Tuesday, July 26, 2011

Rostam amuenzi mjane wa Mwakiteleko

MWENYEKITI wa Bodi ya Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Rostam Aziz ameahidi kumlipa mjane wa mwanahabari marehemu Danny Mwakiteleko, Winfrida, mshahara aliokuwa akipokea mumewe kwa muda wa miaka mitano.

Aidha, ameahidi kuwalipia ada za shule watoto wawili Carol (13) na Vanessa (11) mpaka
kiwango cha elimu ya juu pamoja na wategemezi wawili wa Mwakiteleko aliowaandika
katika faili lake kazini.

Mwakiteleko, (45), aliyekuwa Mhariri wa Gazeti la Rai na Naibu Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006), alifariki dunia Jumamosi alfajiri na alisafirishwa jana kwenda kijijini kwao Ndala Mwakaleli wilayani Rungwe, mkoani Mbeya kwa maziko.

Taarifa hiyo ya Rostam ilitolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Hussein Bashe wakati wa kutoa salamu za rambirambi za kampuni hiyo katikashughuli za kutoa heshima za mwisho zilizofanyika nyumbani kwa marehemu Tabata Chang’ombe
jijini Dar es Salaam.

Alisema Rostam alimtuma kutoa rambirambi hiyo ikiwa ni mchango wa kampuni hiyo kwa kutambua utendaji kazi wa Mwakiteleko.

Alisema kampuni hiyo itawasomesha hao; mmoja aliyeko kidato cha tatu na mdogo aliye darasa la sita mpaka elimu ya juu.

“Pia Kampuni itagharamia masomo ya wategemezi wawili wa Danny ambao mmoja ni mtoto wa kaka yake ambaye pia ni marehemu; mtoto huyo anasoma shule ya msingi na
mwingine mtoto wa dada wa mke wake anayesoma Stashahada katika Chuo cha Diplomasia,” alisema Bashe.

Alisema marehemu alikuwa na ndoto ya kutoa toleo maalumu la mika 50 ya Uhuru pamoja na miaka 12 ya Tanzania bila Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na hivyo watatoa matoleo hayo kumuenzi marehemu aliyekuwa mchapakazi bila kuchoka wala kulazimishwa.

Kabla ya salamu za kampuni hiyo, ibada ilifanyika nyumbani kwa marehemu na kuongozwa na Mchungaji Philemon Kibwana wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Tabata Kuu, aliyewataka wafiwa kulia kwa matumaini katika machungu waliyonayo
huku wakiangalia zaidi maisha yao.

Katika msiba huo, Serikali iliwakilishwa na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi aliyepongeza Jukwaa la Wahariri kwa kuonesha umoja tangu marehemu alipopata ajali hadi katika msiba na kuwatakakuambukiza umoja huo kwa Taifa
zima.

Pia aliipongeza Kampuni ya New Habari (2006) kwa ahadi hiyo kwa familia ya marehemu kwa kuwa katika misiba mingi ni vigumu kusikia waajiri wakizungumzia waliobaki.

Alisema utaratibu huo unasaidia wafanyakazi kufanya kazi kwa juhudi kwani wanaona jinsi mwajiri wao anavyowathamini na kuongeza tija miongoni mwao.

Dk. Nchimbi pia alitoa salamu za pole kutoka kwa Rais Jakaya Kikwete ambaye alitamani kuhudhuria mazishi hayo, lakini jana alikuwa katika maadhimisho ya Siku ya Mashujaa mkoani Mtwara.

“Rais alitamani sana kuwa pamoja nasi, lakini imeshindikana na Ikulu inafanya utaratibu kuwasilisha ubani kwa familia ya marehemu,” alisema Dk. Nchimbi.

Taasisi na kampuni mbalimbali walitoa salamu zao za rambirambi kwa familia ya marehemu zenye zaidi ya Sh milioni tisa.

No comments: