Thursday, August 27, 2009

Kesi za mauaji ya Albino kuanza kusikilizwa mwezi ujao

KESI za mauaji ya albino zilizokuwa zimesitishwa kusikilizwa katika mahakama za Kahama na Shinyanga, zitaanza kusikilizwa mwezi ujao kwa siku 30 mfululizo. Hatua hiyo imekuja baada ya Ofisi ya Msajili wa Mahakama Kuu kukamilisha utaratibu ikiwemo baadhi ya masuala yaliyochangia kusitishwa, Juni mwaka huu.

Msajili wa Mahakama Kuu, John Utamwa alisema jana kwamba ipo bajeti ya kutosha na mchakato wa malipo umekamilika kabla ya kesi hizo kuanza kusikilizwa kuanzia Septemba 7, mwaka huu. Alisema ingawa kesi hizo tano zimepangwa kusikilizwa katika siku hizo 30, lakini zisipotosha, wataongeza ili kuhakikisha kwamba zinaendeshwa kikamilifu.

“Tumejipanga kwa maana kwamba tumejiandaa vizuri,” alisema Utamwa na kuongeza kwamba wamehakikisha mambo yote muhimu ikiwemo bajeti, yanakamilika kabla ya kesi hizo kuanza.

Kesi tatu zinasikilizwa Kahama chini ya Jaji Gabriel Rwakibalira anayetoka Mwanza na kesi mbili zinasikilizwa Shinyanga na Jaji Gadi Mjemmas kutoka Dodoma.

Msajili huyo wa mahakama kuu, akizungumza na gazeti hili wiki iliyopita, alisema kesi hizo za mauaji ya albino ni miongoni mwa kesi ngumu kutokana na mazingira yake. Alitoa mfano wa viungo vya binadamu vinavyotoa harufu ambavyo hulazimika kuwasilishwa mahakamani kama vielelezo.

No comments: