Thursday, June 26, 2008

Mfululizo wa Semina za Jinsia na Maendeleo.

Jumatano wiki hii ya tarehe 25/06/2008 katika mfululizo wa semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS) mada ilikuwa ni Juu ya Sherehe za Kitchen Party iliyowakilishwa na dada Agnes Mutayoba - Mratibu wa elimu wa Kata ya Mzizima na kuwezeshwa na dada Anna Kikwa. Lengo la Mada lilikuwa ni kujadili muundo wa sherehe za kitchen party zinazoendeshwa katika siku za hivi karibuni. Mtoa mada aliamua kutoa mada hii kutokana na utafiti alioufanya katika sherehe mbalimbali zilizofanyika katika jiji hili la Dar es salaam hivi karibuni.

Mtoa mada aliweza kuwachokoza washiriki wa semina kwa kuwauliza maana ya Kitchen Party ambao wengi walikubaliana kwamba ni mafunzo anayopewa Msichana/mwali kabla ya kuolewa ama pindi anapokuwa karibu ya kuolewa. Na karibia kila kabila lilikuwa na jina lake maalumu la mafunzo hayo. Kwa mfano, Wazaramo waliyaita Mkole. Pia mshirki kutoka USA alichangia na kusema kwao Kitchen party huwa ni sherehe ya kutoa zawadi kwa msichana anayekaribia kuolewa, na mara nyingi huandaliwa na wanawake wenye umri mkubwa kwa ajili ya binti yao.
Hivyo kitchen party tangu awali ilikuwa ni sherehe kwa ajili ya maandalizi ya Msichana anayekaribia kuolewa. Mtoa mada akatoa maswali saba ya uchokozi ya kutafakari kwa washiriki wa semina juu ya muundo wa sherehe za kitchen party za siku hizi. Washiriki walitakiwa kukaa katika makundi na kujadili maswali hayo saba, na mijadala iliyoibuka ni pamoja;
1. Je, Kitchen party ni sherehe inayoendana na mila na desturi za kabila husika?
Hapana, kwa sababu sherehe za siku hizi za kitchen party zipo kibiashara sana na hata wahusika hutumia lugha zisizostahili ili kuvutia biashara. Pia walimu wanaofundisha ni watu kutoka makabila mengine, hivyo haijali utamaduni na mila za kabila husika.

2. Sherehe za Kitchen Party zina mabadiliko yoyote?
Mabadiliko yapo wafundishaji hawana sifa, zipo kibiashara sana, mambo ya kufundishia ndani yanafanywa hadharani, na mafunzo yanafanyika kwa muda mfupi sana. Hivyo mafunzo haya yamepoteza dira.
3. Je umri Msichana anyepata mafunzo ya Kitchen party unalingana na elimu anayopewa?
Wasichana wanaweza kufika umri wa kutosha kufundishwa mafunzo hayo ama la, kwa sababu wapo wasichana wanaoozwa chini ya miaka 18, nao pia hupatiwa mafunzo hayo.

4. Kuna elimu nyingine ya ziada anayopewa msichana zaidi ya ile ya Kitchen party?
Ipo, wasichana wanapatiwa elimu mbalimbali za jinsi ya kwenda kuishi na waume zao, ukilingnisha na wanaume ambao ni mara chache sana kupatiwa elimu ya aina hiyo, kitu ambacho kinasababisha matatizo makubwa katika mahusiano yao.
5. Je kitchen party ni kitu cha kuiga au ni asilia?
Kitchen party ni kitu cha kuiga kutoka magharibi, ukilinganisha na sherehe za mafunzo ya zamani ya asili yalivyokuwa. Kuna mambo yameongezeka katika sherehe za siku hizi ikiwa pamoja na matumizi ya zisisokuwa na maadili, na umri wa washiriki katika sherehe hizo.
6. Iwapo msichana anapatiwa elimu ya kitchen party, mvulana anapatiwa elimu gani?
Mvulana hana elimu yoyote ya kuishi katika ndoa kutona na mabadailiko ya utandawazi, hivyo hupelekea kukosa maadili ndani ya ndoa yake. Zamani wavulana walipitia jando kabla ya kuoa na ilisaidia sana kuimarisha mahusiano ya ndoa.
7. Nini kifanyike badala ya Kitchen party?
Kitchen party inaweza ikawa na faida iwapo mambo kadhaa ya kisasa yakirekebishwa tofauti na hali iliyopo, ambapo imepoteza maana yake halisi.

Hitimisho.
Sherehe za kitchen party zinawadidimiza wanawake kwa sababu zinawachukulia muda mwingi katika maandalizi yake na kiasi kikubwa cha fedha. Pia inawadhalilisha wanawake kwa sababu mafunzo yanayotolewa hayazingatii maadili ya Mtanzania hasa katika uvaaji na mada zenyewe. Hivyo kuna haja ya kuangalia upya sherehe hizi ili ziweze kuleta manufaa katika zama hizi za utandawazi.

Picha za Wa-GDSS katika semina hiyo.


Mtoa Mada Bi. Agnes Mutayoba.


Sehemu ya Washiriki.

Washiriki wakiwa katika vikundi wakijadiliana.
Washiriki wakijadiliana.
Mshiriki akichangia mada.

Mshiriki akichangia mada.
Mshriki akichangia mada.

Tuesday, June 24, 2008

FEMACT YAUNGA MKONO WABUNGE KUPAMBANA NA UFISADI

Sisi Mtandao wa wanaharakati wanaotetea usawa wa jinsia, haki za binadamu, ukombozi wa wanawake na maendeleo (FemAct) tunaungana na wabunge wote ambao wameamua kusimama kidete kupambana na ufisadi hapa nchini ili rasilimali za taifa ziweze kunufaisha wananchi wanaoteseka na umaskini mijini na vijijini.

Tunaona hatua ya wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi , kuamua kutumia sauti na fursa zao kupigania maslahi ya wananchi walio wengi ni muhimu kuungwa mkono na kila mtu anayeitakia nchi yetu amani na maendeleo endelevu bila kujali ni mwana siasa au la.

Kitendo cha wabunge kutaka serikali ihakikishe kuwa watu walioiba fedha kutoka Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT) wazirudishe na kuchukuliwa hatua na kisha Umma ufahamishwe ni kina nani hao waliohusika na uovu huo, kinapaswa kupongezwa kama hatua sahihi katika kuleta mapinduzi ya kweli ya kukomesha ufisadi dhidi ya mali na rasilimali za taifa.

Wabunge hao pia wanastahili pongezi kwa kuibana serikali kuhakikisha kwamba shilingi bilioni 216 ambazo na watu wachache walikopa toka Benki Kuu takribani miaka 16 iliyopita ziwe zimerundishwa na wabunge kupewa vithibitisho halisi vya kuonesha kuwa fedha hizo zimerudi serikalini . Kwetu rasilimali hizi ni muhimu sana katika kutekeleza miradi ya wananchi inayolenga kuondoa tofauti za kimkoa,mijini na vijijini na hususan kuboresha huduma za kupunguza vifo vya wanawake katika uzazi, kudhibiti vitendo vya ukatili wa kijinsia, huduma za maji na nishati ili kupunguza mzigo wa kazi za kulea na kuendeleza familia unaofanywa hususan na wanawake na watoto

Kadhalika wabunge wanastahili kuungwa mkono pale wanapoidai serikali isimamie uwajibikaji wa wale wote waliohusika na kashfa kwenye mkataba wa uzalishaji wa umeme wa dharura ambao ulitolewa kwa kampuni hewa ya Richmond.

Hadi sasa serikali inaendelea kulipa mabilioni mengi ya fedha za Watanzania kuhusiana na mkataba huo mchafu wakati maelefu ya wananchi wanaendelea kuteseka kutokana na ugumu wa maisha.

Sisi FemAct tunafarijika sana wabunge wanapofanya kazi zao kwa kuweka mbele maslahi ya Taifa na wananchi walio wengi badala ya tabia iliyozoeleka hapo awali ya kuweka mbele maslahi ya watu binafsi au vyama vya siasa.

Hakika sisi tunaona wakati umefika kwa kila mbunge, kila kiongozi na kila mwananchi kuwa jasiri kutetea haki na maslahi ya umma na nchi yetu kwa ujumla hata kama kwa kufanya hivyo kutaudhi wale ambao kwa ujasiri huo watakuwa wamehatarisha maslahi yao binafsi au vyama vyao vya siasa. Wabunge kuonesha ujasiri katika kutaka hatua sahihi zichukuliwe dhidi ya ufisadi na mafisadi ni muhimu kwa sababu mwisho wa siku kilicho muhimu kuliko vyote ni umma wa Watanzania na taifa letu na si maslahi ya mtu mmoja mmoja au chama cha siasa.

Ndiyo sababu sisi FemAct tumeona tuweke wazi msimamo wetu kuwa tunaunga mkono kwa dhati hatua ya baadhi ya wabunge kujitoa mhanga kwa ajili ya kudai haki za wapiga kura wao kitendo ambacho tunaona kinaashiria dhamira ya wabunge hao ya kupambana na rushwa na vitendo vyote vya ufisadi ambavyo ni chanzo cha umaskini na ufukara wa watanzania walio wengi.

FemAct tunatarajia kuona kwamba serikali inatekeleza yale yote ambao wabunge wamedai serikali yetu iyatekeleze kwa wakati kuhusiana na kashfa ya Richmond, EPA na fedha hizo nyingine lukuki ambazo zilikopwa BOT ambazo hazijarudishwa.


FemAct ni mtandao unaojumuisha mashirika yasiyo ya kiserikali zaidi ya 50 yakiwepo Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP),chama cha waandishi Wanawake Tanzania TAMWA, Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu -LHRC, Kituo cha Msaaada wa Sheria kwa Wanawake -WLAC, Fordia, Shirika la Wanasheria wanawake nchini-TAWLA.

BUNGE LETU LINAELEKEA WAPI ?!!

KUMETOKEA vioja ndani ya Bunge, nalo limeingiliwa na ndumba! Ndiyo, imani za kishirikina zimeingia bungeni. Wakati huu wa Bunge kujadili Bajeti tumeshuhudia Bunge likitumia sehemu ya muda, nguvu na rasilimali zetu katika kufuatilia uvumi wa kishirikina.

Tumekwenda mbali, tunaambiwa Bunge letu tukufu linachunguza uvumi huo! Hiki ni kioja kwa namna yake, maana kama jambo ni la uvumi iweje lichunguzwe. Kwamba tumefika mahali tunatumia muda na fedha zetu kuchunguza uvumi! Hivi ushahidi na vielelezo vya uvumi vinapatikanajamani?

Kama jambo ni la uvumi, basi kawaida ya anayehusishwa na uvumi ni kuukanusha vikali uvumi huo. Tulitaraji Bunge, mara baada ya kuanza kuenea kwa uvumi huo lingekanusha vikali baada ya kujiridhisha kuwa ni uvumi tu. Tena ni uvumi wenye kuhusiana na imani za kishirikina. Imani za kishirikina zimechangia sana kurudisha nyuma maendeleo yetu. Tuna mifano ya mauaji ya akina mama wazee na malbino yanayochangiwa na imani hizo. Bunge liwe mfano wa kupiga vita imani hizo.

Ni ajabu, na pengine ni mambo ya aibu hata mbele ya wahisani wanaochangia Bajeti yetu wanaposikia, kuwa katika karne hii ya Sayansi na Teknolojia, Bunge la nchi linatumia muda wake na rasilimali zake kufuatilia na hata kuchunguza masuala ya imani za kishirikina.

Ili kulinda heshima ya Bunge letu na nchi yetu, jambo hili lingeangaliwa kisayansi na kiteknolojia zaidi ili nasi twende na wakati. Kama inadaiwa kuna mbunge ameingia bungeni usiku na kuweka vitu kwenye viti vya wabunge, basi kuna ya msingi ya kuangalia, kujiuliza na kuyapatia majibu kabla ya kuchukua hatua nyingine.

Haya yafuatayo tunaweza kabisa kuanza nayo kuyaangalia kabla ya kulifanya jambo hili kuwa ni kitu kikubwa kinachotuchukulia muda na fedha zetu; Sote tunaelewa, kuwa Jengo la Bunge ni mahali pa kazi kama ilivyo mahali pengine. Walipa kodi wa nchi hii wamechangia jengo la Bunge lijengwe na liwe ni mahali pa kazi zenye lengo la kumsaidia Mtanzania na kulinda maslahi ya umma wa Watanzania. Kila sehemu ya kazi ina taratibu zake.

Tuna imani kuna waliopewa dhamana ya kuruhusu na kuzuia wageni kuingia ndani ya jengo hilo katika wakati wa kazi na baada ya kazi. Lakini kikubwa, huwezi kuingia ndani ya jengo la Bunge bila kufunguliwa mlango na mwenye dhamana ya kushika funguo za mlango huo. Na kwa nini mbunge aliyeingia humo aingie usiku badala ya wakati wa kazi? Tunaambiwa hakuingia peke yake, je aliingia na nani?

Kilichotokea hapa ni ukiukwaji wa taratibu za kazi. Tuaambiwa aliyehusika anajulikana lakini jina halitajwi. Huku hakusaidii kupunguza uvumi, kunaongeza uvumi na kutupotezea wakati wa kujadili mambo ya kimsingi ya taifa letu. Jengo la Bunge ni la kisasa na la gharama kubwa. Tunaambiwa kamera za kurekodi matukio ndani ya jengo hilo hazikufanya kazi isipokuwa moja tu. Je, ni nani anayehusika na kuhakikisha kamera hizo zinafanya kazi?

Maswali yanayoulizwa hapa na mengineyo yana wahusika wa kuyajibu. Bunge litusaidie kupata majibu ya maswali haya ya msingi ili tupunguze hofu ya kutokea kwa madhara makubwa huko twendako. Maana, tunachokiona hapa ni uzembe wa baadhi ya watendaji katika Jengo hilo la Bunge. Leo kaingizwa Mheshimiwa Mbunge usiku, hatujui kesho ataingizwa nani. Inahusu usalama wa Jengo la Bunge kwa maana ya usalama wa Wabunge wetu. Tuko katika karne ambayo, mbali ya mambo mengine, tunapambana na ugaidi. Kamera za ndani na nje ya ukumbi wa Bunge si za mapambo. Zimewekwa ili kuchangia katika shughuli za usalama. Wahusika wanafanya nini?

Naam. Ni wakati sasa wa Bunge kukemea vikali imani za kishirikina na hasa zinapofika na kuingia ndani ya Bunge. Huko nyuma tumesikia habari za popobawa na kadhalika. Haya ni mambo ya abrakadabra, kama ninavyoyaita siku zote. Hayana maana yoyote. Ni kama vile mbinu ya wajanja fulani kututaka tutoke kwenye mstari wa kujadili mambo ya msingi yenye kuhusu hali yetu ya sasa na mustakabali wa nchi. Tusikubali kutoka kirahisi kwenye mstari wa kujadili ya maana na ya msingi kwa taifa. Na hapa nitarudi kwenye kujadili yenye kumhusu Mtanzania wa kawaida kuhusiana na Bajeti ya mwaka huu.

Jumatatu ya juma hili nilisimama kituo kimoja cha mafuta mjini Iringa. Usiku ulikuwa unakaribia. Mbele yangu nilimwona mama aliyeshika galoni ndogo. Ni galoni tupu ya ujazo wa lita tano. Alisimama sehemu ya kuuzia mafuta ya taa. Nilisogea, nilimsalimia. Akaniambia anamsubiri kijana wa kumpimia mafuta ya taa. Anaitwa Mama Mwajuma.

Mara akatokea kijana anayehusika. Anaitwa Bakari. Mama Mwajuma alinunua mafuta ya taa ya shilingi 200! Bei ya lita moja ya mafuta ya taa kwa siku hiyo ilikuwa ni shilingi 1450. Kwa shilingi 200 hupati hata robo lita. Mama yule alipimiwa nukta kadhaa za mafuta. Ndiyo, alipimiwa matone kadhaa ya mafuta ya taa.

Na kama ilivyo jina lenyewe la mafuta, Mama Mwajuma alikwenda kununua mafuta ya kuwashia koroboi. Hakuwa na uwezo wa kununua lita moja ya mafuta ya taa, ni bei ya juu sana. Bakari, kijana mwuza mafuta aliniambia; kuwa zamani kipimo cha kuanzia ilikuwa ni mafuta ya shilingi 500. Kwamba mpaka mwaka jana lita moja ilikuwa ni shilingi 900. Bakari alizidi kunielimisha, kuwa kutokana na kuelewa unyonge na hali ngumu za watu wengi, wameamua kuwasaidia hata wenye kutaka mafuta ya taa ya shilingi 200.

” Tutafanye kaka, si unaona mama huyu hali yake.Nikimkatalia mafuta ya shilingi 200 atakwenda kulala giza. Ni bora nimpe hayo matone ya mafuta akajaze kibatari chake”.

Naam. Tunachoongelea hapa si uvumi. Ni hali halisi. Bei za mafuta zimepanda sana, hivyo ugumu wa maisha umezidi kwa Watanzania wengi zaidi. Bei ya nishati ya umeme nayo ni ya juu sana. Leo kwenye miji yetu kuna Watanzania wanaotumia vibatari. Hawamudu tena kulipia gharama za umeme.

Tufahamu, kuwa kwenye hospitali na zahanati zetu kuna wagonjwa wanaolala chini kwa kukosa vitanda. Kuna wagonjwa wanaokosa dawa. Katika nchi yetu hii, achilia mbali vijijini, mijini kuna barabara za mitaa zenye mashimo kama mahandaki. Tuna shule vijijini na mijini ambako wanafunzi wanakaa chini na wengine kukosa walimu. Haya yanatokea katika nchi yetu hii.

Kwa nini wagonjwa wetu walale chini na wakose dawa? Kwa nini watoto wetu wakae chini madarasani na kukosa walimu? Fedha zinakwenda wapi? Haya na mengineyo ndio maswali tunayopaswa kujiuliza na kujiumiza vichwa. Haya si mambo ya uvumi. Haya si mambo ya abrakadabla. Ni hali halisi. Hatuhitaji tume kuchunguza. Tunahitaji kuchukua hatua. Sasa.


Chanzo: Gazeti la Raia Mwema
Na Maggid Mjengwa (Blogger).

Saturday, June 21, 2008

Wanamtandao wa Kufuatilia Bajeti ya Afya ya Uzazi na Ukatili wa Kijinsia Wakutana

Kikundi cha kufuatilia ukatili wa kijinsia na bajeti ya afya –hasa afya ya uzazi– katika Manispaa ya wilaya ya Kinondoni chakutana kwa kwa mara ya kwanza. Kikundi hicho kinachojumuisha asasi kumi na mbili zilizopo ndani ya Manispaa ya Kinondoni kiliundwa kutokana na semina juu ya Upimaji na Ufuatiliaji, ilifanyika tarehe 12 na 13 Juni, 2008. Semina hiyo iliyoandaliwa na TGNP na kuhudhuriwa na asasi za kijamii zipatazo 40 kutoka katika mikoa ya Kigoma, Rukwa, Dodoma, Pwani, Sumbawanga, Lindi, Manyara, Mtwara, Kilimanjaro, Unguja, Pemba na Morogoro. Lengo kuu la semina hiyo ilikuwa ni kuzipa asasi uwezo wa kutathimini na kufuatilia mambo mbalimbali katika maeneo yao. Pia malengo mengine ni pamoja na kuwajengea uwezo wa ushawishi na utetezi, kubadilishana uzoefu, kuimarisha mawasiliano, na kutengeza mitandao ya kufanya kazi kwa pamoja. Semina hiyo iliwezeshwa na Lilian Liundi (TGNP)-, Ananilea Nkya (TAMWA), na Salima Mauldi (Sahiba Sisters).

Baada ya semina hiyo washiriki waliweza kuunda mitandao ya kufanya kazi kwa pamoja kulingana na maeneo wanayotoka. Kila mtandao uliweza kupewa kazi maalumu ya kufuatilia na kutathimi ndani ya kipindi cha mwaka mmoja. Ijumaa ya tarehe 20/06/2008 mtandao wa kutathimini utekelezaji wa bajeti ya afya ya uzazi na ukatili wa kijinsia katika Manispaa ya Kinondoni uliweza kukutana kwa mara ya kwanza na kujadili jinsi ya kutekeleza jukumu lao. Asasi zinazounda mtandao huo ni; Precious Jewells Organization (PJO), Tanzania Women in Law and Advocacy (TAWLA), Tanzania Youth For Development (TAYOFODE), Makuburi Women Development Allowance (MWDA), Binti Leo, Kigogo Youth and Women Program (KYWP), Upendo Group, Victoria Agency Tanzania Trust (VTAT), Tanzania Policy Femele Network (TPENET). Mtandao huu unasimamiwa na TAWLA.

Mwenyekiti wa mtandao huu Harrieth Bandari kutoka MWDA na katibu wake Ms. Dorosta kutoka VTAT walifungua na kuongoza kikao. Baada ya kueleza kwa ufupi majukumu yao, wanamtandao walipata nafasi ya kujadiliana maswala mbalimbali muhimu. Wanamtandao walijadiliana juu ya shughuli muhimu ambazo walikubalina waanze nazo katika kukamilisha jukumu lao. Shughuli hizo muhimu ni pamoja na; Utafiti, Uelimishaji, Mafunzo, na Ushawishi na Utetezi. Walikubaliana wachague baadhi ya kata ndani ya Manispaa ya Kinodoni na kufanya utafiti juu ya hali ya ukatili wa kijinsia, hali ya upatikanji wa huduma za kiafya na uelewa wa jamii juu ya tatizo la ukatili wa kijinsia. Walikubaliana utafiti huo uanzie katika ngazi ya serikali ya mtaa na kufikia ngazi ya kikata. Pia walikubaliana waende katika vituo vya polisi, na mahakamani kuona na kupata maelezo na takwimu juu ya ukatili wa kijinsia ulivyo. Kuhusu uelimishaji walikubaliana waandae programu ya pamoja ya kuelimisha jamii juu ya tatizo la ukatili la kijinsia katika maeneo yatakayoonekana ni korofi zaidi baada ya kufanya utafiti. Pia walipendekeza watumie vyombo vya habari katika kuelimisha jamii.
Kuhusu Ushawishi na Utetezi hawakuweza kujadili mada hii kutokana na muda kwisha na hivyo kikao kuharishwa hadi tarehe 24/06/2008, ambapo walikubaliana itakuwa ni siku ya kumaliza ajenda zilizobaki na kugawana majukumu ya utekelezaji.

Kwa maoni yao wanamtandaoo wanaona changamoto zitakazo wakabili katika kutekeleza jukumu lao ni pamoja na ugumu wa kupata pesa za kutekeleza wajibu wao, kitu ambacho wanahisi kinaweza kukwamisha ari waliyonayo katika kufanikisha azima hii. Pia wanaona mtandao huu ni fursa ya pekee kwao katika kufanya kile ambacho wanahisi ni chenye manufaa kwa jamii na kwa muda mrefu walikuwa walihitaji nafasi ya kukitekeleza, na hivyo utaweza kutimiza ndoto zao katika kuleta usawa na huduma bora za afya kwa jamii.


Picha za Wanamtandao Kikaoni.


Wanamtandao wakijadiliana masuala mbalimbali katika kikao.


Kikao kinaendelea...


Picha ya pamoja ya wanamtandao.

Thursday, June 19, 2008

SEMINA YA MJADALA WA MUSWADA WA BAJETI YA 08/09.

Utangulizi.
Mada juu ya tafakari na mapendekezo kuhusu bajeti ya 2008/09 je imekidhi matarajio yetu? Iliyowakilishwa katika semina za kila wiki za Jinsia na Maendeleo katika viwanja vya TGNP. Wiki hii ya tarehe 18/06/2008. Mjadala ulihudhuriwa na wanaharakati kutoka katika vikundi mbalimbali vya kijamii waliofikia 200 hivi na watoa mada wakuu walikuwa ni dada Gema Akilimali kutoka FemACT, mwakilishi kutoka UTU Mwanamke, na dada Mary kutoka Haki Elimu. Wawezeshaji waligusia mapungufu yaliyomo katika bajeti ya 08/09, ambapo watoa mada walitoa mapungufu ambayo wanaharakati waliyaona katika bajeti hiyo, na waligusia maswala ya msingi ambayo bajeti ya mwaka huu yalishindwa kutoa majibu ya kuridhisha na kuhitaji majibu ama marekebisho zaidi kabla ya mswada huo kupitishwa. Ripoti hii fupi inajaribu kuonyesha maeneo ambayo wawezeshaji waliyagusia na kuhitaji marekebishio ama ufafanuzi zaidi kutoka kwa serikali, na mwisho itaonyesha maoni na michango ya washiriki. Kwa ufupi semina hii iliweza kutoa fursa kwa wanaharakati kuwakilisha maoni na hisia zao juu ya mswada huu wa bajeti.

Kwanza, suala la utegemezi wa mapato kutoka nje, utegemezi huu umepungua kutoka asilimia 42% hadi 34% mwaka huu, lakini bado wanaharakati wanaona kuna haja ya serikali kucha kabisa utegemezi kutoka kwa wafadhili kwani kufanya hivyo ni chanzo cha mashinikizo mbalimbali kutoka kwa wafadhili hao katika utungaji wa sera hasa zile za masoko huria.

Pili, upande wa matumizi, mapendezo ya kutumia shlingi 7.1 trilioni ni kiasi kikubwa sana, wanaharakati walipendekeza serikali ipunguze wizara na mawaziri na kuhakikisha kila mtumishi wa umma anafanya kazi kwa ufanisi na kuthamini kazi yake, badala ya kuwa mzigo kwa mlipa kodi. Na rasilimali ziongezwe kwa wafanyakazi wa sekta nyeti kama walimu, madktari, wauguzi, na wataalamu wa kilimo hasa mabwana shamba. Na serikali bado haijaweaka mikakati madhubuti ya kudhibiti matumizi mabovu ya fedha za umma, kama ripoti ya mkaguzi mkuu wa serikali ilivyofichua ubadhirifu mkubwa katika halmashauri katika miaka iliyopita, hivyo wanaharakati wanahitaji mkakati ulio wazi wa kupambana na hali hii.

Tatu, mgawanyo wa kiasi cha 64% ya fedha ya bajeti katika sekta muhimu za elimu, miundombinu, maji, afya, kilimo, na nishati ni hatua ya kupongezwa, hata hivyo tungependa kujua ni kwa kiasi gani rasilimali hizi zitakwenda kwa kila sekta, nani atafaidika, na zitaweza vipi kuimalisha katika utoaji wa huduma kwa kila mwananchi? Na kuhusu swala la kilimo kupewa kipaumbele kwa kilimo cha mashamba makubwa ni kuwafanya wakulima wadogo dogo kukosa nafasi ya ushindani na hivyo kuwanyima ajira na kuwaongezea ugumu wa maisha, hivyo wito wetu kwa serikali ni kwamba waangalie upya suala la wakulima wadogodogo na ambao wengi ni wananchi wa vijijini.

Nne, maji safi na maji taka, serikali imepunguza kiasi cha 40% ya fedha katika bajeati ya maji ukilinganisha na mwaka jana. Wanaharakti wanatoa wito kwa serikali kusikia kilio cha watu wengi wa vijijini waliosahulika katika kupata huduma ya maji safi na salama maji ni kipaumbele kikubwa kwa wanawake/wasichana kwa sababu wao ndio wanajishughulisha kutafuta maji pamoja na kazi nyingine kedekede ikiwemo kutunza wagonjwa, kupika, usafi nk.

Tano, ajira na maisha bora. Bajeti hii haina mkakati wa jinsi ya kuwezesha ajira na uhakika wa maisha bora. Kwa majibu wa ripoti ya umasikini na maendeleo ya binadamu ya 2007 hali ya watu wasio na ajira ni mbaya sana hasa kwa wanawake na vijana, na takribani 40% ya wanawake katika jiji la Dar ers sdalaam hawana ajira ukilinganisha na 23% ya wanaume. Wanaharakti wanasisitiza serikali iweke mipango madhubuti katika kukuza ajira kwa vijana na wanawake na kuboresha maisha ya wananchi wa hali ya chini.

Sita, hotuba ya bajeti haijagusia katika sehemu yoyote kushirikisha sekta binafsi katika kufanikisha malengo ya bajeti, hivyo wanaharakti wanaona kuna umuhimu mkubwa kwa serikali kutoa fursa kwa sekta binafsi hasa mashirika ya kijamii katika kutekeleza mipango ya bajeti ya mwaka 08/09.

Mapendekezo na maoni ya washiriki.

1. Elimu ya shule ya Msingi ipewe kipaumbele zaidi. Ubora uongezwe katika walimu, na vitabu, na sio majengo pekee kama ilivyo sasa.
2. Madini hayajapewa kipaumbele katika kuchangia pato la taifa, bado serikali inatakiwa kuongeza kipaumbele zaidi katika ukusanyaji wa kodi za madini na iachane na mikataba ya zamani ya madini ambayo ni ya kinyonyaji.
3. Serikali idhibiti mfumuko wa bei hasa hasa katika mazao ya kilimo kwani wananchi wa hali ya chini ndio wanaoumia zaidi na hali hiyo.

4. Kodi katika pembejeo za kilimo zitolowe kabisa tofauti na sasa ambapo mkulima bado anatozws kodi kubwa sana tofauti na faida anayopata kutokana na mazao.

5. Kodi inayopatikana kutoka kwa wananchi inaweza kuendesha nchi hii hivyo kinachotakiwa wananchi waongeze ufuatiliaji wa mapato na matumizi ya serikali kuanzia ngazi ya serikali ya mtaa hadi wilayani ili kupunguza mianya ya ubadhirifu unaofanywa na maofisa ambao sio waaminifu.

6. Mchango wa vifaa vya uzazi ufutwe kabisa kama sera ya serikali inavyosema, na tofauti na sasa ilivyo kwani katika hospitali nyingi za serikali bado wananchi wanatakiwa kuchangia vifaa hivyo na ni chanzo cha vifo vya akina mama wengi hasa wale wa kipato cha chini.

7. Serikali itafute vyanzo vingine vya mapato na sio kuongeza kodi katika sigara na bia kila mwaka. Bado kuna vyanzo vingi vya kodi ambavyo havijaguswa.


Baadhi ya Picha za washiriki wa Semina hiyo.

Mtoa Mada wa Kwanza Mama Gema Akilimali (FemAct) akiwakilisha

Mtoa Mada wa Pili Dada Sarah Kutoka Utu Mwanamke akiwakilisha.


Baadhi ya washiriki wakifuatilia semina.

Baadhi ya Washiriki wakifuatilia semina

Dada Subira Kibigi akichangia hoja juu ya mada zilizowakilishwa.

Tuesday, June 17, 2008

SEMINA ZA MAENDELEO NA JINSIA.

Unafuatilia Mjadala Kuhusu Bajeti 08/09?
Je Unadhani Bajeti ya 08/09 Imekidhi Matarajio ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania?
Njoo Katika semina za Maendeleo na Jinsia Tuweze Kutafakari Mapendekezo ya Bajeti ya 08/09 Kwa Upana.

MTOA MADA: GEMMA AKILIMALI
TAREHE: 17/06/2008 MUDA; Saa 9:00 Alasiri – 11:00 Jioni

MAHALI: MTANDAO WA JINSIA TANZANIA, BARABARA YA MABIBO – MKABALA NA CHUO CHA USAFIRISHAJI (NIT) DSM
KARIBUNI WOTE!

Wednesday, June 11, 2008

SEMINA YA KWANZA YA KUJIFUNZA BLOGU

Wanaharakati waliohudhuria semina ya kwanza ya uzinduzi wa blogu iliyofanyika katika ukumbi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Mabibo, Dar-es-Salaam - Tanzania ( Picha kwa hisani ya Dismas Zunda)

KARIBUNI WANAHARAKATI

Karibuni kwenye blogu ya Rudisha Rasilimali Kwa Wananchi. Sisi ni Wanaharakati wa Semina za kila Jumatano za Jinsia na Maendeleo (GDSS) ambao tuko katika harakati za kuhakikisha kuwa rasilimali zetu zinanufaisha jamii nzima kwa ujumla na sio watu wachache tu. Vunja ukimya!