Tuesday, August 11, 2009

Vijana walapo na vigogo mafisadi huisaliti jamii

WAKATI jamii ikiendelea kusukwa sukwa na mawimbi ya bahari iliyochafuka kutokana na ukinzani wa kitabaka, uonevu na ukandamizaji, vijana wa Tanzania nao sasa wanaona kumekucha kudai nafasi za uongozi wakisema wamepuuzwa na kunyanyaswa vya kutosha kwa kuitwa "Taifa la Kesho".

Lakini, pamoja na kujitambua hivyo, hawasemi wataitulizaje bahari iliyochafuka na ni vipi wataiongoza salama meli ya matumaini iliyo mikononi mwa manahodha wakongwe, bila kuzua mtafaruku.

Wakati nchi ikienda kombo kwa kukosa dira, uzalendo kuporomoka, maadili ya taifa kuyoyoma, ufisadi na rushwa kukithiri kwa kukingiwa kifua na vigogo wa Chama na Serikali; vijana wa leo ambao "sasa na kesho" yao inaangamizwa, wamekosa ubavu wa kutahadharisha; badala yake wameungana na wakongwe hao kama washika vipeperushi na mikoba ya vigogo wakati wa chaguzi za kuweka viongozi madarakani. Kama wamejiunga na uozo huu wa tabaka la machweo, nini maana sasa ya wao kudai madaraka?

Wakati nchi ikiangamia kwa kukosa sera makini, uwekezaji usiojali na uporaji wa rasilimali za taifa unaofanywa na wageni kwa kushirikiana na baadhi ya "vigogo" madarakani, na udini na ubaguzi wa kitabaka kutishia amani na utulivu nchini, vijana wamejenga tabia ya mbuni kwa kujivika taji la ukada wa vyama vya siasa, wakijiliwaza kwamba yote yanayotokea ni asali tamu. Je, vijana wa leo wamepeleka wapi ujasiri wa miaka ya 1960 na 1970, wasiweze kulaani maovu katika jamii?

Tusidanganyike, vijana wa leo wametupa zana zao za vita ya kujenga na kulinda taifa, na badala yake wamejiunga na uozo unaoangamiza jamii kwa matarajio ya kuokota ganda la muwa la jana; wakidhani kuwa hiyo ndiyo pepo inayowangojea, kana kwamba wanajiandaa kuishi ughaibuni, na kwamba hapa sio kwao.

Kama kuna mfano bora wa kuigwa na vijana, kuonyesha nguvu na nafasi yao katika kuleta mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na kijamii nchini dhidi ya uozo wa wakongwe wenye kuangamiza nchi; basi, mfano huo ni ule mgomo wa vijana wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Oktoba 1966.

Kwa manufaa ya vijana wa leo nitauelezea mgomo huo, chimbuko lake, ulivyofanyika na jinsi ulivyobadilisha uwanja wa siasa na maisha ya Watanzania pamoja na fundisho tunalopata. Mmoja wa viongozi wa mgomo huo ni Spika wa sasa wa Bunge la Tanzania, Mheshimiwa Samwel Sitta, ambaye umakini wake katika kuliongoza Bunge ni kielelezo tosha jinsi vijana wa zamani walivyopikika wakaiva, ikilinganishwa na vijana wa leo.

Februari 1966 Serikali ilichapisha Muswada kwa madhumuni ya kuanzisha Programu ya Jeshi la Kujenga Taifa [JKT] kwa lazima kwa vijana wote waliomaliza elimu ya Kidato cha Sita na Vyuo vya Elimu ya Juu kikiwamo Chuo Kikuu pekee cha Dar es Salaam.

Mpango huo, ulioendeshwa na kusimamiwa na wakufunzi wa kijeshi kutoka Israeli, uliwataka vijana kutumikia JKT kwa miaka miwili ambapo miezi sita ilikuwa kwa mafunzo ya kijeshi kambini na miezi 18 ya kutumikia Jeshi nje ya kambi kama watumishi wa umma, na kukatwa asilimia 60 ya mshahara kama mchango kwa taifa.

Soma zidi

No comments: