Monday, September 29, 2008

Semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS)

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)
Unakaribishwa Katika Mfululizo wa Semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS)
ambapo:
Matina H. Mbelwa Wa Chuo Kikuu Huria Cha Tanzania)

Atawasilisha Mada Kuhusu:

JICHO LA SHERIA KUHUSU UZEMBE KATIKA UTOAJI WA HUDUMA ZA AFYA NCHINI.

LINI: Jumatano tarehe 8 Octoba 2008
MUDA: Saa 9:00 - 11:00 Jioni.

Mahali: Viwanja Vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu na ChuoCha Usafirishaji, Mabibo Sokoni.

WOTE MNAKARIBISHWA
.

Mrejesho wa Semina za Jinsia na Maendeleo.

Kuelekea Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Kutathimini Hali ya Afya.

Mkutano Mkuu wa kila mwaka wa kutathimini sekta ya afya ambao unatarajiwa kufanyika tarehe 8/10/08 utawashirikisha wadau mbalimbali wa maswala ya Afya ambao ni pamoja na; wizara ya Afya, Tamisemi, Mashirkia yasio ya Kiserikali, na Nchi wahisani na natarajiwa kujadili mambo yafuatayo: Mkakati wa serikali wa miaka sita ijayo katika sekta ya afya; Kutathimini mipango iliyopita; kuangalia ufanisi wa kiutendaji na utoaji wa Huduma; na kuangalia Changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa sera ya afya.

Katika Mkutano huo wanaharakati watawakilishwa na Kikundi cha Utetezi wa Haki sawa kwa Wote Katika Afya (A Group for Health Equity) Kikundi Kinachoundwa na taasisi zinazopigania haki za binadamu. Jumatano ya tarehe 24/09/2008 katika Semina za Jinsia na Maendeleo, Wanaharakati walijadili mapendekezo ambayo wanataka yawasilishwe katika mkutano huo. Pamoja na mambo mengine walipendekeza mambo yafuatayo yakajadiliwe na kupatiwa ufumbuzi; Sera ya Taifa ya Afya ya Mama na Watoto chini ya Miaka Sita Inatekelezwa kama inavyosema; Serikali inatekeleza Makubaliano ya Abuja(Abuja Declaration) yaliyofikiwa na viongozi wa nchi huru za Afrika mwaka 2000 juu ya sera ya afya; Mkakati maalumu wa Kupunguza vifo vya akina mama uliozimiwa na serikali na wadau wengine tarehe 22/04/2008 unatekelezwa kama makubaliano hayo yalivyoafikiwa; na serikali ichukue hatua dhidi ya wale wanaochukua rushwa katika sekta ya afya.

Pia wanaharakaati walipendekeza serikali iangalie upya rasilimali inayotengwa katika afya ya mama na watoto chini ya miaka sita, kwani mpaka sasa vifo vya akina mama wanaojifungua vinaendelea kutokea kwa kasi kubwa na kuhakikisha rasilimali kama wahudumu, vifaa vya uzazi, vifaa vya mawasiliano, miundo mbinu kama maji, umeme, na barabara vinaboreshwa kutokana na kuchangia sana vifo vya wajazito. Wanaharakati wametakiwa kufuatilia kiasi cha fedha na matumizi yake katika maeneo yao wanayotokea kuanzia ngazi ya kata mpaka wilayani, hii itasaidia katika kufuatilia na kutathimini utekelezaji wa sera ya afya kama ilivyopangwa.

Wanaharakati walipendekeza serikali itenge kiasi cha bilioni 10 kwa ajili afya ya akina wajazito kiasi hiko ni sawa na asilimia 1.7 ya fedha ya bajeti ya wizara ya afya, tofauti na sasa ambapo imetenga kiasi cha bilioni 3.6 amabacho ni sawa na asilimia 0.05 ya fedha yote ya bajeti ya wizara ya afya kwa mwaka 2008.

Pendekezo lingine la wanaharakati ni kuishawishi serikali inasimamia utekelezaji wa sera ya Afya ya uzazi kama ilivyo, kwa sasa wanawake wengi wanakufa wakati wa kujifungua kutokana na kukosa fedha za kununulia vifaa vya kujifungulia (Delivery Kit). Vifaa hivyo kwa mujibu wa sera ya serikali ni bure kabisa.

Ndugu mwanaharakati unachangia nini katika kuboresha sekta hii ya afya? Je unadhani serikali imefanya vya kutosha katika kuboresha sekta hii ya afya? Je, nini kifanyike katika kuboresha sekta hii ya afya- hasahasa katika eneo hili la afya ya uzazi?

Friday, September 26, 2008

Shindano la Insha

Dhidi ya Kutumikisha na Kunyanyasa Watoto Kingono

Washiriki: Wanafunzi wote wa Shule za Sekondari na Msingi
nchini Tanzania, wenye umri chini ya maika 18.

Changia maoni yako kuhusu: Nini kifanyike ili watoto waepukane na vitendo vya unyanyasaji na utumikishaji kingono?

Insha yako izingatie: Kutoa suluhisho, mawazo yenye ubunifu na ambayo yanatekelezeka. Insha ifafanue jukumu la viongozi na kila mwanajamii wakiwemo Watoto wenyewe, Wazazi, Walimu, Viongozi wa Dini, Mtaa/Kijiji, Kata, Diwani, Wakuu wa Wilaya, Wabunge, Mkoa na Serikali kuu katika kupambana na hatimaye kukomesha vitendo vya ukatili kwa watoto kama ubakaji, mimba na ndoa za utotoni, kulazimishwa ngono na kupewa fedha au kutumia watoto kufanya biashara ya ukahaba. Kila Insha iliyochapishwa au kuandikwa kwa kalamu, isizidi maneno elfu moja (1,000).
Zawadi:
· Mshindi wa 1 - Tsh. 300,000/-
· Mshindi wa 2 - Tsh. 200,000/-
· Mshindi wa 3 - Tsh.100,000/-
· Washindi 10 bora (Tsh. 50,000/-) kila mmoja

Lugha: Kiswahili au Kiingereza.
Andika: Jina lako, Umri, Jinsi, Jina la Shule na Mkoa.

Insha kumi bora zitachapishwa kwenye kitabu kinachoandaliwa kwa ushirikiano na Vyama vya Wanahabari vya Kenya (AMWIK), Ethiopia (EMWA), Uganda (UMWA) na Tanzania (TAMWA). Kitabu hicho kitasambazwa kwenye shule mbalimbali ili kuwaelimisha watoto juu ya vitendo vya unyanyasaji na utumikishaji kingono na kuwawezesha kushiriki katika kampeni mbalimbali za kupinga vitendo hivyo. Washindi watatangazwa kupitia vyombo mbalimbali vya habari nchini, wiki tatu baada ya kufunga shindano hilo.

Mwisho wa kupokea Insha: Ijumaa, Oktoba 24, 2008.
Tuma Insha yako kwa: Shindano CSAE, SLP 8981, Dar es Salaam
au barua pepe; tamwa@tamwa.org au admin@tamwa.org.
Simu: 0777-002002 au 022-2772681

Au fika:
Ofisi za TAMWA
Sinza-Mori, Block 47
Angalizo: Insha itakayoandikwa na watu walio na umri zaidi ya miaka 18

Thursday, September 25, 2008

Maandamano ya Kulaani Mauaji ya Maalbino.

Muda sasa umepita tangu wimbi la mauaji ya Maalbino liaanze kutokea hapa kwetu Tanzania kwa Imani za kishirikina za kupata utajiri, karibu Maalbino 30 wameshapoteza maisha. Tayari serikali imetangaza adhabu kali kwa wahusika endapo watakamatwa, mpaka sasa wahusika hawajatiwa mbaroni na kusababisha ndugu zetu albino kuishi kwa hali ya wasiwasi kwani mauaji yanaendelea kwa kasi kubwa. Soma zaidi kuhusu mauaji ya Malbino yanayoendelea.

Chama cha Maalbino Tanzania kwa kushirikiana na Wanaharakati wameandaa Maandamano ya kulaani vitendo hivyo na kuikumbusha serikali kwamba inapaswa kukemea na kuchukulia uzito Jambo hilo. Maandamano hayo yataanzia katika viwanja vya Mtandao wa Jinsia Tanzania(TGNP) na kuishia katika Viwanja vya Jangwani, yatafanyika tarehe 18/10/2008 na yanatarajiwa kuhudhuriwa na wanaharakati mbalimbali wa haki za binadamu na wapenda amani kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Wanaharakati na Wapenda Amani Wote Mnakaribishwa katika Maaandano haya ya Kupinga Ukatili Wanaofanyiwa Ndugu Zetu Maalbino.

.

Tuesday, September 23, 2008

Gender and Development Seminar Series (GDSS)

Gender and development Seminar Series (GDSS)

You are Invetd to the Weekly Session in Which HealthEquity Group:

Joint Annual Sector Review: A Community Voice

Wednesday 24th September, 2008
Time: 3:00Pm - 5.00pm

Venue TGNP/Gender Resources Center, Mabibo Road - Adj, NIT Dsm.

Come One...... Come All

Monday, September 22, 2008

Mfululizo wa Semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS)

Mapendekezo ya Wanaharakati Kuhusu Mabadiliko ya Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971
Semina ya tarehe 17th Septemba, mada ilikuwa ni Mapendekezo ya wanaharakati katika sheria ya ndoa, iliyowakilishwa na wawakilishi kutoka kituo cha haki za binadamu. Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 ina vipengele yenye mapungufu ambavyo wanaharakati wamekuwa wakiyapigia kelele vipengele hivyo vifanyiwe marekebisho kwa sababu vipengele hivyo vinawanyima haki za msingi watoto wa kike za kulitumika Taifa. Sheia hiyo inatoa uhalali wa ndoa za umri mdogo kwani inaruhusu watoto wadogo kuolewa waakiwa na umri wa miaka 14 (kwa ridhaa ya wazazi) au miaka 15 kwa amri ya mahakama. Pamoja na juhudi nyingi za wanaharakati bado sheria hiyo haijafanyiwa marekebisho na inaendelea kutumika na kuwakandamiza watoto wa kike. Wanaharakati wanaipinga sheria hiyo ya ndoa kwa sababu inamadhara yafuatayo:

• Kutokana na maumbile yao madogo mabinti wanaolewa wakiwa na umri mdogo wanaweza kupata fistula wakati wanapojifungua au kufa au watoto kuafariki au vyote.
• Binti hanakuwa hayupo tayri kisaikolojia, mabinti wanaolewa wakiwa wadogo sana wanakuwa hawapo tayari kuishi katika maisha ya ndoa, hivyo kusababisha matatizo makubwa ya kisaikolojia kwa wasichana wanaoolewa katika umri mdogo.
• Husababishia maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa wasichana wadogo wanaoolewa. Kwa watoto kuolewa katka umri mdogo kunawasababishia wawepo katika hatari ya kupata maambukizi kwa sababu wanakuwa hawana maamuzi katika tendo la ndoa na kushindwa kujitetea ama kujikinga na maambukizi, pia maungo yao madogo yanawafanya wawepo katika hatari kubwa ya mambukizi.
• Mfumo wa elimu unamtaka katika umri huo binti awe shuleni, hivyo sheria hii inakinzana na sheria nyingine za nchi ambazo zinamtaka kila mtoto awepo shuleni katika umri kama huo wa mika 14 na 15.
• Sheria hii inaendeleza ukatili wa kijinsia, kwa sababu inachangia watoto wa kike kuendelea kunyanyaswa kwa kunyimwa haki yao ya msingi ya kuweza kuchagua aina ya maisha wanayotaka kuishi.

Je wadau mnasemaje kuhusiana na sheria hii ya ndoa? Je Serikali imefanya vya kutosha kuibadilisha sheria hii ya ndoa? Je wanaharakati wanaweza kufanya nini ili kuweza kuleta mabadiliko ya sheria hii?

Friday, September 19, 2008

Mdahalo mlimani Oktoba 10

UNIVERSITY OF DAR ES SALAAM (UDSM)
Mwalimu Julius Nyerere Chair in Pan-African Studies
P. O. Box 35091
Tel: 255-22-2410763,
255-22-2410500-9, x.2326
Cell: 255-754- 475 372
Dar es Salaam
issashivji@cats-net.com


10 OKTOBA 2008
MNAKARIBISHWA MNAKARIBISHWA MNAKARIBISHWA

MADA: ZAHMA ZA CHAKULA NA MAFUTA (FOOD AND FUEL CRISIS)

MCHOKOZI MKUU: JENERALI ULIMWENGU

WASHIRIKI:PROFESA HAJI SEMBOJA [ERB, UDSM] PROFESA AIDA ISINIKA [SUA/OXFAM]
BI. SIHAM AHMED [TUCTA]
DKT. KHOTI KAMANGA [LAW, UDSM]
DKT. ADOLF MKENDA [ECONOMICS, UDSM]
DKT. NG’WANZA KAMATA [POLITICS, UDSM]

TAREHE:10 OKTOBA 2008 (IJUMAA)
MUDA:10 – 12 (MCHANA)
MAHALI:UKUMBI WA NKRUMAH,
CHUO KIKUU,
MLIMANI

Kaulimbiu ya Mbongi:Kila mtu hutafakari; kila mtu huthaminiwa; hakuna anayethaminiwa zaidi au pungufu kuliko mwingine.

Wednesday, September 17, 2008

Siasa za Afrika tunaelekea wapi?

Hivi miaka ya karibuni kumekuwa na tabia ya watawala kuendesha chaguzi,wakishindwa wanapika matokeo,kung'ang'ania madaraka,suluhu yake eti inakuwa serikali mseto vyafaa kukemewa kwa kinywa kipana.Ilianzia zanzibar(ingawa hadi leo hawaafikiana).Ikaja kenya,leo zimbabwe.

Nani anajua kesho itakuwa zamu ya nchi ipi? Afrika tutafika kwa mtindo huu?

Tuesday, September 16, 2008

Mfululizo wa Semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS)

Uchambuzi na Maoni ya Wasomaji kwa Machapisho ya: Hali Halisi Ya Kijinsia Tanzania na Tathmini ya Miaka 10 Baada Ya Beijing.

Hali ya Uchumi

Wanasemina waliona mfumo wa kiuchumi unaoendelea ni wa kibabe na unoendeleza unyonyaji wa rasilimali kutoka kwa wananchi walio wengi na maskini na kuwanufaisha watu wachache matajiri na umesababisha wananchi wengi maskini kukosa huduma za msingi za kijamii. Washiriki waliweza kuonyesha mapungufu katika hali ya uchumi wa Tanzania kwa katika vipengele ambavyo wanahisi vinachangia kudorora kwa uchumi wa nchi, maeneo hayo ni pamoja na;

1. Ukosefu mkubwa wa ajira- wananchi wengi hawana ajira za kueleweka kitu ambacho kinasababisha wengi wao kuishi katika hali duni ya kimaisha. Vijana na wanawake wengi hawana ajira hivyo hufanya kazi ambazo zina kipato kidogo kwa ajili ya kujikimu kimaisha.

2. Ukosefu wa fursa sawa kwa wote. Mfumo wa kiuchumi bado unalea watu wachache kuendelea kujineemesha kiuchumi na ukiacha kundi kubwa katika hali mbaya ya kiuchumi. Watu wachache wenye nafasi nzuri wanawapeleka watoto wao katika shule nzuri, na baadae wanapata nafasi nzuri za kazi katika mashirika mbalimbali hivyo kuendelea kujipatia utajiri zaidi. Pia nafasi na kazi mbalimbali za umma zinatolewa kwa ambao wana nafasi nzuri ya kifedha au wale wanaoweza kuhonga kidogo kwa ajili ya nafasi au kazi hizo.

3. Sekta isiyo rasmi haijapewa kipaumbele katika kukuza uchumi na kupunguza umasikini. Sekta hii ambayo inachukua asilimia kubwa ya wananchi lakini bado haijapewa kipaumbele, na serikali imekuwa ikiwanyanyasa watu ambao wamekuwa wakijiari wenyewe kwa mfano, wafanyabiashara ndogo ndogo kwa muda mrefu wamekuwa wakinyanyaswa na askari wa jijini Dar es Salaam mara kwa mara.

Wadau mnasamaje kuhusiana na haali ya uchumi nchini Tanzania? Je serikali imefanya vya kutosha katika kuinua uchumi wa nchi?

Monday, September 15, 2008

Tanzania iseme hapana kwa EPA hii

WIZARA ya Viwanda, Biashara na Masoko iliandaa warsha ya siku moja mjini Dar es Salaam, kujadili juhudi zinazofanywa na Umoja wa Ulaya (EU), wa kuwa na mpango mpya wa kibiashara wa Makubaliano ya Ushirikiano wa Kiuchuni (EPA) kati yake na nchi za Afrika, Caribbean na Pacific (ACP).

Warsha hiyo iliyoandaliwa maalum kujadili utafiti uliofanywa na Shirika la Kimataifa la Misaada la Oxfam la Uingereza, ilikubaliana na matokeo utafiti huo, kwamba mpango huo mpya wa Ulaya ni kitanzi ambacho kitaua maendeleo ya nchi hizo kufanya ziendelee kuwa tegemezi la wakubwa hao wa kisiasa na kiuchumi.

Tunaunga mkono msimamo ulioonyeshwa na washiriki wote wa warsha hiyo, iliyowashirikisha wadau mbali mbali, wakiwamo wawakilishi wa vikundi vya kijamii na wafanyabiashara, kwamba mpango huo haufai.

Kama ilivyojitokeza katika warsha, kuingia kichwa kichwa kusaini mkataba wa mpango huo mpya wa ushirikiano itakuwa ni kosa la karne, ambalo halipaswi kufanywa na watu wa kizazi cha sasa, waliokwenda shule.

Akichangia katika warsha hiyo, Mzee Arnold Kileo alitahadharisha kwamba kusaini mpango huo itakuwa ni sawa na kuirudisha nchi yetu katika enzi za machifu, waliorubuniwa kwa shanga kuuza ardhi zao kwa kusaini mikataba wasiyoielewa.

Kwa kifupi ni kwamba, vipengele vilivyomo katika Mkataba wa EPA havina maslahi kwa nchi zetu zinazoendelea. Ulaya inataka kutumia msuli wake wa kiuchumi kuziburuza nchi hizo ziendelee kuteseka na umasikini na ukosefu mkubwa wa ajira.

Ushirikiano unaotaka kufanywa na Ulaya unaoweza kulinganishwa na wa Goliati na Daudi, katika uwanja usiokuwa tambarare, utaleta majuto makubwa kwani utavuruga mambo mengi kwa hali ilivyo sasa kiuchumi katika eneo letu.

Kwa mfano, mfumo wa utozaji kodi, kama unavyosomeka katika kifungu cha 15 cha mkataba huo, unazitibua nchi zilizomo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ajili tu ya kuunufaisha Umoja wa Ulaya.

Cha kufurahisha ni kwamba, kupitia warsha hiyo, wadai walihakikishiwa na wachangiaji wa upande wa serikali, kuwa Tanzania haiwezi kutia saini katika mkataba huo kama ulivyo hivi sasa.

Kama kweli kuna umuhimu wa kufanya biashara na Ulaya, basi iwe katika uwanja wa tambarare. Hivyo basi, tunaunga mkono wote wanaotaka serikali iendelee kushirikiana na wadau wote na kufikia uamuzi wa kusaini pale tu marekebisho yatakapofanywa, ambayo yataondoa kasoro zote zilizoonekana kwa wakati huu.

Bila ya hivyo, Tanzania iseme HAPANA kwa mpango huo, kwani utauza uhuru wetu na kutuzidishia umasikini na ukosefu wa ajira utakuwa mkubwa zaidi.

Raia Mwema
Sept 10, 2008.

Friday, September 12, 2008

Mauaji ya Albino ni Ujinga

HAKUNA lugha sahihi ya kuelezea tatizo la mauaji ya albino zaidi ya kusema ni vitendo vya kinyama na vinavyokiuka haki ya msingi ya binadamu wenzetu; haki ya kuishi na kulindwa na jamii inayowazunguka.

Jambo la msingi ni kwamba yote haya yanatokea kwa sababu tu albino wanaonekana tofauti na sisi. Albinism (kuwa albino) ni ugonjwa unaosababishwa na matatizo katika utengenezaji wa chembe chembe za kutengeneza rangi ya ngozi na kwetu sisi Weusi, badala ya rangi ya mwili (ngozi na nywele) kuwa nyeusi, inakuwa nyeupe. Mboni za macho yao huwa ya rangi ya bluu na yenye shida kuona vizuri kwenye mwanga.

Kwa sababu hii, albino wanahitaji kusogeza kitu karibu sana na macho yao ili waweze kukiona vizuri; wanafunzi wanahitaji kukaa karibu na ubao darasani ili waweze kuona vizuri kinachoandikwa ubaoni.

Kuwa albino, inabidi kurithi vinasaba vya tatizo hili kutoka kwa baba na mama ambao inabidi wote wawe aidha albino au wana vinasaba vya ualbino ili mtoto aweze kurithi vinasaba hivi kutoka kwa wazazi wote wawili. Kama albino ataoa au kuolewa na mtu asiye na vinasaba hivi, watoto watakaozaliwa watarithi vinasaba hivi lakini wataonekana watu wa kawaida kama binadamu yeyote.

Unashauri jamii ifanye nini kukomesha mauaji dhidi ya ndugu zetu hawa albino!!!

Mrejesho wa Mfululizo wa semina za GDSS

Uchambuzi na Maoni ya Wasomaji kwa Machapisho ya: Hali Halisi Ya Kijinsia Tanzania na Tathmini ya Miaka 10 Baada Ya Beijing.

Mjadala huu ulifanyika Jumatano ya tarehe 10/08/08 na uliongozwa na dada Anna Kikwa na uliweza kuibua mambo kadha ya
kufuatilia katika kila eneo ambalo wanasemina walijadiliana. Mjadala uligawanyika katika maeneo makuu matano ambayo ni: Afya na Afya ya Uzazi, Hali ya Kiuchumi, Elimu, Haki na Usawa wa Jinsi na nafasi ya Mtoto wa kike katika vyombo vya habari, uongozi(Maamuzi) na familia, na mwisho Hali ya Utamaduni na Mila.

Wanasemina Walikaa katika makundi matano na kujadiliana juu ya maeneo hayo na kutoa michango mbalimbali ambayo inahitaji ufuatiliaji wa pamoja na wanaharakati wote. Hapa chini nimeanza na baadhi ya michango ya wanasemina katika sekta ya afya, ili kutoa nafasi ya kupata maoni kutoka kwa wadau.

1. Sekta ya Afya

Katika sekta hii wanasemina walijadili kwa ujumla hali ya utoaji wa huduma ya afya katika hospitali za serikali lakini mkazo mkubwa uliwekwa katika afya ya uzazi. Mapaungufu yalionekana katika utekelezaji wa sera ya afya ya uzazi ambayo inampa ruhusa mama mzazi kupata huduma bure kitu ambacho hakitekelezwi. Pili, swala la rushwa limeota mizizi na kuonekana kana kwamba haliwezi kudhibitiwa. Rushwa imesemekana ndio chanzo cha vifo vingi vya akina mama wajazito, hasa wale ambao hawana kipato na waishio maeno ya vijijini. Tatu, Swala la kutoa huduma kwa wagonjwa wa UKIMWI ambalo serikali limelirudisha kwa wananchi, washiriki waliona hatua hii ni kuwaongezea mzigo mkubwa wananchi ambao tayari wamezongwa na umasikini wa kutupa, na ikizingatiwa mzigo huu wa ulezi wa wagonjwa majumbani mara nyingi wanaoachiwa ni akina mama, hivyo ni sawa na kusema swala hili nalo ni nyongeza ya mzigo kwa akina mama.

Washiriki wa semina waliazimia walichukue swala hili la afya ya uzazi na kulifanyia
kazi mpaka hali itakapobadilika na kuboreka. Mbinu kadhaa zimeafikiwa zitumike, ikiwa ni pamoja na; kupiga picha(hata za simu) katika wodi za wazazi na kuzipeleka katika vyombo vya habari, kuandika makala katika magazeti (walau kila wiki makala moja), kushiriki katika vipindi vya runinga na redio(nafasi hiyo ipo ni kuifuatilia tu)

Je mwanaharakati utashiriki vipi katika kampeni hii ya kuleta mabadailiko katika sekta ya afya nhini Tanzania? Au ni upi mchango wako katika kampeni hii ya kuleta mabadiliko katika sekta ya afya hapa Tanzania?

Thursday, September 11, 2008

Adhabu ya kifo na Haki za binadamu

Adhabu ya kifo yaibua mjadala Bungeni miezi michache iliyopita na tumeshuhudia mjadala mkali kuhusu hukumu ya kifo. Baadhi ya wabunge walibishana na serikali kuhusu umuhimu wa kuendeela kuwepo kwa adhabu hiyo.

Wabunge wanataka ifutwe wakiwa na hoja mbili; kwanza wanasema adhabu hiyo haitekelezwi inavyotakiwa hapa nchini na pili wanasema ni adhabu ya kikatili.

Mhe.Kilontsi Mporogonyi yeye amesema kuwa hakuna mwanadamu ambaye anayo mamlaka ya kutoa uhai isipokuwa Mungu pekee, na mwelekeo unaonyesha kuwa nchi nyingi duniani zipo katika mchakato wa kufuta adhabu hii.

Hata hivto mjadala huo haukuendelea sana kwa sababu uliibuka katika kipindi cha maswali na majibu, ambapo mkuna kanuni ambayo inadhibiti idadi ya maswali yanayoulizwa. Kwa maana hiyo walichangia wabunge wawili tu.

Aliyeibua mjadala ni Mbunge wa Mchinga, Mhe.Mudhihiri Mudhihiri, aliyetaka kujua kwa nini adhabu hiyo isifutwe au kubadilishwa na kuwekewa kipimo cha kifungo.

Mudhihiri aliuliza swali hilo baada ya Naibu waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Mathias Chikawe, kujibu swali la msingi lililouklizwa na Mhe.Mudhihiri kwa niaba ya Mhe.Richard Ndassa (Sumve-CCM) akitaka kujua idadi ya watu ambao walishanyongwa katika awamu zote za uongozi na awamu iliyoridhia utekelezwaji wa adhabu hiyo.

Ndassa aliitaka serikali kuleta muswada bungeni, ili kuifuta sheria inayotoa adhabu ya kifo kwa sababu uzoefu unaonyesha kuwa utekelezaji wa hukumu hiyo umekuwa mgumu na mzito hasa kwa mamlaka ya mwisho ya kusaini hati ya kumnyonga mwenye hatia.

Akiongezea katika hilo, Mudhihiri alisema tendo la kuua ni la kikatili na mara nyingi watu wanaohukumiwa kunyonga hadi kufa hawanyongwi hadi kufa kwa sababu hukumu hiyo inachelewa mno kutekelezwa.

Kutokana na hilo, Mhe.Mudhihiri alipendekeza kuwa adhabu ya kunyongwa hadi kufa ingetengenezewa mbadala na kuwa na adhabu ya kifungo, ili mtu atakapohukumiwa kunyongwa afahamu kuwa asiponyongwa baada ya muda huo, anakuwa huru kwa sababu amekamilisha adhabu yake.

Hata hivyo, upande wa serikali ulionekana kutokubaliana na hoja zilizoibuliwa na wabunge hao, huku Mhe.Chikawe akisema kuwa pamoja na kuwa nchi nyingi zinataka kuifuta adhabu hiyo, lakini zipo pia nchi ambazo ziliifuta adhabu hiyo na sasa zinataka kuirejesha.

Akipinga dhana kuwa adhabu hiyo haitekelezwi, Mhe.Chikawe alisema kuwa jumla ya watu 82 wameshanyongwa katika awamu zote nne za utawala tangu nchi ijitawale.

Akifafanua, Mhe.Chikawe alisema kuwa kati ya watu hao, kumi (10) walinyongwa katika awamu ya kwanza ya utawala na 72 walinyongwa katika awamu ya pili. Hakuna mtu aliyenyongwa katika awamu ya tatu na nne.

Hata hivyo, ili kujiridhisha kama bado adhabu hiyo bado ni muafaka kwa wakati huu na iwapo inaendana na matakwa ya haki za Binadamu, Mhe.Chikawe alisema kuwa serikali imepanua wigo wa wananchi kutoa maoni.

Alisema kuwa serikali imeiagiza tume ya kurekebisha sheria kuanza mchakato na hatimaye kutafuta maoni ya wananchi ili kuona kama adhabu hii iendelee kuwepo katika vitabu vya sheria za nchi.

Je wewe unaonaje kuhusu kuwepo au kutokuwepo kwa adhabu hii?

Wednesday, September 10, 2008

Mrejesho wa Mada ya Mjadala Juu ya Hotuba ya Rais na Waziri Mkuu.

Rais na Waziri Mkuu walihutubia taifa tarehe 21 na 29 wakiwa na lengo la kuelezea umma juu ya msimamo wa serikali juu ya maswala ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Wana-GDSS walijadili juu ya hotuba hizo mbili Jumatano ya tarehe 3/09/08, mada ambayo iliongozwa na Geofrey Chambua, huu ni mrejesho mfupi juu ya mjadala huo.

Kwa ufupi, washiriki walikubaliana kuwa hotuba zote mbili hazikukizi matarajio ya wananchi juu ya hatua za serikali za kupambana na ufisadi. Ingawa hatua za mwanzo zilizochukuliwa za kumfukuza gavana wa benki kuu, kurudisha baadhi ya fedha zilizochotwa, kufunga akaunti ya EPA na kuunda tume, bado zinaonekana hazitoshi dhidi ya watuhumiwa wa skendo hizo za ufisadi.

Hotuba zote mbili hazikuonyesha matumaini ya kuwashughulikia watuhumiwa, wananchi walitegemea majina ya watuhumiwa kutajwa pamoja na makampuni yaliyohusika katika skendo hilo tofauti na mbinu za kuchelewesha kuwaadhibu zilizojitokeza katika hotuba hizo.

Baadhi ya washiriki wa GDSS waliona hotuba zinatoa changamoto nyingi za kufuatilia, hivyo imeweza kuwaamsha na imewasaidia kufikiria zaidi juu ya hatua za kuchukua hapo baadae. Baadhi ya hatua hizo ni pamoja na; kufuatilia sheria ya uchaguzi itakayotolewa Januari 2009, kuhakikisha kwamba usawa wa aslimia 50 kwa 50 unafikiwa bungeni, sheria ya maadili ya uongozi inazingatiwa, na fedha za EPA zinazorudishwa zinatumika katika shughuli za kilimo kama zilivyopangwa.

Pia wana-GDSS waliona ni muhimu kwa jamii kuelewa hali iliyopo ili iweze kupitia, kuchanganua, na kutathimini vitu kwa undani na huku ikiendelea kuisimamia na kuishawishi serikali ili iwajibike katika maswala ya jamii yetu.

Je wanaharakati wanawezaje kutumia nafasi yao katika kufikisha taarifa hizi kwa jamii hasa ile inayoishi katka maeneo ya vijijini?

Tuesday, September 9, 2008

TANZIA

BURIANI KAKA KITWANA KASANZU
TANZIA

Mtandao wa Wanaharakati wa Haki za Binadamu na Masuala ya Jinsia (FemAct), tumestushwa sana na msiba wa ghafla wa mwanaharakati mkongwe na shupavu kaka
Kasanzu Kitwana(Pichani),kiongozi wa the African Youth Alliance, kilichotokea ghafla nyumbani kwake siku ya Ijumaa tarehe 5 Agosti 2008, majira ya saa mbili na nusu usiku.

Marehemu pamoja na kuwa mmoja wa Wanachama shupavu wa Mtandao wa Jinsia Ngazi ya Kati Kinondoni (KIGN) na Kiongozi wa The African Youth Alliance, pia alitoa mchango mkubwa sana katika harakati za ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi Vijana na Watoto Tanzania. Kwa kweli huu ni msiba mkubwa sana kwetu kwa sababu tumempoteza mpiganaji shupavu na hodari.

Wakati wa uhai wake marehemu alifanya kazi kwa karibu sana na FemAct katika harakati za kudai haki za Wanawake, Vijana na Watoto na kuhakikisha kwamba usawa na haki zao zinazingatiwa pamoja na sera na mipango madhubuti inapangwa na kuwalinda.

Pia FemAct inakumbuka mchango na ushiriki wake mkubwa katika matukio mbalimbali ikiwemo Matamasha ya FemAct ya Jinsia yanayofanyika kila baada ya miaka miwili (GF) Semina za Jinsia na Maendeleo (GDSS) zinazofanyika kila Jumatano TGNP Mabibo. Na Jumatano ya mwisho kushiriki semina hizi, marehemu Kasanzu alikua ni miongoni mwa washiriki katika uzinduzi wa machapisho ya Hali Halisi ya Kijinsia Tanzania pamoja na tathmini ya Miaka Kumi Baada ya Beijing uliofanyika siku ya tarehe 27 Agosti 2008 katika viwanja vya TGNP.

Tunapenda kuungana na Wanaharakati wote katika kuwapa pole wale wote walioguswa na msiba huu hususan kwa watoto na familia yake, Wanaharakati na Taifa kwa ujumla. Hakika marehemu ameacha pengo kubwa katika mapambano ya harakati nchini, pengo ambalo tunaamini litakuwa ni chachu ya kuendeleza Mapambano ya kudai haki za binadamu na Ukombozi wa wanawake wote. Tunapenda kutumia fursa hii pia kutoa mwito kwa Wanaharakati wote tuendeleze utamaduni wa kuwaenzi wanaharakati wenzetu wanapofikwa na mauti kama ishara ya kutambua mchango wao katika mapambano ya harakati nchini

Mwenyezi Mungu ailaze roho ya kaka Kitwana Kasanzu mahali pema peponi.
Imetolewa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa niaba ya FemAct.

Imesainiwa na Sekretariat ya FemAct,

Usu Mallya, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)
Mratibu
Mtandao wa Wanaharakati wa Haki za Binadamu na Masuala ya Jinsia (FemAct),
Tarehe 9, Septemba 2008

Friday, September 5, 2008

Semina za Maendeleo na Jinsia (GDSS)

Semina za Maendeleo na Jinsia (GDSS)

Unakaribishwa katika mfululizo wa semina za kila wiki ambapo wiki hii Gemma Akilimali wa TGNP atawezesha kuhusu:

Uchambuzi na Maoni ya Wasomaji kwa Machapisho ya:

Hali Halisi Ya Kijinsia Tanzania na Tathmini ya Miaka 10 Baada Ya Beijing

LINI: Jumatano 10 /9/2008
Muda: Saa 9:00 – 11:00 Jioni

MAHALI: Viwanja vya TGNP, Barabara ya Mabibo Karibu Na Chuo Taifa Chuo cha Usafirishaji Mabibo Sokoni

WOTE MNAKARIBISHWA!

Michango iliyojitokeza katika Uzinduzi wa Kitabu cha Hali Halisi ya Jinsia Tanzania

Kaka Badi Darusi (Pichani) alichangia juu ya afya ya uzazi, na aligusia juu ya kulega-kulega kwa hali ya utoaji wa huduma hii kwa wazazi ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa kwa vifo vya akina mama hapa Tanzania. Mchangiaji alitolea mfano Hospitali ya Mwananyamala kwa kuhusika mara kwa mara kwa vifo vya wazazi na kutaka hali hii ikomeshwe na serikali kwani ni jambo ambalo kama serikali ikiamua kulitatua inaweza kufanya hivyo.
Wadau mnasamaje juu ya ubora wa afya ya uzazi? Ipo juhudi yoyote ambayo serikali imeonyesha katika kuboresha hali hii? Je Wanaharakati wanaweza kufanya nini ili kuleta mabadiliko na kuboresha hali hii?

Tuesday, September 2, 2008

FEMACT YATOA MAONI KUHUSU HOTUBA YA RAIS BUNGENI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Sisi wanamtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali yapatayo 50 yanayotetea usawa wa jinsia, haki za binadamu na ukombozi wa wanawake kimapinduzi (FemAct) tunatambua umuhimu wa hatua ya Rais Jakaya Kikwete kuhutubia bunge mnamo tarehe 21 Agosti 2008 na kutoleaa kauli masuala kadhaa mazito yanayohusu mustakabali wa taifa letu ambayo kwa muda sasa yamekuwa yakijadiliwa na wananchi. Moja ya masuala hayo ni lile la wizi wa zaidi ya shilingi bilioni 133 kutoka Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) iliyokuwa katika Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

Rais alisema tayari shilingi bilioni 53 kati ya shilingi bilioni 133 zilizoibwa zimesharejeshwa na kwamba alikuwa amewapa muda hadi Oktoba 31 mwaka huu (2008) wale wote ambao hawajarejesha fedha walizoiba wawe wamezirejesha vinginevyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao. Kadhalika Rais aliliambia bunge kuwa watu waliobainika kuiba fedha hizo kutoka akaunti ya EPA Benki Kuu wamefilisiwa na pia kunyang’anywa pasi zao za kusafiria.

Sisi FemAct tunaamini kuwa mafisadi wa EPA ni watu hatari walioifilisi nchi yetu. Kwa hiyo tunamshauri Rais abadilishe uamuzi wake wa kuwasamehe mafisadi hao badala yake aachie sheria ichukue mkondo wake. Tunaona kuwa kitendo cha mafisadi hao kusamehewa kabla ya sheria kuchukua mkondo wake kutafifisha vita dhidi ya ufisadi ikiwa ni pamoja na wizi wa mali ya umma na hivyo kuchafua heshima ya serikali na taifa kwa ujumla. Hakika mahali popote duniani ambapo vita dhidi ya rushwa na wizi wa mali ya umma vimefanikiwa ni pale tu ambapo kumekuwa na uwazi dhidi ya uovu huo.

Aidha Rais anapaswa pia autangazie umma majina ya maafisa wa BOT waliohusika na EPA ambao watakuwa wamechukuliwa hatua na uongozi wa benki hiyo. Kutowataja watu hao na kuchukuliwa hatua za kisheria kutawafanya maafisa wengine wa serikali wenye tabia ya kushiriki kukwapua mali za umma kuendeleza wizi wa mali ya umma kwa kasi. Sisi FEMACT tunaamini kabisa kuwa kashfa hii ya EPA ni fursa nzuri kwa Rais kuudhihirishia umma kwamba yuko tayari kupambana na mafisadi wanaoiba mali ya umma.

Tunahofu kwamba kama mafisadi wa EPA hawatashtakiwa huenda ikawa ni mwanzo wa nchi yetu kujenga matabaka ya wazi ya watu walio juu ya sheria na wengine walio chini ya sheria. Wakati wa uhai wake Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kuonya kwamba kuwaonea huruma watu dhalimu hujenga taifa lenye tabaka jambo ambalo ni hatari kwa amani ya taifa. Katika kuhimiza kuwa wadhalimu wasipewe nafasi katika taifa letu Mwalimu alisema “Wadhalimu muda wote lazima waandamwe hata kama wangekuwa wakubwa kama Mlima Kilimanjaro”.

FemAct tunaona ni muhimu pia kutafakari ni nini hasa athari za wizi wa fedha hizo nyingi bilioni 133 kwa maisha ya Mtanzania wa kawaida hawa wanawake na makundi mengine katika jamii? Kwa mfano kila siku wanawake zaidi ya 24 wanakufa hapa nchini wakati wa kujifungua kutokana na kukosa fedha za kununulia vifaa muhimu vya kumsaidia visivyozidi shilingi elfu kumi tu na ambavyo vingepaswa kutolewa bure na serikali kama huduma ya afya ya msingi. Fedha hizo zilizoibwa kwenye EPA zingetosha kuepusha vifo vya uzazi kwa wanawake zaidi ya milioni 13 na laki tatu na hivyo kuimarisha nguvu kazi muhimu ya maendeleo ya familia na taifa kwa ujumla. Aidha tunapaswa tujiulize je fedha hizo zilizoibiwa zisingeweza kutosheleza kutoa mafunzo kwenye sekta ya afya na hivyo kupata maelefu ya madaktari na wauguzi ambao wangeokoa maisha ya wananchi wengi wanaokufa hasa vijijini kwa kukosa huduma za tiba? Je zisingetosheleza kujenga mabweni mengi kwa shule za sekondari za serikali na kuepusha adha wanazopata watoto wa kike kutokana na kukosekana kwa mabweni? Je zisingetosha kujenga maabara, maktaba na kununulia vitabu kwa ajili ya shule zote za sekondari zinazohitaji huduma hizo?

Rais aliseme fedha zinazorejeshwa na wezi hao zitatumika katika kuongeza ruzuku ya mbolea na dawa za mifugo na nyingine zitawekwa katika Benki ya Rasilimali (TIB) ili wakulima wakopeshwe mikopo yenye masharti nafuu na ya muda mrefu. Sisi FEMACT, hatupingi fedha hizo kuelekezwa kwa wakulima na wafugaji, kwa sababu tunatambua kuwa Watanzania wengi hasa wanawake na makundi mengine ya jamii yaliyopo pembezoni kiuchumi wako kwenye sekta ya kilimo na ufugaji. Lakini suala la msingi ni kuhakikisha usimamizi mzuri wa mgawanyo wa hiyo rasilimali na uwajibikaji. Tunaamini kuwa bunge ndicho chombo pekee kwa niaba ya Watanzania chenye mamlaka ya kuidhinisha matumizi ya fedha za umma na kufuatilia matumizi yake. Tunaona hatari ya fedha hizo kutowafikia walengwa kama hazitagawiwa na chombo chenye mamlaka ya kusimamia rasilimali za taifa. Aidha tunaona hatari ya kuweka fedha hizo TIB kwa sababu kama mafisadi waliweza kupenyeza na kuiba kwenye akaunti ya EPA iliyokuwa kwenye chombo nyeti kama Benki Kuu, watashindwaje kuingia Benki ya Rasilimali na kuiba tena fedha nyingine ili kukidhi matakwa yao?

Usu Mallya, TGNP
Mratibu
Mtandao wa wanaharakati wa Masuala ya Jinsia, Haki za Binadamu na Ukombozi wa wanawake (FemAct)
27th August, 2008

Monday, September 1, 2008

Michango iliyojitokeza Katika Uzinduzi wa kitabu cha Hali Halisi ya Jinsia Tanzania

Mchangiaji kaka Hashim S Luanda (Pichani) alichangia juu ya Ubora wa Elimu Tanzania na hasa juu ya hizi shule mpya za Kata zilizoanzishwa hivi karibuni na serikali. Mchangiaji aligusia ubora wa elimu inayotolewa na shule hizi kwa kuanglia ubora wa waalimu
wanaofundisha katika shule hizi- maarufu kama walimu wa yebo-yebo au Vodafaster kwa sababu ya maandalizi yao ya haraka haraka. Pili aligusi juu ya upatikanaji wa vitabu na dhaan zingine za kujifunzia, pamoja na mazingira ambapo shule hizi zinapatikana.
Je shule hizi za kata zinaweza kuleta maendeleo ya elimu yalikusudiwa? Wadau mnaonaje? Nini kifanyike kuboresha mazingira ya elimu katika shule hizi za kata?