Monday, October 12, 2009

Uandikishaji Uchaguzi Serikali za Mitaa wakosa mwamko

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda anafikiria kuunganisha uchaguzi wa serikali za mitaa na ule wa midiwani katika uchaguzi ujao wa 2015 baada ya kubaini uandikishaji wa wapiga kura katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu kukosa mwamko.

Aidha pamoja na kukosa mwamko huo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa ya Serikali za Mitaa, (TAMISEMI) Celina Kombani, amesisitiza kuwa muda wa kujiandikisha uliofikia tamati jana hautaongezwa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana viongozi hao walitoa matamko hayo baada ya kupata habari ya kutokuwepo kwa idadi iliyotarajiwa ya wapigakura katika maeneo mbalimbali nchini.

Pinda ambaye alijiandikisha jana katika kituo cha Oysterbay Na.2B, jijini Dar es Salaaam ili aweze kushiriki uchaguzi huo, alisema serikali itaangalia uwezekano wa kurudisha uchaguzi wa madiwani kwenye uchaguzi huo.

“Wapo watu wanaohoji ni kwa nini madiwani wanachaguliwa wakati wa Uchaguzi Mkuu wakati wanafanyakazi na Serikali za Mitaa…serikali itajadili na kuangalia uwezekano wa kurudisha uchaguzi wa madiwani kwenye serikali za mitaa,” Pinda alieleza.

Alisema huenda madiwani wakichaguliwa sanjari na viongozi wa Serikali za Mitaa, uchaguzi huo utakuwa na mwamko zaidi.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi alimpatia Waziri Mkuu taarifa ya uandikishaji na kusema kuwa Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na lengo la kuandikisha wapiga kura 1,200,573.

Lukuvi alisema hadi jana mchana ni watu 388,824 tu waliokuwa wamejitokeza kujiandikisha sawa na asilimia 32.38 ya matarajio yaliyowekwa.

Lukuvi alifafanua kuwa Wilaya ya Ilala ilikuwa na lengo la kuandikisha watu 189,5000, lakini waliojiandikisha mpaka wakati akimpa Pinda taarifa hiyo, walikuwa 96,885 sawa na asilimia 51.12.

Wilaya ya Temeke iliweka lengo la kuandikisha wapiga kura 509,000 na waliojiandikisha hadi jana mchana ni 151,333 sawa na asilimia 39.73

Kwa upande wa Wilaya ya Kinondoni, Lukuvi alisema lengo lilikuwa kuandikisha wapiga kura 50,2037 lakini waliojitokeza walikuwa 140,606 sawa na asilimia 28 ya matarajio yaliyowekwa katika wilaya hiyo.

Lukuvi alisema kwa ujumla idadi ya waliojitokeza ni ndogo na kueleza kuwa hali hiyo imesababishwa na mazingira ya wakazi wa Dar es Salaam ambao wengi wao wametinga na shughuli mbalimbali.

“Wakazi wa Dar es Salaam ni wachakarikaji na wengi wao wanapata muda siku za mapumziko ya wiki. Uandikishaji ulianza Jumapili lakini kulikuwa upungufu hivyo kazi ilianza rasmi Jumatatu na kumalizika leo (jana) Jumamosi hivyo watu wengi wamejitokeza leo…kama siku zikiongezwa huenda watajitokeza wengi zaidi,” Lukuvi alisema.

Akijibu hoja hiyo, Waziri Mkuu alisema muda hauwezi kuongezwa kwa sababu uliwekwa kwa kuzingatia kanuni na sheria za uchaguzi ila kama sheria inaruhusu basi serikali itaangalia uwezekano wa kuongeza muda.

Hata hivyo alisema idadi ndogo imesababishwa na upungufu wa kibinadamu kwa sababu baadhi ya watu wanapuuzia uchaguzi wa Serikali za Mitaa bila kujali kuwa umewekwa mahususi ili kuwapatiwa wananchi fursa ya kuchagua viongozi bora kwa maendeleo yao wenyewe.

Naye John Nditi anaripoti kutoka Morogoro kuwa Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ( TAMISEMI), Celina Kombani, amesema kuwa hakutakuwa na muda wa nyongeza wa uandikishaji wa daftari wa wapiga kura la uchaguzi huo.

Wakati Waziri huyo wa akitoa msimamo huo, katika Manispaa ya Morogoro shughuli hiyo jana ilianza kwa kudorora kwa baadhi ya vituo vya kujiandikisha kwenye daftari hilo na kwamba hadi jana mchana watu walikuwa wakiendelea kujitokeza kujiandikisha kwenye vituo vyao.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Sabasaba, Haji Ngatumbula, alisema malengo ya uandikishaji katika Kata hiyo kwenye daftari hilo ilikuwa ni watu 1,560 na hadi kufikia Oktoba 9, mwaka huu watu waliojiandikisha walifikia 816 na kwamba hadi jana mchana baadhi ya vituo 12 vilivyopo viliandikisha watu wa kutosha.

Hata hivyo alisema siku ya kwanza ya uandikishaji jumla ya watu 281 walijiandikisha ambapo wanawake walikuwa 145 na wanaume 132 na siku iliyofuatia idadi yao ilianza kushuka na kufikia watu 145.

Hata hivyo baadhi ya vituo vilivyotembelewa jana mchana kabla ya kufikia muda wa kumalizika kwa shughuli hiyo, vikiwemo vya Ngoto B ambacho kiliandikisha watu sita, Ofisi ya Kata hiyo watu 57 na mtaa wa Betero watu 14 ambao ulivuka lengo waliokusudia la watu 100 na kufikisha 121.

Katika vituo vingine kikiwemo cha kata ya Mlimani iliweka makisio ya kuandikisha watu 2,368 kati ya wakazi 7,316 ambapo mtaa wa Liti wenye idadi ya watu 980 ulipanga kuandikisha watu 508 na ambapo hata hivyo bado hawakufikia lengo.

Naye Merali Chawe anaripoti kutoka Mbeya kuwa mkoa huo umeshindwa kufikia lengo la kuandikisha watu kwa ajili ya upigaji kura wa kuchagua viongozi wa serikali za mitaa ambapo hadi kufikia jana watu waliojiandikisha walikuwa ni 295,929 kati ya watu 665,277 waliotarajiwa.

Mratibu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mkoani Mbeya Prosper Roman aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumzia idadi ya watu waliojiandikisha, ambapo alisema sababu za idadi ndogo ya watu waliojiandikisha imetokana na watu kuchanganya uandikishaji huo na uboreshaji wa daftari la wapiga kura.

No comments: