Thursday, August 28, 2008

MREJESHO WA UZINDUZI WA KITABU CHA HALI HALISI YA KIJINSIA TANZANIA

Uzinduzi wa kitabu cha Hali Halisi ya Kijinsia Tanzania na Tathimini ya Madai ya Miaka Kumi ya Beijing, huu ni uchambuzi mbadala wa hali ya mahusiano ya Kijinsia Tanzania na mabadaliko muhimu yanayotakiwa katika kufanikisha ukombozi wa wanawake
na usawa wa kijinsia. Kitabu hiki kilizinduliwa rasmi na Mwenyekiti wa FemAct dada Jesca Mkuchu katika viwanja vya TGNP.

Wanaharakati walikuwa na madai matano ambayo yalitokana na utafiti uliozaa kitabu hiki na wanahitaji madai hayo yafanyiwe kazi mapema sambamba na ahadi za serikali.
Madai haya yaliwakilishwa na Mwenyekiti wa Tamwa dada Ananilea Nkya, ambayo ni:

1. Elimu – Wanaharakati wanadai usawa wa 50% kwa 50% kati ya watoto wa kike na kiume katika kupata elimu, Walimu bora, na vitabu kwa wanafunzi wote. Pia wanataka
serikali kukomesha mimba za utotoni ambazo zinakwamisha watoto wa kike kuendele na masomo.
2. Afya – Katika afya wanaharakati wanaitaka serikali itekeleze haraka azimio la Abuja ambalo serikali yetu ililisaini pamoja na nchi zingine za Afrika azimio hilo linazitaka nchi za Afrika kutenga kiasi cha 15% ya bajeti ya nchi zao katika maswala ya afya. Ongezeko hilo litasaidia kupunguza vifo vya akina mama vinavyotokana na matatizo ya uzazi.
3. Kazi – Wanaharakati wanadai serikali itekeleze mapendekezo ya mkataba namba 100 wa Shirika la kazi la Mataifa (ILO) linalotaka kuwepo kwa usawa katika ajira kati ya wanaweke na wanaume. Pia wanaharakati wanadai kukomeshwa kwa hali yoyote ya kibaguzi wa kijinsia katika kupandisha vyeo kwa wafanyakazi katika sekta zote binafsi na umma.
4. Kisiasa- Wanaharakati wanadai serikali itekeleze azimio la SADC linalotaka serikali za nchi wanachama kutoa nafasi sawa katika ngazi zote za uongozi kwa wanawake na wanaume kwa asilimia 50% kwa 50%. Pia sambamba na hilo wanataka wanawake watakaopata uongozi waweze kutetea maslahi ya wanawake wenzao.
5. Haki za ujumla kati ya wanawake na wanaume. Katika kipengele hiki wanaharakati wanitaka serikali iondoe sheria ya ndoa ya mwaka 1977 ambayo inanyima mtoto wa kike haki ya kulitumikia taifa hili kwa kuhalalisha ndoa za kuanzia miaka 14.

Dada Mary Rusimbi alifanya hitimisho la nini kifanyike ili kuweza kuleta usawa wa
kijinsia Tanzania, na aligusia swala zima la mgawanyo wa rasilimali Tanzania.
Rasilimali hapa alimaanisha bajeti, Fedha za wafadhili, watu, maliasili n.k. Kwa maoni yake anaona Mgawanyo wa rasilimali haulengi makundi yaliyowekwa pembezoni –vijana, wanawake, na wanaume masikini- badala yake unaendelea kuwanufaisha watu wachache katika jamii kama kipindi cha ukoloni. Pili, Serikali haina mkakati maalumu ?
wa kuwasaidia maskini na wanyonge, na kuwapunguzia kazi wanawake. Tatu, Mikopo midogomidogo-Microfinance- inayotolewa na taasisi za kifedha hazilengi kumkomboa maskini hasa mwanamke bali zinaendeleza unyonyaji kwa jamii. Changamoto ni, tumejizatiti kiasi gani kama taifa katika kuleta mgawanyo unaolingana wa rasilimali za taifa kwa jamii yetu? Uko wapi mkakati wa mgawanyo sawa na wa haki wa rasilimali ya taifa, hasa wenye mrengo wa kuwakomboa wanyonge hasa wanawake?

Thursday, August 7, 2008

Mrejesho wa Mada juu ya Kipindi cha Television cha Longa Mwanaume.

Kipindi cha Longa Mwanaume kinarushwa kila siku ya jumatano na kituo cha ITV, kipindi hiki kinazungumzia mambo mbalimbali ya mahusiano ya wanaume na wanawake -hasa katika ya ndoa. Tangu kiliapoanzishwa -wiki kama tano hivi- kipindi hiki kimekuwa kikijadili mada ambazo zina mlengo wa kuwakandamiza wanawake katika maisha yao ya ndoa, na kujaribu kupaza sauti za wanaume katika jamii au kuonyesha mambo ambayo labda wanaume wanahisi wamepokonywa au wanayoyatakiwa wayashikilie. Hali hii imepelekea wanaharakati kukijadili kipindi hiki katika zama hizi za harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi. Mkanganyiko huo wa maudhui ya kipindi hiki umeibua maswali kadhaa wa kadha ambayo wanaharakati wanaona ni vyema yakajibiwa. Je kipindi hiki ni fursa ama si fursa? Kinaendeshwaje? Au je Kirekebishweje ili kiweze kwenda sawa na harakati hizi za ukombozi wa wanawake kimapinduzi? Maswali hayo na mengine yaliweza kujenga msingi mzima wa mada hii.

Mwezeshaji wa mada hii alikuwa Salma Maulid kutoka Sahiba Sisters Foundation, na alikuwa na maswali makuu manne ya kujadili juu ya kipindi hiki, ambayo ni:

Ni nini madhumuni ya kipindi hiki kulingana na harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi? Wanasemina waliweza kuajdiliana juu ya swali hili na kuafikiana kwamba, kipindi hiki kina lengo la kirudisha nyuma harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi katika kuleta usawa wa kijinsia katika jamii. Kwa kujadili maswala ya uhusiano wa wanaume na wanawake katika jamii huku wakitoa hoja za kuwakandamiza wanawake na kuacha maswala ya msingi yanayoikabili jamii yetu hasa katika kuleta usawa wa kijinsia ni wazi waongozaji wa kipindi hiki wana lengo la kurudisha nyuma harakati zinazoendelea za ukombozi wa wanawake.

Kwa nini kipindi hiki kimekuja sasa wakati vuguvugu la harakati za wanawake kimpinduzi limepamba moto? Hapa majibu mawili yalipatikana, la kwanza; labda meseji ya harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi zimewafikia wale wasiopenda mabadiliko hivyo wakatafuta mbinu ya kujihami mapema kabla mabadiliko kamili hayajatokea. La pili; labda kipindi hiki ni mojawapo ya njia za wasiopenda mabadiliko kukwepa hoja pana ya upiganaji dhidi ya mfumo dume kwa kuibua matatizo madogo-madogo yanayowahusu wanawake hasa katika mahusiano ya kindoa, ili kupotosha dhana nzima ya mapamabano dhidi ya mfumo dume.

Je ipo mijadala mengine inayoendelea huku pembeni inayofanana na hii? Mijadala mingine inayofanana na hii bado ipo katika jamii yetu, washiriki wa semina walitoa mfano wa kipindi kimoja cha redio ambacho kilikuwa kinajadili juu ya watoto wanaopata mimba wakati wakiwa shuleni na hitimisho la kipindi hiko lilikuwa wanafunzi hao wafukuzwe shule moja kwa moja. Pia matangazo ya biashara ya shirika moja la Simu za mkononi na Benki fulani hapa nchini ambayo yote yalihusisha utoaji wa mahali kubwa kwa wasichana waliotaka kuolewa, hii inaendelea kuonyesha wasichana bado wanaonekana kuwa ni vitu ambavyo vinaweza kununuliwa kwa kiasi fulani cha fedha. Matangazo na mijadala kama hii inachangia kurudisha nyuma harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi zinazoendeshwa na wanaharakati wapenda mabadiliko kote duniani.

Je Longa mwanaume Kinazungumzia Maswala ya wanaume? Kipindi hiki cha longa mwanaume hakizungumzii maswala ya msingi yanayowakabili wanaume na wanawake wa Wakitanzania wa leo, badala yake kimekuwa kikijadili vitu ambavyo si muhimu na kuacha maswala muhimu yanayohusu jamii yetu. Kwa mfano, kinashindwa kujadili maswala ya ajira, makazi bora, huduma za afya, kuondoa tofauti za kijinsia na kuleta usawa katika jamii, na vita dhidi ya rushwa. Hivyo kipindi hiki kimekazania kujadili mambo ya mzaha na yasiyokuwa na faida katika jamii yetu hasa kwa mustakabali wa kizazi kijacho.

Kwa kuhitimisha, Wanasemina walipendekza kipindi hiki cha Longa Mwanamume kifanyiwe marekebisho ili kiweze kutoa fursa kwa jamii inayolenga kuleta mabadiliko ya usawa wa kijinsia na ukombozi wa wanawake kimapinduzi. Mada na uongozaji wa kipindi hiki urekebishwe ili uweze kutoa fursa kwa ujenzi wa jamii mpya yenye usawa wa kijinsia na yenye kumthamini mwanamke.

Friday, August 1, 2008

Mrejesho wa Mada Juu ya Ushirikiano Kati ya Jeshi la Polisi na Jamii Katika Mapambano Dhidi ya Ukatili Wa Kijinsia.

Mada hii iliwakilishwa na Kamishina wa Polisi, Bi. E.A Mapunda Mkuu wa chuo cha polisi Kurasini tarehe 30/06/2008 na kuibua hoja motomoto kutoka kwa washiriki wa semina. Jeshi la polisi lipo katika mabadiliko makubwa ya kuboreshwa huduma zake kwa jamii kwa lengo la kupambana na uhalifu pamoja na ukatili wa kijinsia. Mabadiliko hayo yalianza mwaka julai 2006, na yana mihimili mikuu mitatu ambayo ni Polisi jamii, weledi (Professionalism-kuzingatia maadili, taaluma na viwango vilivyowekwa), na usasa (modenization-kuboresha rasilimali watu, vitendea kazi, ofisi, makazi, na maslahi ya askari). Misingi mengine ni pamoja na maboresho ya sekta ya sheria, sekta ya fedha, na maboresho yanayoendana na serikali ya mtaa.

Polisi jamii inalenga kujenga mazingira endelevu ya kuliwezesha jeshi la polisi kufanya kazi pamoja na jamii hasa kudumisha amani. Falsafa hii imejijenga katika nguzo kuu nne ambazo ni; kuwepo kwa mashaurino kati ya polisi na jamii, kutatua matatizo au kero, kuwepo marekebisho au mabadiliko, na kuwepo na uhamisishaji.

Katika kuenenda na mabadiliko haya, tarehe 25/10/2007 jeshi la polisi liliunda Mtandao Wa Polisi Wanawake (Tanzania Police Female Network) kwa lengo la kupamna na uhalifu wa makosa yanayohusiana na ukatili wa kijinsia. Uongozi wa Mtandao huu upo katika ngazi zote kuanzia taifa hadi wilayani katika mikoa yote bara na visiwani.

Dira, Dhima na Madhumuni ya Mtandao wa Polisi.
Dira: kuwa chombo cha utendaji cha kitaalam katika kutoa huduma bora na kuongeza ufanisi katika kazi za polisi.

Dhima: kujenga na kudumisha mshikamano miongoni mwa polisi wanawake, askari wengine na jamii ili kudumisha mahusiano na kuwa karibu na wananchi na hatimaye kuboresha utoaji wa huduma.

Madhumuni: Kuondoa hofu ndani ya jamii dhidi ya jeshi la polisi, kuliweka jeshi la polisi karibu na jamii hasa wanawake ili kuweza kupata taarifa zaidi za uhalifu na wahalifu, kushirikiana na wananchi kwa karibu katika kuyatambua na kuyatatua matishio ya uhalifu yanayowakabili katika maeneo wanayoishi, kubadilishana mawazo na wananchi ni jinsi gani wanaweza kulisaidia jeshi la polisi katika kuwatambua na kudhibiti uhalifu, kusimamia na kukemea suala zima la unyanyasaji wa wanafunzi katika daladala, na kuelimisha jamii juu ya baadhi ya vitendo vinavyoashiria makosa ya jinai ikiwemo ukatili wa kijinsia.

Mtandao umefanikiwa kutoa mafunzo ya ukatili wa kijinsia kwa maofisa, wakaguzi na askari 180 kutoka vituo 18 vya kanda ya Dar es salaam na katika vyuo vyote vya polisi na mafunzo haya yatakuwa ni endelevu. Kuendelea kutoa mafunzo katika shule za msingi mkoa wa Dar es salaam kata ya Kurasini katika somo linaloitwa Usalama Wetu, na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya kazi za mtandao.

Mtandao unakabiliwa na Changamato/Matatizo zifuatazo; raia wengi wanashindwa kugundua ukatili wanaofanyiwa kama una asili ya kijinsia, mila na desturi za badhi ya makabila zinachangia ukatili wa kijinsia, na mtazamo wa jamii kwa polisi bado hauridhishi.

Matarajio ya mtandao huu ni pamoja na; kuwa na dawati katika vituo vya polisi la kusikiliza matatizo ya ukatili wa kijinsia katika mikoa yote ya Tanzania, kuendelea kupata mafunzo zaidi ili kuboresha azima ya jeshi la polisi, na kuendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa dawati hili na kuwa tayari kutoa ushirkiano pale wanapopata matatizo.

Wana-GDSS walipendekeza Dawati hili lipelekwe katika vyombo vya habari ili wananchi wengi zaidi waweze kufahamu, zifanyike juhudi ya kuongeza idadi ya askari wanawake, urasimu katika vituo vya polisi ukomeshwe, wananchi wafikishe taarifa za ukatili wa kijinsia na uhalifu mwingine katika vituo vya polisi na vyombo husika, na jeshi la polisi liwe na mkakati maalumu wa kutetea rasilimali za wananchi wa Tanzania dhidi ya mabepari/wawekezaji.

Kwa kuhitimisha, jeshi la polisi lina safari ndefu ya kuelimisha jamii ili liweze kupata ushirikiano zaidi kutokana na dhana zilizojikita miongoni mwa raia wengi kwa sababu ya manyanyaso wanayoyapata kutoka kwa askri wa jeshi hilo. Uboreshwaji huu unaweza ukafungua ukurasa mpya katika kuelekea jamii bora ya Kitanzania bila uhalifu. Tanzania bila uhalifu inawezekana!