Tuesday, October 6, 2009

Kikwete hataki malalamiko Serikali za Mitaa

RAIS Jakaya Kikwete, amewataka wanaoandikisha wapiga kura na wasimamizi wa uchaguzi wafanye kazi zao kwa makini na weledi ili kuepuka malalamiko kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji, na Vitongoji utakaofanyika Oktoba 25.

Rais Kikwete amesema, iwapo uchaguzi huo utafanyika kwa uhuru na haki, washiriki wote watayaheshimu matokeo hivyo kuepuka kurudia kufanya uchaguzi mwingine.

“Kama ilivyo kwa kila uchaguzi, kutakuwa na washindi na walioshindwa kinachotakiwa kuzingatiwa ni mwamba mshindi atapatikana kwa kuchaguliwa na idadi kubwa ya wananchi,” Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, George Mkuchika amesema wakati anasoma hotuba ya Rais Kikwete.

Rais pia alitumia mkutano huo kuwaeleza wadau wa siasa kuwa Serikali ipo tayari kupokea mapendekezo kutoka kwao kwa ajili ya kumaliza malalamiko yaliyoko kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Amewataka wadau hao wa siasa wautumie mkutano huo kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuondoa mambo yenye utata.

Mpango wa Utafiti wa Demokrasia wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Redet) ndiyo ulioandaa mkutano huo kuzungumzia hali ya siasa nchini.

Ametaja baadhio ya mambo yanayolalamikiwa kuwa ni kufanyika kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa awamu mbili,ukiwemo uchaguzi wa madiwani mwaka mmoja baada uchaguzi mwingine wa Serikali za Mitaa.

Amesema, pia kuwepo kwa mamlaka mbili zinazosimamia uchaguzi wa Serikali za mitaa kunasababisha malalamiko.

Tume ya Taifa ya uchaguzi(NEC) inasimamia uchaguzi wa madiwani, Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) inasimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na vitongoji.

Kwa mujibu wa Rais Kikwete, sifa za wagombea hususani ile inayohusiana na uanachama na udhamini wa chama cha siasa kwa mtu anayegombea nafasi ya uongozi katika ngazi ya kitongaoji/kijiji zimezua mjadala.

“Mjadala juu ya masuala haya ni muhimu ili kujenga na kuimarisha demokrasia nchini,” alisema Kikwete na kuongeza kuwa “naamini masuala haya yatajadiliwa na mkutano huu na kuyatolea mapendekezo.”

“Mimi nisingependa kumaliza utamu wa mjadala huo kwa kutoa maoni yangu mapema, ila niseme tu mapendekezo yenu tutayafanyia kazi kama itakavyofaa,” amesema Rais Kikwete.

Amewasihi wapiga kura wote wenye sifa kutumia haki yao ya msingi kujiandikisha na kupiga kura.

Amewakumbusha wananchi kwamba uchaguzi huo unagharimu fedha nyingi za walipa kodi hivyo kama hawatajitokeza kwa wingi kujiandikisha na kupiga kura taifa litakuwa limepoteza rasilimali zake.

Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba, amesema, ingawa Rais Kikwete ametoa changamoto hizo, mapendekezo yao hayana maana katika uchaguzi ujao kwa kuwa zimebaki siku chache tu ufanyike.

“Kwa hali hiyo inatulazimu kusubiri hadi katika uchaguzi wa 2014 ili mapendekezo yetu yaweze kufanyiwa kazi kwa kweli hii sio kuwatendea haki wadau,” amesema Profesa Lipumba.

Naye Hellen Mlacky, anaripoti kuwa, Rais Jakaya Kikwete amewataka watanzania nchini wajitokeze kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura la uchaguzi wa Serikali za Mitaa ili watumie haki yao ya kuchagua viongozi wanaowataka.

Ameyasema hayo leo baada ya kujiandikisha katika mtaa wa Kivukoni, kituo mamba moja Kivukoni. Rais alikuwa ni mtu wa 12 kujiandikisha katika kituo hicho tangu zoezi hilo lianze rasmi juzi.

Amesema, wananchi wengi wamekuwa na fikra potofu kwamba uchaguzi wenye maana ni ule wa kumchagua Mbunge au Rais.

Rais amesema, wananchi wanapaswa kuuthamini uchaguzi huo kwa kuwa,viongozi wa mitaa ndio wanaopaswa kupewa kipaumbele kwa sababu kila wakati wanashughulikia matatizo ya wananchi.

“Napenda niwasisitizie wananchi kwamba viongozi wa mitaa ndio viongozi muhimu sana… sisemi hivyo ili kuwakataza wasipige kura mwaka kesho kwenye uchaguzi mkuu ila nataka muelewe viongozi wa mitaa ndio wa kwanza hata mtu unapopatwa na shida ya ghafla hata usiku.. hawa ni viongozi wetu wa usiku na mchana” amesema.

No comments: