Tuesday, August 11, 2009

Dk. Asha-Rose Migiro yuko juu



Na Cecilia John wa Maelezo.

Naibu katibu mkuu wa umoja wa mataifa Dk. Asha Rose Migiro ameibuka kidedea katika kura za maoni za kumpendekeza Raisi mwanamke kati ya viongozi wanawake 9 Tanzania kwa asilimia 36.

Hayo yalisemwa na Meneja wa Kampuni ya utafiti ya Synovate, zamani ikijulikana kama Steadman group, Aggrey Oriwo leo katika mkutano na waandishi wa habari mjini Dar es salaam wakati wa kuelezea matokeo ya kura za maoni ya wananchi kuhusu hali ya kiuchumi,kisiasa na kijamii.

Oriwo alisema kwamba Dk. Migiro alishinda kwa kiwango kikubwa dhidi ya wanawake wenzake kwa 36%, akifuatiwa na Anna Kilango Malecela 20%, Margaret Sitta 10%, Anna Tibaijuka 5%, Sophia Simba 4%, Getrude Mongela 2%,Mama Salma Kikwete 2%, na Hawa Ghasia 2%,.

Utafiti huo ulifanyika kati ya tarehe 9-17 mwezi juni mwaka huu ukihusisha wanaume ambao walikuwa 52%,na wanawake 48%, kutoka vijijini 56% ya idadi yote ya watu na mjini 44% ya idadi yote ya watu.
Aidha matokeo ya utafiti huo yametokana na maoni ya watu elfu mbili (2000) ambao walikuwa wanapatikana mikoa yote ya bara na visiwani kwa kuzingatia takwimu na idadi ya watu kama ilivyodhihirika kwenye sensa ya 2002.

Source: issamichuzi.blogspot.com

No comments: