Wednesday, December 22, 2010

Tibaijuka ‘ang’ata’ usiku

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, aliposema atahakikisha watu waliojenga kwenye maeneo ya wazi na yasiyoruhusiwa wavunje wenyewe majengo yaliyopo, hakuwa anatania na wale waliokuwa wakimvimbishia kichwa, watakuwa wamekosea.

Hali hiyo ilidhihirika jana jioni wakati tingatinga la Halmashauri ya Manispaa ya Ilala mkoani Dar es Salaam, lilipofanya kazi ya kuvunja maeneo ambayo yameanza kujengwa majengo kinyume cha utaratibu na ambayo inaaminika kuwa ni ya wazi au hayaruhusiwi majengo hayo.

Jana majengo mawili katika Jiji la Dar es Salaam, kiwanja kilichopo karibu na Hoteli ya Palm Beach, ambacho ndio kwanza kilikuwa kimepandishwa ukuta pamoja na ukuta mwingine uliojengwa jirani na Hospitali ya Aga Khan katika Barabara ya Ocean Road, vilivunjwa jana jioni na askari wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala.

Licha ya mmiliki wa kiwanja cha jirani na Hoteli ya Palm Beach, Taher Muccadam kutoa notisi ya siku saba kwa Waziri Profesa Tibaijuka amuombe radhi na kumlipa fidia ya Sh bilioni mbili kwa madai kwamba alimvunjia heshima kwa jamii vinginevyo atamfikisha mahakamani, agizo hilo limepuuzwa.

Badala yake, umma wa wakazi wa Dar es Salaam waliokuwa wakirejea majumbani mwao jana jioni, walishuhudia tingatinga la Manispaa ya Ilala, lenye namba SM 3937, chini ya ulinzi mkali, likifanya kazi ya kuangusha ukuta huo saa moja jioni kabla ya kuhamia ukuta wa jirani na Aga Khan nusu saa baadaye.

Kazi hizo mbili zilifanywa na tingatinga hilo chini ya ulinzi wa askari zaidi ya 50 waliokuwa katika magari mengine manne, Isuzu; Toyota Land Cruiser Hard Top, Toyota Double Cabin na Toyota Nissan Patrol yenye namba za usajili SM 3096, SM 4360 na STJ 5662, mali ya Manispaa ya Ilala.

Mara baada ya kazi hiyo kukamilika katika eneo la Palm Beach, wananchi waliokusanyika kushuhudia tukio hilo, baadhi yao walisikika wakisema, “huyu ndiye Waziri, siyo viongozi wababaishaji. Watu wanamtisha eti wana vibali kutoka Ikulu, yeye aliwambia hatishiki na vibali vyao.”

Mwingine alisema, “huyu mama (Profesa Tibaijuka) hana mchezo, kama fedha anazo za kutosha, hasumbuliwi na vijisenti…tunahitaji viongozi wenye kusimamia sheria nchini mwetu.”

Mmoja wa viongozi waliosimamia kazi hiyo, hakutaja kutaja jina lake wala kueleza hatua hiyo imefikiwa na nani, akisema, “hatupo hapa kuongea na vyombo vya habari. Kazi mnaiona.”

Kiwanja hicho cha Palm Beach ambacho ni namba 1006 ni kati ya viwanja ambavyo Profesa Tibaijuka alidai kuwa ni cha wazi na kwamba hakiruhusiwi kuwa makazi.

Hivi karibuni, Profesa Tibaijuka akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam aliwataka wananchi waliopora viwanja na maeneo ya wazi nchini na kujenga, wajisalimishe kwa mazungumzo, kwa sababu huenda wakaokoa hata matofali kabla hatua zaidi hazijachukuliwa.

Fedha za kashifa ya rada kurejeshwa Tanzania

KAMPUNI kubwa ya ulinzi ya Ulaya, BAE Systems, imekubali kuilipa Serikali ya Tanzania fidia ya Sh bilioni 67.29 (pauni milioni 30) kama walivyokubaliana na Taasisi ya Kuchunguza Makosa makubwa ya jinai ya Uingereza, SFO, ikiwa ni sehemu ya kumaliza shauri lililokuwa linawakabili mahakamani.

Kauli hiyo imetolewa baada ya kampuni hiyo kuhukumiwa kulipa faini ya pauni 500,000 au dola za Marekani 775,000, sawa na Sh bilioni 1.12 baada ya kukiri kosa la ‘kushindwa kuweka kwa usahihi kumbukumbu za manunuzi.’

Viwango vya ubadilishaji kwa siku ya jana kwa mujibu wa Benki Kuu ni pauni moja sawa na Sh 2,243 wakati dola moja ni Sh 1,442.

Kampuni hiyo imesema kwamba kwa sasa inaangalia utaratibu wa malipo hayo ikiwa ni sehemu ya fedha zilizolipwa na Serikali ya Tanzania kununua rada hiyo ya kisasa.

Mpango huo ulikuwa na thamani ya dola milioni 40 sawa na pauni milioni 28. Mahakama ilitoa hukumu hiyo kwa kuzingatia shauri la kutoweka taarifa vyema.

Suala la kutoa mlungula ambalo awali lilitawala uchunguzi wa SFO halikufikishwa mahakamani.

Jaji David Bean alisema itakuwa ni kuukataa ukweli kufikiri kuwa wakala wa BAE nchini Tanzania, Shailesh Vithlani, alilipwa mamilioni ya dola eti kwa sababu tu anajua kuunganisha vyema masuala ya biashara.

BAE ilikubali kwamba inawezekana kwamba sehemu ya dola milioni 12.4 (waliyomlipa Vithlani) ilitumika kwa ajili kuisaidia kupata zabuni hiyo.

Hata hivyo waendesha mashtaka wamesema kwamba ni vigumu sana kuweza kujua Vithlani alifanya nini na fedha hizo na wala kuthibitisha kwamba sehemu ya fedha hizo zilitumika vibaya.

Kwa mujibu wa maelezo fedha hizo zililipwa kwa kampuni za Vithlani za British Virgin Islands na Kampuni ya Merlin iliyosajiliwa Tanzania.

Kampuni ya BAE imesema kwamba imefurahishwa na shauri hilo kumalizwa na kwamba inaandaa utaratibu wa kuilipa Tanzania fedha zake.

Hukumu hiyo iliyotolewa jana na Jaji David Bean mjini London inahitimisha miezi sita ya uchunguzi wa kina wa shauri hilo.

BAE ilikiri kosa hilo la kushindwa kutunza vyema kumbukumbu za manunuzi mwezi uliopita katika mpango wake na Taasisi ya Kuchunguza Makosa makubwa ya jinai ya Uingereza, SFO.

Kampuni hiyo iliridhia Februari kulipa pauni milioni 30 kama sehemu ya fidia na waendesha mashitaka walisema wangekubaliana na BAE ikiwa wangelipa faini hiyo na kutuma ‘chenji’ kwa Serikali ya Tanzania.

Kampuni hiyo ilikuwa katika uchunguzi nchini Uingereza kuanzia Novemba, 2004 kwa tuhuma za kutoa rushwa ili kushinda zabuni za manunuzi katika nchi sita ikiwamo Tanzania na Jamhuri ya Czech.

Februari mwaka huu BAE ilikubali kulipa karibu dola za Marekani milioni 450 kama fidia ili kumaliza shauri hilo baina yake na SFO na waendesha mashitaka wa Marekani.

Hata hivyo, BAE ililipa dola za Marekani milioni 400 kwa Marekani na kukiri kosa la kutoweka taarifa sahihi ya manunuzi hayo. Kampuni hiyo ilikanusha kutoa rushwa.

“Jukumu langu ni kufikisha kesi mahakamani na kuhakikisha kuwa Jaji anatoa adhabu stahili,” alisema Mkurugenzi wa SFO, Richard Aderman baada ya hukumu.

Alisema ana uhakika kuwa BAE itatekeleza makubaliano yaliyofikiwa ya kuilipa Serikali ya Tanzania ‘chenji’ ya pauni milioni 30 (zaidi ya Sh bilioni 60), baada ya kulipa faini nchini Uingereza.

Wakili aliyekuwa akiitetea BAE, Arno Chakrabarti, alikataa kusema chochote baada ya hukumu hiyo.

Shauri hilo la rada lililoelezwa kufanywa na mfanyabiashara Shailesh Vithlani ambaye alihusika katika mpango huo kuinufaisha BAE, pia limemhusisha aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge ambaye amekuwa akitajwa kuwa mmoja wa wahusika wa kashfa hiyo.

Tuesday, December 21, 2010

Hoseah akanusha uvumi wa Wikileaks

TAARIFA zilizovuja za mtandao wa Wikileaks, ambazo zilizotoka kwa Serikali ya Marekani, zimemgusa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru), Dk. Edward Hoseah, na kwa haraka, amekanusha kuwa Rais Jakaya Kikwete amekuwa ni kikwazo cha utendaji wa taasisi hiyo, kama alivyonukuliwa humo.

Dk. Hoseah, anadai katika taarifa za mtandao huo zilizoripotiwa jana na gazeti la The Guardian la Uingereza kueleza kuwa Rais Kikwete alikuwa anakwamisha kuchunguzwa kwa vigogo wa serikali wanaotuhumiwa kwa vitendo vya rushwa, na pia madai kuwa anahofia maisha yake kama Mkuu wa Takukuru.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Dk. Hoseah anakiri kukutana na ofisa wa Marekani ofisini kwake Julai 2007, lakini katika mazungumzo yake, anakanusha kuwa hakuna mahali popote alipoeleza kuwa Rais Kikwete alikuwa hataki sheria ichukue mkondo wake katika kuwachunguza vigogo wanaotuhumiwa kwa rushwa.

“Nilichosema ni kwamba Rais hataki kuruhusu uchunguzi wa maofisa waandamizi wa serikali au mtu yeyote yule kufanywa kwa kuegemea katika minong’ono au ushahidi dhaifu, kwa sababu kwa kufanya hivyo, serikali inaweza kuwa katika hatari ya kulipa fidia kubwa kama watuhumiwa watashinda kesi mahakamani,” alidai Dk. Hoseah katika taarifa yake jana.

Kuhusu madai ya ‘hofu ya maisha yake’, alisema anakumbuka kuulizwa na ofisa huyo kama anahofia uhai wake au la, akiwa ni Mkuu wa Takukuru, na kwamba jibu lake lilikuwa rahisi, “ndio, wakati unaposhughulika na vigogo au matajiri, ni lazima uwe mwangalifu na tahadhari na maisha yako.”

“Lakini hakuna mahali popote nilipotamka kuwa nina mpango wa kukimbia nchi kwa sababu maisha yangu yalikuwa hatarini. Ni jambo la kushangaza kwa mara nyingine, Ofisa huyo wa Ubalozi wa Marekani amenikariri kinyume na ukweli na sijui nia yake hasa ilikuwa nini.”

Dk. Hoseah alisema kupokea vitisho ni sehemu ya kazi yake kwa sababu anawachunguza watu matajiri na wenye nguvu, lakini kwa kuwa kila kitu kinafanyika kulingana na sheria iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, “hakuna cha kuhofia sana kwa sababu kila kitu kiko katika sheria.”

Aliihakikishia jamii kwamba ingawa kazi yao ni ngumu, wataendelea na dhamira yao ya kupambana na rushwa katika ngazi zote kwa kushirikiana na wadau wote nchini.

“Tunaamini kwa pamoja tutashinda vita hii, lakini tukigawanyika, itakuwa kazi ngumu kufikia dhamira yetu.”

Mgawo waanza tena, bei ya umeme juu

WAKATI Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), ikiamuru wafanyakazi takribani 5,000 wa Tanesco kulipa viwango sawa vya bei za umeme kama ilivyo kwa wananchi wengine, na ikiridhia kupandisha bei ya umeme kuanzia Januari mosi, mgawo wa umeme unaanza tena leo.

Mgawo wa umeme uliositishwa wiki moja iliyopita, umetangazwa jana mjini Kilwa mkoani Lindi ikiwa ni kutokana na Kampuni ya Pan African Energy inayozalisha gesi asili katika kisiwa cha Songosongo kupunguza uzalishaji kwa ajili ya kufanyia matengenezo kisima kimoja kati ya vitano ilivyonavyo.

Mahitaji ya matengenezo ya kisima hicho yaligundulika Septemba mwaka huu.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Felchesmi Mramba alisema Tanesco imelazimika kuanza tena mgawo tena kutokana na upungufu wa megawati 40, akisema “tunalazimika kupunguza uzalishaji katika mtambo wa Ubungo ambapo baada ya kuzalisha umeme wa megawati mia moja, sasa tutalazimika kuzalisha megawati 60, na ratiba tutartoa baada ya kuipanga.”

Mramba alitangaza mgawo huo mbele ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja wakati alipotembea Kilwa Kisiwani kunakozalishwa gesi asilia kwa ajili ya kuiuzia Tanesco na Kampuni ya Songas.

Akitoa taarifa kuhusu kukifanyia matengenezo kisima hicho, Naibu Meneja Mkuu wa Pan African Energy, William Chiume alisema kutokana na matengenezo hayo, watapunguza uzalishaji kwa asilimia 16 kutoka futi za ujazo milioni 86 hadi 76, ambazo ni sawa na megawati 40.

Alisema matengenezo hayo yatachukua kati ya wiki nne na tano kuanzia sasa. Hata hivyo, alisema waathirika wakubwa ni Tanesco, kwani Songas wataendelea kupata gesi kutokana na mkataba walionao. Songas pia wanaiuzia umeme Tanesco.

Songas inaiuzia Tanesco megawati 182 za umeme kwa siku na wakati mitambo ya Tegeta inazalisha megawati 45, Ubungo megawati 100, yote ya gesi asili wakati mahitaji ni megawati 833 kwa siku.

Wakati mgawo huo ukitangazwa Kilwa, jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Ewura, Haruna Masebu alitoa uamuzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Ewura wa maombi ya Tanesco ya kubadilishiwa bei za umeme, na kueleza kuwa Bodi imekubali ombi hilo na imepandisha bei ya umeme kwa asilimia 18.5 kuanzia Januari mosi.

Masebu alisema wafanyakazi hao wamekuwa wakilipia viwango maalumu, hivyo Bodi imeamuru walipe kama ambavyo wananchi wengine wanalipia na endapo hawatotekeleza itaonekana wakati wa ukaguzi.

Akifafanua zaidi, Mkurugenzi wa Umeme wa Ewura, Anastas Mbawala alisema wafanyakazi wa Tanesco wanakadiriwa kufikia 5,000 na wamekuwa wakilipa Sh nne kwa kila uniti ya umeme, ingawaje kwa wale ambao ni mke na mume, alikuwa anapewa mmojawapo na sio wote.

Kuhusu bei ya umeme, Masebu alisema maombi ya Tanesco yalitolewa Mei 28, mwaka huu na mchakato ulianza mara moja wa kukutana na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili kwa kina suala hilo ili kila mmoja aridhike na hatua zitakazofuatia.

Masebu alisema mikutano ilifanyika Agosti katika mikoa ya Mwanza, Mbeya, Kilimanjaro, Tabora na Dar es Salaam, na kwamba “baada ya kukutana na wadau mbalimbali na kujadili kwa kina suala la kubadilishiwa bei hizo, Ewura iliona kuna hoja ila hawawezi kukubali maombi hayo kama yalivyoletwa na Tanesco.”

Alisema Tanesco waliomba kuwe na mpangilio wa kubadilisha bei ya umeme kwa miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka 2011 kwa asilimia 34.6, asilimia 13.8 na asilimia 13.9 ili waboreshe huduma zao na kuwa endelevu wakati wote.

Kadhalika alisema Tanesco waliomba pia mabadiliko hayo yaende pamoja na kuwa na uwezo wa kurekebisha viwango vya umeme wakati wowote, kuruhusiwa kubadilisha bei ya umeme katikati ya kipindi hicho kulingana na mabadiliko ya bei za mafuta na kubadilika kwa viwango vya umeme kadri ya matumizi.

Alisema ni kweli Tanesco wanahitaji zaidi ya Sh bilioni 691 ili itoe huduma endelevu, hivyo Ewura imekubali ombi lao kwa asilimia 18.5 ikiwa ni pungufu ya asilimia 16.1 huku gharama nyingine kutokubaliwa hadi hapo watakapopata mtaalamu mshauri atakayefanyia kazi suala hilo na kuona kama viwango hivyo vinafaa.

Alisema kwa marekebisho hayo, bei ya umeme kwa watumiaji wadogo wanaotumia umeme usiozidi kilowati 50 watalipia Sh 60 kwa kila uniti kutoka Sh 49 za awali huku watumiaji wa kawaida watalipia Sh 157 kutoka Sh 129.

Kuhusu kufungua akaunti maalumu, alisema baada ya kukusanya fedha hizo za viwango vipya, Tanesco wanatakiwa kufungua akaunti ya fedha hizo na kuagiza kuwa zielekezwe katika kazi husika ambapo Ewura watakuwa wakikagua kila baada ya miezi mitatu.

Masebu alisema kutokuwakubalia Tanesco kupandisha umeme wasingekuwa na uwezo wa kujiendeleza na vilevile hatua hiyo inatoa nafasi kwa wawekezaji wengine kujiingiza katika sekta hiyo.

Monday, December 13, 2010

Chadema wamtambua Kikwete

JAKAYA Kikwete aliwaambia viongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwamba hawana mwingine wa kumlilia kwa masuala yao, isipokuwa yeye; na kwamba watakwenda na kurudi kwake kwa sababu yeye ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Rais Kikwete alitoa kauli hiyo Novemba 18, mwaka huu ndani ya Ukumbi wa Bunge mjini Dodoma wakati akihutubia Mkutano wa Kwanza wa Bunge la 10,na sasa aliyoyasema yametimia.

Baadhi ya wabunge wa Chadema walitoka katika ukumbi wa Bunge wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe walitoka nje mara tu Rais Kikwete alipoanza hotuba yake, sasa wamekubali yaishe. Wanamtambua ndiye Rais halali wa Tanzania.

Lakini katika kauli iliyowalenga moja kwa moja wabunge wa Chadema wakati akimalizia hotuba yake bungeni, Rais Kikwete alisema wabunge hao hawana wa kumlilia zaidi yake, kwani yeye ndiye Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Watakwenda watarudi, hawana mwingine wa kumlilia kwa yao, isipokuwa Serikali ya CCM ambayo mimi ndiye Rais wake; Dk. Mohammed Gharib Bilal ndiye Makamu wake. Serikali ambayo Dk. Ali Mohammed Shein ndiye Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad ni Makamu wa Kwanza wa Rais na Balozi Seif Ali Idd ni Makamu wa Pili wa Rais,” alisema Rais Kikwete, Novemba 18, mwaka huu na kushangiliwa na wabunge.

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho katika siku za karibuni, kilitangaza kutomtambua Rais Jakaya Kikwete, kimebadili msimamo.

Kimekubaliana kwamba Kikwete ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kinatarajiwa siku yoyote kuanzia leo kutangaza maazimio ya Kamati Kuu iliyokutana mwishoni mwa wiki Dar es Salaam, ambayo moja ya maazimio yake, ni kumtambua kiongozi huyo wa nchi.

Kamati Kuu ya Chadema pia imeamua kusitisha uamuzi wa wabunge wa chama hicho kwa kumvua nafasi ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, mbunge mwenzao, Kabwe Zitto wa Kigoma Kaskazini.

Baada ya Rais Kikwete kutangazwa mshindi wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu, Chadema ilikataa kumtambua, ikidai alichaguliwa kutokana na uchaguzi uliokuwa na udanganyifu.

Novemba 18, mwaka huu, wakati akianza hotuba ya kulihutubia Bunge jipya mjini Dodoma, baadhi ya wabunge wa Chadema waliokuwa ndani ya ukumbi wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe, walitoka nje ya ukumbi huo.

Lakini sasa, vyanzo vya habari kutoka ndani ya Kamati Kuu ya Chadema, vimeliarifu gazeti hili kuwa wamekubaliana kumtambua Rais Kikwete baada ya mjadala mzito na baada ya kupima athari za kutomtambua Rais Kikwete aliyeshinda kwa zaidi ya asilimia 60.

Kuhusu suala la Zitto, chanzo hicho cha habari, kilieleza kuwa wajumbe wakongwe wa Kamati Kuu walimtetea na kueleza kuwa mbunge huyo machachari hakupewa nafasi ya kujitetea.

Wabunge wa Chadema walikutana Bagamoyo wiki iliyopita na kupiga kura ya kutokuwa na imani na Zitto, wakimtuhumu kwa kwenda kinyume cha msimamo wa chama hicho wa kumsusa Rais Kikwete bungeni.

Zitto hakupatikana kuzungumzia hatua hiyo mpya ya chama chake jana, kwa sababu simu yake iliita bila kupokewa, ikiwa ni siku moja baada ya kutoka Hospitali ya Aga Khan ambako alikuwa amelazwa tangu Alhamisi iliyopita, kwa kusumbuliwa na maumivu ya tumbo, ikidaiwa alikula chakula chenye sumu.

Kutokana na kuchafuka kwa hali ya hewa ndani ya chama hicho, Kamati Kuu iliamua pia kuunda kamati maalumu ya watu wanne ikiongozwa na Profesa Mwesiga Baregu, kwa nia ya kurejesha amani kundini.

Kamati hiyo kwa maudhui, inafanana na ile iliyoundwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), Juni mwaka huu, ikiongozwa na Rais mstaafu Alhaj Ali Hassan Mwinyi kupatanisha makundi hasimu yaliyokuwa yameibuka ndani ya wabunge wake.

Alipoulizwa kuhusu kamati hiyo, Profesa Baregu alithibitisha na kueleza kuwa Kamati yake imepewa jukumu la kuhakikisha amani inarejea katika chama hicho.

“Ndiyo, kuna kamati maalumu inayowahusisha wajumbe wakongwe wa Kamati Kuu iliyoundwa kwa ajili ya kuhakikisha umoja na amani zinarejea katika chama,” alisema Profesa Baregu.

Alisema kurejeshwa kwa umoja na amani katika chama hicho, pia kutahakikisha umma haupotei imani yao kwa chama hicho cha upinzani.

“Tutazungumza na wanachama ambao wana malalamiko au wana matatizo, ili kumaliza tofauti zao na kurejesha tena mshikamano, amani na upendo katika chama…hatutaki kupoteza imani ya umma kwetu,” alieleza Profesa Baregu.

Wajumbe wengine wa kamati hiyo ni Shida Salim ambaye ni mama mzazi wa Zitto, Kitila Mkumbo ambaye ndiye Katibu na mjumbe mwingine aliyetajwa kwa jina la Shilungushela.

Katibu Mkuu wa Chadema, alikataa kuzungumzia maazimio hayo jana alipotafutwa kwa simu, lakini akaeleza kuwa watakuwa na mkutano na waandishi wa habari kesho.

Friday, December 10, 2010

RAIS KIKWETE AMTEUA JAJI MSTAAFU SALOME SUZETTE KAGANDA KUWA KAMISHNA WA MAADILI YA VIONGOZI WA UMMA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemteua Jaji Mstaafu Salome Suzette Kaganda kuwa Kamishna wa Maadili ya Viongozi wa Umma.

Taarifa iliyotolewa Ikulu, Dar es Salaam, leo, Jumatano, Desemba 8, 2010, na Katibu Mkuu Kiongozi, Mheshimiwa Phillemon Luhanjo, inasema kuwa uteuzi huo ulianza Jumamosi, Desemba 4, 2010.

Jaji Mstaafu Salome Kaganda anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Jaji Mstaafu Stephen Ihema ambaye amemaliza muda wake.


Kabla ya kustaafu, Mheshimiwa Salome Suzette Kaganda alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Kusini, Songea.


Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

08 Desemba, 2010

Wednesday, December 8, 2010

MICHANGO YA KUANDIKISHA DARASA LA KWANZA

Tukumbuke kwamba wakati huu ni wakati wa kuandikisha watoto kwenda darasa la kwanza. na Serikali ya Tanzania inasema au tuseme sera ya elimu inasema kwamba elimu ya msingi ni bure. lakini sasa hivi inajitokeza kuwa kila mzazi anayekwenda kumwandikisha mtoto hasa katika shule ya Msingi Bryceson huko Mburahati jijini Dar es salaam kila mzazi/mlezi anayekwenda kuandikisha mtoto anadaiwa apeleke shilingi 22,400 ikiwa ni mchango wa madawati, mlinzi, na mengineyo lakini cha ajabu risiti hazitolewi.

Je uhalali uko wapi? Halafu hili suala la kutochangia kwa maana ya elimu ya msingi bure likoje mbona kama magumashi hivi????????

Najua tukifuatilia kuna mengi mno ambayo tunaweza kuibua. Kazi kwetu!!!

Tuesday, December 7, 2010

Waliokuwa CCJ waibukia CCK

CHAMA Cha Kijamii (CCK), kinaandaa waraka utakaochambua mapungufu ya Katiba ya sasa ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

CCK watauwasilisha waraka huo kwa Waziri wa Katiba na Sheria, ili kutoa hoja yao rasmi ya kwa nini Tanzania inahitaji kuwa na Katiba mpya.

Aidha, kimesema kinakusudia kushiriki katika kufungua au kuwa marafiki wa mahakama katika kesi za kikatiba zinazohusiana na masuala ya uchaguzi mkuu kwa madai kuwa si mambo yote yanaweza kumalizika au kubadilishwa kisiasa.

Mwenyekiti wa CCK, Constantine Akitanda, aliyasema hayo wakati wa mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam jana ambapo pamoja na mambo mengine, alisema wanaendelea kufuatilia usajili wa kudumu.

Akitanda alisema karibu asilimia kubwa ya matatizo yaliyojitokeza katika uchaguzi mkuu yalitokana na kiashirio cha kutokuwepo kwa Katiba mpya yenye kutengeneza mazingira mazuri ya uhusiano kati ya watawala na watawaliwa, na yote yanaweza kusahihishwa vizuri endapo Katiba itaandikwa upya.

“Kama tulivyosema hapo awali kuwa kuna haja ya Katiba mpya, na kwa kuzingatia kauli ya Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani kuwa hadi hivi sasa hakuna chama chochote kilichotoa madai rasmi ya hoja kuhusu Katiba mpya, sisi kama CCK tukizingatia nafasi iliyopo mbele yetu, tunaandaa waraka utakaochambua mapungufu hayo,” alifafanua Akitanda.

Kuhusu kushirikiana na mahakama katika kesi za kikatiba, alisema wameamua kufanya hivyo wakiamini kuwa mambo mengine katika suala hilo yanahitaji nguvu ya chombo hicho na watachukua njia hiyo wakati wowote wanapoiona njia hiyo ni bora.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa chama hicho, Renatus Muabhi, alisema wapo mbioni kufanikisha azma ya kupata usajili wa kudumu ili hatimaye na chenyewe kitoe mchango wake wa kifikra na kiuongozi nchini.

Friday, December 3, 2010

Taarifa ya Lowassa kuchunguzwa balaa

-Raia Mwema lapata msukosuko
-Nakala 10,000 zaharibiwa zisisomwe

HABARI iliyoihusisha familia ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, imeibua utata mkubwa baada ya kuibuka kwa vitisho vilivyosababisha kuzuiwa kuchapwa kwa gazeti la Raia Mwema toleo lililopita Namba 161 katika mazingira ya kutatanisha; huku habari hiyo ikikanushwa kwenye gazeti jingine hata kabla haijatoka.

Utata huo ulisababisha uongozi wa Imprint iliyopo chini ya kampuni ya Jamana Printers kusitisha ghafla kuendelea kuchapwa kwa gazeti la Raia Mwema ikiwa tayari limeshachapwa nakala 10,000 katika mazingira yaliyoonyesha kuwapo shinikizo zito kutoka kwa kigogo mmoja aliye karibu na mwanasiasa huyo la kutaka habari inayomhusu Lowassa iondolewe ndipo gazeti lichapwe.

Raia Mwema ambalo lina makubaliano maalumu na wachapaji hao lilishtushwa na uamuzi huo wa ghafla wa wachapaji hao hasa baada ya uamuzi huo kuambatana na hali ya woga mkubwa uliotawala wafanyakazi wa kiwanda hicho usiku wa Jumanne ya wiki iliyopita.

Taarifa ya Meneja Usambazaji wa Raia Mwema, Omari Mwendapole, ambaye alikuwapo usiku huo, inaeleza kwamba hali ya uchapaji iliendelea katika hali ya kawaida kuanzia saa 11 jioni kabla ya kubadilika ghafla saa 1:30 usiku, ilipotolewa amri ya kusitisha uchapaji wakati zikiwa zimekwishachapwa nakala 10,000.

“Tulifika kiwandani mapema saa 11:00 na hakukua tatizo lolote baada ya wahusika kukagua gazeti letu na kuridhika nalo na wakaanza taratibu zote ikiwa ni pamoja na kuchoma plate saa 11:15 na saa 12:00 kazi ya uchapaji ilianza taratibu hadi saa 12:30 mashine zilipoanza kuchanganya na kutoa gazeti zuri.

“Lakini baada ya muda kidogo, msimamizi wa uchapaji wa Imprint akaitwa na mlinzi kwenda kusikiliza simu na aliporejea akawaagiza mafundi wazime mashine kabla ya kuamua kuzima mwenyewe baada ya kuona wanachelewa kufanya hivyo.

“Baadaye niliitwa kwa bosi wao na kuambiwa natakiwa kwenda kwa Meneja Mkuu, aitwaye Shaber, ambako nilijulishwa kwamba ni lazima habari kuu (inayomhusu Lowassa) iondolewe vinginevyo gazeti halitochapwa kabisa,” anasema Mwendapole.

Kutokana na amri hiyo ya wachapaji, wafanyakazi wote wa Raia Mwema na watu wengine wote waliokuwamo kiwandani wakati huo waliamriwa kutoka eneo la uchapaji na kupekuliwa kuhakikisha hawabebi hata nakala moja ya gazeti hilo.

Habari zinasema kuwa nakala 10,000 ambazo tayari zilishachapwa ziliharibiwa chini ya uangalizi mkali wa maofisa wa kiwanda hicho ili kuhakikisha kuwa haziingii kwenye soko, na hivyo habari hiyo kusomwa na wananchi.

Hata hivyo, wakati uongozi wa Raia Mwema ukihangaika kutafuta mahali pengine pa kuchapa, ilibainika kwamba kigogo huyo pamoja na mbunge mmoja walikuwa tayari na nakala ya gazeti hilo na ilidhihirika siku iliyofuata baada ya gazeti la Mtanzania lenye uhusiano wa karibu na kigogo huyo kuchapisha habari iliyokanusha habari hizo kabla hata ya habari husika kuchapishwa.

Katika habari hiyo, gazeti hilo lilielezea kwamba kuna taarifa “zilizochapwa katika magazeti” huku zikimnukuu Frederick Lowassa, ambaye ndiye aliyekuwa mhusika mkuu katika habari ya Raia Mwema, akijitetea kwa kudai kwamba hakuwahi kusafirisha fedha nyingine Uingereza kama ilivyoandikwa na ‘magazeti hayo.’

Katika tukio hilo la aina yake katika tasnia ya habari, Frederick Lowassa, alisema;

“Jamani mimi nashangaa sana. Watu hawa wanasahau kuwa mimi ni mfanyabiashara kwa zaidi ya miaka kumi sasa. Na katika kufanya biashara ni lazima nisafirishe fedha nje ya nchi kwa nia ya kununua material (bidhaa). Nasafirisha fedha sehemu mbalimbali duniani, na sijui wameliokota wapi hilo.

“Hakuna wakati nimewahi kusafirisha paundi 495,000 nje ya nchi kwa mara moja, ila nasafirisha fedha nje ya nchi kununua bidhaa mara nyingi tu. Hili wanalozungumza la Uingereza ni kweli kati ya Machi na Aprili nilisafirisha kama Paundi chini ya 200,000 hivi, kwa ajili ya biashara kama kawaida. Benki kama kawaida walijiridhisha fedha hizo zilikotoka, tukawasiliana likaisha.

“Sasa nashangaa watu hawa hili wamelitoa wapi? Na ifahamike kuwa mimi nafanya biashara nyingi tu, na moja ya biashara zangu ni kampuni ya Alphatel. Sisi ni mawakala wa Vodacom. Tunover (mzunguko wa fedha) yetu kwa mwezi ni zaidi ya Sh bilioni 8.0. Hizi ni fedha zinazotumiwa kama sehemu ya mtaji na faida kwa kununua bidhaa na kuuza. Sasa walitarajia mfanyabiashara kama mimi nishindwe kutumia kiasi hicho nje ya nchi? Nanunua vitu kutoka Uingereza, China, Falme za Kiarabu (Dubai), Afrika Kusini, Italia na sehemu nyingine. Watu wa ajabu kweli hawa.

“Nasikitika jinsi wanavyoendelea kumchafua mzee wangu. Na ndio maana nimeelewa barua hiyo ya mwaka jana imeletwa leo wiki hii. Tayari nimewasiliana na mwanasheria wangu katika hili na nitatoa vielelezo vyote, hakuna cha kuficha…. Jamani siasa zao wazibakize huko, kazi waliyofanya kumchafua mzee wangu (Lowassa) hawajaridhika kweli? Katika hili nasema hapana.”

Habari hiyo ilifuatiwa na habari nyingine ambayo iliyomnukuu Lowassa mwenyewe akionyesha kwamba Lowassa anaandamwa na katika toleo hilo aligusia tena kuhusu mwanae Fredrick kuchukua hatua za kisheria kuhuhusiana na habari inayohusiana na usafirishaji fedha Uingereza. Habari hiyo imenukuliwa tena katika gazeti lingine jana.

Uongozi wa Raia Mwema tayari umeiandikia barua kampuni hiyo ya uchapaji ukilalamikia tukio hilo la kuzuia gazeti lisichapwe na kuharibu nakala ambazo tayari zilishachapwa, na pia kutoa usiku huo huo baadhi ya nakala za toleo hilo kwa watu wa nje bila idhini ya wamiliki wa gazeti. Pia unataka ulipwe fidia kwa hasara iliyopatikana kwani ililazimu gazeti kuchapwa kwingineko alfajiri, na hivyo kuchelewa kuingia sokoni.

Katika habari yake ya wiki iliyopita iliyoibua mambo yote hayo, Raia Mwema liliripoti kwamba Frederick Lowassa anachunguzwa na Kitengo Maalumu cha Polisi wa Kimataifa wa Uingereza wanaofuatilia utata wa uhamishaji fedha kutoka Tanzania.

Fedha hizo zinahusishwa na ununuzi wa nyumba yenye thamani ya pauni za Uingereza 475,000 (takriban Shilingi bilioni moja) katikati ya Jiji la London.

Hata hivyo, watu walio karibu na Frederick wameelezea kwamba kijana huyo hakuwahi kununua nyumba; bali aliwahi kutaka kupanga kwa ajili ya kuishi akiwa masomoni nchini Uingereza na fedha nyingine alizituma kwa ndugu yake aishie nchini humo.

Nyumba ambayo inatajwa katika maelezo ya awali iko mtaa wa Leinster Gardens, jijini London.

Hata hivyo, hakuna ofisa yeyote wa Serikali ya Tanzania aliyekuwa tayari kuzungumzia suala hilo, pamoja na kuwapo taarifa kwamba tayari vyombo vya dola vya Tanzania vimekwisha kuhusishwa katika uchunguzi huo.

Maofisa wa Polisi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (CID) wanaohusika na uchunguzi wa fedha haramu, wamekwepa kuzungumzia suala hilo na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Robert Manumba, hakuweza kupatikana, na alielezwa kuwa nje ya nchi kikazi.

Ofisa wa CID aliyeelezwa kuongoza kitengo kinachochunguza makosa ya uhalifu wa fedha na nyaraka, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Samson Kasala, alikanusha kufahamu chochote kuhusiana na suala hilo, kabla ya kukata simu alipohojiwa na Raia Mwema kuhusu taarifa hizo.

Taarifa zinaeleza kwamba Kitengo cha Ufuatiliaji wa Fedha Haramu (Financial Intelligence Unit-FIU) kilichopo chini ya Wizara ya Fedha nchini, kilipokea taarifa kutoka Polisi wa Kimataifa wa London, Uingereza, wakitaka taarifa muhimu kuhusiana na Frederick, kabla ya kitengo hicho kuomba msaada wa polisi.

Hata hivyo, Kamishna wa FIU, Herman Kessy, hakutoa ushirikiano na Raia Mwema, kuhusiana na sakata hilo.

FIU imeanzishwa chini ya Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu ya mwaka 2006 (Anti-Money Laundering Act-2006) kwa kuundiwa kanuni mwaka 2007, lakini hadi sasa kitengo hicho kimekuwa kikiendeshwa na maofisa watano tu, Kamishna Kessy, mchambuzi mmoja, mtaalamu wa mawasiliano na wasaidizi wawili wasio wataalamu, kitengo kilichopaswa kuendeshwa na watu wengi zaidi kutokana na unyeti wake.

Habari zinaeleza kwamba hata ofisa wa Polisi aliyewahi kuhamishiwa FIU kwa kazi maalumu alijikuta akitengwa na kutopangiwa kazi na maofisa hao ambao wengi wanatoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), baada ya kuwa ‘wameaminiwa’ sana na uongozi wa juu wa serikali.

Kwa mujibu wa taarifa hizo ambazo bado zinafanyiwa kazi, Frederick ambaye baba yake alijiuzulu Waziri Mkuu kwa kuhusishwa na kashfa ya ununuzi wa mitambo ya kuzalisha umeme iliyokabidhiwa kwa kampuni tata ya Richmond Development LLC, anadaiwa kufanya mawasiliano kupitia kampuni ya uwakala iliyotajwa kwa jina la ‘Mishcon’.

Nyaraka alizowasilisha, zilidai kuwapo ubia kati ya mtuhumiwa huyo na kampuni tatu ikiwamo Integrated Property Investment(T) Ltd na Barare Ltd Company.

Mkataba huo unaonyesha kuwa Frederick Lowassa ana hisa kwenye kampuni hizo, na kwamba fedha za ununuzi wa nyumba hizo zinatokana na fedha za malipo ya hisa anazopata kutokana na kampuni hizo.

Hata hivyo, mkataba huo unaonyesha kusainiwa Machi 25 mwaka 2009 siku moja baada ya Frederick Lowassa kusaini mkataba kati yake na kampuni ya Mishcon kama wakala wake katika ununuzi wa jengo hilo.

Pia aliwasilisha nyaraka zinazoihusisha kampuni ya Alphatel kama moja ya kampuni ambayo pia yeye ni mkurugenzi wake ambayo pia ni chanzo chake kingine cha fedha anazotumia kununua jengo hilo.

Taarifa zimedokeza kuwa ununuzi huo ulikwama baada ya kushindwa kutoa malipo hayo kwa mujibu wa mkataba kati yake na wakala wa ununuzi wa nyumba hiyo (kampuni ya Mishcon) ambao ulimtaka awe amekamilisha kulipa fedha hizo kabla ya Aprili 14, mwaka 2009.

Hata hivyo, siku chache baadaye ndani ya mwezi huo wa Aprili, Frederick aliipelekea Mishcon kiasi cha pauni za Uingereza 199,940 zikitokea kwenye kampuni ya ununuzi fedha ya Wall Street Exchange.

Aidha kiasi cha pauni 100,000 kiliingizwa kwenye akaunti ya kampuni hiyo hiyo ya Mishcon kwa fedha taslimu katika mikupuo 12 tofauti zikitokea kwenye matawi tofauti ya benki ya NatWest Bank plc iliyoko Kaskazini mwa Jiji la London.

Raia Mwema limeelezwa kuwa mazingira ya kuingizwa fedha hizo kwenye akaunti ya wakala huyo ( Mishcon) ndiyo yameifanya Taasisi ya SCD 6 Economics and Specialist Proceeds of Corruption Unit ya Uingereza inayosimamia uchunguzi wa sakata hilo kuwa na mashaka makubwa kuhusu uhalali wa fedha hizo.

Kutokana na mazingira hayo, SCD 6 Economic and Specialist Crime Proceeds of Corruption Unit yenye ofisi zake Victoria Block, New Scotland Yard, London, ililazimika kuwasiliana na FIU ikitaka maelezo ya awali kuwezesha kufanyika kwa uchunguzi kuhusu fedha hizo.

Raia Mwema iliwasiliana na Fred ambaye alikana kununua nyumba Uingereza lakini alikiri kuwahi kutuma fedha huko. Aliliambia Raia Mwema pia kwamba hajawahi kuhojiwa na yeyote kuhusu suala hilo, na pia kwamba hana taarifa kuwa polisi wa Uingereza wanampeleleza.

Hata hivyo kwa upande mwingine, gazeti hili limebaini kuwa, maelezo ya awali ambayo yalitakiwa kutoka Tanzania na makachero hao wa Uingereza, ni pamoja na kutaka kufahamu kama kweli Frederick Edward Lowassa amezaliwa Agosti 26, 1977, Mwanza Tanzania na anamiliki hati ya kusafiria yenye namba AB 109402 iliyotolewa Tanzania na kwamba anwani yake nchini Uingereza ni 71 Hendrix Drive, Milton Keynes, MK8 0DY.

Pia makachero hao waliitaka Serikali ya Tanzania kutoa ufafanuzi wakitaka kujua kama Frederick Lowassa ni mbia katika kampuni za Alphatel Partnership (Tanzania) Barare Ltd na Intergrated Tanzania Limited, kampuni ambazo zimefahamika kumilikiwa na familia ya Lowassa.

Asasi hiyo ya Uingereza pia imeomba kujua kama FIU wana taarifa zozote za uhalifu dhidi ya Frederick Lowassa na kama baba yake Edward Lowassa anachunguzwa kwa tuhuma yoyote ya rushwa na mamlaka za uchunguzi wa rushwa nchini Tanzania kuhusu fedha haramu.

Uchunguzi wa awali uliofanywa na vyombo vya dola, ulielezwa na taarifa hizo kwamba Frederick Lowassa si mbia katika kampuni hizo na kwamba Barare Ltd wenye hisa ni Edward Ngoyai Lowassa mwenye hisa 500 na Regina Mumba Lowassa mwenye hisa 500 huku wakurugenzi wakiwa ni hao hao.

Ofisa wa Uingereza anayesimamia uchunguzi huo, George Simpson, ameliambia Raia Mwema kupitia barua pepe kwamba kanuni za uchunguzi kuhusiana na kesi zenye mguso wa kisiasa huwazuia kukanusha au kuthibitisha kuhusu uchunguzi unaoendelea hadi pale wanapofikia hatua ya kukamata mtuhumiwa ama anapofikishwa mahakamani.

Taarifa ambazo gazeti hili limezipata mwanzoni mwa wiki hii kutoka vyanzo vyake zinasema kwamba uchunguzi wa suala hilo bado unaendelea, na kwamba watendaji wamepewa maelekezo ya kuendelea nao.

Thursday, December 2, 2010

Tohara ya ‘lazima’ kwa wanaume yaja

KUTOKANA na utafiti wa kisayansi kuonesha kuwa kutofanya tohara kwa wanaume ni moja ya sababu zinazochangia maambukizi ya Ukimwi, wanaume katika mikoa saba nchini wanatarajiwa kufanyiwa tohara kuanzia mwakani kwa sababu inayo idadi kubwa ya wanaume wasiotahiriwa.

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesema itaanza operesheni maalumu kwa kushirikiana na wadau wengine yakiwemo mashirika ya misaada kutoka Marekani, kufanya tohara kwa wanaume hao katika mikoa ya Mbeya, Iringa, Rukwa, Kagera, Tabora, Shinyanga na Wilaya ya Rorya mkoani Mara.

Hayo yalibainishwa na Waziri wa Wizara hiyo, Dk. Haji Mponda, jana mjini hapa, katika hotuba yake kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kumkaribisha Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal kuhitimisha maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, Kitaifa mjini hapa.

Dk. Mponda alisema utafiti uliofanyika na taasisi mbalimbali zinazojihusisha na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na Ukimwi, imeonesha kuwa mikoa hiyo inaongoza kwa maambukizi na moja ya sababu ni kuwepo kwa idadi mkubwa ya wanaume wasiofanyiwa tohara.

“Mpango wa Wizara ni kutaka kupunguza kiwango cha maambukizi ya VVU na utafiti umeonesha mikoa hii ina idadi ndogo ya wanaume waliofanyiwa tohara, lakini ina viwango vya juu vya maambukizi,” alisema Waziri huyo.

Hivyo alisema mpango wa Wizara ambao tayari ulianza kwa majaribio katika mikoa ya Iringa, Mbeya na Kagera, itaendelezwa zaidi katika mikoa iliyoainishwa kuanzia mwakani kwa ufadhili wa Serikali ya Marekani kupitia mashirika yao ya misaada sambamba na marafiki wengine wa maendeleo.

Alisema mpango huo wa kuwafanyia tohara wanaume katika mikoa hiyo umelenga kuwafikia wanaume zaidi ya milioni 2.5 na wanaume wa mikoa hiyo wameonesha kufurahishwa na uamuzi huo wa kuwatahiri.

Katika takwimu zilizotolewa na TACAIDS ya viwango vya maambukizi ya VVU ya mwaka 2003/ 2004, Mkoa wa Iringa ulikuwa na maambukizi ya asilimia 13.4 ambapo kwa mwaka 2007/2008 maambukizi ni asilimia 15.7.

Mkoa wa Mara kwa miaka hiyo, maambukizi yalikuwa ni asilimia 3.5 na kuongezeka mwaka 2007/2008 hadi kufikia asilimia 7.7 wakati Mkoa wa Shinyanga maambukizi yalikuwa ni asilimia 6.5 ambapo kwa mwaka 2007/2008 viwango vya maambukizi ni asilimia 7.4.

Naye Mwandishi Wetu, Flora Mwakasala anaripoti kuwa Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Chiku Galawa ametaka mabango yote ya waganga wa jadi yanayotangaza kuwepo kwa dawa za kuongeza nguvu za kiume, yaondolewe kwa kuwa ni kichocheo cha ongezeko la maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi yaliyofanyika jana kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, Galawa alisema mabango hayo yamebandikwa mitaani kwa wingi.

“Huu ni utapeli mkubwa, nani kasema watu wanahitaji kuongezewa nguvu za kiume? Jambo hili ni sawa na kuwahamasisha watu waendelee kufanya uasherati na kuongeza maambukizi mapya ya VVU,” alisema.

Alisema kitendo cha watu kuongeza nguvu za kiume kinawashawishi kuendelea kufanya ngono, jambo linalosababisha kuwepo kwa ongezeko kubwa la maambukizi hasa kwa vijana ambao ni taifa la kesho.

“Tutashirikiana na wananchi pamoja na viongozi wa Serikali za Mitaa kuhakikisha mabango yote yaliyobandikwa mitaani na barabarani yanaondolewa,” alisema.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu, Mkurugenzi wa Mafunzo Taifa wa Chama cha Waganga wa Tiba za Asili, Sadick Kalimaunga alisema kauli hiyo ya Galawa ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Temeke, si sahihi kwa kuwa kazi yao ni kuwasaidia wanaume wenye matatizo ya upungufu wa nguvu za kiume.

“Sisi hatuchochei maambukizi ya VVU kama wanavyodai bali tunawasaidia wanaume wenye matatizo hayo kudumisha ndoa zao kwa kuwaongezea nguvu za kiume ili waweze kufanya tendo hilo kikamilifu,” alisema.

Aidha, alisema kitendo cha Serikali kuondoa mabango hayo kitasababisha baadhi ya watu wanaohitaji tiba hizo ambazo zilikuwepo tangu enzi kukosa huduma na wengine ndoa zao kuvunjika.

Kwa mujibu wa takwimu, Dar es Salaam ni mkoa unaoshika nafasi ya pili nchini kwa kuwa na kiwango kikubwa cha maambukizi ya VVU cha asilimia 9.3. Iringa inaongozwa kwa kuwa na asilimia 15.7.

Wednesday, December 1, 2010

MAADHIMISHO YA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA


Watu mbalimbali waliofika kwenye maadhimisho ya kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia leo kwenye viwanja vya Mtandao wa Jinsia (TGNP) jijini leo.


Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Usu Mallya (Pili kushoto) akimkabidhi mlemavu wa viungo Maria Patrick baiskeli iliyotolewa na Mchungaji wa kanisa la Pentekoste Missionarieis, Gervas Masanja wakati wa maadhimisho ya siku ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia katika viwanja vya TGNP.



Mkurugenzi wa TGNP Usu Mallya akimkaribisha Mwenyekiti wa TGNP Mary Rusimbi pamoja na wageni waliohudhuria maadhimisho ya kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kwenye viwanja vya TGNP

Prof.Tibaijuka aanza kwa kasi: Mliopora maeneo jisalimisheni

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, amewataka wananchi waliopora viwanja na maeneo ya wazi nchini na kujenga, wajisalimishe kwa mazungumzo, kwa sababu huenda wakaokoa hata matofali kabla hatua zaidi hazijachukuliwa.

Profesa Tibaijuka alisema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mikakati ya wizara hiyo na kueleza kuwa masuala ya ardhi yasipofanyiwa kazi, sekta nyingine zitazorota.

“Umefika wakati sasa, tunataka kubadilisha mwonekano wa miji ... na kwa wanaosema wanatumia jeuri ya pesa, tutawashughulikia, lakini baada ya kufanya utafiti wa kutosha, kwa sababu hatuwezi kukurupuka, hivyo waliopora viwanja tunawataka wajisalimishe,” alisema Profesa Tibaijuka ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa zamani wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kushughulikia Makazi (UN-Habitat).

Alisema, migogoro ya ardhi hawataimaliza bila wananchi kuwasaidia na kwa sasa, watarudisha askari wa ardhi ili kuhakikisha wanapunguza migogoro ikiwamo ya wanaojenga holela na katika maeneo ya wazi.

Tibaijuka alisema, kati ya hekta 900,000 ni asilimia mbili tu ya maeneo ndiyo yaliyopimwa, hivyo wizara yake itahakikisha inapimwa, ili miji iwe katika hali inayotakiwa kwa sababu kwa sasa hairidhishi.

Aidha, Profesa Tibaijuka alisema si maendeleo yote yanahitaji fedha, hivyo kwa muda huu waliopewa na Rais, kuna mambo ambayo watayafanyia kazi kwa haraka ikiwamo kuandika majina ya mitaa yote.

“Watu wengi hawatambui mitaa wanayoishi inaitwaje, kwa sababu wala haina majina na unakuta anashindwa kabisa kuelekeza, lakini tukiiandika tutawasaidia, hivyo tutafanya jambo hili kwa haraka maana haihitaji fedha,” alifafanua mbunge huyo wa Muleba Kusini.

Katika hatua nyingine, alisema kuna upungufu wa nyumba milioni tatu nchini, hivyo wanapaswa kujenga miji kwa kuboresha nyumba zilizopo na kuzijenga ambazo hazina viwango na kuziuza kwa wananchi.

“Wananchi wanatakiwa kutambua wanahitaji nyumba au ardhi, lakini watambue kama ni viwanja lazima waende nje ya mji, ila kama ni nyumba zipo ila zinahitaji maboresho na tutafanikiwa, kwa kuwa na benki za nyumba na mikopo ya nje, kwa sababu sekta binafsi pekee hazitaweza bila kuwa na fedha ... tuwaachie wahandisi wetu wajenge nyumba sisi tununue,” alisema.

Alisema, watafanya kazi kwa kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Mazingira ili kuhakikisha miji inakuwa safi na salama; na kuboresha bonde la Mto Msimbazi, Dar es Salaam, ambalo limefanya hali ya hospitali ya Taifa Muhimbili kuwa mbaya.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Patrick Rutabanzibwa, alikiri baadhi ya wafanyakazi wake kushiriki kugawa maeneo ya wazi na kueleza kuwa tayari ameanza kuwachukulia hatua za kisheria, ikiwamo kufanya mabadiliko ya vitengo kwa nia ya kuboresha utendaji kazi.

“Uvamizi wa maeneo ni mtandao wa watu wa wizarani na manispaa nami nimejitolea kuwashughulikia na tayari kuna waliokuwa wamepora viwanja na nimewataka wavirudishe na wengine walipora na kuwauzia wafanyabiashara wakubwa,” alisema Rutabanzibwa.

Pia alisema wamesimamisha ujenzi wa eneo la wazi katika hoteli ya Palm Beach na kuahidi kufanya kazi bila kuhofia kashfa, kwani zipo tuhuma amevumishiwa na amezipeleka kwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) na kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Kwa upande wao, mawaziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Mary Nagu (Uwekezaji na Uwezeshaji) na William Lukuvi (Sera, Uratibu na Bunge), waliripoti rasmi katika Ofisi ya Waziri Mkuu na kuzungumza na wakuu wa idara, vitengo na taasisi chini ya Ofisi hiyo.

Mawaziri hao waliwataka watendaji kufanya kazi kwa ubunifu, ushirikiano, upendo, uwazi na bidii zaidi, ili kukidhi matarajio ya wananchi.

Nagu alisisitiza umuhimu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji bila ngojangoja ambayo ni chanzo cha kuwakatisha tamaa wawekezaji.

Alisema hakuna uchumi duniani uliofanya vizuri bila uwekezaji, iwe wa kutoka nje au ndani ya nchi husika. Alibainisha kuwa Watanzania ndio wanatakiwa kushika hatamu ya uchumi wao.

Lukuvi alisisitiza watendaji kuwa wabunifu na kufanya kazi kwa kasi zaidi ili kuongeza ufanisi na hatimaye kufikia malengo ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taifa kwa jumla.

Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu aliwaambia watendaji wakuu wa wizara hiyo kuwa anawapa uhuru wa kufanya uamuzi wenye tija na ufanisi na atakayeshindwa atajiondoa mwenyewe.

Alizungumza na wakurugenzi wakuu wa idara za uchukuzi na wa taasisi mbalimbali akijitambulisha kwao rasmi na kuanza kazi.

Nundu aliwataka kufahamu dhima waliyonayo katika kuendeleza sekta ya uchukuzi ili katika kipindi cha miaka mitano ijayo, fursa zilizomo zitumike vyema pamoja na kuboresha huduma za usafiri.

Aliwataka kupeana ushauri ili wasonge mbele, kuwa wadilifu na waaminifu huku wakitoa huduma kwa dhati na kwa wakati muafaka.

“Hakikisheni mnawajibika kulingana na wakati, katika suala la uchukuzi hatupo peke yetu ulimwenguni, zingatieni matakwa ya wateja,” alisema Nundu na kuongeza:

“Fanyeni kazi kila mmoja kwa madaraka aliyonayo, toeni uamuzi wenye tija bila upendeleo na hata ubinafsi na hiyo iwe ahadi yenu kwetu,” alisema.

Alisema, anatarajia kuimarisha kampuni ya reli, kwa lengo la kuipa uwezo wa kutoa huduma bora kwa kusafirisha abiria na mizigo ya ndani na nchi jirani, na kuendelezwa kama mhimili wa mpango wa maendeleo wa eneo la ukanda wa kati.

Tuesday, November 30, 2010

Kikwete awaonya Mawaziri

WAKATI Rais Jakaya Kikwete akiwa katika ngwe yake ya mwisho ya uongozi wa nchi ameonesha kuwa mkali kwa mawaziri wake wapya aliowateua hivi karibuni.

Kikwete amewaeleza wazi kuwa safari hii hana simile wala subira kwa Waziri atakayeboronga katika utekelezaji wa majukumu yake.

Rais Kikwete ametoa msimamo wake wakati anawapa majukumu mapya mawaziri hao na akagusia nyanja mbali mbali zikiwemo uwajibikaji, kufuata kanuni, sheria na pia kupambana na rushwa huku akisisitiza kuwa vita dhidi ya rushwa ni suala la kikatiba na kuwataka kuhakikisha kuwa Mpango wa Pili wa Mkakati wa Kitaifa wa Kupambana na Rushwa (NACSAP-11) unatekelezwa.

Akizungumza na Mawaziri na Naibu Mawaziri Ikulu Dar es Salaam jana, Rais Kikwete aliwaeleza mawaziri kuwa katika kipindi hiki cha pili cha uongozi wake hakutakuwa na muda wa kupoteza.

Amesema, hatakuwa tayari kukubali maelezo ya kwa nini utekelezaji wa majukumu ya msingi umeshindikana na amewataka mawaziri kusimamia mapato ya Serikali yasiyotokana na kodi na kudhibiti matumizi ya Serikali.

Pia aliwataka viongozi hao kuzingatia maadili ya uongozi ikiwa ni pamoja na kusimamia sheria za nchi, kuheshimu sheria katika shughuli na mambo yao binafsi na kutunza siri za Serikali kwa mujibu wa kiapo chao.

Rais Kikwete pia alisisitiza umuhimu wa Mawaziri na Naibu Mawaziri kuwasiliana na wananchi kwa maana ya kueleza mafanikio na mipango ya Serikali katika kushughulikia matatizo ya wananchi.

Rais Kikwete aliwataka mawaziri hao kuvitumia kikamilifu vitengo vya mawasiliano ya Serikali katika wizara zao ambavyo ndivyo vyenye jukumu la kutoa taarifa kuhusu Wizara inavyotelekeza majukumu yake.

“Uzoefu unaonesha kuwa mawaziri wengi ni wazito kufanya mawasiliano na wananchi hata pale ambako Wizara imefanya mambo mengi mazuri. Hivyo, mawaziri muwe mstari wa mbele kuelezea mafanikio ya utendaji wa Serikali katika Wizara zetu,” alielekeza Rais Kikwete na kuongeza:

“Lazima ujengwe utamaduni wa kudumu wa kuwasiliana na wananchi wote ambao ndio waajiri wetu kupitia kura zao. Mawaziri wote tumieni vitengo vyenu vya mawasiliano na vyombo vya habari kwa ustadi ipasavyo”.

Akiwapongeza kuteuliwa kwao, Rais Kikwete alisema: “Mnastahili pongezi hasa ukizingatia ukweli kwamba nyinyi mmebahatika kuteuliwa kutoka kwenye orodha ndefu ya wabunge wengi wenye sifa za kushika nafasi mlizo nazo.

Nimewateua kwa imani kuwa pamoja nanyi, tutatimiza matumaini ya wananchi wa Tanzania waliokichagua Chama Cha Mapinduzi kiendelee kuongoza nchi yetu".

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, wakati akizungumza na wakuu wa idara katika wizara yake baada ya kutoka Ikulu aliwaambia kutokana na msimamo huo wa Rais Kikwete, yeye na naibu wake, hakuna kulala hadi matarajio ya wananchi katika wizara hiyo yatakapopatiwa ufumbuzi.

Dk. Kawambwa aliahidi changamoto ya kwanza kufanyia kazi ni kuhakikisha mikopo inayotolewa kwa wanafunzi wa elimu ya juu inaboreshwa, ili kuondoa malalamiko yasiyokwisha kutoka kwa wanafunzi hao.

Akiwa amefuatana na Naibu Waziri wake, Phillip Mlugo, Dk Kawambwa alikiri kuwapo tatizo kubwa la utoaji mikopo, hali iliyofanya wanafunzi karibu wote wa vyuo vikuu kuinyima kura CCM katika uchaguzi wa Oktoba mwaka huu. Licha ya mikopo pia aliahidi kuhakikisha maslahi ya walimu yanaboreshwa ili kuondoa uwezekano wa walimu kugoma.

“Natambua kuwa watoaji na wapokeaji elimu, wote wako kwenye matatizo, hili eneo nitashughulika nalo zaidi.

“Leo tulikuwa na mkutano na Rais (Kikwete) ametwambia wazi, kuwa safari hii hana simile wala subira, anachotaka ni watu tufanye kazi. Na sisi tunakuja hapa kwa hadhari kuwa hakuna kulala,” alisema Dk Kawambwa ambaye awali alikuwa Wizara ya Miundombinu.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Cyril Chami, akianza kazi rasmi aliahidi kuandika waraka kwa Baraza la Mawaziri, kuomba Serikali iboreshe viwanda ikiwamo kufufua vilivyokufa kwa kuvichukua na kurudi kwenye miliki yake.

Waziri huyo ambaye amepandishwa kutoka Naibu Waziri katika wizara hiyo, alisema:“Miaka mitatu nyuma, tulifanya ukaguzi wa viwanda vyote na tukajua kwa nini vingine vilifungwa au havijaanza kazi na sasa tunataka vifanye kazi”.

Akizungumza na gazeti hili mara baada ya kupokewa rasmi wizarani hapo na wafanyakazi huku akifuatana na Naibu wake, Lazaro Nyalandu, alisema baadhi ya viwanda vilivyoshindwa kufanya kazi vitawezeshwa ili vifufuke.

“Kuna viwanda vingine tumeona wamiliki wameshindwa kuzalisha bidhaa walizoomba awali na wanataka kubadili aina nyingine, nao tutawasaidia wazalishe wanachoweza baada ya kutetea hoja zao,” alisema.

Kwa upande wa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, wakati akizungumza na wafanyakazi wa wizara yake, alisema baada ya miaka miwili, watu watajua upole na ujana wake ukoje, kwani anaamini atakuwa amefanya kazi vizuri na kwenye hilo, hana shaka nalo.

Alisema licha ya kutegemea kuteuliwa katika wizara hiyo nzito, atatekeleza Ilani ya CCM kwa kasi zaidi, huku akiahidi kuhakikisha sheria zote zilizotungwa kusimamia maliasili vikiwamo vitalu na wanyamapori zinasimamiwa ipasavyo.

Alisema anaamini kutokana na kuwekwa sheria za uwazi na shirikishi, mianya ya rushwa na vitendo vyake wizarani hapo vitakwisha.

Kwenye Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Waziri Dk Haji Mponda, aliwataka wafanyakazi wa wizara hiyo, kushirikiana kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta hiyo.

Dk Mponda alitaja changamoto kubwa kwa wafanyakazi wa sekta hiyo kuwa ni kutoa huduma bora za tiba katika vituo vyote vya afya nchini ili kuinua uchumi wa nchi “Mtanzania wa leo anataka huduma bora za tiba … mtu anapoingia hospitalini au kwenye zahanati anachotaka ni kumwona mganga na kupata huduma bora, hivyo kila mtoa huduma hana budi kuwajibika katika hilo.”

Miongoni mwa mawaziri walioanza kazi kwa cheche ni wa Ujenzi, John Magufuli ambaye juzi aliagiza Wakala wa Barabara nchini (Tanroads) kusimamisha nafasi za kazi za mameneja wa mikoa zilizotangazwa kwenye vyombo vya habari na kuamuru mameneja wote waliosimamishwa kazi warejee kazini.

Wakati huo huo, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na mashirika yapatayo 50 yanayotetea usawa wa kijinsia, haki za binadamu na ukombozi wa wanawake kimapinduzi (FemAct), yamepongeza uteuzi wa mawaziri na naibu mawaziri uliofanywa na Rais Kikwete Novemba 24 mwaka huu.

Hata hivyo, taarifa ya FemAct iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi, ilielezea kutoridhishwa na idadi ndogo ya mawaziri wanawake na pia ukubwa wa Baraza hilo kwa jumla.

“Idadi ya wanawake walioteuliwa kuwa mawaziri ni ndogo sana. Katika uteuzi huu, jumla ya mawaziri ni 29, kati yao wanaume ni 22 sawa na asilimia 76 na wanawake ni wanane, sawa na asilimia 24.

“Naibu mawaziri ni 21, wanaume ni 18 sawa na asilimia 86 na wanawake ni watatu sawa na asilimia 14. WanaFemAct walitarajia kuwa hiki kilikuwa kipindi mwafaka cha kufikia uwiano wa 50:50 ingawa mikakati iliyowekwa na fursa zilizokuwapo hazikutoa fursa hiyo,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Monday, November 29, 2010

Sitta: Tanzania haiuzwi

MAWAZIRI wateule jana waliapishwa kuanza kutekeleza majukumu waliyopewa serikalini.

Aliyekuwa Spika wa Bunge la Tanzania, ambaye ameteuliwa kuwa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta akisema wamekabidhiwa madaraka hayo kwa umakini ili asijetokea mtu akauza nchi.

Akizungumza muda mfupi baada ya kumaliza kupiga picha ya pamoja na Rais Jakaya Kikwete mara baada ya mawaziri hao na naibu mawaziri kula kiapo chao, Sitta alisema kazi waliyopewa inahitaji ujuzi wa kila namna.

“Kubwa la kuzingatia ni uzalendo, hii kazi (ya Uwaziri wa Ushirikiano Afrika Mashariki), humpi mtu tu, anaweza kutuuza,” alisema Sitta wakati akifafanua changamoto zinazomkabili katika wadhifa huo ambapo awali alianza kwa kumshukuru Rais Kikwete kwa kumteua kushika nafasi hiyo.

Alitamba kuwa utendaji wa kasi na viwango, sasa umehamia serikalini na kushangaa watu wanaoona kuwa atashindwa kupiga vita ubadhirifu kutokana na nafasi yake kama Waziri.

“Wakati ule nilikuwa nje, sasa nimeingia ndani ndio nitajua hali halisi ilivyo na kusaidia. Kwanza tutahakikisha sheria mpya ya maadili ya viongozi inapitishwa haraka.

“Unajua wananchi wanapata shida katika imani yao kwa Serikali hasa wanapomuona mtu aliyepata madaraka, ghafla ana pauni huko Uingereza na nyumba Ufaransa, tutapigia kelele hilo,” alisema Sitta ambaye alikuwa Waziri wa kwanza kuapa.

Alisisitiza nia ya kutetea kuwasilishwa bungeni haraka kwa muswada wa sheria mpya ya maadili ya viongozi ambayo inalenga kutenganisha biashara na siasa, ni ili kuepuka viongozi ambao wanatumia nafasi zao kujitajirisha wenyewe.

“Huwezi kutajirika katika siasa, kwa mfano mimi natakiwa Arusha Jumatatu na nitakuwa ofisini kuanzia asubuhi mpaka usiku, hiyo biashara utafanya saa ngapi halafu tunaambiwa wenzetu ni wachakarikaji, hakuna kuchakarika hapo.

“Ushahidi wa kwanza wa mwanasiasa mla rushwa ni kutajirika ghafla, labda kama aliingia madarakani akiwa na utajiri wake,” alisema Sitta na kujitolea mfano kuwa aliingia serikalini mwaka 1974 akitokea Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kama ofisa na katika hali hiyo asingeweza kujenga nyumba nje ya nchi.

Kuhusu umuhimu wa wizara hiyo kwa sasa, Sitta alisema Tanzania inakwenda kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na katika hilo maslahi ya Watanzania yanatakiwa kulindwa.

Alisema pia kuna changamoto ya kuwaondolea Watanzania hofu ya kuwa baada ya Shirikisho, watapata shida ikiwemo ya kukosa nguvu za kiuchumi na kuhusu mamlaka ya viongozi wao kama Rais.

“Tutaangalia mikataba na kuhakikisha tunaingia katika Shirikisho kwa kuzingatia maslahi ya Watanzania hasa katika ardhi na ajira yanalindwa,” alisema Sitta na kutamba uwezo wake katika sheria na uzoefu serikalini wa karibu miaka 36 umemfanya kuwa mtu mwenye kuweza kazi hiyo.

Alisema, alipoachia aliyekuwa Waziri katika Wizara hiyo, Dk. Diodorus Kamala ndipo atakapoanzia yeye na kusifu uteuzi wa Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dk. Abdallah Juma Abdallah kuwa ni mtu mzuri atakayesaidiana naye kazi.

Alikiri kuwa Tanzania iko nyuma ikilinganishwa na baadhi ya nchi wanachama wa umoja huo na kuongeza kuwa atajitahidi kuomba muda katika mambo kama ardhi na ajira ili nchi isigeuke kama “shamba la bibi”. Alisema pia ataomba kuongezewa bajeti katika jukumu la kutoa elimu kwa Watanzania ili EAC ifahamike na kuondoa hofu.

Magufuli amkaanga bosi wa Tanroads

SIKU moja baada ya kuapishwa,Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli amemtaka Mkurugenzi wa Wakala wa Barabara (Tanroads), Ephraim Mrema kusimamisha mara moja nafasi za kazi za mameneja wa mikoa alizozitangaza kwenye vyombo vya habari kuwa zipo wazi.

Magufuli amewataka mameneja wote ambao wamesimamishwa kazi, warudi kazini mara moja na kwamba tangazo hilo halina nguvu.

Kutokana na uamuzi huo, Dk. Magufuli amemtaka Mrema kutoa tangazo haraka kuanzia leo katika vyombo vya habari, kusitisha tangazo lake la awali la kuwasimamisha kazi mameneja wa Tanroads mikoani kwa kuwa hatua aliyoichukua inaonekana ni ya kulipizana visasi.

Dk. Magufuli alitoa maagizo hayo jana, Dar es Salaam katika mkutano wake na wakuu wa idara na vitengo mbalimbali vya wizara hiyo wakati akijitambulisha kwao.

Katika maagizo yake, Dk Magufuli alimtaka Mrema asifanye kazi kama mtu anayeondoka kesho, bali atekeleze majukumu yake kama atafanya kazi hiyo kwa miaka 100 ijayo.

“Tanroads jipangeni sawasawa, blaablaa ziishe, wewe Mkurugenzi uliona nafasi yako inatangazwa na wewe ukaamua kutangaza za mameneja wa mikoa ili kuchomeana na kila kitu kisimamishwe, kwanini ulitangaza kwamba waliopo hawachapi kazi?”

Alihoji Dk. Magufuli. Aliagiza mameneja wa mikoa waelezwe mara moja kuwa wamerudishwa kazini isipokuwa kwa nafasi ya Dodoma tu ambayo meneja wake hayupo. “

Nakuagiza Mrema, uandike katika vyombo vya habari kuwa umefuta tangazo hilo na mengine yatafuatia.”

Alimtaka Mkurugenzi huyo wa Tanroads, kufanya kazi kwa ushirikiano na kwamba kama Waziri na Naibu wake Dk. Harrison Mwakyembe watauliza jambo lolote, wajibiwe haraka, la sivyo itakuwa ni dharau.

Mkurugenzi huyo wa Tanroads inadaiwa kipindi chake cha kuongoza wakala huo kimemalizika kwa mujibu wa mkataba wake wa kazi, lakini ameendelea kukalia ofisi hiyo.

Dk. Magufuli alisema wao hawakufika katika wizara hiyo kwa ajili ya kutengua Torati, bali kuitekeleza na kwamba wanaweza kufanya kazi na yeyote na kusisitiza kuwa yaliyopita yaachwe na wafanye kazi kwa pamoja.

“Tushirikiane, tupendane, majungu yaishe, tuache rushwa kwa kuwa tutawategeshea hata fedha ya Polisi… na hivi ndio maana Rais ametuteua mimi na Naibu mwenye taaluma ya Sheria,” alisema.

Kuhusu rushwa, waziri huyo aliahidi kupanda lori lililozidisha uzito na kutoa rushwa na akasema akikamilisha kazi hiyo watakaohusika watamtambua. Aliwataka watendaji wa mizani kusimamia sheria, kukamata magari na kupiga faini na kuteremsha mizigo bila kujali mmiliki wa gari au mzigo.

Awali akizungumza katika mkutano huo, Dk. Mwakyembe, alisema uteuzi wao hautakuwa na maana kama wataachia kirusi aliyeingia katika Wizara hiyo na kutia doa kuendelea.

Alisema mwanzoni wizara hiyo ilikuwa mfano wa kuigwa lakini anashangaa kuona ufanisi umepotea na sasa imekuwa sehemu ya kunyoosheana vidole bila kujua ni kirusi gani huyo aliyeingia.

Alisisitiza kuwa sasa wanahitaji kuongea lugha moja na kuimba wimbo mmoja na kuifanya wizara hiyo kuwa ya mfano na kuagiza taarifa za kukinzana zisipewe nafasi kwa kuwa hawaendeshi wizara kwa majungu na umbeya.

Thursday, November 25, 2010

Familia ya Lowassa yapelelezwa London

-Polisi Uingereza wamchunguza mwanawe
-Washitushwa na uhamishwaji wa Sh.bil. moja
MTOTO wa Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa anayeitwa Frederick Lowassa anachunguzwa na Kitengo Maalumu cha Polisi wa Kimataifa wa Uingereza wanaofuatilia utata wa uhamishaji fedha kutoka Tanzania, Raia Mwema limedokezwa.

Fedha hizo zinahusishwa na ununuzi wa nyumba yenye thamani ya pauni za Uingereza 475,000 (takriban Shilingi bilioni moja) katikati ya Jiji la London, .

Hata hivyo, watu walio karibu na Frederick wameelezea kwamba kijana huyo hakuwahi kununua nyumba; bali aliwahi kutaka kupanga kwa ajili ya kuishi akiwa masomoni nchini Uingereza na fedha nyingine alizituma kwa ndugu yake aishie nchini humo.

Nyumba ambayo inatajwa katika maelezo ya awali iko mtaa wa Leinster Gardens, jijini London.

Hata hivyo, hakuna ofisa yeyote wa Serikali ya Tanzania aliyekuwa tayari kuzungumzia suala hilo, pamoja na kuwapo taarifa kwamba tayari vyombo vya dola vya Tanzania vimekwisha kuhusishwa katika uchunguzi huo.

Maofisa wa Polisi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (CID) wanaohusika na uchunguzi wa fedha haramu, wamekwepa kuzungumzia suala hilo na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Robert Manumba, hakuweza kupatikana, na alielezwa kuwa nje ya nchi kikazi.

Ofisa wa CID aliyeelezwa kuongoza kitengo kinachochunguza makosa ya uhalifu wa fedha na nyaraka, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Samson Kasala, alikanusha kufahamu chochote kuhusiana na suala hilo, kabla ya kukata simu alipohojiwa na Raia Mwema kuhusu taarifa hizo.

Taarifa zinaeleza kwamba Kitengo cha Ufuatiliaji wa Fedha Haramu (Financial Intelligence Unit-FIU) kilichopo chini ya Wizara ya Fedha nchini, kilipokea taarifa kutoka Polisi wa Kimataifa wa London, Uingereza, wakitaka taarifa muhimu kuhusiana na Frederick, kabla ya kitengo hicho kuomba msaada wa polisi.

Hata hivyo, Kamishna wa FIU, Herman Kessy, hakuweza kupatikana wiki iliyopita akielezwa kuwapo nchini Afrika Kusini kikazi, lakini hata aliporejea wiki hii Raia Mwema ilikosa ushirikiano kutoka kitengo hicho Jumatatu wiki hii.

FIU imeanzishwa chini ya Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu ya mwaka 2006 (Anti-Money Laundering Act-2006) kwa kuundiwa kanuni mwaka 2007, lakini hadi sasa kitengo hicho kimekuwa kikiendeshwa na maofisa watano tu, Kamishna Kessy, mchambuzi mmoja, mtaalamu wa mawasiliano na wasaidizi wawili wasio wataalamu, kitengo kilichopaswa kuendeshwa na watu wengi zaidi kutokana na unyeti wake.

Habari zinaeleza kwamba hata ofisa wa Polisi aliyewahi kuhamishiwa FIU kwa kazi maalumu alijikuta akitengwa na kutopangiwa kazi na maofisa hao ambao wengi wanatoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), baada ya kuwa ‘wameaminiwa’ sana na uongozi wa juu wa serikali.

Kwa mujibu wa taarifa hizo ambazo bado zinafanyiwa kazi, Frederick ambaye baba yake alijiuzulu Waziri Mkuu kwa kuhusishwa na kashfa ya ununuzi wa mitambo ya kuzalisha umeme iliyokabidhiwa kwa kampuni tata ya Richmond Development LLC, anadaiwa kufanya mawasiliano kupitia kampuni ya uwakala iliyotajwa kwa jina la ‘Mishcon’.

Nyaraka alizowasilisha, zilidai kuwapo ubia kati ya mtuhumiwa huyo na kampuni tatu ikiwamo Integrated Property Investment(T) Ltd na Barare Ltd Company.

Mkataba huo unaonyesha kuwa Frederick Lowassa ana hisa kwenye kampuni hizo, na kwamba fedha za ununuzi wa nyumba hizo zinatokana na fedha za malipo ya hisa anazopata kutokana na kampuni hizo.

Hata hivyo, mkataba huo unaonyesha kusainiwa Machi 25 mwaka 2009 siku moja baada ya Frederick Lowassa kusaini mkataba kati yake na kampuni ya Mishcon kama wakala wake katika ununuzi wa jengo hilo.

Pia aliwasilisha nyaraka zinazoihusisha kampuni ya Alphatel kama moja ya kampuni ambayo pia yeye ni mkurugenzi wake ambayo pia ni chanzo chake kingine cha fedha anazotumia kununua jengo hilo.

Taarifa zimedokeza kuwa ununuzi huo ulikwama baada ya kushindwa kutoa malipo hayo kwa mujibu wa mkataba kati yake na wakala wa ununuzi wa nyumba hiyo (kampuni ya Mishcon) ambao ulimtaka awe amekamilisha kulipa fedha hizo kabla ya Aprili 14, mwaka 2009.

Hata hivyo, siku chache baadaye ndani ya mwezi huo wa Aprili, Frederick aliipelekea Mishcon kiasi cha pauni za Uingereza 199,940 zikitokea kwenye kampuni ya ununuzi fedha ya Wall Street Exchange.

Aidha kiasi cha pauni 100,000 kiliingizwa kwenye akaunti ya kampuni hiyo hiyo ya Mishcon kwa fedha taslimu katika mikupuo 12 tofauti zikitokea kwenye matawi tofauti ya benki ya NatWest Bank plc iliyoko Kaskazini mwa Jiji la London.

Raia Mwema limeelezwa kuwa mazingira ya kuingizwa fedha hizo kwenye akaunti ya wakala huyo ( Mishcon) ndiyo yameifanya Taasisi ya SCD 6 Economics and Specialist Proceeds of Corruption Unit ya Uingereza inayosimamia uchunguzi wa sakata hilo kuwa na mashaka makubwa kuhusu uhalali wa fedha hizo.

Kutokana na mazingira hayo, SCD 6 Economic and Specialist Crime Proceeds of Corruption Unit yenye ofisi zake Victoria Block, New Scotland Yard, London, ililazimika kuwasiliana na FIU ikitaka maelezo ya awali kuwezesha kufanyika kwa uchunguzi kuhusu fedha hizo.

Raia Mwema iliwasiliana na Fred ambaye alikana kununua nyumba Uingereza lakini alikiri kuwahi kutuma fedha huko. Aliliambia Raia Mwema pia kwamba hajawahi kuhojiwa na yeyote kuhusu suala hilo, na pia kwamba hana taarifa kuwa polisi wa Uingereza wanampeleleza.

Hata hivyo kwa upande mwingine, gazeti hili limebaini kuwa, maelezo ya awali ambayo yalitakiwa kutoka Tanzania na makachero hao wa Uingereza, ni pamoja na kutaka kufahamu kama kweli Frederick Edward Lowassa amezaliwa Agosti 26, 1977, Mwanza Tanzania na anamiliki hati ya kusafiria yenye namba AB 109402 iliyotolewa Tanzania na kwamba anwani yake nchini Uingereza ni 71 Hendrix Drive, Milton Keynes, MK8 0DY.

Pia makachero hao waliitaka Serikali ya Tanzania kutoa ufafanuzi wakitaka kujua kama Frederick Lowassa ni mbia katika kampuni za Alphatel Partnership (Tanzania) Barare Ltd na Intergrated Tanzania Limited, kampuni ambazo zimefahamika kumilikiwa na familia ya Lowassa.

Asasi hiyo ya Uingereza pia imeomba kujua kama FIU wana taarifa zozote za uhalifu dhidi ya Frederick Lowassa na kama baba yake Edward Lowassa anachunguzwa kwa tuhuma yoyote ya rushwa na mamlaka za uchunguzi wa rushwa nchini Tanzania kuhusu fedha haramu.

Uchunguzi wa awali uliofanywa na vyombo vya dola, ulielezwa na taarifa hizo kwamba Frederick Lowassa si mbia katika kampuni hizo na kwamba Barare Ltd wenye hisa ni Edward Ngoyai Lowassa mwenye hisa 500 na Regina Mumba Lowassa mwenye hisa 500 huku wakurugenzi wakiwa ni hao hao.

Ofisa wa Uingereza anayesimamia uchunguzi huo, George Simpson, ameliambia Raia Mwema kupitia barua pepe kwamba kanuni za uchunguzi kuhusiana na kesi zenye mguso wa kisiasa huwazuia kukanusha au kuthibitisha kuhusu uchunguzi unaoendelea hadi pale wanapofikia hatua ya kukamata mtuhumiwa ama anapofikishwa mahakamani.

Wednesday, November 24, 2010

BARAZA JIPYA LA MAWAZIRI HILI HAPA

TANZIA


Mtandao wa Mashirika yapatayo 50 yanayotetea Usawa wa Kijinsia, Haki za Binadamu, Maendeleo na Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi (FemAct), tunaomboleza kuondokewa na Mpendwa wetu, dada Mary Mwingira, mpiganaji wa muda mrefu wa haki za wanawake na haki za kijamii, aliyefariki siku ya jumapili usiku, tarehe 21 Novemba 2010, baada ya kuugua saratani kwa muda mrefu. Tunapenda kumuenzi kwa mchango wake katika ukuaji na uimarishwaji wa mashirika ya kijamii hapa Tanzania. Mary Mwingira aliongoza wanawake na mashirika yasiyo ya kiserikali yanayojishughulisha na masuala ya kijinsia hapa Tanzania kushiriki katika Mkutano wa Ulimwengu wa muongo wa Wanawake uliofanyika Nairobi, Kenya, mwaka 1985, wakiunga mkono mashirika mbalimbali kutoka ngazi za kijamii hadi kitaifa na kupata fursa ya wazo mbadala wakati wa Kongamano la mashirika yasiyo ya kiserikali huko Nairobi, pamoja na kubadilishana mawazo na kuunga mkono ujumbe wa kiserikali. Mchakato huu ulipelekea kuanzishwa kwa TANGO, jumuiya mama ya mashirika yasiyo ya kiserikali Tanzania, ambayo Mary Mwingira aliiongoza kwa miaka mingi kama Mkurugenzi Mtendaji. Mary pia alikuwa mwanachama mwanzilishi wa taasisi mbalimbali za wanawake na haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na Taaluma Women and Christian Professionals of Tanzani, na pia alishiriki katika Kongamano la kijamii la Ulimwengu, Nairobi.

Kati ya 1992/1993, Mary Mwingira pamoja na vikundi vya viongozi wengine wa vikundi vya wanawake na jinsia walishiriki katika mchakato wa pamoja katika kutafakari na kupanga mikakati ambayo iliongozwa na waanzilishi wa Mtandao wa jinsia Tanzania katika kuandaa Kongamano la Wanawake la Ulimwengu lililofanyika Beijing, China, mwaka 1995. Kwa kutumia mbinu shirikishi za uraghibishi na uchambuzi wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi, viongozi hawa wanawake wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali walifanya kwa pamoja uchambuzi wa kina wa nafasi ya wanawake hapa Tanzania, mfumo dume na mfumo wa utandawazi kibeberu iliyoendelea kuwakandamiza na kuwanyonya wanawake wakati wa mfululizo wa warsha hizo tatu, na hatimae kupanga kwa pamoja mikakati iliyokuwa inahitajika kwa ajili ya kuendeleza haki za wanawake, usawa wa kijinsia na mabadiliko ya kijamii. Mawazo haya baadaye yaliwasilishwa na viongozi wa TGNP kwa niaba ya Kikundi cha Mashirika yasiyo ya Kiserikali ya Tanzania katika Mkutano wa Maandalizi wa nchi za Kanda ya Afrika ya Mashariki Uliofanyika Uganda mwaka 1993, na kuchapishwa kama Hali Halisi ya Kijinsia Tanzania( Gender Profile of Tanzania), mwaka huo.

Mapema mwaka 1993, viongozi hawa hawa wa mashirika ya wanaharakati wa masuala ya wanawake na jinsia walidai wawezeshaji wa warsha waunde shirika jipya la kudumu na kufanya uchambuzi wa ukombozi wa wanawake kimapindu kwa kutumia mbinu shirikishi. Ni kutokana na mchakato huu TGNP iliweza kuzaliwa, ambapo iliandikishwa rasmi mwishoni mwa mwaka 1993, kwa mchango mkubwa wa Mary Mwingira, kwa upande wa ushauri na kutambulisha wafadhili. Muda mfupi baadaye, wengi kati ya viongozi hao hao wa Jumuiya zisizokuwa za kiserikali za wanawake na haki za kijinsia walianzisha FemAct, kwa ajili ya kuimarisha vuguvugu la ukombozi wa wanawake kimapinduzi na haki za binadamu katika ukuaji wa nguzu za pamoja. TANGO ni mwanzilishi wa FemAct na Mary Mwingira alibakia kuwa mshiriki imara katika mapambano mengi yaliyofanywa nchini Tanzania katika kukuza haki za wanawake na za kijamii kwa wote waliokandamizwa, walionyonywa na waliowekwa pembezoni.

FemAct inatuma salamu zake za rambiambi kwa familia ya Mary Mwingira, ndugu, jamaa na marafiki wote. Katika kipindi hiki cha maombolezo, tumkumbuke kwa uwezo wake wa kusimama imara katika mapambano ya kutetea haki, demokrasia na usawa wa kijamii katika ngazi zote.

Tunaiombea roho ya marehemu dada yetu, ilale mahali pema peponi, Amen.


Imetolewa na

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), kwa niaba ya FemAct.


Na kusaininwa na

……………………………
Lilian Liundi
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP

Monday, November 22, 2010

‘Panga’ lawasubiri manaibu waziri

IWAPO Rais Jakaya Kikwete atatekeleza matakwa ya wananchi ya kupunguza ukubwa wa Baraza la Mawaziri, kuna uwezekano kuwa nafasi zitakazopunguzwa ni za manaibu waziri.

Baraza lililomaliza muda wake lina manaibu waziri 21 huku Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi pamoja na Wizara ya Fedha zikiwa na manaibu waziri wawili kila moja huku wizara zingine 17 kati ya 26 zilizoundwa katika Baraza hilo zikiwa na naibu waziri mmoja.

Wizara saba hazina manaibu waziri, lakini wachambuzi wa mambo ya siasa wamedokeza kuwa kuna uwezekano Rais Kikwete akaendelea kupunguza idadi ya manaibu waziri ili kutoa fursa ya mawaziri kufanya kazi kwa karibu na makatibu wakuu wa wizara.

Kwa mfumo wa wizara, kila wizara ina Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu.

Wizara pia zina wakurugenzi wa idara mbalimbali ambao wanamsaidia Katibu Mkuu hali
iliyoelezwa kuwa inatoa fursa kwa waziri kumudu majukumu ya kazi hata pasipo kuwepo na naibu wake.

Waziri anayeteuliwa na Rais kazi yake kubwa ni kusimamia sera za Serikali iliyoko madarakani na kuhakikisha kuwa Ilani ya chama kilichoko madarakani itatekelezwa na wizara husika.

Makatibu wakuu ndio watendaji ambao mara zote wamekuwa wanasimamia maelekezo na sera za Serikali na kuhakikisha kuwa malengo yaliwekwa na wizara husika kwa kila mwaka yanafikiwa.

Ni kutokana na hali hiyo wachambuzi wanaamini kuwa Rais Kikwete atapunguza manaibu waziri katika baadhi ya wizara. Wizara ambazo kwa sasa hazina manaibu waziri ni Ardhi, Katiba na Sheria, Utawala Bora, Muungano, Utumishi, Sera na Uratibu na Bunge pamoja na Mazingira.

Wizara inayoweza kutokuwa na manaibu waziri ni Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ambayo waziri wake mara nyingi shughuli zake zinafanywa na Mkuu wa Majeshi anayeshirikiana na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa.

Wizara ya Jinsia, Wanawake na Watoto nayo inaweza isipewe naibu waziri pamoja na Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi iliyoundwa na Rais Kikwete ili kuhamasisha ufugaji bora na uboreshaji wa sekta ya uvuvi.

Wizara nyingine ambayo inaweza isiwe na naibu waziri ni Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na Wizara ya Kazi, Maendeleo ya

Vijana na Ajira. Wachambuzi hao pia wamebainisha kuwa ni ngumu Rais Kikwete kupunguza Baraza la Mawaziri hasa kutokana na vipaumbele vya Serikali yake ambavyo viko 13.

Baraza la sasa lina mawaziri 26 ukiacha Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, Rais wa Zanzibar na Rais mwenyewe hivyo kulifanya Baraza hilo kuwa na watu 30.

Lakini Rais pia anaweza kuunganisha baadhi ya wizara ili kuleta ufanisi zaidi na kuepusha migongano ya kikazi, hali ambayo imefanya baadhi ya mambo yasishughulikiwe kutokana na wizara hizo kutupiana mpira.

Iwapo ataunda Baraza kwa kuzingatia vipaumbele hivyo ina maana kuwa kutakuwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi ili kukuza amani na usalama.

Pia kutakuwa na Wizara ya Muungano ambayo iko katika Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo kama atahitaji kupunguza Baraza, atalazimika kuchanganya na Mazingira ambayo nayo iko katika Ofisi ya Makamu wa Rais ili zishikwe na waziri mmoja badala ya mawaziri wawili kama ilivyokuwa hapo awali.

Katika hotuba yake ya kulizindua Bunge, Alhamisi iliyopita mjini Dodoma, Rais Kikwete alikiri kuwa zimebaki kero ndogo ndogo za Muungano, hali inayoonesha kuwa kwa kuwa suala hilo pia husimamiwa na kamati maalumu waziri wake lazima aongezewe majukumu ambayo wachambuzi hao wanahisi ni ya mazingira.

Lakini wengine wanasema kama Waziri huyo ataongezewa jukumu la mazingira, atalazimika kuongeza juhudi za kuhifadhi mazingira hasa wakati huu ambapo makali ya athari za mabadiliko ya tabianchi yanazidi kuiumiza nchi.

Katika Ofisi ya Rais, kunatarajiwa kuwepo na Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambavyo ni moja vya vipaumbele vyake.

Ili kutekeleza jukumu la kuimarisha uhusiano mzuri uliopo baina ya nchi jirani na mataifa mengine lazima, Rais ataunda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Wizara hiyo ya Afrika Mashariki inaweza isiwe na naibu waziri huku Wizara ya Mambo ya Nje lazima itakuwa na naibu waziri ambaye atatoka sehemu moja ya Muungano kutokana na wizara hiyo kuwa ya Muungano.

Wamesema Wizara ya Maliasili na Utalii nayo lazima itakuwepo, lakini pia licha ya umuhimu wake wadadisi wanadokeza kuwa pia naweza kuwa na naibu waziri.

Lakini pia Rais anaweza kuunganisha Wizara ya sasa ya Kilimo, Chakula na Ushirika pamoja na mambo ya umwagiliaji akaiondoa kwenye Wizara ya Maji ambayo inaweza kubaki peke yake.

Kwa vile kilimo kinachosisitiziwa kwa sasa ni cha mwagiliaji, kuna uwezekano wizara hiyo ikawa moja.

Lakini kutokana na vipaumbele vya Serikali, matazamio ya kupunguzwa Baraza hilo yatakuwa ni madogo na kama akifanya hivyo, Rais anaweza kuua wizara tatu na kuziacha zingine 23 zikiendelea kuwepo, lakini kwa kiasi kikubwa akipunguza idadi ya manaibu waziri.

Rais Kikwete anatarajiwa kutangaza Baraza lake la Mawaziri siku yoyote wiki hii.

Friday, November 19, 2010

JK atoa vipaumbele miaka 5

RAIS Jakaya Kikwete amelizindua Bunge la 10 na kutaja vipaumbele vyake 13 atakavyovizingatia katika miaka mitano ijayo ya Serikali yake, huku akiahidi kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha za serikali.

Sambamba na hilo, ameeleza utayari wake kulivalia njuga na kuondoa nyufa za mgawanyiko wa kidini uliotokana na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu.

Rais Kikwete alisema “nitaboresha zaidi ukusanyaji wa mapato ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa pamoja na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha na mali za umma…naahidi tutajipanga zaidi kusukuma kwa nguvu nidhamu na uwajibikaji katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.”

Alitaja kipaumbele kingine ni kuhakikisha kunakuwa na umoja, amani na usalama na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar unaendelea kudumu na kuimarika na kuahidi kero chache za Muungano zilizosalia ambazo hazijapatiwa ufumbuzi, kupatiwa ufumbuzi ulio muafaka kwa pande zote mbili.

Pia Serikali yake katika miaka mitano ijayo itaendeleza juhudi za kukuza uchumi na kupunguza umasikini kwa kuchukua hatua thabiti za kuharakisha mapinduzi ya kilimo, ufugaji, uvuvi na viwanda na kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara ili kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

Katika kufanikisha hilo, alisema bajeti ya kilimo itaendelea kuongezwa na kufikia asilimia 10 na kuhimizwa kilimo cha umwagiliaji; kuongeza juhudi za ujenzi wa viwanda vipya na kurahisisha taratibu za utoaji wa leseni za biashara na upatikanaji wa malighafi na ardhi.

Serikali ijayo itawawezesha wananchi kiuchumi na kuboresha mipango ya kusaidia wajasiriamali wadogo na wanaotaka kujiajiri, kuwatambua na kuwawezesha wajasiriamali wa kati, ili washiriki katika uwekezaji mkubwa wa ndani na nje ya nchi.

Rais Kikwete ameahidi kujenga na kuimarisha sekta binafsi na kutengeneza mazingira mazuri ya ushirikiano na sekta ya umma pamoja na kuifanya Tanzania kuwa lango kuu la biashara na usafirishaji kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati hivyo kutaboreshwa miundombinu ya reli, barabara, viwanja vya ndege na teknohama.

Alitaja kipaumbele kingine ni kuongeza jitihada za kuhakikisha taifa linanufaika na maliasili zake kwa kuhakikisha kunakuwa na sera na sheria za uvunaji na matumizi ya rasilimali hizo zinazonufaisha taifa sawia ambapo sasa Shirika la Taifa la Madini (Stamico) kwa niaba ya serikali litaimarishwa ili kushiriki katika umiliki wa migodi mikubwa na ya kati na hivyo taifa kunufaika.

Vingine ni kukuza ajira hasa kwa vijana na kuongeza kasi ya kujenga majengo ya wafanyabiashara wadogo na kuongeza kuwa yatajengwa Dar es Salaam na Mwanza na baadaye katika miji mingine mikuu ya mikoa.

Alisema wataboresha elimu ya msingi na sekondari ambazo kwa sasa zinakabiliwa na changamoto na mkazo utakuwa katika masomo ya sayansi; kuboresha huduma za kijamii na uchumi kwa kuongeza fedha katika mifuko ya fedha, kuimarisha benki ya rasilimali na kuanzisha benki ya kilimo.

“Tutaendelea kutoa kipaumbele cha kwanza kwa bajeti ya elimu ili tufundishe na kuajiri walimu wengi zaidi, tupate vitabu na vifaa vya kujifunzia na kufundishia na kuongeza matumizi ya teknohama katika utoaji wa mafunzo na kujenga uwezo wa wanafunzi na walimu kiteknolojia ili kwenda sambamba na karne ya utandawazi,” alifafanua Rais Kikwete mbele ya wabunge.

“Tutaendelea kuimarisha uhusiano mzuri uliopo kati ya nchi yetu na majirani na mataifa mengine duniani na mashirika ya kimataifa na tutaendelea kutafuta marafiki wapya na kuboresha diplomasia ya uchumi na tutaongeza juhudi za kuhifadhi mazingira.”

Kwa upande wa afya, alisema huduma zitasogezwa zaidi kwa wananchi, kujenga uwezo wa ndani wa kutibu maradhi ili kupunguza watu wanaopelekwa nje kwa matibabu na bajeti ya afya itaendelea kuongezwa.

Kipaumbele cha mwisho ni kulinda mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na kukamilisha ahadi za mwaka 2005 ambazo hazijatekelezwa.

Rais Kikwete alisema mambo matatu aliyoyaahidi mwaka 2005 ataendelea kuyapa kipaumbele ambayo ni kuhakikisha nchi na watu wake wanakuwa wamoja na yenye utulivu na amani; kukuza uchumi na kupunguza umasikini na kuhakikisha demokrasia inastawi na serikali inaendeshwa kwa misingi ya utawala bora na kuendeleza mapambano ya rushwa na maovu katika jamii.

Akizungumzia kuhusu nyufa ya mgawanyiko wa kidini alisema; “hatuna budi kuchukua hatua za haraka kuziziba vinginevyo hatuna nchi, hatuna taifa, tutafanana na nchi nyingine tu. Nawahakikishia utayari wangu wa kushirikiana na wanasiasa wenzangu, viongozi wa dini na wa kijamii kulitafutia ufumbuzi suala hili.”

“Si vyema na si busara kuliacha likatoa mizizi na kulimong’onyoa taifa letu, nawaomba wenzangu mkubali tushirikiane tuinusuru nchi yetu,” alieleza Rais Kikwete. Kuhusu magereza, alisema, “tutalivalia njuga na kulipatia ufumbuzi muafaka tatizo kubwa la mlundikano wa wafungwa na mahabusu magerezani.”

Kwa upande wa kilimo na mifugo, alisema mavuno kwa mazao ya kilimo ya chakula na biashara yameendelea kuongezeka na mwaka huu, kipo chakula cha kutosha nchini.

Akizungumzia elimu, alisema Serikali yake itaendelea kutoa kipaumbele cha kwanza kwa bajeti ya elimu ili kufundisha na kuajiri walimu wengi zaidi, huku akisisitiza kwamba katika miaka mitano ijayo, “tutaendelea na upanuzi wa fursa za kupata elimu, lakini mkazo mkubwa tutauelekeza katika kuboresha elimu inayotolewa.”

Kuhusu mapato, alisema ukusanyaji mapato ya serikali umeongezeka kutoka wastani wa Sh bilioni 177.1 mwaka 2005 kwa mwezi hadi kufikia Sh bilioni 453 kwa mwezi hivi sasa, huku akiahidi kuongezwa maradufu jitihada za kukusanya mapato na kuimarisha matumizi ya serikali.

“Tutaboresha mfumo wa ukusanyaji mapato ya serikali na kupanua wigo wa walipa kodi. Tutakuwa wakali kuhakikisha mianya inayovujisha mapato inazibwa na pesa za umma zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa,” alifafanua Rais Kikwete na kuongeza: “Uzembe, wizi na ubadhirifu havitavumiliwa.

Tutaendelea kuzipa uzito unaostahili taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali na kuchukua hatua zipasazo kasoro zinapobainika. CAG akamate bila kusubiri Bunge.”

Akitoa hotuba ya kuahirisha Bunge, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alimpongeza Rais Kikwete kwa kutoa maelekezo mahsusi ya kutekeleza katika miaka mitano ijayo, akisema msingi wa maelekezo hayo ni Dira ya Maendeleo 2025, Mkukuta na Ilani ya Uchaguzi ya CCM na Malengo ya Maendeleo ya Milenia.

Alisema kama Waziri Mkuu anamuahidi Rais kuwa yeye pamoja na Baraza la Mawaziri litakaloundwa, kuwa karibu na wabunge, huku akieleza kuwa hotuba ya Rais inayo mambo mazuri kama vile kipaumbele cha umoja wa Watanzania akisema ni jambo lisilopaswa kugeuzwa la kawaida, kwani ni kubwa.

Mengine ni kupambana na umasikini, akisema bado ni changamoto kubwa na ameeleza jinsi Serikali yake itakavyokabiliana nayo katika kilimo, uvuvi na mifugo. “Ulipofafanua nikasema upele umepata mkunaji,” alisema Waziri Mkuu.

Jingine ni suala la ushiriki wa Tanzania katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, akisema ni lazima serikali kwa muda wote itoe maelezo ya kina ya hatua kwa hatua ambayo yanafikiwa kwa wananchi ili azma hiyo itimie kwa kunufaisha Watanzania wote.

Bunge limeahirishwa hadi Februari 8, mwakani. Aidha, wabunge mbalimbali waliipongeza hotuba ya Rais Kikwete, huku Mbunge wa Kilosa, Mustafa Mkulo akisema ameweza kuelezea mafanikio yake na ahadi ya Tume ya Mipango kuanza kazi Januari kutaifanya Tanzania kuwa na dira ya kuleta maendeleo.

Naye Mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwany (CUF), amesema hotuba hiyo imekidhi kutokana na kuelezea kuwa demokrasia itaimarika na kutekeleza suala la amani kwa kudhibiti ujambazi na mauaji ya albino.

Mbunge wa Isimani, William Lukuvi (CCM), alisema imetoa mwelekeo mzuri hasa aliposisitiza serikali iondoe urasimu na watu wachape kazi ambapo alifafanua “hapo tutaondoa kero za msingi na kupata mafanikio.”

Kikwete ataka mawaziri wabanwe

RAIS Jakaya Kikwete amewataka wabunge wawabane mawaziri katika Serikali yake lakini wawasahihishe wakiteleza.

Rais Kikwete pia amewaeleza wabunge kuwa, wasiwe wachoyo wa kuwasifu mawaziri wakifanya vizuri.

Kikwete ameyasema hayo mjini Dodoma wakati akihutubia Bunge la 10 na kulifungua rasmi.

Amewaeleza wabunge kuwa hivi karibuni atateua mawaziri makini, waadilifu na wachapakazi hodari.

Kwa mujibu wa Kikwete, atakaowateua wataiongoza nchi yetu kwa umahiri mkubwa katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na mipango ya Serikali.

Kikwete amesema, atateua watu watakaoondoa urasimu katika katika Serikali, watakuwa karibu na wananchi, na watashirikiana vizuri na wabunge bila kujali vyama vya siasa wanapotoka.

Rais Kikwete amewaomba wabunge wampe ushirikiano Waziri Mkuu kama walivyofanya katika Awamu ya Kwanza ya Serikali yake.

Kwa mujibu wa Kikwete, Serikali atakayoiunda itakuwa na vipaumbele 13 ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba, Tanzania inaendelea kuwa nchi yenye umoja na usalama, na kwamba, Muungano uendelee kudumu na kuimarika.

Ametaja kipaumbele kingine kuwa ni kuendeleza juhudi za kukuza uchumi na kupunguza umasikini kwa kuharakisha mapinduzi ya kilimo, ufugaji, uvuvi na viwanda.

Wabunge wameelezwa kuwa, kipaumbele kingine cha serikali itakayoundwa kitakuwa ni kuongeza jitihada za kuwawezesha kiuchumi wananchi wa makundi yote ili washiriki na kunufaika na uchumi unaokua.

Alisema, Serikali itaendelea kujenga na kuimarisha sekta binafsi nchini na kutengeneza mazingira mazuri ya ushirikiano na sekta ya umma sanjari na kuimarisha uwezo wa serikali kupanga mipango ya maendeleo na kusimamia utekelezaji wake bila kuingilia shughuli za sekta binafsi.

Rais Kikwete amelieleza Bunge kuwa, Serikali itatumia fursa ya kijiografia ya nchi yetu na kuifanya Tanzania kuwa lango kuu la biashara na usafiri kwa nchi za Afrika Mashariki na kati.

Bunge limeelezwa kuwa, Serikali pia itaongeza jitihada za kuhakikisha kuwa taifa letu linanufaika zaidi na maliasili zake zilizo juu na chini ya ardhi hivyo itahakikisha kwamba, kunakuwa na sera za uvunaji na matumizi ya rasilimali hizo.

Alisema, Serikali itaboresha ukusanyaji wa mapato ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa pamoja na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha na mali za umma.

Kikwete alisema, miaka mitano iliyopita ilikuwa migumu sana kwa kazi ya kujenga uchumi na kupunguza umasikini nchini kwa kuwa uchumi ulipata misukosuko mikubwa ukiwemo ukame uliokausha mazao mashambani.

“Hivi sasa uchumi wetu umekuwa tulivu tena, kasi ya ukuaji ni nzuri, mfumuko wa bei umeshuka sana kutoka wastani wa asilimia 12.1 mwaka 2009 hadi kufikia asilimia 4.2 hivi sasa” alisema.

Thursday, November 18, 2010

Kikwete amuapisha Pinda

RAIS Jakaya Kikwete amemuapisha Mizengo Pinda (62) kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania.

Rais Kikwete juzi alimteua Pinda kuwa Waziri Mkuu, Bunge likamthibitisha kwa kupiga kura.

Hii ni mara pili kwa Pinda kuapishwa kushika madaraka hayo, kwa mara ya kwanza aliapishwa Februari mwaka 2008 kuchukua nafasi ya Edward Lowassa.

Pinda ameapa kuwa mwaminifu kwa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na kuitumikia kwa moyo wake wote.

Mbunge huyo wa Katavi, pia ameapa kuihifadhi, kuilinda na kuitetea Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mwanasiasa huyo ameapa kuwa, atamshauri kwa hekima Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na hatatoa siri za Baraza la Mawaziri.

Katika kiapo hicho katika viwanja vya Ikulu Ndogo ya Chamwino, Dodoma, Pinda ameapa kuutetea na kuulinda umoja wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Viongozi wote wakuu wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar wamehudhuria sherehe za kumuapisha Pinda akiwemo Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein.

Wengine waliohudhuria ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Seif Ali Idd.

Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, mawaziri wakuu wastaafu, John Malecela, Frederick Sumaye, na Edward Lowassa pia walikuwepo wakati Pinda anaapishwa.

Viongozi wengine wakuu waliohudhuria sherehe hizo ni Spika wa Bunge la Tanzania, Anne Makinda, Naibu Spika wa Bunge hilo, Job Ndugai, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, aliyekuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta, Jaji Mkuu, Augustino Ramadhani, na Mkuu wa Majeshi, Davis Mwamunyange.

Makatibu wakuu wa Wizara, wakuu wa mikoa, watendaj wakuu wa taasisi za umma na binafsi, mabalozi wa nchi mbalimbali, na viongozi wa vyama vya siasa pia walikuwepo kwenye sherehe hizo.

Tuesday, November 16, 2010

Dk Shein ateua Baraza la Mawaziri la Kitaifa

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameunda Baraza jipya la Mawaziri lenye sura ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kwa kuwapa nafasi nyeti
baadhi ya vigogo wa juu wa Chama cha Wananchi (CUF).

Baraza hilo lenye wizara 16, pia limejumuisha baadhi ya manaibu waziri wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete iliyomaliza muda wake na mawaziri wa serikali iliyopita wa Serikali ya Dk.

Amani Abeid Karume, huku aliyekuwa Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha akiachwa.

Baadhi ya vigogo hao wa CUF walioteuliwa katika baraza hilo, yupo aliyekuwa mgombea mwenza wa urais wa Jamhuri ya Muungano katika Uchaguzi Mkuu uliopita, Juma Duni Haji
ambaye amepewa Wizara ya Afya.

Wengine wa CUF walioteuliwa katika baraza hilo ni pamoja na mwanamama Mwakilishi machachari wa CUF, Fatma Abdulhabib Fereji, ambaye ameteuliwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais.

Wengine kutoka CUF na nafasi zao katika mabano ni Aboubakar Khamis Bakary, ambaye
alikuwa Kiongozi wa Upinzani katika Baraza la Wawakilishi (Waziri wa Katiba na Sheria), Hamad Masoud Hamad aliyekuwa Waziri kivuli wa Miundombinu (Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano).

Pia yumo Abdilahi Jihad Hassan ambaye ni mwakilishi mpya wa Magogoni (Waziri waAhmed Mazrui aliyeteuliwa dakika za mwisho na Rais Karume baada ya maridhiano (Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko).

Dk Shein pia amemteua Said Ali Mbarouk aliyekuwa Waziri Kivuli wa Fedha (Waziri wa Mifugo na Uvuvi), Haji Faki Shaali aliyekuwa Waziri kivuli Uratibu wa Shughuli za Baraza
la Wawakilishi (Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na Waziri asiyekuwa na Wizara Maalumu).

Wengine kutoka CUF ambao wameteuliwa kuwa manaibu waziri ni Zahra Ali Hamad (Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali), Bihindi Hamad Khamis ( Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo) na Haji Mwadini Makame (Naibu Waziri wa Ardhi, Makazi,
Maji na Nishati).

Mawaziri kutoka CCM ni pamoja na Dk. Mwinyihaji Makame (Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Ikulu), Omar Yussuf Mzee, aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi Serikali ya Muungano (Waziri Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo).

Wengine ni Haji Omar Kheri ambaye alikuwa Waziri anayeshughulikia Uratibu wa Shughuli za Baraza la Wawakilishi (Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora), Mohammed Aboud Mohammed aliyekuwa Naibu Waziri wa Afrika Mashariki katika Serikali ya Muungano (Waziri Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais).

Wengine ni Ramadhan Abdulla Shaaban ambaye alikuwa Waziri wa Katiba na Utawala Bora (Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali), Zainab Omar Mohammed aliyekuwa Waziri asiye na Wizara Maalumu anayeshughulikia Pemba (Waziri wa Ustawi wa Jamii na Maendeleo ya
Wanawake na Watoto).

Mawaziri wengine kutoka CCM ni aliyekuwa Naibu Waziri Kiongozi, Ali Juma Shamhuna (Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati), Mansoor Yussuf Himid aliyekuwa Waziri wa
Nishati, Ujenzi na Maji (Waziri wa Kilimo na Maliasili).

Pia yupo Haroun Ali Suleiman aliyekuwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali (Waziri wa Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika), Suleiman Othman Nyanga, aliyekuwa Waziri wa Tawala za Mikoa (Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na Waziri asiyekuwa na Wizara
Maalumu) na Machano Othman Said, aliyekuwa Waziri wa Mawasiliano ( Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na Waziri Asiekuwa na Wizara Maalum).

Katika unaibu waziri, Dk Shein amemteua Issa Haji Ussi (Naibu Waziri ya Miundombinu na Mawasiliano), mmoja wa wawakilishi wapya walioteuliwa na Rais, Dk. Sira Ubwa Mamboya ( Waziri wa Afya) na Thuwaiba Edington Kissasi (Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko).

Mbali na Nahodha, wengine walioachwa ni Samia Suluhu Hassan (Utalii, Biashara na Uwekezaji), Burhan Saadat Haji (Kilimo na Mifugo) na Asha Abdallah Juma (Kazi na
Maendeleo ya Wanawake na Watoto).

Wengine walioachwa ni Sultan Mohamed Mugheiry (Afya na Ustawi wa Jamii Taffana Kassim Mzee (Naibu Waziri wa Nishati, Aridhi na Maji) Shawana Buheit Hassan (Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii ).

Pia yumo Khamis Jabir Makame (Naibu Waziri Elimu na Vyuo vya Ufundi), Khatib Suleiman
(Naibu Waziri wa Kilimo na Mifugo) na Mahmoud Thabit Kombo (Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo).

Mawaziri wapya wataapishwa rasmi leo jioni katika viwanja vya Ikulu, Zanzibar.

Chadema waanza mchakato wa kudai tume huru ya uchaguzi.

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimesisitiza bado hakiyatambui matokeo yaliyotangazwa na tume ya Taifa ya uchaguzi na kumpa ushindi Rais Jakaya Kikwete ,lakini imefafanua kuwa hatua hiyo haina maana kwamba wabunge wake na madiwani hawatatekeleza wajibu wao.

Chama hicho kimesema kuwa kutokana na mfumo uliopo sasa kuendelea kupendelea chama tawala, tayari kimeanza mchakato wa kudai tume huru ya uchaguzi kupitia Bunge na mabadiliko ya katiba ili uwanja wa kisiasa uweze kutoa fursa sawa kwa wote.
Mwenyekiti wa Chama hicho Bwana Freeman Mbowe amewaambia waandishi wa habari Mjini Dodoma kuwa amesema kuwa ni muhimu sasa kuundwa kwa tume maalumu kwa ajili ya kufuatilia mwenendo wa uchaguzi uliopita ili hatimaye ibainishe kasoro zilizopo na kutoa majibu sahihi kwa nini wananchi wengi hawakujitokeza kupiga kura.

Kwa upande wake aliyekuwa mgombea wa kiti cha Urais kupitia CHADEMA Dokta Willbroad Slaa amesema yupo tayari kutaja majina ya maofisa wa usalama wa Taifa waliohusika katika kuvuruga zoezi la uchaguzi iwapo majina hayo yatahitajika kama ushahidi mahakamani maana kitendo kilichofanywa ni kosa la jinai.

Monday, November 15, 2010

UWT wamtabiria Pinda

WAKATI kesho Rais Jakaya Kikwete anatarajiwa kumteua Waziri Mkuu, Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT), umeanza kumtabiria Waziri Mkuu aliyemaliza
wake, Mizengo Pinda, kuwa atateuliwa tena kushika wadhifa huo.

Hata hivyo, Pinda amewaambia kuwa anaogopa, kwani Rais Kikwete anaweza kusema wanampangia, hivyo akafuta uteuzi wake, lakini kama atarejeshwa, ameahidi kushirikiana naye.

Wanawake hao walieleza hisia zao wakati wa sherehe za kumpongeza Spika wa Bunge, Anne Makinda kwa kuchaguliwa kushika wadhifa huo, zilizofanyika jana mjini hapa.

Sherehe hizo ziliandaliwa na UWT Mkoa wa Dodoma pamoja na wabunge wanawake.
Mwanamke wa kwanza kutoa utabiri huo alikuwa Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Dodoma, Fatma Tofiq wakati akitoa risala yawanawake hao, kwa kumtaja Pinda kama Waziri Mkuu mtarajiwa.

Alipompa nafasi ya mke wa Pinda, Tunu Pinda kuwasalimia na kuzungumza na wanawake waliofika katika sherehe hizo, wakati akitoa utangulizi alisema, “Waziri Mkuu mstaafu si ndiyo (akacheka)… Waziri Mkuu mtarajiwa…hapo sawaaaaa (watu wakacheka) na Mbunge wa
Katavi… tumeanza vizuri kuwa na Spika mwanamke na natarajia miaka ijayo, Waziri Mkuu pia atakuwa mwanamke.”

Naye Mwenyekiti wa UWT Taifa, Sophia Simba wakati akitoa utambulisho, alimtaja Pinda kama Waziri Mkuu mtarajiwa akiamini rais atamteua tena.

Hata hivyo, Pinda alipopewa nafasi kusalimia hadhara hiyo, alisema “nimeogopa mlivyosema mimi Waziri Mkuu Mtarajiwa kwa sababu Mzee Kikwete anaweza kusikia akasema mnanipangia, sitaki sasa…kama nitakuwa bounceback (kurejea tena) nitashirikiana
naye”.

Naye Makinda alipopewa nafasi kama mgeni rasmi kutoa hotuba yake, alianza kwa kusema
“Mheshimiwa bounceback” na ndipo watu wakacheka.

Rais Kikwete kesho anatarajiwa kupeleka bungeni jina la mteule wake wa nafasi ya Waziri Mkuu ambalo litapigiwa kura na wabunge ili kuidhinishwa kushika wadhifa huo, kama Katiba inavyoelekeza.

Pinda aliyeingia madarakani Februari 2008, baada ya kujiuzulu kwa Waziri Mkuu wa kwanza
aliyeanza na Rais Kikwete katika Awamu ya Nne, Edward Lowassa, anatajwa kupewa nafasi ya kuendelea na wadhifa huo katika kipindi hiki cha pili na cha mwisho kikatiba kwa Rais Kikwete.

Uadilifu wake na uwezo mkubwa wa kusimamia shughuli za serikali zikiwamo za Bunge; kubana na kusimamia kikamilifu matumizi ya fedha za serikali na kutojihusisha na makundi ndani ya chama chake, ni mojawapo ya sifa zinazompa nafasi kubwa Pinda kuendelea na
kiti hicho katika kipindi chake cha mwisho cha miaka mitano kama mbunge baada ya kutangaza kutowania tena nafasi hiyo mwaka 2015.