Tuesday, July 26, 2011

TGNP YAGEUKA MKOMBOZI KWA MADIWANI VITI MAALU NAMTUMBO

MADIWANI wanawake viti maalum wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma wameanzisha kampeni maalum kupiga vita tabia ya wanaume wa wilaya hiyo ya ukandamizaji wanawake kiuchumi.

Wakazi wa wilaya hiyo ambao hujishughulisha na kilimo cha Tumbaku, wanawake wengi huolewa mitala na kutumikishwa katika kazi za mashambani kuzalisha mazao ya chakula na biashara husasani Tumbaku na kutekelezwa msimu wa mauzo ambapo wanaume hutumia fedha vibaya bila kujali familia na wengine kuongeza kuoa wanawake wasichana.

Madiwani hao ambao hivi karibuni waliainisha vikwazo vya maendeleo ya wanawake na watoto katika wilaya hiyo, walibaini ukandamizwaji kiuchumi unaofanywa na wanaume wa wilaya hiyo unaotokana na mfumo dume.

Kutokana na kubaini hilo umewekwa mpango mkakati wa mwaka mmoja wa kutoa elimu katika ngazi ya familia, kijiji na kuiweka ajenda ya usawa wa kijinsia kuwa ya kudumu katika mikutano yote watakayoshiriki madiwani hao ikiwa ni pamoja na kuyahusisha mashirika yasiyokuwa ya kiserikali kutoa elimu hiyo.

Wakizungumza na Mwandishi wa habari hii mara baada ya kumaliza mafunzo yaliyoendeshwa na Mtandao wa Jinsia (TGNP) katika kampeni yao ya haki za uchumi kwa wanawake walio pembezoni, na ukombozi wa mwanamke kimapinduzi yaliyofanyka mkoan Ruvuma, wamesema mwanamke wa Namtumbo lazima akombolewe.

Diwani Asteria Nchimbi alisema maendeleo ya wilaya hiyo yanakandamizwa na mfumo dume.

“Wanawake ndiyo wanaozalisha mali lakini mapato yote hutumiwa na wanaume,” alilalamika Diwani Nchimbi na kudai watashirikiana na Mkuu wa wilaya hiyo, Saveri Maketa ambaye ameanza kutoa elimu ya umuhimu wa usawa wa kijinsia na kupanga bajeti kwa ushirikishwaji wa familia.

Naye Mkuu wa wilaya hiyo Saveri Maketa alikiri kuwa licha ya mapato makubwa ya fedha wanazozipata wananamtumbo kutokana na uzalishaji wa Tumbaku hali ya maisha inabadilika kwa kasi ndogo hasa kutokana na mfumo dume wa maamuzi yote kufanywa na wanaume.

“ Wanawake wanashiriki kazi zote za uzalishaji lakini kunatatizo katika kupanga matumizi ya fedha,” alibainisha Maketa na kuongeza kuwa hivi sasa elimu anayoitoa inaanza kubadili sura za nyumba kuezekwa bati toka nyasi ingawa kwa kasi kidogo.

Imeandaliwa na Juma Nyamayo kutoka Namtumbo Ruvuma ,Nyumayo ni mwanachama wa mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP) mikoa ya kusini mwa Tanzania na mwandishi wa gazeti la Habari leo mkoa wa Ruvuma

No comments: