Monday, August 3, 2009

Siri za Meremeta kwenye Mtandao

-Serikali yatikisika, Usalama wa Taifa wafuatilia
-Nakala 100 za ripoti hiyo zaandaliwa

SAKATA la kampuni ya Meremeta Limited iliyochota Benki Kuu ya Tanzania Sh bilioni 155 na ambalo sasa serikali imetangaza kwamba inahusiana na mambo ya Usalama wa Taifa, limeingia katika hatua mpya, baada ya kuelezwa kwamba sasa ripoti kamili ya siri kuhusu ufisadi huo itaanikwa katika mtandao.

Taarifa zilizotolewa kwenye mitandao ya Mwanakijiji.com na jamiiforums.com imeeleza kwamba ripoti hiyo inafuatia kile ambacho kilichukuliwa kama tishio lililotolewa na mmoja wa wanachama wa mitandao hiyo kuhusu kuanika siri ya Meremeta.

Mwanachama huyo, ambaye alikuwamo ndani ya serikali wakati wa mchakato wa uanzishwaji wa Meremeta, alielezea kutoridhishwa kwake na maelezo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na kutaka aeleze kuhusu Meremeta; vinginevyo yeye na wenzake wataamua kufanya kazi hiyo ili kuhakikisha kuwa mjadala wa Meremeta unamalizwa.

Raia Mwema limefahamishwa kwamba tayari vyombo vya usalama vimeanza kufuatilia suala hilo na huenda kukatokea mtikisiko mkubwa serikalini baada ya kusomwa kwa ripoti hiyo.

Taarifa hizo ambazo zinaonekana kama kujichukulia majukumu mikononi, kundi la Watanzania hao limeamua kufichua siri ya "usalama wa taifa" inayohusisha kampuni hiyo ya Meremeta ambayo ilianzishwa kwa kazi ya ununuzi na uchimbaji dhahabu.

Kampuni hiyo, ambayo iliandikishwa Uingereza mwaka 1997 na baadaye kufilisiwa huko huko Uingereza mwaka 2006, imezua malumbano makali bungeni hivi karibuni baada ya baadhi ya wabunge kupinga matumizi mabaya ya fedha kuhusishwa na usalama wa taifa.

Ndani ya mtandao huo imeelezwa kwamba kufichuliwa kwa kampuni hiyo kunatarajiwa siku yoyote wiki hii baada ya uchunguzi wa muda mrefu na ukusanyaji wa taarifa mbalimbali ambao umefanywa na Watanzania hao katika ushirikiano wa aina ya pekee wakiwa wametawanyika sehemu nbalimbali duniani.

Akiandika katika mtandao wake, mwanachama huyo alimwambia hivi Waziri Mkuu:

"Kwa vile suala la usalama linahusu usalama wa Taifa letu na wanaoohoji ni wabunge wa Taifa hilo ambao ni wawakilishi wetu, basi hata kama suala la Meremeta haliwezi kuwekwa hadharani (kwa kurushwa kwenye Luninga) basi Bunge lifunge macho na masikio ya nje na Wabunge wote wawe briefed wazi na moja kwa moja kuhusu Meremeta, umiliki wake na uhusiano wake na jeshi na usalama wa Taifa.

"Na endapo wabunge wataridhika, basi, tutapenda kusikia kuwa wameridhika na maelezo hayo na kama wabunge wapige kura kama wasimamizi wa serikali kuamua kama habari hizo kweli zinatishia usalama wa Taifa na kama wananchi wanapaswa kuziona."

Maelezo ndani ya mtandao huo yameeleza kwamba tangu ombi hilo litolewe hakuna dalili yoyote ya serikali kuwa wazi juu ya Meremeta na kuwalazimu Watanzania hao kuunganisha nguvu zao na raslimali zao kufanya utafiti wa kina wa suala zima la Meremeta.

Soma zaidi

No comments: