Thursday, July 21, 2011

Wanafunzi 56 wazuiwa kurudi UDOM

WANAFUNZI wa Shahada za awali wa Chuo Kikuu cha Sayansi za Kompyuta, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (CIVE) katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) waliosimamishwa masomo kwa muda usiojulikana takribani miezi mitatu iliyopita, wameitwa chuoni.

Wanafunzi 56 kati ya waliosimamishwa wamezuiwa kurudi chuoni.

Taarifa iliyotolewa juzi katika tovuti ya chuo, imetaja majina ya wanafunzi 56 ambao wote ni wavulana wasiotakiwa kurudi chuoni na kusema kwamba, watapewa taarifa zao binafsi na mamlaka husika.

Kwa upande wa wanafunzi walioruhusiwa kurudi, uongozi wa chuo umewabana kwa kuwapa masharti kadhaa miongoni mwake ikiwa ni kwamba walitakiwa kurudi chuoni na kufanya usajili upya Julai 7 mwaka huu kabla ya masomo kuanza Agosti Mosi mwaka huu.

Masharti mengine waliyopewa wanafunzi hao ni kwamba wale wanaodaiwa ada, gharama za malazi, mitihani na gharama nyingine, ni lazima walipe madeni hayo kabla ya kurudi chuoni.

Pia kila mwanafunzi anatakiwa kulipa gharama za usajili Sh 10,000 na wameamriwa malipo yote yafanyike kabla ya Julai 23 kupitia akaunti za chuo zilizo mjini Dodoma.

Kila mwanafunzi anatakiwa aape kwa wakili kiapo cha utii wa Sheria Ndogondogo za wanafunzi wa UDOM na za nchi.

“Kiapo kibandikwe picha mbili; moja ya mzazi au mlezi wa mwanafunzi na moja ya mwanafunzi mhusika. Mwanafunzi atakayekiuka kiapo chake atafukuzwa chuo mara moja,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo iliyotolewa na ofisi ya Makamu wa Chuo.

Chuo hicho kilifungwa Aprili mwaka huu baada ya kukumbwa na mgogoro kati ya wanafunzi na Menejimenti.

Uongozi ulichukua hatua hiyo kutokana na hali ya usalama kuwa tete baada ya wanafunzi 27 kusimamishwa masomo hali iliyowafanya wanafunzi wengine kuandamana wakidai wenzao warudishwe.

Chanzo halisi cha ilikuwa ni maandamano yaliyofanywa na wanafunzi hao kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu, mjini Dodoma wakidai wapewe fedha za mafunzo ya vitendo na vitendea kazi zikiwemo kompyuta walizodai kwamba Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika ziara yake ya Januari mwaka huu, alishauri wapewe.

No comments: