Tuesday, August 18, 2009

Kesi za Epa zaahirishwa Kisutu

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, jana ililazimika kuahirisha kusikiliza kesi ya wizi wa zaidi ya Sh bilioni tatu za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu Tanzania (BoT) kutokana na mawakili kuwa Mahakama Kuu kwenye hukumu ya Kamishna Msaidizi wa Polisi, Abdallah Zombe na wenzake.

Kesi hiyo inayomkabili mfanyabiashara Rajab Maranda na wenzake iliahirishwa baada ya wakili wa upande wa utetezi, Majura Magafu kuwa kuwa katika kesi hiyo Mahakama Kuu. Iliahirishwa baada ya kupokea taarifa hiyo kutoka kwa Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Boniface Stanislaus na imepangwa kuanza kusikilizwa leo mbele ya jopo la mahakimu Samwel Kirua na wenzake.

Mbali na Maranda, washitakiwa wengine ni Hussein Farijala, Ajay Somay na maofisa wa BoT, Iman Mwakosya, Ester Komu na Sophia Larika.

Washitakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuiba Sh bilioni 3.8 kutoka BoT baada ya kughushi mkataba wa makubaliano wa kuhamishiwa deni na Kampuni ya Lakshimi Textile Co. Ltd ya India kwenda kwenye Kampuni ya washitakiwa hao ya Mibare Farm. Kati ya Januari 18 na Novemba 3, 2005, kinyume cha kifungu namba 384 cha Kanuni ya Adhabu Sura ya 16, walikula njama ya wizi wa fedha kutoka BoT.

Wanadaiwa kughushi hati ya usajili yenye namba 46218 na kuonesha kuwa zimesainiwa na kutolewa na Msajili wa Biashara kwa Kampuni ya Mibare Farm wakati si kweli. Washitakiwa Farijala, Maranda, Somani, Mwaposya, Komu na Kalika inadaiwa kuwa waliiba fedha hizo baada kudanganya kuwa imepewa deni na Kampuni ya Textile Mills Ltd ya India na kujipatia ingizo hilo.

No comments: