Monday, August 17, 2009

Hatma ya Zombe

JAJI wa Mahakama ya Rufaa Tanzania, Salum Massati, anaendelea kusoma hukumu ya kesi ya mauaji inayomkabili aliyekuwa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Dar es Salaam, Abdallah Zombe na wenzake wanane.

Watu wamefurika ndani na nje ya jengo la Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam kusikiliza hukumu ya kesi hiyo inayovuta hisia za wengi.

Jaji Massati anasikiliza kesi hiyo kwa sababu amekuwa akifanya hivyo tangu ianze mwaka 2006, na wakati huo alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu.

Takribani watu 200 wapo ndani ya chumba namba moja cha mahakama hiyo, mamia wengine wapo nje.

Kwa kuzingatia idadi ya watu waliofika kusikiliza hukumu hiyo, Mahakama hiyo imeweka maspika ili kuwawezesha watu kusikia kinachoendelea ndani.

Zombe na wenzake wameshitakiwa wakidaiwa kuwaua wafanyabiashara watatu wa madini na dereva wa teksi Januari 14 mwaka 2006 katika msitu wa Pande, Mbezi, mkoani Dar es Salaam.

Wafanyabiashara hao, Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi, na Mathias Lunkombe walikuwa wakazi wa Mahenge, Morogoro, dereva wa teksi, Juma Ndugu, alikuwa akiishi Dar es Salaam.

Zombe ni mshitakiwa wa kwanza kwenye kesi hiyo, amedai kuwa ametolewa kafara kama Yesu kwa kuwa maofisa ndani ya Jeshi la Polisi wanamuonea wivu.

Wazee wa Baraza wamesema, hakuna shahidi hata mmoja upande wa mashitaka aliyemtaja Zombe kwamba alihusika kuua hivyo wameshauri aachiwe huru.

Wazee hao wameishauri Mahakama Kuu iwatie hatiani washitakiwa saba kwa kuwa wamekubaliana(wazee) na upande wa mashitaka kwamba walihusika kuwaua wananchi hao.

No comments: