Monday, June 15, 2009

Serikali yajitwisha mzigo bajeti mpya

BAJETI ya serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 iliyopangwa kugharimu Sh trilioni 9.5 ikilinganishwa na bajeti iliyopita ya Sh trilioni 7.3, imeelezwa kuwa mzigo mzito zaidi kwa serikali kutokana na kubebeshwa vipaumbele vingi zaidi ya uwezo halisi wa kiuchumi.

Bajeti hiyo ambayo itasomwa na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, imebebeshwa vipaumbele sita. Kuna maoni kwamba bajeti hiyo na hasa uchumi halisi wa nchi hauna uwezo wa kumudu kutekeleza kwa ufanisi idadi hiyo ya vipaumbele kwa wakati mwafaka.

Baadhi ya wabunge wametoa maoni tofauti na mmojawapo ameonya kuwa, uchumi ni mdogo na haumudu idadi kubwa ya vipaumbele na kwamba unaweza tu kumudu kutekeleza kwa kiwango cha juu cha ufanisi vipaumbele kama vitatu.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na Raia Mwema wiki hii, Mbunge wa Ulanga Magharibi (CCM) na aliyepata kuwa Waziri wa Uchumi, Mipango na Uwezeshaji katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Dk. Juma Ngasongwa anaamini kwamba uchumi wa Tanzania, na hasa baada ya mtikisiko wa uchumi wa dunia, unamudu vipaumbele viwili hadi vitatu tu, na si zaidi ya hapo.

Dk. Ngasongwa, ambaye alishiriki kuandaa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2005, anasema katika mahojiano hayo, yaliyochapishwa katika kurasa za katikati za toleo hili, kuwa kwa uchumi wa Tanzania kubebeshwa vipaumbele zaidi ya vitatu hakutaweza kutoa matokeo ya wazi ya juhudi za Serikali katika sekta muhimu.

Kwa mujibu wa Dk. Ngasongwa, ambaye pia alishiriki kuandaa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000, kuweka vipaumbele vingi katika bajeti kunatokana na kuwapo kwa mahitaji mengi nchini.

‘‘Najua kwa nini watu wanaamua hivyo. Wanaamua hivyo kwa sababu mahitaji yako mengi. Lakini mahitaji ya binadamu hayawezi yote yakatekelezwa kwa wakati mmoja na ndiyo maana ya msingi wa vipaumbele. Mkishakuwa na vipaumbele zaidi ya vinne mna matatizo, si vipaumbele tena hapo.

Soma zaidi

No comments: