Thursday, August 6, 2009

Uchumi wa Tanzania kuimarika mwakani

BENKI Kuu ya Tanzania (BoT), imesema hadi mapema mwakani uchumi wa nchi utakuwa umeimarika baada ya kutikiswa na msukosuko wa kifedha duniani na mfumuko wa bei.

Mchumi wa BoT, Mwigulu Mchemba, aliiambia HabariLeo jana katika viwanja vya Nane Nane Nzuguni mjini hapa, kuwa hivi sasa hali ya mfuko wa bei nchini imepungua ikilinganishwa na ilivyokuwa katika robo ya mwaka uliopita.

Mwigulu alisema mfumuko wa bei katika kipindi hicho ulisababishwa na mambo mengi ukiwamo ukame ambao ulisababisha uhaba wa chakula katika ukanda wa Afrika Mashariki na kupanda kwa bei ya mafuta duniani.

Alisema BoT imejitahidi kukabiliana na changamoto na kuongeza kuwa matarajio ya sasa ni kuhakikisha kuwa mfumuko unashuka na thamani ya sarafu itaimarika kutokana na kuimarika kwa ubadilishaji wa fedha za kigeni.

Aidha, alisema kuimarika kwa thamani ya sarafu nchini, kutaanza katika msimu wa kuanzia Julai mwaka huu ambapo mazao ya biashara yameanza kuvunwa na kuuzwa. Alisema pia katika kipindi hiki cha mwaka mpya wa fedha wafadhili kutoka nje wamekuwa wakitekeleza ahadi zao za kutoa fedha.

Kuhusu mtikisiko wa uchumi nchini, mchumi huyo aliwatoa wasiwasi Watanzania na kuongeza kuwa tayari hatua za kukabiliana na mtikisiko huo zimeshachukuliwa.

Alizitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na BoT kulegeza sera ya kifedha, ili kuruhusu upatikanaji wa mikopo katika sekta binafsi na kulegeza sera ya mapato na matumizi ya serikali, ili iweze kutekeleza miradi yake ikiwamo ya barabara na maji. Alisema hali ya uchumi nchini hivi sasa ni nzuri na kuwa Watanzania wasiwe na wasiwasi juu ya uchumi wa nchi.

No comments: