Monday, July 18, 2011

Resolute yatoa 320m/- halmashauri ya Nzega

WILAYA ya Nzega mkoani Tabora imekabidhiwa Sh milioni 320 na Mgodi wa Dhahabu wa Resolute zikiwa ni malipo ya kodi kwa mwaka wa fedha 2011/12.

Akikabidhi hundi hiyo ya Dola za Marekani 200,000 katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisa Uhusiano wa Resolute, Mariamu Mavura alisema fedha hizo zimetolewa na kampuni hiyo kama kodi.

Mavura alisema fedha hizo zitumike katika miradi inayoonekana kwa wananchi ili kila mkazi wa Nzega aone na kufahamu fedha hizo kutoka Resolute zimefanya nini katika nyanja za maendeleo.

Akitoa mifano ya ujenzi wa maabara za shule pamoja na shule za sekondari za kidato cha tano na sita kwa kila Tarafa nne za wilaya hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Florence Horombe, akipokea hundi hiyo kwa niaba ya Serikali, alisema Serikali inatambua umuhimu wa mgodi huo katika kuchangia mapato ya kodi kwa Halmashauri hiyo.

Horombe alisema mawazo ya mgodi katika matumizi ya fedha hizo yamepokelewa kwa umakini na yatafanyiwa kazi katika matumizi hayo.

DC aliikabidhi hundi hiyo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Kyuza Kitundu, aliyesema fedha hizo zitatumika katika miradi ya ujenzi wa maabara na madarasa ya shule za elimu ya juu kwa kila tarafa.

Kitundu aliupongeza mgodi huo kwa kuwa walipakodi wazuri ambao hawana usumbufu kama baadhi ya wawekezaji wengine.

No comments: