Friday, August 21, 2009

Shahidi kesi ya EPA aeleza akaunti ‘ilivyochakazwa’

SHAHIDI wa kwanza katika kesi ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu zaidi ya Sh bilioni tatu za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu Tanzania (BoT) inayomkabili mfanyabiashara Shaaban Maranda na wenzake watano, jana aliieleza mahakama kuwa akaunti ya Mibale Farm iliyoko katika Bank of Africa (BOA), iliyokuwa na fedha hizo, ilichotwa yote ndani ya siku tisa.

Shahidi huyo, Meneja wa Operesheni wa Benki hiyo, Ronald Msafiri (50), alidai katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa Wakurugenzi wa Kampuni ya Mibale Farm ambao ni mshitakiwa Farijala Hussein na Kiza Selemani ambaye si mshitakiwa katika kesi hiyo, walikuwa wakichota fedha hizo katika tarehe tofauti Novemba 2005 huku wakidaiwa kuingiza Sh 60,000 tu katika akaunti hiyo.

Akiongozwa na Mwendesha Mashitaka Stanslaus Boniface, Msafiri alidai Selemani pamoja mshitakiwa huyo walifunguliwa akaunti ya pamoja kwa jina la biashara la Mibale Farm katika benki hiyo Septemba 12, 2005 baada ya kukamilisha taratibu zote zinazotakiwa katika benki hiyo.

Alidai kuwa Novemba 3, 2005 benki hiyo ilipokea ujumbe kutoka BoT ikieleza kwamba akaunti ya benki hiyo iliyoko BoT imeingiziwa fedha Sh bilioni 3.8 inayotakiwa kuingizwa kwenye akaunti ya Mibale Farm na pia benki hiyo ilipokea nakala ya barua iliyotumwa kwa kampuni hiyo iliyotoka BoT.

Novemba 7, 2005 wabia hao waliomba kuandikiwa na benki hundi ya Sh milioni 580 ambayo benki hiyo iliwaandikia na kutolewa yenye namba 029498; siku hiyo hiyo waliomba hundi nyingine ya Sh milioni 460 na kutoa fedha taslimu Sh milioni 250. Alidai Novemba 8, 2005 waliomba hundi yenye thamani ya Sh milioni 16.5, na kutoa taslimu fedha Sh milioni 1.4 na kuchukua tena Sh milioni 100.

Alidai Novemba 9, 2005, Selemani na Hussein walituma fedha kwa njia ya telegramu Sh milioni 5.7 iliyokuwa imeandikwa kwenda India kwenye Kampuni ya Lakshmi Textile Mills.

Siku hiyo hiyo, walituma tena Sh milioni 394 na kuchukua fedha taslimu Sh milioni 7. Novemba 10, 2005 walituma tena katika kampuni hiyo ya India Sh milioni 465.6 na kutoa tena tofauti Sh milioni nne na Sh milioni 50.

Mbali ya kuchukua fedha hizo, katika tarehe tofauti walichukua fedha nyingine na waliweka Sh 50,000 Novemba 23, 2005 na Sh 10,000 Desemba 3, mwaka huu, na baada ya hapo, hakukuwa na shughuli yoyote ya kibenki waliyoifanya wabia hao katika benki hiyo.

Baada ya kuona akaunti hiyo haitumiwi tena kwa kipindi kirefu, shahidi huyo alisema benki hiyo iliandika barua kwa wahusika kuwataka kutumia akaunti hiyo. Alidai hawakupata majibu yoyote na ndipo walipoamua kuifunga akaunti Mei 22, 2006 na inadaiwa Sh 77,356.21 za makato ya kibenki.

Watuhumiwa mbali na Farijala ni Rajab Maranda, maofisa wa BoT, Iman Mwakosya, Ester Komu na Sophia Larika, wanaokabiliwa na mashitaka ya kujipatia malipo isivyo halali. Kesi hiyo inaendelea leo.

No comments: