Monday, August 17, 2009

Serikali yachambua zabuni za mikataba ya umeme

SERIKALI inaendelea na mchakato wa kuchambua zabuni kabla ya kusaini mkataba wa kuzalisha umeme zaidi nchini. Zabuni hizo zinalenga kuweka mtambo Dar es Salaam utakaozalisha megawati za umeme 100 wakati kwa upande wa Mwanza zitazalishwa megawati 60.

Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alisema jana kwamba Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) linaendelea na mchakato huo wa kuchambua zabuni kabla ya kutekeleza miradi hiyo itakayochukua siyo chini ya mwaka mmoja.

Ngeleja aliyekuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Tuongee Asubuhi kinachorushwa na Televisheni ya Star, alisema hivi sasa serikali ipo katika kipindi cha kuimarisha miundombinu ya Tanesco ili kuhakikisha kuwa inatatua tatizo la upatikanaji umeme katika maeneo mbalimbali. Kwa mujibu wa Ngeleja, katika makusanyo ya kila mwezi ya Tanesco, asilimia 15 zinatumika kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya shirika hilo.

Aliyataja maeneo mbalimbali ambayo serikali imeanzisha miradi kwa lengo la kuwapatia umeme wa uhakika ikiwamo Mkoa wa Ruvuma ambao katika miaka miwili ijayo, utaingizwa katika gridi ya taifa. Miradi mingine inahusisha wilaya za Bukombe, Bariadi (Shinyanga), Magu (Mwanza) na mkoani Arusha na akasisitiza kwamba miradi yote itatekelezwa.

Akisisitiza uamuzi wa serikali kuanzisha miradi hiyo, alisema utekelezaji wa miradi unaendelea kulingana na utaratibu uliopo na si kwa ajili ya kampeni kama ambavyo wengine wanachukulia.

No comments: