Monday, October 19, 2009

Vijana waaswa kutumia ICT kuwa wajasiriamali

VIJANA wanapaswa kuthamini na kutumia ipasavyo ujuzi katika mafunzo ya kompyuta kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha kuwa wajasiriamali.

Ofisa Elimu Mkuu katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Charles Philemon, amesema, ujuzi katika nyanja mbalimbali za teknolojia ya kompyuta pia ni muhimu kwa taifa ili kukabiliana na changamoto za utandawazi.

Philemon aliyasema hayo jana, Dar es Salaam, wakati wa mahafali ya 16 ya taasisi ya biashara na teknolojia inayotoa mafunzo ya masuala ya fedha, na teknolojia ya mawasiliano.

“Hii ni elimu, ni elimu ya kazi, ni elimu ya ujasiriamali” alisema Philemon katika mahafali hayo yaliyoshirikisha jumla ya wahitimu 211 wa ngazi za Shahada, Stashahada ya Juu na Stashahada.

Alisema, wahitimu hao wanapaswa kuwa na nidhamu wakati wa kutekeleza majukumu yao ili waongeze tija na wapate mafanikio. “Ukikosa nidhamu, hata ukiwa na taaluma nzuri utaua nchi” alisema baada ya kuwakabidhi wahitimu hao vyeti na zawadi.

Mwanafunzi bora katika mitihani iliyofanywa mwaka jana katika taasisi hiyo ngazi ya Stashada ya Kimataifa ya Kkompyuta, Elex Ongon, alisema, ujuzi katika nyanja mbalimbali katika teknolijia ya mawasiliano ni nyenzo muhimu kwa kuwa inawawezesha wahitimu wajiajiri.

Ametoa changamoto kwa vijana nchini wajifunze masuala ya teknolojia ya mawasiliano kwa madai kuwa, wahitimu wake wanahitajika sana kwenye soko la ajira nchini.

Alisema, kwa sasa yeye anahitaji mtaji mtu ili aweze kuwa mjasiriamali kwa kuwa, amejifunza kwa vitendo zaidi hivyo ana ujuzi kwenye masuala mbalimbali ya kompyuta.

Meneja wa mafunzo katika taasisi hiyo, Khamisi Mtajuka, alisema, elimu wanayoitoa ni nyenzo mojawapo ya kupambana na ukubwa wa tatizo la ajira nchini linalotokana na uhaba wa ujuzi hivyo kuwafanya wananchi watafute ajira badala ya kujiajiri.

Mtajuka alisema, taasisi hiyo yenye uwezo wa kufundisha wanafunzi 1200 kwa siku inashirikiana na taasisi za kimataifa ili kupata wahitimu wenye ujuzi wa kimataifa kwa lengo la kuwawezesha kuwa wajasiriamali au kumudu ushindani kwenye soko la kimataifa la ajira

No comments: