Monday, August 31, 2009

Zitto: Demokrasia Chadema imenisaliti

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Kabwe Zitto, amesema hofu ya demokrasia waliyokuwa nayo wazee wa chama hicho, imemlazimisha kujiondoa katika kuwania nafasi ya uenyekiti wa chama hicho japokuwa anao uhakika kuwa kama angegombea, angeshinda.

Sanjari na hilo, mwanasiasa huyo kijana pia amesema kwa kuwa nia yake ilikuwa kugombea nafasi ya uenyekiti wa chama hicho na kulazimika kuchukua uamuzi huo mzito juzi kinyume na matarajio ya waliomshawishi, sasa hahitaji kuwania nafasi yoyote katika chama hicho na atabaki kuwa mjumbe wa Kamati Kuu kama Katibu wa wabunge wa chama hicho.

Akiwasiliana kwa ujumbe mfupi wa simu na gazeti hili jana Mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini alikiri kuwasilisha barua ya kuondoa jina lake na kuongeza kuwa chama hicho ni kikubwa zaidi kuliko yeye. Zitto alisema ametoa jina hilo baada ya kuombwa na wazee wa chama hicho ambao wamedai kuwa wanaogopa demokrasia ikifuatwa itazaa makundi ndani ya chama hicho.

“Ni kweli, wazee wa chama wameomba hivyo, chama ni kikubwa zaidi ya Zitto kwa ajili ya umoja na mshikamano, nimetoa jina na wazee wamesema tukichagua kidemokrasia chama kitapasuka, nikubali kujitoa,” alisema Zitto.

Mbunge huyo alisema uamuzi wake huo ni kuheshimu ushauri huo wa wazee na kwamba hana mpango wowote wa kuwania nafasi nyingine ndani ya chama hicho ila ataendelea kuwa mjumbe wa Kamati Kuu kama Katibu wa wabunge wa chama hicho.

Hivi karibuni Mbunge huyo alikaririwa na vyombo mbalimbali vya habari akielezea msimamo wake kuwa hatojitoa katika kinyang’anyiro hicho na kwamba hakutumwa na mtu kuwania nafasi hiyo ili kukivuruga chama.

Hata hivyo katika kikao cha wazee wa chama hicho ambacho waliitwa wagombea wote wa nafasi hiyo akiwamo Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe, ilidaiwa kuwa wazee hao walimtaka Zitto ajitoe jambo ambalo hata hivyo baada ya kikao hicho hakutaka kulizungumzia.

Katibu Mkuu wa chama hicho Dk. Wilbroad Slaa alikaririwa akikiri kupokea barua ya Zitto ya kutaka kuondolewa kwa jina lake ambapo ndani ya barua hiyo alitoa sababu kuwa aliamua hivyo ili kuendeleza mshikamano ndani ya chama chake.

Akitoa maoni kuhusu hatua hiyo ya Zitto, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, na Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), alisema alitarajia mwanasiasa huyo asingefika mbali kwa ‘mbio’ zake hizo za kuwania nafasi hiyo. Mohamed alitoa sababu mbili zilizosababisha yeye kuwa na matarajio hayo kuwa kwa jinsi ‘alivyomsoma’ Zitto, aligundua kuwa hana uwezo wa kuhimili shinikizo la wazee wa chama hicho.

Sababu ya pili alisema mwanasiasa huyo wa Chadema, alionesha kutojiamini tangu mwanzoni na alikuwa akisitasita kugombea. Kiongozi huyo wa Kambi ya Upinzani Bungeni alisema, katika matarajio yake alikuwa haamini kama Zitto angerudisha fomu na kwamba baada ya kurudisha alitarajia kuwa asingefika mbali na nia yake hiyo.

Alisema pamoja na hatua hiyo, CUF itaendelea kufanya kazi na uongozi wowote wa Chadema utakaochaguliwa baada ya uchaguzi mkuu wa chama hicho utakaofanyika mwishoni mwa wiki hii.

Kwa upande wa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, George Mkuchika, alisema yeye hawezi kujiingiza katika siasa za Chadema kwa kuwa kila chama kinazo taratibu zake na kufafanua kuwa CCM inawaachia Chadema waendeshe chama chao kama wanavyotaka.

1 comment:

Anonymous said...

I'm extremely impressed with your writing skills and also with the layout on your weblog. Is this a paid theme or did you modify it yourself? Either way keep up the nice quality writing, it is rare to see a great blog like this one today.

Here is my web blog diets that work