Monday, August 24, 2009

Wanafunzi 12 wateketea kwa moto bwenini

Wanafunzi 12 wa Shule ya Sekondari ya Idodi inayomilikiwa na serikali, iliyopo Tarafa ya Idodi, Iringa Vijijini mkoani Iringa, wamefariki na kuteketea kabisa kwa moto baada ya bweni walimokuwa wamelala kuangamizwa kwa moto.

Wanafunzi hao ambao ni wasichana, wamepoteza maisha usiku wa kuamkia jana baada ya chumba kimojawapo cha bweni la wasichana (Nyerere Hostel), kushika moto kisha bweni zima kuteketea.

Katika tukio hilo la kusikitisha, wanafunzi wengine 22 wamejeruhiwa, kati yao 14 wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa na wanane wamelazwa katika Kituo cha Afya cha Idodi. Shule hiyo ipo katika Jimbo la Ismani linaloongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa Iringa, Dk. Oscar Gabone alithibitisha kupokea miili ya marehemu na majeruhi wa ajali hiyo ambao wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo.

Umati mkubwa wa wananchi wa Manispaa ya Iringa na vitongoji vyake, mapema jana asubuhi ulifurika nje ya chumba cha kulaza wageni cha hospitali hiyo baada ya kupata taarifa za ajali hiyo na kufikishwa kwa miili ya marehemu hao ambayo hata hivyo haitambuliki baada ya kuunguzwa vibaya na moto huo.

Katika tukio hilo, wanafunzi wengine 427 walinusurika kupoteza maisha yao baada ya jitihada za walimu na wananchi waliowahi kufika katika eneo la tukio, kuanza kuvunja madirisha ili kuwawezesha wanafunzi hao kupata sehemu za kupita na hatimaye kuokoa maisha yao.

Bweni hilo lililoteketea kwa moto, lina vyumba 25 na lina uwezo wa kulaza wanafunzi 461 na kwamba wakati moto unashika chumba kimojawapo, wanafunzi hao walikuwemo kwenye bweni hilo.

Taarifa zilizothibitishwa na uongozi wa shule hiyo zimesema kulikuwepo na mifupa ya marehemu hao katika lango kubwa la kutokea na inadaiwa kuwa wanafunzi hao huenda walikufa kabla kwa kukanyagwa na wenzao katika harakati za kujiokoa.

Ofisa Elimu wa Mkoa wa Iringa, Salum Maduhu na Kamanda wa Polisi Mkoa huo, Evarist Mangalla, walisema chanzo cha ajali hiyo ni moto wa mshumaa kushika godoro na kuwaka katika chumba hicho.

Kwa mujibu wa Kamanda Mangalla, mshumaa huo uliwashwa na mwanafunzi, Naomi Mnyali wakati akijisomea, lakini baadaye alipitiwa na usingizi na kuuacha ukiwaka kabla ya kushika kwenye godoro.

Hata hivyo, taarifa iliyotolewa na Kamanda huyo wa Polisi ilisema, mwanafunzi huyo alinusurika katika tukio hilo japo haikuelezwa hali yake ikoje. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Mangalla aliwataja marehemu katika ajali hiyo kuwa ni Matilda Mtewele, Adelvina Kwama na Elizaberth Mtavila ambao walikuwa wanasoma Kidato cha Kwanza.

engine ni Digna Ndunguru, Chake Kuyaa, Seciliana John, Lazia Kihwele, Witness Mbilinyi na Stellah Mwigavilo waliokuwa wanasoma Kidato cha Pili. Pia wamo Falha Abdallah na Jesca Wissa waliokuwa Kidato cha Tatu na Maria Ndole wa Kidato cha Nne. Kamanda Mangalla alisema kutokana na marehemu hao kuteketea kiasi cha kutotambulika, wametumia njia nyingine kupata majina yao.

Majeruhi wa ajali hiyo mbaya ni Mwizarubi Eliasi, Lucy Sawani, Faraja Sodike, Anoda Ambali, Lela Mkuya, Prisca Melele, Evamary Carlos na Sabrina Abdulrahaman. Wengine ni Lenna Barugu, Zuhra Mazora, Veronika Nyamule, Theresia Zuvapi, Esther Zayumba, Ando Mamba, Irene Mponzi, Ares Ndaga, Lucy Luvanda, Upendo Nyamadule, Fraja Palinoo na Helena Mapunda.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza alithibitisha pia kutokea kwa vifo hivyo akiwa Iringa ambako aliwasili jana asubuhi akitokea Songea mkoani Ruvuma kikazi. “Ni kweli bweni moja katika shule ya Idodi , Iringa Vijijini, limeshika moto usiku wa kuamkia leo (jana) na wanafunzi kumi na wawili wamekufa na wengine kama ishirini na tano wamejeruhiwa.

“Niko hapa shuleni tangu asubuhi, hivi sasa tuko katika kikao na uongozi wa Mkoa, Shule na Wazazi kuzungumzia namna ya kufanya maziko,” alisema Mahiza alipozungumza kwa mara ya kwanza na gazeti hili saa 10:32 jioni.

Alisema kikao hicho ndicho kilikuwa kikijadili namna ya maziko ya wanafunzi hao 12; kama wazikwe katika kaburi moja au kila familia ikaandae mazishi yake.

Lakini baadaye, Mahiza alilieleza gazeti hili kuwa wamekubaliana kwamba maziko ya wanafunzi hao yafanyike kesho saa nane mchana shuleni hapo kwa kufuata taratibu za dini zote kubwa mbili; Kiislamu na Kikristo na uongozi wa Mkoa wa Iringa utatafuta eneo hilo la kuzikia.

Kuhusu kutambuliwa kwa marehemu wakati miili yao ilikuwa imeteketea kabisa kwa moto, Mahiza alisema, “Tumetumia kitabu cha majina ya wanafunzi kuwaita walioko hosteli, waliokuwa wamelazwa hospitali ya mkoa na wale waliokuwa katika kituo cha afya Idodi. Kwa hiyo, tukaamini kabisa wale ambao hawapo hata majumbani, ndio waliofariki.”

Mahiza, ambaye wakati akizungumza na gazeti hili, alisema Waziri wake, Profesa Jumanne Maghembe alikuwa anaingia mjini Iringa, alisema shule hiyo iliyoko takribani kilometa 108 kutoka Iringa Mjini katika barabara ya kuelekea Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, ni ya kata na ina wanafunzi wa kike na wa kiume.

Mwalimu wa Idodi aliyeomba hifadhi ya jina lake, alisema kwa kawaida wanafunzi hutakiwa kuzima taa za umeme wa jenereta ifikapo saa sita usiku, lakini limekuwa jambo la kawaida kwa wanafunzi wanaotaka kuendelea kujisomea kutumia mishumaa au taa za mafuta.

Wanafunzi zaidi ya 400 hawana mahali pa kuishi kutokana na ajali hiyo, na jana jioni, mfanyabiashara maarufu wa Iringa, Salum Abri wa Kampuni ya Asas Dairies alijitolea msaada wa mablanketi 200 na magodoro 200 ili kunusuru vijana walionusurika katika ajali hiyo.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ametuma salamu za rambirambi na pole kwa wazazi, ndugu, jamaa na marafiki wa wanafunzi 12 wa Shule ya Sekondari ya Idodi waliothibitishwa kufariki dunia, kutokana na ajali ya moto iliyotokea shuleni hapo usiku wa kuamkia jana.

Katika salamu hizo, Waziri Mkuu alisema, kwa niaba ya serikali na kwa niaba yake binafsi, amesikitishwa na kuhuzunishwa sana na tukio hilo na vifo hivyo na kuwaomba wazazi, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu kuwa wavumilivu na wavute subira katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

litaka waliojeruhiwa katika tukio hilo watibiwe vizuri ili wapate ahueni haraka. Ajali za moto katika shule nchini zimekuwa zikitokea mara kwa mara katika miaka ya karibuni, huku mojawapo ya kukumbukwa zaidi ikiwa ni iliyotokea mkoani Kilimanjaro, katika Shule ya Shauritanga wilayani Rombo mwaka 1994 na kupoteza maisha ya wasichana 43.

No comments: