Friday, August 7, 2009

Sitta aanika majeruhi kashfa ya Richmond

-Hosea naye aligeuzia Bunge kibao
-Achunguza kamati za Shelukindo, Dk. Slaa, Zitto

SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta, ameanika siri ya yeye kuandamwa akisema wanaomuandama wengi ni katika kundi la majeruhi wa tuhuma za ufisadi, hususan za kuhusiana na mradi wa umeme wa dharura uliokabidhiwa kampuni tata ya Richmond Development LLC.

Katika mahojiano maalumu na Raia Mwema kwa njia ya simu kutokea jimboni kwake Urambo Mashariki, mkoani Tabora, mwabzoni mwa wiki hii, Sitta alisema anaamini maadui zake kisiasa ndio wanaopandikiza tuhuma hizo ili ionekane mbele ya umma kuwa yeye ni kiongozi asiyefaa.

Katika hali inayodhihirisha kuwarushia kijembe baadhi ya wanasiasa wenzake, Sitta alisema watu wanaomuandama ni majeruhi wa msimamo mkali wa Bunge katika kupinga ufisadi akilenga moja kwa moja hasa kundi aliloliita kuwa ni 'genge' lililohusika na kampuni hewa ya Richmond.

Akijikita katika kuwaelezea watu hao, Sitta alisema: "Katika genge hili kuna watu watatu vinara. Wa kwanza ni mwanasiasa. Huyu kwa lugha ya kipolisi ni mhalifu sugu; amehusika katika uchotaji wa mabilioni kinyemela katika Commodity Import Support (CIS); amechota mabilioni kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu (BoT); na aliwahi nadhani mwaka 2004 kupewa tenda ya kuingiza mahindi kutoka nje ya nchi, na akapewa malipo ya awali na hakufanya kama ilivyotakiwa. Ni mhalifu sugu.

"Wa pili ni mwanasiasa ambaye amejipatia utajiri wa kupindukia katika hali ya maswali, yupo mwingine anajiita mfanyabiashara naye ameingia katika mkondo huo. Na kwa vigezo vya Tanzania hawa ni mabilionea.

"Tatizo hawa ni viongozi na wana-influence (nguvu kubwa ya ushawishi) na uhusiano mzuri na viongozi wengine wa kitaifa. Wamejenga mitandao ya kuiibia nchi, na wanafanikisha kazi hiyo kwa kutumia influence ya kisiasa na uhusiano kati yao na viongozi wa juu kutisha watendaji waaminifu serikalini.

"Kwa mfano, Richmond ambao ndiyo Dowans, walinunua mitambo mitatu, kwa Dola za Marekani milioni 30, wakapewa barua ya dhamana (letter of credit) na CRDB inayozidi dola milioni 30. Baadaye wakataka kuiuzia serikali mitambo hiyo kwa bilioni 69. Bunge tulitafiti bei hiyo kwa kuuliza inakouzwa na tukaambiwa mitambo mipya ni kati ya bilioni 25 na 30 na bei inaweza kupunguzwa. Tukazuia, wakachukia.

"Sasa watendaji dhaifu wamekuwa wakiwaogopa na hivyo kujikuta wakivunja sheria ili kuwaridhisha. Wamewekeza majengo katika mji wa Dubai, Afrika Kusini na Uingereza. Kinachotokea ni kwamba Bunge sasa linawanyima usingizi, linatibua mitandao yao ya wizi na ulaji, kwa hiyo lazima wawe na hasira.

"Bahati mbaya kwao, wamefuatilia rekodi yangu kiutendaji hawajakuta makosa yoyote na hivyo wamekosa pa kunibana nikiwa kama kiongozi wa Bunge linalowanyima usingizi. Wamegundua track record (utendaji kazi ) yangu ni excellent (nzuri sana). Nimekuwa Waziri wa Ujenzi na kufanikisha miradi mikubwa kama Kiwanja cha Ndege Dar es Salaam, ujenzi wa barabara ya Morogoro-Dodoma, ujenzi wa Daraja la Salender, Dar es Salaam (mwaka 1980), ujenzi wa barabara ya Makambako-Songea (1983).

"Nimesimamia ujenzi wa nyumba 252 kwa fedha za mkopo kutoka Shirika la Bima la Taifa (NIC) na NPF (sasa NSSF). Mwaka 1988 nimekuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, 1990 Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, mwaka 1993 hadi 1995 nimekuwa Waziri wa Sheria na Katiba, 1996 hadi 2005 nimekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), kote huko hakuna ufisadi hata wa senti moja. Track record yangu ni uadilifu mtupu, wamekosa kwa kunikamata, wanahangaika sasa kupotosha ukweli," alisema Sitta.

Akijibu tuhuma zinazomhusisha kutaka gari la thamani kubwa na nyumba ya kifahari, alisema angetamani atumie usafiri hata wa 'Suzuki Vitara' lakini yeye si mwamuzi, bali jukumu hilo ni la vyombo vya usalama vinavyoamua gari gani linunuliwe ili kukidhi vigezo vyao vya ulinzi wa viongozi wa kitaifa dhidi ya changamoto za kisasa za uhalifu.

Amesema yapo magari yasiyopenyeza risasi yanayotumiwa na viongozi ambayo yamenunuliwa kwa Sh bilioni 1.2, na mwamuzi si "anayeendeshwa" bali ni vyombo vya Usalama wa Taifa, ambavyo ni lazima vifanye kazi kwa ufanisi wakati wote.

Kuhusu suala la nyumba, alisema amekuwa akiishi katika ambayo ilikimbiwa na Naibu Waziri, Dk. Makongoro Mahanga, kutokana na nyumba hiyo kuwa na mfumo wa majitaka unaopumulia ndani, na nyumba hiyo ilikuwa katika eneo la makazi ya mawaziri, jijini Dar es Salaam.

Amesema ameishi katika nyumba hiyo kwa takriban miaka minne, na baada ya Rais Jakaya Kikwete kupata taarifa hizo aliagiza ahamishwe na atafutiwe nyumba yenye hadhi yake kama kiongozi wa mhimili wa taifa (Bunge).

Aliongeza Sitta katika majibu yake kuhusu masuala hayo matatu:
"Tuanze kuzungumzia hoja ya ununuzi wa gari. Eti Spika nataka gari la kifahari. Sihusiki kabisa katika utaratibu wa kununua magari ya viongozi wa kitaifa. Nchi inaendeshwa kwa taratibu maalumu si ovyo ovyo namna hiyo, kwamba viongozi wa kitaifa wanalala na kuamkia asubuhi na kuagiza nunua gari jipya.

"Utaratibu ni kwamba kwa viongozi wa kitaifa kama Spika na wengine, anayehusika katika ununuzi wa magari ni Katibu Mkuu Kiongozi, ambaye naye anazingatia maoni ya Usalama wa Taifa katika kufikia uamuzi.

Soma zaidi

No comments: