Thursday, October 1, 2009

'Watakaomkaanga' Liyumba hadharani kesho

UPANDE wa mashitaka katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisabababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh bilioni 200 kupitia ujenzi wa majengo pacha ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), inayomkabili Amatus Liyumba, leo unatarajiwa kutaja idadi ya mashahidi wao.

Kesi hiyo iliyoko katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, upande wa mashitaka umekamilisha upelelezi wake na mara ya mwisho kesi hiyo ilipofikishwa mahakamani, Liyumba alisomewa mashitaka yake kwa mara nyingine ikiwa ni pamoja na maelezo ya mashitaka.

Imedaiwa mahakamani kuwa, Liyumba alifanya mabadiliko katika ujenzi wa majengo hayo bila kupata idhini ya Bodi ya Wakurugenzi ya BoT.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo wa zamani wa Utawala na Utumishi BoT, alishangazwa na madai hayo kuwa alifanya mabadiliko ya ujenzi wa majengo hayo bila kupata ruhusa ya Bodi ya BoT na kuhoji kuwa kama ruhusa haikutolewa, fedha zote hizo za malipo zilitoka wapi.

Mbele ya jopo la mahakimu wakiongozwa na Hedson Mkasmongwa, Liyumba alidai BoT ilisaini mkataba wa ujenzi wa majengo hayo Juni 25, 2002 na ujenzi ulitakiwa ukamilike kwa miaka mitatu.

Ilidaiwa mshitakiwa pamoja na aliyekuwa Gavana kipindi hicho, Dk. Daudi Ballali ambaye sasa ni marehemu, bila kupata ruhusa ya Bodi ya BoT, waliamua kubadilisha ujenzi wa mradi huo na kufanya mabadiliko katika ujenzi mzima jambo ambalo liliongeza gharama kwa asilimia 80.

No comments: