Tuesday, November 22, 2011

Tamko La Kamati Kuu Ya CHADEMA Juu Ya Muswada Wa Katiba


CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

MAAMUZI YA KAMATI KUU YA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA) KUHUSU MCHAKATO WA KATIBA MPYA.

Kamati Kuu ya CHADEMA katika kikao chake maalum kilichofanyika siku ya Jumapili, tarehe 20 Novemba 2011 katika Ukumbi wa Hoteli ya Mbezi Garden, Dar es Salaam, pamoja na mambo mengine, kimepokea na kujadili kwa kina taarifa ya majadiliano na kupitishwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011. Aidha, Kamati Kuu imejadili kwa kina hatua za kuchukua baada ya Serikali, kupitia wabunge wa CCM, kulazimisha kupitishwa bungeni kwa Sheria hiyo bila kuzingatia maoni ya Wananchi na wadau wengine mbalimbali. Baada ya kuyatafakari mambo haya kwa kina, Kamati Kuu imeazimia yafuatayo:

1. Kamati Kuu imewapongeza wabunge wote wa CHADEMA kwa hatua thabiti na sahihi walizochukua, kwa niaba ya wananchi wa Tanzania, kupinga Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 kusomwa kwa mara ya pili na kujadiliwa Bungeni bila ya wananchi kushirikishwa kwa ukamilifu kutoa maoni yao na muswada kuboreshwa kwa kuzingatia muafaka wa kitaifa. Kamati Kuu imewapongeza wabunge wa CHADEMA na wale NCCR Mageuzi kwa kususia vikao vya Bunge vilivyojadili na kupitisha Sheria hiyo kwani kushiriki kwao kungeipa uhalali wa kisiasa na kijamii Sheria ambayo haikuzingatia nia na haja ya dhati ya kuweka utaratibu wa kisheria utakaoiwezesha nchi yetu kupata Katiba Mpya yenye kuzingatia na kukidhi matakwa ya umma wa Watanzania;

2. Kamati Kuu imezingatia kuwa Sheria iliyopitishwa na Bunge ina mapungufu mengi na ya kimsingi ambayo hayatajenga muafaka wa kitaifa juu ya Katiba Mpya na hayataleta mabadiliko yoyote ya kimsingi ya Katiba:

a) Mchakato wa kuipitisha Sheria ndani ya Bunge ulikiuka Kanuni za Kudumu za Bunge kwani Muswada uliosomwa mara ya kwanza Bungeni sio ulioletwa Bungeni kusomwa mara ya pili na baadae kupitishwa; Kamati ilizuiliwa kukusanya maoni ya wananchi katika mikoa na maeneo mbali mbali; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano aliingilia kazi na majukumu ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ikiwa ni pamoja na yeye mwenyewe na baadhi ya wajumbe wa CCM kukusanya maoni nje ya utaratibu wa Kamati na baadae kuingiza wajumbe wengine wa CCM na CUF kwa lengo la kupitisha matakwa ya CCM na Serikali ndani ya Kamati bila kuushirikisha wananchi kwa ukamilifu;

b) Sheria inampa Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi mamlaka makubwa ya kuunda Tume ya Katiba na Sekretarieti yake ambayo sio tu itakusanya maoni ya wananchi na kuandaa ripoti, bali pia ndiyo itakayoandaa na kuandika Rasimu ya Katiba Mpya na kusimamia mchakato wote wa wananchi kuijadili na kuipitisha katika Bunge la Katiba;

c) Sheria inampa Rais na Mwenyekiti wa CCM mamlaka makubwa sio tu ya kupokea ripoti ya Tume ya Katiba bali pia ya kuifanyia mabadiliko ambayo yeye na Serikali yake wataona yanafaa kwa kutumia taratibu za kiserikali za kutunga sheria;

d) Sheria inampa Rais na Mwenyekiti wa CCM mamlaka makubwa ya kuliitisha tena Bunge la Katiba kwa lengo la kufanya mabadiliko kwenye Katiba Mpya endapo litapitisha Katiba Mpya ambayo yeye Rais, au Serikali yake, au chama chake wataona hailindi maslahi yao;

e) Sheria inaunda Bunge la Katiba ambalo litakuwa na Wajumbe hadi 400 wa CCM kati ya wajumbe 545 wa Bunge la Katiba. Idadi hii ya wajumbe itaiwezesha CCM kupata theluthi mbili ya wajumbe wanaohitajika chini ya Sheria hii ili kupitisha jambo lolote katika Bunge la Katiba na kwa hiyo Katiba Mpya itakuwa ni ile inayolingana na matakwa na maslahi ya CCM na itakuwa mpya kwa jina tu;

f) Sheria inatoa nafasi kubwa kwa Rais wa Zanzibar na Makamu Mwenyekiti wa CCM na vyombo vya uwakilishi vya Zanzibar kushiriki kutunga Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano ya mwaka 1964 na Katiba ya sasa ambayo imevipa mamlaka ya kutunga Katiba ya Jamhuri ya Muungano vyombo vya Muungano kama Serikali na Bunge ambako Zanzibar ina uwakilishi wa kutosha;

g) Sheria inahakikisha kwamba muundo wa sasa wa Muungano wa Serikali hautaguswa bali utadumishwa na kutiliwa nguvu licha ya madai ya miaka mingi ya wananchi na mapendekezo ya Tume za Kiserikali kwamba muundo wa Muungano uwe ni wa Serikali tatu;

h) Sheria inaipa Tume ya Taifa ya Uchaguzi iliyoteuliwa na Rais na Mwenyekiti wa CCM mamlaka ya kusimamia mchakato mzima wa kura ya maoni ya kuipa Katiba Mpya uhai wa kisheria. Tume ya Taifa ya Uchaguzi haina uhuru na imeshindwa mara nyingi kusimamia chaguzi huru na haki katika nchi yetu na haiwezi kusimamia kura ya maoni kwa uhuru unaohitajika;

3. Kamati Kuu ya CHADEMA imesisitiza siku zote kwamba mchakato wa kupata Katiba Mpya unahitaji mwafaka wa kitaifa ambao utazingatia maoni mapana ya makundi mbalimbali ya kijamii. Kamati Kuu inasikitishwa na hatua za makusudi za kufifisha juhudi zote zilizofanyika na wadau mbalimbali katika kufikia mwafaka wa kitaifa juu ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Aidha, Kamati Kuu imesikitishwa na upotoshaji wa makusudi wa hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni uliofanywa na wabunge wa CCM na CUF, wakiongozwa na Spika wa Bunge, Anna Makinda, kuhusu msimamo wa CHADEMA juu ya Muungano;

4. Kamati Kuu inasisitiza kwamba njia pekee ya kuunusuru Muungano wetu ni kwa wananchi wa pande zote mbili kupiga kura ya maoni kuamua kwamba wanataka kuendelea na Muungano na kama jibu ni ndio, muundo gani wa Muungano huo wanaoutaka. Aidha, Kamati Kuu inarudia msimamo wa CHADEMA kwamba ili kuondoa kero na malalamiko ambayo yameuandama Muungano wetu tangu kuzaliwa kwake, muundo unaofaa ni wa Serikali tatu kama ilivyopendekezwa pia na Tume ya Nyalali mwaka 1991 na Tume ya Kisanga mwaka 1998;

5. Kamati Kuu inaamini kuwa pamoja na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kupitishwa, bado kuna fursa za kisiasa na kijamii katika kujenga mwafaka wa kitaifa juu ya haja, nia, mchakato na misingi ya Katiba Mpya. Hata hivyo, Kamati Kuu imeshangazwa na kusikitishwa na uamuzi wa Rais Jakaya Kikwete wa kutozitumia fursa hizo na badala yake kujiingiza katika jalala la taka za upotoshaji uliofanywa na Wabunge wa chama chake juu ya misingi na maudhui ya Sheria hiyo. Kamati Kuu inaamini kwamba badala ya kuwaunganisha Watanzania na kujenga muafaka unaohitajika katika mchakato wa Katiba Mpya, hotuba ya Rais Kikwete kwa wazee wa CCM wa Dar es Salaam imezidi kuwagawa Watanzania kwa misingi ya ushabiki wa vyama badala ya kuwaunganisha kwa misingi ya utaifa;

6. Baada ya kutafakuri mambo yote haya, Kamati Kuu imeazimia yafuatayo:

a) CHADEMA itaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau wote juu ya ubovu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na juu ya haja ya kuwa na sheria itakayoweka utaratibu bora zaidi wa kuunda Tume Shirikishi ya Katiba kwa lengo la kukusanya maoni ya wananchi, kuandaa ripoti na Rasimu ya Katiba Mpya, Bunge Maalum la Katiba na usimamizi wa kura ya maoni itakayowezesha wananchi kufanya maamuzi kwa uhuru na kwa haki;

b) Ushiriki wa CHADEMA katika mchakato mzima wa kupata Katiba Mpya uliowekwa na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba utategemea utayari wa Serikali ya Rais Kikwete kufanya mabadiliko makubwa na ya kimsingi katika sheria hiyo kwa lengo la kujenga muafaka wa kitaifa juu ya mchakato huo;

7. Kamati Kuu inawaagiza wabunge na viongozi wote wa chama katika ngazi zote kufanya mikutano ya ndani na ya hadhara yenye lengo la kuwaelimisha wananchi juu ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na madhara yake kwa mchakato wa kupata Katiba Mpya na bora kwa nchi yetu kwa lengo la kuunganisha umma wa watanzania kuweza kufanya mabadiliko ya msingi;

8. Kamati Kuu inaamini kwamba uamuzi wa Serikali ya CCM kulitumia Jeshi la Polisi kuzuia mikutano ya hadhara na maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga mchakato uliopitishwa kuwa Sheria sio tu ni kwenda kinyume na haki za kimsingi za kikatiba bali pia unahatarisha moja kwa moja amani, utulivu na umoja wa nchi yetu. Kamati Kuu inasikitishwa na msimamo huu wa Serikali ya CCM kwani unashindwa kutambua ukweli kuwa matumizi ya nguvu za dola hayajawahi kuokoa serikali za kidikteta kuondolewa madarakani na Katiba Mpya kupatikana katika nchi mbali mbali duniani na katika Bara la Afrika;

9. Kamati Kuu inasisitiza kwamba CHADEMA itaendelea kutumia njia zote za amani, ikiwemo mikutano ya hadhara na maandamano kama ilivyoainishwa na Katiba na sheria husika za nchi yetu kuunganisha nguvu ya umma kupinga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na mchakato wake utakaopelekea Tanzania kutopata Katiba Mpya na bora;

.............................................................................................

Freeman A. Mbowe (MB)

MWENYEKITI WA TAIFA

Novemba 21, 2011

1 comment:

Kichulungu said...

Nahitaji kuwa mwanaharakati wa CHADEMA,NIFANYEJE?