Thursday, October 1, 2009

Makala amshambulia Warioba

KIONGOZI mwandamizi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Amos Makala, amemshambilia Waziri Mkuu mstaafu, Joseph Warioba, kwa kudai kuwa ana ajenda ya siri dhidi ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete.

Makala amesema, Warioba ni sehemu ya matatizo yanayoendelea nchini kwa sababu haoneshi njia za kuyatatua.

"Kauli zake zimeelekea siku zote kutaka kuwaonyesha Watanzania kuwa Serikali ya Awamu ya Nne haijafanya jambo hata moja jema.Ni lini atatoka akasifia mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Nne imefanya mambo mazuri kwa wananchi,” amesema Makala.

Mwanasiasa huyo ni Katibu wa Idara ya Fedha na Uchumi wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM. Taarifa ya Makala imemtuhumu Warioba kuwa ni mtu wa kulaumu tu na hatoi hoja za kujenga.

“Kuna usemi usemao kuwa ukiwa unajua tatizo na huonyeshi njia za kutatatua tatizo, wewe pia ni tatizo. Kwa muda mrefu, matamshi ya Mzee Warioba yamekuwa yakilenga kuilaumu Serikali ya Jakaya Kikwete. Mimi nachelea kusema kuwa Mzee Warioba amekuwa mzee mchochezi namba moja kutengeneza chuki kwa wananchi dhidi ya Serikali yake,” alisema Makala.

Amemshangaa Jaji Warioba kwa kutotaka kuamini utafiti uliofanywa na watafiti kuwa Serikali ya CCM inakubalika na imekuwa kushinda katika uchaguzi mdogo kuonesha kuwa bado iko imara.

“Hivi CCM kuendelea kushinda chaguzi nyingi ndogo, yeye haoni CCM bado imara na wananchi wana imani nayo? Au vita ya kupambana na ufisadi inayoendeshwa na wanaCCM haamini ni matendo ambayo CCM imetamka katika Katiba yake na ni ajenda ya kudumu,” amehoji Makala na kumtaka Jaji Warioba akosoe na ajue pia kusifu.

Amemuomba Warioba aiche Serikali ya Awamu ya Nne iendelee kuwatumikia wananchi kuwaletea maendeleo na kukabiliana na changamoto mbalimbali.

“Msingi wa umoja, amani na mshikamano kwa Watanzania ni mambo muhimu kwa ustawi wa nchi yetu ambavyo kwa kauli za Warioba anataka kuvunja misingi hiyo. Nawataka Watanzania kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, na rais wao kipenzi Jakaya kikwete,” amesema Makala.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, (Utawala Bora), Sophia Simba amesema,Jaji Warioba ana haki ya kusema aliyoyasema, lakini anaamini watendaji wa Serikali wakiwemo mawaziri wanafanya kazi zao ipasavyo na kwa misingi ya utawala bora.

Waziri Simba amesema, kutokana na vyeo alivyowahi kuwa navyo katika serikali kama Makamu wa Kwanza wa Rais; Waziri Mkuu na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yeye(Simba) ni mtu mdogo kumjibu Jaji Warioba.

“Kwa kauli yake ni kama Rais anawashauriwa vibaya na pia labda watu hawatekelezi wajibu wao kuhusu kupambana na rushwa, ana haki kuzungumza haya, lakini marekebisho ya sheria yaliyofanyika ni pamoja na hayo ya kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya rushwa,” amesema.

“Sasa kwa sheria mpya ya rushwa ya mwaka 2007, imeongeza makosa zaidi ya 25 badala ya nane yaliyokuwepo awali, hii yote ni kuwezesha utekelezaji na tunaona kesi kubwa na watu wazito wanafikishwa mahakamani, huusio utani ni kazi inafanyika,” aliongeza Simba.

Simba amesema, hata Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imeweka bayana mapambano dhidi ya rushwa hivyo kazi inafanyika na baadhi imeanza kuonekana.

Amesema, hiyo ni hatua ya kudhihirisha kuwa nchi inazingatia utawala bora na watendaji katika nafasi zao wanafanyakazi zao.

Kwa upande wake, Katibu wa Uenezi na Itikadi wa CCM, John Chiligati amesema leo kuwa, CCM haina nafasi ya kulumbana na wazee wakongwe wa chama badala yake kusikiliza ushauri wao na unaofaa kuzingatiwa.

“Kwanza nisingependa kuingia katika malumbano na wazee wa chama, lakini pia mawazo yake tumeyasikia na tunashukuru,” amesema Chiligati.

Alisema hakuna nchi yoyote duniani ambayo mfumo wa utawala unaoongozwa na binadamu uliokamilika, bali wa Mungu pekee na kukiri upungufu upo kwa kuwa fikra na utendaji kazi unatofautiana.

Amesisitiza kuwa,suala la mpasuko ndani ya chama na mfumo huo wa utawala ni mambo ambayo tayari Rais Kikwete aliyazungumzia alipozungumza na wananchi, hivyo yeye hana cha kuongeza.

Warioba jana aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, mwelekeo wa nchi si mzuri hasa katika suala la kulinda amani, utulivu na mshikamano kutokana na mfumo dhaifu wa kupambana na rushwa uliopo na kutahadharisha kama hautafanyiwa kazi, nchi inaelekea kubaya.

Pia aliwashutumu watendaji na washauri wa rais hasa wa masuala ya rushwa kwamba wanamshauri vibaya kwa kile alichosema si sahihi rais kuzungumzia kesi za rushwa katika hatua za awali huku mfumo wa kisiasa ukilazimisha watu kufikishwa mahakamani bila uchunguzi wa kina kwani kuna hatari serikali ikajiingiza katika kuwalipa wa fidia itakaposhindwa.

No comments: