Wednesday, July 20, 2011

Mahakama yaamuru IPTL ifilisiwe

MAHAKAMA Kuu Tanzania imetoa amri ya kuifilisi Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).

Mahakama imeagiza kuwa, kazi hiyo ya kuifilisi IPTL ifanywe na mfilisi wa kampuni hiyo ambaye ni Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA).

Uamuzi huo ulitolewa rasmi wiki iliyopita na Jaji wa mahakama hiyo, Semistocles Kaijage katika kesi ya madai namba 254 ya mwaka 2003 iliyofunguliwa na kampuni ya Vip Engineering and Marketing Ltd dhidi ya IPTL, Mechmar Corporation (Malaysia) Berhad na Mfilisi.

Jaji Kaijage alisema, kutokana na ombi lililowasilishwa na Kampuni ya Vip Engineering and Marketing Ltd ambaye ni mmoja wa mshirika wa IPTL Februari 25, mwaka 2002 na baada ya kuwasikia mawakili wake kwa njia ya maandishi na ombi hilo kuchapishwa kwenye Gazeti la Serikali Oktoba 10, mwaka 2003, aliamuru kampuni hiyo ifilisiwe.

Mawakili wa Vip Engineering and Marketing Ltd ni pamoja na Michael Ngalo wa Kampuni ya Mawakili ya Ngalo and Company, Respicius Didace wa Kampuni ya Mawakili ya Didace and Company na Dosca Baregu kutoka Kampuni ya Mawakili ya Mutabuzi & Company.

“Mahakama hii inaamuru ifilisiwe kwa mujibu wa kanuni na kazi hiyo ifanywe na mfilisi anayeshughulika na masuala ya IPTL,” alisema Jaji Kaijage.

Aidha, aliamuru mfilisi huyo ambaye ni Rita kwa kushirikiana na wadau wa IPTL kutumia kampuni inayotambulika katika shughuli za ukaguzi wa umma kuchunguza mali za IPTL, madeni yake na kama kuna tuhuma za rushwa na kisha kutoa ripoti hiyo kwa Mahakama Kuu.

Akizungumza na blog hii jana, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Rita, Philip Saliboko alikiri kuwa Mahakama imewaagiza kuifilisi Rita, lakini bado wakala hao hawajapokea barua ya maagizo hayo rasmi kutoka Mahakama Kuu na kwamba, wanasubiri.

“Ni kweli sisi kama wafilisi wa IPTL tumetakiwa tufanye kazi hiyo ya kuifililisi lakini kwa sasa hatujaanza hatua yeyote kwa kuwa bado hatujapata taarifa rasmi za maagizo kutoka Mahakama Kuu,” alisema.

Alisema, iwapo watapatiwa barua na maagizo hayo rasmi, wataanza kwanza na kujitangaza kwenye vyombo vya habari ili wale wote wanaoidai au kudaiwa na IPTL wajitokeze wakiwa na ushahidi wao kwa Rita ambapo pia watatangaza zabuni kwa kampuni itakayochunguza kila kitu kuanzia gharama, madeni na madai ya IPTL.

No comments: