAMA ilivyokuwa Zanzibar, Chama cha Sauti ya Umma (SAU) jana kilikwaa kisiki katika Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Dar es Salaam fomu zake za urais zilipokataliwa kwa kushindwa kutimiza masharti.

Chama hicho na Democratic Party (DP) vilikumbana na kadhia hiyo baada ya kushindwa kutimiza masharti ya kupata wadhamini katikam mikoa 10 nchini.

Hivi karibuni, SAU ilitimuliwa katika ofisi za Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) baada ya wagombea wake wawili kwenda ofisini hapo kuchukua fomu za kuomba kuidhinishwa kugombea urais.

NEC jana ilipitisha wagombea urais kutoka vyama saba vya siasa kuwania nafasi hiyo kati ya vyama 12 vilivyoomba.

Urejeshaji wa fomu za uteuzi wa kugombea nafasi hiyo ya ukuu wa nchi ulifanyika jana kwa siku nzima na wote kutoka vyama saba kupitishwa huku SAU ikigonga mwamba baada ya kuhakikiwa na kukutwa taarifa za wadhamini wake zilizo sahihi ni za mikoa minne tu ya Tabora; Kilimanjaro; Kusini Pemba na Mjini Magharibi.

DP ilikuwa na matatizo ya wadhamini katika mikoa ya Pwani, Kilimanjaro na Dodoma na kukutwa na wadhamini sahihi katika mikoa saba.

Kutokana na kuenguliwa, SAU ilisema itaifikisha NEC mahakamani kwa madai kuwa walitimiza wadhamini wenye sifa katika mikoa 13 lakini Mchungaji Christopher Mtikila wa DP alisema hatakwenda mahakamani hadi NEC itakapomkabidhi nakala ya fomu za mikoa yenye matatizo. Mgombea mwenza wa Mtikila ni Khamis Msabaha.

Akizungumzia hatua hiyo ya kumwengua Paul Kyara wa SAU na mgombea mwenza Kibwana Said Kibwana, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Lewis Makame alisema baada ya kupitia fomu za wadhamini waligundua zilizokuwa na matatizo ni za Pwani; Lindi; Dar es Salaam; Ruvuma; Tanga; Mbeya na Dodoma.

“Mfano, Tanga tuliona kati ya wadhamini wote waliothibitishwa ni 126 na 82 hawakuthibitishwa, wao walitwambia sababu kuu ni wasimamizi wa uchaguzi kukosa na fomu, hivyo NEC imeona hawakukidhi masharti ya kuwa na wadhamini mikoa 10 ambayo minane ni ya Tanzania bara na miwili Zanzibar na kwa masikitiko hawapewi nafasi kugombea,” alisema.

Hata hivyo, Kyara hakusema kitu katika chumba hicho cha mikutano wakati Jaji Makame akitangaza uamuzi wa Tume na alipotoka nje alizungumza na waandishi wa habari na kusema NEC haikuwatendea haki.

“Tatizo ni kwamba baadhi ya mikoa fomu hazikupigwa mihuri na sababu ya kushindikana kuhakiki ni kutopelekewa takwimu na tuliwaeleza makao makuu ya NEC wakasema tuje na fomu hapa wazihakiki na leo (jana) tumekuja saa 6 mchana, lakini wakatuweka chumbani wakatupa soda na saa 9 alasiri wakatuita na kusema hawawezi kuhakiki hadi waende bohari na jioni kuna foleni,” alisema na kuongeza:

“Wakatuweka tena na ilipofika saa 9.45 Kiravu (Rajabu, Mkurugenzi wa NEC), akatuita na kutwambia fomu hazijahakikiwa na tangu tumefika walijua yote, lakini wakachukua Sh milioni moja yetu na baadaye wametuengua na pesa hairudi,” alilalamika.

Awali Kiravu alisema kwa mujibu wa sheria, fedha ya dhamana ya Sh milioni moja inapopelekwa Tume, hairejeshwi isipokuwa kwa chama kilichopata kura zaidi ya asilimia 10.

Urejeshaji huo wa fomu ulianza kwa mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete na mgombea mwenza Dk. Mohamed Gharib Bilal ambao walipata wadhamini mikoa 12 ya Bara na minne Zanzibar.

Walifuatiwa na mgombea wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na mwenza Juma Duni Haji ambao walipata wadhamini katika mikoa minane ya Bara na minne Zanzibar.

Wengine waliorejesha na kuthibitishwa, ni Mutamegwa Mugahywa (TLP) na mwenza Abdullah Othman Mgaza; Dk. Wilbroad Slaa (Chadema) na mwenza Said Mzee Said.

Peter Mziray (APPT-Maendeleo) na mwenza Mchenga Rashid Yusuf, Fahmi Dovutwa (UPDP) na mwenza Hamad Mohamed Ibrahim na Hashim Rungwe (NCCR-Mageuzi) na mwenza Ali Omar Juma.

Akizungumza baada ya kurejesha fomu, Dk. Slaa aliahidi kuwa chama chake kitafanya kampeni za kistaarabu na kuongeza: “kampeni zetu zitakuwa za amani kwani hii ni nchi yetu na wote tunapigania Watanzania … kila mpiga kura naomba azingatie kitabu cha Polisi walichotoa”.

Profesa Lipumba aliwataka wananchi kulinda kura zao na kuahidi akishinda nafasi hiyo kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa, atakuwa amebadilisha Katiba.

Vyama ambavyo havitashiriki kugombea urais ni Demokrasia Makini ambao hawakurejesha fomu na Jahazi Asilia ambao inaelezwa walikosa wadhamini huku NRA ambayo mgombea wake ni Julius Kiyabo haikurejesha fomu hadi saa 10 jioni muda ambao ulikuwa wa mwisho.

Wagombea waliothibitishwa, walikabidhiwa Sheria ya uchaguzi; sheria ya uchaguzi ya serikali za mitaa; sheria ya gharama za uchaguzi; kanuni za uchaguzi wa rais, wabunge, madiwani na maelekezo kwa vyama vya siasa na wagombea na maadili ya uchaguzi.

Kuanzia jana saa 10 jioni hadi leo saa 10 jioni taarifa za wagombea hao zitabadikwa katika ofisi za Tume, ili watu mbalimbali waweze kukaguliwa na wenye pingamizi kuwasilisha Tume.

Hata hivyo, Jaji Makame alisema kampeni ambazo zinaanza leo zitaendelea kwa chama ambacho kitawekewa pingamizi hadi hapo uamuzi wa Tume utakapotolewa.

Monday, August 16, 2010

Walioshinda kura ya maoni CCM 'wapeta'

HALMASHAURI Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), imezingatia maoni ya wanachama wake kwa kuwateua wagombea wa ubunge walioongoza kura za maoni.

Hata hivyo katika baadhi ya majimbo wameachwa walioongoza kwa sababu mbalimbali zikiwemo tuhuma za rushwa na ukosefu wa maadili.

Akitangaza majina ya wagombea hao, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa NEC, John Chiligati alisema sehemu chache chama hicho kiliamua kuteua wagombea ambao hawakushinda kura za maoni.

Uamuzi huo wa kufuata kura za maoni, umekilazimu chama hicho kuwaacha baadhi ya mawaziri wake akiwemo Waziri wa Afrika Mashariki, Dk. Diodorus Kamala aliyekuwa akitetea kiti chake cha Nkenge na Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsa Mwangunga (Ubungo).

Wengine ni Naibu Waziri Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza (Mkinga); Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Joel Bendera (Korogwe Mjini) na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. James Wanyancha (Serengeti).

Mbali na mawaziri hao, chama hicho kimejikuta kikilazimika kuwaacha wakongwe wake wa siasa akiwemo Makamu Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho na Waziri Mkuu mstaafu, John Malecela.

Hata hivyo, imewaengua pia washindi wa kura za maoni wakiwemo Thomas Nyimbo (Njombe Magharibi); Athuman Ramole (Moshi Mjini); Hussein Bashe (Nzega) na Frederick Mwakalebela aliyeongoza kwa Jimbo la Iringa Mjini, kwa sababu za kuonekana kukosa maadili.

Chiligati alisema jana alfajiri mjini hapa kuwa suala la Mwakalebela aliyeongoza Jimbo la Iringa Mjini, halifanani na washindi wengine wa kura za maoni walioteuliwa wakiwemo Basil Mramba (Rombo) na Andrew Chenge (Bariadi Magharibi), licha ya kuwa na kesi mahakamani kama yeye.

“Suala kwa Mwakalebela ni maadili tu, katika mchakato huu, kakamatwa kwa tuhuma za rushwa na Takukuru wamesema wanayo sababu ya kumpeleka mahakamani.

“Lakini alikuwa ndiyo kwanza kaingia katika mchezo wenyewe na katika mchezo huu huu kabla ya dakika tisini, akapigiwa filimbi kuwa amecheza faulo,” alisema Chiligati.

Kuhusu tofauti ya Mramba, Chenge na Mwakalebela, Chiligati alisema, “kisheria wote ni watuhumiwa na hawakukutwa na

hatia, lakini kimaadili ni tofauti…Mramba anatuhumiwa kutumia vibaya madaraka, tuliita wanasheria wakasema hiyo kesi haimuondolei sifa ya kuwa mgombea.”

Hata hivyo, alikiri Mramba alipitishwa baada ya kufanyika mjadala kati ya wajumbe hao wa NEC. “Katika Mkoa wa Shinyanga, Jimbo la Bariadi Magharibi aliteuliwa Chenge kutetea nafasi yake, anayo kesi ya trafiki, haimkoseshi haki ya kuwa mgombea,” alisema Chiligati.

NEC pia imelazimika kuwapoka washindi wengine wa kura za maoni ‘haki’ ya kuwa wagombea kutokana na mmoja kuonekana kuwa hauziki licha ya kushinda kura za maoni, na mwingine kupokwa kwa kuwa alikuwa katika mapumziko baada ya kutumikia adhabu ya chama hicho.

Mgombea aliyeshinda kura za maoni katika Jimbo la Moshi Mjini na kuonekana kuwa hana sifa, ni aliyekuwa Diwani wa Kata ya Kiusa, Athuman Ramole aliyepata kura 1,554 na kufuatiwa na Mwenyekiti wa Wazazi Kilimanjaro, Thomas Ngawaiya (1,539) na Justine Salakana (1,152).

Katika jimbo hilo, NEC imemteua Salakana aliyeshindwa kura za maoni, lakini kwa kigezo kuwa amewahi kuwa Mbunge wa Rombo kwa tiketi ya Chadema, sifa ambayo mshindi wa kwanza hana, lakini wa pili anayo, ila tofauti yake amewahi kuwa Mbunge wa Vunjo kwa tiketi ya TLP.

Sifa nyingine aliyonayo Salakana ambayo wenzake hawana, ni kuwahi kuwa Katibu wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro na Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Utalii Kilimanjaro.

Ingawa Chiligati hakufafanua kwa nini sifa hizo, ziwe muhimu kuliko kura za maoni, lakini duru za kisiasa zilieleza kuwa wamezingatia historia ya jimbo hilo kuwa mikononi mwa upinzani tangu uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi.

Mbunge wake ni Philemon Ndesamburo wa Chadema. Pili ni nguvu za Mbunge anayemaliza muda wake, Ndesamburo ambaye ni wa Chadema anakotoka Salakana na mfanyabiashara wa utalii anayeongozwa na mteule huyo wa CCM.

Katika Jimbo la Njombe Magharibi, mshindi wa kura za maoni Nyimbo amepokwa nafasi ya uteuzi kwa kuwa aliwahi kufungiwa mwaka mmoja asigombee chochote katika chama hicho. Chiligati alisema pamoja na kuwa muda wa adhabu hiyo umekwisha na kuwa ameshinda kura za maoni, wameona wamuangalie kwanza mwenendo wake na hivyo ameteuliwa Gerson Hosea.

Kwa upande wa Viti Maalumu, NEC imewabeba wagombea wote walioongoza kwa kushika nafasi ya kwanza ambao baadhi ya sura mpya ni Vicky Kamata (Geita); Namalok Sokoine (Arusha); Betty Machangu (Kilimanjaro) na Ummy Mwalimu (Tanga).

Pia kwa upande wa Walemavu, wameteuliwa wabunge wawili wa zamani, Al-Shaymaa Kwegir na Margaret Mkanga, wakati kwa upande wa mashirika yasiyo ya kiserikali ni wabunge wawili wa zamani, Rita Mlaki wa Kawe na Anna Abdallah wa Viti Maalumu.

Katika Viti Maalumu, walioshika nafasi ya pili wamo wabunge wengi wa zamani akiwemo Margaret Sitta; Dk. Christine Ishengoma; Devotha Likokola; Rosemary Kirigini na Dk. Maua Abeid Daftari.

Aidha, kutoka katika kapu, nafasi 18 wapo baadhi ya wabunge wa zamani walioanguka katika kura mikoani kama Janeth Masaburi; Aziza Sleyum Ally; Esther Nyawazwa na Florence Kyendesya; na wanawake maarufu kama Asha Baraka; Sifa Swai na Rukia Masasi.

Friday, August 13, 2010

Panga lafyeka wagombea

-Baadhi ya viongozi CCM wahongwa magari
-Dar baadhi ya walioshinda wakatwa majina-
-Arusha, Mbeya na Shy mambo shaghalabaghala

WAKATI baadhi ya wanasiasa walioshindwa kura za maoni ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ngazi ya ubunge na udiwani, wakitajwa kujiunga na upinzani, tayari chama hicho tawala kimeanza mchakato wa kuwakata wagombea wake wakiwamo baadhi walioshinda kura za maoni, Raia Mwema limeelezwa.

Habari za ndani ya vikao vya CCM zimeeleza ‘panga’ limeanza katika ngazi ya mikoa na tayari halmashauri za chama hicho katika baadhi ya mikoa zimemaliza kazi ya kuwachuja wagombea na kupeleka taarifa hizo kwenye vikao vya juu.

Kwa mujibu wa habari hizo ambazo gazeti hili limezipata, baadhi ya wagombea waliokatwa katika vikao hivyo wamerudishwa baada ya kubainika kuwapo kwa nguvu kubwa ya fedha katika kushinikiza uamuzi wa vikao hivyo hali inayoashiria kuenea kwa uoza katika mchakato wa kuwapata wagombea.

Wakati hayo yakijiri, habari za uhakika zinaeleza kwamba baadhi ya wagombea hao wa CCM wametumia fedha nyingi katika kuhakikisha wao na watu wanaowaunga mkono wanapitishwa akiwamo kiongozi mmoja anayetajwa kuhongwa gari mkoani Dar es Salaam kwa lengo la kuhakikisha anatekeleza matakwa ya mgombea mmoja mwenye malengo ya kushika nafasi mojawapo ya juu mkoani humo.

Kwa mujibu wa habari hizo, mgombea huyo (ambaye pamoja na aliyepewa gari kwa sasa hatutawataja) ametumia fedha nyingi katika kuhakikisha anasimika viongozi katika karibu kila kata za mkoa anakotoka na wengi kati ya hao akiwa anawafadhili na kuwasimamia katika kuhakikisha wanapitishwa na vikao vyote vya CCM kuanzia ngazi za wilaya, mkoa hadi Taifa.

Maeneo mengi mkoani humo yalishuhudia si tu vurugu bali pia aibu ya kwamba baadhi ya viongozi wamehusika moja kwa moja kuvuruga uchaguzi katika baadhi ya maeneo kwa maslahi binafsi, baadhi wakielezwa kukiri hadharani kwamba walihongwa na baadhi ya wagombea na watu wazito wenye maslahi katika uchaguzi wa mwaka huu.

Tayari kumeibuka malalamiko kadhaa katika mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara (soma pia ukurasa wa 4 [Kanda ya Ziwa], ukurasa wa 5 [Kanda ya Kaskazini] na ukurasa wa 6 [Kanda ya Kusini]) na Visiwani ambako baadhi ya wagombea wakiwamo wabunge waliomaliza muda wao na wagombea wapya, wamelalamikia kuwa kiwango kikubwa cha ukiukwaji wa taratibu na matumizi makubwa ya fedha.

Taarifa zaidi za kiuchunguzi na ambazo hivi karibuni zimethibitishwa na uongozi wa juu wa CCM kitaifa, zinabainisha kuwa si rufaa zote za wagombea zitapatiwa ufumbuzi, ishara zikionyesha baadhi ya wagombea wanaweza kukataliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kushirikiana na Msajili wa Vyama vya Siasa ambao wanapewa nafasi kufanya hivyo na Sheria ya Gharama za Uchaguzi.

Kanuni za Sheria hiyo mpya ya Gharama za Uchaguzi inatoa nafasi kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuzingatia taarifa za utafiti kutoka kwa Msajili wa Vyama Vya Siasa, kugoma kuteua majina yaliyowasilishwa na chama husika kugombea uongozi kama itabainika mhusika amekiuka sheria hiyo, ikiwa ni pamoja na kuhusika katika vitendo vya rushwa.

Nguvu hizo alizopewa Msajili wa Vyama vya Siasa zilipingwa na baadhi ya wabunge na wanasiasa ndani ya CCM kwa madai kuwa zinaingilia shughuli za vyama vya siasa na kwamba ni vema uamuzi wa nani agombee ukaachwa katika chama husika cha siasa kama chombo cha mwisho.

Mazingira ya nguvu za Sheria ya Gharama za Uchaguzi yanajidhihirisha kutaka kutumika na tayari hivi karibuni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, alikemea namna matumizi ya rushwa yaliyojitokeza katika kura za maoni za CCM akieleza kuwa atashangaa kama chama hicho kitawapitisha wanaotuhumiwa kuhusika na tatizo hilo.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa, ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ndogo ya nidhamu ya chama hicho, amethibitisha kuwa si rufaa zote zitakazoweza kusikilizwa kutokana na wingi wake na muda wa kufanya hivyo kuwa mfupi lakini akiahidi kuwa uamuzi utaendelea kufanyika na ikibidi wagombea walioshinda kwa mchezo mchafu kuenguliwa bila kujali kama wakati wa uteuzi kwa maana ya Tume ya Uchaguzi na CCM kwenyewe umepita.

Msekwa alitoa maelezo hayo Jumatatu wiki hii na kunukuliwa na gazeti la CCM, Uhuru, akisema wataendelea kuyafanyia kazi (malalamiko) hata baada ya uteuzi wa wagombea na adhabu zitatolewa hata kama mtuhumiwa ameshinda ubunge au udiwani na kwamba watendaji wa chama hicho waliozembea na kuvuruga uchaguzi pia wataadhibiwa.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwenye majimbo mbalimbali ya uchaguzi nchini ambako CCM imeendesha mchakato wa kura za maoni, kuna taarifa kuwa mbali na TAKUKURU kukusanya ushahidi na wakati mwingine kulazimika kukamata na kuwahoji baadhi ya wagombea, baadhi ya maofisa wa Serikali walikuwa wakifuatilia nyendo za wagombea katika kinachoelezwa kuwa walikuwa wakikusanya taarifa huru za mwenendo wa kura hizo za maoni. Taarifa hizo zinaaminika kuwasilishwa katika baadhi ya vyombo vya dola na kulinganishwa na zile za maofisa wa TAKUKURU.

Katika hatua nyingine, baadhi ya wasomi wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, wamepongeza utaratibu wa CCM kuwapa wanachama wake nafasi ya kupiga kura za kupendekeza wagombea wakisema hali hiyo kwa sehemu kubwa imesaidia kufichua viongozi wasio na maadili mbele ya jamii.

Kati ya wasomi hao ni Profesa Samuel Mushi ambaye anasema: “Nawapongeza CCM kuamua mchakato wa kura za maoni kufanywa kwa uwazi. Ni uamuzi ambao umetuwezesha kubaini ule uchafu ambao ungeweza kufichwa chini ya zulia. Ni sawa na mtu anaweza kufagia na kuficha uchafu kwenye kapeti akijidai nyumba yake safi.”

Akizungumza na katika mahojiano ya simu na Raia Mwema wiki hii, Profesa Mushi alisema rushwa si jambo jipya, bali ni la muda mrefu na limekuwa likizusha malalamiko mengi miongoni mwa wananchi akiweka bayana kuwa sasa nchi imedhihirika imeingia katika kile alichokiita danger zone (ukanda wa hatari).

“Kitendo hiki kilichojionyesha CCM si cha kufumbiwa macho hasa kwa upande wa wahusika, lakini CCM kama taasisi inapaswa kupongezwa kwa kuamua kuweka uwazi kwenye chaguzi zake. Ni kama vile kimechoka kuonekana kinafungamana na watoa rushwa. Lakini kikubwa kwa upande wa nchi ni kutambua kuwa sasa tupo kwenye danger zone na kwa hiyo ni lazima turejee nyuma kimaadili na kujisahihisha na kukataa wasiotaka kujisahihisha kuwa viongozi wetu.

“Vyombo vya dola lazima vionyeshe dhamira ya kutuondoa kutoka kwenye danger zone, vipiganie dhamira hiyo. Napenda kuipongeza TAKUKURU kwa hatua zake hizi za awali kushughulikia tatizo hili. Sheria zitumike kikamilifu,” alisema Profesa Mushi.

Alipoulizwa kuhusu wimbi la wafanyabiashara kuamua kupenya zaidi kwenye siasa huku kukiwa na mazungumzo ya kuandaliwa kwa muswada unaolenga kutenga siasa na biashara, alisema uamuzi wao huo unaendeleza kile kilichoanza kujitokeza tangu wakati wa Serikali ya Awamu ya Pili, baada ya kufa kwa Azimio la Arusha lililokuwa likipigania masharti na maadili ya uongozi.

“Tangu wakati ule walipoua Azimio la Arusha na kuanzisha Azimio la Zanzibar utaona kuwa nguvu huria ilichukua nafasi yake. Zilianza siasa za soko huria, matajiri walipata njia ya kushawishi na kuhakikisha mifumo ya sheria, kibiashara na hata mifumo ya kisiasa kulinda maslahi yao. Wakapata fursa baadhi wakitumia nguvu za fedha kupenya kwenye siasa kwenye uwaziri…kwa hiyo ni haki yao kwa kuwa mifumo ya sheria imebadilishwa.

“Tatizo kuwa na wimbi la wafanyabiashara linaweza kujitokeza tu pale utajiri wao wanapoamua kuutumia kununua kura za wananchi na kwa mantiki hiyo kununua haki ya wananchi,” alisema Profesa huyo ambaye alipata kushiriki kuandika machapisho mbalimbali yanayoonyesha jinsi soko huria lilivyokuwa soko holela kiasi cha kuvuruga maadili mema yaliyozingatiwa awali katika Azimio la Arusha.

Kwa upande wake, Profesa Haji Semboja, ambaye ni gwiji wa uchumi alizungumzia mchakato wa kura za maoni CCM akisema:

“Mimi natofautiana kidogo. Kama mchumi sitaki kuiita hii eti ni rushwa inayotishia uchumi…kwa nchi masikini kama Tanzania kilichofanywa na wagombea hawa wa CCM ni kama uwezeshaji.

“Tusiache kukabili tatizo kubwa zaidi na wote kujielekeza kwenye tatizo dogo na la mpito. Tukumbuke hii ni nchi yenye watu masikini na kwa hiyo kampeni wakati mwingine ni lazima zihusishe wagombea kujinadi kwa kuzingatia yale ambayo washindani wengine hawawezi kuwa nayo.

“Hakuna anayeweza kujinadi bila kuwa na uwezo wa kuwawezesha wananchi. Tofauti inayojitokeza ni kuzidiana uwezo tu kati ya washindani.””

Hata hivyo, alisema anasubiri kwa hamu kuona jinsi TAKUKURU watakavyoweza kusimamia Sheria ya Gharama za Uchaguzi mara baada ya kampeni kuanza kwa kuwa kwa wakati huo matumizi ya fedha kwa sehemu kubwa yatakuwa yakifanywa na chama cha siasa badala ya mgombea mmoja mmoja, na kwamba inavutia zaidi kuona kama chombo hicho kitakuwa na ubavu wa kudhibiti vyama vyote kwa usawa, kikiwamo CCM.

Lakini akizungumzia kuhusu vigogo walioanguka alisema; “Lakini ieleweke kuwa kwa wale ambao hawakupita si kwamba hawatakiwi au hawawezi bali kilichotokea ni wapiga kura za maoni katika maeneo husika kutaka mabadiliko ya kiongozi au viongozi.

Thursday, August 12, 2010

Mungai kizimbani

WAZIRI wa zamani katika Serikali ya Tanzania, Joseph Mungai jana alipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Mkoa mjini Iringa , kujibu mashitaka ya kutoa rushwa wakati wa kinyang’anyiro cha kura ya maoni katika Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Mungai anakabiliwa na mashitaka 15 ya utoaji rushwa kwa wapiga kura wa CCM wa kata ya Ihalimba katika jimbo la Mufindi Kaskazini.

Imedaiwa kuwa mwanasiasa huyo alitoa rushwa wakati akitafuta ridhaa ya wapiga kura wa CCM wa jimbo la Mufindi Kaskazini ili wamchague kwa mara nyingine kugombea ubunge wa jimbo hilo ambalo ameliongoza kwa miaka mingi.

Katika kura hizo za maoni, Mungai alishika nafasi ya pili kwa Kupata kura 3,430 dhidi ya kura 6,386 zilizompa ushindi Mahamud Mgimwa katika kinyang’anyiro hicho kilichokuwa na wagombea sita.

Kesi hiyo iliyofunguliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inamuunganisha pia Moses Masasi aliyetajwa kwamba ni Mhasibu na Fidel Cholela ambaye ni Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM kata ya Mafinga.

Mungai alikana mashitaka na kurudishwa rumande na watuhumiwa hao wengine kusubiri taratibu za dhama ambapo walihitajika wadhamini wawili kwa kila mmoja.

Mbele ya Hakimu Mkazi, Mary Senapee, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Prisca Mpeka, alidai kuwa Mungai na wenzake walitoa rushwa kwa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Kata ya Ihalimba waliokuwa na kikao Julai 8, mwaka huu kwenye ofisi ya CCM ya kata ya Ihalimba, ili wampigie kura ya maoni.

Alidai kwamba Mungai na watuhumiwa hao wanadaiwa kutoa Sh 10,000 kwa Obadia Mtokoma ambaye ni Mwenyekiti wa CCM wa tawi la kijiji cha Vikula na Katibu wa Uchumi na Fedha wa tawi la CCM la kijiji cha Vikula, Konjeta Kiyeyeu ambaye pia alihongwa Sh 10,000.

Wengine kwa mujibu wa Mpeka na kiasi cha fedha walichopewa kwenye mabano, ni pamoja na Katibu wa CCM wa Kata ya Ihalimba, Aldo Lugusi (Sh 10,000), Mwenyekiti wa CCM wa Ihalimba, Ezekiel Mhewa (Sh 10,000) na Katibu wa Fedha na Uchumi wa CCM Ihalimba, Tulaigwa Kisinda (Sh 10,000).

Wengine ni Jiston Mhagama (Sh 10,000), Maria Kihongozi (Sh 20,000), Lurent Mdaligwa (Sh 5,000), Victory Kalinga (Sh 20,000), Francis Chonya (Sh 2,000) na Alfred Kisinga (Sh 2,000).

Waliohongwa wengine kwa mujibu wa mashitaka, ni Issac Tewele (Sh 2,000), Sosten Kigahe (Sh 10,000), Raphael Lutomo (Sh 10,000) na Andrew Mkiwa (Sh 20,000). Wanakabiliwa na jumla ya mashitaka 15 ya rushwa.

Pamoja na kukana mashitaka hayo, watuhumiwa hao walishindwa kukamilisha kipengele cha dhamana mara moja, na hadi tunakwenda mitamboni walikuwa bado rumande wakisubiri kukamilisha kipengele hicho.

Akitoa masharti ya dhamana kwa watuhumiwa hao, Senapee alisema kila mtuhumiwa anatakiwa kuwa na wadhamini wawili, na kila mmoja akiwa na Sh milioni tano na mmoja wao lazima awe mkazi wa hapa.

Mpeka alisema pia kuwa mwana CCM mwingine Fredrick Mwakalebela, ambaye naye anatuhumiwa kujihusisha na rushwa wakati wa kampeni hizo Iringa Mjini, atafikishwa mahakamani Agosti 17 mwaka huu, baada ya kushindwa kutokea jana kwa kilichoelezwa kwamba ana udhuru.

Wakati huo huo, Kamanda wa Takukuru wa Mkoa wa Iringa, Donasian Kessy aliwaambia waandishi wa habari kwamba katika kesi inayomkabili Mungai wana CCM wanaotuhumiwa kupokea rushwa hizo, watafikishwa mahakamani hapo kama mashahidi kwa sababu ndio walioisadia Takukuru kupata taarifa hiyo.

Kessy alisema pamoja na washitakiwa hao kufikishwa mahakamani alisema suala la kuwaengua kushiriki uchaguzi ni la Msajili wa Vyama vya Siasa ambaye kabla ya kufanya hivyo ni lazima ajiridhishe na tuhuma.

Alisema pamoja na kwamba Takukuru inatambua kuwa katika kesi hizo kuna kushinda au kushindwa, endapo watashindwa hilo halitakuwa kosa la chombo hicho cha Dola.