Tuesday, October 13, 2009

'Wanaopinga ufisadi si malaika'

MWANAZUONI maarufu nchini, Profesa Issa Shivji, amesema wanaotajwa kuwa ni wapinga ufisadi nchini si malaika, na wanaodaiwa kutetea uovu huo si mashetani.

Profesa Shivji amesema, makundi yote hayo yanashabikia mfumo uliozaa ufisadi, na kwamba, vyombo vya habari na wanasiasa wamesababisha makundi hayo yalumbane.

"Lakini viongozi bora hawazaliwi..kwani wakati wa mwalimu viongozi hawakuwa na tamaa ya hela? walikuwanayo, walikuwanayo lakini wangefanya nini na mamilioni ya EPA? amehoji Profesa Shivji.

Kwa mujibu wa mwanazuoni huyo, ufisadi ni matokeo ya mfumo wa sasa wa uliberali mamboleo uliotokana na ubepari.

"Mtu hazaliwi na tabia ya ufisadi, mtu hazaliwi na tabia ya ubinafsi, ubinafsi unatokana na mfumo"amesema.

Amesema, wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa, ufisadi haukuwepo Tanzania ila rushwa ilikuwepo.

"Ubepari ndiyo unaoingiza ubinafsi, ni mfumo" amesema na kubainisha kuwa moja ya misingi ya ufisadi ni ubinafsi, na kwamba, hulka ya binadamu ni ushirikiano na si ubinafsi.

Profesa Shivji amesema, chanzo cha ufisadi si mtazamo wa jamii ila mfumo uliosababishwa na ubepari.

Kwa mujibu wa Profesa Shivji, hulka na tabia ya mwanadamu vinajengeka katika mfumo na si mtazamo wao.

"Je, ufisadi ulikuwepo enzi ya Mwalimu? hapana haukuwepo, rushwa ilikuwepo" amesema Profesa Shivji wakati akiwasilisha mada kwenye kongamano la kumuenzi Baba wa Taifa katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.

Amesema, haitoshi kuhubiri uzalendo wakati mfumo wako ni kinyume cha uzalendo.

"Tunakubali tu kila kitu,kila kitu tunachoambiwa tunakubali tu, hatuwathamini watu wetu ndiyo shida yetu...kauli mbiu yetu ni moja tu, question everything (uliza/hoji) kila kitu"amesema.

No comments: