Thursday, July 21, 2011

Madaktari bingwa kufanya upasuaji bure

JOPO la madaktari bingwa tisa kutoka Shirika la Interplast la Ujerumani linatarajiwa kuendesha huduma za upasuaji wa kurekebisha sura na maumbile kwa wakazi wa mkoa wa Tanga wenye matatizo hayo.

Huduma hiyo itatolewa bure kwa siku 15 mfululizo kuanzia Julai 31 hadi Agosti 14 mwaka huu kwa kuhusisha madaktari hao watakaoshirikiana na madaktari wengine wa Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jijini Tanga jana, mratibu wa upasuaji huo, Dk. Wallace Karata alisema utahusisha midomo iliyopasuka, kaa kaa lililopasuka, makovu sugu yanayozuia muonekano na utendaji kazi wa viungo mbalimbali pamoja na uvimbe mwilini.

Dk. Karata alisema, matibabu hayo yatatolewa bure kwa kuwa shirika hilo limegharamia vitu vyote muhimu kwa ajili ya kufanikisha matibabu hayo isipokuwa gharama za usajili wa mgonjwa pamoja na kulazwa.

“Kwa mara ya nne sasa shirika hilo litaleta jopo la madaktari bingwa wa upasuaji wa kurekebisha viungo mbalimbali hapa mkoani kwetu Tanga, tunaomba wananchi wajitokeze kwa wingi tena mwaka huu kwa kuwa matibabu yatatolewa bure.

“Kila mgonjwa atachangia Sh 1,000 ya kusajili kadi pale hospitali ya Bombo,” alisema na kuongeza kuwa kwa wagonjwa watakaofanyiwa upasuaji mkubwa, watalazimika kuendelea kupata matibabu chini ya uangalizi wa madaktari.

Tangu kuanza kutolewa kwa matibabu hayo kwenye Mkoa wa Tanga, mwaka 2008 hadi mwaka jana tayari wagonjwa 119 wamefanyiwa upasuaji wa kurekebisha maumbile yao huku wengi wao wakiwa ni watu wazima.

No comments: