Saturday, October 24, 2009

Siri mpya ya ufisadi Benki Kuu yaanikwa

-Yahusisha mabadiko yaliyofanywa na Dk. Rashid

WARAKA unaoonyesha siri ya matukio ya ufisadi ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) umepatikana ukionyesha kwamba, sehemu kubwa ya watuhumiwa waliofikishwa mahakamani walitokana na mabadiliko yaliyofanywa na aliyekuwa Gavana, Dk. Idris Rashidi.

Kwa mujibu wa waraka huo na maelezo kutoka kwa baadhi ya watumishi wa BoT, mabadiliko hayo yaliingiza timu mpya ambayo sehemu kubwa ni wale ambao wamehusishwa katika matukio ya ufisadi.

Baadhi ya watumishi wa BoT waliozungumza na Raia Mwema kwa nyakati tofauti wiki hii, wamesema matukio mengi ya kifisadi yalianza kufanyika mara baada ya mwaka 1994, kipindi ambacho timu mpya ya Dk. Rashidi ilianza kazi.

“Kwa muda wote tuliokuwa kazini tulikuwa tukisumbuliwa sana na wafanyabiashara na wanasiasa ambao sasa ndio tunawasikia wakiitwa mafisadi na ukiangalia utaona mahusiano yao na timu mpya yalikuwa makubwa sana na hata utajiri na umaarufu wao ulianza kipindi hicho,” anaeleza mstaafu mmoja wa BoT aliyekuwa kitengo nyeti.

Miongoni mwa walioingizwa katika timu mpya ya Dk. Rashidi iliyotangazwa rasmi Desemba 22, 1993 ni pamoja na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Gray Mgonja, ambaye kabla ya kuazimwa Hazina, alikuwa BoT kama Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha.

Mgonja na waliokuwa mawaziri wake wawili, Basil Mramba na Daniel Yona, wameshitakiwa kwa makosa ya uhujumu uchumi wakidaiwa kutumia vibaya nafasi zao kuhujumu serikali kwa kuisamehe kodi kampuni ya uhakiki wa hesabu za madini ya Alex Stewarts.

Wengine ambao walikuwamo katika timu mpya ya Dk. Rashidi ni Bosco Kimela ambaye pamoja na wenzake ameshitakiwa katika kesi ya wizi wa fedha kutoka katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA).

Katika orodha hiyo ya timu ambayo Dk. Rashidi aliingia nayo BoT yumo Amatus Liyumba, ambaye baadaye alibadilishwa kitengo na kwa sasa ni mmoja wa watuhumiwa katika kesi ya uhujumu uchumi inayohusishwa na ujenzi wa majengo pacha ya benki hiyo.

Kesi nyingine ambayo inamuingiza ofisa aliyekuwa katika timu mpya ya Dk. Rashidi ni inayohusu zabuni ya uchapishwaji wa noti iliyoiingizia BoT hasara ya Sh bilioni 104, ikimhusisha Simon Jengo, aliyekuwamo katika timu mpya pamoja na mtuhumiwa mwingine Bosco Kimela.

Mbali ya walioshitakiwa, wamo baadhi ya watu ambao kwa sasa wametajwa kuwa mashahidi katika kesi ya EPA na inaelezwa kwamba orodha inaweza kuongezeka ama hata mashahidi wakaingizwa na kuwa washitakiwa kulingana na muendelezo wa ushahidi na uchunguzi.

Mashahidi hao ambao wametokana na timu mpya ya Dk. Rashidi ni pamoja na Athumani Mtengeti, Peter Noni, Emmanuel Boazi na Stela Chaula, ambao baadhi wanaelezwa kwamba ni watendaji waaminifu na baadhi wanatajwa tajwa kuwa na mahusiano na watuhumiwa wa ufisadi.

Maofisa waliozungumza na Raia Mwema kwa sharti la kutotajwa majina kutokana na sababu za kiusalama, walisema pamoja na kuwapo kwa watendaji safi waliongia katika timu mpya ya Dk. Rashidi, kulikuwa na mikakati maalumu ya wafanyabiashara na wanasiasa waliokuwa na malengo maalumu ndani ya BoT.

Dk. Rashidi aliingia BoT akichukua nafasi iliyoachwa wazi na marehemu Gilman Rutihinda aliyekuwa Gavana kati ya mwaka 1989 hadi 1993, alipoaga dunia.

Source:www.raiamwema.co.tz

No comments: