Friday, June 29, 2012

Baba wa Dk. Ulimboka aangua kilio MOI

Baba wa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, mzee Steven Mwaitenda akilia hospitalini Muhimbili alipokwenda kumwona mtoto wake.
Baadhi ya wanaharakati wakiwa na nyoso za hudhuni baada ya kilio cha baba wa Dk. Ulimboka jana MOI.
Baba wa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, mzee Steven Mwaitenda (kushoto) akipokea ua kutoka kwa mwakilishi wa wanaharakati anuai waliomtembelea kumfariji.

Na Joachim Mushi, Thehabari.com
BABA wa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, mzee Steven Mwaitenda amejikuta akiangua kilio kwa uchungu mbele ya wanaharakati ambao walimtembelea mwanae, Dk. Steven Ulimboka kumpa pole kufuatia tukio la kutekwa na kujeruhiwa vibaya na watu wasiojulikana.

Hali hiyo ilitokea jana jioni katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI), ambapo wanaharakati kutoka taasisi na asasi mbalimbali za utetezi wa haki za binadamu walifika kwa lengo la kumpa pole Dk. Ulimboka kufuatia kitendo kilichomfika.

Mzee Mwaitenda alijikuta akibubujikwa na machozi na kushindwa kuendelea kuzungumza alipokuwa akitoa shukrani kwa wanaharakati hao, kwa niaba ya mwanaye ambaye wanaharakati hao walishindwa kumuona wote kutokana na hali yake ilivyo sasa.

“Niseme wazi nimefarijika sana kwa ujio wenu kumwona mwanangu dhidi ya mambo ya kikatili aliyofanyiwa akitetea haki za wengine…,” alisema mzee Mwaitenda kabla ya kushindwa kuendelea na kuangua kilio mbele ya wanaharakati.

Baada ya tukio hilo baadhi ya wanaharakati walimshika wakishirikiana na wanafamilia ya mzee Mwaitenda na kumbebeleza kisha kumtoa mbele ya mkusanyiko huo wa wanaharakati na kumrudisha wodini huku wakimfariji.

Wakizungumza mara baada ya tukio hilo wanaharakati wameelezea kusikitishwa na vitendo vinavyoendelea MOI eneo ambalo amelazwa kiongozi huyo wa madaktari ambavyo vimeendelea kutishia usalama wa Dk. Ulimboka.

Akifafanua zaidi mwakilishi wa wanaharakati hao, Markos Albania alisema taarifa walizozipata usiku wa juzi kuna wagonjwa ‘feki’ ambao walijitokeza MOI huku wakitaka kulazwa wodi ya Wagonjwa Mahututi (ICU) alipolazwa Dk. Ulimboka lakini baadaye waligoma kuingizwa wodini.

“Wapo wagonjwa ambao waliletwa na kutaka kupelekwa ICU moja kwa moja…kuna watu wanakuja usiku wa manane wakitaka kumtembelea Dk. Ulimboka…matendo yanayoendelea kutokea ukilinganisha na kauli za Serikali zilizotolewa bungeni yanatishia usalama na uhai wa mgonjwa,” alisema Albania.

Aidha amesema kitendo cha vyombo vya usalama kuendelea kumuhoji Dk. Ulimboka akiwa hoi hospitalini si vya kiungwana kwani tayari muhusika amewataja hadi kwa majina watu ambao anawashuku lakini hadi sasa hakuna aliyechukuliwa hatua yoyote.

Pamoja na hayo wanaharakati hao wameitaka Serikali kuunda tume huru mchanganyiko na raia ambayo itachunguza kiundani suala hilo, kwani hawana imani na Jeshi la Polisi ambalo limedai kuunda timu ambayo inachunguza kwa kina suala hilo.

Dk. Ulimboka ambaye ni kiongozi wa madaktari ambao wanaendelea na mgomo wan chi nzima kuishinikiza Serikali kutekeleza madai yao alitekwa juzi na watu wasiojulikana na kupigwa na kuteswa kikatili kabla ya kutelekezwa katika msitu wa Mabwepande.

Hata hivyo taarifa ambazo bado hazijathibitishwa zilizoufikia mtandao huu zinasema tayari madaktari kadhaa mikoani wamefukuzwa kazi na wale waliopo katika mafunzo ya huduma kwa vitendo kufuatia mgomo unaoendelea nchini kote.

Thursday, June 28, 2012

Chadema yalaani Dk Ulimboka kushambuliwa

Na Boniface Meena
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), kimelaani kukamatwa na kushambuliwa kwa viongozi wa madaktari ikiwamo Dk Ulimboka Steven ikieleza kuwa hatua hiyo haiwezi kuwa suluhu bali itachochea zaidi mgogoro wa madaktari na Serikali.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika inaeleza pia kwamba udhaifu wa Serikali kuharakisha kwenda mahakamani kabla ya Bunge kupewa fursa ya kujadili madai ya madaktari na kuisimamia Serikali umelifikisha taifa katika hali iliyopo sasa.

"Nalaani uamuzi wa Serikali wa kutumia vyombo vya dola kukamata na kushambulia viongozi wa madaktari ikiwemo Dk Ulimboka Steven kwa hauwezi kuwa suluhu bali utachochea zaidi mgogoro kati ya madaktari na Serikali," ilisisitiza sehemu ya taarifa hiyo ya Mnyika na kuongeza:

 “Nichukue fursa hii kuwaomba madaktari kufanya kila kinachowezekana kuokoa uhai wa wagonjwa katika kipindi hiki kigumu.” Mnyika alisema kuwa ameomba wabunge wapewe nakala ya Taarifa ya Kamati ya Huduma za Jamii kuhusu madai ya madaktari na hoja ya taarifa husika iwekwe katika orodha ya shughuli za Bunge katika mkutano wa Bunge unaoendelea ili ijadiliwe na kupitisha maazimio, kuwezesha hatua za muda mfupi, wa kati na muda mrefu kuupatia ufumbuzi mgogoro huo na kuboresha sekta ya afya nchini.

 “Natarajia kwamba Spika atawezesha kamati kuwasilisha taarifa yake na Bunge kujadili baada ya Serikali kutoa kauli yake bungeni,”alisema.  Mnyika alisema ikiwa wabunge wataelezwa ukweli na kupewa taarifa kamili wataweza kuisimamia Serikali na kuwaeleza ukweli madaktari kipi kinawezekana na kipi hakiwezekani.  

Alisema kuwa ingawa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ametoa maelezo bungeni kuwa Serikali itatoa kauli bungeni kuhusu mgomo huo, Bunge halitaruhusiwa kujadili kauli husika, hivyo kukoseshwa fursa ya kuisimamia Serikali kwa niaba ya wananchi.

Wednesday, June 27, 2012

Dr. Ulimboka kutekwa, kupigwa na kuumizwa: Serikali inawajibika kutueleza

Ujumbe huu chini ametumiwa Zitto Kabwe na Daktari yupo pale MOI
‘Kaka Zitto,hali ya Dr.Ulimboka yuko unconscious,multiple ribs fracture na kwenye mikono pia amevunjika pamoja na taya,yuko icu wanamstabilise kwanza kwasababu hapumui vizuri,the situation here is really bad,I agree with you this is outright outrageous’
Nimechukizwa sana na habari za kutekwa, kupigwa na kuumizwa vibaya kwa Dr Ulimboka, Kiongozi wa Madaktari Nchini. Mambo kama haya tumezoea kuyasikia kwenye nchi za kidikteta na kuongozwa kiimla ambapo watawala badala ya kutumia njia ya kidemokrasia na kisheria kushughulikia wanaoamini ni maadui zao katika utawala, hutumia wahuni katika Taasisi za usalama kuteka raia, kuwatesa, kuwafunga na hata kuwaua. Sitaki kuamini kwamba Tanzania imefikia huko.

Nimezungumza na baadhi ya madaktari walio karibu na Dokta Ulimboka na kujulishwa kwamba majeruhi huyu wa vitendo vya hovyo kabisa kutokea hapa nchini alikamatwa jana usiku mnamo saa sita na watu wasiojulikana na kupelekwa katika msitu wa MagwePande na kujeruhiwa vibaya. Habari hizi bado hazijathibitishwa na vyanzo huru lakini ndio zilizopo hadi hivi sasa.

Serikali kama mlinzi wa usalama kwa raia inaWAJIBU kueleza tena kwa haraka ni nini kimetokea kwa kijana huyu msomi na kiongozi wa wataalamu wenzake. Serikali INAWAJIBIKA kueleza katika nyakati kama hizi ambapo kuna mgogoro kati yake na madaktari imekuwa wapi kuhakikisha usalama wa viongozi wa madaktari ili kuepusha watu wanaoitwa ‘agente provocateure‘ kuweza kuhatarisha hali ya amani ya nchi na hata kupelekea kuweka hali ya vitisho kwa madaktari wetu. Serikali INAWAJIBIKA kueleza kama sasa imeamua kutumia njia za kihuni kumaliza matatizo na wananchi wake.

 Nimemuomba Waziri kivuli wa Afya wa CHADEMA kufuatilia suala hili kwa kwa karibu sana ili kuhakikisha kwamba ukweli wote na ukweli mtupu unafahamika. Kamwe hatuwezi kuacha Mtanzania yeyote aonewe, anyanyaswe au akandamizwe eti kwa sababu ya kudai haki yake na za wenzake. ‘An injury to one, injuries to all’ Naomba madaktari wamwangalie kwa karibu daktari mwenzao ili aweze kupata nafuu. Ulinzi uimarishwe ili kuhakikisha usalama wake.

Bilioni 300 za vigogo Uswisi zatikisa nchi

ZITTO AMTAKA PINDA ATAJE WAHUSIKA, WANANCHI WATAKA FEDHA ZIREJESHWE, MABILIONI ZAIDI YAIBWA MTANDAONI

KUBAINIKA kwa Sh303.7 bilioni zilizofichwa katika akaunti za vigogo wa Serikali na wanasiasa nchini Uswisi, kumetikisa nchi huku shinikizo likitolewa kwa vyombo vya dola kuchunguza haraka na kuchukua hatua za kisheria, ikiwamo kurejesha fedha hizo.

Jana kutwa nzima, gazeti hili lilipokea simu kadhaa kutoka kwa wasomaji wake wakiwamo wabunge na mawaziri, huku baadhi wakichangia maoni kwenye tovuti na mtandao mbalimbali ya kijamii, wakitaka kujua majina ya wamiliki wa akaunti hizo.

Bungeni mjini Dodoma, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe aliitaka Serikali kuchunguza tuhuma hizo kisha kuwachukulia hatua watu sita wanaotajwa kwamba wanamiliki akaunti zenye mabilioni hayo ya shilingi chini Uswisi.

Fedha hizo zimebainishwa na ripoti ya Benki ya Taifa ya Uswisi (SNB), iliyotolewa hivi karibuni, ikitaja nchi mbalimbali ikiwamo Tanzania, na kiwango cha fedha zilizohifadhiwa huko.

Tayari Kitengo cha Polisi wa Kimataifa (Interpol) nchini kimeeleza kuwapo kwa fedha hizo katika benki mbalimbali nchini Uswisi, zilizoingizwa na kampuni za uchimbaji mafuta na madini.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nayo imeweka bayana kuwa inafuatilia suala hilo kwa mamlaka za Uswisi, ili kujua fedha hizo ziliko na nani anazimiliki.

Mbali ya Tanzania, nchi nyingine ambazo zina fedha nyingi katika benki za Uswisi ni Kenya (dola 857 milioni), Uganda (dola 159 milioni), Rwanda (dola 29.7 milioni) na Burundi dola 16.7 milioni.

Chanzo cha habari hizo, kilieleza kuwa tangu akaunti hizo zifunguliwe, wamiliki wake halali hawajawahi kuingiza hata shilingi moja.

Kauli ya Zitto
Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, aliliambia Bunge jana kuwa haiwezekani nchi ikaendelea ilhali watu wanakusanya fedha kutokana na utafiti wa gesi na mafuta, ambao bado haujaanza kulinufaisha Taifa.

Akichangia Bajeti ya Waziri Mkuu, Zitto alisema Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB) ielekezwe ili ifanye uchunguzi utakaowezesha wamiliki wa akaunti hizo kufahamika, ili wachukuliwe hatua mara moja bila kujali nafasi wanazozishikilia ndani ya Serikali.

“Viongozi wanaohamisha na kupeleka fedha za Watanzania nje ya nchi wanatakiwa wachukuliwe hatua mara moja. Hili litatusadia katika siku zijazo, kwani kama wapo wengine wanaodhani wanaweza kuficha fedha zao nje basi wajue kwamba popote watakapozipeleka tutazifuata na kuzirejesha,” alisema Zitto na kuongeza;

“Namuomba Waziri Mkuu aagize uchunguzi ufanyike, fedha hizi zirejeshwe na wahusika wachukuliwe hatua,” alisema Zitto.
Zitto alitoa kauli hiyo akiyanukuu magazeti ya Mwananchi, The Citizen na The East African ambayo kwa nyakati tofauti yameandika kuhusu kuwapo kwa kiasi kikubwa cha fedha zinazotokana na rushwa, ambazo zimehifadhiwa kwenye akaunti kadhaa nchini Uswisi.

Alisema kuachia suala hilo kuendelea ni hatari, kwani uchumi wa nchi utahujumiwa hata kabla ya miradi husika haijaanza kutekelezwa.

“Haiwezekani sisi tupo tunahangaika kutafuta gesi na mafuta huko baharini Lindi na Mtwara, halafu watu wengine tayari wameishawekewa hela kwenye akaunti, kwa hakika lazima uchunguzi ufanyike na watu hawa wajue kwamba Serikali ina uwezo wa kuwafahamu na kurejesha hizo fedha hizo nchini,” alisema Zitto.

Alitoa mfano wa Serikali ya India ambayo iliwahi kupata taarifa za baadhi ya watumishi wake kuficha fedha nchini Uswisi na kuchukua hatua za kiuchunguzi zilizowezesha wahusika kutajwa hadharani, kisha fedha zilizoibwa serikalini kurejeshwa.

Katika hatua nyingine, Zitto alitaka mvutano baina ya Tanzania Bara na Visiwani kuhusu masuala ya gesi umalizwe ili kuwezesha utafiti kuendelea kufanywa katika maeneo ya bahari ya Hindi.

Alisema utafiti katika baadhi ya maeneo hasa eneo la Bahari karibu na kisiwa cha Pemba umesimama kutokana na mvutano wa iwapo suala la mafuta ni la Muungano au la.

“Kama visiwani watavumbua gesi ni sawa, wavumbue kivyao, na sisi Tanzania bara tumeshavumbua matrilioni ya gesi, basi tuendelee kivyetu lakini tusisimamishe tafiti kutokana na mvutano usio na maslahi kwa nchi,” alisema.

Lowassa atoa kauli
Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Nje ya Bunge Edward Lowassa, alisema jana kuwa kamati yake imesikia suala hilo kwenye vyombo vya habari na inajipanga kuzifanyia kazi taarifa hizo mara moja.

"Tumesikia kupitia vyombo vya habari na kama kamati tutahakikisha tunazifanyia kazi," alisema Lowassa alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari katika mkutano aliouitisha kuzungumzia safari ya kamati yake nje ya nchi.

Chadema yatoa tamko
Kwa upande wake, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeonya kuwa tatizo la ufisadi halitaisha nchini hadi pale Serikali itakapochukua hatua za dhati za kuwakamata na kuwafikisha mahakamani watu wote ambao wamehusika na ufisadi wa raslimali za nchi.

Chama hicho kimemtaka Rais Jakaya Kikwete kutumia mamlaka yake ya kikatiba kuagiza kukamatwa kwa watuhumiwa wote wa ufisadi wa ununuzi wa rada na wale ambao wanatuhumiwa kuhifadhi Sh 303.7 bilioni nchini Uswisi.

“Chadema kinatambua kwamba kuachwa kwa mafisadi bila kuchukuliwa hatua kamili za kisheria na mali zao kufilisiwa, kunafanya taifa kuendelea na ufisadi ikiwemo ule wa Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), Richmond na sasa tuhuma mpya za ufisadi wa shilingi bilioni 303 kwenye akaunti Uswisi,” ilisema Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika, kupitia taarifa kwa
vyombo vya habari jana.

Wizi mwingie kupitia mtandao
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Pereira Ame Silima alilieleza Bunge jana kuwa hadi sasa kiasi kilichoripotiwa Polisi kuhusina na wizi kwa njia ya mtandao nchini ni Sh2.2 bilioni.
Fedha hizo ni zimegawanywa katika makundi matatu, Sh1.3 bilioni, Euro 8,897 (Sh17,660, 545) na dola 551,777 (Sh882,843,200).

Kauli hiyo ilitolewa wakati Waziri Silima akijibu swali la Hussein Mussa Mzee (Jang’ombe-CCM) aliyetaka kujua ni kiasi gani cha fedha kimeripotiwa Polisi kutokana na wizi kwa njia ya mtandao.
Mzee alihoji Serikali imejipanga vipi kudhibiti wizi wa mtandao, idadi ya waharifu wa wizi huo ambao wamekamatwa huku akitaka itungwe sheria maalumu kushughulikia wizi huo.
Silima alisema kuwa Serikali imetunga sheria inayoshughulikia uhalifu unaofanywa kwa njia ya mtandao, Electronic and Posta Communication Act, 2010 na sheria ya kudhibiti fedha haramu (The Anti – Money Laundering Act – 2006.

Aliongeza kuwa Serikali kupitia vyombo mbalimbali vya dola kama vile Polisi, taasisi za fedha, vyombo vya habari, TRA na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania imejiwekea mikakati ya kuelimisha wananchi kuhusu aina ya uharifu wa kimtandao na jinsi ya kupambana nao.
Waziri alibainisha kuwa jeshi la Polisi limeanzisha Kitengo cha Makosa ya Kimtandao (Cyber Crime Unit) ambacho kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kinafanya kazi kubwa ya kupambana na majanga hayo.
Kilio cha wabunge

Wakati huohuo wabunge wameendelea kumbana Pinda huku baadhi yao wakikataa kuunga mkono hotuba yake hadi pale atakapojibu hoja walizotoa.

Mbunge wa Nkasi Kaskazini (CCM), Ally Keissy akichangia hotuba ya hiyo jana, alisema vita dhidi ya ufisadi haiwezi kufanikiwa kwani vyombo vya husika wakiwamo Takukuru wanashindwa kuchukua hatua kwa makosa ambayo yako wazi.

Keissy alisema mafisadi na walarushwa nchini wanalindwa na Takukuru, kwani licha ya kuwapo kwa ushahidi na viashiria vya wazi, chombo hicho hakichukui hatua zozote.

Alisema, kama wapo watu wanaodiriki kuuza dawa ambazo zilipaswa kupelekwa katika hospitali na matokeo yake wagonjwa wanakufa, mtu huyo hana budi kunyongwa.

“Sheria za nchi hii zinawalinda wezi, ndiyo maana ufisadi hauwezi kuisha, mtu ana majengo makubwa leo, wakati ni jana tu amepata ubunge, amepata wapi utajiri huo wa haraka, aulizwe na akishindwa kutoa maelezo achukuliwe hatua,” alisema Keissy na kuongeza:

“Sasa la ajabu ni kwamba eti wanakwambia kwamba kama unamjua mla rushwa basi uwapelekee taarifa, kwani wao hawawaoni watu wanaotajirika haraka haraka?” alihoji.

Keissy ambaye aliipinga Bajeti ya Waziri Mkuu hadi pale atakapopewa majibu ya kuridhisha, alisema sheria za nchi hii ni dhaifu, ndiyo maana mafisadi wanaoiba mamilioni wanaendelea kudunda barabarani wakati mwizi anayeiba simu hupigwa na kuchomwa moto hadi kufa.

Mbunge huyo alisisitiza ujumbe wake, akisema kuwa, “hata ikitokea mafisadi hao wakafariki basi pingu ziwekwe juu ya makaburini yao.”

Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Riziki Lulida alisema kuna njama zinazofanyika za kudhoofisha maendeleo mkoani Lindi kwa kuwapeleka viongozi wala rushwa katika mkoa huo.

Alisema, uduni wa mkoa huo unasababisha wapinzani kuufanya kuwa kichaka cha wapinzani, kuwadhalilisha na kuwasema kwamba wao ni maskini.

“Viongozi wengi wa halmashauri wanaofanya ubadhirifu wa fedha kutoka mikoa mingine hutupwa Lindi,” alisema Lulida kabla ya kuanza kuwataja kwa majina wafanyakazi hao wa halmashauri:

“Joachim Materu ameiba 577 milioni, akapelekwa Lindi, Eunice Maro ameiba 262 milioni na akapelekwa Lindi, baada ya kufanya wizi huo, Maro aliziweka katika akaunti inayoshukiwa kuwa ni ya rafiki yake, yenye akaunti namba 206660017 NMB ambaye alihamishiwa Ofisi ya Kilimo Lindi,” alisema.

Aliwataja wengine kuwa ni Macha anayetuhumiwa kuiba Sh6 bilioni ambaye amehamishiwa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga na kwamba kuhamishwa kwao ni kusambaza ufisadi katika maeneo mengine.

Lulida aliongeza kuwa, kama Waziri Mkuu anataka aiunge mkono bajeti yake, basi aje na majibu sahihi kuhusu maendeleo mkoani Lindi pamoja na kurudisha programu ya kilimo ya Kanda ya Kusini, (SAGCOT)

Habari hii imeandaliwa na Neville Meena, Florence Majani na Habel Chidawali, Dodoma na Leone Bahati Dar

Tuesday, June 26, 2012

TGNP Wakemea Matusi, Kejeli, Lugha Chafu Bungeni

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP, tumekuwa tukifuatilia kwa karibu sana mjadala wa bajeti ya serikali ya mwaka wa Fedha 2012/2013 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tumestushwa na kusikitishwa jinsi ambavyo baadhi ya wabunge wanaonesha tabia ya kutumia nafasi na dhamana waliopewa na wananchi vibaya, kinyume na matarajio.

Bajeti ya mwaka 2012/2013 imekuja wakati ambapo wananchi walio wengi wanashuhudia hali ngumu ya maisha kutokana na mfumko wa bei, ukosefu wa ajira, ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake, wazee na watoto na kudorora kwa hduma zote muhimu kwa wananchi ikiwemo , maji, afya, nishati, elimu na huduma za kijamii hususani kwa walioko pembezoni. Kwa mantiki hii wananchi wanamategemeo makubwa kwa Bunge na wabunge katika mjadala huo.

Kinyume na matarajio hayo, tumesikitishwa na tabia ya baadhi ya wabunge kutumia Bunge kama sehemu ya malumbano ya kisiasa na kutambiana elimu, vyeti na sifa binafsi badala ya kujadili na kufanya maamuzi yenye manufaa kwa nchi yetu.

Tumesikia matumizi ya lugha chafu ndani ya Bunge zikitolewa na baadhi ya wabunge, dharau, jeuri, na kejeli badala ya kujadili bajeti kwa misingi ya mahitaji ya wananchi ambao wanateseka kwa ugumu wa maisha.

TGNP tunakemea na kukataa matumizi mabaya ya muda na nafasi adimu waliopewa wabunge kwa gharama kubwa za wananchi kutumika vibaya, kujadili maisha ya watu binafsi, kushambulia vyama vya siasa, kufanya utani badala ya kujadili jinsi ya kusaidia na kuboresha maisha ya Watanzania waliowengi.

Sisi kama wanaharakati na watetezi wa ukombozi wa wanawake, haki za bindamu, demokrasia, na usawa wa kijinsia tunawataka wabunge na ofisi ya Spika kufanya yafuatayo:

Kuheshimu kwa dhati muda na gharama za walipa kodi zinazowafanya wawepo Dodoma, mijadala ilenge kuleta tija, mageuzi ya kiuchumi na kubadilisha hali duni na umasikini wa Mtanzania ambaye amebaki kupata mlo mmoja kwa siku na wengine hawana kabisa.

Wabunge wajikite kuchambua, kujadili bajeti na kuishauri serikali namna ya kuboresha na kutekeleza ahadi , mipango yake ya kiuchumi hasa ule wa Miaka mitano (FYDP),MKUKUTA11, Mpango wa Maendeleo(Vision 2025), kwa kurejea Hali halisi ya uchumi wa wananchi kwa sasa iliyosomwa na Waziri wa Nchi (Uhusiano).

Wabunge kuacha mara moja lugha chafu za matusi, kejeli, dhararu, vurugu na kuchana nyaraka za mijadala Bungeni kwani hiyo ni kuwatusi wananchi walalahoi, ambao ni wapiga kura.

Spika asiruhusu ushabiki wa maoni ya mtu binafsi au kikundi bali hoja za bajeti ya serikali ambayo inawagusa wananchi wa Tanzania.

Kwa kushirikiana na wananchi tutaendelea kufuatilia na kudai uwajibikaji wa wabunge na viongozi wa serikali katika nagazi zote kwa maendeleo ya Taifa letu. .

Imetolewa na:

Usu Mallya
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP

Monday, June 25, 2012

Semina: Katiba na Mfumo wa Elimu Nchini


SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO

 UNAKARIBISHWA KATIKA MFULULIZO WA SEMINA ZA JINSIA NA MAENDELEO (GDSS) KILA JUMATANO, AMBAPO WIKI HII CHARLES KAYOKA  ATAWASILISHA

MADA: Katiba na Mfumo wa Elimu Nchini

Lini: Jumatano Tarehe 27/6/2012

Muda: Saa 09:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI:  Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na Chuo cha Taifa Cha Usafirishaji Mabibo Sokoni  


WOTE MNAKARIBISHWA

Mgomo wa madaktari wazorotesha huduma

HUDUMA za matibabu kwa wagonjwa jana ziliendelea kuzorota katika baadhi ya hospitali, hali iliyotajwa kuwa inatokana na mgomo uliotangazwa na madaktari.Madaktari walitangaza mgomo wa kutotoa matibabu nchi nzima kuanzia juzi, wakishinikiza Serikali kutekeleza madai yao likiwamo la kuboreshewa mishahara na mazingira ya kazi.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika Hosptali ya Taifa ya Muhimbili (MNH),Taasisi ya Mifupa (MOI) na hospitali nyingine za Jiji la Dar es Salaam, umebaini kuzorota kwa utoaji huduma.

Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, uchunguzi ulibaini mbali na ulinzi kuimarishwa, huduma za matibabu kwa wagonjwa zilizorota, na katika baadhi ya wodi wagonjwa walikuwa hawajatembelewa na madaktari tangu Ijumaa.

Mmoja wa watu ambao wanauguza mgonjwa wao katika wodi namba 4 katika Jengo la Mwaisela, Vicky Rehani alisema mgonjwa wao alipelekwa hospitalini Ijumaa na hadi jana, alikuwa hajapata huduma yoyote akiwa wodini.

"Mapokezi kweli alionana na daktari akamuandikia dawa na kulazwa katika wodi hii, lakini cha ajabu hadi sasa hakuna huduma yoyote ambayo ameipata," alisema .

Katika wodi zilizopo katika Jengo la Kibasila baadhi ya wagonjwa walidai kuwa, kuna madaktari ambao wamefika wodini, lakini hawakufanya mzunguko kama ilivyo kawaida, na hawakuwa na wasaidizi wao ambao ni wanafunzi wanaokuwa katika mafunzo kwa vitendo.

Daktari mmoja aliyekutwa katika wodi ya Sewahaji (alikataa kutaja jina lake), alipoulizwa kuhusiana na kuwapo kwa mgomo alikataa kusema lolote kwa madai kuwa si Msemaji wa MNH.

"Siwezi kusema lolote, kwani hata mimi mwenyewe nimefuata matibabu," alisema daktari huyo na kuongeza kuwa kama mwandishi anataka kujua kama kuna mgomo au la, basi aende hospitalini hapo kesho.
Hata hivyo, uchunguzi zaidi hospitalini hapo umebaini kupigwa marufuku kwa mikusanyiko ya aina yoyote na hata bustani inayotumiwa na wagonjwa na jamaa zao ambayo ipo mbele ya Jengo la Mwaisela, ilikuwa chini ya ulinzi.

"Hapa haruhusiwi mtu yeyote kukaa, amri hiyo imetoka tangu jana (juzi)," alisema mlinzi aliyekutwa eneo hilo na kuongeza kwamba hata mikusanyiko ambayo haieleweki imepigwa marufuku ndani ya eneo la hospitali.
Hali hiyo pia iliwakuta baadhi ya waandishi wa habari ambao walifika hospitalini hapo na kujikuta wakizuiwa na walinzi kuingia katika baadhi ya wodi.

Msemaji wa Hospitali hiyo, Aminieli Eligaesha wakati wote simu yake ilipokuwa ilikuwa inaita bila kupokelewa, hali ambayo ilijitokeza pia juzi Jumamosi.

Wakati hali ikiwa hivyo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na Moi, uchunguzi uliofanywa katika Hospitali za Mwananyamala, Amana na Temeke ulibaini kuwa huduma ziliendelea kwa kusuasua huku baadhi ya wahudumu wakisisitiza hatma ya mgomo huo itafahamika leo.

“Ukitaka kujua sura ya mgomo subiri kesho (leo) itadhihirika kama kweli madaktari wamegoma au la, lakini kwa leo huduma zinaendelea kwa kusuasua, bado tunaangalia Serikali itatoa majibu gani,” alisema mmoja wa madaktari katika Hospitali ya Amana, ambaye hakutaka jina lake kutajwa.
Aliongeza kuwa jana haikuwa siku ya kugoma, bali ni kushinikiza Serikali kutekeleza madai yao na kwamba, kama itaendelea na msimamo wake huduma zote zikiwamo za dharura zitasitishwa.

Hata hivyo, huduma katika Hospitali ya Amana jana zilikuwa zikiendelea huku baadhi ya wagonjwa wakisema kasi ya upatikanaji matibabu ni tofauti na kipindi ambacho mgomo ulikuwa haujatangazwa.
Katika Hospitali ya Mwananyamala, hali ya matibabu pia iliendelea kwa kusuasua na ulipotafutwa uongozi wa hospitali hiyo kuzungumuzia hali hiyo juhudi hizo hazikuzaa matanda.

Katika Ofisi ya Utawala, mwandishi alikutana na mmoja wa wafanyakazi ambaye alikataa kutaja jina na kueleza kuwa Mganga Mkuu alikuwa amekwenda kutembelea wagonjwa wodini.

“Mimi si msemaji. Hili anaweza kuzungumza Mganga Mkuu, lakini amekwenda kutembelea wagonjwa wodini na ameniambia akimaliza kazi hiyo anakwenda kufanya shughuli ya upasuaji, hatakuwa na muda wa kuzungumza nanyi,” alisema ofisa huyo.

Wakati hali ikiwa hivyo Mwananyamala, katika Hospitali ya Temeke pia huduma ziliendelea kutolewa huku baadhi ya watu waliokwenda kuhudumia wagonjwa wao wakibainisha kuwa kasi imepungua.
Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Edwin Chitage alisisitiza, “Sisi tunaendelea na mgomo kama kawaida, tutafanya hivyo hadi Serikali itakapotekeleza madai yetu, na hadi sasa hatujapata taarifa zozote kutoka serikalini,” alisema Chitage.

KCMC vuguvugu laendelea
 Katika Hospitali ya Rufaa KCMC Moshi, madaktari ambao hawako zamu wamekubaliana kufanya kikao cha dharura kuhakikisha hakuna daktari atakayeingia kazini leo.

Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya madaktari ambao hawakupenda majina yao yaandikwe gazetini, walisema wamepanga kufanya kikao cha pamoja ambacho kitaweka mikakati ya jinsi ya kufanya mgomo mkali leo, tofauti na ilivyokuwa juzi na jana.

“Mgomo uko palepale kama unavyoona walioko kazini ni wale wenye zamu, tumewataka wasaini, lakini kesho hakuna atakayeingia kazini na mgomo utakua mkali, tumekuwa wapole sana, lakini Serikali imetupuuzia,” alisema mmoja wa madaktari.

Chama cha Tiba Asilia
Kwa upande wa Chama cha Watabibu wa Dawa za Asili (ATME), kimewataka madaktari kuacha kugoma na badala yake waendeleze mazungumzo na Serikali ili waweze kufikia muafaka.

Chama hicho kupitia Mwenyekiti wake, Abudulhaman Simba, kimesema mgomo wa madaktari unahatarisha uchumi wa taifa na haki za wagonjwa, hasa wale wenye kipato cha chini.

Mkoa wa Mwanza
Mkoani Mwanza madaktari walio kwenye mafunzo na wale walioajiriwa waliendelea na mgomo wao jana.

Mmoja wa madaktari bingwa wa Hospitali ya Rufaa Bugando ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema mgomo huo kwa sasa haujaonyesha athari kubwa kutokana na kuwa siku za mapumziko.

"Leo (jana) na jana (juzi), hapajatokea athari za mgomo, tunadhani athari itakuwa kubwa katika siku za kesho (leo) na kuendelea kwani wakigoma hawa wa mafunzo na hao wengine, kazi inakuwa kubwa kwetu," alisema.

Katika hatua nyingine, mgomo huo haukugusa Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwani huduma ziliendelea kama kawaida.

Gazeti hili jana lilishuhudia wagonjwa wakipewa huduma za matibabu pamoja na mgomo uliotangazwa kudai maslahi yao.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Dk Omary Chande alisema pamoja na kutangazwa mgomo wa madaktari, Mount Meru haijaathirika na mgomo huo.

Wagonjwa waondolewa Mbeya
Katika Hospitali ya Rufaa Mbeya, mgomo uliendelea na kusababisha baadhi ya wagonjwa kuanza kuondolewa hospitani hapo pia na ile ya wazazi, Meta, kwa ajili ya kwenda kutafuta matibabu kwenye hospitali nyingine za watu binafsi.

Mwananchi jana lilishuhudia baadhi ya wagonjwa wakipandishwa kwenye magari na kuondoka kwenda kutafuta matibabu hospitali za watu binafsi.

Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Mbeya, Dk Eliuter Samky alipoulizwa alikiri kuwepo kwa mgomo wa madaktari walio kwenye mafunzo ya vitendo wanaofikia 70.
Hata hivyo, Dk Samky alisema anao uhakika kuwa madaktari 10 bingwa waliojariwa na Serikali wataendelea kufanya kazi, na hivyo huduma kwa wagonjwa hasa wale walio katika hali ngumu na wale wa dharura zitaendelea kupatikana.

Ombi la wagonjwa
Wagonjwa jijini Tanga,wameiomba Serikali kutekeleza kwa vitendo ahadi iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa madaktari ili kuondoa misunguano iliyojitokeza.

Ombi hilo walilitoa jana walipokuwa wakizungumza na Mwandishi wa habari hizi katika wodi za majeruhi na watoto katika Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo.

"Tunamuomba Rais atekeleze ahadi yake aliyotoa kwa madaktari, wanapogoma sisi walalahoi ndo tunaokufa na wengine kupata madhara zaidi, lakini wao wanapougua wanakwenda hospitali za nje ya nchi," alisema Adamu Abdurahman aliyelazwa katika wodi ya majeruhi ya
Galanosi.

Madaktari waliokuwa zamu katika wodi za Hospitali hiyo walisema hawaamini kama kweli Serikali haina fedha za kuwalipa, kwani kunapotokea masuala mengine imekuwa ikitoa bila ya matatizo.

Joseph Zablon na Geofrey Nyang’oro, Rehema Matowo, Nora Damian, Godfrey Kahango Mbeya, Filbert Rweyemamu, Arusha na Burhani Yakub,Tanga

Source: www.mwananchi.co.tz

Friday, June 22, 2012

Wakazi wa Kata ya Ijombe - Mbeya Vijijini watoa kilio chao kuhusu huduma duni za kijamii kutokana na uongozi mbovu


Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), ni shirika lisilo la kiserikali linalopigania usawa wa kijinsia, haki za binadamu na ukombozi wa wanawake kimapinduzi. TGNP kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inapambana na mifumo kandamizi ikiwemo mfumo wa kibepari, kibeberu, utandawazi na mfumo dume. Kuanzia mwaka 2008, TGNP imeelekeza nguvu zaidi katika ujenzi wa TAPO (vuguvugu) ngazi za kijamii, kama sehemu ya kutambua na kuchambua masuala ya vipaumbele kwa wanawake na wanaume walioko pembezoni.

Kuanzia tarehe 21 hadi 31 Mei 2012, kikundi cha waraghbishi kutoka TGNP wamefanya mchakato shirikishi wa uraghbishi katika vijiji vya Nsongwi Juu, Ifiga, Iwalanje, Nsongwi Mantanji na Ntangano Ijombe,Kata ya Ijombe, Wilaya ya Mbeya Vijijini mkoani Mbeya.

Wakazi wa Kata ya Ijombe wameelezea kero mbalimbali ikiwemo ya ukosefu wa masoko kwa mazao wanayolima, ambapo madalali hununua mazao kwa bei ndogo na kwenda kuuza kwa wafanyabiashara wakubwa bila wao kupata faida. Sambamba na hilo, ushuru pia ni kero kubwa.

Kuna ushuru wa aina mbili ukiwemo ushuru wa mazao shambani na ushuru wa mazao yakifika sokoni, ambao wanalipa bila stakabadhi kutolewa. Kwa ushuru wa shambani kila gunia ni shilingi 1000/- na ushuru wa mazao sokoni ni shilingi 200/- kwa mchuuzi. Wakati huo huo, wakazi wa Ijombe wamedai katika Kata yao hakuna utawala bora kwani baadhi ya viongozi hawaweki wazi taarifa za mapato na matumizi na huu ni uvunjaji wa sheria. 

Vilevile, wanawake wamedai kuwa wanakabialiana na ukatili wa kijinsia toka kwa wanaume ikiwa ni pamoja na kuuza mazao kinyemela, kutokuhudumia familia, kutolipa ada za shule kwa watoto, wanawake kupigwa kutokana na ulevi uliopindukia wa waume zao.

Huu umekuwa ni mzigo mkubwa kwa wanawake wa Ijombe na wameuomba uongozi husika hasa katika ngazi za vitongoji, vijiji na Kata waweze kufuatia kero hizi na kuweka sheria zitakazowabana wanaume kutokana na vitendo vyao. Pia wakazi wa Ijombe wameomba uongozi kufuatilia na kudhibiti muda wa kuuza pombe. Wanapendekeza vilabu vifunguliwe kwa muda maalum uliopangwa. Kisheria vilabu vinapaswa kufunguliwa saa kumi jioni na kufungwa saa tatu usiku, na sio kufunguliwa saa moja asubuhi kama ilivyo kwa sasa.

Kero nyingine waliyotoa ni mimba za utotoni kutokana na ukosefu wa mabweni kwa wasichana wanaosoma katika Shule ya Sekondari ya Kata ya Iwalanje.
Shule ya Iwalanje imekuwa mbali sana na makazi ya walio wengi. Wanafunzi wanatembea umbali wa kati ya kilometa 4 hadi 8 kutoka vijiji vinavyotumia shule hiyo. 

Tatizo hili la umbali limepelekea baadhi ya wanafunzi kupanga vyumba vinavyojulikana kwa jina maalum la ‘GHETO’.
Wakazi wa Kata hiyo wamedai kuwa kutokana na kuishi kwenye magheto kwa muda mrefu kumepelekea wasichana wengi kutokufanya vizuri katika masomo yao.

Wasichana walio wengi, wamegeuka kuwa wapishi na wanasaka maji, kuni kwa ajili ya kujipikia chakula.
Kwa maana hiyo wasichana wamekuwa wakitumia muda wao mwingi zaidi kufanya kazi zilizo nje ya masomo tofauti na watoto wa kiume ambao muda mwingi wamekuwa wakijisomea.
Zaidi ya hayo wakazi wa Ijombe wamekiri kuwa wasichana wengi wamepata mimba za utotoni kwa kukosa ulinzi kwani baadhi ya magheto wanaishi watoto wa kike na wakiume.

Pia kuna hatari kubwa ya kuongezeka kwa maambukiza ya magonjwa hatarishi kama vile Ukimwi.
Vilevile, wakazi wa Kata ya Ijombe wamedai kuwa michango ya shule imekithiri. Kwa mfano michango inayotolewa ni shilingi 10,000/- kwa kila kichwa kwenye kaya. Kwa wale ambao wanaoshindwa kutoa mchango huo, kwa ajili ya maisha kuwa magumu hukamatwa na kupelekwa mahakamani; na ili waachiliwe huru wakazi hao hutakiwa kutoa shilingi 67,000/=.

Pia wakazi wa Ijombe hutoa shilingi elfu ishirikini (20,000/=) kwa mwaka kwa wanafunzi wanaoishi nyumbani na kwenye magheto. Michango yote kwa mwaka kwa mtoto anayeanza sekondari ni zaidi ya shilingi laki tatu na elfu hamsini (350,000/-), zikijumuisha fedha za madawati, vitambulisho, bima za afya, tahadhari, sare za shule,madaftari na rimu za karatasi. Michango hii inakuwa ni kikwazo kwa wazazi ambao kipato chao ni kidogo.

Kwa wanafunzi wanaoishi mashuleni wanalipa laki nne na nusu (450,000/-) tu kwa mwaka.
Vilevile, Kata ya Ijombe hasa kijiji cha Iwalanje kuna tatizo la maji kwa muda mrefu . Wakazi wa Iwalanje wamedai kuwa kijiji chao kimekuwa kikitoa mchango kwa ajili ya kupata maji kwa takribani miaka kumi na nne iliyopita bila mafanikio.

Wanawake ndio waathirika wakubwa wa tatizo hili. Wanawake wa eneo hili wamesema wamekuwa wakiamka saa kumi alfajiri kwenda kusaka maji na kurudi saa tatu asubuhi, wakati huo huo wanawake wanapata kipigo toka kwa waume zao kutokana na kuchelewa kurudi.
Wanawake wa Ijombe wameiomba serikali kufuatilia kwa karibu tatizo hili kwani linawakosesha mapato kutokana na kutoweza kushiriki katika kazi za uzalishaji.

Mwisho wakazi wa Ijombe wamekiri kuwa kero zote zilizokithiri katika Kata yao, zinatokana na uongozi mbovu, hasa viongozi kutokufuatilia kwa karibu masuala yanayowagusa wananchi wao na kuwepo kwa ubinafsi zaidi, kuchanganya masuala ya kisiasa na masuala ya kimaendeleo.

Pia viongozi wametakiwa kujua wajibu wao kila mmoja katika nafasi yake Wakazi hao wameomba viongozi wawe na mawasiliano na wananchi kwa kujadili kero zinazowakabili na kutafuta ufumbuzi wa matatizo yao kwa pamoja.

Imetolewa na Waraghbishi, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)

Walemavu wataka uwakilishi Tume ya Katiba mpya

JAMII ya Walemavu wasiosikia (viziwi) wameiomba Serikali kuweka wawakilishi wao katika Tume ya mchakato wa Katiba mpya ili waweze kuingiza maoni yao kwa kina mara watakapoanza kukusanya maoni juu ya upatikanaji wa Katiba mpya itakayo kuwa na tija kwao pamoja na walemavu wengine.

Wito huo ulitolewa na mmoja wa walemavu hao John Ogonya alipokuwa akichangia mjadala katika mdahalo ulioandaliwa na asasi isiyo ya kiserikali ya Mra Development Forum kuhusu utawala bora na uwajibikaji katika mchakato wa kupata katiba mpya uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Anglican mjini hapa.
Alisema Walemavu viziwi wamekuwa wamekuwa wakitengwa katika masuala mbalimbali ya kijamii na kupelekea kukosa ufahamu wa mambo kutokana na ulemavu wa kutokusikia waliokuwa nao.

John alidai kuwa katiba mpya inapaswa kuwa mkombozi wao kwa kuingizwa vipengere vitakavyoweza kuwasaidia kupata wataalamu wa lugha za alama katika huduma mbalimbali za jamii ikiwa ni pamoja na katika hudumaa afya,mahakama na katika ofisi mbalimbali za umma na vyombo vya habari.

Ameeleza ushilikishwaji kwa walemavu wasio sikia umekuwa mdogo na hata wanapoelekea katika mchakato wa kupata katiba mpya hata ile iliyopo mpaka sasa hawaifahamu na hivyo kukosa cha kutolea maoni bali wameomba kuwepo na uwakilishi katika Tume ya Katiba ili aweze kuingiza maoni yao.

Hata hivyo Walemavu walioshiriki katika mdahalo huo wameishukuru asasi ya Mara Development Forum kwa kuandaa mdahalo huo na kuwawekea wataalamu wa lugha za alama na kupelekea kuelewa kwa kina kile kilichokuwa kikizungumzwa na kuchangiwa kuhusu utawala bora na uwajibikaji katika mchakato wa kupata katiba mpya.

Akichangia katika mdahalo huo Mratibu wa Mara Development Forum George Chibasa alisema lengo la kuandaa Mdahalo huo ambao umekuwa ukifanyika kila Wilaya katika Mkoa wa Mara ni kuwajengea uwezo Wananchi ili kuwa na umakini mkubwa wa kutoa maoni yao katika mchakato wa kupata katiba mpya mara Tume ya kukusanya maoni itakapoanza kukusanya maoni.

Mratibu huyo ameishukuru Taasisi isiyo ya kiserikali ya The Foundation For Civil Society ya Dar es salaam kwa kuendelea kuwapa ufadhiri ambao unawasaidia kuwafikia Wananchi na kutoa elimu mbalimbali juu ya umuhimu wa kutoa maoni yao katika kuelekea upatikanaji wa Katiba mpya.

Hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete alitangaza majina ya wajumbe wa Tume ya kukusanya maoni juu ya upatikanaji wa Katiba mpya itakayokuwa chini ya Waziri Mkuu Mstaafu Joseph Sinde Warioba ambayo bado haijaanza kazi ya kukusanya maoni

Thursday, June 21, 2012

Mfumo dume wawatafuna wanawake Mbeya


Na Esther Macha, Mbeya

KUSHAMIRI kwa mfumo dume katika wilaya ya Mbeya kunaathiri kwa kiasi kikubwa hali ya kiuchumi kwa wanawake ambao ndio nguvu kazi kubwa katika kilimo, kipato wanmachopata baada ya mavuno huishia mikononi mwa wanaume wanaojihusiusha na vitendo vya starehe na kusahau malezi ya familia zao.

Uchunguzi uliofanywa na Majira kwa takribani wiki moja  kwa msaada wa mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP)umegundua kuwepo kwa vitendo vya unyanyasaji na ukatili wanavyofanyiwa wanawake wa vijiji vya Ifiga,Iwalanje na Nsongwi juu  Kata ya Ijombe vinavyotokana na nguvu ya wanaume ya kuhodhi mali zilizopatikana kwa kuwashirikisha wanawake.

Mmoja wa awanawake wa Kijiji cha Ifiga Bi Salah Jailos alisema kuwa wakati wa  msimu wa kilimo unapowadia  hushirikiana na waume zao kwa karibu bila kuwepo ugomvi wowote ndani ya familia zao mpaka  mazao yanapokomaa.

Alisema kuwa inapofika kipindi cha kuvuna wanaume  huanza kubadilika kwa kutafuta sababu mbali mbali  za kuonyesha chuki ndani ya nyumba ili aweze kupata sababu za kuvuna peke yake mazao na kuuza pepe yake bila kumshirikisha mke wake.

“Hali hii inatusikitisha sana kwani akishauza mazao haya huondoka nyumbani na kwenda kufanya starehe zake na wanawake wengine , lakini fedha baada ya kuisha hurudi nyumbani na kuanza kutafuta visababu vidogo vidogo kwa kuanza kudai chakula na kutoa sababu mbali mbali ikiwa  ni pamoja  na kudai kuwa chakula kibichi mara hufai kuishi na mimi mara nataka kuoa mke mwingine maadamu tu apate sababu za kujitetea ili mwanamke nionekane mbaya”alisema mwanamke huyo.

Mwanamke mwingine mkazi wa Usongwe Juu Bi.Benadeta Hamisi alisema kufutia vitendo hivyo vya wanaume tunaomba waache kwani iweje wakati wa kilimo  tulime wote lakini inapofika wakati wa mavuno wawe wababe wa kuuza mazao9 peke yao kwa ujumla huu ni ukatili wa kijinsia kwa sisi wanawake wa Kata ya Ijombe.

“Tunaomba waume zetu waache tabia hii kwani mazao haya tunalima sote hivyo hata wakati wa kuvuna inatakiwa tuwe pamoja na hata kuuza vile vile inatakiwa kusimama kwa pamoja kama mke na mume ioli fedha hizo zitakapopatikana mazao  na kuuza yaweze kusaidia kulea familia zetu pamoja na kusomesha”alisema Bi. Hamis.

Hata hivyo mwanamke huyo alisema athari ambazo wanapata baada ya kuachiwa familia ni kupata shida ya  kuhudumia familia ikiwa ni pamoja na kusomesha watoto namahitaji mengine ya nyumbani ambayo ni muhimu.

Akizungumzia malalamiko hayo kwa Wanawake wa vijiji hivyo, Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Ifiga Bw.Raphael  Siyejele alisema hana taarifa za kiofisi za wanaume kuwanyanyasa wake zao labda kama zipo ngazi zingine.